Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza: - Je, lini Serikali itajenga Jengo la Mama na Mtoto kwenye Kituo cha Afya – Loliondo?

Supplementary Question 1

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa kituo hiki kinahudumia zaidi ya Kata tatu na wananchi wanalazimika kutembea zaidi ya kilometa kumi kutafuta huduma hizi za Mama na Mtoto.

Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwenye Kituo cha Afya Loliondo ili basi ujenzi wa jengo la Mama na Mtoto liweze kujengwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, wananchi wa Kata ya Songoro katika Wilaya ya Meru wamejitolea kwa nguvu zao binafsi kujenga jengo la Kituo cha Afya hadi kufikia kwenye ngazi ya lenta.

Je, ni lini Serikali itawasaidia wananchi hawa kumalizia kituo hiki cha afya ambacho kitakwenda kuhudumia zaidi ya wananchi 10000? Ahsante. (Makofi)

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Loliondo kinahudumia wananchi wengi wa ndani ya Kata tatu. Pia ni kweli kwamba wananchi wanalazimika kutembea umbali mrefu.

Mheshimiwa Spika, dhamira ya Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan ni kupunguza umbali wa wananchi kufuata huduma za afya. Ndiyo maana tayari kituo hiki cha Afya cha Loliondo kimeingizwa kwenye orodha ya vituo 199 vinavyotafutiwa fedha. Vile vile, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutatoa kipaumbele kwenye kituo hiki cha afya ili kiweze majengo hayo.

Mheshimiwa Spika, pili, niwapongeze wananchi wa Kata ya Songoro Halmashauri ya Meru kwa kuanza kwa nguvu zao kujenga majengo ya Kituo cha afya. Tutakwenda kufanya tathmini kuona ni kiasi gani cha fedha kinahitajika ili tuweze kutafuta fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa kituo cha afya cha Songoro. Ahsante.