Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Fakharia Shomar Khamis

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS aliuliza:- Mara nyingi kumekuwa na taarifa juu ya watu wanaokamatwa na dawa za kulevya kwenye maeneo mbalimbali nchini, lakini hatuambiwi nini kinafanyika:- Je, baada ya watu hao kukamatwa, ni nini huwa kinaendelea?

Supplementary Question 1

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nina maswali mawili ya nyongeza.
(a) Kwa kuwa baadhi ya vyombo vya habari vilizungumzia kwamba baadhi ya watuhumiwa ambao walihusika na dawa za kulevya wanapokuwa gerezani wanaishi maisha ya kifahari, je, tuhuma hizi zina ukweli?
(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuwa na sober house zake wenyewe ili iwe ni sehemu ya ufuatiliaji wa vita ya dawa za kulevya kutokana na hivi sasa kuwa kazi inakuwa kama ya zimamoto, haiwi endelevu? Je, wanajipanga vipi ili kuifanya kazi hii iwe endelevu isiwe ya msimu?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na ukweli wa tuhuma ambazo zinasambazwa, kimsingi siyo kweli. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge na Watanzania kwa ujumla kwamba Jeshi la Magereza linafanya kazi zake za kusimamia na kuwahifadhi wafungwa na kuwarekebisha tabia kwa umahiri, weledi na umakini wa hali ya juu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, siyo rahisi. Nasi katika kufuatilia kwetu ambapo tumekuwa tukifanya ziara hizi Magerezani mara kwa mara, tumeshuhudia jinsi ambavyo Askari Magereza ama Jeshi la Magereza linavyofanya kazi yake vizuri na kwa weledi wa hali ya juu. Kwa hiyo, tuhuma hizo kimsingi siyo za kweli na ninaomba Watanzania wazipuuze.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na urekebishwaji wa tabia za watumiaji wa dawa za kulevya, naomba kumjibu Mheshimiwa Fakharia kwa kumjulisha kwamba Serikali kupitia Jeshi la Polisi ina utaratibu huo kwa kutumia vikundi mbalimbali vya michezo na miradi ya kuzuia uhalifu kama vile Familia yangu Haina Mhalifu, Klabu za Usalama Kwetu Kwanza na kadhalika na programu nyingine nyingi ambazo tunafanya kuhakikisha kwamba tunasaidia kurekebisha tabia za watumiaji wa dawa za kulevya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wakati huo huo kupitia sober house ambapo wadau mbalimbali wamekuwa wakizianzisha, tumekuwa tukishirikiana nazo kwa kuweza kuwapatia misaada mbalimbali kuhakikisha kwamba vijana wetu ambao wameathirika na dawa za kulevya wanaweza kutengamaa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyoyatoa, lakini nimevutiwa na swali la Mheshimiwa Fakharia, nimshukuru sana kwa kulileta.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaelezee Watanzania kwamba kuhusu mambo ya Sober house ni kweli, kuna baadhi ya sober house kwa sababu ya kutokuwa na standard zinazotakiwa zimekuwa zikileta matatizo. Kwa maana hiyo, tumekubaliana na Wizara ya Afya na Wizara ya TAMISEMI, chini ya uongozi wa Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwamba tutashirikiana sisi zote ili kwenye Halmashauri zetu tukae na Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya tuweze kutengeneza standard za sober houses zikiwemo zile ambazo zitakuwa kwenye Halmashauri ili watu wetu wanaokwenda kule wasije wakapata matatizo makubwa zaidi. (Makofi)