Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Deogratius John Ndejembi (525 total)

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na naishukuru Serikali kwa majibu yake mazuri na ya kina. Maswali yangu mawili ya nyongeza ni kama ifuatavyo: Swali la kwanza, je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha kanzidata kwa kutumia TEHAMA ili kuhakikisha kwamba wanaonufaika ni wale ambao wanakidhi vigezo vilivyowekwa na pia kuondoa mianya ya watu wanaonufaika kusajiliwa mara mbili kwenye maeneo tofauti?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, ni je, sasa Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba kaya ambazo hazikunufaika awali sasa zitanufaika katika hii Awamu ya TASAF III, hususan wazee siyo tu wa Bukoba Manispaa, Mkoa wa Kagera bali wa Taifa kwa ujumla? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tayari mpango huu wa kuanzisha kanzidata ya walengwa wote wanaopokea fedha za TASAF imeanza. Mwanzo ilianza katika halmashauri 19 nchini lakini hadi hivi ninavyoongea tayari imekwenda katika halmashauri 39 na tayari tunaanza kuweka mfumo kwa ajili ya kuunganisha na NIDA, kuunganisha na mitandao yetu ya simu ili walengwa hawa badala ya kupokea fedha hizi dirishani kwa wale wanaokwenda kugawa, fedha hizi ziende moja kwa moja kwenye simu zao. Tutafanya hivi ili kuhakikisha kwamba hakuna kwanza double payment katika suala hili, kwa sababu kuna maeneo ambayo watu huwa wanalalamika mtu anapokea mara mbili au mtu akiwa hayupo watu wengine wanachukua zile fedha. Sasa ili kudhibiti hilo ndiyo maana tunakwenda sasa katika ku-roll out hii katika halmashauri zote 185 za Tanzania Bara na tuta- roll out katika maeneo yote ya Unguja na Pemba.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali lake la pili, kwamba ni lini Serikali sasa itatanua mpango huu kwa wazee ambao hawakuingia na kaya ambazo hazikuingia. Naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge yeye wa Viti Maalum anafahamu anatoka Kagera, lakini hata wa Jimbo la Bukoba Mjini Mheshimiwa Byabato anafahamu kwamba sasa kaya zote katika Awamu hii ya Pili ya TASAF zinakwenda kuingia kwenye mpango huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niwatoe mashaka Wabunge wote wa Majimbo humu ndani na wa Viti Maalum kwamba mpango huu unakwenda kwenye kaya 1,400,000 ambayo ni sawasawa na watu milioni saba wanakwenda kunufaika na Mpango huu wa TASAF.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naitwa Michael Costantino Mwakamo, Mbunge kutoka Kibaha Vijijini. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, najua TASAF ilianza awamu ya kwanza kwa kuwapatia walengwa miradi ya uwekezaji kama majengo mbalimbali zikiwemo kumbi za maonyesho. Katika Jimbo la Kibaha Vijijini, wazee walipewa mradi huu awamu ya kwanza; je, TASAF wana mkakati gani juu ya kuwafanyia ukarabati jengo ambalo walipewa katika awamu ya kwanza ambalo sasa limechakaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutumia nafasi hii kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge, awamu ya kwanza ilijikita zaidi katika ujenzi wa miundombinu na si Kibaha Vijijini tu bali katika halmashauri nyingi sana katika nchi yetu ambazo majengo haya au miradi hii ilifanyika. Sasa baada ya awamu ya kwanza kuisha na kwenda awamu ya pili na sasa tuko awamu ya tatu phase II, ni kwamba majengo haya na miradi hii yote ilikabidhiwa kwa Wakurugenzi wa Halmashauri husika. Na ni wajibu wa Wakurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha kwamba wanatunza majengo haya na wasiwaachie tu wale walengwa peke yao; ni wajibu wa Wakurugenzi kuhakikisha sustainability ya miradi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, niko tayari kuongozana na Mheshimiwa Mbunge kuelekea katika halmashauri yake na kuhakikisha tunakwenda kuangalia miradi hiyo na kuwaagiza Wakurugenzi ili kuhakikisha kunakuwa na sustainability.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. SAASISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwanza nishukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, majibu ambayo kimsingi yatapunguza maumivu makubwa waliyopata wananchi wa Hai tarehe mbili kutokana na majibu ya swali lao kuhusu suala la ushirika. Niwaambie wananchi wa Hai watulie Serikali yao inawapenda sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niulize swali la nyongeza la kwanza; kwa kuwa hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; na kwa kuwa wananchi wa Hai tarehe 28 walifanya jambo lao kwa asilimia kubwa sana na kuleta utulivu humu Bungeni na huko nje; je, ni lini sasa Serikali itatekeleza kwa kiwango angalau cha asilimia 50 ya ahadi ya Mheshimiwa Rais?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; je, ni lini Serikali italipa madeni ya watumishi wa afya na Walimu ambao ni wastaafu, deni ambalo mimi mwenyewe nimeshaliwasilisha kwa Mheshimiwa Waziri la milioni 171 ili watumishi wa afya waendelee kufanya kazi yao kwa uaminifu? Ikizingatiwa miongoni...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa umeshauliza swali.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Saasisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ameuliza ni lini sasa Serikali itatekeleza ahadi ya kuajiri watumishi wa afya japo kwa asilimia 50. Bunge lako Tukufu na Wabunge wote humu ni mashuhuda wa jitihada kubwa zinazofanywa na Serikali katika kujenga Hospitali za Wilaya, kuongeza vituo vya afya na zahanati. Hivyo basi, pale ambapo bajeti itaruhusu, tutaendelea kuajiri watumishi katika Idara ya Afya; na hawa 75 wanaokwenda Hai, ni sawa na asilimia 18.6 ya watumishi wote ambao wameajiriwa hivi sasa. Kwa hiyo, kadri uwezo utakavyoruhusu, tutaendelea kuleta watumishi katika Wilaya ya Hai.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili juu ya madeni ya watumishi, Mheshimiwa Mbunge kwanza amekuwa mstari wa mbele kupigania haki za hawa watumishi na ili jambo amenieleza mimi mwenyewe zaidi ya mara mbili. Tayari tunashughulikia, ukiacha deni ambalo alikuwa analizungumzia la shilingi milioni 171, tayari yalikuja maombi 137 katika Ofisi ya Rais Utumishi yenye jumla ya thamani ya shilingi milioni 246 ili yaweze kushughulikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa madeni yaliyolipwa ni Sh.50,690,000/= na madeni yenye thamani ya shilingi milioni 148 ambayo ni sawa na watu 88, yamerudishwa kwa mwajiri ambaye ni Mkurugenzi wa Halmashauri ya Hai kwa sababu yalikuwa na dosari mbalimbali. Pale ambapo Mkurugenzi wa Hai atarekebisha dosari zile na kuzileta katika Ofisi ya Rais Utumishi, basi nasi tutazifanyia uhakiki tuweze kulipa madeni hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kuna madeni ya watu 27, sawa na shilingi milioni 33 na kitu hivi, tayari yameshafanyiwa uhakiki na yametolewa katika Ofisi ya Rais, Utumishi na sasa yapo Wizara ya Fedha, tayari kwa malipo muda wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Lushoto ina uhaba mkubwa sana wa watumishi katika sekta ya elimu na afya. Katika sekta ya elimu, msingi peke yake ambapo tuna shule 168, tuna uhaba wa watumishi 1,274. Tuna vituo 63 vya kutoa huduma za afya lakini tuna uhaba wa watumishi 1,218. Ni lini Wizara hii itaiangalia Halmashauri ya Lushoto kwa jicho la huruma na kutuondoa katika kadhia hii ambayo wananchi wanaendelea kupata?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shangazi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuajiri walimu kadri bajeti itakavyoruhusu. Katika bajeti ya mwaka 2021, Serikali ilitenga bajeti ya ajira 9,500 kwa walimu na watumishi katika kada ya afya 10,467. Hivyo basi, pale Serikali itakapoanza kuajiri hawa, tutaangalia pia na Mlalo kule ili aweze kupata watumishi hawa. Ahsante. (Makofi)
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa msamaha ulitolewa kwa wale wote ambao waliondolewa kazini kwa kukosa sifa ya kidato cha nne na baadaye wakajiendeleza kupata sifa hizo; na kuna maeneo ambayo watu hawana mawasiliano ya simu kama Ulingombe, Vidunda, Malolo na Kisanga.

Je, Serikali inatoa tamko gani kwa waajiri kuhakikisha kwamba watu wote ambao wame-qualify kurudishwa na hawana taarifa wanapata taarifa hizi kwa wakati na wanarudishwa kazini bila masharti ya ziada?

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa watumishi hawa ambao walishindwa kujiendeleza kidato cha nne lakini walikuwa na sifa stahiki wakati wanaajiriwa waliondolewa kazini walitumikia hii nchi kwa uadilifu na uzalendo lakini hawakuwa na kosa mahali zaidi ya maelekezo ya Serikali.

Je, ni lini Serikali inaenda kuhakikisha kwamba malipo yao na stahiki zao zinalipwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dennis Lazaro Londo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, msamaha uliotolewa kwa watumishi hawa ambao waliajiriwa baada ya tarehe 20 Mei, 2004 ambapo tangazo la Serikali lilitoka mpaka ifikapo Mei, 2004 watumishi wote wanaoajiriwa Serikalini ni lazima wawe na sifa ya kidato cha nne. Hata hivyo kuna waajiri ambao waliajiri watumishi baada ya tangazo lile la Serikali. Tunatambua kwamba haikuwa kosa la wale watumishi walioajiriwa.

Mheshimiwa Spika, sasa Serikali ilitoa maelekezo kupitia Katibu Mkuu Kiongozi kwamba hawa watumishi wote walioajiriwa baada ya tarehe hiyo wawe wamejiendeleza na kupata sifa ya kuajiriwa Serikalini, yaani cheti cha kidato cha nne mpaka ifikapo Desemba, 2020. Na waliorejeshwa kazini mpaka kufikia Desemba 2020 ni zaidi ya watumishi 4,335 ambao walirudi kwa sababu walikuwa wamejiendeleza.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa wale ambao kama Mheshimiwa Mbunge alivyosema, kwamba hawakupata taarifa popote ya kwamba wajiendeleza na walijiendeleza kabla ya ile deadline iliyowekwa basi niwaelekeze waajiri wote nchini kuweza kuliangalia hili kuwachukua watumishi hawa kama walijiendeleza tu kabla ya kufikia Desemba, 2020 lakini hawakupata tangazo la kurejea kazini basi waajiri waweze kuliangalia hilo.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la pili aliulizia wale ambao hawakujiendeleza lakini waliajiriwa baada ya Mei 2004. Hawa siku ya Mei Mosi Mheshimiwa Rais wetu mama yetu Samia Suluhu Hassan alitoa maelekezo, kwamba watumishi wote waliokuwa na sifa ya elimu ya darasa la saba walipwe stahiki zao kwa sababu hawa hawakughushi wao waliajiriwa siyo makosa yao basi stahiki zao kama hawakurejeshwa kazini na kama hawakujiendeleza walipwe. Tayari ofisi yetu ilishatoa waraka kupitia Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Utumishi kwa waajiri wote nchini kuanza kushughulikia hawa wenye elimu ya darasa la saba ambao hawakurejeshwa kazini, na tayari linafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza, na nimpongeze pia Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kutupandisha daraja kutuita kidato cha saba.

Mheshimiwa Spika, watumishi wa darasa la saba ambao waliondolewa kazini walifanya kazi zao kwa uaminifu, wengine walikuwa watendaji na watu wengine; lakini tamko hili lilitoka na waraka ukatoka mpaka leo asilimia 95 hawajawahi kulipwa wala kuitwa wala kupokelewa tu na waajiri. Sasa ningemwomba Mheshimiwa Waziri kama anaweza kutoa commitment angalau akatupa kopi ya zile nyaraka sisi Waheshimiwa Wabunge ili tuweze kwenda kutetea wale waliondolewa na hawajapata stahiki zao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Musukuma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, watumishi ambao hawakujiendeleza mpaka kufika Desemba, 2020 walikuwa kama 1,491, ambao hawakujiendeleza, na hivyo walikosa sifa ya kurejeshwa katika utumishi wa Umma.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema awali wakati najibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Londo, kwamba Mheshimiwa Rais wetu, mama yetu Samia Suluhu Hassan alitoa agizo lake siku ya Mei Mosi pale Mwanza. Kwamba hawa 1491 stahiki zao zilipwe; na tayari ofisi yetu ya Utumishi ilishatoa waraka tarehe 21 Mei, 2021 kwa waajiri wote kuanza kuhakiki madeni haya na kuangalia stahiki walizotakiwa kulipwa hawa wa darasa la saba. Naamini baada ya muda mfupi hawa 1491 wataanza kulipwa, kwa sababu ilikuwa ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais na hivyo tutalitekeleza kama aliyoelekeza yeye Mheshiwa Rais. Ahsante sana.
MHE. JANEJELLY J. NTANTE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali na juhudi ambazo zimekuwa zikifanywa kwa sasa hivi na Menejimenti ya Utumishi wa Umma kuboresha maisha ya watumishi lakini bado nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, hivi Serikali haioni kumshusha mtumishi mshahara ni mojawapo ya adhabu apewazo anapokuwa na utovu wa nidhamu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni lini sasa Serikali mtatoa tamko la kwamba hawa watumishi wanaofanyiwa recategorization mishahara yao ikiwa chini ya vyeo vile wanavyoenda kuanzia watabaki na mishahara yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nianze kusema siyo adhabu kumshusha mshahara mtumishi ambaye ametaka kubadilishiwa kada yaani recategorization kwa job satisfaction kwa sababu bila kufanya hivyo utakuta mwalimu tayari alikuwa ameshapanda daraja juu na sasa ameomba kuwa Afisa Sheria, natolea mfano, ni lazima aende kuwa Afisa Sheria Daraja la II, entry point ili kutengeneza seniority katika eneo la kazi. Bila ya kufanya hivyo, tunaweza tukawa tunawabadili kada watumishi anakwenda katika idara husika anakuta tayari kuna watumishi wengine waliotumikia kada hiyo miaka mingi yeye akaenda kuwa senior zaidi yao kwa sababu tu alishatumikia cheo kingine na kada nyingine. Kwa hiyo, kwa ajili ya kulinda hiyo seniority ni lazima aende katika entry point ya kazi ile aliyoiomba.

Mheshimiwa Spika, lakini akiwa ametumikia cheo kikubwa zaidi kwingine atahamia kule na mshahara binafsi ataombewa na mwajiri. Akiombewa mshahara binafsi atabaki nao kama nilivyosema katika jibu langu la msingi kwamba baada ya kufikia cheo sasa tuchukulie Afisa Sheria labda kafika kuwa Principal basi atalipwa mshahara ule wa Principal na ataacha mshahara wake wa mwanzo.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la pili, utumishi wa umma unaongozwa kwa sheria, taratibu na kanuni na miongozo mbalimbali inayotolewa. Kwa wale wote ambao wanastahili kufanyiwa recategorization ni wajibu wa waajiri kwanza kutenga bajeti kwa ajili ya kufanya recategorization. Mbili, ni wajibu wa mwajiri kumfanyia recategorization huyo mtumishi na kumwacha na mshahara binafsi endapo kada yake ni ileile ambayo amejiendeleza nayo. Hili si ombi ni kwa mujibu wa sheria, taratibu na miongozo ya utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Mbunge kama kuna mifano maeneo mengine Waziri wangu pamoja na mimi mwenyewe tuko tayari kwenda kuweza kuwashughulikia hawa Maafisa Utumishi na waajiri ambao hawatekelezi sheria.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nihitimishe kwa kusema hivyo, nashukuru sana. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali ambayo yanaonesha mwanga wa kupambana na rushwa katika michezo, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, je, ni hatua gani zimechukuliwa kwa watu ambao wamebainika kujihusisha na vitendo vya rushwa katika michezo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, ni mkakati gani Serikali itatumia kuboresha mifumo ya uuzaji tiketi na kukusanya mapato, lakini pia kuziba mianya ili kuongeza mapato zaidi katika sekta hii ya michezo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, Serikali imechukua hatua mbalimbali katika kuhakikisha kudhibiti mianya ya rushwa katika soka nchini, lakini vilevile imekuwa ikichukulia hatua watuhumiwa waliokutwa na hatia katika kujishughulisha na masuala ya rushwa. Ikumbukwe kwamba mwaka 2017 kuna watuhumiwa ambao walifikishwa mahakamani na kukutwa na hatia na hatimaye kulipishwa faini.

Mheshimiwa Spika, vilevile, mwaka 2018 kuna kesi moja ambayo ilikuwa ni maarufu sana hapa nchini, ambapo kuna mtuhumiwa alikutwa na hatia ya kula shilingi milioni 90 za Chama cha Mpira wa Miguu nchini TFF na yeye vilevile, alifunguliwa mashitaka ikiwemo ya uhujumu uchumi, lakini na baadaye kuweza kulipa fedha hizo kuzirudisha katika TFF. Kwa hiyo, tutaendelea kushughulika na watuhumiwa wa aina hii.

Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la pili la Mheshimiwa Shangazi, ili kuziba mianya sote tunafahamu kwamba sasa tunaenda kwenye ulimwengu wa teknolojia, hivyo basi, niwaase wenzetu wa TFF na timu za mipira za miguu kwamba sasa waende katika kuachana na tiketi zile za vitini vya kuchana na waweze kwenda kwenye electronic ticket, hii itasaidia sana upungufu na upotevu wa mapato, itaongeza mapato kwa timu zao, lakini vilevile kwa TFF.

Mheshimiwa Spika, vilevile niwaagize kwasababu e-government (eGA) ipo chini ya Ofisi yetu niwaagize hapa mbele ya Bunge lako Tukufu washirikiane na wenzetu wa TFF ili kuweka mfumo bora wa kukata tiketi za kuingia katika michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema katika hii trend tulioiona mwaka 2019 ya mwezi Januari kupata shilingi milioni 122 na mwezi Machi, mechi zote hizi zilikuwa ni za timu ya mpira ya Simba; kwa hiyo, kumeonekana kukiwa na timu ya Simba inacheza uwanja unajaa sana, lakini bado mapato yanakuwa hafifu, ukilinganisha na timu nyingine ambayo ni kubwa Afrika Mashariki na Kati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza na hili linahusu rushwa. Weekend iliyopita timu ya Prisons ilicheza na mabigwa wa kihistoria Young Africans kule Katavi na katika mchezo ule baada ya kumalizika na mabigwa hawa kupata ushindi kiongozi wa Prisons alisimama na kusema kwamba na amenukuliwa katika vyombo vya habari kwamba timu yake ilikua iko katika kuhongwa shilingi milioni 40 ili iweze kuachia mchezo ule.

Je, Serikali haioni sasa kwamba taarifa kama hizi ndizo za kuanzia kufanya kazi na kuwahoji watu kama hawa ili tuweze kupata ukweli? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, kumekuwa na tabia ya viongozi wa timu mbalimbali hapa nchini hasa wanapofungwa na Young Africans kwa halali kabisa, kutoa kauli za kwamba waliogwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ifike wakati sasa viongozi wa timu hizi na timu hizi na Watanzania kwa ujumla kwamba wakubali kwamba Young Africans, Yanga moja ndiyo timu bigwa hapa Tanzania na tibu bora hapa Afrika, kwa hiyo, wanapofungwa wakubaliane na matokeo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri Deo Ndejembi kwa kujibu maswali vizuri, hongera sana.

Mheshimiwa Spika, pamoja na Waheshimiwa Wabunge, ningependa kuwahakikishia kwamba Serikali kupitia Wizara ya Michezo ninayoiongoza tunapambana na rushwa kwenye michezo kwa nguvu zote na tunashirikiana na vyombo vya Ulinzi na Usalaam kuhakikisha tunaweka mazingira wezeshi ya michezo nchini kukua bila kuwepo na mazingira ya rushwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ningependa kuwapa uhakika Waheshimiwa Wabunge pamoja na Watanzania kwamba Serikali hii haitafumbia macho timu au mshirika yoyote katika michezo ambaye anatumia rushwa ili kuweza kujipatia ushindi ahsante sana. (Makofi)
MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa utekelezaji wa TASAF III, Awamu ya Kwanza wapo wafaidika 1,000 na zaidi wanaotoka katika Shehia 78 za Pemba ambao walikuwa katika utaratibu wa malipo na majina yao yaliachwa. Je, Serikali inasema nini kuhusu kulipwa fedha zao wafaidika hawa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa wananchi hawa maskini waliingia katika mikopo mbalimbali kwa kutegemea kwamba fedha wanazoendelea kuzipata zinawasaidia katika kujikimu kimaisha. Je, Serikali inaweza kututhibitishia kwamba ni bajeti ipi itawalipa fedha hizi kwa sababu mradi wa TASAF III, Awamu ya Kwanza umeisha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Maida, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mwaka jana mwezi Juni ulifanyika uhakiki wa kaya zote ambazo zinapokea fedha za TASAF. Kaya zile ambazo hazikutokea kwenye uhakiki ziliondolewa kwenye mpango mpaka pale watakapokuja tena kuhakikiwa ili malipo yao yaweze kuendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa kesi hii ya Pemba kwenye Shehia 78 kuna walengwa 1,200 ambao hawakujitokeza kwa ajili ya kufanyiwa uhakiki na malipo yao yalisitishwa. Hata hivyo, ilipofika uhakiki wa awamu ya pili uliofanyika mwezi Desemba, 2020 walengwa 300 walijitokeza na walengwa 900 bado hawajajitokeza kufanyiwa uhakiki.

Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pale tu walengwa hawa watakapojitokeza kufanyiwa uhakiki basi malipo yao yatarejeshwa na wataendelea kupokea fedha hizi za TASAF.

Mheshimiwa Spika, swali lake la nyongeza la pili ameuliza ni nini Serikali inafanya, kama nilivyojibu kwenye swali lake la nyongeza la kwanza ni pale tu hawa 900 watajitokeza kufanywa uhakiki basi malipo yao yatarejeshwa na wataendelea kuwepo kwenye mpango.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Swali la kwanza; kwa kuwa majibu ya Serikali yanathibitisha kuwepo kwa watumishi 332 kukaimu wakiwa na sifa lakini zaidi ya watumishi 1,164 wanakaimu bila sifa yaani hawana kibali cha Katibu Mkuu Utumishi. Sasa na ni ukweli kuwepo kwa viongozi wengi wanaokaimu kunazorotesha utendaji kazi na hivyo kutofikia malengo tarajiwa. Je, ni ipi sasa commitment ya Serikali kuwathibitisha au kuwaondoa watumishi wenye kukaimu zaidi ya miezi sita? (Makofi)

Swali la pili; kwa kuwa mchakato wa uteuzi unachukua muda mrefu sana hata zaidi ya miaka kumi na mfano upo, Katibu Tawala Msaidizi upande wa uchumi na uzalishaji Mkoa wa Kilimanjaro Ofisi ya Mkuu wa Mkoa anakaimu mwaka wa tisa toka 2012. Je, Serikali ipo tayari kutengeneza kanzidata au database ya wale watumishi waliofanyiwa vetting wengi kwa ujumla wao ili waweze kusaidia kupunguza muda ule wa watumishi kukaimu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Issa Mtemvu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali lake la kwanza tumekuta kuna changamoto kubwa sana ya waajiri kukaimisha watu wasiokuwa na sifa bila ya kupata kibali kutoka kwa Katibu Mkuu Utumishi kama mwongozo unavyotaka, matokeo yake mtu anakaa kwenye nafasi muda mrefu anakuwa hafanyiwi upekuzi na hivyo kufanya mtu kukaa kwenye nafasi hiyo kwa miaka mingi. Sasa tayari tulishawaagiza waajiri wote mapema mwaka huu kuleta majina yote ya watu wanaokamimu nafasi zao kwa zaidi ya miaka mitatu ili tuweze kupitia na kuangalia ni wapi wenye sifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, ni kwamba tayari tumegundua kuna watumishi 1,164 wasiokuwa na sifa na tunazidi kuwaomba waajiri waweze kuhakikisha wanakaimisha watu wenye sifa lakini vilevile kwa kibali cha Katibu Mkuu Utumishi. Waache kukaimisha kwa sababu anamtaka fulani au fulani mimi naweza nikafanya nae kazi na kumburuza, bali wakaimishe mtu kwa sababu ndie anayetakiwa kuwepo kwenye nafasi hiyo na hiyo itasaidia sana katika upekuzi na kuweza kuwathibitisha watumishi ndani ya miezi sita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali lake la pili la nyongeza Mheshimiwa ameuliza kama tuna kanzidata, sasa tayari tumeshaanza kukusanya taarifa na tumeshapeleka majina zaidi ya 2,300 kwa ajili ya upekuzi ili yawepo na wiki hii tunapeleka tena majina 2,400 kwa ajili ya upekuzi ili tuweze kuwa tuna watu katika kanzidata yetu wenye sifa. Tunapoona mwajiri amekuweka mtu asiye na sifa, Utumishi tutam-post moja kwa moja mwenye sifa ili akashike nafasi hiyo na aweze kuifanya kwa weledi na kuweza kufanya maamuzi. Nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Wabunge na watumishi wote wale wenye sifa muda si mrefu mtaanza kuwaona na tatizo hili la kukaimu litaondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa kuwa tatizo hili limekuwa kubwa na kwa miaka sasa linazungumzwa na hoja ni hizi hizi na majibu ni haya haya, Serikali haioni umefika wakati wa kutunga sheria iwe ni kosa kumkaimisha mtu kwa muda mrefu. Kwamba tutunge sheria ifikie ukomo kwamba mwisho wa kukaimu ni hapa na baada ya hapa mtu akipitiliza tuchukue hatua ili tuondokane na hili mtu anakaimu miaka Tisa na hakuna mtu anachukuliwa hatua. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nape Moses Nnauye kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyokwishasema awali tatizo hili tunalifahamu na tayari tukishakuwa na kanzidata ya watu wenye sifa hii changamoto inaenda kuisha kwa sababu tutaanza ku-post moja kwa moja watu kwenye nafasi hizi zilizo wazi. Commitment yetu ni kwamba tutaendelea kulifanyia kazi na kuhakikisha kwamba nafasi zote zinazokaimiwa zinakuwa na watu wenye sifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilihakikishie Bunge lako kwamba muda si mrefu tutakuwa tayari tuna watu wenye sifa kwenye nafasi zao. Vilevile, nichukue fursa hii kuwaasa na kuwaagiza watumishi wote nchi nzima kuhakikisha ifikapo mwisho wa mwezi huu, walete majina yote ya watu ambao wanakaimu nafasi zao bila kibali cha Katibu Mkuu Utumishi. Vilevile, ifikapo tarehe 30 ya mwezi huu, walete majina ya wote wanaokaimu kwa vibali vya Katibu Mkuu Utumishi ili tuweze kuwafanyia upekuzi na kama wao wanafaa kuwa kwenye nafasi hizo, basi tuwaache hapohapo kwenye nafasi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nitumie nafasi hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuliangalia suala hili kwa kipekee na kulipa uzito na kuwapa matumaini wafanyakazi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nafahamu ya kwamba taasisi nyingi za Serikali zimekuwa na utaratibu wa kuchukua wafanyakazi kwa muda, kwa maana ya vibarua na wengine wanakuwepo kwa mikataba ya muda mfupi. Inapotokea suala la ajira, mara nyingi sana watu hawa wamekuwa wanasahaulika na kuchukuliwa watu kutoka nje. Kwa mtindo ule ule wa Serikali kuamua kuboresha maslahi ya wafanyakazi, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha vibarua na wale ambao wana ajira za muda, zinapopatikana fursa wanaajiriwa kwanza wao kama kipaumbele na wengine ndio wanafuata?

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Stanslaus Shing’oma Mabula, Mbunge wa Nyamagana, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sera ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma ambayo ilipitishwa mwaka 2008 inaeleza wazi namna ya kupata Watumishi wa Umma kwa njia ya ushindani. Sasa nafahamu kuna maeneo mengi hata majimboni kwa Wabunge wengi kuna watu wengi wanajitolea katika taasisi za Umma.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI Mheshimiwa Ummy Mwalimu alieleza mbele ya Bunge lako hili kwamba kuna database ambayo inaanzishwa kukusanya majina ya wale wote ambao wanajitolea maeneo mbalimbali nchini ambapo watapewa kipaumbele pale ambapo ajira zitajitokeza. Sasa nitumie nafasi hii kutoa wito kwa wote wale ambao wanajitolea kuwasilisha majina yao Ofisi ya Rais, TAMISEMI kama ambavyo alikuwa ametoa maelekezo Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, kwa wale ambao hawapo katika ajira za Serikali za Mitaa, wao pia waorodheshe majina yao na kuyafikisha Ofisi ya Rais, Utumishi ili tuweze kuwa na database ya pamoja na pale ajira zinapotoka, basi tutaangalia. Kwa sababu kumekuwa kuna scenario ambazo watu wanajitolea pale tu wanaposikia ajira zinatoka ili waweze kupata favour ya kuweza kuingia kazini. Ili kudhibiti hilo na kuhakikisha ushindani upo katika kuajiri watu katika Utumishi wa Umma, ndiyo maana ajira zile zinatangazwa.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo hao wanaojitolea, naamini watakuwa na added advantage kwa sababu wameshaifanya ile kazi kwa vitendo na hivyo wanapoenda kwenye usaili watakuwa wako vizuri zaidi katika kuweza kupata ajira hiyo.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza naipongeza Serikali kwa nia hiyo njema ya kutamani kuboresha stahiki za watumishi, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa sasa tathmini imeshafanyika tangu mwaka 2015/2017 ya kufanya marekebisho ya muundo na mishahara ya watumishi: Je, ni lini sasa Serikali itatekeleza jambo hili?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kumekuwa na ucheleweshaji mkubwa sana wa mafao ya watumishi wanapostahili: Ni nini kauli thabiti ya Serikali kuwahakikishia watumishi wanapostahili watapata stahiki zao/mafao yao kwa wakati? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe Mbunge wa Hai kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nitoe pongezi zangu kwa Mbunge wa Hai, Mheshimiwa Saashisha kwa kuwa anafuatilia sana masuala ya kiutumishi hasa yale ya watumishi katika jimbo lake na yale ambayo yanahusu wastaafu wanaotoka katika Wilaya ile ya Hai na jimboni kwake.

Mheshimiwa Spika, sasa nikienda kwenye kujibu swali lake la kwanza, Serikali tayari ilishaanza mpango wa kuweza kufanyia kazi ile tathmini iliyofanyika 2015/2017. Tayari kuna kada ambazo zilishafanyiwa kazi ambapo kwa zoezi lililofanyika mwaka 2015, kada ya Wahasibu, Internal Auditors na hawa washika fedha; kada hizo zilikuwa zinatofautiana sana katika ngazi ya mshahara, lakini ukiangalia elimu wanayosoma, ilikuwa ni moja. Kwa hiyo, tayari Serikali imeanza kufanyia mpango huo.

Mheshimiwa Spika, vile vile mwaka 2017 ilifanyika tathmini ya Watumishi wa Umma wote, kuangalia ulinganifu ikiwemo kwenye ma-engneer ukiangalia katika wanasheria na kadhalika. Sasa katika utekelezaji kama unavyofahamu Serikali itatekeleza pale tu kwa uwezo wa kibajeti katika kulipa mishahara. Kama tunavyoona jitihada zinazofanyika na Serikali za kuboresha uchumi wetu chini wa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, uchumi wetu ukiboreka, basi tutafanyia kazi na kuboresha maslahi ya watumishi wetu.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, Watumishi wa Umma inatakiwa inapofika mienzi sita kabla ya kustaafu, tayari waanze na kujiandaa na nyaraka mbalimbali. Sasa changamoto imekuwa ikijitokeza unakuta mtu ajira yake ya kwanza alianzia Halmashauri ya Kongwa, lakini anapokuja kustaafu, anastaafia Ukerewe, tatizo linakuwa kwenye documentation. Halafu mtu anakuja kukumbushwa suala hili la Maafisa Utumishi limebaki mwezi mmoja, anapoanza kufuatilia barua yake ya ajira, iko Kongwa. Sijui alipata uhamisho kwenda Songea; akatoka akaenda kustaafia Ukerewe.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utakuta changamoto kwenye documentation na mtu huyu hana nauli, ndiyo maana mafao yanachelewa, lakini tayari tumeanzisha mfumo wa HCMIS ambao utahakikisha taarifa zote za mtumishi zipo na zinaanza kutoa notification walau miezi sita kabla.

