Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Primary Question

MHE. EDWARD F. MWALONGO (K.n.y. MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA) aliuliza:- Shule ya Sekondari ya Ndembela Wilayani Rungwe awali ilijengwa kwa nguvu za wananchi na baadaye Kanisa la Waadventista Wasabato liliingia kama wabia na kuiendeleza na hatimaye kuiendesha shule hiyo ikiwa na majengo yaliyokamilika. Baada ya wananchi kuihitaji shule yao, Kanisa limekubali kuirejesha kwa Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe kwa fidia ya Sh.947,862,000/= Halmashauri imeomba Wizara ya Elimu isaidie kulipa fidia hiyo:- Je, ni lini Serikali itasaidia kurejesha shule hiyo mikononi mwa wananchi kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe?

Supplementary Question 1

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Tukiachana na hayo ya huko Ndembela, naomba sasa maswali ya nyongeza nielekeze Njombe kwa maana hii nafasi ni fursa kwangu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imesema kwamba, Shule zote za Kata ambazo zinakidhi vigezo vya kuwa shule za bweni iko tayari kuzichukua na kuzifanya kuwa shule za bweni. Je, baada ya kuzichukua hizi shule kuwa za bweni zitakuwa zinachukua wanafunzi kutoka ndani ya eneo la kata kama ilivyo sasa ama zitachukua kama shule za Kitaifa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, Serikali iko tayari kutuma wakaguzi kwenda kukagua Shule ya Sekondari Uwemba na Shule ya Sekondari Matola zilizoko ndani ya Jimbo la Njombe Mjini ili ziweze kuwa shule za Kitaifa na kupata hiyo keki ya Taifa?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika harakati za ujenzi wa miundombinu ya shule za sekondari toka ilipoanza Awamu ya Nne changamoto kubwa ilikuwa ni suala zima la kuwasaidia vijana jinsi gani waweze kufikia elimu ya sekondari. Mchakato huu umefanyika kwa jitihada kubwa sana ndiyo maana tunaona shule nyingi za sekondari za kata zimejengwa. Baada hapo, tumekuja kugundua kuna changamoto kwamba vijana wa sekondari za kata wanakosa kwenda Form Five and Six kwa kuwa idadi kubwa ya wanafunzi wanafaulu lakini nafasi ni chache. Sasa tumetoa maelekezo kwamba shule hizi sasa zipanue wigo na kuzifanya sekondari hizi kuwa na mabweni ili baadaye ziwe na Form Five na Form Six.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali lake specific lilikuwa linasema ni jinsi gani zile shule za sekondari za kata zilizokuwa na mabweni zitahuishwa rasmi ili ziwe sekondari za bweni za kitaifa. Naomba nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa shule ambazo zitakidhi vigezo zitajadiliwa katika vikao husika vya Halmashauri na kupelekwa Wizara ya Elimu. Wizara ya Elimu itafanya tathmini ya kina ili kuona kama shule husika ina hadhi ya kupandishwa daraja na ikijiridhisha itapandishwa daraja rasmi na kuwa shule ya sekondari ya bweni. Hata hivyo, naomba niseme kwamba Serikali haiwezi kupandisha shule zote za kata kwa mara moja kuwa sekondari za bweni kwa sababu jambo hili vilevile lina changamoto ya kibajeti.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili aliuliza ni jinsi gani hizi shule mbili za Uwemba pamoja na nyingine aliyoitaja zitapandishwa rasmi daraja. Kama nilivyosema katika majibu yangu ya awali kwamba tufanye mchakato ule wa kawaida baada ya mchakato huo, Wizara ya Elimu itaangalia na wataalam watafika watafanya tathmini kama vigezo vitakuwa vimefikiwa Serikali itaona jinsi gani ya kufanya.

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Primary Question

MHE. EDWARD F. MWALONGO (K.n.y. MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA) aliuliza:- Shule ya Sekondari ya Ndembela Wilayani Rungwe awali ilijengwa kwa nguvu za wananchi na baadaye Kanisa la Waadventista Wasabato liliingia kama wabia na kuiendeleza na hatimaye kuiendesha shule hiyo ikiwa na majengo yaliyokamilika. Baada ya wananchi kuihitaji shule yao, Kanisa limekubali kuirejesha kwa Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe kwa fidia ya Sh.947,862,000/= Halmashauri imeomba Wizara ya Elimu isaidie kulipa fidia hiyo:- Je, ni lini Serikali itasaidia kurejesha shule hiyo mikononi mwa wananchi kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe?

