Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 26 Youth, Disabled, Labor and Employment Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu 332 2023-05-16

Name

Halima James Mdee

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HALIMA J. MDEE aliuliza: -

Je, tangu kuanzishwa kwa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ni kiasi gani cha fedha kimewekezwa na nini faida na hasara za uwekezaji huo?

Name

Paschal Katambi Patrobas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Halima James Mdee, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2022 kwa hesabu zilizokaguliwa na CAG, thamani ya uwekezaji wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ilikuwa imefikia jumla ya shilingi trilioni 14.4 ambapo Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) ulikuwa umewekeza jumla ya shilingi trilioni 6.03, Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) ulikuwa umewekeza jumla ya shilingi trilioni 7.49 na Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF) Workers Compensation Fund ulikuwa umewekeza jumla ya shilingi bilioni 521.94.

Mheshimiwa Naibu Spika, faida ya uwekezaji huu ni kulinda thamani ya michango ya wanachama na kuhakikisha Mifuko inakuwa endelevu ili kutekeleza majukumu yake ya msingi ya kulipa mafao. Aidha, uwekezaji huu huchangia na kuongeza ajira, mapato ya Serikali kupitia kodi na kuchochea shughuli za uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyo katika uwekezaji wowote kuna vihatarishi (risk) ambavyo vinaweza kusababisha hasara kwa baadhi ya uwekezaji. Hasara zilizojitokeza kwa uwekezaji uliofanywa na Mifuko ni pamoja na kutolipwa kwa wakati kwa mikopo iliyotolewa kwa wanufaika mbalimbali na baadhi ya miradi kutofanya vizuri ikilinganishwa na matarajio yaliyokuwepo wakati wa kubuni miradi hiyo, ahsante.