Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 9 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 124 2023-09-08

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Primary Question

MHE. MWITA M. WAITARA aliuliza: -

Je, lini Serikali itaongeza posho za Waheshimiwa Madiwani na Wenyeviti wa Vijiji?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Mwikwabe Waitara, Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kazi kubwa inayofanywa na Waheshimiwa Madiwani na Wenyeviti wa Vijiji katika kutoa huduma mbalimbali kwa wananchi. Kwa mujibu wa Sheria ya Mamlaka za Serikali za Mitaa Sura ya 290, kila halmashauri inatakiwa kuweka utaratibu wa kuwalipa posho, Waheshimiwa Madiwani na Wenyeviti wa Mitaa na Vijiji kutoka katika vyanzo vya mapato ya ndani ya halmashauri.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto za mapato kwenye halmashauri nyingi nchini, Serikali ilianza kutenga bajeti katika mwaka wa fedha 2021/2022 kwa ajili ya kulipa posho za Waheshimiwa Madiwani pamoja na Wenyeviti wa vijiji.

Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 22.5 kwa ajili ya kulipa posho za Waheshimiwa Madiwani na Wenyeviti wa vijiji katika halmashauri 168.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuzijengea uwezo Mamlaka za Serikali za Mitaa ili ziweze kubuni na kuimarisha vyanzo vya mapato pamoja na kudhibiti mianya ya upotevu wa fedha kwa kutumia mifumo ya kieletroniki ya kukusanya na kutumia fedha katika kutekeleza miradi ya maendeleo pamoja na matumizi mengineyo ili kuongeza uwezo wa malipo kwa viongozi.