Mheshimiwa Spika, wakati Serikali tunafanyia kazi mfumo huu, nawaasa Maafisa Utumishi wote nchi nzima kuhakikisha wanaangalia records za watumishi wao wanaokaribia kustaafu wawape taarifa walau mienzi sita kabla, ili isije ikafika nauli imekwisha, anakaribia kustaafu kesho, ndiyo anakumbushwa aanze kutafuta taarifa zake. (Makofi)
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nilikuwa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza je, Serikali iko tayari sasa kuweka utaratibu wa muda maalum kwa ajili ya kuhakikisha kwamba hizo moving expenses zinalipwa ili kuondoa usumbufu kwa watumishi wa umma?

Lakini swali langu la pili je, ni lini sasa Serikali pia itafanya marekebisho kwa yale madaraja ya watumishi wa umma yaliyofutwa mwaka 2016 na 2017. Hasa katika Manispaa yangu ya Iringa wapo watumishi zaidi ya 300 ambao hawajafanyiwa marekebisho pamoja na kazi nzuri ambayo imefanywa na Serikali ya kupandisha madaraja. Ni lini itafanya kazi hiyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, na pia tumeshaleta sana hili ombi mara nyingi sana kwa Waziri lakini halijafanyiwa kazi, tunaomba commitment ya Serikali? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Msambatavangu, Mbunge wa Iringa Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la kwanza kama nilivyosema kwenye majibu ya msingi. Waajiri wote wanatakiwa kuhakikisha wanatekeleza matakwa ya Kanuni za Kudumu za Kudumu za Utumishi wa Umma na tayari Kanuni hizo zipo kwamba ni Mtumishi yoyote anapokoma utumishi wake wa umma au mtumishi pale anapohama anastahili kulipwa moving expenses.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nitumie fursa hii kuwataka tena Waajiri kuhakikisha wanatenga bajeti ya moving expenses kwa sababu wanajulikana wale watumishi ambao wanakaribia kustaafu. Sasa ni wajibu wa mwajiri kuangalia wale wanaokaribia kustaafu mwaka unaofuata wa fedha na kuweza kutenga bajeti hiyo. Kwa hiyo, nirudie tena kuwataka Waajiri wote si tu wa local government, si tu wa Iringa Mjini, lakini taasisi zote za umma kuhakikisha wanatenga bajeti kwa ajili ya watumishi wao katika hii moving expenses.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye swali lake la pili, la madaraja ya 2006. Madaraja haya yalisimama kuanzia Mei, 2016 lakini madaraja haya yalianza tena kutolewa mwezi Novemba, 2017 ambapo Serikali ilipandisha jumla ya watumishi 55,000 Novemba, 2017. Hii ya kutoka 2016 madaraja haya yalikoma kupisha uhakiki uliokuwa ukiendelea, lakini sasa tunaangalia ni namna gani bora ya kuweza kuleta msawazo ili kulindi ile Seniority katika eneo la kazi na Serikali bado inalifanyia kazi suala hili na litakapokuwa tayari tutatolea maelezo zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na shukrani kwa majibu hayo yenye matumaini, na ninaamini kwamba nitaweza kupatiwa orodha ya hao walioajiriwa na maeneo waliyoajiriwa, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kufahamu, hiyo kanzidata inafanya vipi kazi yake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa ameeleza kwamba wanaajiriwa kwa kufuata usawa kwa watu wote, lakini mtu mwenye changamoto ni tofauti na mtu mzima. Kwa nini Serikali sasa isifikirie kuweka utaratibu maalum unaolihusu kundi hili ili lisipate tatizo kama ambavyo tunasikia kuna matatizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Engineer Stella Martin Manyanya, Mbunge wa Nyasa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza ameuliza kama kanzidata ipo. Nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge ambaye amekuwa mstari wa mbele vilevile kulifuatilia hili suala, kwamba kanzidata hiyo ipo na inaratibiwa chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Na katika kuratibu huko Ofisi ya Waziri Mkuu imekuwa ikitoa elimu mbalimbali kwa watu wenye ulemavu kupitia vyama vya watu wenye ulemavu, kupitia taasisi za elimu ili kuwaonesha kwamba kanzidata hiyo ipo na taarifa zao zinachukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili, kwamba kwa nini kusiwe na utaratibu maalum; utaratibu maalum upo. Kwa mujibu wa Sera ya Menejimenti ya Ajira katika Utumishi wa Umma, kifungu Na. 5(1)(1) na kifungu Na. 5(1)(2) kimeeleza wazi hii sheria ya mwaka 2008, imeeleza wazi namna ya kuweza kupata ile asilimia tatu ya watu wenye ulemavu katika utumishi wa Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, nirejee tena kutoa rai yangu kwa watu wenye ulemavu na kwa waajiri wote, kwamba watu wenye ulemavu kwanza waombe hizi nafasi zinapotangazwa. Kwa sababu kwa mujibu wa sheria asilimia ile tatu ipo lakini ni lazima wafikie sifa na vigezo vya kuajiriwa katika utumishi wa Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namba mbili, vilevile ni waajiri wenyewe kuwapa kipaumbele hawa watu wenye ulemavu kwa kuhakikisha wakati wa interviews hizi kuwe kuna mazingira rafiki ya kuweza kuhakikisha wanahudhuria interviews hizi, wanafanya mitihani hii ambayo inawekwa ili kuweza kupata ujumuishaji zaidi wa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, ninaomba kuuliza swali dogo la nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tamko ambalo limetolewa na Waziri wa TAMISEMI kuomba kibali cha ajira za watumishi 7,000 walimu. Na kwenye nchi hii tuna walimu wengi wanaojitolea kufanya kazi bila kulipwa. Kule Makete nina watumishi karibia 100 ambao ni walimu wanaojitolea; je, ni upi mpango wa Serikali kuwapa kipaumbele walimu hawa au wafanyakazi hawa ambao wameonesha moyo wa utayari na uzalendo wa kufanya kazi bila malipo na wanakwenda kuomba ajira? Naomba majibu ya Serikali. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Richard Tuntemeke Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Bungeni Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, alishatoa kauli ya kuwaagiza waajiri wote kwa maana ya wakurugenzi wa halmashauri mbalimbali nchini, kuhakikisha wanafikisha majina ya watu wote wanaojitolea katika sekta ya afya na katika sekta ya elimu ili iwekwe katika kanzidata yao katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili waangalie utaratibu bora wa kuweza kuwaingiza katika utumishi wa Umma pale ajira zinapotolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nirudie kauli ile tena ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ya kuwataka wakurugenzi wa halmashauri zote kuhakikisha majina ya wanaojitolea walimu shule za msingi na sekondari, wale wauguzi na katika sekta ya afya kwa ujumla wawasilishe majina hayo Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili utaratibu huo maalum unaoangaliwa uweze kufanyika kwa haraka wakati majina hayo yapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nitoe angalizo; katika kuleta majina hayo watende haki. Walete majina ya wale ambao wamejitolea kwa muda mrefu, wasilete majina ya watu ambao huenda amesikia kauli hii anakwenda kujitolea kesho na anataka jina lake na yeye liweze kuingizwa. Waangaliwe wale waliojitoa kwa muda mrefu na tutashirikiana na wenzetu wa TAMISEMI kuona namna bora ya kuweza kuwaingiza katika utumishi wa Umma. (Makofi)
MHE. OMAR ISSA KOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri sana, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni nimeona baadhi ya wananchi wakifutwa kwenye mpango wakati bado hali zao ni mbaya sana, na naomba nimtaje mwananchi ambaye ni mfano, anaitwa Ndugu Hamad Faki Hamad maarufu Fofofo kutoka Shehia ya Mjini Wingwi, hali yake ni mbaya sana lakini amefutwa.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri anatoa kauli gani kwa TASAF dhidi ya hali kama hizi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, Serikali inatoa kauli gani dhidi ya taarifa ambazo zinasambaa kwa wananchi ambazo zinaleta wasiwasi kwamba wanakwenda kufutwa kwenye mpango wakati hali zao bado ni mbaya. Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya taarifa hizi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kombo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kumpongeza yeye mwenyewe Mheshimiwa Kombo, Mbunge wa Wingwi, kwa sababu pia ni mjumbe wa Kamati ya USEMI ambayo inasimamia Wizara yetu hii Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora na amekuwa akifuatilia sana masuala haya ya TASAF hasa jimboni kwake kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nikienda kwenye maswali yake anauliza ni vigezo gani ambavyo hata huyu amemtaja Mzee Hamad Faki vimemuacha. Sijui hasa kwenye kesi hiyo kama individual na nitakaa naye Mheshimiwa Mbunge ili tuweze kujua kwa nini Mzee Faki alitoka katika mpango wa TASAF, tukitoka hapa nitakutana naye ili tuweze kulijua.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda niseme jambo moja katika mradi huu awamu hii ya pili imekuwa ina component mbili; component ya kwanza ni ile ambayo tulikuwa tumeizoea kwenye awamu ya kwanza ya mradi huu wa TASAF, ni ule wa cash kwenda kwenye kaya hizi, lakini component ya pili ni public works. Kwamba kaya huenda ina watu watano, na mkuu wa kaya anaweza akawa ni mtu mzima labda ana miaka 70 lakini ndani ya kaya ile kuna watu wenye uwezo wa kufanya kazi. Basi watafanya kazi na kulipwa ujira kutoka kwenye mradi wa TASAF, kwenye miradi ile ambayo wameibua wao wenyewe katika maeneo yao husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, ya taarifa hizi kwamba wanufaika wanaenda kufutwa. Niseme taarifa hizi si za kweli, walengwa hawa hawaendi kufutwa, na tulifanya uhakiki kabla ya kuingia kwenye awamu ya pili ya mpango huu na kaya zimeongezwa. Serikali hii ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa maelekezo yake mwenyewe alielekeza tuongeze idadi ya kaya kwenye mpango huu wa TASAF, na kaya zimeongezwa na hauendi kufutwa.
MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri, na nimpongeze sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu wa kulipa kipaumbele suala la jinsia katika ajira katika kipindi chake.

Mheshimiwa Spika, swali langu ni kwamba, kwa mujibu wa Ibara ya 22 na 23 ya katibu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haki ya usawa wa ajira na ujira ni ya raia wote wa nchi yetu kwa shughuli yoyote inayosimamiwa na mamlaka yetu ya nchi.

Sasa, je, Mheshimiwa Waziri kwa nini hamuoni jambo la busara kwenda kumshauri Mheshimiwa Rais ili sasa Serikali ije ilete sheria ili hizo kanuni zenu na miongozo iingie humo iwe sheria, ili yoyote yule ambaye atakiuka sheria hiyo aweze kuadhibiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA. Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Najma Murtaza Giga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, wote humu ni mashahidi, Mheshimiwa Rais wetu wa awamu ya sita Mama yetu Samia Suluhu Hassan ameonesha nia ya dhati ya kuweza kuleta uwiano sawa katika nafasi za uteuzi. Lakini vilevile sisi kama Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, kama nilivyosema awali kwenye majibu yangu ya msingi, tumeanza kuweka miongozo, tunaandaa namna ya kuweza kupata usawa katika utumishi wa umma.

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano, miongozo ya Sekretarieti ya Ajira inasema wazi pale endapo candidate wawili watagongana maksi na mmoja ni mwanamke, basi atachuliwa yule mwanamke katika kuingia katika ajira ya Utumishi wa Umma. Miongozo hii ipo na tutaendelea kuisimamia na kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, lakini niwatoe mashaka, Mheshimiwa Rais ameweza kutafuta fedha kutoka European Union, Serikali ya Finland na Serikali yetu ya Tanzania vilevile imewekeza fedha katika Chuo kile cha Uongozi Institute; ambapo sasa tunaenda kutoa mafunzo ya uongozi kwa wanawake zaidi ya 500. Na hivi ninavyozungumza tayari kuna wanawake 50 ambao wapo katika mafunzo ya uongozi kwenye Taasisi yetu ya Uongozi Institute. Watakapo maliza wao wanakuja tena wanawake mia 100 katika mwaka huu wa fedha kwa ajili ya kuweza kupata mafunzo ya uongozi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Serikali ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan imejipanga vyema katika kuhakikisha wanawake wanapata fursa sawa katika uteuzi na ajira nchini. Naomba kuwasilisha.
MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza naomba kabla sijauliza maswali yangu mawili ya nyongeza, niruhusu nitoe shukrani zangu za dhati sana kwa ofisi ya Rais kupitia TASAF kwa mradi mkubwa ambao wamenipelekea katika shule yangu ya Peak, kukarabati na ujenzi wa uzio shule ambayo Baba wa Mheshimiwa wetu Mzee Suluhu Hassan alifundisha, hivyo wamepeleka fedha nyingi pale nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza niliuliza Wabunge wanashirikishwaje? Nashukuru kwa majibu. Je, Serikali haioni sasa ni wakati baada ya miradi ile ambayo imeibuliwa na wananchi Wabunge nao wakapata taarifa ili kuwa karibu na ile miradi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa mradi mkubwa huu uliopelekwa katika skuli ya Peak Jimbo langu la Mtambwe kukarabati madarasa na uzio kuna baadhi ya maeneo bado hayajakamilika. Je, Serikali haioni ni wakati mzuri sasa hivi wa kuweza kupeleka fedha pale ili kukamilisha baadhi ya maeneo ambayo hayajakamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Khalifa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu Je, sasa Serikali haioni umuhimu wa kuwapa taarifa Waheshimiwa Wabunge, naomba nitumie nafasi hii mbele ya Bunge lako hili kuelekeza ma-TMO wote ambao ni wasimamizi wa miradi hii ya TASAF katika Wilaya husika kuwa wanawapa taarifa Waheshimiwa Wabunge kwa miradi yote ambayo wananchi wameibua kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa tunafahamu Wabunge ndio wawakilishi wa wale wananchi wa yale maeneo husika hivyo ni muhimu sana kuweza kuwapa taarifa, nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge, kwamba miradi mingine itakayoanza kuibuliwa ndani ya Majimbo husika basi Wabunge wataanza kupewa taarifa ile.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, kuhusu mradi wa Peak, bahati nzuri nimefika mpaka pale, hatua ya kwanza iliyoanza kwenye shule ile ilikuwa ni kujenga madarasa ambayo yalikuwa yamechakaa sana. Baada ya kumaliza ujenzi ule wa madarasa yale, wananchi wale wa eneo lile pia waliibua mradi mwingine ambao ni hitaji lao lilikuwa ni uzio katika shule ile. Kwa sababu ilikuwa ni njia ya wakazi wa pale kukatiza katikati ya skuli ile katika eneo la Peak. Baada ya kutambua hilo fedha ikatolewa na mradi wa TASAF baada ya kuibuliwa mradi na baada ya hapo ni uzio ule umejengwa.

Mheshimiwa Spika, kama kuna hitaji jingine wananchi wanaweza wakaibua na TASAF watafanyia kazi. (Makofi)
MHE. MWANTUMU DAU HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nimpongeze Waziri kwa majibu yake mazuri ambayo yanatia moyo na vile vile niwapongeze Mawaziri wangu hawa wa Utumishi kwa jinsi wanavyofanya kazi, wanafanya kazi sana katika hasa masuala haya ya TASAF wanafanya kazi kutoka hapa Tanzania Bara mpaka Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, nina swali moja tu la nyongeza, pamoja na jitihada hizo Serikali inasema nini katika kuhakikisha wanaofikiwa ni walengwa zaidi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumeboresha kwanza mifumo ya namna ya kuweza kuwapata walengwa na tumeenda kidigitali zaidi, wale waandikishaji wanatumia teknolojia, kwa kutumia tablets (vishikwambi), kuwaingiza walengwa katika mfumo wa TASAF.

Mheshimiwa Spika, vile vile kuna mfumo mwingine ambao umeongezwa wa malalamiko kwa wale ambao wanaona huenda walistahili kuwemo kwenye mpango wa TASAF, lakini waliachwa, basi kuna mfumo wa malalamiko na yale malalamiko yao yakiwekwa huwa yanapitiwa na wataalam wa TASAF na kuweza kuwarejea kuwahakiki tena na kuona kama wanastahili.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba mfumo uliowekwa wa namna ya kuwapata walengwa wa kaya maskini huwa hauanzii juu kwenda chini, mfumo ule unaanzia chini kwenda juu kwa maana Serikali ya Kijiji na wananchi hukutana katika mikutano ya kijiji na wanaanza kwa kutambuana wao kwamba fulani ni kaya maskini fulani si kaya maskini. Kwa hiyo, mfumo ule umeanza toka kijijini kuja mpaka juu sasa tayari Serikali imechukua hatua hizo lakini tunazidi kusisitiza wale wanaoenda kuandikisha kule kwa kushirikiana na Watendaji wetu wa Vijiji na Kata kuwa wakweli na kuhakikisha haonewi mtu katika wale wanaostahili kuingia katika mpango wa TASAF, basi waingizwe katika mpango wa TASAF nao waweze kuwa katika walengwa ambao wananufaika na mradi huu.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Spika, kwenye mpango huu wa kunusuru kaya maskini kulikuwa na mapendekezo ya kutoa kipaumbele kwa watu wenye ulemavu wanaokidhi vigezo. Je, ni kwa kiasi gani mapendekezo hayo yamezingatiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kipaumbele kimewekwa hasa kwa watu wenye mahitaji maalum na kuangalia kwamba wanakidhi vigezo vile. Kwa sababu unakuta kuna watu wana hitaji maalum wenye ulemavu, lakini wanapopitiwa na dodoso lile wanagundulika kwamba vigezo vile vinavyotakiwa kuingia katika kaya ya walengwa hawajavifikia, lakini wengi ambao wamefikia huwa wanapewa kipaumbele na wanaingizwa katika mpango.

Mhshimiwa Spika, nimwongezee tu Mheshimiwa Mbunge, tunayo vile vile program ambayo inasaidia watu wenye ulemavu ili kuwa kwenye vikundi vya uzalishaji na wanapewa fedha kutoka Mfuko huu wa TASAF kuweza kuanzisha biashara zao, kwa hiyo tunatoa kipaumbele kwa watu wenye ulemavu.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru lengo la mfuko huu ni kusaidia kaya maskini lakini unakuta bado haileti tija kutokana na pesa ambazo wanatoa elfu 50, laki, mwisho tunawafanya wanakuwa tegemezi. Ni mkakati gani wa Serikali kuhakikisha unabadilisha huu mfumo na matokeo yake kwenda kuwapa mitaji ili wasiendelee tena kutegemea zile 50, 50 waweze kukidhi maisha yao moja kwa moja? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, tunatoa elimu kwa wale waratibu wetu kule chini na wao waweze kutoa elimu kwa walengwa ya namna bora ya kuweza kuzitumia fedha hizi wanazozipokea. Tukiangalia kwamba kaya hizi nyingi zilikuwa hazina uhakika wa kula yao, hazina uhakika wa milo mitatu.

Kwa hiyo kwa kuingia kwenye mpango huu kwa kupata kiwango cha fedha ambacho Mheshimiwa Bulaya amekitaja na wengine hupata zaidi, imeshawapa boost ya kutosha ya kuweza kuanza kufuga kuku, mbuzi ili kuweza kuboresha maisha yao na kuwa na uhakika wa kula kila siku.

Mheshimiwa Spika, vile vile tunawasisitiza sana wenzetu wa Serikali za Mitaa kwa maana Wakurugenzi kule kuhakikisha wanawaweka hawa walengwa katika mpango wa ile 4, 4, 2. Kwa sababu kwenye kaya hizi maskini wapo akinamama, kwenye kaya hizi maskini wapo walemavu, kwenye kaya hizi maskini wapo vijana. Kwa hiyo tunasisitiza sana kwamba hawa walengwa waliokuwepo kwenye kaya hizi kuweza kuingia katika 4:4:2 ili waweze kupata mkopo wa vikundi kuweza kuongeza kipato na kuweza kufanyabiashara mbalimbali.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa mpango huu kwa Wilaya ya Rorya kuna vijiji zaidi ya 20 na nimeshamtumia Mheshimiwa Waziri, ambavyo wengi wao wame-raise malalamiko ya kuachwa kwenye mpango wenyewe kipindi unatekelezwa. Nataka nijue nini mkakati wa Wizara kwenye vile vijiji ambavyo hasa watu wanalalamika kwamba waliachwa kipindi cha awali katika mpango wa utekelezaji wa TASAF. Nashukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, kama nilivyokuwa nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji, naomba nimjibu Mheshimiwa Chege kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, jibu ni hivyo hivyo kwamba kaya zote ambazo zilikuwa zimeachwa na zinastahili kuingia katika mpango, awamu hii ya pili zinaingizwa zote kwenye mpango huu. Vile vile vijiji vyote ambavyo vilikuwa vimesalia havikuingia kwenye mpango huu wa TASAF, sasa vinaenda kuingia katika mpango huu wa TASAF.

Mheshimiwa Spika, sasa huenda nione ni namna gani nitakutana na Mheshimiwa Chege ili tuweze kupanga, tuone tunasaidiaje hivi vijiji 20 ambavyo anavyo jimboni kwake, kuweza kuona tunakwenda kuziona ama tunawaelekeza wenzetu wa TASAF waweze kufika katika jimbo la Mheshimiwa na kuona tunawasaidiaje walengwa hawa.
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niulize swali moja dogo la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwepo na changamoto kubwa kwa watumishi wa umma hasa hawa ambao mashauri yao yanaendelea kusikilizwa kwamba yanachukua muda mrefu sana na hii inawanyima haki kama watumishi wa umma. Nini mkakati wa Serikali kuhakikisha haya mashauri yanakamilika kwa wakati? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Godwin Kunambi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyotoa maelezo kwenye majibu yangu ya msingi, mashauri ambayo yapo, ya watumishi wanaotakiwa kuchukuliwa hatua za kinidhamu ni watumishi 1,477; mashauri yaliyokuwa kwenye Tume ya Utumishi wa Umma ni mashauri 598; na kati ya rufaa hizi ambazo zimetajwa kule Tume ya Utumishi wa Umma, rufaa 411 zina vielelezo vilivyokamilika; na rufaa 187 hazina vielelezo, kwa hiyo, zimerudishwa kwa waajiri na mamlaka za nidhamu ili ziweze kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu kama nilivyoitoa awali, ni kwamba hawa ambao wanapeleka mashauri Tume ya Utumishi wa Umma hayana vielelezo, yaweze kuwa yamewasilishwa na vielelezo kamili ili haki ya watumishi ambao Mheshimiwa Kunambi ameizungumzia hapa, iweze kupatikana kwa haraka zaidi. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumwuliza Waziri swali la nyongeza kwamba kulikuwa na watumishi wa Darasa la Saba ambao wamesimamishwa na walikuwa wamefanya kazi kwa muda mrefu na baadaye hawakupewa kiinua mgongo wala chcohote: Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusu watumishi hawa ambao kwa kweli wametumikia pia Taifa kwa kipindi kirefu kwa ujuzi huo wa Darasa la Saba? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, watumishi wa darasa la saba walioajiriwa baada ya Mei, 2004 wale Serikali ilikwishatoa tamko na ilimradi wawe walikuwa hawakughushi nyaraka zao walipewa muda mpaka ifikapo Desemba, 2020 wawe wamejiendeleza na kuweza kuendelea na ajira zao na wale ambao hawakujiendeleza, tayari mamlaka ilishatoa tamko kwamba wale washughulikiwe walipwe michango yao ya hifadhi ya jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hadi kufikia Desemba, 2020 jumla ya watumishi 1,191 walikuwa hawakujiendeleza na hivyo wanastahili kulipwa michango yao ya hifadhi ya jamii.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza swali langu halijajibiwa. Naomba niulize maswali maeili kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuna mikataba mbalimbali ambayo tunaridhia katika nchi yetu, nini kilitokea mpaka tukajitoa katika OGP?

Mheshimiwa Naiibu Spika, swali langu la pili, kama alivyosema kwamba kuna vyombo mbalimbali ambavyo tunavitumia kama alivyoainisha. Sasa ni nini kinatufanya tusiridhie katika mikataba hiyo wakati sisi nchi yetu si kisiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Grace Tendega kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza, kwamba kwanini tulijitoa; tulikuwa tayari tupo na Mkataba wa Umoja wa Mataifa yaani UPRM, (Universal Periodical Review Mechanism) ambayo inafanyiwa review kila baada ya miaka minne, ambayo ni ya umoja wa mataifa. Wakati huo huo tulikuwa kwenye OGP ambayo ni CSO private sector.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu tayari nchi yetu ipo katika mikataba ya Umoja wa Mataifa kama vile UPRM. Nikienda kwenye swali lake la pili, why tusiridhie. Kama nilivyojibu kwenye swali la kwanza lakini kwenye majibu yangu ya msingi, tayari tuna mechanism zetu za ndani ya nchi, kama vile Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, tuna taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa. Tuna mechanism nyingi ambazo zinaangalia uwazi na utawala bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan imeweka wazi mbele taasisi zetu na mifumo yetu yote hii itafanya kazi kwa uwazi na uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza, nichukue nafasi hii kuipongeza sana Serikali kwa kuweka mazingira mazuri ya kuweza kuwavutia wawekezaji.

Je, nini mpango wa Serikali katika kuajiri watumishi wa kada ya mazingira katika miradi yote mikubwa ambayo inatekelezwa na Serikali?

Swali langu la pili; je, kwa kuwa nchi yetu kwa sasa inakabiliwa na changamoto ya tabia nchi, kwa mwaka huu wa fedha, Serikali imepanga ajira ngapi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Asia Halamga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda kutumia nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa amekuwa hodari sana kufuatilia masuala mbalimbali ya ajira za kada mbalimbali ambazo zinahusu mkoa wake na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la kwanza la je, Serikali ina mpango gani wa kuajiri watu kwenye miradi hii mikubwa; Niseme tu kwamba Serikali inaajiri kwa kuzingatia ukomo wa bajeti kama ambavyo inaidhinishwa na Bunge lako hili Tukufu. Kwa hiyo, tutaendelea kuzitenga kwenye bajeti na kuleta hapa Bungeni kuona namna gani nafsi hizi zitaongezwa Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili:Je, Serikali ilitenga jumla ya ajira ngapi? Kwa mwaka huu wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga jumla ya ajira 30,000 kwa kada zote na taasisi mbalimbali za Serikali nchini na hiyo pia kama nilivyojibu katika jibu langu la nyongeza la kwanza kwamba ni kutokana ukomo wa bajeti ambao tulipatiwa. Hata hivyo tutaendelea kutenga na kuona namna gani tunaweza kuangalia hizi kada zote zikapata watumishi wa kutosha.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri, kwenye jibu lako unasema ajira ambazo Serikali ilitoa vibali kwa mwaka wa fedha 2021/2022 ajira 223 utekelezaji bado unaendelea. Ni kwamba wale waombaji hakuna, au yaani mwaka ule uliopita kipindi kile mpaka sasa hivi bado mnaendelea au kuna changamoto kwenye sekretarieti ya ajira?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, Hapana, siyo kwamba kuna changamoto kwenye sekretarieti ya ajira, lakini hizi nafasi zote 223 zinatokana na taasisi mbalimbali za Serikali. Kwa hiyo, sekretarieti ya ajira inaanza mchakato pale tu zile taasisi zilizoidhinishiwa vibali vyao vya kuajiri zinapoanza mchakato wao kupeleka sekretarieti ya ajira. (Makofi)
MHE. RAMADHAN SULEIMAN RAMADHAN: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nina masuala mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; nje ya utoaji wa rasilimali fedha kwa kaya maskini je, ni mambo gani mengine Mpango huu wa TASAF unafanya kuzinufaisha kaya maskini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, mpango huu unategemea kuisha lini ili kaya maskini zinazonufaika zipate kujiandaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ramadhan Suleiman Ramadhan, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza, kwamba TASAF imefanya nini kingine cha ziada kwa walengwa? TASAF imefanya mambo mengi ikiwemo kuingia MOU na Bodi ya Mikopo Tanzania ili kuweza kutoa mkopo wa asilimia 100 kwa wale wote ambao wanakwenda kwenye elimu ya juu kutoka kwenye kaya hizi za walengwa wa TASAF. Vilevile TASAF imewawezesha walengwa hawa kuwa na bima ya afya. Bima ya afya hii inawawezesha wao kupata matibabu wakati wowote hata pale ambapo wanakuwa hawana pesa. Vile vile mradi huu umejenga miradi mbalimbali ya maendeleo kwenye madarasa, vituo vya afya na zahanati.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, mpango huu kwanza nilijulishe Bunge lako tukufu ulikuwa unaisha mwaka huu 2023. Hata hivyo, kwa jitihada zake Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan na kwa mapenzi yake kwa Watanzania ameweza kutafuta fedha na kuongezea mradi huu fedha na sasa utakwenda mpaka 2025.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Halmashauri yangu ya Kaliua kuna walengwa wa TASAF wapatao 946 ambao wametolewa kwenye mpango wa TASAF kwa kigezo kwamba wamehitimu ilhali hata uwezo wa kupata milo mitatu hawana. Je, TASAF wanaangalia vigezo gani ambavyo vinawapelekea hao walengwa wa TASAF kutolewa kwenye mpango wa kunusuru kaya maskini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rehema Migilla, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tathmini ilifanyika nchini kote ambapo kulikuwa kuna kaya 156,000 ambazo zilionekana zimeboreka kiuchumi. Hata hivyo, bado mwongozo ulikuwa haujatolewa kwa wadau na Halmashauri zote nchini ni namna gani bora ya kuweza kuwaondoa. Sasa nitakaa na Mheshimiwa Mbunge kuweza kuona hizi kaya 946 ambazo wametolewa ni walitolewa kwa vigezo gani, halafu nitampatia majibu yake.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Katika Jimbo langu la Sikonge, mwaka jana baada ya tathmini kufanyika kila kijiji kwa kushirikiana na Viongozi wa Vijiji, kuna orodha ambayo ilikubalika kwa pande zote mbili, lakini ilipofika Makao Makuu ya Wilaya wakapunguza idadi kwa nusu. Hao waliopunguzwa wana malalamiko makubwa sana dhidi ya uamuzi wa kuwaondoa kwenye orodha ya wafaidika wa TASAF. Je, Serikali kwa nini ilichukua hatua hiyo na itarekebisha lini hatua hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, utaratibu uliokuwepo ni kwamba yale majina ambayo yote yanaondolewa imewekwa namna ya kukata rufaa kwa yeyote ambaye anaona anakidhi vigezo vya kuwepo kwenye Mpango huu wa TASAF. Hivyo, nashauri kwamba watu wa Sikonge ambao wanaona kwamba wanastahili kuwepo kwenye mpango huu waweze kukata rufaa na rufaa zile zinapelekwa TASAF Makao Makuu. Inatumwa timu ya wataalam kuweza kwenda kuhakikisha na kuona kama watu hao wanastahili na kuweza kurudishwa kwenye mpango. Vile vile kama kwa Mheshimiwa Migila nitakaa na Mheshimiwa Kakunda ili kuona jinsi ya wataalam wetu kuweza kwenda na kuiangalia hiyo tathmini kwa ujumla.
MHE. ZAHOR MOHAMMED HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali ningeomba Serikali itusaidie kufahamu.

Je, kwa wale ambao walikuwemo kwenye mfuko wa TASAF lakini hawaku–qualify kuondoka lakini hawakurudishwa tena kwenye mfuko huu kwenye muda huu? Tafadhali.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zahor Haji, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa walengwa ambao walikuwemo kwenye mpango wa TASAF lakini baadae ikaonekana hali zao zimeimarika na kutolewa haijazuiwa wao kurudishwa kwenye mpango wa TASAF pale ambapo watakuwa wameshuka chini ya vile vigezo ambavyo vimewekwa vya mtu kuonekana ana hali nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninaomba nitakaa na Mheshimiwa Zahor Haji ili tuweze kuona ni namna gani wataalamu wetu wa TASAF wanaweza kwenda pale Mwera na kuangalia hizo kaya ambazo zilitolewa na ziweze kurudi katika mpango wa TASAF.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri zetu nchini zina mazingira tofauti. Kuna Halmashauri ambazo zina mazingira magumu sana kiasi ambacho walimu wanapoajiriwa wanaripoti halafu wanaenda kutafuta sababu za kuhama kwenda kwenye maeneo mengine kwa kutoa hata sababu za kusema wanaumwa ili waende maeneo ya mjini.

Mheshimiwa Spika, Je, Serikali inatoa motisha gani kwa walimu ambao wapo kwenye mazingira magumu kwa sababu watoto wetu wanapomaliza Kidato cha Nne na Darasa la Saba wanapata mitihani sawa na wale ambao wana walimu wa kutosha sasa tutaendelea kuwa na watoto ambao hawafaulu, wanafeli kwa sababu walimu wanakimbia mazingira magumu, tunaomba Serikali itueleze inandaa mazingira gani mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili Utumishi inachelewa kutoa vibali vya kuajiri walimu na hasa walimu wanapokuwa wamestaafu ama wanapofariki ama wanapoacha kazi kutokana na sababu mbalimbali. Je, ni lini Serikali italeta sheria ibadilishwe au Muswada tutengeneze sheria kwamba TAMISEMI iruhusiwe kuajiri walimu wa kuziba mapengo moja kwa moja badala ya kuomba vibali Utumishi kwa ajili ya kuziba mapengo ya walimu ili kuweza kuokoa elimu katika nchi yetu. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. David Mathayo Mbunge wa Same Magharibi.

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nichukue nafasi hii kutoa pongezi zangu za dhati kabisa kwake yeye Mheshimiwa Mbunge Dkt. David Mathayo wa Same Magharibi kwa maana amekuwa akifuatilia sana maslahi ya Watumishi wa Umma hasa wale wa Jimboni kwake Same Magharibi.

Mheshimiwa Spika, sasa nikienda kwenye swali lake la kwanza la motisha kwa Watumishi wa Umma hasa walimu wale waliopo pembezoni. Serikali imekuwa ikiweka kipaumbele sana cha kuona ni namna gani bora ya kuweza kutoa motisha kwa watumishi wanaoenda pembezoni kutoa huduma kwa Watanzania. Ndiyo maana hata jana nikiliarifu Bunge lako hili tukufu, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ametoa maelekezo pale ofisini kwetu kwa watumishi housing cooperation kuweza kuhakikisha kwamba wanajenga nyumba pembezoni ambazo ni affordable kwa ajili ya watumishi hawa waweze kuweza kupata nyumba kwa gharama nafuu katika maeneo wanayofanyakazi lakini vilevile waweze kulipia kupitia mshahara wao.

Mheshimiwa Spika, ukiacha hilo huwa tunawaasa sana na kuwataka waajiri yaani halmashauri zetu nchini kuhakikisha wanatenga bajeti katika mapato yao ya kuweza kutoa motisha kwa watumishi hawa, hasa wale wapya ambao wanaenda kuripoti. Kuna baadhi ya Halmashauri nchini ambazo zimefanya hivyo wale wanaoripoti kazini wanapewa magodoro, wanapewa baiskeli na vifaa vingine vya kuweza kuwaongezea motisha ya kazi pale wanaporipoti.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili kuhusu ajira mbadala. Tatizo si Ofisi ya Rais, Utumishi. Tatizo linakuwa kwa ajili wenyewe kuto-focus mbele kujua wangapi wanastaafu katika kipindi cha mwaka wa fedha fulani, wangapi ambao wamefariki katika kipindi cha mwaka wa fedha fulani ili waweze kuomba vibali vile vya ajira mbadala kwa wakati. Kwa hiyo, unakuta mara nyingi wanasubiri mwaka wa fedha unapita wanasema kwamba ni utumishi iliyokwamisha vibali vile lakini unakuta hawavi-compile kwa wakati kuvipeleka TAMISEMI ili nao TAMISEMI waweze kuvileta katika Ofisi ya Rais, Utumishi kuweza kuvitoa.

Mheshimiwa Spika, mara nyingi Ofisi ya Rais, Utumishi tunapopata maombi ya vibali vya ajira mbadala huwa Katibu Mkuu anavitoa palepale kwa sababu tayari mshahara wao upo, bajeti yao ipo lakini tunahitaji tupate maombi yale kwa wakati.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Tunaishukuru Serikali kwa kibali cha ajira ya zaidi ya nafasi 30,000. Katika nafasi zilizotangazwa hatuna kada ya Watendaji wa Vijiji na Kata.

Je, Serikali ni lini itatoa kibali cha ajira kwa Watendaji wa Kata na Vijiji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zacharia kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ipo mbioni kuwaajiri Watendaji wa Vijiji na Watendaji wa Kata na muda si mrefu tayari tutaanza kuweza kuwa-post wale Watendaji wa Kata kwenye maeneo yenu lakini vilevile bado tena narudia rai yangu kwa waajiri ku- compile orodha ya mahitaji yao kwenye Watendaji wa Vijiji, Mitaa na Kata na kuiwasilisha TAMISEMI kwa wakati ili waweze kuileta Utumishi ili pale zoezi hili la kuajiri hawa linapoanza basi tuweze kufidia maeneo yote ambayo yanauhitaji wa watendaji hao.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, tunashukuru sana kwamba kuna ajira ya walimu imetokea lakini kumekuwa na changamoto sana kwa ndoa za walimu wengi, kwa sababu walimu wanaajiriwa mbali na familia zao na wanapoomba uhamisho baada ya miaka mitatu bado Serikali imekuwa inaleta ugumu wa kuwakutanisha kukaa kama familia.

Serikali inampango gani ya kuwasaidia walimu hao ili ndoa zao zipate kudumu na kuendelea na maisha ya kawaida. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI
WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakagenda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hivi sasa Serikali ipo katika kufanya HR audit kuweza kufahamu mahitaji ya watumishi ni wapi wa kada fulani wapo wangapi ili kuweza kuja kurahisisha hili analolisema Mheshimiwa Mwakagenda kwamba pale wanapoomba uhamisho kuweza kwenda kujiunga na wenza wao ili kuweza kuona na uhitaji na nafasi iliyopo, kwa sababu kwa sasa ni lazima kuwe na nafasi ambayo iko wazi kule anapotaka kwenda. Lazima kuwe na hiyo vacancy ili kibali kiweze kutoka cha uhamisho. Kwa hiyo, tukishamaliza HR audit tutajua wapi kuna mahitaji gani, wapi kuna mahitaji gani.

Mheshimiwa Spika, nimalizie tu kulijibu hili kwa kusema mara nyingi wenza hawa wapo Mijini kwenye Majiji na Manispaa hawapo pembezoni, kwa hiyo ndiyo maana tunafanya HR audit kuweza kuona ule uhitaji kwa ujumla ili vibali viweze kuwa vinatolewa kwa urahisi wa wenza waweze kuwafuata wenza wao.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru pamoja na changamoto ya upungufu wa watumishi nchi nzima, lakini maeneo ya pembezoni ikiwemo Wilaya ya Nkasi ina upungufu wa watumishi 1,939. Je, Serikali inampango gani wa haraka wa kusaidia maeneo ya pembezoni ikiwemo Wilaya ya Nkasi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutoa kipaumbele cha ajira hasa kule pembezoni ambako kuna upungufu wa watumishi, lakini kama unavyofahamu Serikali inaajiri kulingana na uwezo wa bajeti.

Kwa hiyo, kadri tutakavyozidi kukusanya na bajeti yetu kuruhusu ndiyo tutakapozidi vilevile kuajiri watumishi wa kuweza kwenda kuwahudumia Watanzania hasa wale waliokuwa maeneo ya pembezoni.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kujibu kwa ufasaha na umejibu vizuri kwa kweli. Lakini nitakuwa na maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa ofisi ya maadili ni ofisi ya muungano lazima itakuwa na wafanyakazi wa muungano waliokuwepo Zanzibar nao pia wanahusika.

Je, katika hii warsha na makongamano na semina ambazo unazitoa, kwa upande wa wafanyakazi waliokuwepo Zanzibar, nao pia wamepatiwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa unahitajika lazima ofisi yako iwe na mjengo Zanzibar wa kufanyia kazi.

Je, ofisi yako unayofanyia kazi kwa Zanzibar iko sehemu gani kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Fakharia Shomar Khamisi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, kwamba viongozi wote wa Tanzania na Tanzania Zanzibar wamepewa semina hizi na kufanyiwa warsha mbalimbali na makongamano mbalimbali. Kati ya mwaka 2015 hadi 2022 jumla ya viongozi 28,450 wa pande zote mbili za Taifa letu wamefanyiwa semina hizi na warsha hizi wakiwemo Waheshimiwa Wabunge.

Kwa hiyo, nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge, kwamba tutaendelea kutoa warsha hizi na semina hizi kwa waheshimiwa na viongozi wengine mbalimbali ili wote tuweze kuwa na uelewa mmoja kuhusiana na masuala ya maadili.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, ofisi za maadili zipo kila mahali, kila kanda, kila mkoa. Kwa hiyo, hata upande Zanzibar ofisi hizi za maadili zipo katika kila mkoa. Ndiyo maana hata fomu zetu zile tunazozijaza za maadili tuna uwezo wa kuzirudisha katika ofisi zetu hizi zilizo maeneo mbalimbali ya Taifa letu. Naomba kuwasilisha.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili ya nyongeza: Je, ni lini ujenzi wa Daraja la Ntumbi ambalo linaunganisha barabara ya Ntumbi - Nangongo utaanza kufanya kazi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Nini mpango wa Serikali wa kuweka taa za barabarani katika Mji wa Manyoni ili kuweza kuboresha ulinzi na usalama wa Mji wa Manyoni?

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Pius Chaya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa daraja la Ntumbi, tayari bajeti ilikuwa imeshatengwa shilingi milioni 496 na tayari usanifu ulikuwa umeshafanyika na sasa wapo katika hatua za kutangaza ili daraja hili liweze kujengwa na wananchi wa Mheshimiwa Chaya pale na Watanzania wale wa Manyoni waweze kupata huduma ya barabara hiyo kupitika.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili kuhusu taa za barabarani, katika mwaka huu wa fedha tayari bajeti ilikuwa imetengwa kwa taa 15. Kwenye hili pia nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kulifuatilia sana. Tayari katika bajeti ya mwaka wa fedha unaofuata zimetengwa taa 28 pale Manyoni Mjini ambapo tutaenda kutekeleza.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru nami kupata kupata nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Waziri vikao vya RCC Mkoa wa Songwe vimekuwa vikipitisha barabara ya kutoka Kapalala kwenda Buha kilometa 36 kila mwaka toka nimeingia Ubunge, lakini hatujawahi kupata majibu ya kwamba barabara hiyo imepandishwa hadhi. Kila wakati tunakaa tunapeleka, tukaa tunapeleka, na leo mmesema ndiyo vikao halali vinavyopitisha. Lini barabara hiyo itakuwa ya hadhi ya TANROADS?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Phillipo Mulugo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, suala hili likishapitishwa kisheria kwenye vikao husika linakwenda kwa Waziri mwenye dhamana ya barabara ambaye ni Waziri wa Ujenzi. Sasa sisi kwa pamoja kwa kushirikiana na Wizara ya Ujenzi tutalifuatilia na Mheshimiwa Mbunge tutaona wapi ambapo japo hili limekwama na tutampatia majibu, lakini dhamana yake ipo kwa Waziri wa Ujenzi.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kuwa ujenzi wa kilomita moja ya lami Makao Makuu ya Wilaya ya Nyang’hwale pale Kalumwa, mkandarasi aliingia kwa kasi kubwa na akaweka vifusi na akashindilia; na baada ya hapo hajaweka lami; na leo zaidi ya miezi mitatu haonekani site; tatizo ni nini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hussein Amar, Mbunge wa Nyang’hwale kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tutalifuatilia jambo hili, na tutawasiliana na Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Geita na vilevile wa Wilaya ya Nyang’hwale kujua ni kwa nini mkandarasi huyu amekwama kuendelea na kazi hii? Vilevile nitakutana na Mheshimiwa Mbunge tuweze kulitafutia majawabu leo hii hii hapa tukiwa katika viwanja vya Bunge. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Je, ni lini barabara ya kuanzia Mzumbe kibaoni kwenda mpaka Lubungo mpaka Kibambila ambayo ni Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero, mpaka Kimamba, Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa itajengwa na kupitika kwa mwaka mzima kwa kuunganisha wilaya zote mbili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ishengoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tutalifuatilia suala hili kwa kuona barabara hii kama imetengewa bajeti katika mwaka huu wa fedha tunaokwenda. Nafahamu Waziri wa Nchi, Mheshimiwa Angellah Kairuki amekaa na Waheshimiwa Wabunge wa Mikoa yote na kuangalia vipaumbele katika barabara, afya na elimu. Hivyo, tutaangalia kama barabara hii na yenyewe imo ili tuone ni namna gani ambavyo tunaweza tukawafikia wananchi hawa wa kwa Mheshimiwa Ishengoma.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona kwa nafasi ya swali la nyongeza. Barabara ya kutoka Hoteli tatu mpaka Pande na hatimaye Limalyao katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa imeshafanyiwa mapendekezo ya kupandishwa hadhi ili iwe ya TANROADS na vikao husika. Lini Serikali itapandisha hadhi barabara hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Kassinge, Mbunge wa Kilwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyotoa majibu ya awali kwa Mheshimiwa Mulugo na Mheshimiwa Chaya, ili kupandisha hadhi barabara hizi, baada ya mchakato wote kuwa umeshapitiwa, sasa ni mamlaka ya Waziri mwenye dhamana ya barabara ni Waziri wa Ujenzi. Sasa wakati tunafuatilia suala la Mheshimiwa Mulugo tutahakikisha na hili la Mheshimiwa Kassinge nalo tunaliangalia.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa barabara ya kutoka Kolandoto kwenda Kishapu ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa Kishapu: Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mnzava, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeweka kipaumbele sana katika kuhakikisha barabara zetu zinapitika wakati wote ikiwemo barabara hii ya Kolandoto kwenda Kishapu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tutaliangalia suala hili na kuona ni namna gani barabara hii nayo itaweza kuwekewa fedha na kuweza kutengenezwa.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

(a) Kwa kuwa, Serikali inakubaliana na mawazo ambayo wananchi wa Kijiji cha Mtewele na ndiyo wanahitaji kupata huduma Makambako kwa sababu kutoka Makambako kwenda kwenye Kijiji hicho ni kilometa nne tu na kutoka kwenye Kijiji kwenda kwenye Halmashauri yao ni kilometa 72. Je, Serikali inatuagiza nini ili tuweze kufanikisha wananchi hawa kwa sababu wako tayari kurudi Makambako?

(b) Swali la pili. Kwa kuwa Kata ya Kivavi ni kata kubwa sana na kwa sababu Serikali inania ya kuwahudumia wananchi jirani na maeneo wanakokaa. Je, Serikali itakuwa tayari tuanzishe mpango wa kugawa Kata hiyo ya Kivavi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu Kijiji hiki cha Mtewele kuwa kilometa Nne bado utaratibu ni uleule. Ni wao wenyewe kuanzisha mchakato sasa hapa inahusisha Halmashauri Mbili, kwa maana ya Wanging’ombe wakae kuridhia hili kwenye vikao vyao kama nilivyoeleza kwenye majibu yangu ya msingi na vilevile Halmashauri ya Mji wa Makambako nao waweze kupitia katika vikao vyao na waweze kuleta katika Ofisi ya Rais TAMISEMI ili mchakato huo uweze kuanza.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili nalo vilevile linafanana. Kata hii ya Kivavi kuigawa lakini nataka niongeze tu kidogo hapo. Kwa sasa Serikali imeweka kipaumbele katika kuendeleza maeneo yale ambayo yaligawiwa hivi karibuni na tumeona jitihada kubwa ya Serikali ninyi Wabunge ni mashahidi. Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ametoa fedha nyingi sana kuhakikisha tunakamilisha majengo ya halmashauri, tunajenga nyumba za watumishi, tunajenga ofisi za Wakuu wa Wilaya. Kwa hiyo, kwa sasa kwanza kipaumbele kikubwa cha Serikali ni kuhakikisha tunaimarisha miundombinu kwenye maeneo ambayo yapo kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kuiuliza Serikali. Ni lini wataukwamua mchakato wa kuupanua Mji wa Moshi ambao ulishapita ngazi zote alizozitaja ikiwa ni pamoja na kupata GN Na. 19 ya tarehe 15 Julai, 2016?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Priscus Tarimo, Mbunge wa Moshi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nilimalizia kusema hapa, kwa sasa kipaumbele cha Serikali kwanza ni kuhakikisha tunakamilisha ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya maeneo ambayo yalikuwa yamekwisha megwa kupeleka huduma karibu ya wananchi. Baada ya hapo sasa tutaangalia mchakato huo mwingine wa kuweza kuendeleza maeneo kama ambavyo Mheshimiwa Tarimo amezungumza.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Je, ni lini Serikali kwa kuwa mchakato wa kupata Halmashauri ya Bunda ulishatekelezwa na tulishaandika, sasa ni lini Halmashauri ya Jimbo la Bunda itapata Halmashauri kutokana na umbali wa kutoka kwenye Jimbo langu kwenda kwenye Jimbo lingine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Getere, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, michakato kufika TAMISEMI yote tunaikusanya na kama nilivyoeleza hapo awali bado kwa sasa kipaumbele kikubwa cha Serikali ni kuhakikisha tunakamilisha miundombinu katika Halmashauri ambazo zilikuwa ni mpya na Wilaya ambazo ni mpya, baada ya hapo sasa tutaanza kuangalia tena haya maeneo mengine ambayo Mikoa imepitisha na kuleta kwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais TAMISEMI.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, ni lini Serikali itajenga shule za sekondari katika kata ambazo wanafunzi wake wanatembea umbali mrefu kwa mfano Chilangala, Mkomatuu ambazo ziko katika Jimbo la Newala Vijijini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; tunafahamu na kutambua kwamba shule hizo zimejengwa tunashukuru, lakini mkakati wa kupeleka walimu ukoje kwa sababu shule hizo mpaka sasa haijapelekewa Walimu wa kufundisha? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la kwanza la je, ni lini Serikali itajenga shule hizi kwenye kata zilizosalia? Dhamira ya Serikali ni kujenga shule katika kila kata ya nchi yetu na hii ilikuwa ni awamu ya kwanza tu. Hata hivyo, niwatoe mashaka Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imedhamiria kwenda kwenye awamu ya pili ya kujenga shule hizi za kata na muda si mrefu wataanza kuona shule hizi zikijengwa katika halmashauri zote 184 katika nchi yetu. Kila halmashauri itapata walau shule moja kwenye awamu ya pili.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, Mkakati wa Serikali. Wabunge ni mashahidi, wameona namna gani Serikali hii ya Awamu ya Sita imetangaza ajira zaidi ya 21,000 kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mheshimiwa Angela Kairuki ya kuajiri Walimu na watumishi katika Sekta ya Afya. Hii yote ni kwenda kuhakikisha kwamba Serikali inaziba mapengo haya ya Walimu ambao wanahitajika kwenye maeneo haya. (Makofi)
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, kumekuwa na idadi ndogo sana ya wanafunzi wanaosoma katika A-level Mkoani Mtwara. Je, Serikali haioni sababu ya kutoa motisha kwa kutenga kiasi kikubwa cha wanafunzi wanaotakiwa kusoma sekondari za A-level ambazo ziko katika Mkoa wa Mtwara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mchungahela kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ina mkakati huo anaouzungumza yeye na ndio maana tayari imetengwa fedha ya kujenga shule za sekondari za mikoa kuhakikisha kwamba wanafunzi wanaotoka kwenye maeneo husika wanabaki katika maeneo hayo hasa wasichana. Pia tayari Serikali imekwishatenga Shingi Bilioni tatu kwa mikoa 10 ya mwanzo na sasa itakwenda tena kwenye awamu ya pili kwenye mikoa mitano, halafu itakuja kumalizika katika mikoa mingine, hii ni kuwabakiza.

Mheshimiwa Spika, vile vile kuna shule zile za A - level ambazo zilijengwa na wananchi kule na Serikali ikaja kumalizia, huwa zile zinatoa kipaumbele kwa wanafunzi wa maeneo yale kasoro zile shule maalumu tu za kitaifa ndio zinachukua wanafunzi kutoka katika kila eneo la Taifa letu. Naomba kuwasilisha.
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, nashukuru, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza. Je, Serikali imetenga kiasi gani cha fedha kwa ajili ya usanifu kwa madaraja yote mawili ya Mto Juhe na Piyaya kwa mwaka wa fedha 2023/2024?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; nini commitment ya Serikali pindi upembuzi utakapokamilika kutenga fedha haraka kwa sababu, madaraja haya yatakayojengwa yatasaidia kuokoa maisha ya watoto ambao wamekuwa wakichukuliwa na maji ya Mto Juhe pamoja na Mto Piyaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA – (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Emmanuel Shangai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetoa majibu hapa kwenye majibu yangu ya msingi. Serikali itatenga fedha katika mwaka wa 2024/2025 ili kuhakikisha usanifu unafanyika katika madaraja haya ya Mto Piyaya na Mto Juhe.

Mheshimiwa Spika, lakini katika swali lake la pili; Serikali imeweka kipaumbele sana katika kuhakikisha inatengeneza barabara na madaraja katika Jimbo la Ngorongoro, lakini katika majimbo yote ya hapa nchini. Na tayari maelekezo yalikuwa yameshakwenda kwa mameneja wote wa TARURA wa Wilaya kuhakikisha wanatenga bajeti katika barabara hizi ambazo ni za kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, na ni imani yangu katika bajeti hii, barabara hii itakuwa nayo imetengewa fedha kwa ajili ya upembuzi yakinifu. Naomba kuwasilisha.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, nil in Daraja la Isararo – Ipanzya litajengwa, ambayo imekuwa ni ahadi ya muda mrefu sana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika,
naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hassunga, la ahadi ya kujenga madaraja haya ambayo ameyataja: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimekuwa nikimjibu Mheshimiwa Shangai hapa; maelekezo yalitoka kwa mameneja wote wa TARURA wa mikoa na wote wa Wilaya kuhakikisha barabara hizi ambazo pia ni ahadi za viongozi lakini, lakini ambazo ni kipaumbele katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu yatengewe fedha. nitakaa na Mheshimiwa Mbunge kuweza kuangalia katika ahadi hizi na barabara hii kama imetengewa fedha.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza: -

Je, Serikali iko tayari kutenga fedha kwa ajili ya kutengeneza Daraja la Sanjawe, Mara na Daraja linalounganisha Basodeshi na Gietamo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika,
naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Samweli, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ipo tayari kutenga fedha ya barabara hii ya Sandawe. Na ninaamini katika mwaka huu wa fedha tayari TARURA, kupitia Meneja wa Mkoa na Meneja wa Wilaya, watakuwa wameiwekea fedha barabara hii na tutampatia Mheshimiwa Mbunge Taarifa hiyo.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza: -

Je, ni lini Serikali itajenga daraja linalounganisha Kata ya Kiwele, Kijiji cha Kiwele na Kata ya Nzihi, Kijiji cha Kipera?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika,
naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jackson Kiswaga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyokuwa nimeshasema hapo awali, tayari maelekezo yalikuwa yametolewa kwa mameneja wote wa TARURA wa mikoa na Wilaya kuhakikisha wanatenga fedha kwenye barabara hizi na madaraja haya ambayo ni viunganishi vya kata na kata na Wilaya na Wilaya. Na ninaamini katika barabara ambayo Mheshimiwa Kiswaga ameitaja nayo Meneja wa TARURA Mkoa na Wilaya watakuwa nayo wameifanyia kazi.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, ni zaidi ya miaka mitano sasa daraja la kuunganisha Kata ya Msolwa Station na Mang’ula limekatika sambamba na kivuko cha Chikago – Kidatu na kivuko cha pale Kiberege. Je, ni lini Serikali itajenga madaraja haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA – (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asenga: -

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kumuelekeza Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Morogoro na Meneja wa TARURA wa Wilaya anakotoka Mheshimiwa Asenga, kuhakikisha wanafika kwenye barabara hiyo ambayo ameitaja Mheshimiwa Asenga, ili kufanya tathmini na kujua ni kiasi gani kinahitajika kwa ajili ya kuweza kuunganisha kata hizo mbili.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri: -

Mheshimiwa Spika, umri wa shule hii nilisoma kwenye shule hiyo, kwa hiyo, imechakaa sana. Ni lini Serikali itatuma timu maalum kwenda kutathmini miundombinu ya shule hii?

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili; shule hii ambayo ina O- Level na A-Level haina kabisa mwalimu wa physics, haina kabisa mwalimu wa biology na ina walimu wa mkataba wa geography na history. Naomba commitment ya Waziri kwenye mgawo wa walimu wanaoajiriwa hivi karibuni, shule hii itapata walimu wa kutosha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Constantine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa amekuwa akifuatilia sana suala la shule hii ya sekondari ya Geita ambayo ni ya kitaifa. Nikienda kwenye swali lake la kwanza la, ni lini timu itafika katika shule hii kufanya tathmini.

Mheshimiwa Spika, nimuahidi kwamba, baada ya Bunge hili Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, itahakikisha timu inafika katika shule hii na kufanya tathmini na kuweza kuleta taarifa yake, ili kuweza kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, lakini nikienda kwenye swali lake la pili, la lini Serikali itapeleka walimu: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo wote ni mashahidi humu ndani, Serikali imetangaza ajira zaidi ya 21,000 kwa walimu na watumishi wa sekta ya afya. Na tutahakikisha shule hii vilevile inapata walimu hawa wa sayansi ambao amewataja Mheshimiwa Mbunge.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza. Moja, barabara hii inaunganisha Mikoa Mitatu. Inaunganisha Mkoa wa Singida, Dodoma na Manyara. Naomba kujua ni kwa nini, barabara hii tusiipandishe hadhi iwe TANROADS ili iweze kuhudumiwa kwa urahisi zaidi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Naibu Waziri Jimbo Lake na Jimbo langu linaunganishwa na barabara chafu kweli kweli, kati ya Seya na Zajiro kwake. Nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha barabara hiyo inatengenezwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mohamed Lujuo Monni, Mbunge wa Chemba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu kupandisha hadhi barabara hii ambayo inaunganisha Mikoa Mitatu ya Singida Dodoma na Manyara, utaratibu upo wa kisheria kwa maana lazima vikao vianze katika ngazi ya Wilaya, vikitoka kwenye Wilaya viende kwenye Bodi ya Barabara ya Mkoa na baada ya kutoka Bodi ya Barabara ya Mkoa viende RCC na ndipo hadhi ya barabara hii iweze kupandishwa.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili. Nikiri ni kweli barabara hii inayounganisha kati ya Jimbo la Mheshimiwa Monni na Jimbo langu mimi la Chamwino na tayari maelekezo yalikuwa yameshakwenda kwa Mameneja wote wa TARURA wa Mikoa, kuhakikisha kwamba wanatenga fedha ya kuhakikisha vipande vya barabara hii vinaanza kutengenezwa. Katika mwaka huu wa fedha tuliouombea wa 2023/2024 barabara hii vilevile imo katika barabara zilizoombewa fedha. Naomba kuwasilisha.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itaanza kukarabati barabara ya kuanzia Bwakila Chini mpaka Bwakila Juu katika Halmashauri ya Morogoro Vijijini ili iweze kupitika bila ya matatizo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Dkt. Ishengoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutenga fedha kadri ya upatikanaji wa fedha kwenye bajeti kwa ajili ya ukarabati wa barabara. Ninaomba nichukue nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kumwelekeza Meneja wa TARURA Mkoa wa Morogoro na Meneja wa TARURA Wilaya ya Morogoro Vijijini kuhakikisha kwamba wanaenda kuiangalia hii barabara na kuona kama imetengewa fedha kwenye bajeti hii ambayo tumetoka kuiombea na Bunge lako Tukufu imepitisha ili kama ilitengewa fedha basi ukarabati wake uanze mara moja.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Kutokana na mvua zinazoendelea barabara ya kutoka Kitoho kwenda Mwatasi inayounganisha na Masisiwe kwa sasa imepata madhara makubwa na haipitiki.

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka fedha za dharura ili barabara hii iweze kupitika vizuri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nyamoga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, natoa tena maelekezo tena hapa kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- TAMISEMI kwa Meneja wa TARURA Mkoa wa Iringa na Meneja wa TARURA Wilaya ya Kilolo kuweza kwenda kuifanyia tathmini barabara hii ya Mwatasi - Kilolo na kuona maeneo ambayo yameathirika sana ili waweze kuyafanyia kazi kwa haraka.
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuweza kuniona. Barabara ya kutoka Matundasi kuelekea Itumbi imeharibika sana baada ya mvua hizi ambazo zinazoendelea kunyesha.

Je, ni lini sasa Serikali itatoa fedha ili barabara hii iweze kujengwa kwa kiwango cha changarawe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Masache Kasaka, Mbunge wa Chunya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ya Matundasi mpaka Itumbi ni kweli ipo chini ukilinganisha na usawa wa barabara yenyewe na ardhi ya pembezoni, tayari katika mwaka huu wa fedha wa 2023/2024 barabara hii imeombewa fedha na ukarabati wake utaanza ili kuweza kuinyanyua.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuuliza swali la nyongeza. Mheshimiwa Waziri ni lini Serikali itaanza kujenga kwa lami barabara ya Tabora Mambari ili kuunganisha Tabora Magharibi na Mashariki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Almas Maige kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa barabara hii unategemeana na upatikanaji wa fedha na tutaangalia katika bajeti hii ambayo imepitishwa ambapo ninyi Bunge hili Tukufu limeiidhinishia TARURA matumizi uya fedha ya zaidi ya Bilioni 830, kwa ajili ya kuweza kukarabati barabara mbalimbali nchini mwetu kwenye Majimbo yetu ikiwemo Jimbo la Mheshimiwa Almas Maige, kwa hiyo tutaliangalia na kuweza kulifanyia kazi.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Makamu wa Rais alivyokuwa Shinyanga aliahidi barabara ya kutoka Ndala kwenda Mwawaza ambako kuna Hospitali ya Rufaa, ingetengenezwa kwa kiwango cha lami.

Ningependa kujua ni lini itaanza kutengezenzwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Mnzava, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge barabara hii ni ahadi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, vilevile inaunganisha huduma muhimu kwenye jamii kama vile Hospitali hii ambayo iko hapo, hivyo basi Serikali itaipa kipaumbele na kutekeleza utekelezaji wa barabara hii kama ilivyokuwa maelekezo ya Makamu wa Rais lakini vilevile ni uhitaji mkubwa wa wananchi wa Shinyanga.
MHE. DAUD P. VENANT: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nipongeze Serikali kwa majibu mazuri. Wilaya ya Uyuwi ina upungufu ya watumishi zaidi ya 2,000 lakini pamoja na upungufu huo Serikali imebadilisha utaratibu wa watumishi hasa walimu na madaktari kuwa wakandarasi. Yuko darasani anaambiwa huku mfuko wa simenti umepotea huku anatibu anaambiwa vibarua hawajalipwa.

Je, Serikali haioni haja ya kubadilisha mfumo ili hawa ambao tunao pamoja na upungufu wao wafanye kazi kikamilifu?

Swali la pili, Jimbo la Igaula hatukuwa na shule ya five na six, nashukuru Serikali imetuletea, lakini shule ile ina mchepuo wa sayansi hatuna walimu wa sayansi.

Je, kwenye ajira hizi hauoni unipe upendeleo maalum kwenye ile shule ili iweze kufanya vizuri kwa sababu imeshaanza kufundisha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa
Spika, swali lake la kwanza hili la nyongeza analo sema kwamba walimu sasa au watumishi kwa ujumla wamegeuka kuwa wakandarasi na kuacha kufanya kazi zao; naomba nimkumbushe Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wengine humu ndani, kwamba wale wakuu wa shule na walimu wakuu ni nafasi za madaraka. Hivyo wao ndio accounting officers katika zile shule zao. Ni kama mtu anapokuwa Katibu Mkuu wa Wizara, anapokuwa Katibu Tawala wa Mkoa, yeye ndiye accounting office. Zile pesa zinaingia kwenye account ya shule husika kwenye mradi. Sasa ni wajibu wao kuhakikisha matumizi ya zile fedha yanakuwa ni mazuri na ya uwajibikaji. Sasa nitolee kwa ujumla kwamba halmashauri bado ina mkono kuhakikisha zile kamati za manunuzi kwenye force account, kamati ya mapokezi na kadhalika zinafanya kazi kwa miongozo na wataalam wa halmashauri kusimamia; lakini bado ni wajibu wa Mkuu wa Shule, ni wajibu wa Mwalimu Mkuu kuhakikisha matumizi ya zile fedha yanakuwa mazuri.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la walimu wa sayansi kupatikana katika hii shule ambayo tayari imeshafanywa kuwa A-level ndani ya halmashauri yake. Nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge. Ninyi wote ni mashahidi, katika kipindi kifupi cha uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, maeneo yote yamepata watumishi wa kutosha katika kipindi cha miaka hii miwili; na tayari kuna ajira hizi ambazo zimetangazwa. Kwa hiyo nikutoe mashaka Mheshimiwa Mbunge kwamba katika hizi ajira zilizotangazwa tutahakikisha pia na wewe kule katika shule uliyoitaja mnapata walimu.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante, nilitaka kufahamu ni lini sasa Serikali italeta watumishi wa afya katika Jimbo la Msalala?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, watumishi wa afya kwenda Msalala naamini katika hizi ajira zilizotangazwa sasa ambazo Mheshimiwa Rais ametoa kibali cha kuweza kuajiri watumishi wa afya wa kutosha na Msalala vile vile nanyi mtapata watumishi wa afya.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. halmashauri ya Kyerwa inawatumishi wa kada ya afya 252 ikiwa na mahitaji ya watumishi 1022 ni upungufu wa asilimia 75.

Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha kwenye hii halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa
Spika, katika ajira hizi ambazo Serikali imetangaza tutahakikisha pia na Halmashauri ya Kyerwa ina pata watumishi wa kwenda kwenye kada ya elimu na kada ya afya vile vile.
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, Je, ni lini Serikali itapeleka madaktari kwenye hospitali ya kanda iliyojengwa Mitengo Mkoani Mtwara.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutashirikiana na Wizara ambayo ndio wasimamizi wa hospitali hizi za kanda kuhakikisha kwamba Hospitali hii ya Kanda ya Mtwara kule inapata madaktari katika ajira hizi kwa sababu Wizara ya Afya nao wametoa ajira hizi kupitia mfumo wao.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kuwa Hospitali ya Manispaa ya Kahama inatibu kama hospitali ya mkoa; ni nini kauli ya Serikali kuhusu kuongeza idadi ya watumishi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwenye ajira hizi ambazo Serikali imetangaza na ambazo mchakato unaendelea tutahakikisha hospitali ya Manispaa ya Kahama nayo inapata watumishi wa kutosha kuweza kusaidia wananchi wa pale Kahama.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nashukuru, mbali na Serikali kutoa ajira nyingi, Jimbo la Sumve limeendelea kuwa na tatizo la upungufu mkubwa wa watumishi hasa katika sekta ya elimu, kiasi kwamba Shule kama Nyang’enge, Bukala zina walimu kati ya watano mpaka saba.

Je, Serikali haioni sasa umefika wakati wa kutoa upendeleo maalumu katika ajira zinazofuata kwa Jimbo la Sumve ili kukidhi mahitaji ya walimu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nilikuwa nimeshasema awali kwamba katika kipindi hiki cha miaka miwili ya uongozi wa Doctor Samia Suluhu Hassan, Serikali imejitahidi sana kuhakikisha inaajiri walimu wengi, na ninyi ni mashahidi kwenye halmashauri zenu Waheshimiwa Wabunge mmepata walimu wa kutosha. Kwenye hizi ajira mpya tutahakikisha Sumve pia nanyi mnapata Mheshimiwa Mbunge.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, kwa kuwa hitaji letu ni uhalisia kuliko nadharia, kutokana na uhalisia kwamba hata eneo la dampo sasa tumenunua Moshi Vijijini; na moja ya changamoto ni kwamba barabara inayoelekea kwenye dampo hatuwezi kuikarabai sisi kwa sababu haiwezi kuingia kwenye bajeti ikafanye kazi Moshi Vijijini. Na Moshi Vijijini pia haiko kwenye vipaumbele vyao kwa hiyo inatusababisha sisi tuna operate kwa gharama kubwa sana. Lakini pia inasababisha kwa mfano hospitali ya halmashauri inayojengwa Moshi Mjini inabidi ijengwe kwa ghorofa jambo ambalo ni karibu mara mbili ya gharama za kutengeneza maeneo mengine.

Je, tukiachana na Suala la Jiji ni lini mtakubali tupanue kuendana na GN namba 219 ya tarehe 15, July 2016 ikiwa ni pamoja na kupata maeneo ya makaburi ambayo hatuna?

Swali la pili; yapo maeneo kwenye kata, kwa mfano kata ya Shirimatunda, eneo la Boniti ambalo lilikuwa la viwanda lakini sasa hivi limesharasimishwa kuwa makazi lakini haliwezi kuendelea ili watu wapate hati zao kwa sababu ya kusubiri mchakato huo.

Je, hamuoni kwamba kuna uwezekano wa kutoa upendelea kwa Moshi Mjini kwanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa
Spika, nikienda kwenye swali lake la kwanza la Mheshimiwa Tarimo la uhitaji huu ni uhalisia; Serikali inatambua umuhimu wa kutanua mipaka ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi. Lakini kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, kwamba kwa sasa kipaumbele kikubwa ni kuhakikisha tunaimarisha yale maeneo ambayo ni mapya na halmashauri ambazo ni mpya. Ni muda si mrefu halmashauri nyingi zilihamia katika maeneo yao ya utawala, na kwa sasa Serikali hii ya Awamu ya Sita imeweka kipumbele kuhakikisha majengo ya utawala,kuhakikisha huduma za hospitali za Wilaya, kuhakikisha mashule na kadhalika yanajengwa, na hivyo baada ya haya kukamilika Serikali itaanza kutenga bajeti kuhakikisha maeneo mapya ya kiutawala yanatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, niseme tu kuwa Serikali inalichukua hili ambalo Mheshimiwa Mbunge amelizungumza la Halmashauri ya Manispaa ya Moshi kupewa upendeleo maalumu kwa sababu tayari GN ilikuwepo. Pale ambapo tutamaliza ukamilishaji wa ujenzi wa miundo mbinu katika halmashauri mpya basi Moshi Mjini Manispaa nayo itapewa kipaumbele.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, kimsingi hospitali yetu hii ni kongwe sana inawezekana ni kati ya hospitali kongwe zaidi Tanzania ambayo ilijengwa mwaka 1952.

Je, Serikali inatupa commitment gani kwamba tutapewa fedha hizi maana tumekuwa tukiahidiwa mara nyingi tunaletewa fedha za ukarabati na hatujawahi kupewa.

Je, Serikali ina tupa commitment gani kwamba fedha hizi zitakuja ili hospitali yetu hii ipate kukarabatiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetoa majibu yangu ya msingi katika mwaka wa fedha 2023/2024 hospitali hii kongwe ya Mjini Korogwe ya Magunga imeshatengewa shilingi milioni 900 kwa ajili ya ukarabati.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, wananchi wa Kijiji cha Idunda kata ya Kimara wamekarabati jengo lao wenyewe ili liwe zahanati na limekamilika.

Je, Waziri yuko tayari kuagiza Serikali kupeleka watumishi na vifaa tiba mara moja kwa sababu wanatembea zaidi ya kilometa 40 kupata huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwenye zahanati hii ya Idunda katika ajira hizi ambazo Serikali imetangaza za elimu na afya tutahakikisha kwamba zahanati hii inapata watumishi. Lakini vilevile kuhusu vifaa tiba naomba nichukue nafasi hii mbele ya Bunge lako hili kumuelekeza kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kilolo kuhakikisha anaanza kuweka fedha kwa ajili ya kununua vifaa tiba na sisi huku Wizarani tutaona ni lipi ambalo linaweza likafanyika ku-complement jitihada za Mkurugenzi wa Halmashauri.
MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya kaka yangu Naibu Waziri Deo Ndejembi nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa Shule ya Msingi ya Muhintiri inakabiliwa na changamoto hizo hizo ambazo Mheshimiwa Naibu Waziri ametoa majibu kwa Shule ya Puma.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kuambatana na mimi kwenda jimboni kujionea msongamano mkubwa wa wanafunzi katika shule hiyo na kuangalia namna ya kuweza kuwasaidia wanafunzi wa Shule Msingi ya Muhintiri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niko tayari kuongozana na Mheshimiwa Kingu kuelekea katika shule hii ya Muhintiri ili kujionea msongamano huo na kuweza kuona ni hatua gani Serikali inaweza ikachukua kuweza kutoa msongamano huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru; je, ni lini sasa Serikali itaimarisha Shule za Msingi Salakwa, Salama A na Salama B, Salama na Nyarubundu; ni lini majengo ya shule hizi yamezeeka sana, ya muda mrefu, lini Serikali itatekeleza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba baada ya session hii ya maswali nikae na Mheshimiwa Getere kuweza kuona ni hatua gani tunaweza tukazichukua za haraka kuweza kuzifanyia shule hizi matengenezo ambayo zinahitaji.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Kwa kuwa wananchi wako tayari kukamilisha majengo ya madarasa ambayo Serikali imetoa shilingi milioni 260 na uwezekano upo ndani ya miezi miwili majengo haya yakakamilika.

Je, anihakikishie Naibu Waziri mwezi Julai ujasili na uanzwaji wa kidato cha tano utakuwa tayari?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Shule ya Sekondari Mchoteka ina walimu watano tu wa sayansi.

Je, kukamilisha kidato cha tano na sita Serikali itapeleka walimu wa sayansi zaidi ili watoto wale wawe na ufaulu mzuri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, shule hii kama nilivyokwishakusema kwenye majibu yangu ya msingi imeombewa usajili kutoka Wizara ya Elimu. Na kuona kama itakuwa tayari mwezi wa saba kuweza kupokea wanafunzi tutalifanyia kazi hili kwa haraka sisi Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu kuweza kupata usajili na kuona kama itaweza kupokea wanafunzi mwezi huu wa saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili la ukosefu wa walimu wa sayansi. Bunge lako tukufu ni mashahidi kwamba Serikali imetoa ajira zaidi ya 21,000 ambapo katika hizo zipo za walimu na zipo za Idara ya Afya. Hivyo basi katika ajira hizi tutaiwekeza kipaumbele Shule hii ya Sekondari ya Mchoteka.
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi ya kuuliza swali moja. Shule ya Sekondari Kilindi Girls na Shule ya Sekondari Mlongwema zilizopo Wilaya ya Lushoto zina upungufu mkubwa wa mabweni lakini zinachukua watoto all over the country, ni form five na six.

Je, ni lini Serikali itapeleka mkakati maalum wa kuongeza mabweni katika shule hizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa Serikali upo wa kuendelea kutafuta fedha kuhakikisha kwamba shule zote zenye uhitaji wa mabweni yanaweza kujengwa. Nitoe rai kwa viongozi wa Halmashauri hii ya Lushoto na Kilindi kuanza kuhamasisha wananchi kuanza ujenzi wa mabweni na Serikali inaweza ikaja kuja kuyamalizia majengo hayo kama walivyofanya kule Mchoteka kwa Mheshimiwa Mpakate.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba niulize swali moja fupi. Kwa vile Kata ya Mamba Kaskazini na Mamba Kusini kuna shule nyingi za sekondari lakini hatuna shule hata moja ya kidato cha tano na sita.

Je, Serikali iko tayari kuipandisha hadhi Shule yaSekondari ya Mboni kwa kuijengea pia hosteli?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye shule hizi ambazo amezitaja Mbunge za Mamba Kaskazini na Mamba Kusini, utaratibu ni ule ule kuweza kujenga miundombinu ambayo inatakiwa ili kupandisha hadhi shule halafu kuiombea usajili kutoka Wizara ya Elimu. Tutakaa na Mheshimiwa Mbunge kuona shule hizi kama miundombinu inakidhi vigezo, na kama inakidhi vigezo basi tuone taratibu za kuombea usajili wa kuweza kupata mkondo wa kidato cha tano na sita.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi. Shule ya Sekondari ya Kumkubwa ni shule ya kidato cha tano na sita inayotumia majengo chakavu yaliyokuwa kambi ya wakimbizi.

Je, ni lini Serikali itajengea miundombinu ya madarasa katika Shule hii ya Sekondari ya Kumkubwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lengo la Serikali kuboresha miundombinu ya shule zote, si tu za sekondari, kuanzia za msingi, sekondari na hizi za A-level. Hivyo basi tutaona ni namna gani ambavyo tunaweza tukaanza ukarabati wa shule hii ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, swali langu, nataka kujua ni lini Serikali itaanza ujenzi wa shule ya mkoa ya mfano ya wasichana katika Mkoa wa Mtwara kama ilivyojenga kwenye mikoa mingine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imedhamiria kujenga shule hizi katika kila mkoa na tayari bilioni 30 ilishatoka kwa ajili kujenga shule kumi kwenye mikoa kumi ambao kila mkoa ilipata bilioni tatu. Tunaenda sasa kwenye hatua ya pili ambapo mikoa mitano itapokea hizi bilioni tatu pia kujenga na awamu ya tatu pia tutamalizia hizo shule nyingine na tutahakikisha Mkoa wa Mtwara pia nao unapata shule hii kwa wakati.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri ametamka uhaba wa shule za A-Level na jambo hilo limejityokeza katika jimbo langu. Mpaka sasa hivi kuna A- Level mbili tu zinazofanya kazi wakati kuna kata 18 na tulishaomba kupandisha hadhi Shule ya Makong’onda kuwa A- Level; mchakato huu wa kupandisha hadhi utakamilika lini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, mchakato wa kupandisha hadhi shule kuwa na mkondo wa kidato cha tano na sita ni upo chini ya Wizara ya Elimu, maombi yale yanapelekwa Wizara ya Elimu. Nitakaa na Mheshimiwa Mchungahela kuona mchakato huu umefikia wapi na kuweza kumpa majibu hayo.
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, nashukuru majibu mazuri ya Serikali lakini niombe tu kwa kuwa maeneo ya kanda ya ziwa yamezungukwa na madini ya kila aina.

Je, hamuoni haja ya kujenga chuo cha madini katika Wilaya ya Sengerema ili kuwapatia wananchi wetu wapate ujuzi lakini waweze kuchimba kitaalamu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kwa, kuwa sasa uvuvi umekuwa ni wa kisasa;

Je, hamuoni haja ya kujenga chuo cha uvuvi katika Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema ili wavuvi wetu waweze kuvua kitaalam tuendane na kasi ya Uganda nan chi nyingine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo umesema hapa haya masuala ambayo ni yako chini ya Wizara ya Madini. Sisi kama Ofisi ya Rais, TAMISEMI tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Madini. Swali lake la pili ni la Wizara ya Uvuvi, kuona mipango waliyonayo juu ya kuweka vyuo hivi katika kanda ya ziwa.

MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali; lakini hata hivyo nina swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa barabara ni moja ya barabara ambazo wananchi wa Mbarali wanazitumia sana kusafirishia mazao na sasa barabara nyingi zimeharibiwa mno na mvua hali inayopelekea ugumu wa kufanya shughuli hizi.

Je, ni ipi kauli ya Serikali kwa wanambarali kuhusu adha hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyozungumza Mheshimiwa Mbunge, barabara nyingi ambazo zimeharibika kutokana na msimu huu wa mvua zimewekewa kipaumbele cha matengenezo katika mwaka huu wa fedha tunaoenda kuuanza Julai, Mosi mwaka huu.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nataka nijue Serikali ina mpango gani wa kujenga Barabara ya mkato inayotoka Komaswa – Tarime Vijijini kuja mpaka Rorya kupitia Nyatorogo pamoja na Daraja lake la Nyatorogo kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024, kama ina mpango wowote wa ujenzi wa daraja pamoja na barabara hii? (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa unaweza ukataja vizuri hizo barabara zako kutoka wapi mpaka wapi?

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara inayotoka Komaswa – Tarime Vijijini kuja Rorya kwa kupitia Kata ya Nyatorogo ikiwa ni pamoja na daraja lake linalounganisha Tarime Vijijini pamoja na Rorya. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakaa na Mheshimiwa Mbunge kwanza kuona kwamba barabara hii ni ya TARURA au ya TANROADS halafu kuona ni hatua gani ambazo tunaweza tukazichukua kuweza kufungua Barabara hii ya mkato ya Komaswa hadi Rorya. (Makofi)
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti nishukuru kwa kunipa nafasi. Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI kipindi hicho Ummy Mwalimu aliahidi shilingi bilioni 1.5 kuunganisha Wilaya ya Tanganyika na Wilaya ya Uvinza kupitia Kata ya Kalia na Kata ya Mwese.

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo ili wananchi waweze kupata huduma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa barabara hii ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutakaa na wenzetu wa TARURA kuona mpango wao juu ya kutenga fedha hii ya bilioni 1.5 ya kuunganisha barabara kati ya Tanganyika hadi Uvinza. (Makofi)
MHE. MASACHE J. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kuniona. Barabara inayoanzia Chunya Mjini kupita Igundu mpaka Sangambia ambako itaunganisha na Mbarali kwa kipindi hiki imeharibika sana kutokana na changamoto za mvua. Je, ni Serikali itatenga fedha hili barabara hii ijengwe kwa kiwango cha changarawe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, TARURA ina bajeti ya bilioni 11 kwa ajili ya dharura na hivi sasa maombi tayari yamefanyika kwa ajili ya kuongeza bajeti hii kwenda bilioni 46 ili kuhakikisha wana fedha ya kutosha kuweza kutengeneza barabara hizi wakati wa dharura. Kwa sasa tutaangalia barabara aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge kuona katika mwaka fedha unaoenda kuanza tarehe 1, Julai inapewa kipaumbele cha kutengenezwa.
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Tuna ahadi ya Waziri wa TAMISEMI katika Wilaya ya Kibiti kutoa fedha kujenga barabara kwa kiwango cha lami kutoka Kibiti Mjini kwenda kule kwenye Halmashauri yetu ya Kibiti.

Je, ni lini Serikali itatoa fedha hizo kukamilisha ujenzi huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hii ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri ya Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutakaa na wenzetu wa TARURA kuona ni namna gani wamejipanga katika kutekeleza ahadi ya hii ya Mheshimiwa Waziri ya kuweka barabara ya lami kutoka Kibiti Mjini mpaka ambapo wamejenga halmashauri yao. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ahadi ya Mheshimiwa Waziri Ummy Mwalimu ni kuiunganisha Kata ya Nyahua na Makao Makuu ya Wilaya ya Sikonge na zilitengwa bilioni 1.86 mwaka juzi na mwaka jana, lakini haijatoka hata senti moja. Je, ni lini sasa Serikali itatekeleza hiyo ahadi kwa kutoa hizo fedha ambazo zilitengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimeshawajibu Waheshimiwa Wabunge wengine hapa kwamba, kwa kuwa hii ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutakaa na wenzetu wa TARURA kuona ni namna gani wamejipanga katika utekelezaji wa ahadi hii.
MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali: -

Kata za Mahuta na Mkwedu hazina shule ya sekondari kabisa; je, Serikali inaweza ikatupa fedha kwa ajili ya kujenga sekondari hizo kwa sababu tayari wananchi wameshaanza kujenga maeneo yale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kata hizi alizozitaja Mheshimiwa Katani hapa Serikali tayari iko mbioni kupeleka shilingi milioni 470 kwenye halmashauri 184 nchi nzima kwa ajili ya ujenzi wa shule nyingine za sekondari katika kata zile ambazo bado hazijapata shule hizi za sekondari. (Makofi)
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, imekuwa ni utaratibu kwa wananchi kutumia nguvu zao kujenga shule ama zahanati. Lakini bahati mbaya sana kumekuwa kuna udanganyifu kwenye halmashauri, hawazielezei kwa kina thamani ya kifedha ambazo wametumia nguvu za wananchi. Matokeo yake wanaomba Serikali pesa kwa madhumuni kwamba wanataka kumalizia maboma lakini hawaelezi ile nguvu, matokeo yake ni kwamba Serikali inatoa pesa lakini pesa ambayo inatolewa na Serikali haitumiki kwa matumizi yanayotakiwa kwa sababu kuna udanganyifu wa fedha ambayo imetolewa na wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni lini Serikali itafanya uchunguzi wa kina ili kujua kama fedha zinazotolewa kwa ajili ya kumalizia maboma ni za kumalizia maboma na nguvu za wnanachi vilevile zinajulikana ni kiwango gani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Halima James Mdee, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikifanya tathmini ya mara kwa mara katika halmashauri zetu kuangalia hali ya maboma ambayo yanaripotiwa na wakurugenzi wa halmashauri. Hivi tunavyoongea tayari kuna timu ambayo inafanya tathmini ya kuweza kuona maboma yaliyopo na hizi fedha zinazopelekwa kwenye shule za sekondari na hizi tunazopeleka kwenye shule za msingi kuona wamekwenda kumalizia maboma yaliyokuwepo ama wameanza madarasa mapya. Kwa hiyo Serikali muda wote imekuwa ikifanya tathmini hiyo.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile ipo mifuko ya halmashauri ambayo pia inatoa huduma kwenye vikundi vya wajasiriamali na mfuko huu wa maendeleo wa jimbo umeonesha ugumu wa utekelezaji kutokana na masharti yaliyowekwa, kwa nini sasa Serikali isione haja ya kuleta hii sheria ili iboreshwe ili kukidhi mahitaji ya akinamama, vijana na watu wenye ulemavu kama ambavyo wananchi wamekusudia? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Joseph Kizito Mhagama, Mbunge wa Jimbo la Madaba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimesema kwenye majibu yangu ya msingi, kwamba mfuko huu upo kisheria na ulianzishwa kisheria. Nachukua maoni ya Mheshimiwa Mhagama na tutaona ni namna gani tunakusanya maoni pia kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge wengine humu ndani kabla Serikali haijaanza mchakato wa kubadili sheria hii.
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa Wabunge wote wa Viti Maalum na Wabunge wa Majimbo wako sawa kwa mujibu wa Katiba. Je, Serikali haioni haja ya kuleta sheria ambayo itaruhusu Wabunge wa Viti Maalum waweze kupewa mfuko wa jimbo ili na wao waweze kushiriki katika maendeleo ya halmashauri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Salome Wycliffe Makamba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, pale tutakapoanza kukusanya maoni ya wadau ambao ni ninyi Waheshimiwa Wabunge kwa ajili ya kuona namna gani tunaleta katika Bunge lako hili Tukufu Mabadiliko ya Sheria hii ya Mfuko wa Jimbo, tutazingatia pia hili suala la Wabunge wa Viti Maalum.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Maweni, wananchi walijenga boma la kituo cha afya, miaka ya 2012, lakini mpaka sasaivi halijakamilishwa; je, nini kauli ya Serikali kuhakikisha kwamba boma hilo linaenda kukamilishwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Serikali ilitoa shilingi milioni 50 kwa ajili ya kukamilisha Zahanati ya Mhalala, Sasajila, Igose, Magasai na Mahaka; bahati mbaya zile fedha hazijatosha: Nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba zile zahanati zinakamilishwa ili ziweze kuanza kutoa huduma? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, la kwanza; kwenye Kata ya Maweni, ujenzi wa kituo cha afya ambapo boma limekamilika toka mwaka 2012, Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma haya ambayo yamejengwa na wananchi kwenye vituo vya afya na zahanati.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge, ameleta orodha hii ya zahanati ambazo anazitaja, na alinikabidhi mimi mwenyewe juzi hapa. Tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ta umaliziaji wa zahanati hizi, lakini kwa sasa kuna tathmini ambayo inafanyika kwa ajili ya ramani zile ambazo zilipelekwa mwanzoni kwenye majimbo mbalimbali hapa nchini kwa ajili ya ujenzi wa zahanati ili kuweza kujua ni kiasi gani sasa kinahitajika kwa ajili ya kumalizia.
MHE. ALMASI A. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniruhusu nami niulize swali la nyongeza kwa swali hili 226. Lini Serikali itaendeleza na kumalizia vituo viwili katika Kata za Usagali na Shitage? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kumalizia vituo vya afya hivi ambavyo amevitaja Mheshimiwa Mbunge na kadiri pale bajeti itakavyoruhusu, basi tutakwenda kuvimalizia.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika,
ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Napenda kuuliza, ni lini Kituo cha Afya Mwaya, kilichopo Tarafa ya Mwaya, Wilayani Ulanga, kitafanyiwa ukarabati? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni kipaumbele cha Serikali kufanya ukarabati kwenye vituo vya afya ambavyo ni vya muda mrefu na tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuweza kufanyiwa ukarabati kituo cha afya ambacho amekitaja Mheshimiwa Dkt. Ishengoma.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ni lini sasa Serikali itatekelea mapendekezo ya Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba ya ujenzi wa vituo vya afya katika Kata za Mwabomba na Bugando?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali imeshatafuta fedha ya kuweza kuangalia ujenzi au kuanza ujenzi wa vituo vya afya katika maeneo ya kimkakati hapa nchini. Tutaangalia vilevile Kwimba imetengewa kiasi gani kwa ajili ya kuanza ujenzi wa vituo vya afya hivi ambavyo Mheshimiwa Mbunge amevitaja.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kata ya Idodyandole, Kata ya Gondi na Kata ya Ipande ni kata kubwa sana, na tulileta mapendekezo: Je, lini Serikali itatoa pesa kwa ajili ya kituo hiki cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwa bahati nzuri, ni hivi karibuni tu Mheshimiwa Massare ameleta orodha hii ya kuomba vituo hivi vya afya na Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kwenda kujenga kituo cha afya kipya katika maeneo ambayo ameyataja.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Wananchi wa Kata ya Busangwa, Kijiji cha Mwanima, wameshaandaa eneo la ekari 15 kwa ajili ya ujenzi wa health center na tayari wameshaanza ufyatuaji: Nini mpango wa Serikali wa kuhakikisha kwamba wana-support kwa ajili ya kukamilisha mradi huu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba tunajenga vituo vya afya kwenye maeneo ya kimkakati. Tayari kuna fedha ambayo imeshatengwa kwa ajili ya ujenzi wa vituo hivi vya afya kwenye maeneo kama anavyotaja Mheshimiwa Mbunge hapa. Kwa Busangwa, tutaangalia kama eneo hili pia limetengewa kwenye mwaka wa fedha huu ambao tunaenda kuuanza.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Jengo la Tunduru Kusini, Kata ya Marumba, ni moja ya kata ya kimkakati kwa ajili ya kujenga kituo cha afya, ambayo ina umbali wa kilometa 80 kutoka Makao Makuu ya Halmashauri: Je, ni lini Serikali itapeleka pesa kwa ajili ya kujenga kituo cha afya katika Kata ya Marumba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nilisema hapo awali, tayari Serikali imetafuta fedha kwa ajili ya kujenga vituo vya afya vya kimkakati katika maeneo mbalimbali nchini. Tutaangalia pia Kata ya Marumba kama ipo imetengewa bajeti kwenye mwaka wa fedha unaokuja, kama haijatengewa, basi tutaitengea fedha kwenye ule mwaka mwingine wa fedha wa 2024/2025.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, Mbulu Vijijini tumeshaanzisha slogan ya kuhamasisha ujenzi wa vituo vya afya mimi na DC Kheri James. Tuna vituo vya afya vya Hayderer, Geterer, Masqaroda, Dinamu, Ladha, Endamilay na Maghang. Je, uko tayari sasa kupeleka fedha hizo ili kuzihamasisha juhudi za wananchi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa, Hospitali ya Halmashauri bado haijaisha na inahitaji Shilingi milioni 500 na Kituo cha Hydom hakina jengo la upasuaji: Je, ni lini utapeleka fedha hizo ambazo maombi yetu unayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la kwanza la nyongeza la lini Serikali itapeleka fedha kuunga mkono juhudi za wananchi za kujenga vituo vya afya; kwanza, nampongeza Mheshimiwa Mbunge na Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya, tumeona jitihada kubwa wanayoifanya katika kujenga vituo hivi vya afya. Serikali itajitahidi kadiri ya upatikanaji wa fedha kuweza kutenga bajeti kwa ajili ya kwenda kuongeza nguvu pale ambapo wananchi watakuwa wameishia.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, tayari Hospitali ya Wilaya imeshawekwa kwenye bajeti hii tunayoenda kuitekeleza ya 2023/2024, shilingi milioni 500. Fedha hizi zitakwenda kwa ajili ya ukamilishaji wa hospitali hiyo. (Makofi)
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Ujenzi wa Kituo cha Afya Kitaya umeshakamilika: Ni lini dawa na vifaa tiba vitapelekwa ili kianze kutoa huduma kwa wananchi wa Kitaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tayari Serikali imeanza kupeleka vifaa tiba kwenye vituo vya afya mbalimbali hapa nchini na Waheshimiwa Wabunge wengine watakuwa ni mashahidi, vifaa tiba vinavyoenda ni vile vya kisasa kabisa ambapo zamani vilikuwa vinapatikana kwenye Hospitali za Rufaa. Hii ni juhudi kubwa sana ya Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Katika kituo hiki cha afya ambacho amekitaja Mheshimiwa Mbunge, tutahakikisha vifaa tiba vya kisasa kabisa vinaenda pale kuweza kupeleka huduma karibu, kwa Watanzania.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, Jimbo la Kibaha Vijijini kwenye Kata ya Kwala, tulipokea pesa kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya; je, ni lini Serikali itamalizia fedha zilizobaki kwa ajili ya kukamilisha na kuanza kazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali inafanya tathmini ya vituo vya afya vyote vilivyopelekewa pesa na ambavyo havikukamilika. Pale tathmini itakapokamilika, basi tutatenga fedha kwa ajili ya kuweza kumalizia vituo hivi vya afya.
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza. Ni nini mkakati wa Serikali wa kujenga mabweni ya wasichana katika shule za sekondari za kata nchini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Je, katika shule hizo kumi ambazo mnajenga, ni nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha shule hizo zinafunguliwa ifikapo Julai, mwaka 2023? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI
ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimesema kwenye majibu yangu ya msingi, kwa sasa kipaumbele cha Serikali ni kujenga shule maalum hizi za bweni za wasichana katika kila mkoa katika nchi yetu hii. Hii itaenda kusaidia kupunguza dropout na mimba za utotoni, kwa sababu watoto wote katika mkoa ule wataenda kwenye shule hizi maalum.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, baadhi ya shule hizi ambazo zimejengwa, shilingi bilioni 30 imekwenda katika mikoa kumi kwa maana ya shilingi bilioni tatu kila Mkoa. Tayari baadhi ya shule hizi zimesajiliwa na ifikapo Julai mwaka huu 2023 shule hizi zote kumi zitaanza kupokea wanafunzi wa kike ili kuanza masomo yao ya sayansi katika maeneo hayo ambayo fedha imeshaenda.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Bweni la Sekondari ya Mlongwema ni dogo sana na halikidhi mahitaji kwa wanafunzi wale; je, Serikali ina mpango gani wa kujenga bweni kubwa ambalo linaweza kukidhi mahitaji ya wanafunzi wa Mlongwema? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni kipaumbele cha Serikali kujenga mabweni katika shule zote za A-Level. Tutakaa na Mheshimiwa Mbunge kuweza kuona shule hii ambayo ameitaja mahitaji hasa ni yapi ili tuweze kutafuta fedha ya kwenda kumalizia au kujenga mabweni mapya katika shule hiyo.
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Wananchi wa Jimbo la Kwela wamejitahidi kuanza kujenga mabweni katika Sekondari za Mpui, Mzindakaya, Milenia na Vuma. Je, ni lini Serikali mtaunga mkono jitihada hizi kwa kuwapelekea fedha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deus Clement Sangu, Mbunge wa Kwela, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali itapeleka fedha kuunga mkono juhudi za wananchi wa Kwela kwa kadiri ya upatikanaji wa fedha. Ni kipaumbele kuhakikisha kwamba tunajenga mabweni katika shule hizi ambazo hasa ni za A- Level katika maeneo mbalimbali hapa nchini.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Wananchi wa Kata ya Lumuli ambayo iko Jimbo la Kalenga, Mkoa wa Iringa, walijenga maboma kwa ajili ya mabweni ya watoto wa kike, kwa miaka 13 sasa hayajamaliziwa. Ni lini Serikali itamalizia mabweni haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyokuwa nimeshasema hapo awali, Serikali itamalizia mabweni haya, hata hili la Lumuli kule Kalenga, kwa kadiri ya upatikanaji wa fedha. Na tutaangalia katika mwaka huu wa fedha ambao tunakwenda kuuanza wa 2023/24 kama shule hii imetengewa fedha ili mabweni haya yaweze kukamilishwa na Serikali kuunga mkono juhudi za wananchi katika eneo hili.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali ambayo yanatia moyo, kuna barabara nyingine ndani ya Mkoa wetu wa Songwe ambazo zimekwama, kwa mfano barabara ya kutoka Mlowo – Itaka – Kamsamba na Barabara ya Mbalizi – Utengule mpaka Mkwajuni kule kwa Mheshimiwa Mulugo, zote hizo zina ahadi nyingi na ninaomba Serikali itilie mkazo zipate kutekelezwa.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Ranwell Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kujenga barabara hizi, hasa hizi alizozitaja Mheshimiwa Mbunge kwa kadiri ya upatikanaji wa fedha. Katika mwaka huu wa fedha tunaokwenda wa 2023/2024, Bunge lako tukufu limeiidhinishia TARURA zaidi ya shilingi bilioni 772 kwa ajili ya kutengeneza barabara mbalimbali hapa nchini, na ninaamini katika hizi barabara za Mlowo ambazo amezitaja Mheshimiwa Mbunge nazo zitawekwa katika kipaumbele cha mwaka huu wa fedha tunaokwenda kuutekeleza.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati barabara ambazo zimeathirika na mvua katika Jimbo la Mbagala?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Abdallah Jafari Chaurembo, Mbunge wa Mbagala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni mkakati wa Serikali kutengeneza barabara hizi na ndiyo maana TARURA walikuwa na emergency fund ya shilingi bilioni 11 na sasa wameomba tena nyongeza iweze kufika shilingi bilioni 46 kwa ajili ya kutengeneza barabara hizi za Mbagala na za maeneo mengine ya Waheshimiwa Wabunge ambayo yameathiriwa na mvua ambazo zimeendelea kunyesha hapa nchini.
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa niulize swali dogo la nyongeza. kwa kuwa Mji wa Makambako ni mji mkubwa unaokuwa kwa kasi na unaunganisha nchi ya Zambia na nchi jirani ya Congo. Ni utaratibu upi wa haraka utakaofanyika kuhakikisha hayo majibu ya Mheshimiwa Waziri yatakamilika kwa muda muafaka ili wananchi wa Makambako wapate huduma iliyo bora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Mji wa Makambako upo katika Tier III katika mradi huu wa TACTIC. Tier One, ndiyo sasa wakandarasi wamepatikana, michakato imekamilika na wanakaribia kusaini mikataba ya kuanza kazi na wale wa Tier II design ya miradi ndiyo inafanyika hivi sasa tunavyozungumza, na tayari wale consultants wamepatikana. Hii Tier III ambayo Mji wa Makambako upo, nayo wanapatikana wataalam kwa ajili ya kuangalia Master Plan na feasibility study ya mji ule. Kwa hiyo, muda siyo mrefu mradi huu utaanza pale katika Mji wa Makambako.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nina swali moja la nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri. Kwa kuwa jengo hili la Halmashauri ya Bagamoyo limejengwa toka miaka ya 1970, na sasa hivi linavuja, nyaraka nyingi zinaloa na Mkurugenzi anapata shida kufanya kazi na wafanyakazi wake ambao wako katika maeneo tofauti tofauti: Je, Serikali haioni umuhimu katika bajeti ya mwaka huu kutuongezea pesa kuanza ujenzi huo mara moja, kwa sababu, mapato yetu ya Halmashauri ni madogo sana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni kweli jengo la Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo linalotumika sasa ni la muda mrefu. Kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, wao wenyewe Halmashauri walitenga fedha, shilingi milioni 500 kwenye mapato yao ya ndani na katika bajeti ya mwaka wa fedha unaokuja vilevile wametenga tena shilingi milioni 500.

Mheshimiwa Spika, vilevile wao wameenda na mchoro ambao utatumia zaidi ya shilingi bilioni 5.34, lakini mchoro ule uliotolewa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ulikuwa una gharama ya shlingi bilioni 2.7 tu. Kwa hiyo, inaonesha wao walikuwa wana uwezo wa kujijengea jengo lao wenyewe na kutenga hizi fedha kwa sababu walichagua mchoro wa ghorofa mbili badala ya ghorofa moja, naomba kuwasilisha.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Shule ya Sekondari ya Igwachanya kuna boma la bwalo ambalo limejengwa kwa nguvu za wananchi takribani miaka kumi sasa. Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Jafo alipita akaahidi kupeleka pesa, na vilevile Mheshimiwa Bashungwa alipita tena akaahidi kupeleka pes: Je, lini mtapeleka pesa hizo zaidi ya Shilingi milioni 200 ili ziweze kukamilisha bwalo lile la Shule ya Sekondari ya Igwachanya?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Kuna Shule ya Msingi ya Saja, Usuka na Udonja, ziko kwenye hali mbaya sana, miundombinu yake ni chakavu sana: Je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha kwamba shule zile zinakarabatiwa na kuwa bora kama shule nyingine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu swali lake la kwanza la boma la bwalo katika shule hii ya sekondari ambayo ameitaja Mheshimiwa Neema, Serikali itaendelea kutafuta fedha na kuweka kipaumbele katika kumalizia bwalo hili. Kama alivyosema yeye, ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Hivyo tutakaa na wataalam wetu kuona tutapata wapi fedha kuweza kwenda kumalizia mabwalo haya.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, la shule hizi za msingi ambazo ni chakavu, Mheshimiwa Mbunge amezitaja; Serikali inaendelea kufanya ukarabati wa miundombinu ya shule za msingi na ninyi Waheshimiwa Wabunge humu ndani mtakuwa ni mashahidi, kuna zaidi ya Shilingi bilioni 230 ya mradi wa boost ambayo tayari fedha zile zimeshakuwa disbursed katika shule hizi kwa ajili ya kuanza ukarabati na ujenzi wa miundombinu mipya katika shule hizi za msingi na ni nchi nzima.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nawashukuru sana TAMISEMI kwa kazi wanazozifanya katika Jimbo la Ushetu. Tumepokea vifaa vya meno na x-ray, lakini hatuna wataalamu wa meno na mtaalamu wa mionzi: Je, katika ajira hizi 8,000 tutapatiwa hao wataalamu wa mionzi kwa ajili ya kuwahudumia wananchi wa Jimbo la Ushetu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Nina Zahanati ya Bugomba A, Elias Kwandikwa, Bugera, Manungu pamoja na Makongoro, zina watumishi wawili wawili tu, inafika mahali Jumapili na Jumamosi wanafunga kwa ajili ya kupumzika. Katika watumishi hawa 8,000, na hizi zahanati zitapata watimishi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa
Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cherehani, swali lake la kwanza la wataalamu wa meno na mionzi, kwa sasa Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ina timu ambayo inazunguka katika Halmashauri mbalimbali zilizopokea vifaa tiba kwa ajili ya kutoa mafunzo kwa wataalamu wetu kule kuweza kujua namna ya kutumia vifaa hivi vya kisasa vinavyokwenda. Kwa hawa wataalam wa meno na wa mionzi, tutahakikisha kwamba hospitali hii pia inapata wataalamu hawa kwenda kusaidia wananchi wa kule Ushetu.

Mheshimiwa Spika, nikijibu kwenye swali lake la pili, kama ambavyo nimesema kwenye majibu yangu ya msingi, hawa watumshi 8,070 ni katika upungufu uliopo nchi nzima, ikiwepo kule Ushetu. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Ushetu nayo itapokea watumishi hawa wa afya.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kituo cha Afya Nkwenda na Hospitali ya Wilaya ya Kyerwa ina upungufu mkubwa wa watumishi. Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi na vifaa tiba ili kuondoa adha wanayoipata wananchi wa Jimbo la Kyerwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, katika hawa watumishi 8,070 ambao Serikali itaajiri hivi punde, tutahakikisha Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa nayo inapata watumishi hawa. Kwenye vifaa tiba, Serikali ilikuwa imeshatoa shilingi bilioni 34 nchi nzima katika kuhakikisha hospitali hizi za Wilaya zinapata vifaa tiba na tutaangalia pia kama hospitali ya Wilaya ya Kyerwa imo na kama haimo, basi itaingia katika mwaka wa fedha ambao unafuata.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza. Kata ya Ndanda wananchi walijitolea, lakini pia walishiriki na nguvu ya Ofisi ya Mbunge kwa maana ya Mfuko wa Jimbo, kukamilisha Kituo cha Afya baada ya kupata pesa Shilingi milioni 50 kutoka Serikali Kuu. Sasa hivi limebaki suala moja tu ili iweze kufunguliwa, ambalo ni choo. Mheshimiwa Waziri yuko tayari kutoa maelekezo kwa DED wa Halmashauri ya Wilaya ya Masasi, DC, wakamilishe choo hicho ili zahanati ianze kutumika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwanza nikiri mbele ya Bunge lako hili kwamba Mheshimiwa Mwambe alishakuja kulifuatilia jambo hili ofisini kwa karibu kabisa. Nitumie nafasi hii kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kumwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha anajenga choo hiki kupitia mapato yake ya ndani ili huduma ziweze kuanza kutolewa katika kituo hiki.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naitwa Aloyce John Kamamba.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tunaishukuru Serikali kwamba imekamilisha ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Kakonko, lakini tuna upungufu mkubwa wa watumishi na vifaa tiba. Lini Serikali itapeleka watumishi na vifaa tiba katika hospitali yetu ya Wilaya ya Kakonko? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, Serikali inaajiri watumishi wa afya 8,070, na katika hawa ambao wataajiriwa, Hospitali ya Wilaya ya Kakonko nayo itapata watumishi hawa.

Mheshimiwa Spuika, kwenye vifaa tiba, vilevile Serikali imetenga zaidi ya Shlingi bilioni 34 ambazo zimeshakwenda kwa wenzetu wa MSD kwa ajili ya kupeleka vifaa tiba kwenye hospitali za Wilaya mbalimbali hapa nchini na tutaangalia kama Hospitali ya Wilaya ya Kakonko nayo ipo, kama haipo tutaiweka katika mwaka wa fedha unaofuata.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali; lakini pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina swali dogo moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunashukuru na kupongeza mpango wa TARURA kwamba taa hizo zilizozungumzwa zimefungwa kwenye barabara ya mtandao wa TARURA ambayo ziko pembezoni mwa mji. Lakini kuna barabara ya TANROADS ambayo inapita katikati ya mji ambapo ndipo sura ya Tunduru Mjini. Je, ni lini Serikali itatufungia taa za barabarani kwenye barabara ile ya TANROADS? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kuhususiana na barabara hii ya TANROADS ambayo inapita katikati ya Mji wa Tunduru, nafahamu wenzetu wa TANROADS wana mkakati wa kufunga taa katika barabara zote zinazopita katika makao makuu ya wilaya nchi nzima si kwa Tunduru peke yake kwa sababu tayari za TARURA kuanzia sasa barabara yote ya lami inayojengwa na TARURA lazima ifungwe taa; hivyo hivyo na wenzetu wa TANROADS nao wameweka mkakati huo wa kuhakikisha barabara zote kubwa zinawekewa taa.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika barabara muhimu kiuchumi kutoka Kalenga kwenda Uwasa imeharibika sana eneo moja la Kiponzelo.

Je TARURA inampango gani wa dharura kuweza kutupa fedha kwa ajili ya kurekebisha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa barabara hizi ambazo zimeathirika sana kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha nchini TARURA ilikuwa na bajeti ya bilioni 11 kwa ajili ya dharura lakini sasa wameomba fedha iweze kuongezwa kutoka bilioni 11 na kwenda bilioni 46 ili kuweza kutengeneza barabara mbalimbali nchini ikiwemo za Kalenga kule kwa Mheshimiwa Kiswaga.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itafunga taa za barabarani katika Mji wa Kakonko?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara za Kakonko anazozizungumzia Mheshimiwa Mbunge pale ni kama lilivyokuwa swali la kwanza la Tunduru Mjini ni barabara ya TANROADS na tayari ni mkakati wa TANROADS kuhakikisha kwamba wanafunga barabara katika barabara zote zinazopita makao makuu ya wilaya, na hivi karibuni zoezi hilo litaanza.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Namshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Nimuulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa daraja la Mto Tungu ni muhimu sana Wilaya ya Maswa, inaunganisha Maswa na Kishapu.

a) Je, ni lini Serikali itatenga pesa za kujenga daraja hilo?

b) Je, ni lini Serikali itajenga Daraja la Sandai, Wilaya ya Itilima kwenda Hospitali ya Wilaya ya Nkolo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kipaumbele cha Serikali kupia TARURA kuhakikisha kwamba barabara zote zinazounga wilaya na wilaya zinapata huduma bora ya barabara, na barabara hii ambayo Mto Tungu umepita inayounganisha Wilaya ya Kishapu na Maswa nayo itatengewa fedha kwa ajili ya kuweza kujenga daraja hii ili iweze kupitika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali lake la pili la barabara ya Saadaye-Nkolo, hii barabara inaelekea katika hospitali kama sikosei nimeshawahi kupita maeneo hayo, na ni kipaumbele cha Serikali kuhakikisha kwamba barabara hii inatengenezwa vilevile ili wananchi waweze kuapata huduma ya afya katika hospitali ya mission iliyokuwepo kule. Kwa hiyo tutatenga fedha kuhakikisha kwamba barabara hii inatengenezwa.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je ni lini Serikali itajenga Daraja la Unguuni katika Kata ya Nduruma ambayo imeshafanyiwa upembuzi yakinifu na TARURA na sasa wananchi wanateseka hasa katika kipindi hiki cha mvua na mafuriko yanayowasumbua wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, daraja hili la Kata ya Nduruma tutaangalia kama lipo kwenye bajeti ya mwaka huu ambayo imeshapitishwa lako Tukufu kwa Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (TARURA). Kama haipo basi tutahakikisha inatengewa fedha katika mwaka wa fedha unaofuata.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa. Ni lini Serikali itajenga daraja la kutoka Itununu kwenda Igodi kafu ambayo ni Jimbo la Isimani kuhakikisha kwamba wananchi wanaweza wakapata huduma ya kwenda kwenye Hospitali ya Wilaya na wanafunzi wanashindwa kwenda shule?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itajenga barabara hii ya Itununu kwenda Igodi Kafu kadiri ya upatikanaji wa fedha. Na kwa sababu kuna huduma muhimu kama ya shule na vilevile kituo cha afya ambapo wananchi wanapata huduma basi tutaiangalia na kuiwekea kipaumbele ili barabara hii nayo iweze kutengenezwa.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Ni lini Serikali itatoa fedha kujenga Daraja la Mto Ruvuma kati ya Lusomba -Magabula kwa Mheshimiwa Jenista Mhagama hadi Iyale ambapo Mheshimiwa Jenista tumehangaikia sana hili daraja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itajenga daraja hili la Lusonga hadi Liyanja kadri ya upatikanaji wa fedha; na tutaangalia kama imetengewa fedha katika mwaka huu wa fedha ambao tumepitishiwa ili tuweze kwenda kuweka kipaumbele katika daraja hili ili wananchi waweze kupata huduma hiyo.
MHE. TECLA M. UNGELE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa majibu ya Serikali. Nina maswali mawili ya nyongeza.

a) Je, ni lini malambo ya kunyweshea maji mifugo hiyo yatajengwa maeneo ya Ngunichile, Kibutuka na Njilinji ili kuondoa migogoro hiyo?

b) Je, ni lini utengaji wa ardhi utafanyika katika maeneo ambayo kunatokea vifo na migogoro hiyo hususani Kibutuka na Njilinji, Ngunichile Natekwe na kwingineko?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali lake la kwanza Mheshimiwa Ungele tutashirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuweza kuona ni namna gani tutajenga kwa haraka sana haya malambo ya maji Mtekwe na Kimambi kuhakikisha kwamba mifugo iliyokuwepo kule inaweza kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, kuhusu upangaji wa ardhi, sheria zipo wazi, kuna Sheria Namba Tano ya Ardhi ya mwaka 1999 Toleo la 2002 juu ya matumizi bora ya ardhi ambapo inatoa mamlaka kwa vijiji kupanga matumizi bora ya ardhi ambapo wanatakiwa kutenga malisho, maeneo ya masoko, mashamba na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nichukue nafasi hii kwenye Bunge lako tukufu kuwaomba na kuwaasa viongozi katika halmashauri zetu nchini ikiwemo Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi kuhakikisha wanasimamia sheria hii kwa kupanga matumizi bora ya ardhi ili kuepuka mogogoro ya ardhi na hasa ile ya wakulima na wafugaji.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza. Pamoja na kutengewa fedha, shilingi milioni 900 hali ya hospitali ile ni mbaya na fedha hiyo ni ndogo. Serikali iko tayari kuwaahidi wananchi wa Handeni Mjini kwamba itaendelea na utaratibu wa kupoteza fedha hizi kila mwaka ili hospitali hii ifanyiwe ukarabati yote? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Wananchi wa Handeni Mjini, kama walivyo wananchi wa Korogwe Vijijini, wamejenga sana zahanati, maboma yamesimama na hayajakamilika; Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inayamalizia na kuyakamilisha maboma yote ya zahanati nchini ambayo wananchi wameyajenga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza, la kwanza kwamba fedha ni ndogo; fedha hii inatengwa na Serikali kuhakikisha wanafanya ukarabati wa yale majengo ambayo yalikuwepo toka zamani. Kwa mfano, nikisema kwenye Hospitali hii ya Handeni Mjini, wao walitaka kujenga hospitali mpya kabisa ya wilaya, lakini fedha iliyotengwa ilikuwa ni kwa ajili ya ukarabati wa majengo yaliyopo. Tutaendelea kutafuta fedha na kuhakikisha kwamba tunaendelea kupeleka fedha kwenye Halmashauri hizi kwa ajili ya ukarabati zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la kumalizia zahanati, nyote ni mashahidi humu ndani, katika majimbo yetu na Halmashauri zetu, Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, imekuwa ikileta fedha shilingi milioni 50 za kumalizia zahanati na tutaendelea kutafuta fedha, na kadri ya upatikanaji wa fedha hizo basi tutaendelea kuleta katika majimbo hayo kuweza kumalizia zahanati ambazo zimejengwa kwa nguvu ya wananchi.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, Kata ya Lutende ambayo unasema mmetenga shilingi milioni 300 ambayo itaenda kumalizia kituo cha afya, fedha hiyo haijaenda mpaka siku ya leo; je, ni lini fedha hiyo itakwenda kumalizia Kituo cha Afya cha Kata ya Lutende?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Wananchi wa Kata ya Igalula wamejenga boma la wodi ya kulazia wagonjwa na Serikali imeleta fedha nyingi na tumenunua vitanda, hakuna sehemu ya kuvipeleka; je, Serikali haioni haja ya kupeleka fedha kumalizia wodi hiyo kwa sababu operation mpaka sasa hivi ni 27 hakuna sehemu ya kuwalaza? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Venant, la kwanza fedha hii shilingi milioni 300 katika Kituo cha Afya Lutende, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi kwamba ilikuwa ni kwenye mwaka wa fedha ambao umepita, sasa nitakaa na Mheshimiwa Mbunge tuweze kuona nini kilitokea hata fedha hii mpaka sasa haijafika, na kama kuna mkwamo wowote, basi tutashirikiana kwa pamoja kuhakikisha kwamba fedha hii inafika katika Kituo cha Afya cha Lutende.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la Igalula, fedha ya kukamilisha wodi. Serikali itaendelea kutoa fedha kadiri ya upatikanaji ili kukamilisha majengo mbalimbali kwenye vituo vya afya, zahanati na hospitali za wilaya kote nchini. Kwa hiyo, fedha itakapopatikana, basi tutahakikisha Kituo cha Afya Igalula nacho kinapata fedha.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, hii barabara ili ilete tija inayokusudiwa, ni muhimu kufungua barabara ya Mashaw - Waranga, barabara ya Masusu – Gisambalang – Mhanda; je, Serikali iko tayari kutenga fedha haraka ili barabara ziweze kufunguliwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Wilaya ya Hanang’ ina maeneo mengi ambapo mvua ikinyesha yanakuwa kama kisiwa. Mfano Mara, Uteshi, Merekwa, Gaulol, Ghetaghul na Gijetamogh; je, Serikali haioni ni wakati muafaka sasa kuingozea TARURA Wilaya ya Hanang’ bajeti?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza; la kwanza, hii barabara ambayo ameitaja ya Marang, Masusu, Gisambalang na maeneo ya kule Hanang’ Serikali itaendelea kutenga fedha kadiri ya upatikanaji wa fedha hizi. Vile vile kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, barabara hii ilikuwa ni ya kupita mifugo (Pario). Kwa jitihada kubwa za Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na TARURA kuongezewa fedha, imeanza kufunguliwa na sasa zaidi ya kilometa 30 tayari zimetengenezwa na kadiri miaka inavyokwenda tutazidi kuhakikisha barabara hii inafunguliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la barabara hii za Katesh, Berekwa na maeneo yale ya kule Hanang ambayo ameyataja Mheshimiwa Hhayuma, TARURA kwa mwaka wa fedha huu unaomalizika ilitengewa shilingi bilioni 2.33 kwa Wilaya ya Hanang peke yake. Hii ni zaidi ya mara tatu ya bajeti ambayo ilikuwa 2020/2021 ya barabara katika Wilaya ya Hanang’. Hivyo Mheshimiwa Mbunge awe tu imani kwamba katika bajeti inayofuata hii, vilevile TARURA wametengewa bajeti hiyo hiyo ya shilingi bilioni 2.33 kule Wilaya ya Hanang na barabara nyingi zitafunguliwa kuhakikisha kwamba wananchi wake kule wanapita bila matatizo yoyote.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali pamoja na kupeleka fedha ile shilingi milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni na kazi inaendelea bado kuna uhitaji wa walimu pindi kazi itakapokuwa imekamilika. Vilevile kuna uhitaji wa uzio ili kuweza kuweka usalama kwa watoto hao wenye mahitaji maalum. Je Serikali ina mpango gani wa kupeleka fedha hizo na walimu pindi kazi itakapokamilika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; je, Mheshimiwa Naibu Waziri uko tayari kufanya ziara katika Jimbo la Morogoro Kusini na kuandamana na mimi ili kwenda kuangalia mahitaji mengine ya elimu na afya katika halmashauri yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu maswali yake haya mawili kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge Mheshimiwa Kalogeris kwa sababu jambo hili ni wiki iliyopita tu alikuja kulifatilia pale ofisini kuhakikisha kwamba wanapata walimu. Nimuhakikishie mbele ya Bunge lako Tukufu nikijibu swali lake la kwanza kwamba katika ajira hizi ambazo zimetolewa kibali na Mheshimiwa Rais kuweza kuajiri tutahakikisha shule hii kwa sababu ni watoto wenye mahitaji maalum wanapata walimu wa kuweza kuwafundisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili nipo tayari kuongozana na Mheshimiwa Mbunge mpaka kwenda Jimbo Lake la Morogoro Kusini kwenda kuitembelea shule hii na tuone ni nini kinaweza kikafanyika na Serikali kwa ajili ya kujenga uzio ambao ameuzungumzia Mheshimiwa Mbunge pale.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, majibu yaliyotolewa na Serikali yamejielekeza kwenye barabara ndogo iliyokuwepo wakati swali langu lilikuwa ni kutaka barabara kubwa ili malori yasipite mjin,i (barabara ya pete), kwa hiyo nina maswali mawili ya nyongeza.

Je, Serikali iko tayari kujenga barabara ya pete kutoka Kigwa B kwenda Magiri ili kuepusha magari makubwa yanayokwenda Burundi na Rwanda kupita Mjini na kuharibu barabara za Mjini?

Swali la pili, kwa vile Miji yote inayojengwa sasa ina barabara za pete pamoja na Jiji letu la Dodoma na Mji mdogo wa Nzega. Je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga barabara za pete kuzunguka Mji wa Tabora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Athuman Almas Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iko tayari kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami kadiri ya upatikanaji wa fedha, lakini tayari katika bajeti hii ya 2023/2024 TARURA imetenga fedha ya kufanya upembuzi yakinifu kujua gharama jumla itakuwa ni kiasi gani kwa ajili ya ujenzi wa lami wa barabara hii. Hivi ilivyo sasa bado ina uwezo wa kubeba malori na ndiyo maana tunaifanyia periodic maintenance.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusu barabara za pete (ring roads); Serikali iko tayari kujenga barabara ya pete (ring road) katika Mji wa Tabora, tunashirikiana na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi kuweza kuona tunaanzaje mchakato wa kufanya feasibility study ili Mji huu wa Tabora uweze kupata barabara hiyo ya pete.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna shule katika Mji wetu wa Tarime inaitwa Bugosi, ina zaidi ya wanafunzi 1,000 lakini ina madarasa Sita na wananchi wamejitahidi sana kujenga lakini jitihada za Serikali kuwatia nguvu inakuwa ni kidogo: -

Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kujenga madarasa ya kutosha katika shule hii? (Makofi)

Swali langu la pili, zipo jitihada za wananchi wanazofanya kuhakikisha kwamba wanajenga shule mpya. Kwa mfano katika Kata ya Kenyamanyori kuna Shule zinaitwa Chira, Nyamitembe na shule nyingine ambazo zimejengwa na zimefika katika hatua ya upauaji lakini Serikali haijapeleka fedha kwa ajili ya kumalizia na shule zile zifunguliwe: -

Je, ni lini fedha zitapelekwa ili majengo yale yakamilike na wanafunzi waweze kusoma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Kembaki.

Swali lake la kwanza kwenye hule hii ya Bugosi yenye wanafunzi zaidi ya 1,000 na madarasa Sita, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, kwamba tunapeleka shilingi bilioni 1.5 katika Halmashauri ya Mji wa Tarime kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa shule hizi kupunguza msongamano. Kwa hiyo Serikali iko tayari kupeleka fedha na tayari imeshatengewa.

Swali lake la pili, kwenye Kata hii ya Kenyamanyori, nitaa na Mheshimiwa Kembaki tuweze kuangalia upungufu ambao upo katika shule hizi alizozitaja za vijiji vya Kata hii, ili tuone ni namna gani tunaweza tukafanya kuweza kukarabati shule hizi ama kuongeza madarasa.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shule ya Msingi Kizota ambayo iko katika Jiji la Dodoma ni miongoni mwa shule ambazo zina wanafunzi wengi sana na hivyo kusababisha wanafunzi kuingia kwa zamu.

Nini mkakati wa Serikali wa kujenga shule katika eneo la mnada mpya ambapo hakuna shule kabisa kwa sababu watoto wengi wanatokea eneo lile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ipo tayari kujenga shule nyingi kwa wakazi wa kule Kizota kadri ya upatikanaji wa fedha. Tutaangalia katika mradi huu wa BOOST ambao Waheshimiwa Wabunge ninyi ni mashuhuda, fedha nyingi sana imetolewa na Serikali hii ya awamu ya Sita kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa shule tuone ni namna gani tunaweza tukafanya kwa ajili ya wakazi wa Kizota wapate shule nyingine na wanafunzi waache kwenda kwa zamu pale.
MHE. MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa barabara nyingi za Jiji la Dar es Salaam, hasa zile zilizo chini ya TARURA huhitaji matengenezo ya mara kwa mara. Je, Serikali haioni ipo haja kwa TARURA kuwa na kitengo maalum cha matengenezo badala ya kuwatumia Wakandarasi?

Swali la pili, kwa kuwa Jimbo la Kinondoni linazungukwa na mito midogo midogo ambayo husababisha mafuriko hasa katika Kata za Mwanayamala, Kijitonyama, Tandale, Kigogo na Ndugumbi. Je, Serikali ipo tayari kufanya upembuzi wa kitaalam ili kubaini njia bora za kukabiliana na hali hii ya mafuriko?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la kwanza la Mheshimiwa Tarimba la je, TARURA ipo tayari kuanzisha kitengo maalum kwa ajili ya kuangalia ukarabati wa barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuanzisha kitengo maalum kunahitaji rasilimali fedha, rasilimali watu na vifaa. Hivyo basi, kwa sasa TARURA inaona ni bora kufanya outsourcing kwa sekta binafsi. Hii pia inasaidia kutoa ajira kwa Watanzania wengine ambao wanafanya kazi katika sekta binafsi. Vilevile ina-assure quality control na kunakuwa kuna checks and balances akipewa mtu na TARURA wakamkagua.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, tayari mito ya Jimbo la Kinondoni imetengewa fedha kwenye Mradi wa DMDP II ambao utaanza Novemba, mwaka huu 2023. Kwenye DMDP I tayari walikuwa wameshatengenezewa Mto Ng’ombe ambayo imezuia mafuriko makubwa sana katika maeneo yanayozunguka barabara hizi na makazi ya watu wa Jimbo la Kinondoni.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Wakati Kinondoni wanaomba fedha kwa ajili ya kujengewa lami, Wilaya ya Makete na Mkoa wa Njombe tunaomba fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara za changarawe kwenye barabara ya kutoka Kinyika – Kikondo – Nkenja – Ikuwo, barabara ambazo zimeharibika sana kutokana na mvua nyingi zinazoendelea Jimboni Makete.

Je, Serikali itafanya nini itusaidie tupate fedha hizo kwa sababu barabara hizi ni barabara za uzalishaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mwaka wa fedha huu Bunge lako tukufu limeipitishia TARURA bajeti ya zaidi ya bilioni 772 tutaangalia barabara hii ya Kinyika – Kikondo katika Jimbo la Makete kule kama nayo imetengewa fedha kwenye bajeti hii. Kama haijatengewa fedha tutaangalia mwaka wa fedha unaofuata tuweze kutenga fedha kwenye bajeti kutengeneza barabara hii.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Wananchi wa Wilaya ya Tanganyika wanapakana na Wilaya ya Nkasi Kusini na upande wa Kaskazini wanapakana na Wilaya ya Uvinza. Maeneo haya kwa wananchi wanaoishi mwambao wa Ziwa hawana njia mbadala tofauti na njia ya majini.

Je, ni lini Serikali wataongeza bajeti kwa upande wa TARURA ili tuzifungue hizi njia tuepushe maafa kwa wananchi na mali zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ni lengo la Serikali kuiongezea TARURA fedha. Kama mlivyo mashahidi, mwaka wa fedha 2021/2022 bajeti ya TARURA nchi nzima ilikuwa shilingi bilioni 228, lakini baada ya bajeti ya 2021/2022 chini ya uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, TARURA imeongezewa fedha zaidi ya mara tatu kwenda shilingi bilioni 772. Tutaangalia hizi barabara zinazounganisha Tanganyika, Nkasi na Uvinza ili ziweze kupata fedha na kutengenezwa, kadri ya fedha itakavyopatikana.
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafsi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Barabara ya Banana – Kitunda – Kivule – Msongola inatajwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ukurasa wa 78, kilometa 11.5, na mpaka sasa Serikali imetenga kilometa 2.2 tu. Ni lini Serikali sasa itatenga fedha za kumalizia kilometa 9.3 ili kutekeleza ahadi iliyoko kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2020? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ambayo ameitaja Mheshimiwa Mbunge ya Msongola ya kilometa 2.2 ambayo ndiyo imetengewa fedha, tayari nilikaa na Mheshimiwa Mbunge, alikuja kulifuatilia na lenyewe na tukakaa na wataalam wa TARURA kuhakikisha kwamba tunaona ni namna gani tunapata fedha hii ya kilometa 9.3 iliyosalia kama ambavyo iliahidiwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakaa kuangalia tunafanya vipi ili fedha hizi ziweze kupatikana na barabara hii iweze kutengenezwa.
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Barabara ya Suka – Golani ambayo ilianza kujengwa mwaka jana, kilometa nane zimeshajengwa mita 400 lakini imesimama baada ya flow ya fedha kushuka.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza akaahidi hapa kwamba mwaka huu flow ya fedha itakuwa nzuri kwa barabara hii ili wananchi wahakikishiwe kwamba barabara inakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, baraba hii ya Suka – Golani kama ambavyo nimeshasema hapa kwenye baadhi ya maswali niliyoulizwa, kwamba TARURA imeongezewa fedha sasa na tutaangalia kupitia Meneja wa TARURA katika Mkoa wa Dar es Salaam na Wilaya ya Ubungo kuona ni namna gani katika bajeti ambayo ameitenga barabara hii itaweza kuendelea kufanyiwa matengenezo.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona.

Katika Jimbo letu la Kilwa Kaskazini lina mtandao wa barabara za TARURA kilometa 528 ambazo zote ni za vumbi. Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hizo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia TARURA itaanza kujenga barabara za lami katika Jimbo la Kilwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Ninarudia tena tayari TARURA imeongezewa bajeti na Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan, tutaangalia na Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Lindi na Wilaya ya Kilwa kuona katika bajeti ambayo imepitishwa hapa ni kilometa ngapi ya lami ambayo imetengwa ili katika hizi barabara za Kilwa alizotaja Mheshimiwa Ndulane angalau moja ianze kupata lami.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Kigamboni ina mtandao wa barabara za TARURA takribani kilometa 1,000, lakini ni kilometa tano tu ambayo ni asilimia 0.5 percent ambazo zina kiwango cha lami. Bajeti ya TARURA pale ni shilingi bilioni 3.5.

