Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 8 Sitting 3 Public Service Management Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 42 2022-09-15

Name

Najma Murtaza Giga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA aliuliza: -

Je, nini Sababu ya kukosekana uwiano wa jinsia ya kike kwenye nafasi za uteuzi na ajira nchini?

Name

Deogratius John Ndejembi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chamwino

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI NA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Najma Murtaza Giga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha kunakuwepo na uwiano sawa wa kijinsia kwenye nafasi za uteuzi na ajira nchini kwa kuweka mazingatio ya usawa wa kijinsia katika nyaraka zinazosimamia Utumishi wa Umma, ikiwemo Sera ya Menejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma ya mwaka 2008 inayotaka kila mamlaka ya ajira kuhakikisha uwiano wa kijinsia katika uteuzi na ajira zote. Pia Sheria ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2019, Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma ya Mwaka 2009 pamoja na Kanuni za Uendeshaji wa Shughuli za Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma ya Mwaka 2021.

Mheshimiwa Spika, hatua hizi zimeiwezesha Serikali kuwa kwenye nafasi nzuri ya kufikia uwiano sawa wa kijinsia katika nafasi za Uteuzi na ajira nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua kuwa suala hili ni kipaumbele cha Dunia kupitia ajenda 2020/2030 kuhusu Maendeleo Endelevu, Lengo Na. 5 Usawa wa Kijinsia, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameazimia kuhakikisha uwepo wa uwiano sawa wa kijinsia katika nafasi mbalimbali za uteuzi katika kipindi chake cha uongozi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, hivyo, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora iko katika hatua za mwisho za kutoa Mwongozo wa Ujumuishwaji wa Jinsia katika Utumishi wa Umma. Mwongozo huu unatoa maelekezo kwa mamlaka za ajira katika utumishi wa umma kote nchini kuhakikisha kuwa wanawake na wanaume wanakuwa na fursa sawa kuanzia katika mchakato wa ajira, upandishaji madaraja, uteuzi, mafunzo, ubadilishanaji pamoja na urithishaji madaraka. Lengo likiwa ni kuondoa vikwazo kwa kujenga uwezo wa ushindani kwa jinsia zote ili kupata sifa stahiki za kushika madaraka na fursa mbalimbali.