Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Emmanuel Adamson Mwakasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Primary Question

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA,aliuliza:- Kumekuwa na migogoro mingi ya ardhi nchini inayosababisha uvunjifu wa amani miongoni mwa wananchi na hata katika baadhi ya maeneo migogoro hiyo imesababisha vifo; (a) Je, Serikali imechukua hatua gani kutatua migogoro hiyo? (b) Kwa kuwa Maafisa Ardhi wengi ndiyo chanzo cha migogoro hiyo, je, ni Maafisa Ardhi wangapi wamechukuliwa hatua kwa kusababisha migogoro hiyo?

Supplementary Question 1

MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Tabora Manispaa imeathirika sana na migogoro ya ardhi. Kuna kata ambazo zinapakana na maeneo ya jeshi, ambazo ni Kata za Cheyo, Mbugani, Tambuka Reli, Uyui na Micha. Maeneo yale yamekuwa na migogoro ya mipaka ya muda mrefu. Je, Wizara ya Ardhi imejipangaje kwa kushirikiana na Wizara ya Ulinzi ili waweze kuoanisha sasa mipaka halisi ili kuweza kutatua migogoro hii ya mipaka katika kata hizo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Tabora kama nilivyosema manispaa imekuwa na migogoro mikubwa ya ardhi na hasa bomoa bomoa. Tabora imeathiriwa sana na zoezi la bomoa bomoa; si maeneo ya reli tu lakini hata maeneo mengine yanayopaka na mashule kama Tabora Girls…
Wananchi wale na maafisa kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri wengine si waaminifu. Je, Serikali kwa kuwa hawa wananchi wengi waliobomolewa hayakuwa makosa yao, inawachukulia hatua gani hawa ambao wamesababisha wananchi wamepata hasara kubwa na sasa hawana hata amani na wamekuwa katika hali isiyoeleweka?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza amezungumza habari ya mipaka kuathiri maeneo yaliyopakana na Jeshi na ametaja kata ya Cheyo, Tambuka Reli na nyingine. Naomba tu nimthibitishie Mheshimiwa Mwakasaka kwamba Wizara ya Ulinzi ilishachukua hatua ya kuunda Kamati ambayo imepitia katika maeneo yote ambayo yana migogoro ya Jeshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo hayo walikuwa wakifika wanaongea na watu wa eneo lile na kuweza kubainisha mipaka; kwa sababu kuna mengine ambayo wananchi lakini maeneo mengine Jeshi liliingia ndani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kabla ya kuanza kuweka mipaka upya au kuipitia kwanza wanachambua yale maeneo. Wakishamaliza shughuli hiyo ndiyo Wizara itaingilia kati katika suala la kupanga. Hata hivyo, kwanza tuitambue tuibaini ili kuondoa ile migogoro. Zoezi limeshaanza katika baadhi ya wilaya na Kamati ile inafanya kazi vizuri kwa sababu inashirikisha uongozi wa maeneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la bomoa bomoa katika maeneo ambayo yamevamiwa au watu wamebomolewa pengine hawakuwa na tahadhari; kwanza naomba nitoe tahadhari kwa wananchi wengi, kwamba maeneo mengi ya taasisi za umma yamevamiwa sana na wananchi na wengine wamejenga nyumba za kudumu kwa muda mrefu. Hata hivyo, unapoangalia kisheria na taratibu na ukubwa wa shule yanayotakiwa kuwa unakuta sehemu nyingi yamevamiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa makosa ya watendaji wetu kuna wengine pia walithubutu kutoa hati katika maeneo ambayo ni ya shule. Kwa hiyo zoezi hili linafanyika ili kuhakikisha kwamba maeneo yote yanapimwa na yanatambulika na wale wote walioingia ndani basi sheria inachukua mkondo, wake kwa maana ikiwa ni pamoja na kuvunjiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wale ambao watakuwa wamevunjiwa kimakosa ni lazima uhakiki ufanyike tuweze kujua pengine hata ile hati aliyonayo si sahihi. Kwa hiyo kama tukikuta mtu amevunjiwa katika utaratibu ambao ni wa kimakosa basi tutaona namna ya kuweza kumpatia kiwanja mbadala. Nitoe rai tu kwamba wale wote walioko kwenye maeneo ya umma ni vizuri wakayaachia.