Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Primary Question

MHE. MOSHI S. KAKOSO aliuliza:- Je, upi Mkakati wa kuwapa kipaumbele cha ajira walimu wanaojitolea katika shule za msingi na sekondari pindi ajira zinapotoka?

Supplementary Question 1

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa idadi ya walimu wanaojitolea ni wengi na ajira zinapotoka huwa hawapati nafasi ya kuajiriwa hawa ambao wamejitolea. Halmashauri yangu ina zaidi ya walimu 60 ambao wamejitolea na waliopata ajira wamepata walimu watatu tu.

Je, Serikali haioni kwamba inavunja moyo wale walimu wanaojitolea na wanaopata ajira ni wale ambao wapo mitaani? Tunataka tupate mwongozo sahihi wa Serikali na majibu stahiki kwa wale ambao wanajitolea. (Makofi)

Swali la pili, kuna tabia ambayo imejengeka ajira zinapotolewa Halmashauri ambazo ziko vijijini zinapokea watumishi ndani ya miezi mitatu wale watumishi wote wanarudi maeneo ya mijini; Serikali haioni hii tabia ambayo imejengeka ni tabia ambayo inakuja kuua mfumo wa elimu au utumishi wa umma kwenye maeneo ya vijijini? (Makofi)

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeendelea kuajiri watumishi wote bila kujali wanaojitolea na ambao hawajitolei. Changamoto ya kuajiri walimu wanaojitolea ilitokana na utaratibu ambao haukuwa rasmi wa kuwasilisha majina ya walimu wanaojitolea. Kwa sababu baadhi ya Wakuu wa Shule wasio waaminifu walikuwa wanatumia fursa hiyo kuingiza majina ya walimu ambao hawajitolei na mara nyingine wanaachwa walimu wale ambao wanajitolea.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua hilo Serikali imeandaa mwongozo mahsusi na imeandaa mfumo ambao walimu wenyewe wataingia online kuji-register, kujiandikisha kwamba ni walimu wanaojitolea katika shule fulani na Serikali itafanya uhakiki na kuthibitisha kwamba walimu wale wanajitolea katika maeneo hayo. Hii itasaidia mara ajira zinapojitokeza kuona nani amejitolea kwa muda mrefu apate kipaumbele cha kupata ajira hizo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hili jambo linafanyiwa kazi seriously na Serikali itahakikisha kwamba linakamilika mapema iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili kuhusiana na walimu pia watumishi wa sekta nyingine ambao wanapangiwa katika Halmashauri za Vijijini na kuhama, kwenye utaratibu wa ajira kwa mfumo wa kieletroniki kwa sasa, tumeshaelekeza kwamba watumishi wote wa elimu au wa afya wakishaajiriwa kwenye Halmashauri hawatakiwi kuhama ndani ya angalau ya miaka mitatu tangu kuajiriwa. Unless kuna sababu ya msingi sana ya kulazimisha watumishi hao kuhama. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kwanza kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wale maeneo ambayo kuna watumishi ambao waliajiriwa maeneo ya vijijini na wamehamishwa kabla ya umri huo tupate taarifa hizo. Tumeshapata Ludewa tumeshapata maeneo mengine, tumeanza kushughulikia na watarejeshwa katika Halmashauri zilezile ili waendelee kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili tunalifanyia kazi, ahsante. (Makofi)