Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 20 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 169 2017-05-09

Name

Zainabu Nuhu Mwamwindi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAINABU N. MWAMWINDI aliuliza:-
Gereza la Wilaya ya Iringa ambalo lipo jirani na Hospitali ya Mkoa wa Iringa limekuwa likisababisha usumbufu kwa wananchi wanaotembea kwa miguu hasa nyakati za usiku.
Je, Serikali ina mpango gani kwa kuondoa mwingiliano wa shughuli za kijamii na shughuli za gereza hilo?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainabu Nuhu Mwamindi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifutavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli yalikuwepo malalamiko ya wananchi kupata usumbufu wa kuingia na kutoka Hospitali ya Mkoa wa Iringa ambapo barabara ya kuingia inapita mbele ya lango la Gereza la Iringa. Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Iringa katika kutafuta ufumbuzi wa tatizo hilo, hasa baada ya kufungwa kwa barabara inayopita mbele ya gereza kuelekea hospitalini kwa watumiaji wa magari ilikutanisha uongozi wa Manispaa ya Mkoa wa Iringa na uongozi wa Jeshi la Magereza mkoani humo na kutoa maangizo yafuatayo:-
Moja, uongozi wa Manispaa ya Iringa kuandaa barabara mbadala itakayotumiwa na wananchi wanaokwenda hospitalini kwa kutumia gari; pili, uongozi wa Manispaa uandae ramani ya ukuta utakaozuia matumizi ya barabara inayopita gerezani kwa kutumia gari. Ukuta huo ulilengwa kuzuia magari kutoka eneo ambalo waenda kwa miguu wangepita bila kuingilia shughuli za gereza; na tatu, baada ya kupatikana ramani, uongozi wa gereza ulitakiwa kujenga ukuta huo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Magereza tayari limeshatekeleza maagizo hayo kwa kujenga ukuta unaotenganisha barabara ya watembea kwa miguu wanaokwenda hospitali kwa kutumia eneo la mbele ya gereza ili wasiingiliane na shughuli za gereza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Halmashauri ya Manispaa ya Iringa imeshatekeleza agizo la kujenga barabara mbadala inayotumiwa na wananchi wanaokwenda hospitalini na magari. Hata hivyo, pamoja na kujengwa kwa barabara mbadala, gereza limeendelea kuruhusu magari yanayokwenda hospitalini kutumia barabara hiyo mbele ya gereza kwa wakati wa dharura.