Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Deodatus Philip Mwanyika (28 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi nipate kuchangia kwenye hoja iliyo mbele yetu. Kwanza nitoe shukrani kwa chama changu na Mwenyekiti wa Chama kunipa nafasi ya kuwa mgombea na mwisho wa siku kuwa Mbunge katika Bunge hili, lakini la pili vilevile nawashukuru sana wananchi wa Njombe Mjini kwa kuniamini na kunipa nafasi ya Ubunge nasema sitawaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hotuba ambayo Mheshimiwa Rais ameitoa ni hotuba ambayo imetoa matumaini makubwa sana. Ni matumaini yaliyojengwa katika msingi wa mafanikio yaliyopatikana katika miaka mitano iliyopita, yameongelewa hapa kwa wingi hatuna sababu ya kuyataja yote, lakini mimi niongelee moja ambalo limenigusa na litaendelea kunigusa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais tumeshuhudia akifanya mabadiliko makubwa sana katika sekta ya madini. Mimi nasema yalikuwa ni maamuzi sahihi katika wakati sahihi. Tumeshuhudia sasa sekta hii ya madini kuwa ni sekta ambayo inaongoza kwa kuongezea nchi fedha za kigeni, lakini ni sekta inayokua kwa haraka sana. Naomba sasa Serikali iendelee kujikita na kuangalia madini mengine na hasa kwa vile utafiti katika sekta ya madini ni jambo la muhimu sana. Tunaelewa hatuwezi kutegemea wawekezaji kutoka nje kufanya utafiti, kwa hiyo, wazo langu au ushauri wangu kwamba Serikali ijikite kuiongezea STAMICO hela za kutosha ifanye utafiti. Na sisi tunawakaribisha kule Njombe kuna madini ya kila aina waweze kuja kufanya utafiti.

Mheshimiwa Spika, la pili ambalo nilitaka niongelee ni suala zima la viwanda na uwekezaji. Ukisoma hotuba ya Mheshimiwa Rais imejikita sana kuongelea sekta binafsi na viwanda. Ni jambo muhimu na ni jambo ambalo litatufanya sisi tuweze kufikia lengo la zile ajira milioni nane. Kule Njombe tumejikita katika uwekezaji na ukulima, lakini kwetu sisi suala la viwanda ni suala la muhimu sana na Mheshimiwa Rais anaongelea kutengeneza mazingira mazuri ya kuwavutia wawekezaji katika viwanda.

Mheshimiwa Spika, lakini niseme moja kwamba wakati tunawavutia wawekezaji katika viwanda tuangalie wawekezaji waliopo katika maeneo yetu. Kule Njombe tuna zao moja la kimkakati la chai, ni zao ambalo linatakiwa lipewe umuhimu mkubwa sana. Kwa sasa zao hili linalegalega na kuna uwezekano kama hatua za haraka hazitachukuliwa litafikia mahali pabaya.

Mheshimiwa Spika, nitoe wito, naelewa katika hotuba ya Mheshimiwa Rais ameongelea kuweka mazingira wezeshi ambayo yatasaidia uwekezaji uweze kufufuka katika maeneo mbalimbali. Nipende kusema kwamba bado pamoja na kwamba kuna blue print na tunaelewa inakuja, tumeshuhudia kwamba bado kuna tozo za kila aina ambazo zimekuwa ni kero kwa wawekezaji na kero hizo kwa vile ni suala la viwanda na kwa vile tunaongelea chai, tunaongelea mkulima wa kawaida ambaye mwisho wa siku ndiye kipato chake kitashuka.

Mheshimiwa Spika, ukilinganisha ukulima viwanda vya chai ambavyo viko katika maeneo sio tu ya Njombe, lakini na maeneo mengine ya jirani tozo zake ukilinganisha na viwanda vingine vya Kenya vya chai na viwanda vingine vya nchi kama Malawi unakuta wenzetu tozo ni chache sana. Kuna study imefanyika inaonesha tozo za viwanda vya chai peke yake zinafika karibu 19 wakati wenzetu hawana tozo, kwa hiyo, ningeomba Serikali ilitupie macho jambo hilo kwa ukaribu sana.

Mheshimiwa Spika, lakini niongelee vilevile kero nyingine ambazo zinajitokeza katika kushughulikia masuala ya wafanyabiashara, hasa wa mazao ya miti katika Jimbo la Njombe na Jimbo la Njombe ni Jimbo la Njombe Mjini, lakini lina vijiji vingi sana.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, naomba niunge hoja mkono, lakini nipende kusisitiza iko haja ya kutatua kero za wakulima wa miti na mashamba ya mbao kule Njombe kama vile Rais alivyoahidi wakati wa kampeni. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia. Kwanza ningependa kutoa mchango wangu kwenye eneo la kilimo na biashara. Mpango huu ni mzuri, lakini unachangamoto hasa kwenye eneo hilo la kilimo na biashara ambalo ni eneo muhimu sana kwa uchumi wa nchi. Nianze kwanza ku-declare interest hata mimi ni mkulima wa chai kwa sababu nitachangia kwenye eneo la chai. Mpango huu kwa eneo la kilimo kwa maelezo ya Waziri mwenyewe haujaonyesha mafanikio makubwa kwa eneo la kilimo, ukuaji wa uchumi eneo la kilimo umekuwa mdogo na tunasema mchango wa kilimo kwenye pato la Taifa umekuwa mdogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo ambalo naliona kwamba linaweza likaleta mabadiliko makubwa ni eneo la chai. Zao la chai kwa ujumla wake na sekta ya kilimo kwa ujumla wake imekuwa chini kwa sababu moja kubwa, uwekezaji katika eneo la chai umekuwa mdogo, uwekezaji upande wa Serikali lakini hata uwekezaji kwa upande wa watu binafsi. Kwa hiyo ipo haja ya kuongeza kwa kiasi kikubwa sana uwekezaji kwa namna nyingi na nitazitaja hata chache tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo kubwa ni kuweka mazingira wezeshi kwa ajili ya wakulima wa maeneo ya chai. Ukiangalia kwa undani kabisa utaona wazi kabisa utaona wazi kabisa wakulima wetu wa chai hasa wadogo wadogo bado wana-struggle sana kuzalisha chai yao. Kule kwenye maeneo ya Njombe kuna viwanda vikubwa vya chai kama kumi na tisa. Viwanda hivyo vyote vinakuwa own na watu wa nje, wakulima wetu bado wanafanya njia za kizamani za kulima na hawawezi kutoa mchango mkubwa. Ni vizuri sasa Serikali ikajikita zaidi huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia eneo ambalo unaliona lazima tuongeze uwekezaji, ni eneo la ugani. Katika global average wakulima 400 wanatakiwa wahudumiwe na Mgani mmoja, lakini kwetu sisi hapa ni wakulima 1,100. Ukienda kwenye upande wa miundombinu ya umwagiliaji bado tuko nyuma sana, hatuwezi kwenda na kilimo ambacho tunategemea mvua hasa kwenye mazao ya chai na mazao ya avocado. Kwa hiyo tuna kila sababu, Tanzania mpaka leo kwa eneo lililolimwa kwa mwaka 2019, karibu hekta 13,000,000 ni asilimia 20 tu ambayo ina umwagiliaji kama hekta laki nane. Tunatakiwa twende juu zaidi na zaidi ili tuweze kuona tija kwenye eneo la kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tu fungamanishe hii sekta ya kilimo ya process na eneo la Nyanda za Juu Kusini Njombe ikiwemo, ni eneo lenye potential kubwa sana ya kuwa game changer kwenye kilimo kama tutafanya uwekezaji mkubwa na tutaita uwekezaji. Hata hivyo, tukumbuke tuna wawekezaji kule wana-struggle kwa sababu ya tozo nyingi sana ambazo kwa kweli pamoja na jitihada za Serikali na tumeona kwenye kitabu hapa, lakini tozo bado ni nyingi sana. Kwenye chai peke yake kuna tozo zaidi 19.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kitabu na kwenye hotuba ya Rais na kwenye Mpango tunakwenda kwenye kilimo cha biashara maana yake kilimo cha biashara unakuwa competitive ukilinganisha na wenzako. Tuwaangalie Kenya kilimo chao chai, tozo ziko mbili tu; Uganda wana tozo moja; sisi tuna 13. Twende kwenye avocado na matunda matunda tuna tozo karibu 45; pamoja na kazi nzuri ya serikali bado jitihada zinatakiwa zifanyike. Nafahamu kuna blue print inaendelea, lakini kwa kweli impact kwa wakulima bado ni kubwa na negative.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee eneo la wakulima ambalo ni la viwanda sasa hivi vya chai vilivyopo. Nipende kusema wana mchango wao mkubwa, lakini wanaweza wakachanga Zaidi. Kuna mmiliki mwenye viwanda vya chai ametoka Kenya anaitwa DL, sasa hivi anashindwa hata kulipa mishahara, anashindwa kulipa pension, ni miezi 12 wafanyakazi hata pensions zao hazijalipwa, wafanyakazi wana maisha magumu, wakulima wana maisha magumu, wana mwaga chai. mahindi ukikosa mwekezaji au ukikosa mnunuzi utaweka ghalani, utauza mwaka unaofuata, lakini chai ukikosa mnunuzi unamwaga. Kwa watu ambao wanaisha maisha magumu wanatafuta mitaji kwa shida, wanalima chai, wana kila haki ya kuhakikisha kwamba wanasaidiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la mwekezaji huyu ni moja, amenunua viwanda vya chai lakini hajakamilisha process nzima ya ku-transfer viwanda vya chai na sababu kubwa tunaambiwa ni TRA kwamba wanasema kuna capital gain tax haijalipwa, lakini anayelipa capital gain tax ni yule aliyeuza. Kwa hiyo huyu anashindwa kwenda kukopa, anashindwa kwendelea, anashindwa kuchukua chai, watu wanamwaga chai yao, lakini kosa siyo lake. Sasa kama tunataka mpango huu na tunataka chai iweze kwenda kuzalishwa zaidi na malengo ya Serikali ni kufanya chai kama zao la mkakati liweze kuingia na pesa za kigeni; tuwaangalie wawekezaji hawa, hata huyu mmoja ambaye ana viwanda karibu zaidi ya vinne na anaajiri zaidi ya watu 2,000 na anasaidia kwa kutoa mbolea, kwa kutoa madawa kwa kulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye moja lingine la avocado, avocado it is not be a big business, avocado can be a big changer, tunaita green gold, kwa kweli tunatakiwa tujipange vizuri na naomba sana Serikali tunapozungumzia miundombinu wenzeshi, lazima tuangalie zao hili. Kwenye mazao ya mbao naomba niseme na nimalizie kwa kusema, wakulima na wafanyabiashara wa Njombe wana hali mbaya sana, kwa sababu tunahitaji mahusiano mazuri kati yao na TRA, tunapokwenda siyo kuzuri kwa maana watu wanaona hakuna faida ya kulima misitu, wamelima misitu hawawezi kuiuza, hawawezi kupata faida, ni jambo tunatakiwa tulitiliee maanani na Waziri wa Fedha ameshaandikiwa ili atoe nafasi kwa hawa Watanzania, wafanyabiashara wa Njombe waweze kukaa na TRA kuona namna gani wata-improve.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia bajeti hii, ambayo ni bajeti ya kwanza ya awamu ya sita na vilevile ni bajeti ya kwanza katika mpango wa miaka mitano, wa 2021/2022 kwenda mpaka 2025/2026 ambayo dhima yake ni uchumi wa viwanda shindani na shirikishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili linanigusa sana na nimeliongelea sana hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nianze kwanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake pamoja na Naibu Waziri na timu yake kwa kutupa bajeti hii ambayo kwa kweli imegusa mioyo ya Watanzania. Sisi Wabunge ni mashahidi, mengi yaliyosemwa katika bajeti hii ni yale ambayo sisi kama Wabunge tuliomba Serikali iyashughulikie. Kwa hiyo tunamshukuru sana, na kwa vile hii ni Bajeti ya Taifa, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais jemedari wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuwa ndiye chachu kubwa ya bajeti hii, tunamshukuru sana. Mimi kibinafsi namshukuru kwanza kwa sababu ndani ya bajeti hii tunaona dhamira ya dhati ya kuishirikisha sekta binafsi katika kuendesha uchumi wa nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tupende tusipende sekta binafsi ndiyo sekta ambayo tunaitegemea kwa kupata mapato makubwa ya nchi. Lakini si hilo tu, ndani ya bajeti hii tunaona wazi kabisa kwamba Mheshimiwa Rais anatoa maono ya wazi na miongozo ya kuonesha kwamba miradi mbalimbali ambayo ilikuwa ni ya sekta binafsi ambayo imekwamba sasa ipate ufumbuzi na iweze kuendelea mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kwa kifupi kabisa nimpongeze Mheshimiwa Rais kiukweli kabisa kwa kutoa muongozo kuhusiana na mradi wa Mchuchuma na Liganga. Mradi huu umeongelewa kwa muda mrefu sana, na ulifikia mahali ukawa kama ni wimbo tu; unaimbwa unaisha. Lakini sasa tunaona dhamira ya dhati kabisa ya Mheshimiwa Rais, kwamba majadiliano yale ambayo yalikuwa yamekwama yaweze kuendelea na kukamilishwa; na kama hayawezekani basi tutafute alternative nyingine. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa maamuzi hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongelee sekta ya kilimo. Sekta hii ya kilimo wote tunafahamu kuwa ni sekta ambayo imetoa mchango mkubwa sana kwenye uchumi wa nchi; asilimia 26 ya Pato Ghafi la Taifa linatokana na sekta hii ya kilimo. Asilimia 65 ya waajiriwa ambao wanatoka katika maeneo ya vijijini Watanzania wanatoka katika sekta hii ya kilimo. Lakini siyo hilo tu mchango wa sekta hii kwa upande wa kuleta pesa ya kigeni ni takriban asilimia 24.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha kushangaza ni kwamba sekta hii inatia huruma. Kwa sababu pamoja na hizo namba tunazoziongea hapa uwekezaji kwenye sekta hii bado ni mdogo sana, na wengi wameliongea hilo. Tunaongelea chini ya asilimia 0.8 wengine wanasema asilimia 1.9 lakini ukweli ni kwamba ni mdogo mno; na udogo wa uwekezaji huo si kwa Serikali peke yake kupitia bajeti bali hata kwa sekta binafsi.

Mheshimiwa Naibu Spika, benki zetu bado hazijachangamkia fursa kubwa ambazo zipo katika sekta hii kubwa ya kilimo. Ukiangalia mgawanyo wa fedha ambazo zimekwenda kwenye sekta binafsi kwa ajili ya kilimo inasikitisha kuona kwamba takriban asilimia 35.8 ya mikopo ya benki imekwenda kwenye mambo binafsi tu ya watu. Asilimia 15.7 imekwenda kwenye biashara za kawaida, asilimia 10 kwenye viwanda, lakini kilimo ni asilimia nane tu. Kwa hiyo tuna tatizo kubwa la uwekezaji kwenye sekta hii upande wa Serikali kupitia bajeti lakini vile vile kupitia sekta binafsi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani sasa wote tuna kazi ya kufanya hapa, lakini la kwanza kabisa tuanze na maamuzi ya kibajeti. Naelewa hakuna kitu tunachoweza tukakifanya katika bajeti hii kwa sasa, lakini tunaiomba sana Serikali na tunamuomba sana Mheshimiwa Waziri, wote tutambue kwamba lazima tuitendee haki Tanzania; na huwezi kuitendea haki Tanzania kama hautatoa pesa za kutosha kwenye sekta hiii ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika miaka mitatu minne iliyopita sekta hii uwekezaji wake umeteremka. lakini huko nyuma angalau tulifikia asilimia tano ya total collection. Lakini tukiweza angalau tukafika angalau tufikie hata asilimia sita, tukiweza kufikia asilimia saba ambayo ndiyo declaration ya Maputo nadhani tutakuwa tayari tunaenda katika mlolongo mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi nitoe ushauri; tunahitaji kuvutia uwekezaji kwa namna ya pekee kwenye sekta hii ya kilimo, na ninavyoona tunahitaji kuwa na special scheme za sekta ya kilimo pamoja na vivutio katika sekta hii. Tunajua sekta hii iko katika maeneo ya vijijini huko mikoani. Wengine walisema na mimi nalisisitiza, kwamba iko haja ya kuwa na vivutio vya kikodi na vya kisera ambavyo vita-focus kwenye sekta ya kilimo na kwenye viwanda ambavyo vitakua na vitajengwa katika maeneo ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaloliona sasa hivi kiwanda kinachojengwa eneo la kilimo mikoani na kinachojengwa mikoa ambayo haina kilimo vinakuwa treated sawa; hatuwezi kufika katika utaratibu huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejitahidi kuweka vivutio vya aina fulani katika bajeti hii kwa upande wa cold rooms na vifungashio. Lakini mimi nasema kwamba, pamoja na hilo tunawashukuru lakini bado tutatakiwa tuangalie wapi hasa panahitaji kuwekewa hivyo vivutio. Tuangalie mnyororo wa thamani katika sekta ya kilimo. Mimi nasema, vifungashio sawa, cold rooms sawa, lakini twende tukaangalie pale ambapo kunafanyika uzalishaji wa mazao yetu ya kilimo ndipo hasa tuweke hivyo vivutio. Tuangalie maeneo ambayo kama kuna viwanda vya madawa, tuangalie viwanda vya mbolea, tuangalie vilevile pale ambapo tunahitaji utaalam na utaalamu hatuwezi kuupata hapa basi tulegeze masharti ya vibali kwa watu ambao watakwenda kufanya kazi kama wataalamu kwenye sekta ya kilimo. Tunahitaji kufanya kazi kimkakati ili tuweze kuifunua hii sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kuhusu zao la avocado, kwa kifupi tu. Nchi hii ina uwezo mkubwa sana wa kuongeza mapato makubwa sana kama tukiweza ku-focus kwenye zao la avocado. Zao hili linaweza kui-transform Tanzania. Ukichukua nchi kama ya Mexico ambayo eneo lake ni dogo, hata ukubwa wa mkoa wa Njombe Mexico ni ndogo lakini kwa mwaka 2018/2019 Mexico kwa avocado peke yake wameingiza 2.7 billion dollars. Hayo ni mapato yanayofikia mapato yetu yote ya dhahabu. Kwa hiyo iko haja ya kuliangalia hili jambo kwa umakini sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwa sasa watafiti wanasema katika miaka mitano ijayo Tanzania inaweza ikawa nchi ya uzalishaji mkubwa wa avocado kuliko hata Kenya. Lakini tuna kilio hapa ndani, kwamba avocado zetu sisi tunazi-register kama zinatoka Kenya, na kwa hiyo kuna upotevu wa mapato, lakini vilevile nchi yetu inakosa fedha ya kigeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme kwamba tatizo hili litaendelea kama tusipoweka mikakati mahiri sasa hivi. Ukiangalia kwenye bandari yetu ya Dar es Salaam ambayo ndiyo port of exit kubwa tunayoitegemea uwekezaji unaoendelea ni mkubwa lakini bado hauja focus kwenye perishables. Nchi hii inategemewa kuwa projected kuzalisha takriban laki sita za avocado.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda ukilinganisha na Mombasa watu wanakwenda Mombasa kwa sababu slot za cold rooms Mombasa ziko 1800, unakwenda na container una slot unangojea meli Tanzania TICTS Pamoja na TPA slot zipo 120. Kwa hiyo hakuna uwezo wowote utakaotufanya sisi tuende kwenye huo ushindani na tukashinda.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kuongea kidogo sekta ya Madini, ukiangalia utakuta kwamba tumelegalega na nchi yetu kwa kiasi kikubwa sana sekta ya utalii ime-collapse, lakini sekta ya Madini imeweza ku-balance na imenyanyua kwa kufanya shilingi yetu i-stabilize kwa sababu ya dhahabu. Tunamshukuru Mungu kwamba tunaiyo dhahabu, lakini kwa kiasi kikubwa dhahabu yote hiyo imetoka kwenye migodi kama miwili pamoja na wachimbaji wadogo wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema kwamba, tunatakiwa tuendelee kuvuta wawekezaji kwenye Sekta hii ya Madini ili tuweze kupata mapato makubwa. Pia tunatakiwa tu-identify, twende kwenye sekta nyingine au sub- sector nyingine ambazo ndiyo sasa hivi dunia inakwenda na huko tuna wawekezaji kuna maeneo kama ya helium gas, kuna maeneo kama ya rare earth. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika maeneo haya tayari tuna wawekezaji, lakini wawekezaji hawa wanagombea mitaji na nchi nyingine na kama hatutafanya maamuzi haraka ina maana hiyo opportunity haitakuwepo na hatutaweza kukua na kupata mapato makubwa ambayo kama tungekuwa na migodi kila mahali inafanya kazi, kila mahali inazalisha, tungekuwa na uchumi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema kwamba, mambo mengi yamefanyika ya kikodi hapa ambayo yanataka kusisimua uchumi, lakini tukiwa na utendaji na uzalishaji na migodi na huku wewe unalima uchumi huu siyo kwamba utasisimuka lakini utazimuka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niunge mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa mchango wangu katika mapendekezo ya
mpango wa 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhima nzima ni uchumi shirikishi na shindani. Nami nilikuwa namsikiliza jirani yangu hapa Mheshimiwa Engineer Magessa aki-analyze data za kuonesha namna gani uchumi wa nchi yetu unaonekana kwamba kukua kwake ni kwa asilimia 0.1 na amelinganisha sana na nchi nyingine. Nami nakubaliana naye kabisa, lakini mimi naona kabisa sababu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza inatakiwa tu interogate statistics zetu kama zinasema ukweli na ziko halisia kwa sababu kwa kuangalia tu wenzetu walikotoka na walikokwenda, inaonesha kabisa kwamba sisi tuna tatizo. Pia kuna tatizo zaidi katika uchumi wetu, kwa maana ya kwamba bado productive sectors hatujaweza ku- implement kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakwenda kwa mifano katika moja ya mapendekezo yangu na nitachangia zaidi kwenye sekta ya kilimo ambayo naielewa zaidi kwa sasa. Tukianza na zao la chai kwa mfano, sisi kama Tanzania bado tupo chini sana kwenye uzalishaji wa chai, na kwa kweli chai inaweza ikatupa faida na ajira kubwa. Zao la chai hata kama hupati kodi kubwa sana, lakini ni zao ambalo linaongeza sana ajira kwa wananchi wetu wa kawaida, na kwa hiyo, linaongeza sana multiplier effect kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, ni lazima tuhakikishe tunaendeleza kwa kiasi kikubwa zao la chai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotokea sasa, pamoja na mipango mizuri ya Wizara ya Kilimo, tunatakiwa tujue tunashindana kwenye zao hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu Kenya tayari wanazalisha karibu tani 570,000. Sisi bado tupo kwenye tani 30,000, lakini tuna wakulima wa chai ambao wanalima chai katika mazigira magumu. Naongelea wakulima wa chai wa Njombe, Tarafa ya Egweminyu kuna wakulima karibu 2,189, hao ni wakulima wa kawaida kabisa, smallholder farmers, siyo watu wakubwa. Hawa uzalishaji wao wa chai ni kilogramu milioni 3.6, lakini katika miaka mitano watakwenda kuzalisha kilogramu milioni 7.2, lakini ili waweze kufanya hilo wanahitaji kuwa na miundombinu wezeshi, sasa mpango wetu unaongelea vizuri sana kwamba kutakuwa na miundombinu wezeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhalisia ni kwamba wakulima hawa ukiangalia bajeti yao ya barabara za vijijini inaangaliwa kama bajeti ya TARURA. Ukienda kwenye TARURA wanapogawa bajeti wanasema, tutatoa Shilingi bilioni moja kwa kila Jimbo. Ukweli ni kwamba hatufanyi kazi kimkakati, tunataka wakulima hawa wafike kwenye huo uzalishaji wa chai, lakini ikifika kwenye barabara, hatuwapi fedha za kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtandao wa barabara wa Njombe nzima ni kama kilometa kama 890. Katika 890, hizi za wakulima wa chai hazihesabiwi. Peke yao, mtandao wao mzima wa chai hawa watu 2,100 ni kama kilometa 400. Kilometa 400 hizi hazina huduma, hazina msaada, hivi tutawezaje kuzalisha chai? Tunawezaje kusema kwamba tunaweza tuka-compete na Kenya, tunawezaje kuwawezesha watu wetu wakawa washindani kwenye ukulima wa chai? Kwa hiyo, hatufanyi mambo kimkakati ingawa tuna nia nzuri ya kufanya haya mambo kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye zao la parachichi (avocado). Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, amekwenda China akaweza kufungua Soko la China kwa maana ya kuanzisha. Hii imetengeneza matumaini makubwa sana kwa Watanzania na wakulima wa avocado. Hata hivyo bado kazi ni kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema, tunapoongelea kilimo shindanishi na uchumi shindanishi katika mazao haya ya kupeleka nje, hapa ndipo ambapo kwa kweli Serikali na mapendekezo ya bajeti lazima yaangalie kwa umakini sana ni namna gani matumaini ya Watanzania ambao wanalima avocado kwa kiasi kikubwa sana wamechangamkia zao hili, wataweza kufanikisha ndoto zao kwa kuhakikisha kwamba wanapeleka kwenye masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kufungua soko ni jambo moja, lakini kuna mambo mengine mawili. Kwanza ni ubora, na pili, ni gharama. Kwenye gharama ndiyo hapo pa kuja kwenye mpango. Kwenye gharama za export na hasa mazao ya horticulture Bandari yetu ya Dar es Salaam ndiyo moyo wa export na ndiyo moyo wa uchumi shindanishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia na tukilinganisha, kwenye zai la avocado unachogombania ni bei nzuri, lakini unachogombania, uwe na zao zuri. Moja ya kitu ambachoni ni cha muhimu sana kukiangalia tunaita shelf life. Kwa kweli watu wa THA wanatakiwa watusaidie sana kuongeza shelf life ya avocado yetu Tanzania. Tukilinganisha na Kenya, nitatoa statistic kidogo tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uki-export avocado kutoka Kenya, kwanza unapofikisha mzigo ambao uko kwenye kontena refrigerated, inachukua siku hiyo hiyo mzigo unaingia kwenye dock, unaondika kwenye meli. Ukichelewa sana ni ndani ya masaa 24. Hapa kwetu ukipeleka mzigo kwenye bandari utakaa kwa siku kumi kabla haujaondoka; kati ya tano mpaka siku kumi. Hiyo yote inakupunguzia shelf life ya product yako na matokeo yake ni kwamba wenzetu kwenye uchumi shindanishi wanaweza wakafikisha avocado kwenye soko zikiwa na shelf life ya siku kumi na tano. Sisi tunafikisha parachichi kwenye masoko zikiwa na Shelf Life ndogo sana ya siku tano mpaka siku nane. Kwa hiyo, matokeo yake itakuwa ni ngumu sana sisi kushindana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kwenye mpango, jambo hili limeelezewa vizuri kwamba tutaangalia miundombinu wezeshi, tutaangalia bandari zetu, lakini mara nyingi tunaongea mambo haya kwa ujumla sana, hatuendi kuangalia ni ni hasa kifanyike ili kusaidia wakulima wengi ambao wanahitaji kufikisha haya mazao na kuondoa umasikini wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuangalia hilo, kuna gharama. Kwa miaka mingi tutaendelea kutumia Bandari ya Mombasa tupende tusipende. Pia tuna uwezo mkubwa wa kutumia bandari yetu kuondoa kontena la avocado kutoka Njombe, kutoka southern highlands, au eneo lolote lile, unatakiwa ulipe zaidi ya mtu anayetoa kutoa kontena kutoka maeneo mengine kama ya Nairobi hata maeneo mbalimbali ya Kenya. Sisi tunatakiwa tulipe Dola 4,000 mpaka 5,000 kwa kontena kuliondoa huku na kulifikisha bandarini. Maana yake ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, inatakiwa THA itusaidie kwa kuhakisha kwamba moja, ipunguze angalau zile gharama za pale kwenye bandari, lakini ya pili angalau tuwe na dedicated birth, najua inaongelewa siku zote, lakini naomba kwenye bajeti hii Mheshimiwa Waziri tuje na mipango kabambe, ioneshe wazi kabisa plan yetu ni nini? Inakwisha lini? Lini itaanza kuwa implemented?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke shippers hawana mahusiano na mtu yeyote anayezalisha. Wao wanaangalia biashara yao ya ku-ship, wanaangalia risk ambayo ikoinvolved kwenye ku-ship products zetu, wao wataangalia lini walete meli hapa, na kama kuna mzigo wa kutosha, na kama hakuna risk yoyote ya hayo mazao kuharibika kabla hawajayachukua. Kwa hiyo, hayo mambo yanafanyika yote kwa pamoja na tuyaangalie kwa makini sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana utaona sisi tunaongelea kwamba uchumi wetu kama vile unakua pole pole, lakini ni kama uchumi umeshikwa, umefungwa, tuna bandari, wengine wameongelea SGR hapa, inataengenezwa lakini bado kule hatuangalii itafika wapi? Itatoa wapi mzigo? Haya ndiyo mambo ambayo yanafanya tuseme kwamba uchumi wetu ni mkubwa, mnasema uko stable, microeconomics ziko vizuri, lakini ni kama uchumi umekamatwa, umeshikwa, haupanuki na hauchechemki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuongelea kidogo tu sekta ya madini. Nilikuwa naangalia hapa kwenye Mpango. Ukiangalia kwenye kilimo, tunaongelea utafiti kwamba utafiti ufanyike kwenye mbegu, masoko na miundombinu, lakini ukija kwenye madini, bado suala la utafiti haliongewi hata kidogo, na ile ni moyo na uhai wa sekta ya madini yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuseme wazi kabisa kwamba tuna options mbili kwenye utafiti, au Serikali i-invest kiasi kikubwa kwenye makampuni yetu makubwa ya utafiti ya Kitanzani kama STAMICO, lakini tunachokiona, na nimesoma ripoti ya CAG; katika moja ya kampuni au mashirika ya kimkakati ambayo yana ukwasi ni pamoja na Shirika la STAMICO. Hawana fedha zozote za kutosha kufanya utafiti. Utafiti unataka fedha nyingi sana. Kwa hiyo, option iliyobaki ni kuwa na sekta binafsi iweze kuingia kwa kiasi kikubwa kwenye utafiti. Ila sekta binafsi haina urafiki na mtu, yenyewe inaangalia kwamba inaweza ikafanya hii kazi kwa faida huko mbele ya safari?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia sheria zetu kwa ujumla pamoja na improvement yote kwenye production, lakini bado kwenye eneo la utafiti sheria zetu hazivutii utafiti katika sekta ya madini. Kwa hiyo, mpango huu kama Waziri atakubali, wajaribu kuangalia ni kwa kiasi gani tunaweza tuka-incentivize zaidi sekta ya utafiti ili tuweze kuchimba madini mbalimbali. Mungu ametujalia madini ya kila aina katika nchi hii, kila kona unakoenda kuna madini.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimwa Mwanyika kwa mchango mzuri.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja iliyo mbele yetu. Nianze kwanza kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Alhaj Aweso kwa juhudi zake na nyingi sana katika kubadilisha Wizara hii. Lakini nimshukuru vilevile Naibu Waziri dada yangu Engineer Maryprisca, vilevile kwa juhudi zake nyingi. Nimshukuru lakini Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu na Watendaji wote katika Wizara hii. Tumeona kwa kiasi kikubwa sana tulikotoka, tulipo na tunakoenda nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Njombe kama unachangamoto kubwa kuliko zote ni maji. Ukiniambia changmoto tatu nitazitaja maji, maji, maji. Laikini Mji huu una kitendawili kikubwa sana wengi hapa wanalalamika maji kwa sababu maji inabidi yavutwe kutoka sehemu nyingi. Njombe ni tofauti, Njombe tuna maji mengi ya kutosha, tuna vyanzo vingi vya maji, lakini cha ajabu ni kwamba bado kuna malalamiko makubwa sana ya ukosefu wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wetu wa Njombe pamoja na Vijiji ambavyo vipo katika Jimbo la Njombe Mjini tunapata maji kwa kiasi, wakati mvua kwa kiasi cha kama asilimia 60 mpaka 65. Lakini wakati wa masika tunapata maji kwa kiasi cha asilimia 40. Huwezi kuamini kama hii ni sehemu ambayo ina mvua nyingi, ina maji mengi, ina chemchem nyingi, ina vyanzo vingi vya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yametokana na kutokuwa na mipango thabiti ya kuwekeza katika Miradi ya Maji kwa muda mrefu sana wa takribani miaka 20. Na Mji wa Njombe ni Mji unaokuwa kwa haraka sana kwa hiyo ulihitaji kuwa na mipango thabiti. Ndiyo maana nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri na Watendaji wote kwa kuwa na mipango thabiti sasa ya huko tunakokwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nipende kusema kwamba pamoja na changamoto hizi lakini bado wananchi wa Njombe wana matumaini na nitasema kwa nini wanamatumaini. Katika hiki kipindi cha bajeti iliyopita wananchi wa Njombe tumeweza bado kunufaika na yale ambayo niliyaleta hapa kama kilio. Tumepata Mradi wa Kibena Howard Awamu ya Pili kiasi cha kama milioni 800 tulitengewe na Rradi ule umeshatekelezwa kwa asilimia 90 bado kiasi kidogo kuna tank kubwa sana linajengwa katika maeneo yale litakaloleta lita 150,000. Ni maendeleo makubwa na watu wameanza kupata maji katika maeneo yale. Tunamshukuru sana na Mheshimiwa Naibu Waziri alitutembelea na alitia changamoto katika kuhakikisha jambo hili linafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kutuangalia na sisi watu wa Njombe. Pamoja na matatizo yetu na vilio vyetu, tulipata fedha za UVIKO kiasi cha Shilingi milioni 520. Tumeweza kuongeza mtandao na kuboresha mtandao wa maji ingawa bado tuna shida kwenye vyanzo. Kwa hiyo, tuna Kilometa 12 mpya za mtandao wa maji ambazo zimekwenda katika mitaa mbalimbali kama SIDO, Posta, Matalawe, Mgendela na maeneo ya Ngalanga ambayo bado yalikuwa na tatizo kubwa la maji. Tumeanza kuona dalili nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa na miradi mingine ya vijijini. Jimbo hili lina Kata za Vijijini na Kata za Mjini. Tuna miradi ambayo imekamilika, kama mradi wa Lugenge, Kisilo, Ihalula mpaka Utalingoro umeanza kutoa maji kwa mara ya kwanza. Tuna mradi wa Iduchu umezinduliwa tayari. Tuna mradi wa Kidunda na wenyewe kwa kiasi fulani umeanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuishukuru sana Serikali kwa maendeleo haya pamoja na hizo changamoto ambazo tunazo na bado ni kubwa na nitazielezea. Tuna miradi mingine midogo midogo ya vijijini ambayo tuna matumaini makubwa sana kwamba nayo itatekelezwa. Miradi hiyo ni kama vile Kijiji cha Kilenzi, wamekuwa na mradi wa muda mrefu ambao wao wenyewe walijitolea kutaka kuanza, tukawazuia tukisema Serikali yenu itawasaidia. Mradi huu najua sasa umetengewa fedha na nina uhakika katika kipindi hiki utatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna Kijiji cha Idihani na chenyewe kimeingia katika mpango wa utekelezaji katika mwaka huu wa fedha. Ombi langu kubwa kwa Wizara ni kuhakikisha kwamba fedha hizi ambazo zimetengwa hata kama ni kidogo kwa kuanzia, ziweze kupatikana kwa wakati ili Mkandarasi atakapoteuliwa aendelee na kazi mwanzo mpaka mwisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna miradi mingine miwili mikubwa ambayo na yenyewe ni muhimu sana katika kukomboa Mji wa Njombe kwa suala la maji; mradi wa Livingstone na Ijunilo wa kiasi kama cha Shilingi bilioni kama 10 hivi, ambazo na zenyewe tunajua ndiyo zinazohitajika lakini zilizotengwa ni fedha chache kwa muda huu kama shilingi bilioni moja. Tunaomba sana Wizara ituangalie, mradi huu uweze kupata fedha za kutosha ili uweze kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sasa kwenda kwenye matumaini makubwa na masikitiko makubwa ya watu wa Njombe. Mradi wa Miji 28 Njombe tulikuwemo, tumekuwemo siku zote, na namshukuru Mungu kwamba bado tumo katika mradi huu. Nimekuwa nikiwaambia wananchi wa Njombe kwamba Serikali yenu bado ina mradi huu na bado mradi huu utatekelezwa. Imekuwa ni vigumu kuamini kwamba ni kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku ya tarehe 16 Aprili, 2022 wananchi wa Njombe waliniweka Kitimoto kwa kupitia mtandao mmoja mashuhuri sana unaitwa Uwanja wa Siasa, wakitaka maelezo ya mradi huu. Niliwapa maelezo ambayo namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwamba ameweza kukamilisha nilichokisema kwa kusema, mradi huu upo, utatekelezwa na fedha zitapatikana. Hiyo ni habari njema na niwatie moyo wananchi wa Njombe Mjini kwamba mradi tulioungojea kwa miaka sita, sasa unakwenda kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe ombi. Mradi huu umechelewa sana, ulitakiwa uanze muda mrefu. Tunafahamu jitihada ambazo Mheshimiwa Waziri pamoja na Timu yake wamejitahidi kuondoa changamoto zote zilizokuwa zinakwamisha mradi huu. Tunafahamu na tunaelewa mchango mkubwa wa Mheshimiwa Rais katika kuukwamua mradi huu katika yale majadiliano na Serikali ya India. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaambiwa hapa kwamba kilichobaki ni Saini tu. Tuseme kweli, kwa wananchi jambo la kikwazo chochote hawaelewi, wanachotaka ni maji. Hata ukiwaambia kwamba Mkandarasi atakuja site wiki ijayo, hawaelewi, wanachotaka kuona ni maji.

