Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 23 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 9 2023-05-11

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Primary Question

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba risala ya Serikali kuhakikisha kwamba inatatua migogoro kati ya wananchi na maeneo yenye hifadhi za Serikali. sasa ningependa kujua nini mkakati wa Serikali kukomesha migogoro hii katika maeneo haya niliyoyataja?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Waitara Mbunge wa Tarime, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waitara analizungumza hili akijua kwamba tumelifanyia kazi sana pia kwenye eneo lake ambako kuna mgogoro wa wananchi na hifadhi; na tulliunda timu ya mawaziri walienda kwenye eneo lake. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie, kwamba mkakati wa Serikali wa kukomesha haya ni kushirikisha wananchi kwenye maeneo haya yote ambayo yamejitokeza na migogoro hii ili kuwa na mapitio ya pamoja ya mipaka ilipo kila mmoja ajue mpaka upo wapi. Serikali tumeagiza mamlaka hizi za hifahdi kuweka vigingi kama alama inayoonesha pande zote mbili kwamba hapa ndio ukomo wa watu kuingia kwenye upande mwingine; na vigingi hivi navyo tumesema viwe virefu siyo vile vidogodogo kirefu wapake rangi nyeupe kionekane kwa mbali ili kila mmoja apate kuelewa. Sasa jukumu hili tunapolifanya kwa kushirikiana pamoja tunaamini migogoro itapungua kwa sababu kila mmoja atakuwa anajua.

Mheshimiwa Spika, siku tatu/nne zilizopita hili limejitokeza sana kule Tarime ambako kata kadhaa na vijiji kadhaa kulikuwa na mgongano wa kutoeleweka kwa mipaka yake, na hili pia tumeona hata juzi siku mbili zilizopita kwa kutoelewana viongozi wa Serikali za vijiji walijiuzulu. Nafurahi kusikia pia jana viongozi wa Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Tarime wameenda kuwatembelea wananchi wamewaelimisha. Nawashukuru sana viongozi wale kwamba wamerudi kwenye nafasi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie wananchi wale ambao wako kwenye migogoro si Tarime lakini maeneo mengine yote, Serikali tunajipanga kufanya mapitio ya maeneo yote ili kuhakikisha kwamba hii migogoro haijirudii, lakini kila mmoja anakuwa na uelewa kwa kushirikisha na viongozi wale ambao wamerudi moja kati ya taarifa ambazo tumezipata ni kwamba wanahitaji kupata taarifa zaidi. Kwa ile Timu ya Mawaziri iliyoenda inakamilisha taarifa yake wataileta kwangu, tutaipitia kwa pamoja, tutashirikisha kwanza ndani ya Serikali, tutakwenda sasa Mkoa Mara, Wilayani Tarime mpaka kwenye vile vijiji. Tutakuwa na mikutano kwenye vile vijiji vya kuendelea kuelimisha zaidi kwa ukaribu na kuwashirikisha ili kila mmoja awe anajua. Sisi ndani ya Serikali tunaamini kwamba vijiji vyote, wananchi wote wanaoishi pembezoni mwa mipaka hii ya hifadhi watakuwa walinzi nambari moja wa kulinda hifadhi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tutawajibika kwenda kutoa elimu maeneo yote. Tunajua hata hapa Kondoa kuna Pori la Mkungunero lina mgogoro, Babati, eneo la Tarangire lina mgogoro. Tunaambiwa Bunda pale katikati, katika ya Daraja na Mji wa Bunda pale kuna eneo lina mgororo, Serengeti nako pia kuna mgogoro. Haya maeneo yote tutayapitia eneo moja baada ya moja, tutakutana na wananchi, tutawaelemisha. Tunataka Watanzania tuone umuhimu wa hifadhi, lakini na sisi wahifadhi tuone umuhimu wa raia wanaokaa pembezoni mwa hifadhi. Tukiwa na dhana hii itatusaidia sasa kutunza rasilimali zetu popote zilipo kwa pamoja zaidi, wananchi pamoja na miundombinu tuliyonayo ndani ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa swali hili na huo ndio ufafanuzi wangu. Ahsante. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister