Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 23 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2023-05-11

Name

Aysharose Ndogholi Mattembe

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuumuliza swali Waziri Mkuu. Kila ifikapo tarehe 15 Mei ni Siku ya Maadhimisho ya Familia Duniani. Kwa sasa jamii inapita katika wakati mgumu sana kutokana na mmonyoko wa maadili na ukiukwaji wa haki za wanawake na watoto.

Je, ni nini mkakati wa Serikali wa kuitumia siku hii kama sehemu ya kuielimisha jamii na kuhamasisha umuhimu wa malezi bora pamoja na maadili ili kukabiliana na changamoto hiyo?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asharose Mattembe, Mbunge wa Mkoa wa Singida kama ifuatanyo: -

Mheshimiwa Spika, tunalo tatizo na changamoto ya ukiukwaji wa maadili kwenye maeneo mengi kwa watoto wadogo, wanawake wakati mwingine hata wanaume nao wanaonewa; hayao yote ni mmomonyoko wa maadili na Serikali tuko mstari wa mbele kukemea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, dunia iliamua kuwa na siku moja maalumu ya kuelimisha umma juu ya kila mmoja kuhakikisha kwamba tunapiga vita mmomonyoko wa maadili lakini pia ukatili wa kijinsia na watoto vilevile, na sisi Tanzania tumejiunga kwenye siku hiyo. Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge anataka kujua Serikali tumejipangaje? Na sisi pia tunasheherekea siku hiyo, siku hiyo pia tunakutana, siku hiyo pia tunatoa elimu kwa umma ya namna ya kila mmoja kushiriki katika kuhakikisha kwamba nchi hii mila zetu, desturi zetu utamaduni wetu lakini maadili ya nchi hii yanazingatiwa ili kupata kizazi ambacho kitakuwa endelevu katika sekta mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kwamba tumejipangaje siku hii; tunajua tarehe 15 ni siku tatu nne zijazo, nitoe agizo kwa wakuu wa mikoa na wakuu wa wilaya chini ya usimamizi wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia pamoja na TAMISEMI kila mkoa upange mpango thabiti wa kuwaleta pamoja wananchi kwenye siku hiyo ili haya ninayoyasema yaweze kutekelezwa. Kwanza tutoe elimu, tutoe makaripio lakini pia tuonyeshe dira ya nchi ya umuhimu wa kukinga mmomonyoko wa maadili hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa kufanya hivyo sasa huu ndio mkakati ambao tunaweza kuutumia. Lakini mkakati huo hauishii tarehe 15 tu, hili suala la kukemea kukiukwa kwa maadili na mmomonyoko ni suala endelevu kwa hiyo wakuu wa mikoa nawaagiza tena, wakuu wa wilaya nawaagiza tena. Tunataka ishuke mpaka kule chini maafisa tarafa, watendaji wa kata, vijiji mpaka vitongojini. Ni muhimu sana Taifa hili tulilinde kwa kuwa na maadili mema, tuendeleze utamaduni wetu na mila na desturi zetu ili kujenga kizazi kipya ambacho kitakuwa endelevu kwa nchi hii na wataweza kufanya kazi yao vizuri.

Mheshimiwa Spika, huo ndio mkakati wa Serikali wa namna ya kuitumia vizuri tarehe 15 mwezi wa tano siku hii ya kupinga mmomonyoko wa maadili.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister