Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 23 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2023-05-11

Name

George Ranwell Mwenisongole

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Primary Question

MHE. GEORGE. R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Sera ya Ushirika ya Vyama vya Msingi ililetwa kwa nia njema ya kumsaidia mkulima wa Kahawa lakini kwa wakulima wa kahawa ya Arabica nchini sera hii imekuwa kama kaburi kwao. Kwa sababu kwenye hivi vyama vya msingi makato ni mengi, wizi na viongozi wengi wa vyama vya ushirika ni wezi na wanawaibia wakulima na imekuwa kama inamdidimiza mkulima.

Je, Serikali haioni ipo haja sasa ya ku-review hii sera ili kuwaruhusu wanunuzi binafsi nao wapate nafasi kumruhusu mkulima auze kokote anakotaka? Ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kujibu swali la Mheshimiwa Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, niungane na Watanzania wote kuipongeza klabu yetu ya Dar young Africans. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakika Dar Young Africans inaendelea kupeperusha vema bendera ya Tanzania na niwapongeze sana kwa matokeo ya jana. Tunawaombea sana kwa mchezo wa marudio kule Afrika Kusini mshinde kwa magoli mengi. Watanzania tuna hamu ya kuona Tanzania ikiingia kwenye mashindano haya kwenye ngazi ya fainali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia niipongeze Klabu ya Simba kwa hatua waliyofikia, tunaamini wamejifunza na wameona kutoka klabu jirani na hatua waliyofikia. Kwa hiyo, msimu ujao tunaamini vilabu vyetu viwili au zaidi vitafanya vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nirudi kwenye swali la msingi linalohusu ushirika. Ni kweli kwamba ushirika una malengo mazuri sana kwa wakulima, si tu kwa wakulima bali kwenye vikundi vilivyoamua kukaa pamoja. Ushirika kwa mazao yetu nchini unatazamiwa na unatarajiwa kuwakusanya wakulima, mazao hayo pamoja ili kuwaongezea nguvu ya kupata maelekezo bora ya namna ya kulilima zao lenyewe lakini pia namna ya uhifadhi, elimu ya jumla ya zao hili lakini pia kuwapa nguvu ya pamoja ya kutafuta masoko.

Mheshimiwa Spika, tunakiri kwamba tunazo changamoto kwenye ushirika kutokana na baadhi ya viongozi waliopewa dhamana ya kuongoza ushirika kufanya mambo tofauti na misingi ya ushirika ulivyo. Kwa bahati nzuri siku tatu zilizopita Mheshimiwa Hussein Bashe, Waziri wa Kilimo, alitumia muda mrefu sana kueleza faida na umuhimu wa ushirika na kwamba ushirika hauepukiki katika kuleta maendeleo ya mkulima na mazao haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja kati ya mambo makubwa ambayo yameleta udhaifu kwenye ushirika ni pale viongozi wanapoona kwamba hiyo ni fursa ya kupata kipato kupitia uongozi wao kwenye ushirika. Hiyo ni kasoro na tutaendelea kuisimamia. Tumeshuhudia viongozi wasiokuwa waadilifu kuweka makato mengi sana kwenye ushirika na kupunguza mapato ya mkulima.

Mheshimiwa Spika, tumeyaona hayo kwenye zao la korosho ambako kulikuwa na makato zaidi ya 25 tumeyapunguza na yakabaki matano na inawezekana na ndio yanayoendelea. Kwenye zao la kahawa lenyewe kulikuwa na makato 47 tumeyapuinguza tumefika makato matano mpaka sita yale ya msingi tu na kumwezesha mkulima kupata fedha nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushirika huu pamoja na changamoto hizo ambazo Serikali tunaendelea kuzifuatilia na kuzitatua imeleta pia mafanikio ya kupanda kwa bei ya mazao kwa mfano zao lenyewe la kahawa. Nitoe mfano wa mkoani Kagera ambako zao hili wakulima wake wengi walikuwa wanaamua kulipeleka nchini Uganda kwa gharama kubwa tu kwa sababu tu ya kero walizoziona. Baada ya Serikali kuingilia kati na kuzitatua changamoto hizi leo wanauza kutoka shilingi 1,200 ya awali tumeenda mpaka shilingi 1,800 mpaka shilingi 2,000 kwa sasa na kupitia usimamizi wa ushirika.

Mheshimiwa Spika, hii ina maana ya kwamba ushirika unaweza kuongeza nguvu ya wakuilima kupata soko zuri badala ya kuruhusu mnunuzi mmoja mmoja kwenda kwa mkulima nyumbani kwake na kumshawishi kununua kwa bei ambayo anaona yeye inafaa, wakati mwingine anauza kwa bei ndogo sana kuliko hata ile iliyokuwa inauzwa. Hata hivyo, tunaendelea kuangalia mifumo mizuri zaidi ya kuuza mazao yetu chini ya ushirika. Ushirika unaweza ukatoa kibali kwa watu waliolima kahawa nyingi kama soko linakuwa lina mwelekeo mzuri tunaweza kuruhusu.

Mheshimiwa Spika, nataka niwaahidi na nimwahidi Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge ambao pia tunalima mazao yale makubwa yenye ushirika, kwamba tunaendelea kufanya mapitio, tunaendelea kusimamia kikamilifu ushirika ili ulete manufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha majibu ya swali hilo.

Additional Question(s) to Prime Minister