Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Magdalena Hamis Sakaya

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Kaliua

Primary Question

MHE. MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:- Kwa kuwa lengo la Serikali kuruhusu vyombo vya usafiri wa pikipiki kubeba abiria na mizigo ni kusaidia kurahisisha usafiri na pia kutoa ajira kwa vijana hapa nchini lakini ajali zinazotokana na vyombo hivi kwa sasa ni nyingi kuliko vyombo vingine. (a) Je, Serikali inaweza kueleza ni ajali ngapi za bodaboda zimetokea kwa miaka mitatu toka mwaka 2015 - 2017 na ni watu wangapi wamepoteza maisha kwenye ajali hizo na walemavu ni wangapi? (b) Je, Serikali ina mikakati gani ya uhakika ya kuokoa maisha na nguvukazi ya Taifa inayopotea kwa usafiri huu?

Supplementary Question 1

MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, suala la ajali hizi kutokana na jibu la msingi imekuwa ni hatari kubwa na ukiangalia idadi ya watu waliopoteza maisha, waliopata ulemavu na majeruhi ni wengi. Vilevile ajali hizi zinasababisha kuwepo kwa walemavu, wategemezi, wajane na wagane wengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hatua ambazo zinachukuliwa na Wizara na Serikali kuona kwamba ajali zinapungua lakini bado ajali zinaongezeka.
Je, Serikali haioni sababu kubwa ya ajali hizi ni kwamba madereva wa bodaboda hawafuati sheria za barabarani ikiwepo ku-overtake kushoto badala ya kulia? Serikali haioni sababu ya kuendesha masomo au mafunzo maalum kila Wilaya kwa bodaboda wote waweze kuelewa kanuni na sheria za barabarani na hivyo kuweza kupunguza ajali za barabarani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, baadhi ya maaskari barabarani badala ya kuwaelimisha bodaboda wamefanya bodaboda ni vyanzo vya mapato, kila wakiwaona wanakimbizana nao barabarani matokeo yake wao wanakuwa ni kisababishi cha ajali badala ya kupunguza ajali. Serikali inafanya nini na inachukua hatua gani kwa wale maaskari wote ambao wanakimbizana na bodaboda barabarani hajali amebeba abiria au hajabeba abiria ili kupunguza ajali hizi na kuokoa maisha ya Watanzania wanaopoteza maisha? Ahsante.

Name

Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mbunge kwamba jambo hili linamgusa na ameongea kwa hisia kama mama na kama mwakilishi wa vijana wetu hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu Serikali imefanya jitihada kubwa kama ambavyo nimeelezea, jambo ambalo limesalia ni familia zetu kuanzia ngazi za familia na ngazi za vijiwe, kuliongea jambo hili kama moja ya jambo linalomaliza maisha ya vijana wetu. Kila tunapokaa tuambizane kwamba ukienda mwendo kasi, usipofuata taratibu za uendeshaji wa vifaa hivi vya moto, madhara yake ni kupoteza maisha ya mwendeshaji mwenyewe ama yule aliyebebwa. Kwa hiyo, hili jambo likienea elimu yake itakuwa kubwa kuliko hii tu ambayo mpaka sasa tunaendelea kuifanya ya kutoa semina Wilaya kwa Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusu vijana hawa kukimbizwa na askari, niwaambie tu Waheshimiwa Wabunge ukichukulia kwenye sura moja unaweza ukaona kama vijana wanaonewa sana lakini niseme kuna utaratibu ambao unakuwa unakosewa. Moja, vijana wanakuwa wameshapewa leseni lakini inatokea wanapokuwa kule vijiweni wanakabidhiana bodaboda hizi kwa mtu ambaye hana leseni, mtu ambaye hana mafunzo yaani amejaribisha tu akaona pikipiki inatembea naye anabeba abiria, hili ni kosa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimewaelekeza viongozi wa vijiwe vile vya bodaboda kwamba na wenyewe watimize majukumu ya kiuongozi kwamba akitokea mwenzao aliyekosea na wenyewe wawe tayari kumwambia unatakiwa uripoti kistaarabu polisi ili uweze kumaliza jambo lako la kisheria. Kama hawatafanya hivyo, polisi itakuwa haina njia nyingine zaidi ya kumtafuta kwa nguvu na kuweza kumkimbiza popote pale ambapo yupo aweze kufikishwa katika mkono wa sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge tunawapenda sana vijana wetu lakini mapenzi yetu kwa vijana wetu ni kuhakikisha tunaokoa maisha yao. Kwa hiyo, huruma tunayoweza kufanya ni kuhakikisha tunadhibiti jambo hili na hamna njia mbadala zaidi ya kuweza kuhakikisha tunachukua hatua za kisheria kwa yule ambaye anaonekana anakiuka sheria. Kwa wale ambao kwenye vijiwe vyao watatimiza maelekezo haya, tumeelekeza askari wasikimbizane nao bali wamalize kistaarabu mambo ambayo yanahusu sheria.

