Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 14 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2024-02-01

Name

Anatropia Lwehikila Theonest

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Napongeza uthubutu wa Serikali kubadilisha mitaala kwa lengo la kuboresha elimu, lakini tutambue pia kwamba katika shule, muda ni wa msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyoongea leo, kuna changamoto kubwa ya vitabu havijawafikia walengwa. Printing ya vitabu lakini pia vitabu kwenye shule wametumiwa softcopy, sasa vijijini watazitumiaje? Pia elimu haijafika. Naomba kujua mkakati wa Serikali, wakiangalia umuhimu wa muda, kwa sababu leo ni mwezi umetimia, shule zimefunguliwa. Ni upi mkakati wa haraka wa kuhakikisha vitabu vinafika na elimu inafika kwa wakati ili watoto waweze kupata elimu hiyo kwa wakati?

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali na kupokea ushauri kutoka kwa Mheshimiwa Anatropia. Kwanza nimhakikishie kuwa tumeendelea kuzalisha vitabu kulingana na mahitaji ya mtaala tulionao. Wakati huu tunapoanza kufundisha kwa Sera mpya ya Elimu kwenye mitaala mipya, kwenye mipango yetu ya bajeti, ndiyo tumesema tumeanza awamu kwa awamu. Hatukuanza full string, yaani hatukuanza madarasa yote. Tumeanza na awali, darasa la kwanza, darasa la tatu, na kidato cha kwanza kwa sekondari.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tumeanza hivyo ili kujipa uwezo wa kupata vifaa, miundombinu ikiwemo na vitabu vya kujifunzia na kufundishia. Mkakati huu kama nilivyosema mwanzo kwamba tunaendelea kuongeza uwezo wa Serikali kibajeti kila mwaka ili kusheheneza maeneo haya, kumfanya mwanafunzi aweze kuipata ile elimu na aendelee nayo hata kule mwisho anapopimwa, apimwe akiwa ana uelewa na mahali pa kupata vitabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Wizara ya Elimu imeweka mpango wa kuimarisha elimu ya TEHAMA ambayo pia itasaidia wanafunzi kupata taaluma hiyo kupitia mitandao yetu na kumwezesha kuwa na uwanda mpana wa kupata elimu kwa vitabu ambavyo tunapeleka, na hata kwenye mitandao ili iweze kumsaidia kuelewa zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, huo ndiyo mpango wetu wa Serikali.

Additional Question(s) to Prime Minister