Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 14 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2024-02-01

Name

Husna Juma Sekiboko

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Mheshimiwa Waziri Mkuu, elimu, hasa kwa upande wa mtaala mpya kwa maana ya amali, ni jambo mtambuka. Baada ya utekelezaji wa mtaala, wanafunzi watakaohitimu watahitaji kuwezeshwa kwenye sekta nyingine, kwenye maeneo kama TAMISEMI, kilimo, afya na maeneo mengine hasa ya ufundi: Ni kwa vipi Serikali inajiandaa kuweka mazingira wezeshi kwa ajili ya watoto watakaohitimu upande huo wa amali?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sekiboko, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo hili, kwanza nataka kutoa uelewa kwamba tunapotekeleza Sera yetu mpya ya Mitaala, hatuendi moja kwa moja na madarasa yote, tunaanza na makundi machache. Wanaoanza kufundishwa mwaka huu wa 2024 kama tulivyosema tunaanza mwezi Januari, ni darasa la awali, darasa la kwanza na darasa la tatu. Kwa sababu kwenye Elimu ya Msingi tuna makundi matatu; tuna awali, halafu darasa la kwanza na la pili; kundi la tatu, ni darasa la tatu na darasa la sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wanaoanza kufundishwa mtaala mpya ni awali, darasa la kwanza na darasa la tatu. Tunaanza nao mwaka huu. Hiyo ni kwa Shule za Msingi. Kwa upande wa Sekondari, tunaanza na Kidato cha Kwanza. Pia kwa Sekondari, tunajua tuna elimu jumla na kuna zile shule za ufundi. Kwa hiyo, tumechagua Shule za Ufundi, siyo zote, chache ambazo tayari zina miundombinu na walimu wa kuanzia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa utaratibu huu, utawezesha sasa Serikali kujipanga kupitia Bajeti yetu kuweza kumudu kuongeza pia hata idada ya walimu, kununua vifaa ili kufanya utekelezaji huu wa sera kuwa endelevu. Mwaka huu tunapoanza na awali na darasa la kwanza, darasa la pili hawahudhurii, wanaanza darasa la tatu, tunamfanya kijana wa awali anapohitimu, anapokwenda darasa la kwanza, anaendelezwa. Darasa la pili hapati, lakini anaanzia darasa la tatu, huyu wa darasa la kwanza anakuwa darasa la pili. Kwa hiyo, utakuta awali mpaka darasa la pili itakuwa endelevu kuanzia mwakani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kila mwaka tutakuwa tunaenda hivyo. Yule wa darasa la tatu anaenda la nne, la tano, mpaka la sita, mwisho wa Elimu ya Msingi. Utakuta sasa tunaweza ku-cover maeneo yote, kila mwanafunzi anapata elimu hiyo vizuri. Wizara ya Elimu sasa itajitahidi, itapangilia mtihani kulingana na muda waliosoma masomo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunawezaje kuimarisha eneo hili? Ni pale ambapo bajeti sasa tutakuwa tunaiimarisha, kwanza kuongeza miundombinu ya majengo ya kusomea, vifaa vinavyohitajika, na walimu wenye uwezo wa fani hizo. Kwa hiyo, kila mwaka tutakuwa tunaongeza uwezo wetu. Serikali tumejipanga vizuri kuhakikisha kwamba tunaweza kufanikiwa hayo ili sera hii mpya iweze kutekelezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, huo ndiyo mpango wa Serikali uliopo. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister