Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 15 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 188 2023-04-28

Name

Francis Leonard Mtega

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbarali

Primary Question

MHE. FRANCIS L. MTEGA aliuliza: -

Je, lini Serikali itajenga barabara ya mkato kati ya Wilaya za Mbarali na Chunya ili kupunguza gharama za usafiri na kukuza biashara?

Name

Deogratius John Ndejembi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chamwino

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Jimbo la Mbarali, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa umbali kutoka Wilaya ya Chunya hadi Wilaya ya Mbarali kwa kupitia Wilaya ya Mbeya ni mrefu ukilinganisha na umbali wa kupitia barabara ya mkato kati ya Wilaya ya Chunya na Mbarali. Serikali inatambua changamoto ya kutokuwepo kwa barabara hiyo na kusababisha adha ya mzunguko mrefu kwa wananchi wa wilaya hizo mbili ndani ya mkoa wa Mbeya na kusababisha gharama kubwa kwa wananchi wanaosafiri kati ya wilaya hizo mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu wa uhitaji wa barabara hiyo ya mkato, Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Mbeya kupitia kikao chake cha tarehe 09 Januari, 2023, kilitoa mapendekezo kwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi kuipandisha hadhi barabara ya Njiapanda – Sangambi – Shoga na kufungua barabara mpya kutoka Shoga Wilaya Chunya hadi Udindilwa katika Wilaya ya Mbarali inayokadiriwa kuwa kilomita 22.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mapendekezo hayo kuwasilishwa kwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, aliiagiza Kamati ya Kitaifa ya kupanga barabara katika hadhi stahiki (NRCC) kufika mkoani Mbeya na Kamati hiyo ilifika mnamo tarehe 24 Februari, 2023 na kutembelea barabara zilizoombwa kupandishwa hadhi ikiwemo barabara ya Njiapanda – Sang’ambi – Shoga na kipande cha Shoga - Udindilwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo ya Kamati yaliwasilishwa kwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi na yanachambuliwa na uchambuzi ukikamilika taarifa itatolewa. Kama barabara hiyo itakidhi vigezo vya kupandishwa hadhi, itakuwa barabara ya mkoa na itahudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS).