Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 30 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Wizara ya Kilimo 398 2023-05-22

Name

Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Primary Question

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI aliuliza: -

Je, lini Serikali itarejesha utoaji ruzuku ya pembejeo za dawa kwa Wakulima wa Kahawa ili wazalishe zaidi kama awali?

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Patrick Alois Ndakidemi, Mbunge wa Moshi Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, matumizi ya viuatilifu katika zao la kahawa ni njia ya udhibiti wa visumbufu vya zao la kahawa ili kulinda ubora wa mazao yanayozalishwa dhidi ya magonjwa ya Kutu ya Majani na Chole Buni. Aidha, utafiti wa zao la kahawa umebaini kuwa upandaji wa miche bora ya kahawa ni njia pekee inayowezesha kuzalisha mazao yenye tija nzuri, ukinzani dhidi ya wadudu waharibifu na magonjwa ya zao la kahawa na kupunguza matumizi ya viuatilifu kwenye kahawa kwa takriban asilimia 40.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Serikali haina utaratibu wa kutoa ruzuku ya viuatilifu vya kahawa bali kupitia Taasisi ya Utafiti wa Kahawa (TaCRI) na Bodi ya Kahawa Tanzania imeendelea kuzalisha, kusambaza na kuhamasisha wakulima kubadilisha mikahawa ya zamani kwa kupanda miche mipya ambayo ina ukinzani dhidi ya magonjwa ambapo katika kipindi cha mwaka 2019/2020 hadi 2021/2022 jumla ya miche 41,348,628 imezalishwa na kugawiwa bure kwa wakulima.