Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AMINA N. MAKILAGI aliuliza:- Zao la mwani limekuwa ni ukombozi kwa vikundi vya akina mama katika mwambao wa Pwani:- (a) Ni lini Serikali itavipatia mtaji vikundi vya wanawake wa kilimo cha mwani ili kuongeza uzalishaji kutoka tani 12,000 hadi 20,000 kwa mwaka? (b) Ni lini Serikali itawapatia nyenzo na utaalam ili vikundi vya wanawake na vijana viweze kuzalisha chaza, walulu, kaa, kamba na pweza?

Supplementary Question 1

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri Tizeba kwa kuchaguliwa kuwa Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi na pia kumshukuru kwa majibu mazuri sana pamoja na kwamba ameanza kazi leo. Sasa naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa zao la mwani limekuwa likikabiliwa na changamoto nyingi sana ikiwemo kutofahamika kwa zao lenyewe lakini vilevile kukosa soko, pembejeo na hivyo kufanya wakulima wa mwani na hasa wanawake kuhangaika kutafuta masoko na pembejeo. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha zao hili la mwani linaongezewa thamani kwa kujenga viwanda katika maeneo yote yanayozunguka ukanda wa bahari ili zao hili lilete tija kwa wanawake na hasa ikizingatiwa kwamba zao hili limekuwa linachukuliwa tu na Wachina na soko lake liko China, Korea na maeneo mengine? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa vikundi vya ujasiriamali kwa asilimia kubwa vimekuwa vikitegemea mabenki ya kibiashara ambayo kwa kweli riba yao imekuwa kubwa sana na hivyo kufanya vikundi vya wanawake na vijana kushindwa kabisa kumudu kwenda kukopa katika mabenki hayo. Serikali ina mkakati gani kupitia upya mabenki yote na vyombo vyote vya fedha ili kuangalia hizi riba zinazotozwa na kulinganisha na hali halisi ilivyo ili wanawake na vijana waweze kunufaika na mabenki haya? Ahsante.

Name

Dr. Charles John Tizeba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buchosa

Answer

WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kwa sasa hili zao la mwani soko lake siyo zuri sana hapa nchini. Kama alivyosema yeye mwenyewe, wakulima wa mwani wanauza kwa makampuni ya kutoka huko Korea, China na India.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sababu kubwa ya msingi ya kutoongeza thamani ya zao hili hapa hapa nchini ni uzalishaji mdogo ambao uko katika zao hili kwa sasa. Ili uzalishaji uweze kuwa na tija kwa mwekezaji mwenye kiwanda kwa uchache zinahitajika tani 12,000 kwa mwaka au zaidi, ndiyo mtu akiwekeza kwenye kiwanda cha kuchakata mwani anaweza kupata faida. Sasa hivi uzalishaji tulionao ni tani 600 tu kwa mwaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana sasa Serikali, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, kupitia huu mradi wa SWIOFish tunajipanga kupitia vikundi vya uzalishaji wa mwani ili viweze kupatiwa mikopo. Nitoe wito kupitia nafasi hii kwamba Halmashauri zote ambazo ziko katika Ukanda wa Pwani watie jitihada kubwa katika kuviorodhesha hivi vikundi ili hizi fedha ambazo zinatolewa na Benki ya Dunia ziweze kutumika vizuri kwa vikundi hivyo vya akina mama na hata wasio akina mama kwa sababu zao hili siyo kwa ajili ya akina mama na vijana peke yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, ziko fedha ambazo Serikali imeshapata kutoka Benki ya Dunia, Dola za Kimarekani milioni 36. Dola za Marekani milioni 17 zitatumika kwa Tanzania Bara na Dola milioni 11 zitatumika kwa Tanzania Zanzibar na Dola milioni 8 hivi zitatumiwa na taasisi zinazohudumia utafiti katika eneo hili la uzalishaji viumbe katika Ukanda wetu wa Pwani.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kujibu swali lake la pili la nyongeza, hivi vikundi vijiorodheshe. Hizi fedha hasa ndiyo zimelenga kuwakomboa hawa watu wa vikundi kuondokana na mikopo ambayo siyo rafiki sana wakati mwingine kutoka kwenye taasisi za fedha kwa sababu, watapewa msaada wa pembejeo, ruzuku za dawa na vitu vingine ili kuwawezesha kuongeza uzalishaji wao. Tutakapofika tani 12,000 au zaidi, watu wengi wanayo nia ya kuwekeza katika viwanda hapa nchini vya kuchakata hizi mwani na ndiyo hapo sasa hata thamani ya hili zao itaweza kuongezeka.