Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 6 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 64 2021-11-09

Name

Eng. Ezra John Chiwelesa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu kwa wananchi wanaozunguka Hifadhi ya Burigi – Chato ili waache kuingiza Mifugo ndani ya Hifadhi na kumaliza mgogoro kati ya wananchi hao na Hifadhi hiyo?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI, MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia TANAPA imeendelea kutoa elimu ya uhifadhi kwa wananchi wanaoishi maeneo yanayozunguka Hifadhi ya Taifa ya Burigi - Chato. Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2020/2021 jumla ya shilingi 20,836,200 zilitumika kutoa elimu ya uhifadhi katika vijiji 37, ambapo katika Wilaya ya Biharamulo elimu hiyo ilitolewa kwa vijiji sita vya Kiruruma, Nyabugombe, Ngararambe, Kabukome, Katerela na vya Kitwechembogo.

Aidha, kwa mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga jumla ya Shilingi Milioni 96.7 kwa ajili ya utoaji wa elimu ya uhifadhi katika maeneo ya vijiji 38 vinavyopakana na hifadhi hiyo vikiwemo vijiji 10 vya Wilaya ya Biharamulo.

Mheshimiwa Spika, sambamba na utoaji wa elimu kwa vijiji, Serikali imejipanga kutumia makundi maalum wakiwemo viongozi wa dini, wanasiasa na wanafunzi wa shule za msingi na sekondari ili waweze kusaidia katika kuelimisha faida za uhifadhi.
Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)