Name

Asha Abdullah Juma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:- Kwa kuwa lengo la Serikali kuruhusu vyombo vya usafiri wa pikipiki kubeba abiria na mizigo ni kusaidia kurahisisha usafiri na pia kutoa ajira kwa vijana hapa nchini lakini ajali zinazotokana na vyombo hivi kwa sasa ni nyingi kuliko vyombo vingine. (a) Je, Serikali inaweza kueleza ni ajali ngapi za bodaboda zimetokea kwa miaka mitatu toka mwaka 2015 - 2017 na ni watu wangapi wamepoteza maisha kwenye ajali hizo na walemavu ni wangapi? (b) Je, Serikali ina mikakati gani ya uhakika ya kuokoa maisha na nguvukazi ya Taifa inayopotea kwa usafiri huu?

Supplementary Question 2

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi, napenda niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mashaka, matatizo, huzuni na gharama kubwa za matibabu zinaendelea kuwakabili vijana wetu hawa kutokana na hizi ajali za bodaboda. Je, ni lini Serikali itaongeza usimamizi na udhibiti wa kuhakikisha kwamba helmet na reflector zinavaliwa na vilevile kudhibiti upakianaji wa kimishikaki ambao unasababisha watu wengi zaidi kuumia kwa wakati mmoja? Ahsante. (Makofi)

Name

Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu maelekezo tulishatoa na tunachukua hatua kwa maswali yote mawili aliyoyauliza. Moja likiwepo hili la kuvaa kofia ngumu, tumeweka hiyo ni sheria na tumeenda mbali zaidi tunataka si tu mwendesha bodaboda tunataka hata abiria naye atimize wajibu huo wa kuvaa kofia ngumu. Pamoja na hilo, hili lingine la ubebaji wa mishikaki kama alivyoita, abiria zaidi ya moja na lenyewe tumeelekeza popote pale yanapotokea lichukuliwe kuwa ni kosa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema mwanzo kwamba jambo hili ni vema likaongelewa kwa ngazi ya kijamii na familia kwamba tuendelee kuwaelekeza vijana wetu. Mara nyingi vijana wetu wakielekezwa kwa mkono wa Serikali wanaona kama wanaonewa lakini wakielekezwa kuanzia ngazi ya familia, tunapokaa tuwaambie vijana wetu tunawapenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwenyewe niliwahi kuwapa vijana bodaboda kule Jimboni, niliwahi kuwapa wadogo zangu, watoto wa dada zangu lakini jambo la kwanza nililowaambia, niliwaambia nawapa chombo hiki cha moto lakini chombo hiki kinauwa. Wakiambiwa mkono ambao usio wa kisheria ambao ni wa kifamilia linawakaa zaidi kutambua kwamba ukikosea masharti ya uendeshaji ukaenda kasi, ukakosea sheria za uendeshaji barabarani, gharama yake ni kupoteza maisha ya mwendeshaji mwenyewe na abiria aliyebebwa kutoka kwenye hicho chombo.

