Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 50 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 430 2019-06-21

Name

Mbarouk Salim Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Wete

Primary Question

MHE. MBAROUK SALIM ALI aliuliza:-

Je, ni mafanikio gani yameweza kupatikana katika kushirikisha jamii katika jitihada za usimamizi wa maliasili nchini?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbarouk Salim Ali, Mbunge wa Wete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, dhana ya Ushirikishwaji wa Jamii katika Usimamizi wa Misitu nchini (Participatory Forest Management) inatekelezwa katika nyanja kuu mbili: Kuwashirikisha wananchi katika usimamizi wa misitu iliyopo kwenye ardhi ya vijiji (Community Based Forest Management) na kuwashirikisha wananchi katika kusimamia hifadhi ya misitu kwa ubia na Serikali (Joint Forest Management). Madhumuni ya dhana hii ni kuwapa fursa wananchi kushiriki katika usimamizi na uhifadhi endelevu wa rasilimali za misitu iliyopo katika maeneo yao hali wakiboresha maisha yao kupitia mapato mbalimbali yanayopatikana kutokana na misitu iliyopo katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu zinaonyesha jumla ya hekari milioni 7.7 zimehifadhiwa kupitia dhana hii ya ushirikishwaji wa jamii. Aidha, dhana hii imesaidia sana katika kupunguza matukio ya uharibifu wa misitu kama ukataji wa misitu hovyo, uchomaji wa mkaa holela na matukio ya moto yaliyokuwa yakifanyika katika misitu husika katika misitu ya hifadhi ya mazingira asilia (nature reserves). Ushirikishwaji huu umekuwa ni nyenzo muhimu ya kufanikisha ustawi wa misitu ambayo mingi kati ya hiyo ni misitu ya lindimaji (catchment forest).

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo faida mbalimbali ambazo jamii husika imefaidika kupitia dhana hii ikiwepo kupata msamaha wa mirahaba ya Serikali juu ya mazao ya misitu, kubakiza asilimia 100 ya mapato yatokanayo na mauzo ya mazao ya misitu japokuwa kodi zingine kama kodi ya mapato, Kodi ya Ongezeko la Thamani zimeendelea kulipwa, kubakiza tozo ya faini mbalimbali na utaifishaji wa mazao ya misitu na vifaa kutokana na uvunaji haramu katika misitu ya hifadhi ya kijiji. Aidha, sehemu ya fedha zinazopatikana zimetumika katika shughuli za maendeleo ya vijiji kama kujenga vyumba vya madarasa, zahanati, nyumba za watumishi, walimu na waganga, kutengeneza madawati na kuchimba visima. Vilevile sehemu nyingine ya fedha hiyo imeendelea kutumika katika shughuli za usimamizi wa misitu ikiwemo kununua vifaa vya walinzi wa misitu hiyo ikiwemo sare, buti, filimbi, baiskeli na kadhalika.