Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Eng. Joel Makanyaga Mwaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chilonwa

Primary Question

MHE. JOEL M. MAKANYAGA aliuliza:- Barabara inayounganisha Vijiji vya Msanga na Kawawa ni muhimu sana kiuchumi kwa Kata ya Msanga na Wilaya ya Chamwino na pia mazao mengi ya uhakika kutoka Kawawa na Vitongoji vyake lakini barabara hiyo ni korofi sana kwa sababu ya mbuga iliyopo kati ya vijiji hivyo viwili na daraja kubwa lililopo limevunjika kabisa kiasi kwamba halipitiki kabisa wakati wa mvua na wakati wa kiangazi hupitika kwa taabu sana. Je, Serikali ina mpango gani wa kurekebisha barabara hiyo na kulijenga daraja husika ili kuboresha mawasiliano ya vijiji hivyo viwili na masuala ya usafirishaji?

Supplementary Question 1

MHE. JOEL M. MAKANYAGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri na kwa sababu hiyo naomba niwe na swali moja tu la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, baada ya barabara hii sasa kutengenezwa na kuwa inapitika angalau kwa uzuri, magari makubwa na yanayobeba mzigo mzito sasa yanaitumia barabara hiyo kiasi kwamba eneo la kama kilometa moja limetengeneza tifutifu kubwa sana ambayo kama isiposhughulikiwa kipindi hiki, mvua itakaponyesha itakuwa shida sana kupitika. Mheshimiwa Naibu Waziri anasema nini kuhusu kuirekebisha sehemu hiyo kipindi hiki kabla mvua haijanyesha ili isije ikakosa kupitika tena? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, anachosema Mheshimiwa Mbunge ni kweli, bahati nzuri nimeenda kui- survey barabara ile na lile eneo moja kati ya Kijiji cha Msanga na Kawawa pale katikati hali imeharibika sana. Uharibifu ule ni kutokana na kwamba katika ujenzi wa Ikulu Ndogo ya Chamwino, malori ya TBA yanatumia barabara ile.
Mheshimiwa Spika, hata hivyo, tumeongea na Mkurugenzi, bahati nzuri watu wa TBA wamekubali kufanya marekebisho katika barabara ile.
Mheshimiwa Spika, niwashukuru sana TBA kwa sababu sasa hivi nao wanachonga barabara ya kilometa tano kutoka pale Kawawa kwenda maeneo ya Matelu ambayo ni mafanikio makubwa.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge, Ofisi yetu ya Chamwino chini ya Mkurugenzi tumeshafanya hiyo harakati na watu wa TBA wamekubali wataona jinsi gani ya kufanya ili mradi kurekebisha eneo lile liweze kupitika kwa wananchi wa Chamwino.