Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 6 Water and Irrigation Wizara ya Maji 79 2021-02-09

Name

Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Primary Question

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE Aliuliza:-

Je, lini utekelezaji wa mradi wa maji kwa vijiji 57 vya Wilaya ya Kyerwa utaanza kwa kuwa usanifu wa kina wa mradi huo umeshakamilika?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sebba Innonent Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kukabiliana na changamoto za upatikanaji wa huduma ya maji katika Wilaya ya Kyerwa, Serikali katika mwaka wa fedha 2019/2020 kupitia Programu ya PforR na Programu ya Malipo kwa Matokeo (PBR) imetekeleza miradi ya maji katika vijiji vya Nkwenda, Rugasha, Kitwechenkura, Kaikoti, Rwensinga, Kagenyi pamoja na sehemu ya Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya Kyerwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kwa mwaka huo, ukarabati wa visima virefu na vifupi umefanyika katika vijiji vya Kibale, Nyamiaga, Magoma, Rutunguru, Kihinda, Rwenkende, Kyerwa, Mirambi na Nyakakonyi ambapo wananchi wapatao 51,025 wananufaika na huduma ya maji safi. Utekelezaji wa miradi katika vijiji tajwa hapo juu ni sehemu ya utekelezaji wa miradi katika vijiji 57.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha vijiji vilivyobaki kati ya 57 vya Wilaya ya Kyerwa vinapata huduma ya maji, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni 1.56 kwa ajili ya ujenzi wa miradi ya maji katika vijiji 12 vya Runyinya, Nkwenda, Nyamweza, Rwabwere, Karongo, Iteera, Muleba, Chanya, Muhurile, Kimuli, Rwanyango na Chakalisa. Pia vijiji hivi viko ndani ya mradi wa vijiji 57.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka wa fedha 2021/ 2022, Serikali itaendelea kutekeleza ujenzi wa miradi ya maji katika vijiji 35 vilivyobaki ili kukamilisha utekelezaji wa mradi wa vijiji 57. (Makofi)