Kwa hiyo, naomba lifanyiwe haraka, signing ifanyike kwa haraka na tumwombe Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyepo hapa aweze kuli-raise na Mheshimiwa Rais ili liweze kuangaliwa kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee mradi mwingine mkubwa ambao ulikuwa ni chechefu; mradi wa Igongwi wa Shilingi bilioni 4.5. Mradi huu ni wa maji ya mserereko. Namshukuru sana Waziri pamoja na Katibu Mkuu, kwani tulikuwa tumekata tamaa; ni mradi ambao utapita katika Kata tatu, katika Vijiji mbalimbali kama Kitulila, Kona, Danceland, Madobole, Lukonde, Njomlole na Majengo na unaishia kwenye Kijiji changu cha Uwemba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana fedha zipatikane. Nime-check kwenye kitabu, fedha iliyotengwa ni kama Shilingi milioni 600. Tunafahamu kwamba Mkandarasi alishapewa kama Shilingi bilioni 1.6 katika mradi huu. Fedha ambazo zinahitajika bado ni Shilingi bilioni tatu ziweze kutekeleza. Huu ni mradi ambao utakuwa na matunda makubwa na matokeo makubwa kwa watu wengi kwa mufa mfupi ukitekelezwa. Naiomba sana Serikali itekeleze mradi huu kwa haraka, umekuwa ukisubiriwa kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Njombe unakuwa kwa haraka na uko katika mchakato wa kuwa Manispaa. Moja ya mambo yanayochelewesha Mji wetu wa Njombe kuwa Manispaa ni kukosekana kwa majitaka. Mifumo ya majitaka hatuna mpaka leo. Nimefurahi kuona kwamba Mheshimiwa Waziri katika bajeti yake ameweka fedha kidogo ambazo zitatusaidia. Tunamshukuru sana kwa hilo, lakini naomba mradi huo na wenyewe utekelezwe kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumalizia kwa kuelezea jambo moja kwamba maendeleo yanakuja na changamoto nyingi. Mji wa Njombe unakua kwa haraka, mahitaji ya maji ni makubwa na yataendelea kuwa makubwa. Miradi hii iliyotajwa hapa itakwenda kumaliza hili tatizo na nina uhakika tutafikia kiwango ambacho Ilani ya Uchaguzi inatutaka tukifikie katika mwaka 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme, changamoto kubwa ambayo tutaipata, watu wengi wamechangamkia jitihadi za kulima parachichi katika Mkoa wa Njombe na hasa Mji wa Njombe na Vijiji vinavyozunguka Njombe. Parachichi watu wanazidi kuigundua kwamba bila maji huwezi kuizalisha kwa tija. Kwa hiyo, huko mbele tunaona tatizo la mashindano ya kugombea maji. Kwa hiyo, nitoe wito kwa Wizara hii ifanye coordination na Idara ya Umwagiliaji ili wanaotoa vibali kwa ajili ya umwagiliaji wa parachichi watoe wakitambua kwamba kuna watu wengi wanahitaji maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwa kumalizia, wakulima wa parachichi walio wengi hawatoki Njombe tu, wanatoka karibu Tanzania nzima wanakwenda kulima parachichi Njombe. Wengine hawawi wakazi wa Njombe, interest yao kubwa ni wafanyabiashara walime parachichi, wapate, wanahitaji maji. Katika hali hiyo, tunahitaji kutunza vyanzo vyetu vya maji visiingiliwe. Tu-balance kati ya matumizi ya maji kwa ajili ya wakulima wa parachichi pamoja na matumizi ya maji kwa ajili ya wananchi walio wengi ambao ni wakazi wa Njombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niwapongeze sana watendaji wote wa RUWASA pamoja na NJUWASA wa Njombe pamoja na Ma-Director General na hasa Injinia Kyauri wa NJUWASA na Injinia Malisa. Tunawashukuru sana kwa kunipa ushirikiano wa kuwatia moyo na kuwafikisha wananchi wa Njombe kule ambako wanakutegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja iliyo mbele yetu ya kilimo. Nianze kumpongeza sana mdogo wangu Mheshimiwa Bashe na Naibu Waziri na Watendaji wote katika Wizara hii. Kwa kweli wameonyesha njia, tunaona mambo yanakwenda vizuri, wamefanya ushawishi mkubwa, wamekuwa wasikivu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile namshukuru Mheshimiwa Rais toka mwanzo kabisa kwa kuonesha nia ya dhati kabisa na kutekeleza nia hiyo ya dhati kwa vitendo. Tulilalamika sana hapa Bunge lililopita kuhusiana na mbolea tukamwona Mheshimiwa Rais kwa nafasi mbalimbali kupitia Waziri Mkuu akatuambia asingeweza kulitekeleza jambo lile kwa sababu muda ulikuwa ni mfupi na fedha zilikuwa hakuna. Akatuahidi, analishughulikia. Tunamshukuru sana kwamba ameweza kulishughulikia hili jambo kwa wakati. Tumetoa ahadi majimboni kwamba linashughulikiwa na kwa kweli limeshughulikiwa. Ahsante sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sasa kuongelea mambo mawili; moja, ni kilimo cha biashara au ushindani ambacho ndiyo dira ambayo ndiyo inaonekana tunakwenda kwenye mazao ya kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema, kilimo cha ushindani au cha kibiashara tunapokiongelea tunaangalia ni namna gani tunafika kwenye soko. Vile vile tunaangalia vitu viwili; tunaangalia ubora na gharama. Ubora huo tunaupata kwa gharama gani? Sasa kuna mambo ambayo tumshukuru sana Mheshimiwa Bashe pamoja na Naibu Waziri na Wizara nzima, kuna mambo ambayo yapo ndani ya uwezo wao wameanza kuyafanya na tumeyashuhudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulizungumzia ubora kwamba lazima uanze kwenye miche, kwenye kitalu. Tulisema sana mwaka 2021 kwenye bajeti iliyopita na kweli wamelitekeleza, tumeona wazi kabisa wameanza mafunzo, wameanza kuwatambua wazalishaji wa miche na wengine wengi wamekuwa hapa kwenye training na wengine tumewaona hapa walikuja Bungeni kwa ajili ya kuangalia kinachoendelea hapa. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kutekeleza hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna mambo mengine ambayo nadhani pamoja na kuangalia ubora, bado tulikuwa tunamwomba Mheshimiwa Waziri ajaribu kuona ni kwa namna gani; kwa sababu kwa kweli kwenye mazao ya mbogamboga na parachichi lazima tukubali kwamba ubora ndiyo utakaotutoa. Hizo Shilingi bilioni mbili anazoziongelea Mheshimiwa Waziri au Wizara hatutaweza kuzipata kama hatutakuwa na ubora kwenye soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna mambo ambayo ni ya muhimu sana kuyaangalia kwenye soko ikiwa ni pamoja na kuangalia uthibiti wa ubora. Tulikuwa tumeongea hapa ni vizuri tukawa na agency au tukawa na chombo kitakachosaidia kwenye kuthibiti ubora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua na ninafurahi kwamba hata hilo nalo Mheshimiwa Waziri ametuonesha wazi kwamba lipo katika mchakato. Tunaomba likamilishwe mapema. Hatutaki chombo hiki kiwekwe kwa ajili ya kuingilia biashara, lakini tuna uhakika chombo hiki ni muhimu kwa ajili ya kuhakikisha kwamba hakutakuwa na mazao ambayo yatakwenda sokoni bila kuwa na ubora. Tuna uhakika chombo hiki kitapewa mandate zaidi ya kuhakikisha kwamba hili zao lenyewe linakuwa promoted. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema, kuna mambo ambayo Mheshimiwa Bashe na Wizara yake hawana uwezo na ni mambo ya muhimu sana ya kutelepeka kwenye soko. Zao hili la parachichi na mazao ya mbogamboga yanalimwa kwenye mashamba, lakini yanachukuliwa na wachukuzi, yanasafirishwa na wasafarishaji mpaka yanafika kwenye masoko, lakini ni mazao ambayo yapo sensitive, yanataka ubora wa hali ya juu, pia ni mazao ambayo yanapoteza ubora kwa haraka sana. Kwa hiyo, ni dhahiri kwamba yapo mambo lazima tuyafanye kwa umakini na kimkakati na hasa yale yanayohusiana na miundombinu kwa ujumla. Wengine wanasema kwa jina rahisi logistics. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli napenda kusema, tukianza na barabara, tuna vizuizi bado vinasumbua wasafirishaji wa mazao ya mbogamboga na mazao ya parachichi. Ukienda ma-gate fulani fulani, na kuna gate moja lipo pale Iringa, wana maswali mengi sana ambayo yanaonesha bado hawatambui kwamba maswali hayo hayasaidii sana kwa sababu mchukuaji amechukua perishable goods na maswali yanayoulizwa hayapo relevant. Kwa hiyo, naomba Wizara zinazohusika ziweze kutusaidia kwenye hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matatizo makubwa sana yapo kwenye maeneo ya Mamlaka zetu za Usafirishaji za Anga na Mamlaka ya Bandari. Kwa kweli kama tupo kwenye ushindani tutambue kwamba tunatakiwa kufanya kazi kubwa sana katika Mamlaka ya Bandari. Nafahamu kuna kazi kubwa inafanyika, lakini bado wana mambo mengi ya kufanya tukilinganisha na wenzetu, bado tupo nyuma sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, ukiangalia kwenye maeneo yetu ya Airport bado cold rooms facility hazina uhakika. Ukienda Songwe ambako kuna uzalishaji mkubwa wa parachichi Southern Highlands kwa mtu ambaye atataka kusafirisha kwa haraka, atapeleka Songwe Airport. Hatuna cold room facility pale au kama zipo, bado zinatengenezwa na zinakwenda pole pole sana. Ipo haja ya kuharakisha zoezi hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye Bandari yetu ya Dar es Salaam, hakuna dedicated berth, ipo ya export kwa ujumla, lakini kwa vitu ambavyo ni perishable hakuna dedicated berth. Ukienda kwa wenzetu ambao tunashindana nao wana berth zaidi ya tatu, nne, mpaka saba ambazo zipo dedicated kwa perishable. Wafanyakazi kwenye hizo berth akili yao yote kila wakati inafikiria ni namna gani wa-facilitate mzigo uondoke ili uweze ku-maintain ubora wake. Kwa hiyo, haya ni mambo ambayo Wizara ya Kilimo wanatakiwa wasaidiwe kimkakati kama nchi tuhakikishe kwamba tunafikia hilo lengo linaloongelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiangalie soko la nje tu kwenye mazao ya mbogamboga na parachichi, tuangalie na soko la ndani. Ipo haja ya kuwa na mkakati wa kuhakikisha zao la parachichi hata hapa ndani linapewa elimu ya kutosha, watu wafahamu, siyo kulima na kusafirisha tu, tunaweza tuka-process zao la parachichi hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeongolea gap la laki nne, mafuta hatuna ya kutosha, tunahitaji mafuta. Parachichi inawezekana. Kuna watu duniani wana technology ya kuzalisha parachichi kwa wazalishaji wadogo. Njombe sasa hivi tuna viwanda tisa vya packing na exporting ya parachichi. Viwanda vyote hivyo vinamilikiwa na watu toka nje, ukiacha kimoja tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge na Mheshimiwa Waziri, tuliangalie hili kwa makini sana. Nafahamu nchi ina mkakati wa kuwa na packing facility lakini tuelewe kwamba tupo kwenye ushindani. Hawa wenzetu wenye viwanda wakiwa na mazao kule kwao, mazao ya wakulima huku hawatayachukua kwa muda, watayaacha, wata- process, wata-export mazao yao. Kwa hiyo, ni vizuri tukahakikisha kwamba na sisi tunafanya hiyo shughuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwenye umwagiliaji; parachichi inahitaji maji kama vile chai. Tulipokuwa tunaongea mwaka 2021 hapa, namshukuru Mheshimiwa Waziri na timu yake wameweza kuwa na mkakati mzuri wa kufanya umwagiliaji. Sina uhakika ni kwa kiasi gani mkakati huo wa umwagiliaji unakwenda vile vile kwenye maeneo. Imeongelewa Njombe kwa ujumla, Mheshimiwa Waziri atakapohitimisha hapa naomba nielewe anaongelea maeneo gani huko Njombe? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake kuna maeneo ambayo ni ya flat, lakini maeneo mengi ya uzalishaji ya parachichi ni maeneo ya milima ambayo unaweza ukafanya umwagiliaji kwa urahisi sana. Ni kutafuta bonde la asili linazibwa, unapata maji mengi yanatawanywa, yanakwenda mbali, yanakamata wakulima wengi kwa pamoja. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile muda hautoshi, niongelee chai kwa haraka haraka…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwanyika muda wako umekwisha.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi naomba ni-windup.

MWENYEKITI: Sasa naona umegusia chai hapo. Mheshimiwa dakika moja basi, angalau. (Makofi)

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye chai tumeona matunda mazuri na tumeona mikakati mizuri, lakini bado napenda kusema, tuna Bodi ya Chai, tuna Wakala wa Chai. Kwa kweli pamoja na kazi wanazozifanya zinaonekana ni nzuri, lakini bado mandate zao hawazitumii vizuri. Kwa mfano, wakulima wa chai bado mpaka sasa wananyonywa sana kwa maana ya kwamba hawalipwi kwa wakati na wanadai madeni. Bodi ya Chai tuna uhakika inatakiwa iwasaidie hawa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi ni hawa watu Tea Agency. Hawa watu wa Tea Agency wanatakiwa waelewe kwamba zao la chai siyo lazima lilimwe na watu wakubwa. Unaweza ukawa na wakulima wadogo ambao wanaweza wakazilisha chai ikapelekwa na maisha yao yakawa mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema, hawa watu wa Tea Agency wamepata muda, walikwenda…

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwakagenda taarifa. Unataka kumuongezea taarifa kwenye dakika yake moja ya nyongeza siyo! Maana muda wake ulishaisha.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa taarifa.

T A A R I F A

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa taarifa mzungumzaji, anasema Bodi ipo vizuri, wakati huohuo anasema hawafanyi vizuri. Bodi haisimamii chai vizuri, aseme wazi. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwanyika, unapokea taarifa.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa kwa maana ya kwamba wana kazi nyingi ambazo wamezifanya na ni nzuri, lakini wana maeneo bado wako very weak hawa watu wa Bodi, na mojawapo ndilo nililolisema hilo la kwamba hawasimamii wakulima kupata fedha zao wanazozidai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuongelea suala la wakala kidogo tu. Nipende kusema…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwanyika nakushukuru sana kwa mchango wako, muda wako umekwisha.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye Mpango huu wa Tatu wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichangie maeneo machache; eneo la kwanza ni sekta binafsi kwa ujumla. Ni ukweli usiopingika kwamba kwa kweli kama tunataka kufanya uchumi ukue sekta binafsi haikwepeki. Sekta binafsi ni muhimu, kwa hiyo, tuiwezeshe ili iweze kusaidia kwenye kukuza uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachojitokeza kwa kiasi kikubwa sana kwa miaka hii ya karibuni, nachelea kusema kwamba sekta binafsi imeingia katika challenge kubwa sana na kwa kiasi kikubwa tumesikia kwamba baadhi ya wawekezaji katika sekta binafsi na hapa tunaongelea ngazi mbalimbali hatuongelei wakubwa peke yao, tunaongelea wakubwa wa kati na wadogo wamefika mahali wamekatishwa tamaa na baadhi yao wamefunga biashara au wamekaa pembeni wakiangalia kitachoendelea kama watazamaji. Hii haina afya kwa uchumi wetu na haina afya kwa mpango wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri jambo hili limeshapewa mwelekeo na Serikali. Nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kutoa kauli ambayo imetoa mwanga mpya kwa nchi yetu. Mkubwa akishasema watendaji tunatakiwa tuwe tumeshaelewa, this is the tone from the top. Kwa hiyo, tunatakiwa sasa watendaji wajipange wakijua mwelekeo wa nchi yetu inavyoiangalia sekta binafsi ni tofauti na ilivyokuwa miaka ya jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uhusishwaji wa sekta binafsi uko katika maeneo mengi, uko katika ngazi ya sera lakini uko katika ngazi ya mambo ya kikodi. Sekta binafsi ina vyombo ambavyo ndivyo maalum kwa ajili ya kufanya dialog na Serikali. Vyombo hivyo vipo, kazi imekuwa ikifanyika lakini wote tunafahamu mwisho wa siku challenges ambazo sekta binafsi inazipata wengi tunaambiwa hapa zimefikia mahali ambapo wote tunangoja kitu kinaitwa blue print mkakati ambao ndiyo unaenda kujaribu kushughulikia masuala mengi ambayo dada yangu pale Jesca amezungumzia, ametamka neno pale nisingependa kulirudia lakini urasimu ambao ndiyo upo umeonyesha kwa kiasi kikubwa unaua sekta binafsi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitoe tu angalizo hii blue print inayoongelewa ni karatasi tu tunahitaji kuwa na mindset change kwa viongozi wa Serikali. Tunahitaji kuwa na mindset change katika taasisi mbalimbali zinazosimamia mambo yote ya kiuchumi kuanzia Benki Kuu, TRA na vyombo vyote vya udhibiti kwa maana ya regulators. Hawa watu wasipobadilisha mindset ya kuiona sekta binafsi kama engine ya kusaidia kukuza uchumi tutakuwa tunatwanga maji kwenye kinu, hatutapata matokeo tunayoyakusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushirikishwaji wa sekta binafsi ni pamoja na kuifanya sekta binafsi ishiriki kwenye uchumi. Serikali ndiyo mtumiaji mkubwa wa rasilimali fedha ambazo mwisho wa siku zinaishia kwenye mikono ya Watanzania kwa kupitia shughuli zao mbalimbali. Tulichokiona ambacho mimi naamini kinadumisha uchumi wetu ni Serikali kuona kwamba inaweza ikafanya mambo mengine mengi yenyewe ya kibiashara. Tumeona Serikali wakati mwingine inajenga yenyewe, tumeona maeneo ambayo hata kazi za kawaida ndogo ndogo taasisi za kibiashara za umma ndiyo zinapewa zifanye kazi hizo, hii haisaidii kuinua uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumetunga sheria hapa za local content ambazo zinatakiwa zisaidie Watanzania ili waweze kushiriki kwenye uchumi. Napenda kusema sheria hizi zitabakia kuwa makaratasi tu kama Serikali yenyewe haitakuwa na initiative ya kuhakikisha mambo haya yanatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee eneo lingine la kilimo. Ndugu yangu pale ameshaongelea eneo la kilimo na maeneo ambayo ameyaongea mimi sitaongelea lakini ni ukweli usiopingika kwamba bado sekta ya kilimo itabakia kuwa ndiyo sekta kiongozi ambayo itasaidia kwa kiasi kikubwa kupeleka mbele uchumi wa nchi yetu. Sekta hii tunafahamu ina matatizo mengi na makubwa, inahitaji vichocheo vya kila aina na kikubwa kuliko vyote ni miundombinu wezeshi. Tumeshaongea kwa kiasi kikubwa hapa sitapenda kulirudia lakini kwa kweli tukubaliane kwa wakulima hasa wa mazao fulani fulani mkakati kama tutaendelea kutokuwa na utaratibu wa kuwa na umwagiliaji wa mazao yetu, nina uhakika sekta ya kilimo bado itaendelea kubakia nyuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuangalia Mpango ulivyoandikwa unaona bado umwagiliaji ni chini ya 20%. Mazao kama chai ambalo ni zao kubwa sana maeneo ya Nyanda za Juu Kusini, ili uweze kupata mavuno hasa unahitaji kuwa na miundombinu ya umwagiliaji. Kuna makampuni makubwa yanafanya uzalishaji wa chai lakini makampuni hayo sisi tunasema yana mchango wake tunahitaji kwenda sasa kuwa na wakulima wadogo wadogo wa chai walio wengi ambao watatoa mchango wa moja kwa moja katika sekta ya chai.

Mheshimiwa Naibu Spika, tujifunze kwa waliofanikiwa ukienda Bangladesh, sisi tuna viwanda 21 vya chai lakini Bangaladesh wana viwanda vidogo vidogo vya chai 700. Wao Serikali imechukua jukumu kubwa la kuhakikisha hili linatokea kwa sababu chai inaajiri watu wengi sana katika uchumi hivyo una uhakika wa kupata kodi nyingi katika uchumi wako. Siyo hilo tu unasaidia kuinua maisha ya watu na hii inaendana na dhana nzima ya uchumi shindani na viwanda kwa ajili ya maendeleo ya watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme moja ambalo limekuwa ni kikwazo kwa sekta ya chai. Chai ni zao la mkakati na la export lakini ukiangalia kuna tatizo kubwa sana la VAT. Kinachojionyesha ni wazi kabisa kwamba urejeshaji wa VAT katika maeneo mengi ya mazao ambayo yanapelekwa nje ya nchi umekuwa ni hafifu sana. Hii inawaondolea wawekezaji na wafanyabiashara mbalimbali uwezo wa kuweza kuwa na mtaji wa kuendeleza biashara zao na hiyo inaondoa na inapunguza ulipaji wao wa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kwa kifupi madini. Eneo la madini tumeona na tumeshuhudia mafanikio makubwa lakini naomba niseme wazi kwamba kama ambavyo Prof. Muhongo alituambia asubuhi na mimi nikazie tusijidanganye, tusipime success ya sekta hii kwa kuangalia mapato ambayo tumeyapata mpaka leo kwani hayatokani na kuongezeka kwa uzalishaji. Inawezekana kuna ongezeko la uzalishaji lakini sehemu kubwa ya ongezeko hilo limetokana na kazi nzuri ya Serikali ya kuzuia utoroshaji hasa uliokuwa unafanyika kwa kutumia njia za panya. Kwa hiyo, inaonekana kama kuna ongezeko lakini kwa kweli uzalishaji haujaongezeka, hakuna migodi mipya mikubwa iliyojitokeza au iliyojengwa katika miaka mitano mpaka sita toka tumebadili sheria zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, inabidi tuwe makini kwa sababu tunapoangalia Mpango tuangalie na threats za wapi tunaweza tukashindwa kuendelea. Mimi naliona hili bei ya dhahabu siku zote huwa inakwenda juu na chini, wakubwa wameshaanza kukaa na tunaweza tukaona hali ya stability katika ulimwengu ambayo itasababisha bei ya dhahabu pengine, hatuombei, ianze kwenda chini na mara moja tutapata impact kubwa negative kwenye Mpango wetu, hili tulielewe na tulitilie maanani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tufanyeje sasa? Tufanye yale ambayo tumeshayasikia, twende kwenye maeneo ya madini mengine ambayo ni muhimu na tusichelee kuona kwamba Liganga na Mchuchuma ni eneo ambalo hatuna sababu kwa nini mpaka leo hatujaweza kuanza kuzalisha pale mawe pamoja na chuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kama hiyo ni kengele ya pili. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika Bajeti hii ya Wizara ya Madini. Baada ya mageuzi makubwa katika sekta hii ya madini, tumeshuhudia sasa mabadiliko makubwa. Mchango wa sekta umeongezeka, kukua kwa sekta kumeongezeka kwa kiasi kikubwa. Mchango wake sasa hivi ni asilimia 5.2 ya pato la Taifa na bado unaendelea kwenda, imekuwa projected kwamba, utaongezeka zaidi. Kwa hiyo, niwashukuru sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote ambao wameweza kutufikisha hapa na hasa kwa kuweza kutupa matokeo ya haraka kwenye maeneo mbalimbali ya sekta hii na hasa kwenye utoroshaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu, kama nitakavyoeleza hapo baadaye tumeshuhudia sekta hii kukua lakini, hatujashuhudia sekta hii kuongeza uzalishaji kwa maana ya migodi mipya. Nianze kwa kusema Bajeti ya Wizara hii ni bilioni 66.8; kati ya hizo, bilioni 15.0 ni miradi ya mkakati na katika miradi ya mkakati tunaona kuna bilioni kama tatu zinakwenda STAMICO na bilioni 3.5 zinakwenda GST. Ni jambo jema kwa sababu, wengi wameongea hapa kwamba utafiti ni jambo la muhimu. Nipende kukazia maisha ya sekta ya madini yanategemea sana utafiti na utafiti wa uhakika. Wengi wamelia na kusema maneno mengi hapa hata kwa wachimbaji wadogo kuhusiana na suala la utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipende kusema kukua kwa sekta hii na kuongezeka kwa mchango wa sekta hii, kwa kiasi kikubwa bado naweza nikasema sio himilivu, inatakiwa tufanye kazi za ziada na sababu kubwa ni kwamba, bado sekta hii kwa kiasi kikubwa inategemea dhahabu kama zao ambalo ndio hasa linaifanya hii sekta ionekane na itoe mchango mkubwa. Kwa maana hiyo basi, kama nia ni kufanya by 2025 tufikie asilimia 10 ya pato la Taifa, bado tuna kazi kubwa kwa sababu, napenda kuliambia Bunge lako kwamba, dhahabu ina tabia ya kupanda bei na kushuka bei.

Mheshimiwa Spika, tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwamba bei imekuwa ikipanda na nilishawahi kusema humu ndani kuna majira yanakuwa mabaya. Kwenye sekta ya madini tunasema kuna bust na kuna boom, tupo kwenye boom la madini lakini bust na yenyewe iko mahali fulani. Kwa hiyo, tujiandae na cha kufanya kama nilivyosema mara ya mwisho tuanze kuangalia madini mengine na madini haya, tunasema ni madini ya viwanda (industrial minerals). Tuna madini ya kila aina katika nchi hii, tuna utajiri mkubwa cobalt, graphite, helium gas, rare earth, mwenzetu mmoja ameongea kuhusu niobium hapa asubuhi, kwa hiyo, tuangalie haya.

Mheshimiwa Spika, vile vile, tujitendee haki kwa kuangalia ukuaji wa sekta hii, kwa kuangalia jambo la exploration. Ni ukweli usiopingika kwamba, sekta ya utafiti kwa maana ya pesa ambayo inaingia ndani ya nchi yetu kufanya utafiti imepungua sana kama haipo kabisa. Hata kwenye Bajeti ya Mheshimiwa Waziri sijaona akiongelea pesa ya utafiti na utafiti unaoendelea ndani ya nchi kwa pesa inayotoka nje kuja kufanya utafiti hapa ndani, ni ya muhimu. Lingekuwa ni jambo jema tukafanya utafiti kwa pesa zetu, tunalipenda lifanyike hilo, maana litatupa nguvu ya kuweza kujua nini kiko wapi kwa ukubwa gani na kwa miaka mingapi? Hiyo itatusaidia kuweza kuongea na watu wote ambao wanataka kuwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na hali halisi tuliyonayo, inabidi tukubali kwamba uwezo huo hatuna. Tukitaka tufanye ili tujue kila kitu kiko wapi katika nchi hii, hiyo bajeti tunayoongelea ya bilioni 400 au 500 ya Wizara ya Madini itabidi tuzidishe mara tatu au mara tano tuizike yote kwenye exploration. Sidhani kama litakuwa ni jambo la busara wakati tuna mahitaji mengi makubwa. Hata hivyo, sekta binafsi inaweza kuifanya hilo, tena kwa vizuri kabisa. Tukubaliane kabisa kwamba, katika utafiti kuna utafiti wa aina mbili; kuna utafiti ambao unafanywa na migodi ambayo ipo tayari sisi tunaita, brown exploration na utafiti huu unaendelea bado kwa migodi ile kwa sababu, wanataka wao waendelee kuongeza mashapo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utafiti tunaouongelea ambao ni mkubwa wa kuongeza na kukuza hii sekta, ni utafiti unakwenda kwenye maeneo mapya ambayo bado hayajaonekana tunaita green field exploration. Tunahitaji kuwa na uwekezaji kwenye eneo la green field exploration, ni muhimu kwa uhimilivu wa sekta ya madini.

Mheshimiwa Spika, nNipende kusema vile vile pesa nyingi za uwekezaji katika sekta hii ya madini kwa upande wa exploration, mara nyingi ni pesa za watu mbalimbali wanakusanya na kuziweka na kuzifanya ziwe available kwa nchi au kwa wawekezaji. Nadhani baada ya miaka mitano ya kuwa na mafanikio mazuri baada ya mageuzi makubwa kwenye sekta hii, lazima tuanze kujiuliza maswali magumu. Hatuna budi kujiuliza ni kwa nini kwanza, hatupati hizi pesa kutoka nje za uwekezaji kwa maana ya exploration?

Mheshimiwa Spika, vile vile ni miaka 10 sasa, hatujaona migodi mipya ikifunguliwa katika nchi yetu. Tunasikia michakato ya kutaka kufungua migodi, lakini ni wazi tunatakiwa kuwa makini sana ili tuweze kuhakikisha kwamba nchi yetu inanufaika, ni jambo jema. Pia ni wazi kwamba, bado tunaweza tukanufaika kwa kufanya fine-tuning tu katika sheria zetu. Hatuna sababu, tumefanya makubwa kwa kufanya mengi ya kubadilisha sheria, lakini kuna mambo madogo tunaweza tukayafanya ambayo yanaweza yakatupa faida zaidi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Deo Mwanyika, dakika tano zimeisha.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, tuliambiwa dakika saba.

SPIKA: No, ni tano! Ili orodha niliyonayo iweze kutimia, tunashukuru sana. (Makofi)

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, basi, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja iliyo mbele yetu ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, ninamshukuru sana Mwenyezi Mungu kunipa uhai kuweza kusimama hapa kwa siku nyingine. Pili, ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Jumaa Aweso, kwa kutuletea bajeti nzuri na kwa kazi yake nzuri. Niwapongeze vilevile Naibu Waziri, Dada yangu Mheshimiwa Mahundi na Watendaji wote ndani ya Wizara wakiongozwa na Katibu Mkuu Injinia Kemikimba, Naibu Katibu Mkuu. Kwa namna ya pekee, Jimbo la Njombe, mimi ndiye Mwakilishi wao, naongea kwa niaba ya wananchi wa Njombe, ninawapongeza sana Maafisa wa RUWASA ambao nimekuwa nikifanya nao kazi kwa karibu sana katika siku zote hizi. Resident Manager Ndugu Shaka na Injinia Malisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Njombe lina mjini na vijijini na nitaiongelea hiyo kama moja ya sehemu yangu kubwa ya mchango wangu wa leo. Kwa hiyo nimpongeze Injinia Kyauri ambaye ni MD wa NJUWASA kwa maana ya kwamba yeye ana-cover eneo la mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya matatizo makubwa sana ya Mji wa Njombe toka nimeingia hapa Bungeni ilikuwa ni ukosefu wa maji katika Mji wa Njombe na katika vijiji vyake, jambo hili lilikua linaleta sintofahamu kubwa kwa sababu Njombe tuna vyanzo vingi vya maji, nami ninapenda toka ndani ya roho yangu kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan kwa kuwa mtu wa kwanza kutukomboa kwenye matatizo ya maji. Maji bado hayajaanza kutoka lakini tuna miradi ambayo inaleta matumaini makubwa sana kwa Mji wa Njombe kwa mara ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna miradi mikubwa mitatu pale Njombe Mjini ambayo italeta maji kwenye eneo la mji, pia tuna mradi mkubwa sana, naishukuru sana Serikali, mradi wa Benki ya Exim - India, mradi huu tumeungojea kwa hamu, sasa tunajua Wakandarasi wameanza kazi, kwa hiyo tuna uhakika sasa ahadi ambayo Chama cha Mapinduzi kilitoa kupitia Ilani, mimi Mbunge niliitoa na Mheshimiwa Rais akitembelea Njombe aliitoa kwa wananchi, kwamba utakapofika wakati wa uchaguzi tutakuwa na maji yanayomwagika, kwa lugha ya kwetu tunaita maji bwerere pale Njombe. Nafurahi sana kwamba mambo haya tutakwenda kuyatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna mradi mwingine nimeuona kwenye bajeti ya Mheshimiwa Aweso wa majitaka. Mji wa Njombe unakua kwa haraka sana na sasa tuko katika maandalizi ya kuomba kuwa manispaa. Kwa hiyo kwetu mradi wa majitaka ni mradi muhimu sana, tunakushukuru sana Mheshimiwa Aweso na timu yako nzima kwa kuona umuhimu wa kuipa Njombe mradi huu kwa wakati huu, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye jambo la pili ambalo ni kubwa sana kwangu. Nashukuru sana nina ushirikishwaji mzuri sana katika kupanga miradi hasa ya vijijini, katika kufuatilia nikagundua kwamba baadhi ya miradi ambayo tulitegemea tungeipata mwaka huu katika vijiji vyetu haijaingizwa kwenye mpango, nilivyozidi kudodosa na kuuliza nikakuta kwamba tuna mradi mkubwa wa Benki ya Dunia unaitwa P4R (Utaratibu wa Malipo kwa Matokeo) bilioni 350. Nilikuwa na matumaini makubwa sana kwamba vijiji vyetu vitaingia katika mradi huo, lakini kwa bahati mbaya sana havimo, maelezo yanaonekana kama yana-make sense lakini nilipenda nieleze na Mheshimiwa Aweso anisikilize kwa makini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tumeondolewa kwenye mradi huu ambao ni muhimu sana kwa wananchi wa Njombe. Njombe ni Njombe Mjini lakini asilimia 40 ya Njombe Mjini iko mjini, asilimia 60 iliyobaki yote ni vijijini, vijiji zaidi ya 40. Sasa complication hiyo na mradi huo mkubwa ambao una-cover maeneo ya vijijini, Njombe Mjini haimo kwa sababu ina jina linaitwa mjini, lakini Njombe actually asilimia kubwa ni vijiji. Inayo Kata 13, lakini Kata 10 zote ni maeneo ya vijijini, Kata tatu ndiyo za mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, umbali wa vijiji vya Njombe vijijini, niite sasa vijijini ili ieleweke vizuri, unakwenda kilometa 120 nje ya Mji wa Njombe, lakini siyo hilo tu katika Halmashauri zote za mji katika Tanzania, Njombe ndiyo Halmashauri ya mji iliyo kubwa kuliko zote, ina square kilometers 3,210.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika mazingira hayo ni kwamba lengo la kupeleka maji vijijini kwa asilimia 85, Mheshimiwa Aweso kwa ku-exclude Halmashauri ya Mji Njombe na Jimbo la Njombe Mjini, unakwenda ku-distort hiyo figure kwa sababu unabakia na vijiji vingi unavyoviona kwamba viko mjini lakini vyenyewe viko vijijini. Kwa hiyo ni vizuri sana jambo hili likaangaliwa upya tukawa realistic. Kuna majina hapa mimi nimeyakuta tu yako kisiasa, kuita Jimbo la Vijijini Mjini na hili jambo nimeshalifikisha TAMISEMI, tutaangalia huko mbele ili tusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana, hili ni ombi mahsusi kutoka kwa wananchi wa Njombe, kwamba tunaomba sana tufikirie upya kwenye ule mradi mkubwa ambao una- cover maeneo ya vijijini. Tulikuwa na vijiji kama vitatu au vinne ambavyo tayari vilikuwa vinaingia kwenye hiyo program, kuna Kijiji cha Lilombwi, Kijiji cha Ihanga hakina maji ni kijiji kikubwa na kina uwekezaji mkubwa, hivi vijiji vyote vina wawekezaji wakubwa wa parachichi, mahindi, viazi ni watu wanajiweza, hata ukiweka mradi pale kulipia wala siyo tatizo. Kwa hiyo tuwaangalie kwa jicho tofauti, nimelisema hili kwa nguvu sana kwa sababu nina uhakika Wananchi wa Njombe wananitegemea na wanategemea majibu kutoka kwa Mheshimiwa Aweso.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kulisema hilo, ninamshukuru sana Mheshimiwa Aweso, tuna mradi mwingine ambao nilipoingia hapa Bungeni ulikuwa mradi chechefu, mradi wa Igongwi. Maji ya mserereko ambayo yanakwenda kwenye Kata Nne, vijiji zaidi ya Kumi. Mradi huu tunaishukuru sana Wizara imeweza kutoa fedha kwa kiasi fulani mpaka hapo ulipofika. Mradi huu umefika hatua za mwisho, mradi huu bado una lot moja ambayo naishukuru tena Serikali kwamba imeingizwa kwenye bajeti hii, lot five kwa ajili ya kufanya mtawanyiko wa maji kwenye kijiji cha mwisho kabisa katika vijiji zaidi ya nane. Vijiji hivyo ni Kitulila, Kona, Denseland, Madobole, Luponde, Njomlole, Majengo, Uwemba na Ikisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Aweso bado tuna tatizo, nina uhakika kwamba mradi huu unapata fedha kutoka kwenye Mfuko wa Maji. Mfuko wa Maji kwa mwaka jana tunaambiwa kwamba ulipokea karibu bilioni 105, na ilikuwa ni kati ya mwezi Aprili mwaka huu ulikua ni asilimia 60. Kwa hiyo, ni wazi miradi ni mingi sana na mahitaji ni makubwa na Mfuko wa Maji hauwezi ku-cover miradi yote. Ndiyo maana umesema kwenye hotuba yako na mimi naungana mkono na wewe kwamba ni lazima tutoe vipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapanga vipi vipaumbele, umetuambia utapanga vipaumbele kukamilisha miradi ambayo imefikia hatua za mwisho ili wananchi waanze kupata maji. Nami napenda kusema mradi wa Igongwi umefikia hatua za mwisho kabisa, naomba sana kwamba mradi huu upewe kipaumbele katika kupewa fedha hizi za mwisho ili wananchi wa Njombe wa vijijini, vile vijiji vingine ambavyo vyenyewe viko vijijini kabisa, waweze na wenyewe kuanza kupata maji haraka iwezekanvyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kukumbusha kwamba Mheshimiwa Rais akiwa Makamu wa Rais, akiwa kwenye kampeni alisimamishwa na wananchi wa vijiji hivi walikusanyika na walimwomba sana vitu viwili, kimojawapo ilikuwa barabara hicho kimeshatekelezwa mkandarasi yuko site, pili ilikua ni kukamilisha mradi wa Igongwi. Kwa hiyo, ni matumaini yangu ukiongezea na nguvu na ahadi ya Rais mwenyewe kwenye mradi huu, tutaukamilisha kwa hizi hatua chache za mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme wazi kabisa, tumshukuru sana Mkandarasi ambaye alisimamia mradi huu, mradi huu

ulikuwa chechefu, tuliutoa ulikuwa mradi wa 2017 ulikuwa umekufa kabisa, 2020/2021 tumeuanza upya. Niendelee kusema kwamba Mkandarasi aliyesimamia mradi huu baada ya kuufufua amefanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba yako na Kamati wamesema kwa kweli tutoe motisha kwa wafanyakazi na makandarasi ambao wanafanya kazi vizuri. Kutoa pongezi ni moja ya motisha nzuri sana, tusiogope kusema kama mkandarasi ametufanyia kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkandarasi huyu ana madai bado, ninaomba sana mkandarasi aliyefanya kazi nzuri kwa kujitoa kizalendo kama huyu Jobea General Construction kwa kweli tumfikirie tumkamilishie malipo yake maana yake ni miezi sita toka ame-raise certificate yake na kazi karibu ameimaliza, naishukuru sana Kampuni hii ya Jobea kwa kazi nzuri sana iliyotufanyia Wananjombe.

