Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 14 Sitting 11 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 191 2024-02-13

Name

Godwin Emmanuel Kunambi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlimba

Primary Question

MHE. GODWIN E. KUNAMBI aliuliza: -

Je, lini Serikali itarejesha eneo lililokuwa linamilikiwa na RUBADA kwa wananchi wa Utengule – Mlimba?

Name

Geophrey Mizengo Pinda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kavuu

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Godwin Emmanuel Kunambi, Mbunge wa Mlimba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shamba Namba 949 linalojulikana kwa jina la Ngalimila lina ukubwa wa hekta 5,128.483 (sawa na ekari 12,820). Shamba hili lipo Mkoa wa Morogoro katika Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba katika Kata ya Utengule. Shamba hili limezungukwa na Vijiji vya Ngalimila, Ipugasa, Ngombo, Mpanga, Miembeni na Viwanja Sitini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya mwaka 2009 ardhi hii ilikuwa inamilikiwa na Kijiji cha Ngalimila ambapo tarehe 18 Mei, 2009 kilifanyika kikao maalum kwa ajili ya kujadili maombi ya ardhi kwa ajili ya RUBADA kutoka kijiji cha Ngalimila kwa ajili ya uwekezaji. Wanakijiji walikubali kutoa ardhi hiyo kutokana na manufaa ambayo walielezwa yangepatika na kutokana na uwekezaji mkubwa katika kilimo cha mpunga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 16 Aprili, 2014 iliandaliwa taarifa ya kusudio la kuhaulisha ardhi ya kijiji kuwa ya kawaida. Baada ya RUBADA kufutwa, mali mbalimbali ikiwemo shamba la Ngalimila zilirejeshwa Wizara ya Fedha na Mipango na kuwa chini usimamizi wa Ofisi ya Msajili wa Hazina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufuatia ardhi ya shamba hili kutoendelezwa kwa muda mrefu, Serikali ilipokea maombi ya wananchi kurejeshewa shamba hili. Hata hivyo, uchambuzi wa maombi hayo ulibaini kuwa eneo lenye ukubwa wa hekta 1,820.494 sawa na asilimia 35 ya shamba hilo lipo katika eneo la Pori Tengefu la Kilombero. Aidha, ili kufika katika shamba hili, sharti kuvuka Mto Mpanga na Mto Mnyera ambayo ndiyo chanzo cha kupeleka maji katika mradi wa ujenzi wa bwawa la kuzalisha umeme wa maji wa Julius Nyerere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa rai kwa wananchi wanaotumia shamba hili kwa sasa ambao ni wavamizi kutokuweka miundombinu ya kudumu ili kuepusha hasara inayoweza kujitokeza endapo Serikali itatoa maamuzi tofauti na maombi yao. Aidha, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa suala hili litashughulikiwa na kutolewa maamuzi kwa uharaka unaohitajika kwa maslahi mapana ya jamii na Taifa kwa ujumla, ahsante. (Makofi)