Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 2 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 28 2019-09-04

Name

Sabreena Hamza Sungura

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SABREENA H. SUNGURA aliuliza:-

Je, ni muda gani mchakato wa kuandaa hatimiliki unatakiwa kukamilika kwa mujibu wa sera na taratibu?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sabreena Hamza Sungura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na kuthamini umuhimu wa kuwapatia wananchi hatimiliki kwa muda mfupi, Wizara yangu pamoja na uwepo wa sera na sheria za ardhi inao Mkataba wa Huduma kwa Mteja (Client Service Charter) ambao unaweka bayana kuwa ndani ya siku thelathini tangu nyaraka zifikishwe Ofisi ya Kanda kutoka Halmashauri, hatimiliki husika inapaswa kuwa imekamilika kwa hatimiliki za kawaida (analog system). Aidha, kwa upande wa hatimiliki zitolewazo kwa njia ya mfumo unganishi wa kielektroniki (ILMIS) ulioanza kufanya kazi katika Wilaya ya Kinondoni na Ubungo, hatimiliki inapaswa kuwa imekamilika ndani ya siku saba tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu ndiyo imepewa dhamana ya kusimamia utekelezaji wa sheria za ardhi ambapo pamoja na mambo mengine inahakikisha kuwa wananchi, taasisi, makampuni au mashirika yanamilikishwa rasilimali hii adhimu ya ardhi kwa kupatiwa nyaraka za umiliki. Nyaraka hizo ni Hati ya Hakimiliki ya Kimila ambayo hutolewa kwa ardhi ya kijiji na Hatimiliki ya kupewa ambayo hutolewa kwa ardhi ya kawaida na ya hifadhi. Hati hizi zikishasajiliwa hukabidhiwa kwa wahusika ili wazitumie katika kujiletea maendeleo na kuwahakikishia usalama wa miliki zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa rai kwa watumishi wa sekta ardhi nchini kuhakikisha kuwa wanakamilisha taratibu zote za umilikishaji kwa wakati. Aidha, napenda kuwahakikishia wananchi wote kuwa Wizara yangu itaendelea kuboresha taratibu za utoaji wa huduma hii muhimu ikiwemo kupunguza muda wa upatikanaji wa Hatimiliki na kuwasogezea huduma katika ngazi za mikoa.