Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2021-11-11

Name

Nusrat Shaaban Hanje

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi nami niweze kumwuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali. Tarehe 10 Julai, Soko la Kariakoo liliungua, ambapo tarehe 11 Julai, wewe mwenyewe ulikwenda Kariakoo kwa ajili ya kuwapa pole wahanga na pia kutoa maelekezo ya Serikali. Mheshimiwa Waziri Mkuu tunashukuru sana Serikali kwa sababu wamechukua jitihada za kujenga upya soko la Kariakoo ambako tarehe 6 Novemba, 2021 Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI alikwenda Kariakoo kwa ajili ya kutoa maelekezo kuhusiana na kujenga Soko la Kariakoo, kulijenga upya.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, ramani mpya ya Soko la Kariakoo jipya ina masoko mawili ambapo kama sasa hivi yako masoko mawili. Ramani inataka na utaratibu wa kujenga unataka soko dogo na kubwa lijengwe kwa pamoja. Mheshimiwa Waziri Mkuu jambo hili linaweza kupelekea ghasia na sintofahamu kwa wafanyabiashara.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu ni kwa nini sasa Serikali isiweke utaratibu wa kujenga masoko haya kwa awamu ili wafanyabiashara wa soko dogo wabaki pale ili soko kubwa lijengwe halafu baadaye wahamishiwe likamilike kwa pamoja? Nashukuru sana.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat, Mbunge wa Mkoa wa Singida, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tulipata tatizo la soko la Kariakoo kuungua na wote tunajua, lakini Serikali imefanya jitihada kubwa sana. Tulienda kutembelea na kuwapa pole, lakini tulitaka tujiridhishe ajali ile ilitokana na nini? Tukaunda Timu ambayo pia ilifanya kazi yake vizuri na ikatupa mrejesho wa nini kilisababisha soko lile lakini Kamati ile ilienda mbali zaidi na kutuambia madhara ya soko lile yakoje.

Sasa lile soko pale lilipo limezungukwa na nyumba za watu binafsi, lakini pia kuna soko dogo liko karibu kabisa na lile soko, usalama wa soko lile dogo haukuwa mzuri pia nao. Kwa hiyo katika maoni au mapendekezo ambayo waliyatoa ile Tume ni pamoja na kuliondoa lenyewe na kulijenga lingine jipya ambalo pia litafanya kazi yake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Rais, atatutengea shilingi bilioni zisizopungua 32 mpaka 34 ambazo zitajenga masoko yote mawili na tumeona tufanye maboresho makubwa. Hawa walioondolewa kwenye eneo lile, kimsingi hata pale baada ya kuungua, hawa waliokuwa soko dogo walikuwa hawafanyi kazi zao. Nao tuliwasihi wapishe eneo lile, ili eneo lile sasa uchunguzi upite na sasa maandalizi ya ujenzi yaendelee na tumewapeleka Kisutu pamoja na eneo la Machinga Complex na wengine wameenda kwenye masoko jirani.

Mheshimiwa Spika, wale wote wameorodheshwa, wanafahamika nani alikuwa wapi. Malengo yetu, baada ya kukamilisha katika kipindi tulichokubaliana soko likamilike, wale wote waliokuwa soko dogo waliokuwa mle kwenye soko kubwa, tunawarudisha na kuwaweka kwenye nafasi zao. Kwa kuwa sasa soko tumeliboresha, soko dogo sasa tumelijenga kwenye ghorofa, ghorofa mbili mpaka tatu, tumeongeza na wengine waliokuwa wanazagaa kule nje wakakosa mahali, sasa tunawaingiza kwenye lile jengo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yote haya ni maboresho ambayo tumeyafanya ya kuhakikisha kwamba hawa walioko hapa si kwamba wanapata shida kubwa kwa sababu wengine tumewapeleka pale Kisutu wanaendesha biashara zao na wale kwa sababu wana uhakika jengo likijengwa watarudi na watapata nafasi, naamini wanaiamini Serikali yao kwamba tutatenda hivyo na tutasimamia hilo ili kazi hiyo iweze kukamilika.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI inasimamia kwa karibu na sasa iko kwenye zabuni ili ujenzi uanze katika kipindi kifupi, wafanyabiashara warudi kufanya biashara zao. Ahsanye sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister