Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Ally Juma Makoa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kondoa Mjini

Primary Question

MHE. ALLY J. MAKOA aliuliza:- Je, ni lini TANROADS watalipa fidia kwa kujenga shule mbadala baada ya shule ya Msingi Unkuku kupitiwa na Barabara ya Dodoma – Arusha?

Supplementary Question 1

MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa fidia aliyoitaja Mheshimiwa Naibu Waziri ililipwa mwaka 2014 wakati barabara ilikuwa na upana wa mita 22. Mwaka 2017 walipokamilisha ujenzi wa barabara ile waliongeza mita nane kufika 30 na yenyewe ikachukua madarasa na nyumba ya malimu, na kwa kuwa Mheshimiwa Waziri Mbarawa alifika akaiona ile hali na akatoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri kutoa michoro pamoja na gharama na Mkurugenzi akafanya hivyo.
Napenda kujua sasa ni lini Serikali itatekeleza kupitia TANROADS ujenzi wa ile Shule ya Msingi Unkuku kwa sababu imeliwa sana na barabara?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; je, Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari niambatane naye pamoja na wataalam wake tukaione hii Shule ya Msingi Unkuku ilivyo katika mazingira hatarishi kwa watoto?

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza kwa pamoja. Ni kweli kwamba Serikali ililipa fidia wakati huo barabara ikiwa na upana wa mita 22.5. Kama alivyosema kwa sababu mimi mwenyewe sijaenda, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Kondoa na Dodoma ni karibu, nataka nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaongozana, tutafute siku mimi pamoja na wataalam ili twende eneo la shule tukaangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umetolewa mwongozo kwamba pale ambapo miundombinu ya shule, zahanati ama hospitali zinakuwa zimepitiwa na barabara kwa maana ya kuifuata, hatutakuwa tunatoa fidia badala yake tutakuwa tunajenga ile miundombinu yote iliyoathirika. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutakwenda na haya yote yatajibiwa ikiwa ni pamoja na kuona uwezekano kama kuna haja ya Serikali kujenga hiyo shule upya ama kutoa fidia, basi tutafanya hivyo baada ya kufika site, ahsante.