Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 23 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2023-05-11

Name

Ritta Enespher Kabati

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Mheshimiwa Waziri Mkuu, Tanzania imekuwa nchi ya kwanza Afrika Mashariki kutumia gesi asilia. Kwa sasa takwimu zinaonesha zaidi ya magari 2000 yameanza kutumia gesi hiyo.

Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kusambaza huduma hii nchi nzima ili wananchi waweze kufaidika na gesi yetu? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge Mkoa wa Iringa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunayo gesi asilia nchini na ni kweli tumeanza kuitumia kwenye maeneo mbalimbali. Kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema tunatumia kwenye magari lakini gesi hii tunaipeleka viwandani na tunao mpango wa kupeleka gesi hii majumbani.

Mheshimiwa Spika, wizara yetu ya Nisjhati imeweka utaratibu mzuri wa kupanua wigo wa matumizi ya gesi hii. Sasa hivi tunakamilisha ujenzi wa kituo cha kukusanyia gesi hii kutoka kule Mtwara - Songosongo pale Jijini Dar es Salaam ili sasa tuweke utaratibu mzuri wa kusambaza gesi hiyo iende kwa matumizi hayo tuliyoyasema.

Mheshimiwa Spika, pia tumeshirikisha sekta binafsi baada ya kuona uwezo wetu Serikali peke yetu hatutamudu kuifikisha gesi hii kwa wananchi. Pamoja na uwezo tulio nao tukiunganisha nguvu na sekta binafsi tunaamini tutawafikia kwenye matumizi haya. Iwe ni kupeleka viwandani, majumbani hata kwenye matumizi mengineyo ikiwemo na hayo magari.

Mheshimiwa Spika, tayari zabuni zimekwisha tangazwa na watu wengi wameomba. Sasa hivi wako wachache ambao wameruhusiwa kutekeleza mfumo huo na wengine mchakato unaendelea na bado tumefungua fursa kwa sekta binafsi kushiriki katika mchakato wa usambazaji wa gesi.

Mheshimiwa Spika, nchi yetu tumeigawa kwenye zone ambazo tutalaza mabomba kuelekea huko. Tutakwenda na bomba la kwenda Kaskazini kwa mikoa ya Kaskazini, tutakuwa na bomba linalopita Kanda ya Kati mpaka Magharibi ili kufikia mikoa ya hapa kati na tutaweka bomba kule kule Kusini ambako inatoka gesi hii kwa ajili ya mikoa ya Kusini. Lengo ni kuifikia kwa ukaribu na kwa haraka, mikoa, wilaya na kama uwezo utakuwa mzuri na sekta binafsi ikiingia ikiwekeza zaidi tunataka tufike vijijini ili wananchi walioko vijijini nao wanufaike na hii gesi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo basi, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imejipanga vizuri kwenye eneo hili na ninaamini kupitia bajeti hii Wizara ya Nishati itakapokuja hapa itatoa ufafanuzi zaidi kwenye eneo hili. Pia nimwagize Mheshimiwa Waziri, sasa moja kati ya maelezo ambayo tutahitaji kwenye Bunge hili iwe ni namna ambavyo gesi itawafikia watanzania kwenye maeneo yao. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister