Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 38 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2023-06-01

Name

Ally Mohamed Kassinge

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Primary Question

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Mheshimiwa Waziri Mkuu Serikali imekuwa ikitekeleza sera yake ya elimu bila malipo au maarufu kama elimu bure kwa misingi ya kuwapunguzia gharama wazazi au walezi wa vijana ambao wanasoma katika shule zetu za sekondari hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo bado kumekuwa na michango kadhaa katika shule zetu za umma, ikiwemo michango ya ulinzi, shajara pamoja na chakula;

Je, Serikali haioni umuhimu wa kupitia upya sera hii ili hii michango ambayo nimeainisha ambayo kimsingi inabebwa na wazazi au walezi iwe ni jukumu la Serikali kwa dhana ile ile ya kuwapunguzia gharama wazazi au walezi wa vijana wetu?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini na mkuu wa wilaya mstaafu kama ifuatavyo: - (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutekeleza Sera ya Elimu bila Bila Ada kwa lengo la kuwaondolea adha wazazi ya kuwa na michango mingi na ile michango holela, michango holela. Kila mwezi Serikali yetu inapeleka fedha kwenye halmashauri kwa ajili ya kuwezesha shule zetu za Sekondari, wale wakuu wa shule na uongozi wa shule kuweza kutumia kwenye maeneo ambayo walikuwa wanatarajia sana kupata michango kutoka kwa wazazi ili wazazi wasichangie maeneo hayo na badala yake wazazi waendelee kusimamia maboresho ya mtoto mwenyewe kwenda shule kwa kumnunulia sare, viatu na vitu vingine.

Mheshimiwa Spika, natambua kwamba si maeneo yote yameweza kupata fedha hii hasa eneo la chakula na ulinzi, kama ulivyoeleza. Maeneo haya ambayo tumetolea fedha ni yale maeneo ambayo yanafanya ukarabati mdogo mdogo wa majengo yanayoharibika, vifaa vya kufundishia na kujifunzia, vitabu, chaki na vitu vingine ili kuondoa adha ya waalimu kuwachangisha wazazi fedha.

Mheshimiwa Spika, eneo ambalo sasa tunaendelea kushughulika nalo ni maboresho sasa. Tunazo shule nyingi za sekondari ambazo wanafunzi wanaenda asubuhi na kurudi jioni na wanapokuwa shule hawapati chakula. Nikiri kwamba eneo hili Serikali bado tunaendelea kuchakata ili tuone namna nzuri ya kutoa huduma ya chakula shuleni; ingawa tumeona sekta binafsi zinashiriki, wakati mwingine wazazi wenyewe wanaweka mpango wao.

Mheshimiwa Spika, sasa, niliposema michango holela; Tunayo ile michango holela ambayo labda waalimu wanasema njoo kesho na shilingi mia mbili, elfu moja, mia tano, ambazo zinakera kwa wazazi. Hiyo tumeidhibiti na tumepiga marufuku na haipo kabisa na kama ipo, tumeshatoa maelekezo na hapa pia nitatoa maelekezo. Sisi tunaruhusu michango rasmi inayokwenda kufanya shughuli za maendeleo. Shule za msingi, shule za sekondari hizi ni shule za wananchi. Kila kijiji kina shule ya msingi na kinasimamiwa na kijiji chenyewe, na tumeunda kamati ya shule kwa shule za msingi. Sekondari ziko kwenye kata, tumeunda bodi ya shule na inamilikiwa na kata kwenye vijiji vitatu, vinne au vitano, wanasimamia na Mtendaji wa Kata ndio kiongozi wetu anayesimamia maendeleo ya shule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inapotokea labda choo kimebomoka hatuzuii wazazi kukaa na kukijenga kwa kuchangia na kujenga hiyo ni michango ya maendeleo. Ingawa michango hii pia tumeiwekea masharti kidogo kwamba anayetakiwa kusimamia michango hii ni mkuu wa wilaya pekee au yeyote ambaye mkuu wa wilaya amemchagua kusimamia. Tunaogopa sasa watu kuchangisha kule holela na ndiyo kwa sababu nilisema michango holela. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo basi Serikali inaendelea kufanya mapitio ya sera hii ili kuwezesha mzazi kupata unafuu zaidi wa kutoa michango kwa ajili ya maboresho ya shule zetu. Lakini pia bado hatuondoi nafasi ya uwajibikaji wa wananchi kwenye shule zao katika kufanya maboresho. Na niliposema mkuu wa wilaya mstaafu najua hili umelisimamia vizuri sana ulipokuwa mkuu wa wilaya kabla hujawa Mbunge na kwa hiyo Serikali tunaendelea kusimamia haya.

Mheshimiwa Spika, nitoe wito kwa wakuu wa wilaya wote nchini, kwenye halmashauri zao kusimamia kutokuwepo kwa michango holela inayokera wananchi na kushindwa kufanya shughuli nyingine na badala yake kuwa wanasababisha wanafunzi wanaondolewa shuleni; hiyo tulishapiga marufuku kabisa. Lakini pia Wakurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha kwamba wanatuhudumia hizi shule lakini na kuweka mpango mzuri kwenye maeneo ambayo yanahitaji pia Halmasjhauri isimamie kupitia bajeti zao, kama ni lazima kuzungumza na wazazi lakini wazazi wenyewe kupitia kamati zao wafanye maamuzi haya ndiyo ambayo kwa sasa tunayasimamia. Lakini niwahakikishie tu kwamba ombi la Mheshimiwa Mbunge la kufanya maboresho ya sera yetu hayo tumepokea na tunayafanyia kazi, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister