Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 23 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2023-05-11

Name

Ramadhan Suleiman Ramadhan

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Chake Chake

Primary Question

MHE. RAMADHAN SULEIMAN RAMADHAN: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, siku za hivi karibuni kumekuwa na taarifa ya baadhi ya balozi zimetangaza kwamba zitafunga ofisi zake hapa Tanzania ikiwemo Balozi ya Denmark na tumepata wasiwasi taarifa hizi zimefika mbali zaidi kwamba hakuna mahusiano mazuri baina ya Tanzania na balozi hizo. Ni ipi kauli ya Serikali juu ya jambo hili?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ramadhan Suleiman Ramadhan, Mbunge wa Chakechake, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Tanzania inayo mahusiano na nchi mbalimbali za kibalozi na tumefungua ofisi kwenye nchi hizo. Lakini na nchi rafiki nazo zimekuja kufungua balozi hapa Tanzania na hiyo Denmark ni miongoni mwa nchi ambazo zina ubalozi hapa na sisi pia kwenye nchi zao.

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie kwamba Tanzania ina mahusiano mazuri sana na Denmark ya kidiplomasia, tumejikita kwenye siasa lakini pia kiuchumi, tunafanya biashara, tuna wawekezaji pia wako hapa nchini na Watanzania wachache waliowekeza nchini Denmark wanaendelea na shughuli zao. Balozi wa Denmark aliyepo nchini Tanzania ameendelea kufanya kazi yake na hana matatizo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa bahati nzuri sana wiki mbili zilizopita tumekuwa tukifanya mawasiliano na Waziri Mkuu wa Denmark juu ya maboresho ya mahusiano haya. Ni kweli Dernmark imebadilisha sera zao, sera za nchi na nchi, kwamba wanakusudia kupunguza baadhi ya ofisi kwenye Bara la Afrika kwa lengo la kufikia malengo ya sera yao. Sera yao wanasema wanajikita zaidi kwenye nchi ambazo hazina usalama, nchi ambazo zina tatizo la kiusalama; Tanzania ni nchi salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya pia tulipata nafasi ya kuzungumza na Mheshimiwa Balozi wa Denmark hapa nchini, alieleza haya na sisi tuliendelea kuonesha faida inayopatikana kwa nchi zote mbili kwa mahusiano haya na wanakusudia kufanya hivyo mwaka 2024, bado wako kwenye mchakato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi kupitia Wizara ya Mambo ya Nje, kupitia viongozi wakuu yako mazungumzo yanaendelea kubadilisha mwelekeo huo ili waendelee kubaki na pawe na ofisi nchini Tanzania na sisi tuwe na ofisi Denmark ili tuendelee kuimarisha mahusiano yetu kwa ukaribu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunataka tuone shughuli zetu zote ambazo ziko kwenye makubaliano yetu zinaendelea kama zilivyo. Kwa kuwa mazungumzo yanaendelea basi tuna matumaini kwamba Denmark watatusikiliza Tanzania na watabaki nchini na sisi tuendelee kushirikiana nao na tuendelee kunufaika na yale yote yanayopatikana kupitia shirika lao la maendeleo linaitwa DANIDA.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, naomba mpokee hilo na kwamba tuhakikshe kwamba mazungumzo yanaendelea ili kufikia hatua nzuri, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister