Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Ameir Abdalla Ameir (3 total)

MHE. AMEIR ABDALLAH AMEIR: Mheshimiwa Spika,ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri ningeomba kuuliza masuala mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tuna maeneo ambayo yana vielelezo vya kihistoria kati ya Tanzania bara na Tanzania visiwani yanayo shabihiana; kwa mfano hatuwezi kuzungumza biashara ya utumwa tukaielezea sehemu moja ina elezeka sehemu zote mbili wanahistoria Dkt. Livingstone.

a) Je, Wizara yako sasa inaampango gani wa kuyahuisha maeneo haya yenye vielelezo vya kihistoria vinavyotegemeana ili sasa kuusaidia utalii wetu wa ndani kukua zaidi kimapato?

Mheshimiwa Spika, kutokana na mtikisiko wa Uviko 19 tumeona kwamba utalii wetu wa ndani kidogo uliyumba;

b) Je, Wizara sasa ina mpango gani wa mikakati mipya na imara ukiachia mbali hii ya kawaida unayoelezea ya kuweza sasa kuufanya utalii wetu wa ndani uweze kujitegemea angalau kwa asilimia hamsini kwa hamsini, huku ukizingatia kwamba tunapoboresha vya kutosha Tanzania kutokana na ongezeka la watu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ameir Abdallah Ameir, Mbunge kutoka Baraza la Wawakilishi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ipo mikakati kabambe ambayo imeshaandaliwa na Serikali kuhakikisha kwamba tunaendelea kutunza maeneo haya ya kihistoria. Moja ni kuhakikisha kwamba tunaendelea kuyatunza maeneo hayo yenyewe ili lengo na madhumuni sasa tuweze kuvutia watalii wengi; lakini cha pili kuendelea kufanya utafiti kwa sababu tunachoamini kwamba bado yapo maeneo ya vivutio vya watalii inawezekana bado hatujayavumbua yakiwemo maeneo ya kihistoria ya hiyo historia utumwa na vitu vingine. Sasa kuendelea kuyatangaza, kwa sababu kuwa nayo na kuyavumbua ni suala moja lakini kuendelea kuyatangaza ili walio nje na ndani ya nchi yetu waweze kutambua wapi wanaweza wakajifunza na wakapata kujua hiyo historia.

Mheshimiwa Spika, swali lingine, ni nini sasa matarajio yetu, Matarajio yetu ni kuhakikisha kwamba tunaongeza idadi kubwa ya watalii kutoka idadi tuliyo nayo kuendelea idadi kufika hata watalii milioni tano. Lengo na madhumuni ni kuongeza sasa mapato ya nchi.

Mheshimiwa Spika, ili tuweze kufikia hayo matarajio kwanza tuhakikishe kwamba tunatoa elimu kwa wananchi ili waweze kutambua umuhimu wa utalii wa ndani, lakini cha pili kutoa huduma bora hicho tumekipanga ili lengo na madhumuni wanapo kuja kujifunza waweze kupata huduma bora.