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Primary Question

MHE. MAGDALENA H. SAKAYA aliuliza:- Kwa kuwa lengo la Serikali kuruhusu vyombo vya usafiri wa pikipiki kubeba abiria na mizigo ni kusaidia kurahisisha usafiri na pia kutoa ajira kwa vijana hapa nchini lakini ajali zinazotokana na vyombo hivi kwa sasa ni nyingi kuliko vyombo vingine. (a) Je, Serikali inaweza kueleza ni ajali ngapi za bodaboda zimetokea kwa miaka mitatu toka mwaka 2015 - 2017 na ni watu wangapi wamepoteza maisha kwenye ajali hizo na walemavu ni wangapi? (b) Je, Serikali ina mikakati gani ya uhakika ya kuokoa maisha na nguvukazi ya Taifa inayopotea kwa usafiri huu?

Supplementary Question 3

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Jimbo la Ukonga lina kata 13 na kata zote zina bodaboda karibu vijiwe zaidi ya kumi kila kata moja. Ukonga tumechangishana fedha tukajenga Kituo cha Polisi kule Chanika na kingine kinataka kujengwa pale Kata ya Kivule, lakini kwa hali ilivyo sasa, wananchi wa Ukonga na hasa bodaboda nikiwaambia wachangie fedha hawatachangia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninavyozungumza usiku wa kuamkia leo, wanakuja askari zaidi ya 20 wana bodaboda, walikuwa wanakuja na gari wanaificha, halafu wanapiga watu mpaka na marungu, wana-search kwenye wallet, kwenye pochi kila mahali wanaomba fedha. Sasa wanaenda wanakusanya bodaboda zile wanaomba shilingi 10,000 kwa lazima, kama huna zinapakiwa kwenye gari zinapelekwa central.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natakiwa nijue, ili kuleta mahusiano mazuri kati ya vijana wa bodaboda na polisi, Waziri anatoa kauli gani kuhusiana na jambo hili? Hata haya mambo ya mauaji kama watu wana uhasama hawatoi taarifa. Wanawakimbia kwa sababu ukikamatwa na polisi wala hakuulizi leseni, wala hakuelekezi, kama huna pesa unatembea. Naomba Waziri atoe kauli hapa kusaidia vijana wa bodaboda Mkoa wa Dar es Salaam na hasa Jimbo la Ukonga. Ahsante Mwenyekiti.

Name

Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba maelekezo ya Wizara tuliyotoa ni kwamba kuwa na bodaboda sio kosa na tumeelekeza watu wanaofanya makosa ndiyo wakamatwe. Kuwa tu na bodaboda haitoshi kuwa kosa kwa sababu hilo ni jambo ambalo lipo kisheria. Kwa maana hiyo nimepokea tu hiyo ya nyongeza aliyoisema ambayo yenyewe imekaa kituhuma zaidi nitalifanyia kazi, kama kweli lipo tutachukua hatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini maelekezo yetu tumesema kama vijana wamekosea wafikishwe kwenye mkono wa sheria lakini kama hawajakosea waachwe wafanye kazi zao za kujitafutia maisha kwa uhuru na usalama na wala wasikimbie. Nilielekeza nikasema kuna wakati mwingine hata wanaweza wakawamata kwa bahati mbaya na ikafika mpaka vituoni, niliwaambia wasione aibu kumuachia yule ambaye walimkamata kimakosa ambaye alikuwa hausiki.
Nilisema hata wamuombe radhi kwamba wewe si tuliyekuwa tunakutafuta nenda kaendelee na shughuli lakini isiwe kosa kwamba yeyote ambaye ameshakamatwa akifika kituoni basi inakuwa kazi kutoka, tuwatendee haki kufuatana na kosa kama amefanya ama hajafanya.