Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Primary Question

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza: - Je, ni lini Serikali itahakikisha kuwa Vyumba vya kuhifadhi maiti nchini vinakuwa na majokofu?

Supplementary Question 1

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwanza swali hili lilikuwa limeulizwa kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu niliuliza mimi mwenyewe na ninakushukuru kiti chako kuamua Wizara ijibu na leo amekuja kuleta majibu.

Nina maswali madogo mawili ya nyongeza, swali la kwanza, kwa kuwa sasa Halmashauri ya Mji wa Mbulu haina jokofu kwa muda wa mwaka mmoja au zaidi ya mwaka sasa, na kwa mapato yetu ya ndani hatuwezi kununua jokofu hilo linalohitaji takriban Milioni 70.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutununulia hilo jokofu ili hospitali ya Mbulu ipate huduma hiyo na kuondoa adha hiyo kwa wananchi?

Swali la pili, kwa kuwa kumeonekana kuna gharama kubwa sana ya uagizaji wa dawa na vifaatiba nchini kupitia Wakala wa MSD Serikali haioni kuwa ni wakati muafaka wa kutazama gharama hizo ili kuona namna mbadala ya kupunguza gharama kwa Serikali na kutoa huduma hiyo kwa Umma?

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Kwanza ninampongeza kwa ufuatiliaji wake makini wa hili suala kwa ajili ya Wilaya yake. Kwanza ameshafika Wizarani na nimhakikishie kwamba majokofu yameshafika MSD siku tatu zilizopita, kwa hiyo mpaka mwisho wa wiki itakuwa jokofu la kubeba miili 12 litakuwa limefika Kanda ya Kaskazini kwa ajili ya kuelekea kwenye hospitali yake ya Wilaya.

Swali lake la pili ni suala la gharama ya bei ya MSD kuwa ni ghali. Kwanza nimwambie MSD ni Shirika la Serikali na kweli huko nyuma kulikuwa na tatizo hilo lakini halipo sasa hivi, ndiyo maana Rais wetu Samia Suluhu Hassan ametoa fedha na tumejenga viwanda kule Idofi ambavyo vinazalisha dawa pamoja na gloves ukienda sasa hivi MSD ukilinganisha na bei zilizopo mtaani, MSD ni bei rahisi kuliko ilivyo mtaani. Kwa hiyo, hilo tatizo limesha tatuliwa na linaendelea kufanyiwa kazi zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako niseme tu moja kwenye eneo hili la mortuary, Mbunge wa Meru amejenga yeye mwenyewe mortuary kwa asilimia 80 kwa fedha zake na niipongeze Halmashauri yake ikachangia asilimia 20 iliyobaki na katika majokofu yanayokuja, jokofu lako linakuja na Mbunge wa Makete.