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika hoja iliyopo mbele yetu ambayo ni hotuba ya Waziri wa Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema naunga mkono hoja hii iliyopo mbele yetu. Ninapenda vilevile nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu yake nzima, tunaanza kuona sekta inavyozidi kujipambanua, tunaanza kuona transparency kwenye hii sekta, uwazi, Waziri ametuonesha na ametuunganisha na wataalam wa kila aina katika maonesho ambayo tuliyaona hapa karibuni, kwa hiyo ninampongeza sana, ni jambo ambalo linaonekana ni dogo lakini ni kubwa sana, hiyo ndiyo inaitwa leadership. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kwa kuanza, kuongelea jambo ambalo nimelisikia leo hapa kwamba tayari tumefikia mahali ambapo LNG tutakuwa kwenye hatua ya kwanza ya kusaini. Hii hatua ni kubwa sana na sijui kama Wabunge wanaweza kuelewa vizuri kwa nini nasema ni kubwa sana. Jambo hili ni zito, uchumi sasa tunajua kuliko tulivyojua huko nyuma. Kwamba uchumi wa gesi ni uchumi ambao tutautegemea sana tunakokwenda lakini uchumi wa gesi siyo uchumi tu, gesi ni silaha, gesi ni usalama wa Taifa na Mheshimiwa Mwijage ameweza kuielezea vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema na kusisitiza, tunaomba sana kwamba haya majadiliano ambayo yamefikia mahali ambapo sasa wanakwenda kusaini wayakamilishe kwa haraka, hizo signing zifanyike na tuende kwenye hatua nyingine. Tumepoteza muda mwingi sana kwenye suala la gesi, tumepoteza muda mwingi sana, leo hii tusingekuwa hata na kilio cha haya mafuta ambayo tunayasema kwa sababu gesi hii tumekuwa nayo kwa miongo zaidi ya 40.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hilo nipende kusema kama alivyosema mdogo wangu Mheshimiwa Sanga, Njombe tunayo potential kubwa sana ya ku-generate power, peke yetu tunaweza tukafika megawati karibu 1,200 hata bila Nyerere Dam, Njombe tunao huo uwezo. Kwa sababu ukiangalia tuna megawati 600 pale Liganga na Mchuchuma, ukienda Ruhuji tunakaribu megawatt 360, ukija Lukamali hapa amepazungumzia kuna megawatt 200, ukienda Makambako tunazo megawati karibu 150 za upepo. Lakini tuna mito mingi midogo midogo na maporomoko ambayo yanaweza kuzalisha umeme kwa wingi. Kwa kiasi kikubwa tumekuwa mbali na tumetoa mchango mkubwa sana katika energy sector. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuongelea tu uzalishaji kutoka katika maporomoko madogo madogo. Nchi nyingine pamoja na yote wakiwa na uwezo wa kujaliwa na Mwenyezi Mungu kupata maporomoko ambayo Njombe tunayo, leo hii tungekuwa tunaongelea uzalishaji mkubwa sana wa umeme kutoka katika maporomoko mbalimbali ya mito midogo midogo katika Mkoa wa Njombe, kwa bahati mbaya sisi katika Jimbo langu bado tuna matatizo makubwa ya umeme. Nimepata faraja leo kusikia kwamba na umekuwa muwazi Mheshimiwa Waziri kusema kwamba kilichokwamisha ni nini na Serikali inakwenda kufanya nini. Nipende kumpongeza sana sana Waziri, lakini nipende kumpongeza Mheshimiwa Rais sana kwa haya makubwa mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hilo la LNG ni jambo kubwa anastahili kupongezwa na kwa kweli, kwa LNG nchi hii inaenda kuwa nchi ya uchumi wa gesi. Tunajua itachukua muda kwa vile tumechelewa, lakini tulipeleke kwa nguvu kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye maporomoko madogo madogo ambayo napenda kuyazungumzia. Pamoja na matatizo niliyonayo katika Jimbo langu ya kutokuwa na umeme kwenye vijiji zaidi ya takribani 20 mpaka leo hii na mitaa kadhaa kama 15, tumeweza kuzalisha umeme kutoka kwenye maporomoko haya madogo madogo. Ninapenda kusema tukienda kwenye kijiji kimoja kule kinaitwa Boimanda na Matola, pale tuna umeme ambao unazalishwa na Masista. Kuna mradi wa Masista ambao wameshaunza ni wa maporomoko. Mradi ule umekwama, na nipende kuishukuru Wizara kupitia REA wameweza kuwasaidia kwa kuwapa baadhi ya fedha. Mradi ule unahitaji 2.6 billion dollars wameweza ku-invest wao wenyewe kwa nguvu zao 1.6 billion dollars. Walikuwa na gap ya karibu one million dollars naongelea million dollars siyo billion. Serikali imewasaidia lakini Mheshimiwa Waziri nipende kusema, ukiangalia Masista wale ni Masista wa Benedict Getrude. Masista wale tayari wameshapeleka transmission line mpaka kwenye maeneo ya vijiji wakitegemea kwamba wangeweza kukamilisha generation. Kwa bahati mbaya hawakuweza kwa ukosefu wa fedha, Serikali imeamua kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TANESCO kwa makubaliano na REA walikubaliana waende kwenye maeneo yale, watumie transmission line ambazo zimeingia kwenye maeneo ya vijijini ili waweze kuchukua umeme ambao unatoka kwenye gridi ambao unapita yale maeneo kwenda maeneo mengine ya Ludewa, wautelemshe kwa transfoma uingie kwenye maeneo ya vijiji vile vya Matola na Boimanda na waweze kuwasha umeme mapema. Tunavyoongea wako gizani lakini wana nyaya za umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ninapenda kukuomba wakati umewaleta wataalam hapa niliweza kuongea nao kidogo lakini naomba utie mkazo ili transformer ile ambayo tayari imeshawekwa kwa gharama za TANESCO lakini haifanyi kazi iko idle, ifanye kazi ili wananchi wale waweze kupata umeme kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye jambo la pili la umeme wa maporomoko vilevile. Ninapenda hapa kuzungumzia mradi mdogo wa umeme unaitwa Mapembasi. Mradi huu ni wa siku nyingi, na ninapenda kusema toka mwanzo ni-declare interest kwamba ni mmoja katika waanzilishi wa mradi ule na mradi ule ni mradi ambao una Watanzania professionals katika Serikali, katika Mashirika ya Umma, vijijini wameungana, wamekusanya fedha zao, wengine wazee wamekusanya fedha ya pension kwa ajili ya kuendeleza mradi wa Mapembasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kusikitisha ni kwamba mradi huu mpaka leo haujaweza kuendelea na kinachokwamisha ni urasimu ambao umejitokeza kwa muda mrefu ndani ya TANESCO na hasa kabla ya TANESCO haijapata uongozi mpya. Nina matumaini makubwa sana mradi huu utakwenda kufanyika sasa. Pia mradi huu unapata tatizo ambalo tunasema ni la kiufundi, kwa sababu ndani ya vifungu vya sheria ambavyo Mheshimiwa Sanga hakuviongelea kwa undani, nipende kufafanua kidogo na hii ni miradi mingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria ambayo ni ya mwaka 2000 ni regulation inasema kwamba, hakuna mtu ataruhusiwa kuingia kwenye miradi midogo midogo ya SPPA kama uzalishaji wake unazidi demand katika maeneo yale ambayo yeye anazalisha umeme. Kwa hiyo, Njombe tunazalisha, tuna-consume megawatt Tano lakini Mapembasi wanaweza kuzalisha megawati 10. Kwa utaratibu wa regulation hii TANESCO hawawezi kuwapa mkataba Mapembasi kwa sababu wao wanazalisha umeme zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nadhani hata logic inakuwa defeated hapa, kwa sababu hawa wanazalisha umeme siyo kwa ajili yao, hawazalishi umeme kwa ajili ya Njombe, wanazalisha umeme kwa ajili yaku-feed kwenye gridi, uende kwenye maeneo mengine na ikiwezekana uuzwe mpaka nje ya nchi. Kwa hiyo, ni wazi kwamba sheria hii inawezekana iliwekwa kwa maksudi Fulani lakini nadhani imepitwa na wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumewasikia hapa Wajumbe wa kamati ya Nishati wakisema ikiwezekana ni vema tutumie kila nafasi yakuweza ku-generate umeme katika nchi yetu kwa kutumia rasilimali tulizonazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuna rasilimali zinachukua megawati 10. Tunawezaje kwa miaka karibu Saba bado tunasema kwamba majadiliano yanaendelea? Nimeona katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameongelea hapa, na nimshukuru Waziri toka ameingia amelisukuma hili jambo lakini bado linakwamba huko TANESCO. TANESCO wanataka umeme huu uuzwe siyo zaidi ya senti Saba American Dollars. Lakini sheria ya EWURA ya SPPA imeshaweka vigezo kwamba ukizalisha umeme kutoka katika maporomoko madogo madogo yasiyozidi megawati 10 unaweza ukauza umeme huo kwa senti 7.8. Lakini wao hawataki, sifahamu wana-interest gani na ndiyo maana watu wengine huwa wanakuja na mawazo kwamba labda kuna kitu ambacho wanakitaka. Kwa sababu sheria iko wazi, vitu viko wazi, lakini hatufanyi progress kwenye mradi huu mdogo wa Mapembasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Mheshimiwa Waziri uendelee na nguvu ile ile ambayo ulishaonesha kwamba utasukuma miradi midogo midogo na hasa ile ambayo iko ndani ya uwezo wa sheria. Hakuna mtu anavunja sheria hapa, sheria inaruhusu, ukiweza ku-develop na mradi huu siyo mradi mdogo ni mradi utakaotumia karibu Dollar Milioni 30 na watu wame-invest. Katika hao ma-shareholder tunao wazee wengi, Mzee Luhanjo alikuwa Secretary ni moja ya wanahisa kwenye mradi ule. Mzee Profesa Mbilinyi mpaka amekufa hajaona hata megawati moja ikizalishwa na ameweka hela zake pale, na kuna professionals wengi, Madaktari na Maprofesa kutoka Chuo Kikuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu ni moja ya mradi ambao ni mfano wa mkusanyiko wa Watanzania waliojitolea ili kuweza kutengeneza power iingie kwenye gridi. Unawezaje kuanza kusita, unawezaje kuanza kuwa na wasiwasi na mradi ambao Watanzania wameamua ku-invest na wanataka kuuza umeme kwa bei ile ambayo inakubalika kwa minajiri ya sheria ya Tanzania. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Deodatus.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na ninaomba nifanye marekebisho ya jina, naitwa Deodatus, ukipenda Deo.

Mheshimiwa Spika, nianze moja kwa moja kwanza kwa kusema kwamba, ninaunga mkono bajeti hii. Bajeti hii ni nzuri na niseme bila kificho nampongeza sana Waziri wa Fedha kwa kutuletea bajeti hii inayojaribu kuakisi wapi nchi hii inakwenda na wapi imetoka. Ni bajeti ambayo inajaribu kutilia maanani matatizo ya wananchi, inajaribu kuleta vilevile balance kwenye uwekezaji. Tumeona hatua nyingi za kikodi ambazo zimechukuliwa katika kuifanya sekta ya uwekezaji katika kilimo na viwanda iweze kuwa na hali nzuri zaidi, kwa hiyo nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa nampongeza Mheshimiwa Rais. Kwa kweli, kwa haya ambayo yanafanyika inaonesha kabisa ni uthubutu wa hali ya juu kabisa wa kutaka ku-address matatizo ya Watanzania. Tumeona mengi ambayo yamefanyika na hatuwezi kuyataja yote hapa maana muda hautatosha, lakini itoshe kusema nchi yetu imekuwa stable kiuchumi, macro-economic indicator zote zinaonesha tuko katika hali nzuri tunawazidi wenzetu majirani kwa kiasi kikubwa, inflation iko within reach katika single digit, Shilingi imeimarika, reserve ziko kwenye 4.8 na iko within reach. Haya yote ni maendeleo makubwa ni maeneo ambayo yanazidi kufanya uchumi uendelee kukua.

Mheshimiwa Spika, vilevile kipekee nipende kushukuru Serikali,kilio kikubwa cha wananchi ili kuwafanya wawe na hali nzuri tumeona Serikali imejaribu kuweka hiyo ruzuku katika mafuta ni jambo jema, lakini nipende kusisitiza na kusema kwamba, kama kuna eneo tutawasaidia wananchi ni kwenye mbolea.

Mheshimiwa Spika, tunaelewa fika kabisa Serikali ina mpango mahususi wa kutoa ruzuku kwenye mbolea. Niseme wazi kabisa wananchi wamepata matatizo makubwa sana kwa kulima bila kutumia mbolea, hasa maeneo ya kule Njombe, tunahitaji sana ruzuku ya mbolea. Na niombe sana Mheshimiwa Waziri aliwekee mkakati vizuri, Waziri wa Fedha ndiyo mtu ambaye sasa atatoa hizo fedha ili ziweze kwenda kwenye ruzuku. Kuwe na uratibu mzuri wa kuhakikisha ruzuku hii inawafikia wananchi kwa wakati na kusiwe na janja-janja ambayo itawafanya wafanyabiashara waweze kupata faida katika mwenendo wa ruzuku kwa hiyo, niombe sana jambo hili.

Mheshimiwa Spika, nikiwa kama Mjumbe wa Kamati ya Viwanda tulifanikiwa kutembelea baadhi ya viwanda na hasa tulitembelea viwanda vya chuma. Dhima ya bajeti hii ni kuwa na bajeti ambayo itafanya uchumi shindani, viwanda vya chuma kwa ujumla wake bado vina matatizo makubwa sana ambayo yanatokana na ushindani ambao hauko sawa au hauko linganifu.

Mheshimiwa Spika, ninapenda kusema ni vizuri, na ninashukuru Mheshimiwa Waziri amechukua baadhi ya hatua nyingi za kikodi na za kiutawala ili kusaidia viwanda hivi vya chuma, lakini bado kuna maeneo ambayo naona yanahitaji kuangaliwa kwa karibu ili yaweze kusaidia katika kuimarisha sekta. Sekta hii inaajiri karibu watu elfu 10, watu elfu tatu moja kwa moja na waliobaki wote ni mawakala na watu mbalimbali. Vijana wengi, machinga, wako katika sekta hii ya chuma kwa hiyo ni sekta muhimu sana kwenye kutengeneza ajira.

Mheshimiwa Spika, pia kuna maeneo ya kodi ambayo yalitakiwa yabadilishwe na recommendations zilitolewa. Kwa mfano, ukiangalia HS Code 7210.3 na 722599 unaona bado eneo hili lipo duty kwenye 25. Ilipendekezwa iwe 35, sasa wale wanaoingiza bidhaa nyingine za chuma ambao wale wanatengeneza migongo tu, hawa wanakuwa na advantage kubwa katika biashara hii na kwa hiyo, wana-affect wazalishaji. Kwa hiyo, iko haja ya kuangalia kwa karibu sana.

Mheshimiwa Spika, kuna eneo moja kwa sababu ya muda niliongelee, ni eneo la kitu iinaitwa PED ambayo ni Pre-Engineered Design Structures. Hizi structures ni muhimu sana kwa kilimo, ni structures ambazo ndio wafugaji hutengenezea mahema, maghala, viwanda na show rooms. Hizi structures zinaweza zikaagizwa kirahisi na watu ambao wanazileta kwa sababu kodi iliyowekwa hapa inawa-encourage wao kuzileta badala ya kampuni zetu kubwa za chuma ambazo zingeweza kutengenezwa hapa. Kampuni hizi zilikuwa zimeomba zipewe remission kwenye suala hili ambalo haijafanyika, ningependa sana kumuomba Mheshimiwa Waziri aliangalie lina-impact kubwa sana kwenye uzalishaji, kwenye kilimo na kwenye ufugaji. Kwa hiyo ni vizuri akaangalia hizo ni H Code 94062090.

Mheshimiwa Spika, nipende kuongelea kilimo, sisi wananchi wa Njombe ni wakulima wakubwa na tunashukuru sana kwamba kumekuwa na hatua mbalimbali ambazo zimepunguza baadhi ya kodi hasa kwenye misitu, sasa tunakwenda kwenye asilimia tatu ya cess, kwa hiyo hilo ni jema, tunamshukuru. Hata hivyo, tuangalie vile vile kwamba sisi tunalima chai kwa wingi sana pamoja na avocado. Njombe ina grow kubwa avocado hub lakini ukiangalia miundombinu na infrastructure bado iko nyuma sana.

Mheshimiwa Spika, nimeangalia kwenye bajeti ya Wizara ya Ujenzi, nimeangalia bajeti ya Wizara ya Kilimo, nimeangalia bajeti hii, sisi Njombe tunahitaji kuwa na Uwanja wa Ndege kwa sababu kwenye bajeti tunaongelea ndege tano zitaingizwa au zimeshalipiwa, lakini katika hizo tano moja ni ya mizigo. Hiyo mizigo inatakiwa itoke Njombe, tuna hub kubwa sana ya uzalishaji wa parachichi na itakuwa ni hub kubwa sana huko mbele ambayo inahitaji usafiri. Katika mipango ya Serikali hatulioni kabisa hilo likijitokeza, kwa hiyo niombe sana liangaliwe tena upya na Njombe iweze kuonekana ikipewa eneo hili.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni Liganga na Mchuchuma. Limeongelewa sana sana katika Bunge hili, mara ya mwisho tulivyoongea tuliambiwa kwamba mazungumzo yamefikia mahali pazuri, wengine wangeweza kusema yamefikia patamu. Hata hivyo, kinachojionyesha ni mradi wa mkakati ambao hakuna mkakati wowote ambao upo kwa sababu hakuna taarifa tunazopewa kwamba mazungumzo yamefikia wapi. Mradi ule una Liganga na una Mchuchuma, Mchuchuma ndiko ambako kuna makaa ya mawe, makaa ya mawe bei yake imepanda. Sisi Watanzania ni watu wa ajabu, tuna makaa ya mawe ambayo bei yake ni nzuri, lakini bado tunafanya mchezo na mradi huu.

Mheshimiwa Spika, nasema ni mchezo kwa sababu hatuelewi umefikia wapi, tunafahamu Mungu ametupatia haya makaa kwa muda mrefu na makaa haya sasa yana bei nzuri sana. Shirika letu la Maendeleo ambalo limepewa hili jukumu la kuendeleza huu mradi, tunaona kwamba aidha, halina uwezo au watu wetu wanao-negotiate hawajafika mahali ambapo wanaweza wakatuambia tatizo ni nini? Tunahitaji kama Watanzania na wananchi wa Mkoa wa Njombe kuelewa Mradi wa Liganga na Mchuchuma umefikia wapi. Nimwombe Mheshimiwa Rais aweke mguu kwenye mguu huu kama alivyofanya kwenye masuala ya gesi na LNG ili mradi huu uweze kukwamuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi huu una tatizo lingine ambalo ni kwamba, tunafahamu kabisa Paris Climate Agreement inafikia mwisho 2030 sasa tuna makaa ya kuzalisha kwa miaka 140 kwa tani milioni tatu kila mwaka, maana yake tuna tani zaidi ya 428 lakini tuna miaka nane tu ya uzalishaji kama tungekuwa tumeanza kuzalisha leo. Kwa hiyo unaona bado tuko katika maeneo ambayo hatuoni kwamba tuna mali inayoweza ikawaondolea umaskini watu wetu mpaka leo. Niombe sana Serikali iliangalie hili kimkakati na isiliangalie hili kama jambo ambalo liko kwenye bajeti na halifanyiwi kazi yoyote.

Mheshimiwa Spika, niongelee kwa haraka haraka Sekta ya Madini kama muda utaniruhusu. Nimemsikia Profesa Kabudi akiongelea, ukiangalia sekta hii uzalishaji wake umepungua katika bajeti hii kwa kiasi cha asilimia 7.2. Ukweli wa mambo ni kwamba ni kweli tulifanya mambo makubwa, tukabadilisha sheria zetu, lakini baada ya miaka mitatu ni wakati sasa wa kuziangalia hizo sheria kwa makini zaidi kwa sababu tulifanya haya mambo kwa haraka na kulikuwa na sababu za muda kwa nini yalifanyika yaliyofanyika, lakini ukweli ni kwamba wawekezaji walio wengi wakati na wa juu na hata wadogo bado wana matatizo makubwa sana. Sekta hii haikui kwa sababu moja hakuna migodi mipya na migodi ambayo itakuwa mipya inaongelewa pengine itafunguliwa 2025 ambayo utafiti wake ulifanyika zamani. Hakuna utafiti unaofanyika sasa hivi especially kwenye maeneo mapya ya green field.

Mheshimiwa Spika, vile vile financing kwenye Sekta ya Madini imekuwa ni ngumu kutokana na sheria ambazo zipo. Hatusemi hizi sheria zote ni mbaya, tunasema tukae chini tuangalie upya na ikiwezekana watu waziangalie hizi na jicho lingine, kwa sababu hasara mwisho wa siku ni kufanya utafiti ili uweze kuzalisha, ili uweze kuwasaidia wananchi wako kuondoa umaskini. Sasa kama hatuwezi kufanya hivyo, tunashukuru kwamba tuna sheria ambazo ukizalisha tuna uhakika na sisi tutapata kitu fulani kwa maana ya hizo hisa.

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye regulations mbalimbali za local content zinaongelea masuala yote ya procurement. Kwenye Serikali tumeanza kuangalia upya procurement kwa kiasi gani inazuia au inachelewesha miradi mingi, hata huku kwenye madini kuna hayo matatizo. Mfumo mzima wa manunuzi unatakiwa uangaliwe upya, ni vizuri kuwa na local content lakini tuiangalie isiwe na athari kwenye uzalishaji. Tumepunguza mapato kwenye Sekta ya Madini moja ya sababu ni kwa sababu uzalishaji umepungua. Uzalishaji umepungua kwa sababu kuna drawbacks nyingi katika mfumo, kwa hiyo kuna economics sense, kuna legal sense ya kuweza kuangalia upya. Ukiangalia kwa mfano sheria inayozungumzia participation ambayo Profesa ameiongelea, ni sheria inatupa Serikali 16%, ni jambo jema, jambo lenye afya, lakini wording ya section inayoongelea suala hilo, ukiangalia kwa makini sana ina ambiguity na kwa mwekezaji mpya yoyote akiisoma anaangalia kwamba inaweza ikawa interpreted kwamba hata ukiomba mkopo na mkopo ule ukiwa unarudishwa au ukiomba financing aina yoyote ikiwa inarudishwa, Serikali inatakiwa ipate 16% ya mkopo unaorejeshwa ndiyo sheria ilivyoandikwa na ndiyo ambavyo inaweza ikawa interpreted.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa mtu ambaye yuko nchini anaweza akaliangalia aka-assess risk akaona ni sawa, lakini kwa mtu ambaye anataka kuja Tanzania, anataka kutafuta fedha awekeze, atakuwa na kigugumizi kikubwa kuendelea kufanya kazi au kuja kukiwa na ambiguity kama hiyo.

Mheshimiwa Spika, ameongelea pia ring fencing, ni tatizo lingine kubwa, ni kitu kizuri kilifanyika katika Sheria ya Madini lakini kilifanyika katika Sheria ya Kodi ya mwaka 2004. Ring fencing ina-apply vizuri na ina-make sense pale ambapo una uzalishaji, ukiweka ring fencing kwenye exploration ni kwamba unaua utafiti, hakuna mtu anakuja kufanya utafiti asiweze ku-recover gharama zake. Kwa hiyo ni vizuri tukawa sober, tukarudi nyuma kidogo, tukaangalia haya mambo kwa jicho lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika hoja iliyo mbele yetu ya Wizara ya Maji. Nianze kwa kumpongeza Waziri na watendaji wote ndani ya Wizara hii kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kuhakikisha Watanzania wanapata maji. Naelewa kwamba ni kazi ngumu na tunaelewa kwamba ina changamoto nyingi lakini niseme tu kwamba kazi hii wamepewa ni lazima wafanye kwasababu iko ndani ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwamba wananchi wa Tanzania wa vijijini kwa asilimia 82 watapata maji na asilimia 95 watapata maji ifikapo mwaka 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hayo maneno ndani ya Ilani watu wa Njombe bado yanatutatiza Mji ya Njombe Wabunge wengi hapa wamelalamika na wanalalamika kwamba hawana maji ni tatizo kubwa lakini wengi wanalalamika kwa vile wana uhaba wa maji, lakini Njombe ni tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tuna maji ya kutosha, tuna maji mengi, tuna mito inapita kati kati ya mji wetu wa Njombe upande wa huku kula Agafilo upande huku kuna mto mwingine wa Ruhuji lakini tuna visima ukichimba tu unapata maj. Pia tuna maji ya chemichemi lakini cha kushangaza ni kwamba bado mji wa Njombe tatizo kubwa kero kubwa kuliko zote ni maji, hatuna maji ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Njombe wanapata maji kwa kiwango cha asilimia kama 60 tu na wakati wa kiangazi inakuwa mbaya zaidi, sasa niseme ni aibu lakini ni aibu ambayo lazima tuishughulikie. Kumekuwa na miradi midogo midogo ambayo Serikali imekuwa ikiitekeleza kwa ajili ya kutoa tatizo hili na Rais alipotembelea Njombe Marehemu Mungu Amrehemu mara mbili alipouliza shida yenu hapa ni nini wananchi wa Njombe walisema ni maji mwaka 2015 akigomea alisema shida yenu nini watu wakasema ni maji alipokuja tena kuomba kura akawauliza watu wakamwambia hatujapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Prof. Mbarawa alikuwa pale aliitwa na akasema kwamba atahakikisha ndani ya miaka miwili maji yanapatikana ni miaka mitano sasa wananchi wa Njombe mjini hawana maji tunaongelea mjini. Jimbo la Njombe Mjini lina kata 13 kata 10 ni za vijijini na Kata tatu ni za mjini naongelea kata za mjini hazina maji sijaenda hata vijijini bado, tatizo ni kubwa tunafahamu kabisa kuna mradi mkubwa ambao umekuwa ukiongelewa lakini sisi wana Njombe tunapata wasiwasi bado hata na mradi huu mkubwa ambao tunasema wa miji 28.

Mheshimiwa Naibu Spika, na sababu kubwa ni kwa vile tulikuwa ndani ya miji 16 au 17 scope yake ilikuwa inaeleweka sasa tunaongelea miji 28. Kwa hiyo, fedha zilizotengwa ni hizo hizo miji imeongezeka shida kubwa ya Njombe kwa miradi ya nyuma ilikuwa ni kwamba bado ilikuwa ni miradi ambayo haiwezi kutatua tatizo kwa kiasi kikubwa tukaambiwa huu mradi mkubwa unakuja kumaliza tatizo tunapata wasiwasi kama kweli mradi huu utamaliza tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimuombe Waziri atuhakikishie wana Njombe kwamba maeneo yote yaliyokuwa kwenye scope yatapata maji, maeneo ya Magoda yatapata maji, maeneo ya Lunyanyu yatapata maji Chuo Kikuu cha Lutheran kitapata maji, maeneo ya Ngalange yatapata maji na maeneo ya Msete yatapata maji, mji wa Njombe ni katika miji inayokuwa haraka sana katika Tanzania ukuaji wake ni karibu asilimia 3.5 ni kidogo juu ya average kwakweli na kuna eneo la Nundu linakuwa kwa kasi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana Mheshimiwa Waziri hata kama scope imebadilika watu wa Njombe wawaangalie kwa tofauti kwasababu ni mji mpya ni Mkoa mpya, Mikoa mingi iliyoongezwa ina miradi mingi ya maji, hapa Njombe hatujawahi kupata mradi mkubwa hata mmoja wa Serikali, na ndio maana Rais alisema wazi Njombe tutahakikisha maji yanapatikana na Mheshimiwa Prof. Mbarawa ni shahidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo jingine tuna mradi mwingine mkubwa ambao umekuwa ukiendeshwa kwa takribani miaka mitano sasa miaka sita unaitwa EGOGWI ninashukuru kwamba mradi huo umeonekana katika bajeti ya Mheshimiwa Waziri lakini bado ni kwa kiwango kidogo sana cha fedha, mradi huo ni kama wa bilioni nne wakati Mheshimiwa Rais Mama Samia anapita katika maeneo ya Njombe kuomba kura alisimamishwa eneo ambalo mradi unapita na akaahidi kwamba maji yatapatikana katika eneo hili. Nimkumbushe Mheshimiwa Waziri kwamba kwakweli ahadi ya Mheshimiwa Rais ambaye wakati huo alikuwa ni mgombea ilikuwa ni kwamba maji lazima yatoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nipende kusisitiza mradi ule ni moja ya miradi ambayo hadi leo haijakamilika kwasababu ninaamini ni uzembe wa watendaji waliopita ndani ya Mamlaka ya maji wakati ule ilikuwa chini ya halmashauri kwakweli tunauhakika kabisa na tunaomba tunapokwenda mbele wataalam wafanye stadi za kutosha za maeneo kujua kama kuna maji ya kutosha na wahakikishe wanatumia hata wananchi wa kawaida kuwaeleza kwamba jamani pamoja na stadi zetu eneo hili lina maji ya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, wataalam kwenye Mradi wa EGOGWI waliambiwa kwamba chanzo hicho mnachotaka kuweka vijiji zaidi ya nane hakitoshi lakini walibisha matokeo yake pipe zimewekwa maji hayatoshi scope imebidi ianze kuandaliwa upya, ninadhani ni matumizi mabaya ya fedha za Serikali. Kwakweli Mheshimiwa Waziri tunawashukuru sana Watendaji ambao wako RUWASA kwa sasa maana yake wameweza kuja na mradi mpya ku-scope upya hilo eneo na kuja na mradi mpya ambao unatupa moyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini watendaji waliopita nadhani ni vizuri kauli ya Rais ianzie hapo kuhakikisha mnashughulika nao maana yake wapo na wapo kwingine na huko watafanya hivyo watafanya hivyo watatengeneza miradi isiyotoa maji na fedha za Serikali zinatumika, ni vizuri tukachukua hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kuongelea mradi mwingine mdogo wa mji wa Njombe eneo la Kibena, tunaishukuru Serikali ilitumia fedha za kutosha kwa kiasi fulani kuleta maji katika mji wa Kibena Kata ya Ramadhani. Lakini kilichotokea ni kwamba ndani ya mradi huo mdogo maji yameweza kuja kwa maana Serikali imeweza kuongeza Capacity ya pumps imejenga Intech mpya imeongeza mabomba ukubwa wake kutoka inchi tatu mpaka inchi tisa, sasa kuna maji ya kutosha na hospitali yetu ya Wilaya ya Njombe ya Wilaya inapata maji ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha kushangaza na cha kusikitisha ni kwamba eneo lile lina wananchi wengi waliounganishwa ni wananchi kama 3,000 bado kuna uhitaji wa watu wengine 3,500. Hapa niliuliza swali la msingi nikaomba kwenye swali la nyongeza kwamba tunaomba eneo la Kibena ile project ambayo maji ni mengi yanaonekana yanamwagika iongezewe fedha kidogo basi ili distribution line iweze kuenea na watu wapate maji kuliko wao wapo mjini wanaangalia maji kwa macho na maji yanamwagika kwenye matenki sababu tu project ya kwanza ilikuwa ni ndogo haikukamilika, nakuomba Mheshimiwa Waziri uliangalie hilo kwa jicho la huruma kwa wananchi wa Njombe eneo la Kibena ili angalau tupate fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sijaona fedha zimetengwa katika bajeti hii labda kama nimeshindwa kusoma maeneo yote, lakini sijaona eneo lolote ambalo Kibena Project ya kuongezea ili wananchi waweze kupata maji ya kutosha, wananchi 3,500.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kunipa hii nafsi na niombe kwa kumalizia kwa kusema tuna matumaini makubwa sana na Mheshimiwa Waziri na wana Njombe wanamatumaini makubwa sana na Mheshimiwa Waziri Mheshimiwa Naibu Waziri na Katibu Mkuu wa Wizara hii wanachapa kazi lakini tutawapima kwa matokeo wana Njombe watawapima kwa matokeo niwatie moyo kwamba bado tunategemea kwamba mtafanya kazi nzuri na mtakamilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja iliyopo Mezani. Nianze kwanza kwa kuunga mkono hoja, lakini niseme sekta hii ya kilimo ndiyo inabeba maisha ya Watanzania walio wengi. Kwa hiyo, ningetegemea labda wangekuwa na bajeti kubwa ya kutosha, lakini matarajio hayo na bajeti iliyopangwa ni sidhani kama itakidhi matarajio ya wengi.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, nianze kwa kusema bado nampongeza Waziri na Naibu Waziri na Watendaji kwa juhudi zao mpaka muda huu. Kwenye bajeti hii nilichokiona pamoja na kwamba hakuna pesa za kutosha, lakini wamejaribu kuweka maeneo ya mikakati ambayo yanakwenda kushughulikia baadhi ya matatizo.

Mheshimiwa Spika, napenda kusema, itategemeana sana kama hata hiyo pesa ndogo iliyotengwa kama itapatikana. Kama isipopatikana tutakuwa tunatwanga maji kwenye kinu na sidhani kama kuna mafanikio yoyote ambayo yatapatikana kulinganisha na matarajio.

Mheshimiwa Spika, napenda niongelee mazao mawili ambayo ndiyo yapo katika Jimbo letu la Njombe Mjini, lakini yapo katika Ukanda mzima wa Nyanda za Juu Kusini. Tukianza na chai, wachache wameliongelea humu ndani, lakini ni zao ambalo tuna uhakika na tunaelewa kwamba kwa sasa hivi ni zao ambalo katika soko la dunia bei imetikisika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, nchi yetu uzalishaji wa chai umeshuka chini kwa maana ya majani mabichi ya chai, lakini napenda kumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Mheshimiwa Waziri, walikuja Njombe tarehe 10 mwezi wa Tatu, wakakaa na wadau wa chai, tukawaeleza matatizo yote ya chai, kwa hiyo, tukayajenga tukaweka mikakati.

Mheshimiwa Spika, jambo kubwa ambalo wanalielewa ni kuhusiana na umwagiliaji. Tunahitaji tija kwenye zao la chai, tunahitaji kuwa na bajeti ya kutosha ya umwagiliaji. Nimeona katika bajeti ya leo kwamba umwagiliaji umepewa pesa kidogo. Nina matumaini makubwa kwa sababu Mheshimiwa Waziri alikuja Njombe, akayasikia mwenyewe. Katika pesa hizo atahakikisha kwamba wakulima wa chai wa eneo hilo wanaangaliwa.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ni la muhimu…

T A A R I F A

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa.

MHE. JUSTINE L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nataka nimtaarifu msemaji kwamba, wakati wanahangaika na umwagiliaji pale Kilolo kuna eka zaidi ya 300 za chai. kwa miaka 30 ile michai sasa inachomwa mkaa; na hata hiyo ambayo mvua inanyesha yenyewe, bado haijafanywa kitu chochote na hakuna kiwanda na majani hayachumwi.

Mheshimiwa Spika, nampa taarifa hiyo ili aweze kujenga hoja vizuri. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Deo.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa yake, nami nilikuwa naenda huko. Najua wanakwenda kuongeza uzalishaji wa chai, lakini nilisema kwamba waanze na maeneo ambayo tayari chai ilishalimwa na imeachwa porini na mojawapo ni hilo la Kilolo. Ndiyo maana naongelea Nyanda za Juu Kusini na chai.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine kubwa ni miundombinu wezeshi katika zao la chai. Ni ukweli usiopingika kwamba kama hatuta-address tatizo la miundombinu wezeshi kwenye zao la chai hatutapata mafanikio wala hatutapata yale malengo yetu ya kuongeza uzalishaji wa chai kutoka tani 37,000 kwenda kule ambako wanataka, hatutafanikiwa.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni ambalo limeongelewa sana hapa, la ugani, ni jambo la muhimu sana. Naelewa kwenye chai kwenye eneo la Njombe kuna Kampuni ya NOSC ambayo imeleta ushirikiano mkubwa na imesaidia, lakini kuna maeneo mengi bado tunahitaji Maafisa Ugani.

Mheshimiwa Spika, naelewa umeliongelea hapa ukielezea kwamba Serikali haiwezi kuajiri. Ni kweli haiwezi kuajiri Maafisa Ugani wa kutosha, lakini kuna wakulima wadogo wadogo wa chai ambao wanahitaji msaada mkubwa wa Maafisa Ugani. Kwa hiyo niombe waendelee kuliangalia na nimeona kwamba bajeti yao imeongezwa.

Mheshimiwa Spika, soko ni tatizo kubwa sana, Njombe na zao la chai soko letu sisi ni viwanda, kiwanda kikifanya kazi maana yake tuna soko. Kinachojitokeza, Njombe tuna viwanda vinne vya chai, tuna uhakika wa hilo soko, lakini kwa bahati mbaya, katika waendeshaji wa viwanda vya chai katika Mkoa wa Njombe na maeneo yote ya Njombe ni mwekezaji mmoja tu ya Unilever ambaye yeye anaendesha kwa ufanisi na anaweza kulipa wakulima. Waendeshaji wengine wa viwanda vya chai ni jambo la kusikitisha sana kwamba wameshindwa kabisa kuwalipa wakulima wa chai. Naelewa jambo hili Waziri Mkuu aliliingilia, Mkuu wa Mkoa ameliingilia, Waziri amelisikia, lakini bado tatizo bado linaendelea. Tunaomba sana Serikali ioneshe kwamba ni Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika kiwanda kilichobaki kimoja ambacho kinafanya kazi kina tatizo bado la kupata majani ya chai ya kutosha. Kuna uwezekano kama tatizo hili halitakuwa-addressed, kwa sababu mfumo wa kile kiwanda ilikuwa ni kupata majani ya chai kutoka kwa wakulima wadogo wadogo, majani ya chai hayatoshi. Ni kweli kwamba maeneo mengine yanayozalisha majani ya chai yanaweza yaka-supply kiwanda kile, lakini kwa sababu ya mikataba ambayo imeingiwa, wakulima wale wanatakiwa wapeleke chai kwenye kiwanda au viwanda vya yule mtu ambaye hawezi kulipa ambaye ni Mkenya wa Kampuni inaitwa DL Group.

Mheshimiwa Spika, hili ni jambo ambalo Wananjombe hatulikubali kwa sababu kama wananchi wanaweza wakapeleka majani kwenye Kiwanda cha Unilever ambacho kinalipa kwa nini wazuiwe. Kwa hiyo, naiomba Bodi ya Chai ifanye kazi yake, lakini namwomba vile vile Mheshimiwa Waziri naye aingilie…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Deodatus Mwanyika.

DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri ambayo amekuwa akifanya.

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya Mheshimiwa Waziri tunaambiwa sasa ni vijiji karibu 1,952 ndiyo bado havijapata umeme na katika REA III round II ndiyo vitapata umeme. Kwa Jimbo letu la Njombe tuna tatizo na nilishaonana na Mheshimiwa Waziri kumueleza matatizo ambayo tunayo. Njombe ni vijiji vinne tu ndiyo ambavyo vimeingia katika mradi wa REA III round II. Mheshimiwa Waziri alinihakikishia kwamba kulikuwa na makosa na kwamba vitajumuishwa.

Mheshimiwa Spika, Waziri ametushauri hapa kwamba tuwasiliane na wakandarasi ili tuweze kujua scope ya kazi yao na wanafanya nini. Nimewasiliana na wakandarasi kama Waziri alivyosema lakini cha kusikitisha ni kwamba wakandarasi mpaka sasa scope yao ya kazi inafahamu hivyo vijiji vinne tu.

Mheshimiwa Spika, naelewa pengine kuna mchakato wa kubadilisha hiyo scope lakini nimuombe Waziri kwa niaba ya wananchi wa Njombe awahakikishie kwamba vijiji vile 20 vyote vitaingizwa katika mpango huu.

Tunaomba sana asitupeleke kwenye Peri-Urban Project maana vijiji hivi ni vijijini kabisa siyo maeneo ya mjini kwa vile Jimbo la Njombe linaitwa Njombe Mjini. Vijiji hivyo ni kama vifuatavyo; Makoo, Ngelamo, Mamongolo, Lugenge, Kisilo, Kiyaula, Idihani, Utengule, Ngalanga, Uliwa, Igoma na kijiji ninachokaa mimi vilevile kina matatizo cha Makanjaula nacho hakina umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimuombe sana Waziri atuangalie kwa jicho la huruma. Njombe program nzima ya REA I, II, III zote hizi kwa kiasi kikubwa sana zimekuwa propelled na Mkoa wa Njombe kwa sababu sisi ndiyo supplier wakubwa wa nguzo karibu zote ambazo zinakwenda katika project hizi zote. Kwa hiyo, tuna kila sababu ya kuona Mheshimiwa Waziri na sisi anatuangalia.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa namna ya pekee nimuombe Waziri, tuna Shule ya Sekondari Yakobi, REA III round I uli-target taasisi mbalimbali za afya na za elimu lakini kwa bahati mbaya sana shule hii ambayo ina watoto karibu 600 mpaka leo wako gizani. Tunamuomba sana Mheshimiwa Waziri ajaribu kuiingiza shule hii nayo ili iweze kupata umeme katika kipindi hiki.

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee suala la nishati jadidifu. Sekta madhubuti ya nishati ni ile ambayo ina mchanganyiko wa vyanzo mbalimbali vya umeme. Kwetu hapa tunaona kabisa kwamba kwa kiasi kikubwa umeme wa maji na umeme wa gesi ndiyo unachukua sehemu kubwa lakini tuna potential kubwa ya kuwa na umeme tofauti na huo au wa kuongezea kama umeme wa upepo au solar. Wawekezaji siyo kama hawapo lakini majadiliano na wawekezaji hawa yanachukua muda mrefu sana. Njombe tuna potential ya kuzalisha mpaka megawatt 150 kwa umeme wa upepo kama vile wenzetu wa Singida. Mheshimiwa Waziri ametuambia wanakwenda kufanya majadiliano na ni kweli wawekezaji tunajua wameshaitwa kwa majadiliano lakini majadiliano haya yafike mwisho basi ili na umeme wa upepo nao uingie katika mpango wetu wa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama muda utaniruhusu niongelee kidogo kuhusu mradi wa kusindika umeme wa gesi. Kwenye vitalu Na.1, 2 na 4 ndipo ambapo tunategemea kwamba mradi huu mkubwa wa LNG utajengwa au utapata resource yake ya umeme. Tuseme wazi Tanzania ina bahati kuwa na endowment kubwa sana ya gesi 57 tcf ni umeme mkubwa, ukiu-put kwenye context ni umeme ambao unaweza uka-power nchi ya UK kwa miaka 20 bila wasiwasi, kwa hiyo, ni umeme mwingi mno. Hata hivyo, suala siyo kuwa na resource ni namna gani resource hii sasa tunakwenda kuifanya ifanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niseme kimoja katika global scale bado Tanzania hatupo hata katika top twenty wenye resource kubwa ya gesi. Kwa hiyo, wawekezaji ambao tunao kwenye sekta hii ni vizuri tukakamilisha mazungumzo hayo. Tunafahamu siyo kitu cha kukimbilia au cha kufanya haraka lakini tuseme kama alivyosema Mbunge mmoja hapa kwamba kwa kweli hatuna muda mwingi wa kupoteza.

Mheshimiwa Spika, naomba niunge mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Eneo Huru la Biashara la Afrika
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hoja iliyo mbele yetu ya Kuridhia Mkataba wa Eneo Huru la Afrika. Napenda kuanza kwa kusema kwamba Mkataba huu tunaelewa kabisa umeridhiwa na baadhi ya nchi na nchi hizo ziko katika eneo letu la Afrika Mashariki. Hata hivyo kuchelewa kwa Tanzania kuridhia mkataba huu kumeleta hisia kwamba pengine wafanyabiashara wa Tanzania wanaogopa au wana uoga. Napenda kukudhihirishia, wafanyabiashara wa Tanzania hawana uoga wa kuingia kwenye ushindani, wafanyabiashara wa Tanzania wanaamini ushindani ndiyo utakaoboresha biashara zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa na nafasi ya kuwa Mjumbe wa Baraza la Biashara la Tanzania nikiwakilisha sekta binafsi katika nafasi yangu ya huko nyuma. Tatizo kubwa la wafanyabiashara wa Tanzania ni kuhakikishiwa kwamba kutakuwa na ushindani ambao upo level au uko sawa au una usawa, Waingereza wanaita level playing ground.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hilo naomba niwashauri Wabunge kwamba wafanyabiashara wetu wanaiona hii ni fursa, nao ndio watakaokwenda kwenye soko hili. Wafanyabiashara/sekta binafsi ndio watakaokwenda kwenye soko hili na tuna kila sababu ya kuwasaidia na kuwa-support. Nao wanachotaka siyo Serikali iwape fedha, Serikali iendelee kuboresha mazingira ya biashara. Tumeisema kwenye Kamati kwamba Serikali iendelee kuboresha mazingira ya biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami napenda kusema kwenye hili, Serikali ina forum ya kuongea na wafanyabiashara on almost quarterly basis. Tunaomba sana forum hii itumike vizuri ili kuweza kujua matatizo ya wafanyabiashara wa Tanzania kila wakati ambapo yanajitokeza, isiwe inangojewa mpaka malalamiko yanafika mbali au yanakuwa makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan hapa kwa juhudi zake kubwa sana za kuliweka hili jambo wazi na kuwaambia Watendaji ndani ya Serikali na kuonyesha mwelekeo wa nchi yetu kwenye masuala yote ya uwekezaji pamoja na kutoa kauli ambazo sasa zinatabirika katika Jumuiya ya Wafanyabiashara. Jambo hili ni zuri kwa nchi yetu, jambo hili ni zuri kwa wafanyabiashara wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ni la muhimu sana ili tuweze kufanikiwa kwenye suala hili ni kuhakikisha tunakwenda kwenye ushindani. Ushindani ni suala la bei na ubora. Sasa kwenye ubora, kwa kiasi kikubwa ni suala la mwekezaji mwenyewe au mfanyabiashara. Serikali kazi yake ni kuhakikisha kwamba standards zinakuwa met. Kuna suala la bei. Kwenye bei wafanyabiashara wetu lazima tuwasaidie. Nasi msaada wetu kama nchi au kama Serikali ni kuhakikisha kwamba tunawapunguzia gharama ambazo siyo za lazima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu wameliongea, kuna gharama nyingi ambazo siyo za lazima; nyingi tunasema ni kama tozo, lakini kuna gharama nyingine. Kwa mfano, ukichukua mkataba unaohusiana na masuala ya electronic stamp, tumeliongea sana hili hapa Bungeni. Gharama ya mkataba ule ni kubwa mno. Wenzetu watakaokuwa wanazalisha vitu hivyo na kuvileta katika soko letu, pengine hawana hiyo gharama au kama wanayo ni ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nasi tuliangalie. Kwa mfano, TBL wanatumia dola milioni tisa kwa mwaka kwa kuweka hizo stamp tu. Hiyo gharama ni kubwa sana, nayo inakwenda kwenye masuala mengine vilevile. Tuangalie pia utaratibu mzima wa wafanyabiashara kuhakikisha kwamba tunaweza kuwarudishia kile ambacho wanadai kama VAT. Ni jambo la muhimu sana. Wengi tunashindwa kuelewa kwamba mtaji wa mfanyabiashara siku zote unahesabiwa kwa shilingi. Anapokuwa anadai Serikali marejesho na yanachukua muda mrefu, inampunguzia mtaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo napenda niliseme, naomba sana Serikali ifanye uchambuzi vizuri. Najua ndani ya mkataba huu unatoa nafasi ya kuhakikisha kuna maeneo ambayo tunadhani kwamba bado hatujafikia uwezo wa ku-compete au pengine tuna-comparative advantage. Serikali iyachambue vizuri. Nitatoa mfano, kuna maeneo ya nguo tumeambiwa kwamba haya yatabakia kuwa yetu, lakini kuna maeneo mengine uchambuzi ufanyike na hasa maeneo yale ambayo SMEs zetu zitashiriki. Iko haja ya kuona namna gani tutawasaidia ili waweze kuingia kwenye soko hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hii hoja na naomba sana Wabunge wenzangu tuipitishe kwa nguvu zote. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. DEO P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Mpango na Mapendekezo ya Mpango ulio mbele yetu wa mwaka 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa nijikite kwenye maeneo mawili; eneo moja ni eneo la uwekezaji kwa maana ya Mradi wa Liganga na Mchuchuma na muda ukiruhusu niweze kuangalia Sekta ya Kilimo kama wenzangu ambavyo wameangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango huu unajaribu kujikita kutoa msingi wa maandalizi ya Mpango wa Maendeleo wa 2022/2023 na umeainisha maeneo muhimu ya vipaumbele. Katika maeneo haya kuna maeneo ya miradi ya kielelezo. Kwenye maeneo haya kuna eneo la Liganga na Mchuchuma; nipende kusema na mwenzangu Mbunge wa Ludewa ameliongelea, lakini mimi nitaliongelea kwenye angle tofauti kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashindwa kuelewa kinachoelezwa katika Mpango, kuhusiana na mradi huu ni kwamba, majadiliano yanaendelea na tunakubali, lakini tuishauri Serikali kwamba mradi huu ni mradi mkubwa, ni mradi ambao unaweza ukawa game changer. Leo nataka nitoe takwimu kidogo tu hapo baadaye za kwa nini Mpango unaokuja ni lazima uzingatie kuona matayarisho ya Mradi huu wa Liganga na Mchuchuma kwa maana ya makaa pamoja na chuma uweze kuanza kuonyeshwa na kuandaliwa wakati majadiliano yanaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, majadiliano hayo ambayo hayaishi hatuelewi ni majadiliano gani. Tunaelewa kwamba pengine kuna ugumu kwenye kujadiliana, lakini tufike mahali maamuzi yafanyike na option za uwekezaji katika sekta hizi za madini kama chuma ni muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wachumi wanasema kuna gharama au kuna hasara ya kutofanya jambo fulani kwa wakati fulani, wao kitaalamu wanaita opportunity cost. Sasa tukiangalia sasa hivi bei ya chuma ndani ya miezi 24 imefika dola za Kimarekani kwa tani 400 ni ongezeko kubwa la asilimia 200. Wachina peke yao ndiyo wanao-dominate soko hili la chuma kwa sasa. Wanazalisha karibu asilimia 56.5 ya chuma chote duniani. Afrika peke yetu tunazalisha kama asilimia 17, Tanzania ni sifuri, lakini tuna chuma hapa na tuna resource hapa kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kusema kuna research imefanyika na Institute ya Global for Development Studies ya Boston University ambayo inaonesha katika kipindi cha 2008 mpaka 2019 Wachina peke yao wametoa mikopo ya financing ya maendeleo duniani ya karibu dola za Kimarekani bilioni 462. Ndani ya hizo dola bilioni 462 asilimia 80 imeenda kwenye miradi ya infrastructure, maana yake unaongelea bandari, reli, madaraja na kadhalika. Afrika peke yetu tumepata dola bilioni 106 katika hizo dola bilioni 462.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninachotaka kusema ni nini? Hizo dola bilioni 106 ni karibu trilioni 230 za Kitanzania. Hoja hapa ambayo Mpango lazima uangalie ni kwamba tuna kila sababu ya ku-take advantage ya uchumi wa makaa ya mawe na chuma sasa hivi ili tuweze ku-benefit huko tunakokwenda. Kama Tanzania peke yetu tungeweza kupata, maana yake katika hii 80 percent infrastructure na Afrika ni dola bilioni 106, sisi tuna chuma, kama tungekuwa tumeanza uzalishaji hata tukapata asilimia 50 tu ya hiyo biashara ya ujenzi wa infrastructure katika maeneo ambayo yanahitaji chuma sana madaraja, SGR, barabara, ports, zote zinataka chuma, tungepata asilimia 20 tu ya hiyo biashara ya kuzalisha hiyo chuma, bajeti yetu nzima yote trilioni 39 ingeweza kutoka katika biashara ya chuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ipo haja tuone kwamba tuna haja na tuna kila sababu ya kuhakikisha haya majadiliano yanafika mwisho ili tufanye huu uwekezaji katika hili eneo la chuma pamoja na makaa ya mawe. Tuliangalie vile vile pengine nje ya box, kama tunaona maana yake hapa hatuhitaji pesa ya Serikali, pesa ya uwekezaji kwenye maeneo haya ipo duniani na wawekezaji wapo duniani. Kama tuna mwekezaji ambaye hatuwezi kwenda naye anatuchelewesha, tujue kwamba hiyo opportunity cost inakula kwetu.

Mheshmiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ningependa niombe sana sana Mpango huu, ukiangalia kwa mfano katika Mpango, matumizi ya mwaka jana katika robo ya kwanza hata wachukue robo mbili, matumizi ya Serikali kwenye maandalizi ya mradi huu huwezi kuamini wametumia shilingi za Kitanzania milioni 3.7, nadhani ni kuwalipa walinzi wanaolinda yale maeneo. Kwa hiyo ni kwamba hakuna uwekezaji wa aina yoyote kwenye eneo hilo na kwamba ni kama hatuoni umuhimu kwenye hii mradi huu wa kielelezo, ambao ni muhimu. Nchi yoyote ambayo ina chuma leo na ikaanza kuchimba itakuwa na bajeti nzuri, itakuwa na chanzo kikubwa sana cha mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuliongolea hilo, kwa hiyo nisema maandalizi ni pamoja na kuhakikisha kwamba hizo fidia zinalipwa kutengeneza hilo eneo ili mambo yakikamilika haya ya majadiliano, uwekezaji uanze, siyo tena tuanze kuhangaika kwamba kwenye bajeti hakuna compensation, hakuna hela za kulipa. Kwa hiyo Mpango ujaribu kuliangalia hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna masuala pia ya miundombinu, project hii ita entail vilevile kuendeleza SGR kutoka Mtwara mpaka Mbamba Bay mpaka kwenye Mchuchuma. Kwa kweli kwenye Mpango inaonyesha kwamba bado wanaendelea kufanya tathmini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba haya mambo yaharakishwe kwa sababu si lazima Serikali itumie pesa kujenga SGR, tufanye hii kitu tofauti na tulivyofanya kwenye central line, kuna watu wanaweza wakajenga kwa pesa zao tu-negotiate nao ili tuweze kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee haraka haraka kilimo, wengi wameongelea, suala zima la tija katika kilimo tuliliongelea hapa na tumeliongelea muda mwingi kwamba tunahitaji kupata mbolea kwa wakati na mbolea ambayo ni affordable. Hali si nzuri wote tunaelewa, tunajua kwamba Serikali itakuja na maelezo hapa kabla Bunge halijaisha kutuambia kuhusu suala la mbolea. Hata hivyo, nipende kusema, tunashukuru Serikali imefanya jitihada za kuona namna gani itashusha bei ya mbolea au itawapa nafuu wakulima. Ukweli wa mambo ni kwamba bado hakuna nafuu, tuiombe Serikali na Kamati imejaribu kuongea na imesema ni vizuri Serikali ikaangalia uwezekano wa kutoa ruzuku katika suala hili la mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuongelea zao la parachichi, kwa sababu nalo ni chanzo kingine kizuri sana cha mapato. Zao la parachichi ukiangalia kidunia Watanzania tumezalisha kama asilimia 0.2 ya mazao yote ya parachichi duniani. Ukweli ni kwamba, Tanzania ndiyo nchi pekee yenye potential kubwa sana ya kuendelea kukamata soko la parachichi katika dunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaweza tu kufanya hiyo iwapo tutahakikisha kwamba sasa hivi Serikali ina-invest katika kilimo kwa maana ya kuhakikisha kwamba wakulima wote kwenye masuala ya mbegu, ubora wa mbegu, yanaangaliwa kwa umakini sana, kwa nini? Kwa sababu unalima parachichi leo, unaanza kuzalisha baada ya miaka mitatu, lakini full production inaanza baada ya miaka saba. Kama mbegu tunazotumia hazina uhakika, hazina ubora tutafika kule mwisho hatuta-realize hayo tunayotaka kuyafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana tulikuwa na promise ya Serikali ya kuweka mamlaka ya kusaidia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele ya pili.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naomba niunge mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuanzia Januari, 2021 hadi Februari, 2022 pamoja na Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa Kipindi cha Januari 2021 hadi Januari 2022
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie suala la Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili ni la muda mrefu na kama ripoti ya Kamati ilivyooneshwa hatujaridhishwa kabisa Wanakamati na taarifa tunazozipata kuhusu mwelekeo na muendelezo wa mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu tunachoambiwa ni kwamba uko kwenye majadiliano. Majadiliano haya ambayo hayaishi tunashindwa kuelewa ni majadiliano gani. Tuna uhakika kabisa wataalam wetu wana uwezo wa kufanya majadiliano na tumewaamini na tuna hakika pengine wanapigania maslahi makubwa ya nchi yetu ili tupate mkataba mzuri, lakini miaka 11 toka mkataba umesainiwa mpaka leo hatujaweza kukamilisha jambo hili? Hivi hatujui na hatuoni umuhimu wa chuma katika maendeleo ya nchi?

Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kusema wote tunafahamu majadiliano siku zote sio lazima ushinde kila kitu, lakini majadiliano yanataka compromise, ufike mahali ukubaliane na hasa kama unajua lengo lako ni nini. Sasa sisi tunaelewa chuma tunahitaji, tunaelewa mradi huu ni mkubwa, mradi huu utabadili maisha ya watu, mradi huu tunaouita mradi wa kielelezo, mradi huu tunauita upo katika mpango wa kwanza ulioishia 2021, upo kwenye mpango wa pili unaoishia 2026, upo kwenye kila bajeti ya kila mwaka, upo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM. Ndugu zangu, hivi tunataka nini? Tunafahamu kabisa kwamba tunapoteza kwa kutoendelea na uwekezaji kwenye mradi huu mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi napenda kupendeza; nafahamu Waheshimiwa Wabunge kwamba Kamati yetu inajaribu ku-negotiate ili tupate better terms, lakini nitoe ushauri hebu wajaribu kuangalia maslahi mapana ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, unajua approach ikiwa ni kuangalia negotiations kama kama kihasibu, unaangalia tu faida kwamba, tutapata faida, hatupati mpaka mwisho unapiga hesabu unasema hapa hatupati faida, nadhani hiyo approach sio nzuri. Waende na approach ya kiuchumi ya kuangalia multiplier effect kwenye mradi huu; mradi huu ajira 5,000 za moja kwa moja, mradi huu ajira 33,000 ambazo hazitakuwa moja kwa moja. Ndani ya mradi huu…

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mchango mzuri sana wa Mheshimiwa Mbunge, Mradi huu wa Liganga na Mchuchuma, sio tu kwamba utasaidia kuzalisha chuma ambacho tungeweza kutumia katika maendeleo mengine, lakini ni mradi ambao ni unganishi kwa kuendeleza pia Makaa ya Mchuchuma na chuma cha Liganga,

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa maana hiyo, kulikuwa na mpango sahihi kabisa wa kuzalisha megawati 600 ambazo nyingine zingetumika kuchenjua chuma na megawati nyingine 400 zingeingizwa katika njia ya msongo wa kilovoti 400 pale Makambako ili uweze kuingia kwenye Gridi ya Taifa kwa hiyo, ni mradi muhimu kwa ustawi na maendeleo ya nchi.

NAIBU SPIKA: Ahsante, Mheshimiwa Mwanyika, Taarifa hiyo.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana kaka yangu kwa kuendelea kunifilisi nilichotaka kuongea, lakini niseme mradi huu ni special. Mradi huu ukiuangalia kwa haraka upande mmoja ni mradi wa kiuchumi, lakini ni mradi wa kiundombinu; tunaongelea ujenzi mkubwa wa reli katika mradi huu ambao utaiunganisha Bandari ya Mtwara, inakuja mpaka Manda inapata mchepuko inakuja kwenye huu mradi. Kwa hiyo, ajira ngapi zitazalishwa katika hiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tuangalie kitu kingine, tunatumia fedha nyingi sana nnchi hii katika masuala ya chuma; ujenzi wa maghorofa, ujenzi wa madaraja, ujenzi wa SGR, ujenzi wa towers. Mheshimiwa Naibu Waziri hapa ameongea kwamba hatuna towers, nchi hii ina towers za simu zaidi ya 10,000; hivi hiyo miradi yote hiyo ya towers ni chuma na sisi chuma tunacho hapa na tunalialia kwamba, hakuna towers za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ukiangalia ni mengi, miradi hii itapunguza gharama nyingi sana ya vitu vingi. Kwa mfano, tunaongelea uzalishaji wa gesi, nani anafahamu?

Mheshimiwa Naibu Spika, kifungashio cha gesi unachokiona, unakiita cylinder, asilimia karibu 50 ya ile gesi, gharama…

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kumpa Taarifa kaka yangu Mheshimiwa Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini kuhusu suala la Liganga- Mchuchuma sio tu itasaidia hayo anayoyasema, lakini pia itasaidia kuanzisha viwanda vya magari katika nchi yetu. Kwa hiyo, itaongeza na kukuza uchumi kwa zaidi ya asilimia 100. Ahsante. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Haya, ahsante. Taarifa hiyo.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakubali taarifa na mambo ni mengi ni mengi sana ambayo chuma kingetusaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kumalizia kwa kusema wenzetu Serikalini watusaidie. Mheshimiwa Engineer Chiwelesa amesema huyu mwekezaji kama hawezi basi aondolewe, lakini tunachoambiwa ni kwamba kuna tatizo la tax incentives au vivutio.

Sasa mimi nimeangalia vivutio vinavyoongelewa, ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, hivi vivutio vinavyoongelewa kwa mradi mkubwa wa aina hii tuangalie maslahi makubwa kwamba tukijenga hii infrastructure ambayo ni Liganga – Mchuchuma, power na steel, tukajenga na hizi reli, uchumi mkubwa wa eneo zima la Kusini utasisimka na tunaweza tukapata hii kodi ambayo tunaweza tukaisamehe hapa mwanzoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hata ukiziangalia hizi kodi zinazoongelewa hapa tuliuliza swali hivi tunazipata leo? Kwa hii chuma kuwa bado hazijachimbwa? Tunazipata hizo kodi? Hatuzipati.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Kwa hiyo, tuliangalie kwa karibu nashukuru muda ni mfupi lakini naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika hoja iliyo mbele yetu ya ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza sana Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa mambo makubwa ambayo wote tumeyashuhudia katika hiki kipindi cha mwaka mmoja na miezi kadhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Njombe tumeshuhudia madarasa mapya mazuri, karibu madarasa 38 lakini tumeona maeneo ya afya, vituo vya afya vikiendelea kujengwa kwa kasi kubwa, lakini kubwa kuliko yote katika azma ya kazi iendelee tumeshuhudia hospitali yetu kubwa ya rufaa ikipata fedha zote ili iweze kukamilika na huduma iweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee kabisa nimshukuru sana Mheshimiwa Rais pamoja na Serikali ya Awamu ya Sita kwa kutekeleza na kuchukua hatua kubwa sana ambayo ilikuwa ni kilio kikubwa cha wananchi wa Njombe kutupatia barabara ya Itoni mpaka mpakani mwa Njombe na Ludewa. Tunaambiwa sasa barabara hiyo inakwenda kuanza kujengwa kwa sababu mchakato mzima wa manunuzi umekamilika na mkataba umesainiwa. Kwa hiyo, nishukuru sana kwa jambo hilo kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuongelea kuhusu uwekezaji. Nashukuru sana Serikali kuendelea kufungua milango na kuboresha mazingira ya uwekezaji, tumeshuhudia kwamba miradi zaidi ya 300 yenye gharama ya karibu Dola Bilioni 8.4 tunazungumzia Shilingi Trilioni 18, hili ni jambo kubwa sana kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kushauri kwamba bado tunaomba sana Serikali iendelee kupitia sheria na sera za uwekezaji ili ziweze kuendana na hali halisi. Tunadhani kwamba baadhi ya maeneo na mitazamo ya kisera inawezekana imepitwa na wakati hasa unapoangalia miradi mikubwa ya kimkakati kama Liganga na Mchuchuma. Tuondoke kule kwenye kuangalia zaidi kodi peke yake tuende kwenye kuangalia faida kubwa, tuangalie multiplier effect. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitaliongelea Liganga na Mchuchuma kwa sababu nina uhakika tutapata nafasi hapo mbele na kwa vile Waziri mhusika ameshatuambia kwenye Kamati kwamba ataongea nasi kutupa update ya suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuendelea kuchangia kwenye eneo la kilimo, tumekuwa na changamoto kubwa sana ya mbolea na imeongelewa hapa, nipenda kushukuru sana Serikali kwa suala hili kwamba sasa kilio kikubwa cha Watanzania kimepata kusikika na Serikali imeamua sasa kwamba tutakuwa na mfuko wa pembejeo. Katika bajeti hii wananchi watapunguziwa maumivu, katika hali ya bei kupanda haya ni maamuzi makubwa sana na tumshukuru na kumpongeza sana Rais wetu kama alivyosema Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, utashi wa kisiasa katika jambo hili ulihitajika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Njombe ni moja ya maeneo yanayokuwa kwa haraka na takwimu zinaonyesha wazi ni Mkoa ambao una mchango mkubwa sana kiuchumi na hasa katika maeneo ya vijijini. Kwenye kilimo asilimia 90 ya wananchi wa Njombe ni wakulima na mchango mkubwa wa pato la Taifa unatoka katika kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kufanikiwa zaidi katika Mkoa wa Njombe tunahitaji miundombinu wezeshi kwa kiasi kikubwa. Serikali yetu imekuwa na miradi mikubwa miwili ambayo inafadhaliwa na wafadhali ya kusaidia maeneo ya kilimo kutengeneza miundombinu wezeshi. Kwa bahati mbaya sana Njombe haikuwemo katika maeneo hayo au katika miradi hiyo, kwa sababu ambazo zimeelezewa kwamba ni Njombe Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Njombe Mjini ni Jimbo lakini asilimia 70 ya Njombe Mjini ni vijiji ambapo ndipo uzalishaji mkubwa unapotoka. Napenda kuiomba sana Serikali pamoja na kwamba hatupo kwenye miradi hii mikubwa ya fursa za kiuchumi ya kufungua miundombinu wezeshi, tupate fedha za kutosha na ninawashukuru kwamba katika bajeti iliyopita tulichangiwa fedha za kutosha kiasi cha Shilingi 1.5 Bilioni kwa ajili ya maeneo ya vijijini. Ninaomba na mwaka huu tuweze kuangaliwa ili miradi ya kufungua maeneo ya vijijini na uzalishaji yanayokuza ajira kwa kiasi kikubwa, yaweze kupata fedha na barabara zetu ziweze kukabaratiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa elimu, tunashukuru Serikali kama nilivyosema tumeona makubwa lakini napenda kusema kwamba bado tuna changamoto kubwa ya watumishi, tuna tatizo la watumishi kiasi cha Walimu kwa upande wa Shule za Msingi karibu 350 hiyo ni gape ambayo tunayo. Tunashukuru Serikali na maamuzi ya Serikali kuwaajiri Walimu 32,000 tuna matumaini makubwa sana nasi katika kipindi hiki tutaangaliwa kwa jicho la karibu kwa vile tuna uhitaji mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hilo lipo pia kwenye afya, tuna upungufu mkubwa wa watumishi katika afya. Lakini kwenye afya napenda kusema watu wa Njombe Mjini ni watu wa kujituma ni watu wa kufanya maendeleo, katika kilimo na katika kujitolea. Katika Mji wa Njombe tayari tulishajenga Vituo vya Afya kabla hata Serikali haijatoa mkakati wa kuwa na kituo cha mkakati cha afya katika kila Kata. Tuna vituo ambavyo vinakuja vimeshakamilika na vinangoja vifaa tiba na watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuiomba Serikali kuangalia kwa karibu ili maeneo haya vituo hivi ambavyo vimeshakamilika kwa asilimia 90 na vinangoja tu vipate vifaa tiba viweze kuangaliwa ili huduma ziweze kumfikia mwananchi kwa karibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa umeme tunashukuru tunaendelea na mradi REA, lakini napenda kusema ni vizuri Serikali ikajitahidi tuweze kupata fedha za kutosha mradi huu ni mzuri na tunaelewa kwamba ndani ya miaka hii mitano vijiji vyote vitapata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwe realistic kwa speed ambayo REA wanakwenda nayo tunaanza kupata wasiwasi kwamba tutafanikiwa kukamilisha kupata hii miradi yote ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuongelea jambo moja kubwa ambalo wananchi wa Njombe tuna wasiwasi nalo, aliongea Mheshimiwa Chumi hapa kuhusiana na nguzo za umeme, uchumi wa Njombe ardhi nzima ya Mji wa Njombe au Mkoa wa Njombe asilimia 30 ni miti ambayo ndani ya miti hiyo tunatoa nguzo na ndiyo tumesaidia nchi hii kuweza kuendelea na miradi mikubwa ya REA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa habari tuliyoisikia kwamba wenzetu wa TANESCO wanataka kuanza kuagiza nguzo kutoka nje ya nchi, jambo hili pamoja na kwamba la kibiashara lakini halina afya, litakwenda kuongeza umaskini kwa wananchi wengi ambao tayari wameanza kujikomboa na wanajitolea na kufanya kazi kwa bidii kujenga maisha yao, itapunguza mapato ya Halmashauri zetu kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Halmashauri ya Njombe kwa mwaka tunapata kutoka katika msitu karibu Shilingi Bilioni Mbili ambazo zinakwenda kusaidia maendeleo ya wananchi. Vile vile tuna viwanda Sita ambavyo vinashughulikia nguzo na katika muda mfupi huu viwanda vimeongezeka katika nchi ya Tanzania, kwa sababu sera zimefunguka na wawekezaji wanazidi kuja na kuna wawekezaji wa ndani hapa hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni ya TANWOOD peke yake katika miaka miwili iliyopita imelipa zaidi ya Shilingi Bilioni Nne kama corporate tax, lakini inaajiri wafanyakazi wengi karibu 200 na inalipa mishahara ambayo ni mizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kujiajiri kuna Watanzania wananchi wa Njombe wengi wanajiajiri katika sekta ya misitu. Napenda sana kuiomba Serikali ifanye maamuzi ikizingatia kwamba katika Ilani yetu ya Uchaguzi tunataka kuwawezesha watanzania waweze kujitegemea wao wenyewe na sekta ya misitu inatoa hiyo fursa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona muda wangu umeisha, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye taarifa ya mwaka ya Kamati ya Katiba na Sheria kwa kipindi cha Februari 2022 hadi Januari 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongelea masuala kama matatu, muda ukiruhusu masuala manne. La kwanza masuala ya lugha katika mahakama zetu. Kama wanakamati walivyosema, mimi sipo kwenye Kamati hii lakini kama Wanakamati walivyosema, mimi niko katika Kamati ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipata nafasi ya kuongea na wawekezaji walio wengi; wakati tunapitisha sheria mpya ya uwekezaji, moja ya jambo lililojitokeza kama concern kubwa ya wawekezaji ilikuwa ni kwamba; kuwa na sheria kwa Kiswahili ni jambo jema lakini ni vizuri sana sheria zile badala ya kungoja translation, zikatafsiriwa halafu wawekezaji wakapewa au zikatumika kuwavuta wawekezaji kwa kuzisoma huko waliko, ilionekana ni vyema na itakuwa na tija kama sheria zetu zitakuwa kwa Kiswahili na Kingereza. Hilo linaendana na dhima nzima ya kutaka kuona kwamba tunapata wawekezaji na kwa kweli tuko katika ushindani wa wawekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipata mifano mingi iliyoonesha kwamba kuna nchi nyingi ambazo zimekwenda kwenye lugha zao kutunga sheria lakini vile vile zimetumia lugha ya Kingereza kama moja ya lugha ambazo zitatumika pamoja na lugha ya nchi ile. Nchi kama Rwanda na India zina utaratibu huo. Kwa hiyo mimi niungane na kuiomba sana Serikali kwamba kwa maslahi mapana ya kuangalia kwamba tunakwenda kuwa-include watu wote na vile vile tunajaribu kupunguza migogoro. Tukumbuke kwamba tafsiri ya sheria kwa lugha moja kama itatumika na watu wengi kuna uwezekano mkubwa, pamoja na kwamba sisi tunaifahamu lugha hiyo ikaleta mgogoro kwenye tafsiri. Ukishakuwa na mgogoro ni gharama. Kwa hiyo ni vizuri basi wazo hilo likatiliwa maanani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; kuna suala la taasisi ambayo iko katika utekelezaji na inasimamiwa na Wizara hii, Taasisi ya Baraza la Biashara. Taasisi hii ya Baraza la Biashara imeundwa kwa mujibu wa Waraka Namba Moja wa Mheshimiwa Rais wa mwaka 2001. Moja ya changamoto ambazo Kamati imeziona katika baraza hili ni suala zima la maamuzi kutotekelezwa. Baraza hili halikutani kila siku, halikutani kila mwezi linakutana kwa mwaka mara mbili; na ni baraza ambalo limeundwa kwa ajili ya kuwa ni forum ya dialogue kati ya wawekezaji wa ndani na wa nje na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa maamuzi yanapokuwa yamefikiwa yanataka utekelezaji. Haitakuwa inatutendea haki kama nchi iwapo tutakuwa na baraza kama hili. Litafanya maamuzi yanayotaka utekelezaji, maamuzi hayo yasitekelezwe. Niombe sana Serikali, kwamba ihakikishe kwa kweli baraza hili likishafanya maamuzi, maamuzi yale yanatendewa haki. Tulichobaini kingine katika utafiti wangu wa haraka ni kwamba wanapokwenda kwenye kikao kingine wanaanza kuongelea regulations mpya ambazo zimetungwa ambazo hazi- encourage uwekezaji; kwa hiyo imekuwa kama vicious cycle. Kwa hiyo ningeomba sana baraza hili lifanye kazi kama vile ilivyokusudiwa na Waraka wa Rais, kwa maana ya kuwa ni dialogue, forum ya maongezi na forum ya kutatua matatizo na changamoto za wawekezaji wa ndani na wa nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nilipenda niongelee ni suala zima la Ofisi ya Mashtaka. Kamati imetuambia hapa kwamba ofisi hii imefanya kazi kwa mafanikio. Kuna ukweli pengine kama imefanya kazi kwa mafanikio, lakini vile vile wameonesha kwama bado kuna matatizo hasa ya ucheleweshaji wa utekelezaji wa hukumu. Suala hili ni suala ambalo lina impact kwenye kutenda haki na kwenye kuvutia uwekezaji wa ndani na nje. Hii ni kwa sababu sisi tunaangaliwa na mataifa mengi pamoja na tunaangaliwa na wawekezaji kwamba ni nchi ambayo inathamini sheria zake. Sasa hukumu inapotoka na inapokuwa DPP ameshindwa kesi ni suala la governance kwamba hukumu hiyo itatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niende mbali zaidi, hatuwezi kufumbia macho, kwamba ofisi hii ya DPP imekuwa na sintofahamu nyingi kubwa katika utekelezaji wa majukumu yake. Jambo hili limeongelewa na Mheshimiwa Rais mwenyewe, na amekwenda mbali zaidi akataka akaunda Tume ya Jinai ili iweze kwenda kuangalia haki jinai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ofisi hii ni ofisi muhimu sana katika utawala bora. Nipende kumuongelea Jaji Samatta ambaye wengi tunamfahamu, ni jaji ambaye alifanya kazi kama DPP miaka ya 1970 lakini akawa Jaji Mkuu ambaye alistaafu mwaka 2007. Yeye alisema maneno yafuatayo; “DPP na maofisa walio chini yake ni watumishi wa nchi ambao wajibu wao ni kulinda maslahi ya umma, yakiwemo yale yanayohitaji mtu asiyeonyeshwa na ushahidi kuhusika na utendaji wa kosa la jinai hashitakiwi na mshtakiwa ambaye ushahidi dhidi yake hauthibitishi kwamba alitenda kosa hatiwi
hatiani.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, maneno haya ni ya msingi sana na ofisi kama ingezingatia maneno haya nadhani tusingekuwa na sintofahamu ambazo Mheshimiwa Rais ameziongelea kwa kina. Nipende kusema, wahasibu wao tunasema wanajumlisha na kutoa lakini wanasheria wana mambo matatu. Unaangalia facts, unaangalia evidence, una-apply law. Inasikitisha kuona kwamba inawezekanaje tukawa na ofisi ya DPP ambayo inakwenda kwenye kesi, inashindwa kwa sababu kesi ambayo hawatakiwi washindwe, hawatakiwi hata waipeleke mahakamani kwa sababu hizo ni basic principles za sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nipende kusema kwamba suala la kutokutekeleza hukumu ingekuwa ni vizuri hii Tume ya Haki Jinai itakapofanya tathmini yake ichunguze kwa kina kuona maofisa ndani ya ofisi ya DPP ambao kwa makusudi wanafanya mambo ambayo yanaitia nchi hasara na inasababisha wao washindwe kesi halafu inapofika kwenye kulipa, wao wenyewe tena hawataki kutekeleza hukumu kwa kutolipa. Jambo hili lina madhara kwenye uwekezaji wa nchi, lina madhara kwa kuonyesha kwamba sisi hatuwezi kutekeleza mikataba; na hukumu ni kama mkataba ambao mahakama imeutoa ili utekelezwe kwa mujibu wa Katiba ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja iliyo mbele yetu. Kama wenzangu walivyosema nianze kwanza kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Amiri Jeshi Mkuu, Samia Suluhu Hassan, kwa mambo yote ambayo Wananjombe na hasa katika Jimbo langu tumeyaona yakija katika maeneo yetu. Tumekuwa na miradi mikubwa ya maji, kero ya maji ilikuwa ni kero kubwa sana katika Halmashauri ya Njombe lakini sasa tunayo miradi mikubwa miwili inayoendelea Mkandarasi anakwenda vizuri. Afya kwa mara ya kwanza wananchi wa Njombe sasa wamepata CT scan na wanaweza wakaacha kufunga safari kwenda Mikoa ya jirani kwa ajili ya kupata huduma hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa barabara kwa kweli tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais tunayo barabara ya Itoni kwenda mpaka mpakani na Ludewa ambayo ilikuwa ni changamoto kubwa sana. Barabara hiyo sasa Mkandarasi yupo site, bilioni 95 zimekuwa allocated na ina kilometa 55. Baada ya kusema hayo niende kwenye kuchangia lakini nimshukuru sana sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na kwa hotuba yake aliyoitoa hapa Bungeni na Wasaidizi wake wote waliohusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuchangia mambo kama matatu ama manne kama muda utaniruhusu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza kabisa ni kilimo na mifugo. Kwenye kilimo, Jimbo la Njombe lina mazao mbalimbali lakini zao la kimkakati linalotambuliwa Kitaifa ni zao la chai, nami napenda kuliongelea zao hili kwa kuanza kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu lakini kumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Bashe. Kilio kikubwa kilikuwa ni bei na wananchi walikuwa wanalalamika sana kuhusiana na bei ya chai na nililiongea hapa, baada ya vikao vya wadau, Serikali ikiongozwa na Mheshimiwa Bashe, wameweza kufikia mahali ambapo hata kama siyo pale ambapo wananchi walipataka angalau sasa hivi bei ya kilo ya chai ilikuwa inauzwa shilingi 314 kwa kilo, imefika 366 kwa kilo. Walipenda sana ingefika 400 lakini uhalisia ndiyo huo, kwa hiyo tushukuru kwa hicho kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema wananchi hawa, wakulima hawa wanaweza wakapata hata hiyo shilingi 400 kwa sababu ukiweza kulima kwa ubora kuna malipo yanaitwa bonus payment, ukiweza kulima ukapata ubora ambao ni asilimia 68 unapata bonus payment ya Shilingi 90 kwa kila kilo. Ukilima ukapata ubora wa asilimia 75 unapata bonus ya karibu shilingi 112 kwa kila kilo, kwa hiyo uwezekano wa kufika 400 inawezekana, sasa ni nini ambacho kinaweza kikafanyika na Serikali na nitoe ushauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo kubwa hapa ni umwagiliaji, Serikali iliongeza bajeti ya kilimo hapa na sehemu kubwa ya bajeti hiyo ilikwenda kwenye maeneo ya umwagiliaji, lakini kwa masikitiko makubwa sana wakulima wa chai kwenye miradi ya umwagiliaji bado hawajaingizwa, hakuna kinachoendelea kwa wakulima wa chai kwenye upande wa umwagiliaji. Ninaomba Serikali iweze kuhakikisha kwamba hata wakulima wa chai wanaingizwa kwenye miradi. Miradi hii imeendelea kuwa kwenye scheme nyingine tu lakini kwa wakulima wa chai hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunacho Kiwanda cha Chai pale kina–process chai kinaitwa Kabambe. Kiwanda kile kina capacity Kubwa lakini kinatishiwa kufungwa kwa sababu uwezo wa kuki-feed kiwanda ni mdogo. Wakulima wa chai wamejitahidi walipoweza kufika lakini bado hawawezi kufikisha na jambo linalozuia ukiacha suala la umwagiliaji ni suala la miundombinu wezeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana Serikali ilikubali kutoa fedha kutusaidia kwa upande wa barabara, lakini kwa masikitiko makubwa nipende kusema tuna tatizo kubwa sana la ujenzi wa barabara ambazo ziko chini ya TARURA. TARURA inatakiwa ijipange vizuri kuweza kusimamia Wakandarasi wajenge hizi barabara haswa za maeneo wezeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jinginje ninapenda kiliongelea kwenye mifugo ni kiwanda cha maziwa ambacho kipo katika Mji wa Njombe. Ninaongea kwa masikitiko makubwa sana kwenye kiwanda hiki, ni kiwanda pekee ukiacha viwanda vya avocado au parachichi kiwanda pekee ambacho kinakusanya maziwa, kiwanda hiki kilipata mkopo wa Benki ya Kilimo - TADB lakini kiwanda hiki kimefungwa kimesimama, niliomba hapa msaada wa Serikali uweze kuingilia mpaka leo haijaweza! Ninasikitishwa sana na ethical behavior na integrity ya TADB kwenye kushughulikia suala la kiwanda hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli ni kwamba wananchi wafugaji wana-own asilimia 30 ya kiwanda hiki, ungetegemea TADB wao wana jukumu la ku-promote na kusaidia wafugaji na wakulima, kwa hiyo wangeingia katika scheme ya kuasaidia hata kama wamekopa na kwamba fedha hazijarudishwa. Wananchi hawa kwanza TADB wao wenyewe wako responsible kwa default kwa kiasi kikubwa kwa sababu hawakutoa fedha kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TADB walichofanya kwa masikitiko makubwa, wamechukua madalali kwenda kuuza kile kiwanda na siku zote wanapeleka madalali karibu na sikukuu wakati watu hawapo, wameuza eneo la shamba lakini wameuza warehouse kwa milioni 500, kwenye kiwanda ambacho thamani yake ni bilioni 2.6 hii hakiubaliki na tunaomba Serikali iingilie kunusuru maisha ya wakulima hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana tu nimesikia tena hapa baada ya kuuza jingo, TADB wamekwenda tena na dalali mwingine wanataka kuuza mashine! Nadhani TADB ilianzishwa kwa minajiri ya kuwasaidia wafugaji, wakulima ili waweze kujikomboa. Wakulima na wafugaji 1,000 wa sekta hii ya maziwa watakwisha maisha yao kabisa iwapo Serikali haitasaidia, siyo kwamba hawawezi kulipa hilo deni, mkakati wa kilipa hilo deni upo lakini TADB wana-interest na ndiyo maana nimesema ethical behavior ya TADB lazima iangaliwe, nina uhakika CAG ni eneo ambalo anatakiwa akaliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine napenda niliongelee ni eneo la usafiri wa anga. Mji wa Njombe kwa kweli tuna uhitaji mkubwa sana wa kuwa na kiwanja cha ndege. Napenda kuiomba sana Serikali iweze katika bajeti inayokuja iweze kuona hata kama hatutaweza kupata ujenzi wa kiwanja cha ndege upgrade ambayo inafanyika sehemu nyingine lakini kwa kuanzia angalau fedha ziwe allocated tuweze kuona eneo hili kubwa la uchumi linapata huduma ya usafiri wa anga wa uhakika. Tuna Wawekezaji wengi kwenye maeneo mengi, wangependa kuja katika kuwekeza katika Mkoa huu wa Njombe na Mji wa Njombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipitisha sheria hapa ya Uwekezaji. Mimi napenda kuiongelea Sheria ya Uwekezaji wa harakaharaka. Wakati tunaongea hapa tuliiomba sana Serikali na ninashukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu ameongelea kwamba Serikali itaendelea kuangalia kuboresha mazingira ya biashara, pia itaendelea kuangalia sera zake kwa nia ya kuboresha. Moja ya maeneo ambayo tuliomba na ninaomba liendelee kuangaliwa kwa haraka ni kuangalia uwezekano wa kuona ni namna gani viwanda katika nchi yetu vinaweza vikapelekwa kwenye maeneo mengine kwa kuweka incentive scheme, tunaliomba hilo na tunaomba Serikali iendelee kuliangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili watu wengi hatuliangalii kwa umakini, ni lazima tufanye mambo kwa mkakati tunaagiza ndege ya mizigo, hiyo ndege ya mizigo haitakuwa economical kama itakuwa inakwenda kuchukua mizigo tu ambayo ni ya kilimo na kupeleka sokoni. Inatakiwa iwe na mizigo mingine inayopeleka maeneo hayo na mizigo hiyo ukianzisha viiwanda na shughuli nyingine za kiuchumi ndipo unaweza kuifanya hii ndege iweze ku-add value katika maeneo yetu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa sekunde 30 malizia mchango wako.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishie hapo na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja iliyo mbele yetu. Nitajikita zaidi kwenye mambo yanayohusu jimboni kwangu kwa sababu kuna mambo ambayo hayajakaa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri na Naibu Waziri wake kwa kutuandikia speech nzuri sana. Pamoja na hayo, Wananjombe bado tuna masikitiko kwa sababu sekta hii ya mifugo, kama wengi wanavyosema, tunaiona ina potential kubwa, lakini bado ina matatizo makubwa sana na yanaji- reflect katika namna bajeti ilivyogawanywa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wazi kabisa kwamba, ukiangalia importation ya maziwa kama moja ya main product ya sekta hii, ni kubwa mno kuliko export. Tuna-export karibu lita 280,000, hazifiki hata milioni moja, lakini tuna-import lita milioni 11.6 kwa gharama ya Shilingi bilioni 22. Ni wazi kwamba hapa kuna tatizo, aidha tija ni ndogo au hakuna uwekezaji. Kwa kesi yetu hapa, ni wazi kwamba vyote viwili vina-apply; kwamba hakuna tija kwenye uzalishaji, na hakuna uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, msemaji aliyepita amejaribu kuliongea vizuri sana, nami nisingependa kurudia yale aliyoyasema, lakini niseme wazi, iko haja ya Serikali kuongeza uwekezaji katika sekta hii na katika Wizara hii ya Mifugo. Twende mbali zaidi, tuangalie kwamba mwekezaji mkubwa ni Serikali kwa kutengeneza mazingira, lakini tuangalie kwamba mwekezaji anayeweza akawa game changer ni private sector kwenye sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimefarijika kuona Waziri anaongelea kwamba wanakwenda kupitia taratibu, kanuni na sheria za sekta hii. Nina matumaini kwamba zinapitiwa kwa nia ya kuondoa maeneo ambayo yana-frustrate hii sekta. Wizara inatakiwa i-facilitate, siyo i-frustrate hii sekta. Kwa hiyo, ni matumaini yangu kwamba hilo litafanyika na likifanyika nina uhakika sekta inaweza ikatoa mchango mkubwa na tukaacha kulalamika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye mambo ambayo yananitatiza. Jimbo la Njombe Mjini ni Jimbo la wakulima na wafugaji. Tumeanza kufuga kule Njombe toka miaka ya 1930 na ufugaji umekua na kumekuwa na taasisi nyingi zimesaidia ufugaji. Miaka ya karibuni kumekuwa na mdororo mkubwa sana wa eneo la ufugaji. Mwaka 2018 tulikuwa na kaya 2,190, karibu kaya 3,000; kila kaya ilikuwa na angalau ng’ombe watatu; mwaka 2022 tumeporomoka mpaka kaya 1,000. Kaya moja ina ng’ombe mmoja mpaka mmoja na nusu au wawili. Sababu kubwa kwa wakati wa miaka hii ya karibuni ni kutokana na kutokuwa na kiwanda au soko la uhakika la maziwa kwa mkoa wetu, wilaya yetu na Halmashauri yetu ya Njombe Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Njombe tuna kiwanda cha maziwa. Kiwanda kile ni moja ya viwanda ambavyo ni model nzuri sana, kwa maana ya kwamba kinamilikiwa na wafugaji, Halmashauri zetu na taasisi binafsi kama makanisa. Kiwanda hiki kimeingia katika mgogoro wa deni. Tunawashukuru TADB kwa kutaka kukikwamua kiwanda hiki na kuleta deni kubwa la karibu shilingi bilioni 1.2. Deni hilo lingeisha mwaka 2025, lakini kutokana na trend mbaya TADB waliamua kwamba ingekuwa ni vizuri pengine kufanyike re-organization.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa, napenda kusema, TADB hawajaweza kutusaidia sana kwenye ku-reorganize na ku-restructure kiwanda hiki. Napenda kusema, kumekuwa na jitihada nyingi za makusudi za kukikomboa kiwanda hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda hiki bado kina potential, ukiandika business plan inaonyesha kabisa kiwanda hiki kinaweza kikalipa deni la TADB bila matatizo yoyote. Kiwanda hiki kina asset value ya 2.6 billion lakini deni la TADB ni kama 1.6 billion. Kama kiwanda hiki TADB watachukua approach ya kusaidia kama ambavyo nia ya TADB ni kusaidia na ku-promote wakulima na wafugaji, nina uhakika tunaweza tukafikia mahali pazuri kwa sababu wazalishaji, wazaaji wakubwa wa products za kiwanda hiki ni mahoteli ambayo mengi yako Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda hiki kwa cheese pekeyake kinaweza kikazalisha kwa mwaka karibu shilingi bilioni tatu. Kwa hiyo, naona kina potential kubwa. Hakuna sababu kwa nini tusiweke focus kwenye hiki kiwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kusikitisha wenzetu wa TADB badala ya kuliangalia jambo hili kwa upana na kwa kuangalia nia kubwa ya Serikali ya kuchakata mazao ya kilimo na biashara hapa hapa nchini wameamua kuweka dalali auze hiki kiwanda. Sasa hatuna tatizo na TADB kutafuta njia za ku- recover lakini tatizo ni njia gani wanazitumia za ku-recover? Njia wanazotumia za kuweka dalali zinaenda kinyume kabisa na matakwa na dhima nzima ya kwa nini TADB iliundwa ili isaidie wafugaji na wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiwa na kiwanda ambacho kina matatizo unachotakiwa kufanya ni ku-reorganize na ku- restructure. Ukiweka dalali kazi yake ni moja tu. Yeye anafanya kitu kinaitwa asset stripping, anaua. Kwa hiyo, nipende kuiomba sana Serikali kwa kweli ifanye utaratibu na nimelisema hili hapa Bungeni siyo mara moja. Nimeongea na Waziri aliyepita, nimeongea na Waziri aliyepo lakini vile vile Mheshimiwa Waziri Mkuu naye nimeongea naye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba sana Waziri na ninashukuru Waziri ametoa commitment kwamba atakwenda kulishughulikia. Naomba jambo hili lishughulikiwe mwanzo mpaka mwisho lifikie mwisho ieleweke kwamba tunawakomboa wakulima ambao wao wenyewe wamejikomboa kwa kuanzisha kiwanda wakishirikiana na halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii modal ni modal nzuri, tuiendeleze badala ya kuiua kwa kutumia benki yetu ambayo kazi yake ni kuendeleza wakulima na wafugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye mambo mawili matatu ambayo nayo yamejitokeza katika bajeti hii ambayo kwa watu wa Njombe.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Deo muda wako umeisha malizia.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza; ni mawili tu. Sisi watu wa Njombe tumesahaulika kwenye uhimilishaji. Sisi tunasemekana kwamba kuna tatizo kubwa sana la udumavu na tungetegemea Serikali ingeipa focus Njombe kwenye masuala yote yanayosaidia maziwa kuzalishwa kwa wingi ili kutatua tatizo hilo. Kwenye majosho tuna shukuru Serikali kwa kutupa fedha ya kutosha lakini tungeomba tuongezewe angalau majosho mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa kwenye ufugaji wa samaki nipende kuomba sana vile vile tumesahaulika tuna ufugaji wa samaki karibu wafugaji 200 mabwawa karibu 300 lakini kwa vile tunaonekana ni Njombe mjini inadhaniwa kwamba hatuhitaji na hatufugi samaki. Tuombe na sisi tupate majosho na madarasa ya samaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hoja iliyo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kusema namshukuru sana Mheshimiwa Bashe kwa kutupa bajeti ambayo imekuwa ni nzuri. Lakini niseme wazi, napata tabu sana kusema naunga mkono kwa asilimia mia. Kama nitaunga ni kwa sababu tu bajeti hii bado inaendelea kuwapa ruzuku ya mbolea wakulima; lakini nina matatizo makubwa sana na maeneo ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeiangalia sana bajeti hii, na nimeangalia fedha tulizotumia kwenye eneo la umwagiliaji. Kuna skimu za kila aina hapa; skimu 42 mpya, kuna block farms zimeanzishwa, kuna mabonde ya umwagiliaji, kuna skimu nyingine 30 za hekta 69,000. Skimu zote hizi ukiziangalia kwa ujumla wake watu wa njombe hatumo. Kwa hiyo inanipa shida kuelewa allocation ya resources hizi muhimu kwa watu wa Njombe na mikoa mingi ya Nyanda za Juu Kusini, hatumo. Sasa, kinachonisikitisha zaidi…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba ukiangalia kwa karibu zaidi watu wa Njombe tuna zao la chai. Mwaka 2015 tulikuwa na chai vision ya kuweza kuzalisha chai na ku-recruit watu wakulima wadogo wadogo wa chai 2,500. Lengo hilo limefanikiwa, wameweza kulima takriban hekta 2,300 na tume-recruit wakulima wadogowadogo takriban 300.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Njombe Vision kilikuwa na kujenga kiwanda, kiwanda kimejengwa, ni kiwanda kikubwa, kimejengwa na kampuni ya Uniliver kama package ya kusaidia wakulima wadogowadogo. Kiwanda hiki kinapokea majani kilo 50,000 capacity yake. Lakini wakulima wadogowadogo hawa wameshindwa kupeleka majani kufikisha kiwango cha capacity ya kiwanda, wanaweza kupeleka majani tani kilo 15,000. Na watu wa Lupembe wameongezea, tumefika angalau kilo 30,000, bado tuna deficit ya kilo 20,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kiwanda hiki kinatishiwa kufungwa kwa sababu capacity yake ni kubwa na uwezo wa kuleta majani ni mdogo. Kitakachotuwezesha pekee, ili kiwanda hiki kiweza kuendelea na wakulima wadogowadogo kuendelea ku-supply majani na wao kuongeza kipato na ajira ni kama tunaweza tukaongeza uzalishaji wa majani ya chai mabichi. Na itakayo tuwezesha ni umwagiliaji pekee. Katika mazingira kama haya nipende kusema nilitegemea sana kwamba, kwa kweli bajeti hii ingeangalia maeneo kama hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na turudi nyuma tuangalie; katika principle za uchumi ni vema ku-consolidate the game. Watu ambao wamejituma wamefia mahali wameanza, wadogowadogo wanauwezo, wamejiwezesha wenyewe, tuka wa-support kwanza kuliko kuchukua resources nyingi na kuzitupa na kuzituma kila mahali. Hakuna ubaya kuwa na block farms, lakini tuangalie tu-consolidate pale ambapo tumefanya vizuri kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ukisoma kwenye mpango mzoma bajeti ya Mheshimiwa Waziri kwenye maeneo hayo ya chai si kwamba ameyaacha kabisa, anachosema wataendelea kufanya utafiti. Hivi, ni utafiti gani wa umwagiliaji wa chai unataka kuufanya? Mwaka 2019 Halmashauri ya Njombe ilianzisha mpango wa umwagiliaji wa chai kama pilot project. Mimi nilipoingia Bungeni mtu wa kwanza niliyemchukua na kumpeleka Njombe alikuwa ni Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Prof. Mkenda. Walikwenda, tukaangalia maeneo yale na ile project ni nzuri sana, ya block farming ya wakulima wadogowadogo. Hatuongelei large scale farming hapa, wakulima wadogowadogo wa kawaida akina mama, akina dada na akina kaka. Ile program ilitakiwa sasa i-run kwenye zile hekta 2,500.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika mazingira kama hayo kuna sababu gani ya Wizara kutoliangalia eneo hili na muhimu sana la umwagiliaji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ukiangalia Mheshimiwa Bashe anasema yeye anaangalia bajeti yake inaangalia ilani ya chama inaangalia mpango wa miaka mitano. Lakini kwenye ilani ya chama akisoma vizuri page 38 mpaka 41 kifungu 37 “D” kinasema; Serikali kupitia Wizara ya Kilimo ita- focus zaidi kuongeza uzalishaji wa majani ya chai na kuongeza tija kwa wakulima wadogowadogo wa chai. Sasa unawezaje kuacha hawa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuliongelea hilo kwa sababu ya muda, lakini niseme, chai ni ubora, Tanzania bado chai yetu haina ubora. Bodi ya Chai inatakiwa iongeze nguvu kwenye kusimamia ubora wa chai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwa haraka kwenye mbolea. Sisi tunaishukuru sana Serikali na wakulima wa Njombe wanaishukuru sana Serikali kwa kuendelea kutoa mbolea ya ruzuku, na tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa mpango huu mkubwa. Nipende kusema kwamba, tulitegemea kwamba dosari za mpango ule uliopita zingeangalia ili kuweza kuboresha mbolea ifike kwa wakati, kama walivyosema wenzangu, lakini kwa Njombe tuna kitu tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ni wakulima wakubwa, Wananjombe ni watu wanaojituma, ni watu hodari wa kilimo na hili halipingiki mahali popote. Msimu wetu wa kulima ni tofauti na maeneo mengine. Mbolea ya kupewa mifuko mitatu kwa eka haitutoshi, hiyo mbolea ni kwa ajili ya mahindi pekee yake. Ukienda kwenye viazi tunalima misimu mitatu kwa mwaka mmoja, Oktoba, Novemba yaani tunavuna Desemba. Tukipanda Februari tunavuna mwezi Juni. Halafu wananchi wa Njombe wamejiongeza, wanalima kilimo cha kumwagilia cha asili ambacho na chenyewe mwezi Juni wanaanza kuvuna Mwezi Septemba. Tungetaka tuongezewe mifuko ya mbolea angalau sisi tupate kwenye kilimo cha viazi pekee yake mifuko minne mpaka sita, ingefaa kwa kila eka ili tuweze kuendelea mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kusema kwenye hili unaona kunatokea uchakachuaji na hatuwezi kuwa-protect wachakachuaji, lakini ukweli ni kwamba demand ya mbolea kwa maeneo yale ni kubwa mno kuliko supply na haiji kwa wakati. Hiyo inasababisha watu wasiwe waaminifu kuingia katika schemes za kutaka kutengeneza na kuuza mbolea ili kujipatia fedha. Namuunga mkono Waziri kusema kwamba sasa tutafanya hili jambo liwe jinai na isiwe jinai tu, tulifanye kabisa liwe ni uhujumu uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa parachichi kwa sababu muda unaniishia. Nimeona tuna mpango wa kuongeza uzalishaji wa parachichi na wapongeza wakulima wa Tanzania na hasa wa Njombe maana yake ndio wazalishaji wakubwa wa parachichi katika nchi hii. Tunategemea tumefika tani 29,000 na tumepata karibu milioni 52, lakini tunategemea kwenda kwenye tani 50,000 by mwaka 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kufikia hapo bado tunahitaji mambo mengi sana ya kufanya lakini mojawapo Njombe tunaomba kwenye viatilifu tuangaliwe kama vile ambavyo korosho wanapewa, ruzuku kwenye pamba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Mwanyika.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: …na sisi tupate ruzuku kwenye madawa ya ukungu ili tuweze kuongeza uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na nitaomba maelezo mazuri kwa nini Njombe …

