Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 23 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2023-05-11

Name

Emmanuel Peter Cherehani

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ushetu

Primary Question

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kumekuwa na malalamiko makubwa sana hapa nchini kwa ndugu zetu wafugaji waliotaifishiwa na kuuziwa ng’ombe wao katika hifadhi zetu, na wakaenda Mahakamani wameshinda kesi na Mahakama ikaamuru Serikali iwarejeshee mifugo yao hawa wananchi, sasa Serikali imekaa kimya. Nini kauli ya Serikali juu ya suala hili?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Cherehani Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, natambua kuwepo kwa migogoro mingi kati ya wafugaji na wakulima, wafugaji na maeneo ya hifadhi. Wiki moja iliyopita siku ya Alhamisi nilikuja hapa mbele yako kutoa ufafanuzi wa kero hii ambayo inagusa maeneo yote kwa wafugaji, wakulima lakini pia maeneo yetu ya hifadhi, nilitolea kauli hapa, hili ni eneo moja kati ya maeneo ambayo nilitolea kauli. Tunatambua na tunajua kwamba tuna kesi nyingi ambazo wafugaji wameweza kupeleka Serikali Mahakamani au hifadhi imepeleka wafugaji Mahakamani. Kwa kuwa jambo hili ni la kisheria sana na lina sheria zake, pale ambapo imeamriwa ni lazima tutekeleze kwa sababu hakuna ambaye anaweza kupinga amri ya Mahakama.

Mheshimiwa Spika, kama imetokea kuna mahali hukumu imetoka, Mahakama imeamua, halafu hakuna aliyetekeleza jambo hili tunaweza kupata taarifa ni wapi huko ili tuwaambie Serikali watekeleze mara moja kwa sababu ni hukumu na hatuwezi kupinga Mahakama. Lakini pia nitoe wito pale ambapo kuna migogoro ya aina hii Mahakama imetoa maamuzi yake uko utaratibu, kama eneo moja hilo iwe wafugaji au hifadhi hawajaridhika ni kukata rufaa badala ya kupinga moja kwa moja kutotekeleza amri hiyo.

Mheshimiwa Spika, Kwa hiyo nitoe wito kwenye maeneo yote ambayo yana amri hii lazima tuheshimu mamlaka ya Mahakama na tutekeleze maamuzi ya Mahakama. Kwa kufanya hivyo tutajenga mshikamano zaidi kwenye mihimili yetu hii mitatu ambayo pia inafanyaka kazi kwa kuheshimiana na tunaenda vizuri. Kasoro kama hizo, tukipata mahali kuna tatizo hilo basi Mheshimiwa Mbunge atujulishe ili tuchukue hatu ili tuweze kuhakikisha kwamba kila mmoja anapata haki yake kupitia chombo kinachosimamia haki, ambayo ni Mahakama.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister