Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Joseph Zacharius Kamonga (1 total)

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu, na nitambue dhamira ya Serikali katika kuhakikisha kuna usalama wa hali ya juu kwa wananchi wanaosafiri kwenye maziwa makuu kama Ziwa Victoria, Ziwa Nyasa na Ziwa Tanganyika. (Makofi)

Vilevile wananchi wamekushuhudia Mheshimiwa Waziri Mkuu namna unavyosimamia ujenzi wa meli kwenye Ziwa Victoria, lakini kwa bahati mbaya katika Ziwa Tanganyika na Ziwa Nyasa wananchi wamekuwa kwa muda mrefu wanatumia usafiri wa jadi kama mitumbwi na maboti, na maziwa haya yana mawimbi makali sana na eneo hili ni nyeti sana kwa kukuza diplomasia ya kiuchumi na biashara kati ya nchi jirani na Malawi na kwa Ziwa Tanganyika, meli MV-Liemba inasemekana ililetwa na wakoloni mwaka 1905.

Sasa je, nini mkakati wa Serikali kisera na kisheria kuhakikisha kwamba wananchi wanaosafiri kwenye Ziwa Tanganyika na Ziwa Nyasa wanapewa usafiri ambao ni mzuri ambao utalinda usalama wao, lakini kuuza biashara kati ya Tanzania, DRC, Burundi, Congo na nchi jirani ya Malawi? Nashukuru. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kamonga, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, najua swali lilikuwa refu, lakini anataka kujua Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba tunapeleka usafiri kwenye maeneo haya ya maziwa haya matatu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa ili kuwawezesha Watanzania wanaoishi hapo kutumia fursa zilizopo za kibiashara katika kuongeza uchumi wao.

Mheshimiwa Spika, ziko jitihada zinaendelea za kuhakikisha kwamba maeneo haya ya maziwa hata bahari kuu tunaimarisha usafiri ambao utawezesha pia Watanzania na ndugu zetu walioko majirani kufanya biashara zao na kujiongezea kipato kwa kusafirisha biashara pia na uvuvi kwenye maeneo haya.

Waheshimiwa Wabunge wote ni mashahidi, jitihada ziko zinaendelea za ujenzi wa meli Ziwa Victoria na hivi karibuni mwanzoni mwa mwaka huu Mheshimiwa Rais alikuwa Mkoani Mwanza kushuhudia kutia sahini wa ujenzi wa meli za Ziwa Victoria, Ziwa Tanganyika na Ziwa Nyasa. Pia Wizara ya Uchukuzi na Ujenzi imeshafanya kazi kubwa ya kukarabati meli na vivuko kwenye maeneo yote matatu hayo, Victoria, Tanganyika pamoja na Nyasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa bahati nzuri nimefanya ziara maeneo yote haya. Mbali ya ujenzi wa meli ambazo zinaendelea kujengwa na kukarabatiwa Ziwa Victoria, Tanganyika na Nyasa pia tunaimarisha na bandari zake. Ziwa Victoria tumeimarisha bandari mkoani Mara na bandari zake zote mpaka Bunda, Kisorya, lakini pia Mwanza, Geita na Kagera, na kule Mkoani Kigoma mimi pia nimetembelea Kibirizi, nimeenda pia Kabunga ambako tulishajenga bandari na haikutumika kwa muda mrefu, lakini nimeenda Kabwe, Kasanga kule Rukwa kuona bandari hizi, na bandari kubwa tunaijenga pale Karemie Wilayani Tanganyika Mkoani Katavi hizi ni jitihada kubwa.

Mheshimiwa Spika, hat akule Ziwa Nyasa, bandari ya Itungi imeimarishwa sana na mimi pia nimeenda kuzindua na meli, kwanza kukagua ujenzi wake, lakini nimezindua na meli kule Wilayani Mbambabay. (Makofi)
Kwa hiyo, jitihada zote hizi malengo yetu ni kufikia azma ambayo Mheshimiwa Mbunge hapa ameieleza ya kuimarisha usafirishaji na kuwawezesha Watanzania kutumia fursa hiyo kufanya biashara na nchi jirani. Na tunaendelea pia kushirikiana na nchi jirani nao kama wana meli tunaziruhusu kuingia. Kwa hiyo, tunataka tutengeneze network ambayo itaendelea kupanua wigo wa kufanya biashara na kuingiliana kwenye maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jitihada hizi zitaendelea na tutakapoanza kuimarisha ujenzi wa meli hizo tutafanya biashara. Lakini bahari kuu pia nako miongoni mwa zabuni zilizotangazwa ni ujenzi wa meli yenye uwezo wa tani kuanzia 3,000 mpaka 3,500 ambayo itakuwa inasafirisha abiria, mizigo na shughuli za kibiashara kati ya Zanzibar na Bara, lakini tunataka twende mpaka Comoro. Ujenzi huu utakapokamilika kutakuwa na usafiri wa ndani tutapita mpaka Mafia pia. Malengo ni kuimarisha fursa za Watanzania kufanya biashara kwenye maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niwahakikishie Watanzania kwamba tutaendelea kuimarisha njia za usafirishaji kwenye maziwa, lakini pia na nchi kavu ili kutoa fursa kwa Watanzania wanaotaka kufanya biashara, wanaotaka kufanya utalii kwa nchi jirani waweze kwenda, lakini nchi jirani kuja kuingia nchini. Kwa hili tunaendelea kulifanyia kazi, ahsante sana. (Makofi)