MWENYEKITI: Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi, angalau ni nafasi ndogo lakini naweza nikaongea machache.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Waziri kwa hotuba nzuri inayohusiana na mambo ambayo yapo mbele yetu. Pili ninapenda niongelee sekta ya misitu. Sekta ya utalii kwa kuanzia tunaona kwamba ina mchango mkubwa wa asilimia karibu 17 kwenye Pato la Taifa. Sekta hii ya misitu inaonekana kama ni sekta ambayo mchango wake ni mdogo sana, lakini mimi nataka leo niseme bahati mbaya muda ni mfupi, nitaongea mbele ya safari. Niseme kwamba sekta ya misitu ina uwezo mkubwa wa kuchangia kwenye uchumi wa Taifa tukiweka mikakati mizuri. In fact, sekta ya utalii ni very fragile, ni tete, ikitokea shida kidogo tu inatetereka. Imekuja COVID hapa ikaporomoka, ikitokea vita inakuwa ni shida.

Mheshimiwa Spika, sekta hii ya misitu ndiyo sekta ambayo Wizara inatakiwa iiangalie kwa makini sana ili iwe sekta ambayo itaitegemea, ni sekta himilivu, ni sekta jumuishi, ina watu wengi, inatoa ajira kwa watu wengi, kwa hiyo wawe na mikakati mikubwa zaidi.

Mheshimiwa Spika, nami nataka kusema kuwa kuna mambo matatu au manne ambayo wakiyafanya sekta hii katika kipindi cha miaka mitatu kwenda minne tutaona mabadiliko makubwa.

Mheshimiwa Spika, kwanza, tubadilishe mtazamo na fikra. Hivi ni nani aliyesema kwamba samani, milango fremu, lazima ziwe za mninga, mvule au mpodo, nani alisema? Kuna uwezekano mkubwa tukawa na samani nzuri sana zinazotumia mbao laini.

Mheshimiwa Spika, napenda kusema wengi tumetembea hapa, tumekwenda sehemu nyingi, tumekwenda kwenye mahoteli, nitajie hoteli moja tu ambayo utakuta mlango wa mninga, hakuna! Sekta hii tupende kusema, lazima tuanzie kwanza kwenye mchakato mzima wa Serikali wa manunuzi.

Mheshimiwa Spika, tuweke permissive provision inayosema kama soft wood ina-meet kiwango na yenyewe iwe included kama sehemu ya mambo ambayo yanaweza yakatumika. Serikali ita-create demand na iki-create demand itaendelea kukua na kukua na kuongeza ajira.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni suala zima la technology kwenye sekta hii. Tukiangalia, sisi tukivuna mti wa mbao kutoka kwenye gogo tunatumia asilimia 30 tu, iliyobaki yote inapotea. Ukiangalia tuna viwanda vingi vya kuchakata, katika viwanda asilimia 70 vyote ni mbao tupu.

Mheshimiwa Spika, kule Njombe kwa mwaka kuna semi-trailers karibu 40,000 zinazoondoka. Kwa siku kuna semi-trailers karibu 39, ni mbao tu. Tufike mahali sasa kama nchi tufanye maamuzi ya kuongeza thamani kwenye mbao, kwenye mnyororo mzima wa mazao ya misitu, tutafanyaje, tutafanya kwa kuingiza kitu tunakiita EWP (uhandisi katika mazao ya mbao).

Mheshimiwa Spika, nipende kusema tuna products nyingi sana, siyo mbao tu, tuna veneers, tuna plywood, tuna MDF, tuna boriti zile ambazo zinakuwa treated, zote hizi ni products ambazo tunaweza tukileta technology nzuri kwenye soko la mbao au kwenye industry ya mbao tutaweza kuongeza mapato kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Spika, sasa napenda kusema technology ambayo tunaiongelea hapa ni ile ya second level, tutoe vivutio, kwanza kabisa kama Mbunge mmoja alivyosema hapa, tuangalie uwezekano wa ku-zero rate mashine zote ambazo zinakuja kwenye sekta ya mbao, hakuna hasara kwa Serikali, medium term, long term, Serikali itapata fedha zaidi, tuta-create employment zaidi katika sekta hii ya mbao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo tunaweza kufanya ni kuendelea kuiangalia hii sekta kuiondolea vikwazo na kuangalia ada na tozo mbalimbali ambazo zipo kwenye sekta. Bado kuna tozo nyingi sana kwenye hii sekta, GN Na. 59 tuiangalie kwa makini. Lakini kule Njombe kwa mfano…