Je, nini mkakati wa TARURA kuongeza bajeti ili barabara za Wilaya ya Kigamboni zifanane na barabara nyingine za Jiji la Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia TARURA itaendelea kuongeza fedha katika Wilaya ya Kigamboni na Jimbo la Kigamboni kwa Mheshimiwa Ndugulile kadri ya upatikanaji wa fedha. Ni lengo la Serikali hii ya Awamu ya Sita kuhakikisha TARURA inakuwa na nguvu ya kutosha kutengeneza barabara nyingi zaidi za lami katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu ikiwemo kule Kigamboni.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Akheri inayoanzia Sangisi kwenda Ndoombo ilikuwa ni ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne kujengwa kwa kiwango cha lami miaka kumi iliyopita. Mwaka jana barabara hiyo imeanza kujengwa: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuimalizia mwaka huu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ya Akheri – Sangisi ambayo ameitaja Mheshimiwa Dkt. Pallangyo hapa ambayo tayari imeshaanza kuwekewa lami itaendelea kuwekewa lami kwa sababu ni ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kadri ya upatikanaji wa fedha na tutaendelea kuitengea bajeti kwenye miaka ya fedha ambayo inafuata.
MHE. JOHN M. SALLU: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, lakini kule kwenye Tarafa ya Kwamsisi ni tarafa iliyoko pembezoni sana. Sasa ni lini Serikali itaona umuhimu wa kujenga Kituo cha Afya katika Kata ya Kwa Msisi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Handeni Vijijini tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi, takribani tuna upungufu wa zaidi ya asilimia 60. Sasa je, ni mkakati gani wa Serikali katika kupambana na upungufu huo wa watumishi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA YA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la kwanza la Tarafa ya Kwamsisi ni lini itapata kituo cha afya; nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge katika mwaka wa fedha 2024/2025, tarafa hii na Kata ya Kwa Msisi itatengewa fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya.

Mheshimiwa Spika, nikienda katika swali lake la pili la upungufu wa watumishi, kama ambavyo wote ni mashahidi katika Bunge lako hili tukufu, Serikali inaendelea kuajiri na hivi sasa kuna ajira zaidi ya 21,000 ambazo zimetangazwa na Serikali itaendelea kuajiri vile vile kadri ya uwezo wake wa kibajeti na katika hawa watumishi 21,000 ambao wanaajiriwa hivi karibuni vile vile Handeni Vijijini watapata watumishi.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kumuuliza Mheshimiwa Waziri, maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Serikali, lakini ni ukweli usiofichika kwamba mazingira ya walimu wetu kwa maeneo ya vijijini ni tofauti kabisa na maeneo ya mjini. Sasa kumekuwa na upungufu mkubwa wa walimu wa kike kutokana na mazingira hususan kwenye halmashauri ama majimbo ama wilaya za vijijini.

Swali langu la kwanza; je, ni lini Serikali itaanza kulipa posho kwa ajili ya mazingira magumu kwa walimu wetu Tanzania, hususan wa kike? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kutokana na upungufu mkubwa wa walimu, Wilaya ya Chemba tuna shule zaidi ya sita ambazo wanafunzi wameshindwa kuendelea na masomo, hatuna walimu. Shule hizo ni Shule ya Magarasta Sanzawa, Mialo Kwa Mtoro, Hanaa Gwandi, Magandi Soya, Mkandinde Soya pamoja na Lugoba Kata ya Kimaha.

Je, ni lini Serikali itapeleka walimu hawa ili watoto wetu kwenye shule hizi sita waanze masomo ili na wao waweze kutumiza haki yao ya kikatiba? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA YA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge; swali lake kwanza la mazingira, Serikali hakuna incentive maalum ya mazingira na hivi sasa Serikali inaandaa mwongozo kwa ajili ya posho ya masaa ya ziada. Incentive kubwa ambayo inatolewa na Serikali kwa sasa ni kuhakikisha kwamba inaweka mazingira bora kwa kujenga nyumba, kutengeneza miundombinu ya barabara, kuvuta umeme kwenye vijiji vyote vya nchi yetu hii ambayo nayo inatengeneza mazingira bora kwa watumishi wetu kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, nikijibu swali lake la pili, Mheshimiwa Mbunge la maeneo haya ambayo ni Sanzawa, Gwandi, Soya ni lini yapata watumishi. Kama nilivyosema hapo awali Serikali imetangaza ajira zaidi ya 21,000 ambapo katika ajira hizi za Walimu na maeneo haya yaliyotajwa nayo yatapata. Nimueleze tu Mheshimiwa Mbunge kwamba katika ajira za mwaka uliopita, Halmashauri ya Wilaya ya Chemba ndio ilipata Walimu wengi zaidi wa kike katika Mkoa huu wa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mkoa wa Simiyu una upungufu sana wa walimu kwa upande wa sekondari na shule ya msingi. Walimu wa kike ni wachache sana na shule zingine hazina kabisa walimu wa kike.

Je, Serikali ina mpango kutuletea walimu wa kike katika Mkoa wa Simiyu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA YA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tayari Ofisi ya Rais, TAMISEMI ilishatoa maelekezo kwa Makatibu Tawala wote wa mikoa ya Tanzania Bara. Kuhakikisha wanafanya msawazo katika shule zilizo ndani ya mikoa yao na kupeleka walimu wa kike na wakiume katika maeneo ambayo hayana.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii ya Bunge lako tukufu kwa Niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kumwelekeza RAS wa Mkoa wa Simiyu kuhakikisha anafanya msawazo na kupeleka walimu katika shule ambazo hazina Walimu wa kike wa kutosha.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi ya maswali ya nyongeza. Nitakuwa na maswali mawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali haina utaratibu maalum wa ulipaji wa posho kwa hawa Wenyeviti wa Mitaa, Vitongoji na Vijiji na wamejitengenezea utaratibu wa kujipatia fedha kupitia mihuri yao na uuzaji wa viwanja kitu ambacho kinaleta migogoro mingi sana kwenye jamii na kaadhia kubwa kwenye jamii na urasimu mkubwa.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwa na utaratibu maalum wa kuwa na posho ya madaraka kwa viongozi hawa wa ngazi ya mitaa, vijiji na vitongoji? (Makofi)

Swali la pili, Wenyeviti hawa wa Mitaa, Vijiji na Vitongoji pamoja na Madiwani wamekuwa na dhamana kubwa sana ya usimamizi wa miradi ya Serikali kwenye maeneo yao, lakini mpaka leo hawana posho ya usimamizi wa miradi.

Je, nini kauli ya Serikali kuhakikisha kunakuwa na posho ya usimamizi wa miradi kwenye maeneo yao? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwandabila.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza la Serikali haina utaratibu maalum na ni nini kauli ya Serikali kuweka utaratibu huo. Kama nilivyokwishasema kwenye majibu yangu ya msingi kwamba kwa mujibu wa Sheria ile ya Mamlaka za Serikali za Mitaa Sura Namba 290, posho hizi zinatakiwa zilipwe kutoka kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri husika na ndiyo maana Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kuziimarisha hizi Halmashauri zetu kwa kuwapa miradi ya kimkakati kuwajengea vyanzo vya mapato mbalimbali ambavyo vitaongezea nguvu kuweza kulipa posho hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili ya usimamizi wa miradi. Ni kweli Wenyeviti wa Vijiji, Vitongoji, Mitaa wanafanya kazi nzuri katika kusimamia miradi, hasa miradi mingi ambayo kwa sasa tumeona Taifa letu Mheshimiwa Rais amemwaga miradi katika Sekta mbalimbali. Nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kulileta hili hapa na tunalichukua kama Serikali kwa sababu lina budget implication na pale ambapo tutaona Serikali ina uwezo wa kuweka kwenye bajeti zake tutaweka lakini kwa sasa bado tutaendelea na utaratibu ule kama sheria inavyotaka ile ya Mamlaka za Serikali za Mitaa Sura Namba 290.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa, Serikali imezipokea halmashauri kulipa ile posho iliyokuwa ya Madiwani.

Je, sasa Wizara haioni kwa nini isielekeze zile posho zilizokuwa zinalipwa kwa Madiwani na Halmashauri ziende zikawalipe Wenyeviti wa Serikali za Vijiji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, hili nalipokea kwa niaba ya Serikali na tutakwenda kuliangalia na kulifanyia kazi na kama tutaona liko viable basi tutachukua hatua.
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Serikali katika Bajeti yake ilipitisha posho ya Watendaji wa Kata ya kila mwezi, lakini posho hii imeonekana ni hisani. Baadhi ya Halmashauri zinalipa zingine hazilipi.

Je, Serikali mna tamko gani kuhusu posho hizi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Naibu Spika, posho hizi zilipitishwa kwenye bajeti na Bunge hili Tukufu na tutaenda kuhakikisha kwamba linatekelezwa kwa sababu tayari zilitengwa ili Watendaji hawa waweze kupata posho hizi za madaraka.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili.

Mosi, kwa kuwa ujenzi wa Kituo cha Afya Kitaya umeshakamilika, je, ni lini Serikali sasa itapeleka vifaatiba na wataalam ili huduma ziweze kutolewa?

Swali langu la pili, katika Bajeti ya TAMISEMI ambayo tumepitisha hivi karibuni zimetengwa fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo vipya vya afya. Je, Serikali inatoa tamko gani sasa kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Kata ya Nyundo au Mnongodi au Kata za kimkakati katika Jimbo letu la Nanyamba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la kwanza la nyongeza la Mheshimiwa Chikota la Kituo cha Afya Kitaya. Serikali imetenga katika mwaka wa fedha huu 2023/2024 shilingi milioni 400 kwa ajili ya Halmashauri ya Mji wa Nanyamba kwa ununuzi wa vifaatiba kwa ajili ya zahanati na vituo vya afya. Sasa ni maamuzi ya kwao wao kwamba shilingi milioni 400 hizi wazi-allocate wapi kwenye zahanati zipi, vituo vya afya vipi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la kupata vituo vya afya. Tutaangalia katika bajeti iliyotengewa kwa mwaka wa fedha huu 2023/2024 tuone Nanyamba imetengewa vituo vya afya vingapi lakini kama haijatengewa katika mwaka wa fedha huu Serikali itahakikisha inatenga fedha kwa ajili ya vituo vya afya vya Nanyamba katika mwaka wa fedha wa 2024/2025.
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Naishukuru Serikali kwa kutuletea walimu wa sayansi 197, lakini bado tuna upungufu mkubwa sana wa walimu wa masomo ya sayansi 889; je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Mkoa wa Mara ili waweze kutatua changamoto hii iliyowakabili na watoto wao waweze kufaulu vizuri?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kwa kuwa walimu wengi wa masomo ya sayansi ni walimu wa jinsia ya kiume: Je, Serikali haioni haja ya kuwa na program maalum ya kuwawezesha watoto wa kike kufundisha masomo ya sayansi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Chomete, la kwanza la upungufu mkubwa wa walimu wa sayansi katika Mkoa wa Mara; kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, kwamba tunaajiri walimu 13,130 na tutazingatia maeneo yenye upungufu mkubwa hapa nchini ikiwemo Mkoa wa Mara. Hivyo nimtoe shaka Mheshimiwa Mbunge kwamba Mkoa wa Mara nao upo katika mikoa ya kipaumbele kupata walimu hawa wa sayansi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali la pili, nitoe rai kwa watoto wa kike waweze kwenda kwenye vyuo hivi vya ualimu na kusomea kufundisha masomo ya sayansi, ili tuweze kupata pool kubwa ya maombi ya watoto wa kike wanaoenda kufundisha masomo ya sayansi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tena kwamba katika ajira hizi mpya, tutahakikisha wale walimu ambao wanakidhi vigezo na ni walimu wa sayansi wanaajiriwa katika mwaka huu wa fedha. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwa kuwa tunakubaliana kwamba tuna tatizo kubwa la walimu wa sayansi nchini na pia tunatambua kuna maendeleo ya sayansi na teknolojia: Ni kwa nini Serikali isione namna ambavyo inaweza kutumia TEHAMA kwa ajili ya kuhakikisha kwamba inatatua tatizo la walimu kwa mwalimu mmoja kuweza kufundisha shule nyingi kwa wakati mmoja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa TEHAMA, na ndiyo maana Serikali hii ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ilitoa vishikwambi kwa walimu wote kama kianzio cha kwenda kwenye TEHAMA kwa walimu hawa. Kadiri siku zinavyokwenda, kuna shule ambazo zinajengwa za kimkakati kama shule ya mfano iliyokuwepo hapa Iyumbu Jijini Dodoma ambazo zitakuwa ni shule za TEHAMA kuweza kufundisha wanafunzi wetu wengi zaidi, na miaka inavyokwenda, tutazidi kuongeza kama Serikali.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na uchambuzi mzuri uliofanyika na Serikali, wananchi wa Igurusi wanapata shida hasa wazazi wanapokuwa na uzazi pingamizi: Je, ni lini sasa maboresho yataanza kufanyika?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Je, kuna mpango gani wa kupeleka vifaa tiba katika Kituo cha Afya cha Chimala ili waweze kusaidiwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali lake la kwanza la lini maboresho yatafanyika, kama nilivyoshasema kwenye majibu yangu ya msingi, ni kwamba tumefanya tathmini na kugundua kuna vituo vikongwe hapa nchini 193, na hivi sasa tuko katika mchakato wa kutafuta fedha na kuhakikisha tunavikarabati na kuviongezea majengo vituo hivi vya afya ambavyo ni vikongwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili tutapeleka fedha kadiri ya upatikanaji wa fedha hizo na tutaangalia katika mwaka wa fedha huu ambao bajeti imepitishwa, kama kuna vituo ambavyo viko allocated Mkoa

wa Mbeya, basi tutakaa na Mheshimiwa Mbunge kuona ni namna gani Mbarali nao wanaweza kupata. (Makofi)
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwa kuwa ni zaidi ya miezi mitano sasa tokea Serikali imepeleka x-ray machines kwa kwenye Vituo vya Afya vya Muriti, Bwisya na Hospitali ya Wilaya ya Nansio, lakini mpaka sasa vifaa hivi havijaanza kutoa huduma kwa wananchi; nini kauli ya Serikali? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Naibu Spika, jitihada za Serikali zimekuwa ni kubwa sana kupeleka vifaa tiba maeneo mbalimbali hapa nchini ikiwemo Muriti na Bwisya kule Ukerewe. Nitumie nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kuagiza timu yetu ambayo inazunguka mikoani kutoa mafunzo kwa wataalam wetu kutumia vifaa hivi vya kisasa, wahakakikishe wanafika Ukerewe mara moja na kutoa mafunzo kwa watumishi hawa wa Muriti na kule Bwisya.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kituo cha Afya cha Endasaki miundombinu yake ni chakavu sana; je, ni lini Serikali itatoa fedha zote zinazohitajika ili kukarabati miundombinu ya kituo hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itatoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Endasaki pale ambapo upatikanaji wa fedha hizo utakuwepo. Tutaangalia katika mwaka wa fedha huu 2023/2024 kama kituo hiki kimetengewa, ili fedha hizo ziweze kwenda mara moja. Kama hakijatengwa katika mwaka huu wa 2023/2024, tutahakikisha mwaka 2024/2025 kituo hichi kinatengewa fedha.
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ninapenda kujua sasa ni lini Serikali itaanza kuimarisha miundombinu ya shule hizo 56 lakini niombe na miundombinu ya Shule ya Mkalapa pia iboreshwe?

Swali la pili, ninapenda pia nijue Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba shule zote zinapata walimu wa michezo ili kusudi vijana wetu waweze kushiriki katika michezo kikamilifu? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itaboresha miundombinu ya shule hizi 56 ikiwemo kama nilivyosema tathmini inafanyika katika Shule ya Sekondari Mkalapa ambayo imefanya vizuri sana katika michezo ya UMISETA lakini vile vile michezo ya Afrika Mashariki. Kwa hiyo Serikali inafanya tathmini na itaijumlisha na yenyewe Shule ya Mkalapa na tutatafuta fedha na kwenda kujenga miundombinu kwa awamu.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la walimu wa michezo. Katika ajira ambazo Serikali imetangaza hizi 21,000 ambapo 13,390 hizi ni ajira za walimu. Tutaangalia ni namna gani nayo tuna-accommodate walimu wa michezo, walimu wa kilimo, walimu wa ufundi ili kuweza kuboresha elimu yetu hapa nchini.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Shule ya Sekondari Ngoreme Wilayani Serengeti kumekuwepo na jitihada nyingi za wananchi na wadau mbalimbali za kujenga miundombinu kwa lengo la kuifanya kuwa shule ya Kidato cha Tano na cha Sita. Yamekuwepo maombi yangu mbalimbali mara kadhaa kwa TAMISEMI.

Je, ni lini sasa TAMISEMI mtaipandisha hadhi shule hii kuwa ya Kidato cha Tano na cha Sita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Amsabi Mrimi kwa jitihada zake za kuhakikisha shule hii ya Ngoreme inapandishwa hadhi. Kwa sasa walikuwa wanamalizia ujenzi wa mabweni ili kuweza kuhakikisha kwamba shule hii inakidhi vigezo vya kuwa A level na baada ya hapo Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Wizara ya Elimu zitafanya jitihada za kuhakikisha shule hii inasajiliwa kuwa na mkondo wa Kidato cha Tano na Sita.
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Swali la kwanza; je, kwa shule ambazo zimekwishakukamilisha maabara, Serikali ina mkakati gani wa kupeleka wataalam wale lab technician ili waweze kutoa huduma katika maabara hizo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, je, Serikali ina mkakati gani kwa maabara ambazo zimekwishakukamilika kupeleka vifaa ili wanafunzi waanze kujifunza kwa vitendo zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la kwanza la nyongeza lini shule hizi ambazo maabara zimekamilika zitapelekewa wataalam. Serikali imetangaza ajira 21,000 kwa sekta ya elimu na afya na katika walimu tutaajiri jumla ya walimu karibia 13,390 ambapo wengi watakuwa ni walimu wa sayansi ili kwenda kukidhi hitaji hili la maabara katika shule hizi ambazo Serikali ilipeleka fedha kumalizia maabara.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la vifaa. Serikali itapeleka vifaa hivi kadri ya upatikanaji wa fedha lakini ni priority ya Serikali kuhakikisha wataalam wanapofika katika maabara hizi vilevile na vifaa vinakuwepo vya kufundishia.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nashukuru sana kwa Serikali kutoa hizo fedha ambazo zimetumika katika hilo eneo.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kipande cha Idunda – Soga kuelekea katika eneo la Mbeya Vijijini, Serikali imelima tu lakini haikuweza kuweka changarawe na kujenga kidaraja kidogo katika lile eneo. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inakamilisha hilo eneo ili liwe linapitika wakati wote wa mwaka?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa ili wananchi wa Idunda, Ipyana waweze kusafiri hadi Iyula hadi kuelekea Makao Makuu ya Jimbo la Vwawa ni lazima kipande cha Iyula – Hatete – Mbewe kikamilike ambacho mpaka sasa hivi bado hakijakamilika.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inakamilisha kipande hicho ili kuwasaidia wananchi hao waweze kusafiri kiurahisi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu swali lake la kwanza la kipande cha Idunda – Soga ili kiweze kujengwa kuwa changarawe na kuna daraja ambalo Mheshimiwa Hasunga amelitaja lina changamoto. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 TARURA katika Wilaya ya Songwe, Halmashauri ya Songwe DC ilikuwa imetengewa shilingi milioni 650 tu, lakini katika mwaka wa fedha 2021/2022 na huu tunaokwenda wametengewa zaidi ya shilingi bilioni 2.8 kwa ajili ya utekelezaji wa barabara. Hivyo basi, nichukue nafasi hii kumuelekeza Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Songwe kuhakikisha wanafika kwenye barabara hii na kuona changamoto ambayo ipo ili waweze kutengeneza daraja hili ambalo amelitaja Mheshimiwa Hasunga la kuunganisha wananchi kati ya Songwe na Mbeya.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la wananchi wa Igana kupita barabara ya Iyula - Katete na Mbewe. Nirejee tena yale maelekezo ambayo nilikuwa nimeyatoa kwenye swali lake la kwanza, Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Songwe anapotembelea barabara hii ya Idunda – Soga ahakikishe anaangalia nini kimekwamisha barabara hii ambayo nimetoka kuitaja hivi sasa na kuweka mikakati ya kuweka changarawe na kuimalizia.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kwa vile Mamlaka ya Mji mdogo wa Mbalizi kwa muda mrefu sasa imeshakua, na ina uchumi mkubwa, ni lini Serikali itaipandisha hadhi kuwa Halmashauri ya Mji wa Mbalizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kuhusu kupandisha hadhi Mamlaka ya Mji Mdogo Mbalizi kuwa Halmashauri ya Mji, kwa sasa Serikali inamalizia kwanza majengo ya kiutawala na huduma za kijamii katika mamlaka ambazo zipo tayari. Baada ya kukamilisha ujenzi wa miundombinu katika mamlaka hizi, tutaanza sasa kuangalia ni wapi panahitaji napo kupandishwa hadhi na kuwa mamlaka ya mji kama vile kule Mbalizi?
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mamlaka ya Mji Mdogo Namanyere, tumeshafanyiwa tathmini na tumekidhi vigezo: Ni lini sasa tutapandishwa hadhi kuwa mamlaka ya Mji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Mji Namanyere kupandishwa hadhi itakuwa ni baada ya Serikali kumalizia ujenzi wa miundombinu katika Halmashauri, Mamlaka za Miji na Majiji ambayo yamehama katika maeneo yao ya kiutawala, na sasa Serikali inapeleka fedha nyingi kumalizia maeneo hayo.
MHE. LEAH. J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa maboresho yaliyofanywa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Kwa kuwa changamoto kubwa ya mkaguzi wa nje CAG katika POS ilikuwa ni matumizi ya fedha mbichi na kusababisha kushuka kwa mapato ya hamashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka kufahamu je, mfumo mpya wa TAUSI unakwenda kukabiliana nayo vipi hii changamoto?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wakusanya mapato wengi hawana taaluma. Nilitaka kujua mkakati wa Serikali wa kuajiri wahasibu wa kutosha katika halmashauri zetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali lake la kwanza nianze kwa kusema changamoto kubwa ambayo ilikuwepo kwenye halmashauri zetu na hizi POS kuwa ziko offline ilikuwa ni uadilifu wa watumishi wetu. Tayari Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI ilichukulia hatua wale wote waliopatikana na hatia ya kucheza na POS hizi na hivyo kupotezea mapato halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna Dashboard hivi sasa katika mfumo mpya wa TAUSI ambapo katika halmashauri zote, Mkurugenzi ana uwezo wa kuona mapato yaliyokusanywa kwa wakati huo na kama kuna POS yoyote itakwenda offline basi nayo Mkurugenzi ataona. Hata hiyo, dashboard ile ile iko Mkoani na vilevile Ofisi ya Rais, TAMISEMI tuna uwezo wa kuona. Kwa hiyo, tumefanya maboresho makubwa sana na kuanzia tarehe 1 Julai ndio mfumo pekee ambao utatumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali la pili; la taaluma, Kuajiri watu wenye taaluma ya uhasibu. Hili tunalipokea na kadri ya uwezo wa Serikali wa kibajeti tutaajiri watu kuendana na taaluma ya uhasibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa hii nafasi. Kwa kuwa Serikali imekuja na mfumo mpya wa kukusanya mapato unaojulikana kama TAUSI, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba madiwani wote wanapata elimu ya huu mfumo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa Serikali kwenye mfumo huu wa TAUSI, kwanza ni Ofisi ya Rais, TAMISEMI ilitoa technical specification kwa halmashauri zote za aina ya POS ambazo zinatakiwa kununuliwa ambazo zitaendana na mfumo huu. Kadri tunavyokwenda tunatoa mafunzo kwa wale wanaohusika na POS hizi kule kujua ni namna gani wanatumia POS hizi ambazo zinaendana na mfumo huu wa TAUSI.
MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana nina maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri sana ambayo Mheshimiwa Naibu Waziri ameyatoa ningependa kujua kwamba Serikali inafikiriaje kwa halmashauri ambazo hazina uwezo mkubwa kimapato wa kuweza kugharamia uwekaji wa taa barabarani kupitia ruzuku inayotolewa na REA kwamba halmashauri hiyo ikapata ruzuku asilimia 75 mpaka 100 ukilinganisha na asilimia 50 ya sasa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; ni kwamba, sasa hivi tunajua tunafanya juhudi kubwa ya kujenga barabara za mijini hususani pale Masasi na kwenye majimbo ya wenzangu. Kwa nini TAMISEMI sasa isiamue kufungamanisha fedha ambazo zinatolewa kwa ajili ya ujenzi wa barabara na fedha kwa ajili ya uwekaji wa taa ili Mkandarasi anayepewa kujenga zile barabara pale mjini anamalizia na kuweka taa moja kwa moja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwambe, la kwanza hizi Halmashauri ambazo haazina uwezo kupata ruzuku ya REA. Hili tunalichukua kama Ofisi ya Rais, TAMISEMI na tutahakikisha tunakaa taasisi yetu ya TARURA kwa kushirikiana na taasisi ya REA ambayo iko chini ya Wizara ya Nishati kuona ni namna gani tunaweza kufanya kazi ka Pamoja na kutoa hiyo ruzuku iende kwenye barabara hizi kwenye miji ambayo haina uwezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, kwa sasa barabara zote zinazojengwa na TARURA nchini kote hasa zile zinazopita kwenye Katikati ya miji zinawekewa taa. Pia, kama Masasi kule hawajaanza naamini wakimaliza tu katika ujenzi wa barabara hizi taa zitaanza kufungwa kama nilivyokuwa nimesema kwenye majibu yangu ya msingi.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mji wa Mugumu kama unakuwa kwa kasi na shuguli za maendeleo wakati wote zinaendelea.

Je, ni lini sasa Serikali itatusaidia kuhakikisha tunapata taa za barabarani katika mji wa Mugumu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejipanga kuweka taa katika mji wa Mugumu kwenye barabara zinazokamilika. Mheshimiwa Mbunge ni shahidi kuna barabara inayozunguka Soko kuu la Mugumu ambayo inakamilika muda si mrefu na barabara ile itakapokamilika taa zile zitafungwa kama nilivyosema awali kwamba sasa TARURA katika barabara zote zinazojengwa katikati ya miji ni lazima ziwekewe taa.
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Naibu Waziri, alipokuja Katibu Mkuu wa CCM, Kiteto alituahidi taa za barabarani pale mji wa Kibaha na tumeleta maombi. Ni lini Serikali itatuletea hizi fedha tuweke taa za barabarani pale mjini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Mbunge amesema ilikuwa ni ahadi ya Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi ambae Serikali hii ndio inatekeleza Ilani yake ya uchaguzi, tutakaa na wenzetu wa TARURA ambao ni taasisi iko chini ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuona wamejipangaje katika kutekeleza uwekaji wa taa hizi kama ambavyo Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi inavyotaka.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na ninashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali madogo mawili ya nyongeza. La kwanza, kwa kuwa wako walimu wanaojitolea kwa muda mrefu katika Shule ya Sekondari ya Wilaya ya Babati: Je, katika ajira mpya, Serikali iko tayari kuwapa kipaumbele hao wanaojitolea?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kwa kuwa kati ya shule 38, kuna shule sita ambazo zina mwalimu mmoja mmoja wa kike wa Shule za Sekondari ya Taraget, Burunge, Nar, Kameri, Ndeku na Endamanang’; je, Serikali iko tayari kuongeza walimu wa kike katika shule hizi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la kwanza la Mheshimiwa Sillo la wale ambao wanajitolea; katika ajira hizi ambazo nimezitaja, Serikali imetoa 13,390, tutakwenda kwa kuangalia vigezo, kwa sababu ajira hutolewa kwa usawa.

Hao wanaojitolewa kama wameomba ajira hizi na wanakidhi vigezo vilivyowekwa katika tangazo la ajira, basi nao pia watapata, lakini hakutakuwa na upendeleo maalum ambao utatolewa kwa wale tu wanaojitolea kwa sababu wanajitolea, ili kutoa fursa sawa kwa wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali la pili la upungufu wa walimu wa kike katika shule ambazo Mheshimiwa Sillo amezitaja, hili agizo lilishatolewa kwa Makatibu Tawala wote wa Mikoa Tanzania kuhakikisha wanafanya msawazo wa walimu katika mikoa yao. Sasa katika ajira mpya hizi zinazokuja, kuna walimu wa kike nao wataajiriwa, wakifika mikoani kule wapangiwe katika shule zenye upungufu wa walimu wa kike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie tena hapa kuelekeza Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara kuhakikisha anafanya msawazo katika shule ambazo amezitaja Mheshimiwa Sillo kupeleka walimu wa kike kutoka ndani ya Mkoa wake.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa kuna upungufu mkubwa wa walimu katika Shule za Msingi na Sekondari katika Mkoa wa Simiyu: Je, ni lini Serikali itatuletea walimu wa kutosha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyokuwa nimeshasema kwenye majibu yangu ya msingi, Serikali imetangaza ajira 13,390 na kipaumbele pale watakapokuwa wanapangiwa shule walimu hawa, ni kwa mikoa ile yenye upungufu mkubwa, ukiwemo Mkoa wa Simiyu.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Katika ajira mpya ambazo zinaendelea sasa, Serikali ina mpango gani kupeleka walimu katika shule mpya sita; Shule ya Sekondari Kimusi, Nyagisya, Barata, Inchugu na Nyanungu pamoja na Kubiterere ili watoto wetu waweze kusoma, na shule hizi zimejengwa na nguvu ya wananchi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ajira mpya hizi ambazo Serikali imetoa, tutaangalia maeneo yenye upungufu ikiwemo shule hizi za Kimusi, Nyagisya, Nyamongo, zilizopo kule Tarime na Mkoa mzima wa Mara kwa ujumla.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba tu kumwuliza swali Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwa sababu ni muda mrefu hapo nyuma ajira zilikuwa hazijatoka na kuna vijana wengi waliomaliza elimu zao toka mwaka 2014, 2015 mpaka sasa: Ni nini kauli ya Serikali kwamba baada ya kuwa mmetangaza ajira hizi 13,000 na kuwapa kipaumbele waliokuwa wame-graduate mapema zaidi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika tangazo la ajira ambalo Serikali imetoa kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa walimu 13,390 imewekwa pale kwamba wale wa 2015 ndiyo wataanza kuingia, watakuja wa 2016 wa 2017 ili wasikae muda mrefu baada ya kuwa wamemaliza masomo yao ya ualimu. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali. Kwa kutambua kwamba Solwa inahudumia watu karibia 31,000 na imebeba jina la Jimbo la Solwa; napenda kujua, Mganga Mkuu atatumia siku ngapi kumaliza ukaguzi huo? Swali la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Wananchi wa Mkoa wa Shinyanga na sehemu nyingine wamekuwa wakijitolea kuongeza majengo ya zahanati ili yaweze kuwa vituo vya afya ili kukidhi huduma, sasa napenda kujua, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba zahanati zote ambazo zinakidhi na zimeshaongeza majengo, zitabadilishwa kuwa vituo vya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ni siku ngapi zitachukuliwa kwa ajili ya ukaguzi huu wa Zahanati ya Solwa ambayo inahudumia watu 31,000 katika Jimbo la Solwa, nitoe agizo kwa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga kuhakikisha ndani ya mwezi mmoja, taarifa hii iwe imefika Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili kuona zahanati hii inaanza mchakato wa kupandishwa hadhi na kuwa kituo cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali la pili la Mheshimiwa Dkt. Mnzava kwamba wamejenga zahanati nyingi katika maeneo ya kimkakati, ni lengo la Serikali kuhakikisha kwamba zahanati hizi ambazo zimejengwa kwa nguvu ya wananchi kwenye maeneo mbalimbali ya nchi yetu ya Tanzania, siyo Shinyanga peke yake kwamba zinapatiwa fedha na kuweza kuwa upgraded yale kwa yale maeneo ya kimkakati, na Serikali itafanya hivyo kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi. Wananchi wa Kata Kilimilile wamejenga zahanati kwa nguvu ya wananchi na wafadhili na hiyo zahanati ina majengo ya wodi ambazo hazitumiki kwa sababu hadhi ya zahanati hairuhusiwi kulaza wagonjwa: Je, sasa ni lini Zahanati hiyo ya Kata ya Kilimilile itapandishwa hadhi ili iweze kutoa huduma katika Kata za Mabale na Kilimilile kwa wananchi hao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchukua nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kumwelekeza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kagera kufika katika Zahanati ya Kilimilile katika Kata ya Kilimilile kufanya tathmini na kuona yale majengo ambayo yamejengwa kama yanakidhi vigezo vya kuweza kupandisha zahanati hii kuwa kituo cha afya na taarifa hii kuwasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Naye nampatia mwezi mmoja ili iweze kuwa imefanyika tathmini hii.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kata ya Msaada kuna jengo ambalo lilikuwa likijengwa kwa mpango wa MAMM tangu mwaka 2008 mpaka leo halijakamilika. Naomba kujua, ni lini Serikali itamalizia jengo hilo, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Monni kuhusu Kata ya Msaada, Serikali itamalizia jengo la Msaada hapa kadri ya upatikanaji wa fedha. Tutaangalia katika mwaka wa fedha huu ambao umeshapitishwa na Bunge lako Tukufu, kuona kama kuna fedha imetengwa kwa ajili ya Msaada lakini kama haipo, basi tutatenga fedha kwenye mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii niulize swali la nyongeza.