Supplementary Question 2

MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa niweze kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tatizo la Shule ya Sekondari Ndembela linaendana sana na tatizo la Shule Sekondari ya Kandete Wilayani Rungwe ambapo sasa tumeanza kujenga ili iwe ya wasichana pekee. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza akawadhibitishia wananchi wa Busokelo kwamba Serikali itashiriki kikamilifu ili ianze mapema mwakani?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge amesema kwamba kama ikiwezekana Serikali ianzishe mchakato wa kuifanya Shule ya Sekondari ya Kandete ili kuwa sekondari ya bweni. Nimerudia hapa mara kadhaa kwamba tumekuwa na changamoto kubwa ya vijana wetu wasichana kupata mimba na nikasema tumetoa kipaumbele sana katika ujenzi wa shule za bweni. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Halmshauri yake ikianza na sisi Ofisi ya Rais – TAMISEMI lazima tutaweka nguvu ya kutosha kwa sababu ajenda kubwa ni jinsi gani tutamsaidia msichana aweze kupata elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama Mheshimiwa Mbunge watakuwa wameanza juhudi hizo basi, naomba nimuambie kwamba na sisi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, kwa vile watakuwa wameweka katika bajeti yao tutahakikisha bajeti hizo zinapitishwa ili sekondari hiyo ambayo inatarajiwa kubadilishwa kuwa sekondari ya wasichana iweze kuwa sekondari ya wasichana vijana waweze kumaliza vizuri, waweze kupata elimu na hapo baadaye tuwe na viongozi wengi wasichana kutoka maeneo hayo.

Name

Juma Selemani Nkamia

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chemba

Primary Question

MHE. EDWARD F. MWALONGO (K.n.y. MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA) aliuliza:- Shule ya Sekondari ya Ndembela Wilayani Rungwe awali ilijengwa kwa nguvu za wananchi na baadaye Kanisa la Waadventista Wasabato liliingia kama wabia na kuiendeleza na hatimaye kuiendesha shule hiyo ikiwa na majengo yaliyokamilika. Baada ya wananchi kuihitaji shule yao, Kanisa limekubali kuirejesha kwa Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe kwa fidia ya Sh.947,862,000/= Halmashauri imeomba Wizara ya Elimu isaidie kulipa fidia hiyo:- Je, ni lini Serikali itasaidia kurejesha shule hiyo mikononi mwa wananchi kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe?

Supplementary Question 3

MHE. JUMA S. NKAMIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza. Shule ya Sekondari ya Kuryo, iliyoko Wilayani Chemba ina historia ndefu sana. Shule hii inamilikiwa na Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha Mapinduzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Chama cha Mapinduzi kupitia Jumuiya ya Wazazi kimeshindwa kuiendesha shule hii na sasa hivi imefungwa na ina miundombinu yote, je, Serikali iko tayari sasa kuichukua shule hii kutoka mikononi mwa Chama cha Mapinduzi na kuikabidhi Halmashauri ya Chemba ili iweze kufanya kazi yake vizuri?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Nkamia amezungumzia Shule ya Sekondari ya Kuryo ambayo inamilikiwa na Jumuiya ya Wazazi ya Chama cha Mapinduzi. Kwa sababu hii ni mali ya Chama sitaki kuleta ugomvi kati ya Mheshimiwa Mbunge na Mheshimiwa Bulembo ambaye ni Mwenyekiti wa Wazazi Taifa. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, najua lengo kubwa la Mheshimiwa Mbunge ni vijana wale waende shule wakapate elimu kwa sababu majengo yapo na yana miundombinu mizuri. Mimi nimshauri Mheshimiwa Nkamia kwa sababu katika ahadi yetu tulipanga twende Chemba, siku tukienda Chemba, hata wiki ijayo, tufike angalau tukaione shule hiyo, tufanye ushawishi na Jumuiya ya Wazazi ili shule hii iweze kutumika na hivyo iwasaidie vijana wa Chemba kupata elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wazo la Mheshimiwa Mbunge ni zuri nadhani linataka consultation meeting kati ya watu wa Chemba na Jumuiya ya Wazazi. Kwa sababu Ilani ya Chama cha Mapinduzi ina lengo la kuhakikisha vijana wanapata elimu nadhani jambo hili litafikia mahali pazuri katika kuhakikisha vijana wa Chemba wanapata elimu.