SPIKA: Malizia sentensi Mheshimiwa.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, upande wa vibali watu wetu wanaosafirisha mbao wanapata taabu sana humu njiani, unatakiwa u-scan document unapoondoka, upite una-scan document mpaka unafika, vituo zaidi ya 15 kwenye destination. Kwa nini tusi-scan pale mwanzo ili biashara iendelee waka-scan mwisho kwenye destination? Kwa hiyo kwenye upande wa vibali tuliangalie kwa karibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile ukisafirisha mbao unatakiwa upate kibali unapotoka, lakini ukapate kibali unapouza. Kwa nini kuwe na vibali viwili? Na tunapoteza muda, tunapoteza mapato, tunapoteza ajira. Niombe sana tuiangalie sekta hii kwa makini sana na tuiongezee fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja ya bajeti kuu iliyoko mbele yetu, pamoja na mwenendo wa uchumi wa nchi yetu. Nianze kwa kumpongeza sana ndugu yangu Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Mwigulu Mchemba, Daktari wa Uchumi; Naibu Waziri wa Fedha, Makatibu Wakuu wote ambao wapo katika Wizara hii na watendaji wote kwa ujumla. Kwa kweli, wameleta bajeti ambayo inatupa mwelekeo mzuri wa tunakokwenda na tunakotoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi wetu unakwenda vizuri, unaonesha uhimilivu. Sekta ya benki inaonekana ina afya, lakini siyo hilo tu, mapato yetu ya ndani yamezidi kuongezeka mwaka hadi mwaka pasipo kutumia nguvu kwa utawala wa sheria wala bila mabavu wala kuwindana. Dalili inaonesha kabisa kwamba mambo haya hayaji kwa bahati mbaya, ni kwa sababu ya uongozi mahiri wa Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na kuwa na maono mazuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii imekuja na msukumo mkubwa sana kwenye sekta ya binafsi. Tumeweza kuona mambo mengi ambayo yamekuwa yakifanyika na yanayoonekana yatafanyika katika kipindi hiki cha mwaka unaokuja, yanayoashiria ni kwa namna gani Serikali sasa inaona sekta binafsi ni muhimu kwa ajili ya kukua kwa uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona Sheria ya Kwanza ya PPP ambayo imetengenezwa kwa ajili ya kuleta sasa miradi ya sekta binafsi ya kimkakati. Tumeona hatua nyingi za kikodi, nisingependa kuzitaja hapa kwa sababu ya muda, lakini nitaje moja tu kwenye eneo la sekta ya madini ambako kwa kweli kulikuwa na ukakasi mkubwa wa kuweka vifungu ambavyo havitabiriki katika sekta ya madini ambavyo vilikuwa vinazuia kutafuta fedha pale ambapo ungeweza kutumia shares zako za kampuni ambayo iko hapa ndani kwa ku-invite wanahisa wale wale au wanahisa wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Sheria ya Kodi ilikuwa inaonekana kama ni deemed realization na kwa hiyo, ilikuwa ina-attract kodi. Sasa hiyo imeondolewa na nina uhakika sekta yetu ya madini inaenda kupaa kwa kasi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mengi ambayo yamefanyika, lakini napenda niliongee lingine moja kuhusu mambo ambayo Serikali imeamua kuyafanya kwenye uthibiti. Kwenye BRELLA kulikuwa na ukakasi mkubwa sana, nami nilikuwa kwenye Kamati ya Viwanda, Uwekezaji na Biashara ambapo tulikuwa tumetoa maoni kwamba ni vizuri Serikali ikaangalia, kule ndipo kwenye MSMEs nyingi zinakuwa registered, lakini kwa mfumo uliokuwepo ilikuwa ngumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu uchumi wake umekua, sasa tunaongelea Shilingi bilioni 85.4 na umetoka bilioni 69.9. Ni nchi ya sita na tuna nchi tano juu yetu. Kwa jinsi ninavyoona, uwekezaji unaoendelea, hali ya kutabirika inavyozidi kuwa katika nchi yetu, miradi ya mikakati, uwekezaji katika sekta ya LNG na rasilimali tulizonazo, bila kusita uongozi kamili, barabara, mahiri wa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, nadhani katika miaka michache ijayo, lazima nchi hizi tatu za juu yetu tutazipita kama tutakwenda katika mwendo tunaoendanao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuongelea sekta moja kwa undani kidogo. Sekta ambayo nadhani ingeweza kuwa na mchango mkubwa zaidi katika uchumi wetu ni sekta ya isitu. Sekta hii ni kubwa, lakini mchango wake kwenye uchumi ni mdogo sana. Sekta hii kwa nchi nyingine ni sekta inayoleta mchango mkubwa sana katika uchumi wa nchi nyingine, lakini sekta hii inaweza kutusaidia kuokoa fedha za kigeni. Sasa hivi pamoja na ukuaji wa uchumi hapa nchini, lakini bado tuna tatizo la kwamba balance of payment kidogo tuko kwenye deficit, kwa sababu, bado tunaagiza vitu vingi kuliko tunavyopeleka nje. Kwa hiyo, sekta hii ya misitu inaweza ikasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta hii ni sekta jumuishi, inatoa ajira nyingi sana, ina uwezo mkubwa wa kuchochea viwanda mpaka ngazi ya vijiji. Ndiyo maana lazima Wizara na Serikali iangalie hii sekta kwa makini sana, kwa sababu mwisho wa siku sekta hii ina uwezo mkubwa sana wa kuchangia mapato makubwa kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uhalisia, sasa hivi ukichukua mti wa mbao unaweza ku-recover asilimia 30 tu peke yake. Asilimia 62 ya mazao ya misitu ni mbao. Uki-process mbao hizo utapata katika meta za ujazo 200,000, uta-recover meta za ujazo 80,000. Kwa bei ya shilingi 250,000 utapata shilingi bilioni 24. Hiyo ndiyo value ya container moja la mita za ujazo 200,000. Ukienda kwenye mazao ambayo yamehandisiwa katika magogo ya mita za ujazo hizo hizo 200,000 unaweza uka-recover up to 80 percent ukapeleka kwenye MDF. Ukisha-recover hiyo unapata meta za ujazo 170,000. Bei ukiwa China kwa hiyo MDF, ni shilingi 600,000. Maana yake ni kwamba, hizo meta za ujazo 200,000 unaweza kupata shilingi bilioni 102. Kutoka shilingi bilioni 24 kwenda shilingi bilioni 102. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ukichukua hilo container la ujazo wa 200,000 linaweza likazalisha pieces 283,000. Hizo pieces zinaweza zikazalisha furniture. Kwa bei ya China, furniture hizo ambazo sisi tunanunua hapa shilingi milioni 10, zinauzwa shilingi 800,000. Maana yake ujazo wa hizo mbao unaweza ukapata shilingi bilioni 226. Kwa hiyo, umetoka kwenye Shilingi bilioni 24 ambayo tunapata hapa, kama tungekuwa tumeongeza value tungepata shilingi bilioni 102, lakini ukipeleka kwenye furniture unapata shilingi bilioni 226. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sekta hii inatakiwa iangaliwe. Ukiangalia TFS wana mashamba karibu 11. Mashamba hayo yanazalisha karibu TCF 1,300,000. Sasa mimi nimechukua 200,000 tu peke yake, uki-multiply hizo na uzalishaji wetu wa mwaka mzima wa 1,300,000 mara 200 hata calculator inakupa error. Maana yake ni trillions of money tunazipoteza kwa kutokufanya value addition on a serious way katika nchi hii. Kwa kweli, hii forestry is gold by itself. Inaweza ikatuzalishia kuliko hata dhahabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi kama Vietnam, juzi juzi tu tulikuwa na uchumi sawa sawa kabisa, lakini Vietnam wameingia kwenye eneo hili la forestry wame-move, na sasa wana-export mazao ya misitu kwenda nchi nyingine bilioni saba walianza mwaka 1989, wamepanda wakafika bilioni 12. Sasa target yao ni bilioni 25 kwa misitu tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema, Wizara inatakiwa iliangalie hili eneo kwa ukaribu sana. Cha kufanya kwanza ni ku-import technology ambazo ni rahisi, ambazo zitasaidia sisi kuingia kwenye uhandisi wa mazao ya misitu. Tunaomba sana kwa kuanzia tu watupe zero rating katika importation. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na suala la madawati, mtu amelia hapa; tuna uwezo mkubwa wa madawati. Kuna vijana hapa wana uwezo mkubwa wa kutengeneza madawati 1,500 kwa siku. Tukiweza kuwa-empower, tunasema tutatengeneza mabilionea, mabilionea tuanze kwa kuwa-empower watu watu watumie soft wood kutengeneza madawati ya nchi nzima, inawezekana. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: …proposal ilikuja lakini mtu mmoja akadhania kwamba watu wana maslahi binafsi, tukapoteza miaka mitano ya kutengeneza madawati, sasa tunatumia madawati ambayo kwa kweli bado tunalia kilio kikubwa katika madawati. Tuna mbao,tunahitaji technology tunaweza tuka-import halafu tukatengeneza madawati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Kudhibiti Utakatishaji wa Fedha Haramu wa Mwaka 2022
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na kunikumbuka ili nami niweze kutoa mchango kwenye muswada uliyo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze moja kwa moja kwanza kwa kumpongeza sana Waziri wa Fedha na Mwanasheria Mkuu kwa kuja na Muswada huu. Muswada huu pamoja na kwamba mawanda yake yanaongelea zaidi mambo ambayo ni ya kuimarisha zaidi udhibiti ili Tanzania nayo isiwe ni sehemu ambayo labda utakatishaji unaweza kushamiri, lakini tukumbuke vilevile kwamba sheria hii inawahusu Watanzania wa kawaida, mmoja mmoja na wengine walio wengi. Kwa hiyo wengine leo watakuwa na mawazo kwamba labda sheria hii itawapa ahueni kwenye mambo fulani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Kwanza kabisa, mimi naichukulia sheria hii kama ni mwendelezo wa yale ambayo tuliyaanza jana ya kuendelea ku-improve utoaji haki katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hili kosa la utakatishaji ni kubwa, lina madhara makubwa kwenye uchumi na tuna kila sababu ya kuhakikisha kwamba utakatishaji fedha ni jambo ambalo linapigwa vita kwa nguvu zote na udhibiti unakuwepo katika nchi. Pamoja na kusema hayo, nimeridhishwa na kufarijika na kuona marekebisho ambayo yamefanywa katika Muswada huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana Serikali kwa ku-take into account mawazo mengi ya Kamati ambayo waliyatoa, yameturahisishia kazi na yanaonesha kabisa kwamba tuna ushirikiano mzuri katika kuendeleza suala hili la kupeleka sheria ambazo zina maslahi makubwa na mapana kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo mawili tu ambayo napenda niyaongelee; moja ni kifungu cha tatu ambacho tafsiri yake imepanuliwa, imeongezwa, imebadilishwa na imeandikwa upya. Kifungu hiki cha tatu katika sheria ya zamani kulikuwa na hilo kosa linaloitwa kosa mtangulizi au la msingi (predicate offense).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa wanaojua historia ya Muswada huu au sheria hii watagundua kwamba kwa muda mrefu makosa yaliyongezwa mpaka ikafika wakati kosa la kawaida kabisa na lenyewe linaweza lika-qualify kuwa ni utakatishaji. Hiyo ilisababisha matatizo makubwa, hisia mbaya dhidi ya Serikali yetu kwa kudhani kwamba kosa lolote unalolifanya linaweza likawa ni utakatishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Muswada huu sasa umekuja na umetibu tatizo hilo. Nimefurahia kuona namna interpretation katika sheria mpya inavyojaribu kwa kusoma kifungu kile cha 12 ambapo sasa makosa haya yametenganishwa; kosa lile ambalo ndilo la msingi (predicate offense) na kosa lenyewe la utakatishaji, ni makosa ambayo sasa hayatakuwa pamoja. Huko nyuma tukumbuke kwamba makosa ya utakatishaji ni makosa ambayo hayana dhamana. Kwa hiyo ukweli ni kwamba pamoja na kudhibiti fedha haramu lakini mwisho wa siku vilevile kuna uwezekano wananchi wakaumia kama jambo hili lisingeangaliwa kwa umakini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza, moja, ningependa kifungu namba 28B ambacho ni kipya ambacho kinaongelea eneo la wakurugenzi wa makampuni, mameneja, kwamba watakuwa-presumed kwamba wame- commit offense chini ya Sheria ya Anti-money Laundering iwapo hawatajitetea na kuonesha kwamba hawakuhusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili uweze kujitetea kwamba haukuhusika unatakiwa upite katika mfumo wa kisheria na tukumbuke kwamba sheria hii isiangaliwe peke yake iangaliwe na sheria nyingine. Sheria hii na makosa katika sheria hii ni makosa ya kihujumu uchumi, kwa hiyo hayana dhamana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni vizuri basi huko mbele Mwanasheria Mkuu angeliangalia hili baada ya kupitisha sheria tukaangalia na sheria nyingine ambazo zinaendana na hii ili ziweze kutoa matumaini makubwa zaidi ambayo Mheshimiwa Rais wetu ameahidi umma wa Watanzania na anaendelea kuyafanyia kazi kwa haraka sana katika utoaji wa sheria kama wote tunavyoona mambo yanavyobadilika na kuwa mazuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania wa Mwaka 2022
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania wa mwaka 2022 uliyoko mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kwa kupongeza Serikali kwa kuleta Muswada huu ambao umekuja kwa wakati muafaka, umekuwa ukingojewa na Watanzania, wawekezaji wa ndani na wa nje kwa muda mrefu. Kwa hiyo, naipongeza sana Wizara na Serikali.

Mheshimiwa Spika, ni mwendelezo tu wa yale ambayo Mheshimiwa Rais alituambia alipokuja kutuhutubia hapa tarehe 22 mwezi Aprili, mwaka 2021, aliposema kwamba nchi yetu imekuwa ikilalamikiwa kwa kutokuwa na mazingira mazuri ya biashara na uwekezaji, ikiwemo kutokuwa na sera zinazotabirika na utaratibu wa kodi usio na utulivu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ameanza kutekeleza. Tumeshuhudia katika miaka mmoja na nusu au miwili, ambayo amekuwa madarakani, hali ya uwekezaji imeongezeka ambayo inaashiria wazi kabisa kwamba utekelezaji wa yale aliyotuambia ndani ya Bunge hili unakwenda vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, napenda kusema, sumu ya uwekezaji whether uwe ni wa ndani au ni wa nje, uko katika maeneo mawili ambayo ni sheria ya kutotabirika na urasimu. Niseme kwamba suala la kutotabirika kwa kiasi kikubwa tunaendelea kuishukuru Serikali na tunatambua, ndiyo maana tuna blueprint, utekelezaji wake umeanza. Tulikuwa tunaiangalia muda mfupi uliopita, wameweza kuondoa tozo nyingi sana, wameweza kurekebisha baadhi ya tozo; katika tozo karibu 300, tayari wameshashughulika na zimebakia tozo 114 ambazo wanaendelea kuzishughulikia. Kwa hiyo, inasaidia kwenye kutabirika kwa mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, urasimu bado ni tatizo kwa wawekezaji. Kwa kweli tulikuwa tumetegemea na Mwenyekiti wangu wa Kamati ameweza kuyasema hapa, tulikuwa tumelichakata hili jambo vizuri tukiamini kwamba labda mawazo yetu katika kamati yanaweza kusaidia kupunguza urasimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa utafiti wetu na kwa kuangalia majirani na tuelewe uwekezaji ni ushindani; unapoongelea uwekezaji, maana yake unaongelea ushindani, uwe wa ndani au wa nje.

Mheshimiwa Spika, tuliloliona ni kwamba hata ukipewa cheti cha uwekezaji kwa maana ya incentives za TIC, bado unatakiwa uanze kuhangaika na kushughulika na taasisi na idara za Serikali, ushughullike na wakala za Serikali ambazo ndiyo zinatoa vibali. TIC wao wanakupa kibali kikubwa kimoja, lakini sheria inawataka, ukisoma kwenye section 18 subsection 1 mpaka 5, unakuta mwendelezo mzima wa nini kinatakiwa kitokee? Sasa tuwashukuru Wizara wamechukua mawazo ya kamati kwa kiasi fulani walipokubali kuweka limit ya kutoa hiyo certificate. Ilikuwa ndani ya siku 14, sasa itatolewa ndani siku saba. Kwa hiyo, ni maendeleo mazuri, yanaashiria kwamba tunakwenda vizuri na tunakwenda mwendo wa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado kuna mitego mingi ndani ya sheria hiyo. Maana unatoa ombi la kupewa incentives. Ukishapewa ombi lako na TIC, unahitaji kupata vibali vingine. Ndani ya vibali hivyo, inatakiwa upewe majibu ya vibali vile ambavyo unavihitaji katika idara na taasisi nyingine za Serikali ambako ndiyo imekuwa ni tatizo. Sheria inasema kwamba wanatakiwa ndani ya siku saba wawe wamekupa majibu na kwamba usipopata majibu, aidha upate leseni au upate idhini ya kile unachokitaka, au (na ndiyo hapo lilipo tatizo) upewe mrejesho.

Mheshimiwa Spika, hili neno “mrejesho”, wakati mwekezaji ameomba vibali, ndiyo kansa ya uwekezaji, kwa sababu mrejesho haujawa defined, mrejesho hauelezewi. Maana yake ni kwamba utajibiwa kwa barua kwamba jambo lako linashughulikiwa na maana yake ni kwamba ukishajibiwa linashughulikiwa, siku saba ni kama hazina maana tena, kwa sababu haziwezi ku-run tena, kwa sababu umeshajibiwa kwamba jambo lako linashughulikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ndiyo maana sisi kwa busara, tuliona ni vema TIC, unapopata nafasi ya kutunga sheria, hii sheria imetungwa zaidi ya miaka 25 iliyopita na inatungwa upya, tuliona ni wakati muafaka kwa Serikali kuja na kitu tofauti kitakachoweza kukidhi haja ya wawekezaji wa ndani na wa nje. Hilo lingetokea kwa kuifanya TIC kuwa mamlaka kamili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado TIC inaitwa kituo. Maana “kituo”, kuna Kituo cha Polisi, kuna Kituo cha Basi; sasa wawekezaji wa ndani na nje, kwa kweli tulidhani kwamba kuweka mamlaka ingesaidia nchi. Ingeisaidia kuifanya TIC iwe na mamlaka, iweze kufanya maamuzi na kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuongea hilo, niongelee vile vile ushiriki wa sekta binafsi. Tunashukuru na kwamba Serikali imeendelea, Wizara imeendelea kuiamini sekta binafsi katika vyombo vya maamuzi. Kwa hiyo, Bodi ya TIC, ina private sector, lakini chombo kikubwa cha maamuzi ni kile ambacho kinatoa vile vile vivutio vya ziada. Chombo hicho kina Wajumbe 11 jumlisha mmoja. Hawa 11 ni Wajumbe wote kutoka Serikalini. Unaanza na Mawaziri saba, Waziri Mkuu akiwa ndiyo Mwenyekiti. Halafu unakuta BOT Governor, then unamkuta kiongozi wa TIC kwa maana ya Secretary General kwa maana ya Katibu wa TIC. Pia kuna mtu mmoja ambaye huyo anaweza akawa invited muda wowote. Sasa tungependa angalau kuwe na mtu mmoja wa private sector.

Mheshimiwa Spika, najua tunatunga sheria, tulitakiwa tulete mabadiliko. Niseme hatuwezi kuleta mabadiliko sasa lakini busara ya Serikali itumike. Tunakwenda kwenye kipindi ambacho tunafanya kazi na private sector. Hapa Waziri wa ujenzi alituambia, miradi mingi mikubwa ya barabara na ujenzi wa ma-airport sasa itakwenda kwa mtindo wa PPP, maana yake ni Private Public Partnership. Sasa tufike mahali tuanze kuamini kwamba tunahitaji private sector kwenye vyombo vingine vikubwa vya maamuzi kwa ajili ya maslahi ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, wengine wanadhani maslahi ya Taifa maana yake lazima uwe Serikalini ndiyo utambue maslahi ya Taifa. Unaweza kuwa kwenye private sector ukayafahamu vizuri na ukaisaidia nchi vizuri zaidi. Ni kwa nia njema kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho kabisa, vivutio vya uwekezaji vya ziada vinatolewa katika mazingira ambayo inatakiwa mwekezaji aombe. Tufike mahali tujue tunashindana. Kwa hiyo, vingekuwa vinaeleweka angalau kwa kiasi fulani ili mtu asiende Rwanda au Kenya ambako wana mamlaka tayari na wanafanya maamuzi kwa haraka sana tunavyosikia na kupitia taarifa mbalimbali tulizonazo ili sasa vivutio hivyo viweze kuwavuta watu katika maeneo mbalimbali hasa yale ya mbali kama vile maeneo ya mikoani ambako kuna viwanda vile vya zamani vya processing, vya agriculture na vya skin na hides vingeweza vikajengwa kwa wingi na vikawa modernized.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naona muda wangu umekwisha, naunga mkono hoja iliyoko mbele yetu. (Makofi!)
Muswada wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi wa Mwaka 2022
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania wa mwaka 2022 uliyoko mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kwa kupongeza Serikali kwa kuleta Muswada huu ambao umekuja kwa wakati muafaka, umekuwa ukingojewa na Watanzania, wawekezaji wa ndani na wa nje kwa muda mrefu. Kwa hiyo, naipongeza sana Wizara na Serikali.

Mheshimiwa Spika, ni mwendelezo tu wa yale ambayo Mheshimiwa Rais alituambia alipokuja kutuhutubia hapa tarehe 22 mwezi Aprili, mwaka 2021, aliposema kwamba nchi yetu imekuwa ikilalamikiwa kwa kutokuwa na mazingira mazuri ya biashara na uwekezaji, ikiwemo kutokuwa na sera zinazotabirika na utaratibu wa kodi usio na utulivu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ameanza kutekeleza. Tumeshuhudia katika miaka mmoja na nusu au miwili, ambayo amekuwa madarakani, hali ya uwekezaji imeongezeka ambayo inaashiria wazi kabisa kwamba utekelezaji wa yale aliyotuambia ndani ya Bunge hili unakwenda vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, napenda kusema, sumu ya uwekezaji whether uwe ni wa ndani au ni wa nje, uko katika maeneo mawili ambayo ni sheria ya kutotabirika na urasimu. Niseme kwamba suala la kutotabirika kwa kiasi kikubwa tunaendelea kuishukuru Serikali na tunatambua, ndiyo maana tuna blueprint, utekelezaji wake umeanza. Tulikuwa tunaiangalia muda mfupi uliopita, wameweza kuondoa tozo nyingi sana, wameweza kurekebisha baadhi ya tozo; katika tozo karibu 300, tayari wameshashughulika na zimebakia tozo 114 ambazo wanaendelea kuzishughulikia. Kwa hiyo, inasaidia kwenye kutabirika kwa mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, urasimu bado ni tatizo kwa wawekezaji. Kwa kweli tulikuwa tumetegemea na Mwenyekiti wangu wa Kamati ameweza kuyasema hapa, tulikuwa tumelichakata hili jambo vizuri tukiamini kwamba labda mawazo yetu katika kamati yanaweza kusaidia kupunguza urasimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa utafiti wetu na kwa kuangalia majirani na tuelewe uwekezaji ni ushindani; unapoongelea uwekezaji, maana yake unaongelea ushindani, uwe wa ndani au wa nje.

Mheshimiwa Spika, tuliloliona ni kwamba hata ukipewa cheti cha uwekezaji kwa maana ya incentives za TIC, bado unatakiwa uanze kuhangaika na kushughulika na taasisi na idara za Serikali, ushughullike na wakala za Serikali ambazo ndiyo zinatoa vibali. TIC wao wanakupa kibali kikubwa kimoja, lakini sheria inawataka, ukisoma kwenye section 18 subsection 1 mpaka 5, unakuta mwendelezo mzima wa nini kinatakiwa kitokee? Sasa tuwashukuru Wizara wamechukua mawazo ya kamati kwa kiasi fulani walipokubali kuweka limit ya kutoa hiyo certificate. Ilikuwa ndani ya siku 14, sasa itatolewa ndani siku saba. Kwa hiyo, ni maendeleo mazuri, yanaashiria kwamba tunakwenda vizuri na tunakwenda mwendo wa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado kuna mitego mingi ndani ya sheria hiyo. Maana unatoa ombi la kupewa incentives. Ukishapewa ombi lako na TIC, unahitaji kupata vibali vingine. Ndani ya vibali hivyo, inatakiwa upewe majibu ya vibali vile ambavyo unavihitaji katika idara na taasisi nyingine za Serikali ambako ndiyo imekuwa ni tatizo. Sheria inasema kwamba wanatakiwa ndani ya siku saba wawe wamekupa majibu na kwamba usipopata majibu, aidha upate leseni au upate idhini ya kile unachokitaka, au (na ndiyo hapo lilipo tatizo) upewe mrejesho.

Mheshimiwa Spika, hili neno “mrejesho”, wakati mwekezaji ameomba vibali, ndiyo kansa ya uwekezaji, kwa sababu mrejesho haujawa defined, mrejesho hauelezewi. Maana yake ni kwamba utajibiwa kwa barua kwamba jambo lako linashughulikiwa na maana yake ni kwamba ukishajibiwa linashughulikiwa, siku saba ni kama hazina maana tena, kwa sababu haziwezi ku-run tena, kwa sababu umeshajibiwa kwamba jambo lako linashughulikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ndiyo maana sisi kwa busara, tuliona ni vema TIC, unapopata nafasi ya kutunga sheria, hii sheria imetungwa zaidi ya miaka 25 iliyopita na inatungwa upya, tuliona ni wakati muafaka kwa Serikali kuja na kitu tofauti kitakachoweza kukidhi haja ya wawekezaji wa ndani na wa nje. Hilo lingetokea kwa kuifanya TIC kuwa mamlaka kamili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado TIC inaitwa kituo. Maana “kituo”, kuna Kituo cha Polisi, kuna Kituo cha Basi; sasa wawekezaji wa ndani na nje, kwa kweli tulidhani kwamba kuweka mamlaka ingesaidia nchi. Ingeisaidia kuifanya TIC iwe na mamlaka, iweze kufanya maamuzi na kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuongea hilo, niongelee vile vile ushiriki wa sekta binafsi. Tunashukuru na kwamba Serikali imeendelea, Wizara imeendelea kuiamini sekta binafsi katika vyombo vya maamuzi. Kwa hiyo, Bodi ya TIC, ina private sector, lakini chombo kikubwa cha maamuzi ni kile ambacho kinatoa vile vile vivutio vya ziada. Chombo hicho kina Wajumbe 11 jumlisha mmoja. Hawa 11 ni Wajumbe wote kutoka Serikalini. Unaanza na Mawaziri saba, Waziri Mkuu akiwa ndiyo Mwenyekiti. Halafu unakuta BOT Governor, then unamkuta kiongozi wa TIC kwa maana ya Secretary General kwa maana ya Katibu wa TIC. Pia kuna mtu mmoja ambaye huyo anaweza akawa invited muda wowote. Sasa tungependa angalau kuwe na mtu mmoja wa private sector.

Mheshimiwa Spika, najua tunatunga sheria, tulitakiwa tulete mabadiliko. Niseme hatuwezi kuleta mabadiliko sasa lakini busara ya Serikali itumike. Tunakwenda kwenye kipindi ambacho tunafanya kazi na private sector. Hapa Waziri wa ujenzi alituambia, miradi mingi mikubwa ya barabara na ujenzi wa ma-airport sasa itakwenda kwa mtindo wa PPP, maana yake ni Private Public Partnership. Sasa tufike mahali tuanze kuamini kwamba tunahitaji private sector kwenye vyombo vingine vikubwa vya maamuzi kwa ajili ya maslahi ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, wengine wanadhani maslahi ya Taifa maana yake lazima uwe Serikalini ndiyo utambue maslahi ya Taifa. Unaweza kuwa kwenye private sector ukayafahamu vizuri na ukaisaidia nchi vizuri zaidi. Ni kwa nia njema kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho kabisa, vivutio vya uwekezaji vya ziada vinatolewa katika mazingira ambayo inatakiwa mwekezaji aombe. Tufike mahali tujue tunashindana. Kwa hiyo, vingekuwa vinaeleweka angalau kwa kiasi fulani ili mtu asiende Rwanda au Kenya ambako wana mamlaka tayari na wanafanya maamuzi kwa haraka sana tunavyosikia na kupitia taarifa mbalimbali tulizonazo ili sasa vivutio hivyo viweze kuwavuta watu katika maeneo mbalimbali hasa yale ya mbali kama vile maeneo ya mikoani ambako kuna viwanda vile vya zamani vya processing, vya agriculture na vya skin na hides vingeweza vikajengwa kwa wingi na vikawa modernized.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naona muda wangu umekwisha, naunga mkono hoja iliyoko mbele yetu. (Makofi)
The Finance Bill, 2022
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi na maelezo uliyoyatoa sasa hivi yananiweka katika ngumu zaidi. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, sina mawazo mapya lakini mawazo nilikuwa nimeshayatoa nikiwa na matumini yangekuwa yamejumuishwa katika sheria. Kwa maana ya mabadiliko lakini nitaongea kwa kifupi na kwa ujumla tu, kwa sababu bado nadhani ni mambo ambayo Mwenyekiti wetu wa Bajeti na Kamati yetu ya Bajeti imelisisitiza sana.

Mheshimiwa Spika, Muswada huu na bajeti hii tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwamba imekwenda kuanza kuangalia namna gani inaweza ikaondoa matatizo na ikafanya ile blue print ianze kufanyika katika maeneo mbalimbali, kwenye kilimo na kwenye viwanda na hasa kwenye kulinda viwanda vyetu, kwa hiyo, kuna hatua nyingi za kikodi zimefanyika.

Mheshimiwa Spika, wakati nachangia niliongea wakati ule kwamba kwenye viwanda vya chuma bado kuna tatizo, nilikuwa nimetegemea labda lingesikika na sikuona mapema labda ningeweza kulileta lakini nitaliongelea kwa haraka tu.

Mheshimiwa Spika, bado tuna tatizo ukiangalia kwenye HS code zimewekwa sasa hivi HS code 9406.2090 ambayo kimsingi inaongelea pre-fabricated designs, sasa hivi imewekewa zero rate.

Mheshimiwa Spika, nilisema wakati ule na ninasema tena kwa kifupi kwamba kwa kuweka zero rate kwenye pre-fabricated designs za materials, buildings tumewaweka katika disadvantage viwanda vya ndani kwa sababu wao bado wanaagiza material kwa ajili ya kutengeneza hizo designs mbalimbali za pre-fab na matokeo yake ni kwamba itakuwa ni cheaper kwa mtu kuagiza kitu ambacho kimeshakuwa molded, kimeshatengenezwa kukileta nchini, wakati kingeweza kufanyika hapa.

Mheshimiwa Spika, tuna viwanda vya chuma capacity ni kama asilimia 40 tu ya uzalishaji vingeweza vikafanya kazi hapa vika-design na vikajenga, kwa kufanya hii kitu tunajikoshesha sisi kwanza mapato lakini cha pili tunaua ajira. Ninafikiria kwa mbele basi waliangalie kwa makini sana hili jambo.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili kwenye Muswada wa Sheria uliyopo mbele yetu ya Wakala wa Meli, Sura 415, tunamshukuru Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Waziri kwa kufanya maamuzi ambayo kwa muda mrefu yamekuwa ni magumu kufanyika na sasa wameyafanya katika Muswada huu.

Mheshimiwa Spika, kuondoa mandate ya TASAC kufanya kazi kwenye maeneo fulani Fulani, sasa wameacha maeneo matatu tu, kutoa mizigo yote inayohusiana ambayo ni silaha, makinikia na nyara za Serikali.

Mheshimiwa Spika, sasa kuna suala la msingi hapa ambalo ni kwamba kwa sheria za nchi yetu tumekuwa tukiangalia viwanda vya cement kama vile ni viwanda vya uzalishaji wa madini, hilo jambo limepelekea sasa hata kwenye utunzi wa sheria na utaratibu wa sheria kwamba baadhi ya vitu ambavyo visingetakiwa viwe katika sekta hii ya uzalishaji wa cement tunaviingiza kama vile vipo katika madini.
Mheshimiwa Spika, ninapenda kusema kwamba kwenye HS Code 2523 ambayo mimi nilidhania ingetolewa, haikutolewa baada ya Serikali kuwa imeridhia kulimiti mandate ya TASAC, unakuta bado vitu kama clinker ambayo ni raw material kwenye cement bado itaendelea kuwa cleared na TASAC.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli jambo hili linaipa tu urasimu, linaongeza gharama kwenye viwanda vya cement, ni vizuri basi hata kama sikuleta mabadiliko liangaliwe kwa makini ili huko mbele nayo hii iondolewe kwa sababu haina uhusiano wowote na makinikia. Nadhani ni kosa tu la kiutaalam la muda mrefu, tungeiondoa hiyo ili na yenyewe isiwe sehemu ya makinikia na ifanyike katika utaratibu wa kawaida ili kuvipa efficiency viwanda vyetu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)