Kwa kuwa baadhi ya halmashauri malipo au stahiki za Madiwani zinapishana sana mathalani malipo ya simu kwa wenyeviti wa halmashauri na kadhalika, je, nini kauli ya Serikali katika hili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, aina za posho za Madiwani zimeainishwa ambazo ziko wazi. Posho ya kwanza, ni posho ile ya mwezi ambayo nimetoka kuitolea majibu katika swali la msingi. Posho ya pili, ni posho ya madaraka ambayo posho hii pia inatolewa kwa mujibu wa waraka wa viwango vya posho vya Serikali. Posho ya tatu ni posho ya kuhudhuria vikao na posho ya kujikimu na safari mbalimbali za ndani ya halmashauri husika na nje ya halmashauri husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hizi posho za ndani zinategemeana na uwezo wa halmashauri husika. Kwa hiyo, hili tutaendelea kuwaasa wakurugenzi wa halmashauri mbalimbali nchini kuangalia walau wanatenga posho ya mawasiliano na kadhalika kulingana na uwezo wa mapato yao wenyewe ya ndani.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nilikuwa nataka niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza; kwa kuwa hawa Madiwani kwa muda mrefu sasa na hasa sisi wa Chama cha Mapinduzi wakati tunapokuwa kwenye kampeni za uchaguzi huwa tunasema kuna mafiga matatu kwa maana ya Madiwani, Wabunge na Rais na wao ndio wanaosimamia miradi ya Serikali. Sasa hatuoni kuna haja kwa kweli ya kuwaongeza kiasi fulani angalau kutoka kwenye eneo walipo ili kufika eneo wanalolitaka wao kwa sababu eneo ni kidogo sana? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; hawa Madiwani kwa muda mrefu sasa huko nyuma wengi wamechaguliwa na hawapati mafunzo ya Serikali. Lini sasa Serikali itaandaa mafunzo kwa Madiwani ili na wenyewe wawe na uelewa wa kusimamia miradi yetu katika maeneo yetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la kwanza la nyongeza la kuhusu kuongeza posho hizi za Madiwani, Serikali itafanya tathimini na kuangalia ni namna gani hili linaweza likatekelezeka kulingana na bajeti ambayo Serikali inayo. Kwa sbabu haya mambo yanahusisha ongezeko la matumizi kwa Serikali. Tayari kama ambavyo mnafahamu Waheshimiwa Wabunge wote humu ndani kwamba mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali ilichukua jukumu kutoka kwenye halmashauri zote la kulipa hizi posho kwa mwezi zilienda Serikali Kuu. Kwa hiyo, tutaliangalia na lenyewe na kuona kama uwezo wa Serikali utauhusu kwenye bajeti zijazo tuweze kulichukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda kwenye swali la pili la mafunzo kwa Madiwani; hili liko kwa Wakurugenzi wa Halmashauri zenyewe. Kuna halmashauri ambazo zinatoa maunzo haya kwa kushirikisha Taasisi za Uongozi Institute, kwa kushirikisha Taasisi kama Chuo cha Utumishi wa Umma. Kwa hiyo, niwatake wakurugenzi katika halmashauri mbalimbali nchini kuhakikisha wanatenga bajeti ya kutoa mafunzo kwa Madiwani wa halmashauri zao.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kati ya watu muhimu sana ni Wenyeviti wa Vitongoji, Vijiji na Mitaa; hawa ni watu ambao wanapata posho kama ni posho inakuwa ni ndogo sana. Nini mkakati wa Serikali kuhakikisha watu hawa ambao ni muhimu wanaongezewa posho kubwa itakayowasaidia utendaji wao wa kazi uwe mzuri katika halmashauri zetu, vitongoji na vijiji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyokwisha sema hapo awali kwamba posho hizi zinategemeana na bajeti ya Serikali na uwezo wa makusanyo ya Serikali, lakini upo waraka maalum na Sheria katika Sheria ya Serikali za Mitaa ambayo inazitaka Mamlaka za Serikali za Mitaa kote nchini kutenga fedha kwa ajili ya posho za Wenyeviti wa Vitongoiji, Wenyeviti wa Mitaa na Wenyeviti wa Vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi, nitumie tena nafasi hii mbele ya Bunge hili tukufu kuwataka Wakurugenzi wa Halmashauri kutenga posho hizi za Wenyeviti wa Vijiji, Wenyeviti wa Mitaa na Wenyeviti wa Vitongoji kwa mujibu wa Sheria ile ya Serikali za Mitaa, Sura 290.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Tabora Mjini lina kata za mjini na vijini, lakini licha ya kuwa na Hospitali ya Rufaa ya Kitete na hospitali ya wilaya kumekuwa na mrundikano mkubwa wa wagonjwa. Je, nini mikakati ya Serikali kuzisaidia kata za vijijini kupata vituo vya afya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, Sera ya Serikali ni kujenga vituo vya afya kwa kila kata lakini mwaka 2021 Waziri wa TAMISEMI, wakati huo Mheshimiwa Ummy Mwalimu alituletea Wabunge kuandika kata za kimakakati ambazo katika Jimbo la Igalula tuliandika Kata ya Goeko, kizengi na Miswaki.

Je, ni lini mtatekeleza yale maagizo ya kata za kimkakati ili tuweze kujenga vituo vya afya na kusogeza huduma za wananchi katika maeneo hayo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali lake la kwanza la utofauti wa Mjini na vijijini katika Jimbo la Tabora Mjini na Serikali kusaidia. Serikali itaendelea kutenga fedha kadri ya bajeti ambavyo inaruhusu kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu ikiwemo Jimbo la Tabora Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali la pili la nyongeza la Kata za Goeko, Kizengi na nyinginezo katika Jimbo la Igalula. Serikali itajenga vituo hivi vya afya vya kimkakati kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Jimbo la Nkasi Kaskazini lina vituo vya afya vitatu na vinavyofanya kazi ni viwili kati ya kata 17. Ni lini Serikali itajenga vituo 13 vilivyobaki katika Jimbo la Nkasi Kaskazini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeweka kipaumbele katika kuboresha afya za watanzania na tayari Serikali inatenga fedha katika vituo vya afya kwenye kata za kimkakati pote hapa nchini, ikiwemo kata ambazo amezitaja Mheshimiwa Aida Khenani za kule Nkasi ambayo ina vituo vya afya vitatu tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutangalia katika mwaka wa fedha huu ambao unakwenda kuanza kuutekeleza mwezi Julai, kuona Nkasi imepangiwa vituo vya afya vingapi kwa ajili ya utekelezaji. Kama bado itakuwa haijapangiwa basi Mheshimiwa Mbunge tutaangalia katika bajeti ya 2024/2025 ili tuweze kuwapangia wana Nkasi kupata huduma bora za afya kupitia vituo vya afya.
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wananchi wa Wilaya ya Kilindi wanatambua jitihada za Serikali za kupeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya. Lakini tunazo kata tatu kwenye vituo vya afya vitatu kwenye Kata ya Jaila, Masagalu na kata ya Maswaki tunahitaji at least milioni mia, mia ili kuweza kumalziia vituo vya afya. Je, ni lini Serikali italeta fedha katika maeneo hayo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhamira ya Serikali kujenga vituo vya afya katika Mkakati ikiwemo kata za kwa Mheshimiwa Kigua kule Kilindi Kata hizi za Jaila, Masagalu na Mswaki na tutaangalia katika mwaka wa fedha kama zimetengwa fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo hivi vya afya na umaliziaji. Kama fedha hizo hazijatengwa nimhakikishie Mheshimiwa Kigua katika mwaka wa fedha 2024/2025 ili Jaila, Masagalu na Mswaki ziweze kupata fedha hizi kwa ajili ya umaliziaji.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kabla sijauliza maswali naomba niweke kumbukumbu sawa ni Shule ya Sekondari Gwanumpu na Shule ya Sekondari Shuhudia. Baada ya masahihisho hayo ninashukuru kwa majibu ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kakonko inayo shule moja tu ya sekondari ambayo ni Shule ya Sekondari Kakonko, na katika majibu ya Serikali amebainisha kwamba Shule ya Sekondari Muhange inapungukiwa mabweni mawili tu.

Je, lini sasa Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kujenga hayo mabweni mawili ili masomo yaweze kuanza pale?

Swali la pili, amebainisha shule hizi za Sekondari Shuhudia, Kasanda, Nyamtukuza na Gwanumpu zinapungukiwa miundombinu mbalimbali, lakini kinachohitajika hapo ni fedha. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba miundombinu hii inayopungua inakamilika na masomo yaweze kuanza katika shule hizi? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Spika, nikijibu swali lake la kwanza la lini fedha itakwenda kukamilisha mabweni haya ambayo tayari yameshaanza kujengwa. Serikali itapeleka fedha kadiri ya upatikanaji wake na tutaangalia katika bajeti hii iliyopitishwa ya mwaka wa fedha 2023/24 kuona kama hiyo shule imetengwa fedha, kama haijatengewa tutajitahidi tuitengee fedha 2024/2025.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili kuhusu Shule za Gwanumpu, Shuhudia na Nyamtukuza ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitaja, tutaangalia vilevile kuona uwezekano wa kuzitengea fedha katika mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kutokana na Sensa ya Watu na Makazi iliyokuwa imefanyika hivi karibuni, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kuweza kutoa tamko kwamba irudi tu katika mfumo ule wa zamani wa vijiji kuliko hivi sasa kuweza kusubiri kwa sababu imekuwa ni muda mrefu, tangu mwaka 2009?

Swali la pili, pale kwenye Jimbo la Kibiti, Kata za Kibiti, Dimani na Mtawanya ilitangazwa kuwa Mamlaka ya Mji Mdogo tangu mwaka 2014, shughuli za maendeleo, vikao vya kisheria, mali zimekuwa haziwezi kumilikiwa ipasavyo.

Je, Serikali ina tamko gani kuhusiana na suala hili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la kwanza la tamko la kurudisha kuwa na vijiji badala ya Mamlaka ya Mji Mdogo. Nirejee kwenye majibu yangu ya msingi, kwamba vigezo vya kupandisha Mamlaka za Mji Mdogo kuwa Halmashauri za Mji zimewekwa wazi kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa na Mamlaka nyingi za Miji Midogo hizi bado hazijakidhi vigezo hivyo.

Mheshimiwa Spika, kuna Mamlaka za Miji Midogo asilimia 67 ambazo haziwezi kufikia malengo yao wanayojiwekea ya kibajeti na ni asilimia 33 tu ambazo zinafikia malengo yao ya kibajeti kwa asilimia 100, ikiwemo Mamlaka ya Mji Mdogo wa Bagamoyo. Serikali itaendelea kuliangalia hili na pale tutakapokuwa tumeboresha miundombinu katika maeneo ya kimamlaka yaliyopo sasa tutaendelea kufanya review na kuona ni namna gani tunakwenda kuzipandisha hadhi mamlaka hizi.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la Kibiti. Vivyo hivyo kama nilivyotoa majibu yangu kwenye swali la nyongeza namba moja, kwamba tunaangalia vigezo vya mapato vilevile na kuweza kufanya huduma mbalimbali za kijamii, wao wenyewe kupitia mapato yao ya ndani. Mji Mdogo wa Kibiti tutafanya tathmini kama unakidhi vigezo vile vya kimapato basi tutaona ni namna gani ambavyo unaweza kuwa Mamlaka ya Mji Mdogo katika Mji wa Kibiti.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mpaka sasa barabara za vumbi ni zaidi ya asilimia 70 na barabara ya lami ikiwa ni asilimia 0.4 na changarawe asilimia 29.

Swali la kwanza, ni kwa nini bajeti imeendelea kuwa kidogo, ambayo ni shilingi bilioni tatu, wakati barabara za vumbi na za udongo bado ni zaidi ya asilimia 70?

Swali la pili, ni lini itatengenezwa barabara ya kutoka Kyerwa kwenda STAMICO ambako kuna biashara kubwa ya madini ya bati, ni lini barabara itatengenezwa, sambamba na kuunganisha Kata ya Mabira na Kata ya Kibale?

Mheshimiwa Spika, naomba majibu.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetoa maelezo katika majibu yangu ya msingi, bajeti imeendelea kuongezeka ndani ya miaka hii mitatu. Ukiangalia trend mwaka wa fedha 2020/2021 bajeti katika Wilaya ya Kyerwa ilikuwa shilingi bilioni 1.26 tu, lakini hivi tunavyozungumza bajeti hiyo imekwenda mpaka shilingi bilioni 3.18 kwa maana imeongezeka mara mbili ya vile ilivyokuwa 2020/2021.

Mheshimiwa Spika, hiyo inaonesha dhamira ya dhati ya Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuiboreshea nchi yetu barabara zake za vijijini na mijini kupitia Wakala wa Barabara (TARURA). Kwa hiyo, nikutoea mashaka Mheshimiwa Mbunge, tutaendelea kuweka fedha kuangalia ni namna gani barabara hizi zinatengenezwa.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la barabara hii ya Kyerwa – STAMICO kupitia Kata ya Mabira na kadhalika, tayari katika kiwango cha lami tulianza kwa kujenga kilometa mbili kwenye Mji Mdogo wa Nkwenda, kuna barabara ambayo ipo kutoka Kido Hospitali katika Mji wa Kyerwa, vilevile tutakwenda sasa kuangalia hii kwenye bajeti zijazo tuweze kutenga fedha kwa ajili ya barabara hii ya Kyerwa mpaka STAMICO.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza niipongeze Serikali kuendelea kuongeza bajeti kwenye barabara za TARURA Wilayani Kyerwa.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kasoni kwenye Kata ya Nyakatuntu kwenda mpaka Mkuyu Kata ya Kikukuru niliiombea fedha na fedha imeshapatikana.

Je, ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha changarawe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI):
Mheshimiwa Spika, barabara hii ya Kasoni – Nyakatuntu – Mkuyu kwa maana imetengewa fedha kwenye bajeti hii ambayo tunaanza kuitekeleza tarehe 1 Julai mwaka huu, tutahakikisha kwamba barabara hii inapatiwa mkandarasi haraka ili iweze kuanza kujengwa.

Mheshimiwa Spika, ninapongeza jitihada za Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Bilakwate, kwa maana amekuwa akiifuatilia sana barabara hii na kuhakikisha kwamba inatekelezwa kwa wakati. (Makofi)
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana kwa majibu ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapozungumzia hospitali ambazo ni kielelezo na zipo mpakani ni Hospitali ya Kyela, lakini hospitali hii ni hospitali kongwe sana ambayo kwa sasa hivi haitamaniki na hata ukifanya usafi haioneshi kwamba ni hospitali ambapo watu wanaweza wakatibiwa na kupata faraja.

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kwa Serikali kuhakikisha majengo haya yanajengwa upya na yanakuwa mapya kwa ajili ya kuwa na manufaa kwa wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; ikama ya wafanyakazi walioko katika Wilaya ya Kyela imepungua sana na iko kiwango cha chini kukidhi mahitaji ya magonjwa mengi ambayo yako Kyela.

Je, Serikali haioni haja ya kuongeza wafanyakazi kwa kipindi hiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mlaghila Jumbe; la kwanza la fedha kutengwa kwa jili ya ukarabati wa hospitali hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kama nilivyokuwa nimeshasema kwenye majibu yangu ya msingi, tayari Serikali imeshatenga fedha zaidi ya bilioni 2.75 ambazo zimekwenda katika Hospitali ya Wilaya ya Kyela ili kuhakikiusha kwamba inafanyiwa ukarabati; na katika mwaka huu wa fedha tumetenga shilingi milioni 800 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi huo. Nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge, kwamba ni adhma ya Serikali hii ya awamu ya sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha inakarabati hospitali kongwe zote nchini, ikiwemo ya Kyela, na tutaendelea kutafuta fedha kufanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali la pili la ikama ya watumishi. Bunge lako tukufu hili ni mashahidi, Serikali imetangaza ajira zaidi ya 21,300 kwenye sekta ya elimu na sekta ya afya. Ajira hizi zitakapokamilika tutahakikisha vilevile Hospitali ya Kyela inapata wataalamu ambao wanatakiwa kuhudumia Watanzania waliopo Kyela pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Pamoja na maswali mazuri sana na Serikali lakini nilitaka kujua, je, ni lini katika ajira hizi zilizotangazwa watumishi hawa wataingia kazini ili waende wakawatibu Watanzania wengi ambao wanahitaji huduma hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ajira hizi zilizotzngazwa zote 21,300 katika sekta ya elimu na afya zitaanza kutumika au wataingia kazini baada ya mchakato wa ajira hizi kukamilika ndani ya mwaka huu wa fedha. Kwa hiyo muda siyo mrefu Mheshimiwa Malleko kule Kilimanjaro lakini na Waheshimiwa Wabunge wote hapa wataanza kuona wale watumishi wapya wanaaanza kwenda kwenye maeneo yao.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kuna jitihada nyingi katika Jimbo la Serengeti Kijiji cha Nyamatale pale Nyirongwa wamejenga boma, pale Kitalahota Kitongoji katika Kijiji cha Nyamakobiti, pia wamejenga boma kwa jajili ya zahanati, Kijiji cha Bisalala, Ngalawani na Kenokwi.

Je, ni lini sasa Serikali itatoa mchango wake kusaidia jitihada hizi za wananchi kukamilisha zahanati hizi? ahsante
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Amsabi la zahanati hizi za vijiji ambavyo amevitaja Serikali itaunga mkono juhudi za wananchi hawa kadri ya upatikanaji wa fedha. Na tutajitahidi, kwa sababu ni adhma ya Serikali hii ya awamu ya sita kuhakikisha afya za Watanzania zinaimarika zaidi kwa kupata huduma iliyobora. Tutahakikisha kadri ya upatikanaji wa fedha tunachangia nguvu za wananchi wa pale.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mheshimiwa Waziri katika Wilaya ya Rungwe Mheshimiwa Mbunge wa jimbo pamoja na Diwani wa Kata ya Kiwila na wananchi wameweza kujenga Zahanati ya Kiwila lakini bado haijamalizika.

Je, ni lini, Serikali mtaenda kuweka nguvu ili tuweze kumaliza zahanati ile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Zahanati hii ya Kiwila kule Rungwe itatengewa fedha kadri ya upatikanaji wa fedha; na tutaangalia katika mwaka wa fedha huu 2023/2024 ambao tunaenda kuanza kuutekeleza kama imetengewa fedha. Kama haijatengewa fedha tutaangalia kuitengea fedha katika mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia nafasi. Katika Jimbo la Momba kuna vijiji zaidi ya 20 ambavyo wananchi wamejenga maboma na wanahitaji kuungwa mkono na Serikali. Mfano, Kijiji cha Mwenehemba, Mamsinde one, Namsinde two, Kakozi, Chilangu na vinginevyo.

Je, ni lini, Serikali itatusaidia ili kumalizia maboma haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itasaidia umalizaji wa maboma haya 20 aliyotaja Mheshimiwa Condester Sichalwe kadri ya upatikanaji wa fedha. Nitumie nafasi hii kuwataka Wakurugenzi wote wa Halmashauri nchini kuhakikisha wanatenga fedha katika mapato yao ya ndani kuunga mkono juhudi za wananchi katika maeneo yao ya kiutawala ili kuweza kumalizia iwe ni katika zahanati iwe ni katika shule.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Nishukuru kwa majibu mazuri ya Serikali ambayo ameyatoa Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Biharamulo kijiografia ni eneo kubwa sana na tumekuwa katika scarcity hiyo ya watendaji kwa muda mrefu sana. Sasa kwa sababu umesema tayari maombi yetu mnayo.

Swali la kwanza; je, ni nili tutapatiwa kibali tuweze kuajiri watendaji ku-cover zile nafasi ambazo zimebaki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali la pili kama unavyojua Wilaya ya Biharamulo sasa population yetu ni watu 457,114. Jimbo hili ndilo linaloongoza kwa idadi kubwa ya watu kwa Mkoa wa Kagera, lakini kijiografia pia ni Jimbo kubwa zaidi lina vijiji 79, kata 17 lakini zilizotawanyika sana.

Je, huoni kwamba iko haja ya Serikali kutupatia usafiri kwa ajili ya watendaji wa vijiji na kata ili huduma za wananchi ziweze kufika kwa haraka zaidi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la kwanza la Mheshimiwa Ezra Chiwelesa, la lini kibali hiki cha ajira. Nikirejea majibu yangu ya msingi, tutatoa vibali hivi kadri ya bajeti itakavyoruhusu, lakini tayari Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo imeshapata watendaji wa vijiji 20 katika mwaka wa fedha 2021/2022 na 2022/2023. Kwa hiyo, nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge Serikali inatambua upungufu huu na inaendelea kulifanyia kazi na muda si mrefu mtaona watendaji hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali la pili la usafiri. Wote humu ndani ni mashahidi katika awamu hii ya sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanya kwa mara ya kwanza kuanza kutoa pikipiki kwa watendaji wa kata zetu zote nchini. Tayari walikuja Dodoma hapa na wakakabidhiwa pikipiki hizo. Na zile kata ambazo bado zimesalia kuna baadhi ya Wakurugenzi ambao wameanza kununua kwa mapato yao ya ndani na kuunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais wetu. Kwa hiyo niwatake tena Wakurugenzi wa Halmashauri kote nchini kuhakikisha wanatenga fedha ya kununua usafiri kwa ajili ya watendaji wa kata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na inaporuhusu bajeti basi hadi kwa watendaji wa vijiji, lakini mpaka sasa Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kupunguza upungufu huu wa usafiri.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Katika Mkoa wa Arusha kuna watendaji wa vijiji wengi wamekuwa wakikaimu. Mfano tu, katika Wilaya ya Longido kuna watendaji wa vijiji 23 wamekaimu kwa muda mrefu na wana sifa.

Je, ni lini Serikali itatoa ajira kwa watendaji wa vijiji hawa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itatoa ajira za watendaji wa vijiji kadri ya bajeti itakavyoruhusu. Niseme tu, kukaimu utendaji wa kijiji huu, hawa 23 hai-guarantee kwamba ajira zitakapotangazwa kwamba wao ndi wataingia, zitafuata mchakato kama inavyotaka kwa ushindani na wale ambao wataonekana wana sifa za kuajiriwa ndio ambao wataajiriwa na kuwa watendaji wa vijiji. Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge avute subira na kadri ya bajeti itakavyoruhusu Serikali itaajiri.
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Jimbo la Nachingwea lina kata 36, kati ya hizo kata mbili hazina watendaji wa kata, lakini lina vijiji 127 na vijiji 37 havina watendaji wa vijiji. Na kwa kuwa tunajua watendaji hawa ndio wanaosukuma shughuli zote za maendeleo katika maeneo yetu;

Je, ni lini Serikali itatoa vibali kwa ajili ya kupata hawa watendaji ambao watatusaidia kwenye maendeleo kwenye maeneo yetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kata mbili ambazo hazina watendaji na vijiji 37 ambavyo havina watendaji kule Nachingwea ni adhma ya Serikali kuhakikisha kwamba kila kata, kila kijiji kina watendaji. Kadri ya bajeti itakavuoruhusu basi viabali hivi vitaendelea kutolewa. Na nikutaarifu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali iko mbioni kuajiri watendaji wa kata katika kata zote ambazo ziko wazi nchini. Kwa hiyo ni kuvuta Subira, nikuhakikishie kwamba hilo linafanyiwa kazi.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa kuwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan analeta fedha nyingi sana za miradi katika Halmashauri ya Mji wa Ifakara, na kwa kuwa miradi hiyo mingi haiendi vizuri na sababu moja wapo ni kukosekana kwa mtumishi Mkuu wa Idara ya Ujenzi;

Je, ni lini Serikali inapeleka injinia mzoefu wa majengo ya ujenzi Halmashauri ya Mji wa Ifakara ili kunusuru miradi hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikiajiri mainjinia, kulitokea changamoto ya kuwa na upungufu wa mainjinia katika halmashauri zetu nchini, baada ya kuanzishwa TARURA; mainjinia wengi wa halmashauri walihamia wakala wa TARURA. Mwaka wa fedha uliopita Serikali iliajiri mainjinia zaidi ya 265 ambapo kila halmashauri nchini ilipata injinia mmoja, na hivi sasa Serikali ipo katika mchakato wa kuajiri tena mainjinia kwa ajili ya kutoa upungufu huu ambao upo ikiwemo kule kwa Mheshimiwa Asenga na tutaangalia pale ambapo ajira hizi zitapatikana basi kule kwa Mheshimiwa Asinga nao watapata injinia.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Halmashaui ya Wilaya ya Rorya ni mwaka wa tatu sasa haijawahi kuajiri watendaji wa vijiji wala wa kata na kwa kuwa sasa tumeomba kibali kwa ajili ya kupata kuajiri watendaji hawa;

Je, Serikali inachelewa nini kutupa kibali na sisi tuweze kuajiri kwenye maeneo ambayo yana upungufu wa watendaji wa vijiji na watendaji wa kata?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itatoa vibali hivi vya ajira kadri ya bajeti itakavyoruhusu, na tutaangalia katika bajeti iliyotengwa mwaka 2023/2024, kama kuna nafasi hizi zilizotangazwa basi kule Rorya ambapo kuna upungufu na wameomba kibali, kibali kiweze kutolewa. Kama hakuna iliyotengwa basi tutaipa kipaumbele katika mwaka wa fedha wa 2024/2025.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Namshukuru Mheshimiwa Naibu kwa kutupatia baadhi ya shule chache, kama alivyosema, miongoni mwao zikiwepo Rivango, Chikolopola pamoja na Lulindi Maalum, lakini kama Waziri anavyoona shule zilizokuwa mbovu au chakavu ni nyingi sana kwenye majimbo hayo mawili, hususan kwenye Jimbo la Lulindi anaweza akaona, ziko zaidi ya 20 na kitu. Ni lini atafanya jitihada kwa ajili ya kumalizia hizo shule nyingine chakavu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwambe. Serikali inatambua kwamba, shule nyingi za msingi nchini ni chakavu na tayari tumeona jitihada kubwa za Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan za kutafuta fedha kwa ajili ya kupunguza uchakavu huu katika shule zetu za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari katika Halmashauri ya Wilaya ya Masasi ambayo ina Jimbo la Mheshimiwa Mchungahela na Mheshimiwa Mwambe, Shule ya Chikolopa imepokea shilingi milioni 331, Shule ya Rivango imepokea shilingi milioni 101, Shule ya Mkalapa imepokea milioni 120, Shule ya Mwena milioni120 na Shule ya Lulindi Maalum imepokea milioni 54. Fedha hizo ni kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vipya vya madarasa na ukarabati katika shule hizi. Hizi ni jitihada za wazi za Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha upungufu huu wa majengo katika shule za msingi na uchakavu unakwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwatoe mashaka Waheshimiwa Wabunge, Serikali itaendelea kujitahidi kutafuta fedha hizi kwa ajili ya kukarabati shule nyingi zaidi.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika Wilaya ya Itilima kuna shule mbili, shule ya kwanza ni Shule ya Msingi Itubilo ambayo imejengwa mwaka 1965. Majengo yake yamechakaa sana, lakini pia kuna Shule ya Msingi Mwagindu, imejengwa mwaka 1950, nayo majengo yake yamechakaa sana. Je, ni lini Serikali itakarabati majengo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema hapo awali kwamba, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba, inakarabati shule zote ambazo ni za siku nyingi au kongwe katika halmashauri zote nchini. Hivyo basi, Mheshimiwa Mbunge awe na subira, Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kukarabati shule hizi kongwe zilizopo Itilima.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nataka kufahamu ni upi sasa mkakati wa Serikali wa kutenga fedha kuweza kwenda kurekebisha shule chakavu kwenye Halmashauri ya Msalala, ikiwemo Shule ya Msingi Isaka, Kata ya Isaka, Shule ya Msingi Kilimbu, Kata ya Mwaruguru na Shule ya Msingi Butegwa, Kata ya Ngaya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, shule hizi za kule Jimbo la Msalala alizozitaja Mheshimiwa Iddi Kassim zitakarabatiwa kadiri ya upatikanaji wa fedha. Tayari Halmashauri ya Msalala pia imepokea fedha ya kukarabati shule kongwe na chakavu na kujenga shule nyingine kutokana na Mradi wa BOOST ambao fedha zimekwenda. Ni zaidi ya bilioni 230 ambayo Serikali hii ya Awamu ya Sita imetoa kwa kila halmashauri hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kuwaelekeza Wakurugenzi wote wa Halmashauri Nchini, kuhakikisha wanatenga fedha na kuanza ukarabati wa shule chakavu katika maeneo yao ya halmashauri zao kwa sababu, tayari Serikali hii imeshasaidia sana katika ujenzi wa miundombinu mbalimbali kwa kutafuta fedha kutoka Serikali Kuu na wao sasa waanze kutenga kutoka kwenye mapato yao ya ndani.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa, Shule ya Mwanhale, Kata ya Mkula, Wilaya ya Busega, majengo yake yamechakaa sana. Je, ni lini Serikali itakarabati majengo hayo?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itakarabati shule hizi chakavu zilizokuwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Busega kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Pamoja na majibu ya Serikali nina mswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, barabara hii ni mihimu sana, ndiyo barabara fupi na rahisi kuunganisha Kijiji cha Msomela Kijiji cha mfano, na barabara kubwa ya Segera - Arusha. Sasa kwa sababu ya umuhimu huo;

Je, ni lini Serikali itakubali kuipandisha hadhi barabara hii iwe barabara ya Mkoa ihudumiwe na TANROADS, barabara hii pamoja na zile barabara nyingine kama ile ya Msambiazi - Lewa - Lutindi na barabara ya Kwetonge – Tonge – Kizara?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Mvua zinazonyesha sasa hivi Korogwe zimeathiri sana barabara zetu za changarawe;

Je, Serikali iko tayari kuwapa TARURA fedha za dharura ili wakatusaidie kurekebisha hali ya barabara zetu kwenye maeneo ambayo yameathiriwa na mvua?
NAIBU WAZIRI, 0FISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikubaliane na Mheshimiwa Mnzava kwamba barabara hii ni muhimu sana na barabara hii pia imetajwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2025 Ibara ya 55(c)(4) katika ukurasa wa 77. Hivyo ni kipaumbele cha Serikali kuhakikuisha barabara hii inajengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kupandisha hadhi taratibu ziko wazi za kisheria, inatakiwa wao kule waaanze katika vikao vyao vile vya DCC itoke pale ipite katika kikao cha Bodi ya Barabara ya Mkoa, na ikitoka kwenye Bodi ya Barabara ya Mkoa waende wapitishe kwenye RCC na iwasilishwe kwa Waiziri mwenye dhamana na TANROADS ambaye ni Waziri wa Ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili; fedha za dharura kwa TARURA, tayari Serikali inaliangalia hilo na tayri ilikuwa bajeti yao TARURA wao kwa mwaka ya dharura ilikuwa ni bilioni 11. Hivi sasa tunaangalia namna ya kuweza kuwaongezea fedha Kwenda mpaka bilioni 43 ili kuhakikisha kwamba wana fedha ya kutosha ya dharura kwa ajili ya ujenzi wa barabara wakati wote; ije mvua lije jua barabara ziwe zinapitika na ndiyo maana Serikali pia imeiongezea TARURA bajeti kubwa sana kutoka bilini 226 mpaka bilioni 776.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Barabara hii iliyotajwa na Mheshimiwa Mnzava lini Serikali wataanza kuiwekea changarawe ili angalau ianze kupitika wakati wote maana kwa sasa kuna maeneo mengi hayapitiki.
NAIBU WAZIRI, 0FISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi ni barabara ambayo ipo kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, na inaunganisha pia wilaya mbili. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 barabara hii ilitengewa shilingi milioni 230 kwa ajili ya ukarabati wa kiwango cha changarawe, na Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa barabara hii kuhakikisha makalavati yanapitika lakini pia na ule upembuzi yakunifu kwa ajili ya kuwa barabara ya lami.
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa ya maswali madogo ya nyongeza. Nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa maneno yenye matumaini kwa wananchi wa Kata ya Msanda Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza. Serikali imetumia fedha takribani shilingi 500,000,000 kujenga kituo cha afya katika Kata ya Kipeta, Tarafa ya Kipeta lakini mpaka sasa haijapeleka vifaa tiba;