Mheshimiwa Spika,nakushukuru.
MHE. AMEIR ABDALLAH AMEIR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza. Tumeshuhudia hivi karibuni nchi ya Afrika Kusini wametangaza uhitaji wa walimu wa lugha ya Kiswahili katika nchi hiyo; je, Serikali sasa inatumiaje fursa hii katika kuhakikisha kwamba walimu wetu waliobobea katika lugha ya Kiswahili wanafaidika na fursa hii hususan walimu kutoka Tanzania Bara na Tanzania Visiwani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Miongoni mwa Balozi ambazo zimekuwa zikifanya vizuri katika kuikuza lugha ya Kiswahili ni Ubalozi wa Tanzania nchini Italy, tayari wameshasajiisha Vyuo Vikuu vitatu ndani ya nchi hiyo, vinafundisha lugha ya Kiswahili, kikiwemo Chuo Kikuu cha Torino, Chuo Kikuu cha Roma na Chuo Kikuu cha Napoli. Vilevile nauliza swali; je, Serikali haioni haja kwamba Balozi zetu ambazo zinatuwakilisha katika nchi mbalimbali ziweze kufuata modality hii ya Ubalozi wa Italy nchini Tanzania, ambapo kwa muda mfupi tu tunaweza tukafaidika kwa hali ya juu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna uhitaji wa Serikali ya Afrika Kusini kuanza kufundisha Kiswahili. Hizi ni juhudi za Serikali vile vile kwa ushirikiano na Serikali ya Afrika Kusini. Kama nilivyoeleza katika jibu la msingi, kimsingi walimu wetu wamenufaika na hizi fursa na wanapelekwa kwa kasi sana kwa sababu ni matangazo yanakuwa ya hadhara kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Balozi zetu kuiga mfano wa Italy, tumepokea ushauri wa Mheshimiwa Mbunge na tunasisitiza kabisa kabisa. Yapo mambo mengi ambayo katika hali ya kawaida sisi kama Watanzania tunatakiwa kujivunia, Kiswahili chetu kinauzika duniani kote. Tuna redio zaidi ya 13 nje ya Tanzania ambazo zinatumia Kiswahili. Kwa mfano, tuna Idhaa ya Kiswahili ya BBC, tuna Sauti ya Amerika, tuna Redio Japani, Tuna Sauti ya Ujerumani, tuna Sauti ya Umoja wa Mataifa, tuna Redio China na nchi zetu zote hizi za Afrika Mashariki zote zinatumia Kiswahili katika baadhi ya matangazo yake. Kwa hiyo, ni sisi Watanzania kujitangaza katika mazingira yote tunapokuwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naziomba Balozi zetu huko nje zianzishe majukwaa mbalimbali yakiwepo matamasha ya Kiswahili katika nchi wanazotuwakilisha ili kukitangaza Kiswahili katika uhalisia wake.
MHE. AMEIR ABDALLA AMEIR: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; kwanza teknolojia hii ya habari na mawasiliano ina mchango mkubwa sana katika kuziba lile pengo la uhaba wa Maafisa Ugani wetu kwa muda mfupi na kwa eneo kubwa, sasa Wizara ina mpango gani sasa wa kuanzisha Apps au mifumo mbalimbali ya TEHAMA, ambayo mifumo hii itawasaidia wakulima wetu wadogo wadogo kupata taarifa kwa wakati na kwa usahihi?

Pili, Wizara sasa haioni kuna umuhimu wa kuyashawishi makampuni mbalimbali ya simu kutoa kifurushi maalum cha huduma za wakulima, ambapo sasa wakulima wetu watakuwa wanapata taarifa hizi wakiwa maeneo mbalimbali? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara inatambua matumizi ya teknolojia ambapo ndiyo dunia ya leo inapoelekea, katika kurahisiha utoaji wa huduma kwa wakulima na hasa kupitia Maafisa Ugani, tunao mfumo ambao tunauita N-Kilimo ambao mpaka hivi sasa tumeshasajili Maafisa Ugani 9,725, ambao kazi yao kubwa ni kuhakikisha kwamba tunasambaza taarifa hizi kwa wakulima kupitia programu hii. Pia tunayo call center yetu ya Wizara ya Kilimo ambayo pia wakulima ambao wanapata changamoto mbalimbali wamekuwa wakipiga simu na kupata ufafanuzi na kujibiwa baadhi ya changamoto ambazo wanakabiliaba nazo.

Mheshimiwa Spika, nitoe tu rai na kuwaomba wakulima wote nchini Tanzania kuendelea kuitumia namba yetu ile ya 0733 800 200 kwa ajili ya kuweza kupata huduma mbalimbali za kilimo kupitia teknolojia hii.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ushauri tunaupokea wa kukaa na kampuni za simu kurahisisha utoaji wa huduma hizi za ugani kwa wakulima wetu. Ushauri huo tumeupokea ni mzuri, tutaona namna ya kuweza kuboresha ili wakulima wetu waweze kupata taarifa kwa wakati. (Makofi)