Je, ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba kwenye kituo hiki ambacho kilisubiriwa kwa muda mrefu na wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili. Serikali ilipeleka fedha takribani shilingi milioni 100 kwa ajili ya kujenga zahanati katika Vijiji vya Nderema, Mpembano, Mpona na Lyapona, lakini mpaka sasa zahanati hizo zimekamilika na hazina vifaa tiba;

Je, ni lini sasa Serikali mtapeleka vifaa tiba?
NAIBU WAZIRI, 0FISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kumpongeza Mheshimiwa Sangu, kwa sababu ni majuzi tu alikuja ofisini kwa ajili ya kuangalia zahanati hizi katika Jimbo lake la Kwela. Tayari kuna milioni 150 ambayo imetengwa. Kwenye swali lake la kwanza imetengwa shilingi milioni 150 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kwenye bajeti hii ya 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile nikienda kwenye swali lake la pili; kwenye zahanati zilizokamilka vilevile imetengwa shilingi milioni 50 kwa jili ya ununuzi wa vifaa tiba. Na fedha hizi mtakaponunua vifaa tiba pale Sumbawanga DC ninyi ndio mtaamua viende kwenye vituo vipi; lakini priority iwe katika hivi ambavyo vimekamilika na vinasubiri kutoa huduma kwa wananchi.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tarafa ya Nkwenda ina kituo cha afya kimoja na kituo hiki kimezidiwa na wagonjwa wengi;

Je, ni lini Serikali itajenga kituo ha afya kwenye kata ya Songambele ambako tayari tulishaleta maombi?
NAIBU WAZIRI, 0FISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la Mheshimiwa Bilakwate linalohusiana na Tarafa ya Nkwenda kuzidiwa; ni adhma ya Serikali kuhakikisha inajenga vituo vya afya katika kata za kimkakati kote nchini ikiwemo Jimbo lake lile la Kyerwa. Tutaangalia katika bajeti ya 2023/2024 kama imetengwa fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya. Kama haikutengwa tutatenga fedha katika mwaka wa fedha 2024/2025 kadri ambavyo fedha itapatikana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wananchi wa kata ya Kenyamanyoli waliamua kujenga kituo cha afya kwa nguvu zao wenyewe, kwa maana Kituo cha Afya cha Kenyamanyoli, lakini Serikali iliahidi kupeleka fedha kuanzia mwaka 2019 kwa ajili ya umaliziaji wa maboma yale, mpaka leo hawajapeleka. Ningetaka kujua ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa yale maboma ili wananchi wa Kenyamanyole waweze kupata huduma ya afya?
NAIBU WAZIRI, 0FISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kipaumbele cha Serikali kuhakikisha inaunga mkono jitihada za wananchi popote pale nchini ambapo wamejitoa kujenga huduma mbalimbali wao wenyewe kwenye jamii yao; na Serikali itatafuta fedha kadri ya upatikanaji wake ili iweze Kwenda kuunga mkono hujudi hizo katika Kituo hiki cha Afya cha Kenyamanyoli. Vilevile nichukue nafasi hii kumuelekeza Mkuruhenzi wa kule Tarime Mjini, kuhakikisha anatenga fedha kwenye mapato yake ya ndani kuunga mkono jitihada hizi za wananchi wa Kenyamanyoli.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa taratibu kama hizo kama alivyoeleza Mheshimiwa Naibu Waziri zipo, lakini utekelezaji wake wakati mwingine unaleta changamoto;

Je, ni kwa nini Serikali sasa isifuatilie kujua hatma ya yale mazungumzo yanakuwaje ili mwisho wa siku wananchi wapate huduma wanazozitarajia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali la pili. Kituo cha Afya cha Nakatunguru Jimboni Ukerewe ni muhimu sana, kinahudumia watu zaidi ya 10,000 kwenye Mji wa Nansio pale lakini kina upungufu mkubwa wa miundombinu;

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa miundombinu kwenye kituo kile cha afya cha Nakatunguru ili kiweze kutoa huduma zinazostahili kwa wananchi wa ukerewe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana.
NAIBU WAZIRI, 0FISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi katika majibu yangu ya msingi kwamba utaratibu upo wa kamati hizi za kitaalamu za kushauri katika ngazi ya mkoa. Kuna timu ya mkoa, kuna timu ya halmashauri na mashirika ya kidini ambayo yanamiliki hospitali hizi. Kwa hiyo nipende kuchukua nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kuwataka waganga wote wakuu wa mikoa hapa Tanzania kuhakikisha wanakaa vikao hivi ambavyo vipo kisheria na wenzetu wamiliki wa hospitali hizi ambao ni taasisi za kidini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kweenye swali lake la pili la kituo cha Nakatunguru kule Nansio Ukerewe, kwamba ni lini Serikali itapeleka fedha kumalizia. Serikali itapeleka fedha kumalizia kituo hiki kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa nafasi. Kwa kuwa changamoto za hospitali za kidini inaikumba pia hospitali ya Mbagala Mission kwa jina jingine kwa Buluda, ni hospitali ya muda mrefu, na wananchi wote wa Mbagala na maeneo mengine ya Dar es Salaam wanaitegemea sana hospitali hiyo;

Je, Serikali haioni haja kuwaongezea nguvu kituo kile cha Consolata Sisters Mbagala Mission ili waweze kusaidia vizuri zaidi wananchi?
NAIBU WAZIRI, 0FISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nirejee tena majibu yangu ya msingi, kwamba Serikali inao utaratibu wa kukaa na hospitali hizi teule katika maeneo mbalimbali hapa nchini na kama nilivyokwisha toa maelekezo kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI kwa waganga wakuu wote wa mikoa kuhakikisha wanakaa kuangalia uendeshaji wa hospitali hizi teule na kuona ni namna gani ambavyo zinaweza zikaboreshewa huduma zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongezee tu kwa faida ya Bunge lako Tukufu, kwamba Serikali hupeleka watumishi katika hospitali hizi teule lakini vile vile inapeleka mgao wa fedha katika hospitali hizi teule kuweza kusaidia ili wananchi wa maeneo hayo waweze kupata huduma ambayo wanastahili.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Hospitali ya Mji wa Mafinga inahudumia watu wengi sana kwa sababu jiko barabarani pale, watu wa kutoka Mufindi wanahudumiwa pale lakini miundombinu yake ni chakavu;

Je, ni lini Serikali itakarabati miundombinu hiyo?
NAIBU WAZIRI, 0FISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itakarabati miundombinu hii chakavu pale katika Hospitali ya Mji Mafinga kadri ya upatikanaji wa fedha. Lakini nirudie tena kwamba Wakurugenzi wa Halmashauri wana wajibu wa kuhakikisha wanatenga fedha kwa ajili ya kuanza kutengeneza miundombinu mbalimbali kwenye halmashauri zao. Tayari Serikali kuu mmeona imefanya mengi chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kupeleka fedha nyingi kwenye halmashauri hizi. Ni wakati umefika kwa wakurugenzi, mabaraza ya madiwani nao kuweka kipaumbele cha kusaidia wananchi pale na kuujnga mkono juhudi ambazo Serikali hii ya awamu ya sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imefanya kwa kupeleka fedha nyingi kwenye sekta hizi za elimu na afya.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri yenye matumaini ya Serikali, eneo husika lina umbali wa takribani kilometa 10. Je, Serikali inatoa commitment gani ya kumaliza kilometa tisa zilizobaki?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; Halmashauri ya Mji wa Nanyamba imeazimiwa kujengwa kilometa 20 kwa lami kwa mpango wa TACTIC. Je, lini ujenzi huo utaanza?

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota, Mbunge wa Nanyamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, la kwanza, hii commitment ya fedha kwa barabara kilometa zilizosalia. Kwanza, barabara hii ina jumla ya kilometa 9.5 na tayari katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali ilitenga shilingi milioni 270 kwa ajili ya ujenzi wa madaraja mawili, vilevile kuhakikisha kwamba mifereji ya maji kilometa mbili inajengwa.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa kama nilivyokwishasema kwenye majibu yangu ya msingi, kwamba Serikali imetenga hiyo kilometa moja kwa shilingi milioni 517, tutaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, tayari Mheshimiwa Mbunge mwenyewe, Mheshimiwa Msongozi, lakini vilevile Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro, Mbunge wa Jimbo pale naye amekuwa akiifuatilia sana barabara hii; Mheshimiwa Nyoka, Mheshimiwa Judith Kapinga, wote walikuwa wakifuatilia sana barabara hii na tutaendelea kuitafutia fedha kama Serikali ili kuweza kuhakikisha kilometa zote 9.5 zinakwisha.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali la pili la kilometa 20 za Nanyamba kule Mkoani Mtwara. Mradi huu wa TACTIC hivi sasa upo katika kupata wale wakandarasi ambao watajenga barabara za TACTIC hapa nchini. Tayari timu zile za evaluation zilishakaa kule Jijini Arusha kuhakikisha kwamba tunapata wakandarasi wenye uwezo wa kukamilisha mradi huu. Nimtoe mashaka Mheshimiwa Chikota kwamba muda si mrefu mradi huu utaanza.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Tunaishukuru Serikali kwa kuanza ujenzi wa kilometa 600 za lami kutoka Benki ya CRDB pale Mjini Mugumu kuelekea Hospitali ya Wilaya. Pamoja na ujezni huu barabara hii imesimama sasa kwa muda, na kwa vile inaelekea hospitali ya wilaya, imekuwa na usumbufu mkubwa sana kwa wananchi. Pamoja na jitihada nyingi za mawasiliano na TARURA, wilaya na mkoa bado ujenzi huu hauendelei. Je, ni lini changamoto hizi zitatatuliwa na ujenzi ule ukamilike? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jeremiah Mrimi Amsabi, Mbunge wa Serengeti, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii anayozungumzia Mheshimiwa Mrimi ya CRDB – Hospitali katika Mji wa Mugumu imekuwa na changamoto ya mkandarasi mwenyewe kuwa anafanya kazi kwa taratibu sana. Mkandarasi huyu ameshaitwa kwenye Kamati mbalimbali za pale katika Wilaya ya Serengeti kuangalia ni namna gani anaweza akamaliza barabara hii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tukitoka hapa tutakaa naye tuweze kuona tunaweka mkakati gani na Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Mara na Meneja wa TARURA wa Wilaya ya Serengeti kuona mkandarasi huyu anarudi site vipi kwa haraka sana kumalizia barabara hii.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ni lini Serikali itajenga barabara ya Mijengweni – Shiri Njoro, kilometa 15 tu? Barabara hii ni muhimu sana kwa kusafirisha mazao ya wananchi, lakini wananchi kuja kupata huduma huku Bomang’ombe.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ya Mijengweni itajengwa kwa kadri ya upatikanaji wa fedha, lakini Mheshimiwa Mbunge ni shahidi kwa jitihada za Serikali ambazo zimefanyika katika Wilaya ya Hai, tayari kupitia TARURA tumejenga Barabara ya Nyerere yenye mita 600; tumejenga Barabara ya Stendi – TTCL kwenda RC Church; tumejenga Barabara ya Bomang’ombe pale na tunaendelea. Kuna barabara nne kwa jitihada zake ambazo zinaendelea kujengwa na tutatafuta fedha kwa ajili ya kujenga hizi kilometa 15 kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameomba.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Swali langu ni hili hili nalirudia kila wakati. Ile bypass road kutoka Chekereni kwenda Kahe – Mabogini na TPC wataifanya nini au wana mkakati gani kwa sababu hii iko kwenye Ilani na ahadi za viongozi wetu wakubwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika bypass road hii Serikali inaifanyia kazi kupitia Wakala wa Tanzania ambao ni TANROADS na tutakaa pamoja na wenzetu wa TANROAD kuona mipango yao ni ipi kuhakikisha barabara hii inatekelezwa kama Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ambavyo ilielekeza.
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa, changamoto hii ya miundombinu ya maji mashuleni bado ni kubwa sana hasa katika Mkoa wa Mara. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha ina peleka miundombinu hii ya maji katika shule za Mkoa wa Mara?

Swali la pili, kwa kuwa sasa Serikali inatekeleza miradi ya ujenzi wa madarasa, ujenzi wa mabweni katika shule zetu. Je, haioni haja sasa ya kutenga fungu maalum wakati ikitekeleza miradi hiyo, inaweka na fungu la utekelezaji wa miundombinu hiyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Chomete, swali la kwanza juu ya mkakati wa Serikali kuhakikisha changamoto hii inaisha.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, mradi huu wa SRWSS ni wa miaka mitano na utaisha mwaka wa fedha 2024/2025 na value yake jumla ni shilingi bilioni 119.6, hivyo basi Serikali inaendelea kadri siku zinavyokwenda kupunguza changamoto kwenye mashule kupitia mradi huu.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili la miradi yote inayotekelezwa sasa ya ujenzi wa madarasa na ujenzi wa shule mpya, katika shule zinazojengwa hivi sasa, shule mpya lakini katika ukarabati wa vyumba vya madarasa kwenye shule mbalimbali nchini kupitia miradi ambayo ipo ya EP4R, SEQUIP, BOOST na LANES na mingineyo, component ya matundu ya vyoo vilevile na maeneo ya kuoshea mikono ipo, kwa hiyo sasa hivi Serikali inapopeleka fedha katika maeneo mbalimbali inahakikisha na hizi facilities zinakuwepo.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika,ahsante kwa kunipa nafasi sasa niulize maswali mawili ya nyongeza.

Kwanza, nishukuru sana kwamba Serikali ina mpango wa kutekeleza mradi wa ujenzi wa soko la kisasa eneo la Madiira, lakini ningependa kujua kwamba huo mradi utaanza lini?

Pili, soko hili la Tengeru tunalolizungumzia hapa ni soko maarufu sana la wafanyabiashara hasa akina mama wanafanya biashara zao kwa mateso makubwa wakati wa mvua, kwa sababu wanafanya kwenye matope na mvua nyingi lakini pia wakati wa jua wanaungua jua.

Je, Serikali haioni sasa ni busara kuliboresha soko hili kwa kujenga hanga kama Machinga Complex ya Dodoma? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali yake mawili Mheshimiwa Pallangyo kwanza kuhusu mradi huu utaanza lini?

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, mradi huu utaanza pale ambapo Halmashauri ya Wilaya ya Meru itawasilisha michoro yake Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili na sisi tuweze kuipitia na kuona ni namna gani ambavyo tunaweza tukafanya marekebisho na baadae tukaipeleka Wizara ya Fedha kwa ajili ya kupata fedha kwenye miradi ya kimkakati kama Halmashauri nyingine zinavyopata.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili la kuboresha eneo la soko hili. Hizi zinatakiwa pia ziwe jitihada za Mkurugenzi wa Halmashauri pale ya Meru. Tumeona hapa katika mradi anaoutaja wa Jiji la Dodoma ilikuwa ni mradi wao wenyewe wa Jiji na wametumia mapato yao ya ndani kama Jiji la Dodoma, tumeona katika Halmashauri nyingine nchini kama Shinyanga ambapo wamejenga soko la machinga wadogo wadogo hawa kwa hela zao wenyewe za ndani na maeneo mengine ya Halmashauri zetu hapa Tanzania. Hivyo basi, nichukue nafasi hii kumwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru kuhakikisha anatenga fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa soko kwa ajili ya wafanyabiashara wadogo wadogo.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wakati Mheshimiwa Rais alipofanya ziara Arusha, wananchi wa Jimbo la Meru Magharibi katika Kata ya Kisongo Mateves alituahidi soko: -

Je, ni lini sasa Serikali kupitia TAMISEMI itajenga soko la Kisongo Mateves?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwa sababu hii kama anavyosema Mheshimiwa Lembris ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, tutakaa na wenzetu wa Halmashauri ya Wilaya kuona kama michoro iko tayari iwasilishwe Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kuiombea fedha Hazina na kuanza ujenzi wake mara moja.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika,ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Rungwe soko la Kiwira ni soko maarufu kwa ndizi lakini lina mazingira magumu. Ni lini Serikali itatuongezea fedha kwa ajili ya kulijenga liwe la kisasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itaongeza fedha kwa ajili ya soko hili la Kiwira pale Wilayani Rungwe kadri ya upatikanaji wa fedha lakini ni wao wenyewe kupitia Mkurugenzi wa Halmashauri kuwasilisha maombi hayo Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kuweka katika miradi ya kimkakati na kuanza ujenzi wa soko hili la Kiwira.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Mji wa Chemba ni Mji ambao unakuwa kwa kasi sana lakini hauna soko, naomba kujua nini mkakati wa Serikali kujenga soko katika Mji wa Chemba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali unaanza na wao wenyewe Halmashauri ya Wilaya, hatuwezi tukakaa Ofisi ya Rais, TAMISEMI tukajua kuna uhitaji wa soko katika Halmashauri ya Wilaya ya Chemba, ni wao kupitia Baraza lao la Madiwani liibue mradi huu na kisha kufanya andiko kupitia Mkurugenzi na Afisa Mipango wake na kuwasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kutafuta fedha kwa ajili ya kuwajengea soko wananchi wa Chemba.
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali. Pamoja na demokrasia yetu ya uwakilishi nchi zilizoendelea wamekuwa na utaratibu wa kupokea hoja za wananchi za kimaendeleo na pale wanapoziona zina maana mwananchi huyo huitwa kuja kutetea hoja yake na ambayo inaweza kutumika kwa ajili ya kuendeleza eneo husika, jambo hili limeendelea kufanyika katika nchi nyingi zilizoendelea.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, hivi karibuni Serikali imesitisha utoaji wa asilimia kumi kwa akina mama, vijana na watu wenye ulemavu. Kwa kuwa jambo hili lina maslahi mapana ya nchi yetu. Je, Serikali haioni haja ya kuruhusu kwamba sasa wananchi watoe maoni kuhusu jambo hili, namna bora ya kuweza kulitekeleza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la Mheshimiwa Nollo ni kwamba wananchi wanapewa fursa ya kuhudhuria Mabaraza ya Madiwani na kusikiliza mijadala ambayo inaendelea, kama kuna hoja mahsusi kwa mwananchi au ana idea yoyote ambayo anataka kuiwasilisha anaweza akaonana na Mwenyekiti wa Halmashauri, akazungumza nae na kumpa wazo hilo, kisha Mwenyekiti wa Halmashauri anawasilisha lile kwa wenzake ambao ni Baraza la Madiwani, wakiona inafaa anaalikwa yule mwananchi ili aweze kutoa presentation mbele ya Baraza la Madiwani.

Mheshimiwa Spika, utaratibu huo upo, kwa hiyo niombe tu wananchi wa kule Bahi na maeneo mengine, kuhakikisha kwamba kama kuna mwananchi ana idea nzuri ya kusaidia jamii na Halmashauri, basi awasiliane na Mwenyekiti wa Halmashauri ili Mwenyekiti wa Halmashauri aweze kuongea na Madiwani wenzake na kumkaribisha mwananchi huyo katika Mabaraza ya Madiwani kwenda kufanya presentation. (Makofi)
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Spika, ninaishukuru na kuipongeza Serikali kwa hatua hii kubwa na muhimu iliyofikiwa kama ambavyo imeelezwa kwenye jibu la msingi. Kwa sababu haya yalikuwa ni maombi na mapendezo ya muda mrefu na mara kwa mara kupitia Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, ninaomba niishauri Serikali, mapendekezo yaliyoelezwa kwenye jibu la msingi yaweze kuzingatiwa ili kwa siku za usoni lugha ya alama iweze kuwa lugha ya kufundishia na mawasiliano katika nchi yetu ya Tanzania. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ndiyo, ushauri huo Serikali imepokea.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, kwa sababu ndani ya kipindi cha muda mfupi cha miaka miwili amejenga vituo zaidi ya vinne vya afya ndani ya Wilaya ya Makete kitu ambacho kwa historia ya Wilaya ya Makete hakikuwepo kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa maswali yangu ya nyongeza ni haya swali la kwanza; kuna Kituo cha Afya Kitulo, Kituo cha Afya Bulongwa, Kituo cha Afya Lupalilo na sasa Kituo cha Afya Mbalache hivi vimejengwa, vimekamilika lakini havina vifaa tiba, ipi ni kauli ya Serikali ili vifaa tiba vianze kupelekwa hapa na wananchi wa maeneo yale waweze kuanza kupata huduma kwa ajili ya kuwasaidia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; kuna Kituo cha Afya cha Ipepo au kwa maana ya eneo la Ipepo, wananchi wale wameandaa tofali zaidi ya laki moja, wameandaa mawe kwa ajili ya kuanza kujenga kituo cha afya. Je, ni upi mkakati wa Serikali kuwasaidia wananchi wa Kata ya Ipepo ili waweze kuwa na kituo cha afya kwa sababu wanasafiri umbali wa zaidi ya kilomita 50 hadi 100 kwenda kufuata huduma ya afya kwenye Jimbo langu la Wilaya ya Makete? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la kwanza la Mheshimiwa Sanga la vifaa tiba, Serikali imetenga fedha katika mwaka wa fedha huu ambao tupo wa 2022/2023, shilingi milioni 450 kwa ajili ya kununua vifaa tiba kwa vituo vya afya vilivyopo Wilayani Makete lakini vilevile kuna shilingi milioni 50 kwa ajili ya zahanati zilizokuwepo katika Wilaya ya Makete.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge na Wanamakete kwa ujumla kwamba kuna shilingi milioni 600 ambayo imetengwa kwenye bajeti ya mwaka 2023/2024, kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kwenye vituo hivi vya afya ambavyo Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan imejenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda katika swali lake la pili la lini Serikali itasaidia nguvu za wananchi pale kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Ipepo katika Kata ya Ipepo kule Makete. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba inakuwa na vituo vya afya katika maeneo ya kimkakati na hivi Mheshimiwa Mbunge ameitaja hapa kwamba ipo kilomita 50 kutoka Makao Makuu ya Wilaya, basi nichukue nafasi hii kumwelekeza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Njombe kuhakikisha anafika katika eneo hili la Ipepo na kufanya tathmini na kuona kama kituo hiki cha afya kinastahili kupandishwa hadhi sasa kuwa kituo cha afya kamili na walete taarifa yake Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hiki cha afya.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kata ya Manolo, Halmashauri ya Lushoto wameshajenga Wodi ya Mama na Mtoto na wodi mbili za baba na za akinamama, lakini sasa wako katika ujenzi wa theater. Je, Serikali iko tayari kuunga mkono juhudi hizi za wananchi ili sasa tuweze kukipasisha kiwe kituo rasmi cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la la nyongeza Mheshimiwa Shangazi la Kituo cha Afya Manolo kule Wilayani Lushoto, Serikali itafanya tathimini katika ujenzi huu wa theater ya pale Manolo na kadri ya upatikanaji wa fedha tutahakikisha kwenye bajeti hii tunayoenda kutekeleza kama ipo tutapeleka fedha kuwasaidia wananchi hawa, lakini kama haipo tutatenga katika bajeti ya mwaka 2024/2025, ili kusapoti jitihada zile za wananchi pale.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika Kata ya Mwandoya kuna kituo kikubwa sana cha afya ambacho kinahudumia zaidi ya watu 3,500, lakini kuna upungufu mkubwa sana wa majengo, hakuna jengo la mama na mtoto wala jengo la x-ray. Je, ni lini Serikali itajenga majengo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba wananchi wake wanapata huduma ya afya iliyo bora hasa Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan na ndiyo maana katika mwaka wa fedha uliopita ilitengwa bilioni 117 ya kuhakikisha kwamba tunajenga vituo vya afya vya kimkakati. Sasa tutaangalia kituo cha afya hiki cha Mwandoya ni namna gani tunaweza tukatafuta fedha kama Serikali ya kwenda kujenga majengo ya mama na mtoto. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Halmashauri ya Bunda inajenga hospitali yake kwenye Kata ya Bunda Stoo na tunatambua Serikali imeshatoa bilioni moja na zinahitajika zaidi ya bilioni tatu ili ile hospitali ikamilike. Je, Serikali ina mkakati gani wa kutoa hizo pesa haraka ili hospitali ikamilike na wananchi wa Bunda wapate mahitaji sahihi na kwa karibu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Mheshimiwa Bulaya alivyokuwa ameshasema, Serikali imeanza kupeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya kule Bunda na tutaangalia katika mwaka wa fedha unaokuja huu wa 2023/2024 ni shilingi ngapi imetengwa kwa ajili ya kuendelea na ujenzi huu wa Hospitali ya Wilaya na tutahakikisha kama Serikali tunapeleka fedha mara moja kuendelea na ujenzi huo.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu ya Serikali yanaonyesha kwamba hata hiki Kituo cha Afya kilichopo Misha bado hakijakalimika, hivyo wananchi kushindwa kuona thamani ya fedha za Serikali zinazokwenda maeneo hayo na matokeo yake ni kuweza kuwaambia Wakurugenzi wetu wa Halmashauri wamalizie wakati wanajua kabisa mapato yanayopatikana kwenye halmashauri zetu.

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka fedha ili kumalizia kituo hiki ambacho kitasaidia wananchi wa Kata za Ikomwa, Kakola pamoja na Kabila? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; Tabora Mjini ni moja kati ya Majimbo ambayo yana kata nyingi ambazo ziko mbali, watu wanatembea umbali mrefu mpaka kilomita 30 au 40 kufuata huduma za afya kwenye maeneo ya mjini. Je, Serikali haioni sasa umefika wakati wa kuangalia maeneo ambayo yana changamoto za huduma za afya ili kupunguza changamoto hizi hususani kwenye mikoa yetu ya pembezoni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hawa Mwaifunga, la kwanza hili la fedha za kumalizia. Ni kipaumbele cha Serikali kuhakikisha kwamba inamaliza vituo hivi Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli nikiri hapa mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba Kituo hiki cha Afya cha Misha kinahudumia Kata ya Uyui, Kalunde, Misha, Ikomwa na Kabila na hivyo basi Serikali itatafuta fedha na kuhakikisha zinakwenda mara moja kwa ajili ya kwenda kumalizia majengo haya ili huduma iweze kupatikana kwa wananchi wale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la changamoto hii. Ni kweli katika Manispaa ya Tabora kuna vituo vya afya vitatu ambavyo vimekamilika ambavyo vinatoa huduma kwa wananchi na hiki Kituo cha Misha kikikamilika kitakuwa ni kituo cha afya cha nne na tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya vya kimkakati katika Manispaa ya Tabora ili kuhakikisha huduma ya afya inasogea karibu kwa wananchi.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Tunaishukuru Serikali kwa ujenzi wa Kituo cha Afya Machwechwe pamoja na changamoto zingine ndogo ndogo nimewasilisha TAMISEMI mara kwa mara juu ya changamoto ya kukabiliana nayo ya gharama kubwa za vifaa vya ujenzi. Sasa je, ni lini Ofisi ya Rais, TAMISEMI watatuongezea fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa kile Kituo cha Afya cha Machwechwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaangalia, tutakakaa na Mheshimiwa Amsabi Mrimi kuhakikisha tunaangalia katika mwaka wa fedha huu unaoenda kuanza wa 2023/2024, ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya kumalizia Kituo cha Afya cha Machwechwe kule Wilayani Serengeti na ikiwepo basi tutahakikisha fedha hizo zinaenda mara moja.
MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Katika mpango wa Serikali wa kujenga vituo vya afya vya kimakakati, Kata ya Utiri Halmashauri ya Mji wa Mbinga ni moja ya kata ambazo ziliainishwa kujenga kituo hicho. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hiki cha afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hiki Kituo cha Afya cha Utiri, Wilayani Mbinga, kama nilivyosema hapo awali Serikali ilitenga zaidi ya bilioni 117 kwa ajili ya ukamilishaji wa vitu vya afya vya kimkakati hapa nchini. Tutaangalia kwamba kituo hiki kama kimetengewa fedha, basi fedha hizo ziweze kwenda mara moja na kuanza kufanya ujenzi ili kutoa huduma kwa wananchi wa Utiri na kama fedha hiyo haijatengwa tutahakikisha bajeti inayokuja nayo, tutakitengea fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa kituo hiki.
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, nina swali moja la nyongeza. Kutokana na tatizo hili kuwa kubwa katika Halmashauri ya Mji wa Bunda na hasa kwa sababu kuna kata tatu, nne Kata ya Bunda Stoo, Kata ya Kunzugu, Kata ya Balili na Kata ya Mcharo ambazo zimepakana na Hifadhi ya Mbuga ya Serengeti tatizo ni hili hili. Je, Serikali itakuwa tayari na yenyewe kuweka mipaka kwenye maeneo hayo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Serikali kuhakikisha kwamba mipaka yote katika maeneo ya nchi yetu inatambulika vizuri na hizi kata tatu alizozitaja ambazo zinapatikana na Hifadhi ya Serengeti. Kwanza, nitumie nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kumwelekeza Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya hii na Kamati yake ya Ulinzi na Usalama kufika katika kata hizi na kuangalia mipaka hii kama iko sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama iko sahihi, basi wahakikishe pillar zinazoenda kuwekwa kwenye kata ile ambayo nimetoka kuitaja kwenye majibu yangu ya msingi, basi wahakikishe wanaweka pia pillars katika mipaka hii kati ya kata hizi tatu za Bunda Mjini na Serengeti.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri hayo ya ndugu yangu Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Serikali haijali kuona mashine zile zimekaa kwenye makasha ya kusafirishia kwa miaka saba kuwa zinaweza kuharibika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Serikali ina ushauri gani juu ya wagonjwa wanaokaa kusubiri huduma za x-ray mashine na ultrasound ili kufanyiwa upasuaji, ukizingatia kuwa hata katika hospitali ya Wilaya iliyoko kilomita tano tu kutoka Upuge nako huduma hizi hazipatikani kwa sababu mtumiaji wa mashine hizo hayupo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Maige kama ifuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inajali sana na ndiyo maana kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi fedha ilitengwa kwa ajili ya ujenzi wa majengo yaliyokuwapo mwanzo, lakini nimtoe shaka Mheshimiwa Mbunge ndani ya wiki hii nitaomba mbele ya Bunge lako tukufu, niongozane naye na wataalam wa afya kufika katika Kituo cha Afya cha Upuge na kuona ni namna gani tunaweza kuchukua hatua kwa sababu haikubaliki miaka saba vifaa hivi vikakaa bila kutumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili nirejee kwenye jibu langu la kwanza katika maswali yake ya nyongeza. Tutatatua changamoto hizi tukiwa site palepale na Mheshimiwa Maige, lakini nikiwa katika ziara hiyo kwa sababu kuna Mbunge mwingine wa Tabora ambaye alizungumzia basi tutatembelea pia Kituo cha Afya cha Misha kuhakikisha tuone changamoto zilizopo na kuhakikisha tunazitatua. (Makofi)
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nataka kujua tu ni lini Serikali italeta fedha kwa ajili ya kukamilisha Kituo cha Afya cha Kisaki? Pia ikikupendeza Mheshimiwa Waziri wakati unaenda Tabora upitie Singida uzungumze na wananchi wa Singida pale Kisaki. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema Mheshimiwa Sima tutapokuwa tunaelekea Tabora basi tutahakikisha tunapita Manispaa ya Singida ili kuona kituo hiki cha Kisaki na tutafanya maamuzi tukiwa pale kadri ya bajeti itakavyoruhusu.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana. Kwa kuwa huduma ya ultrasound imekuwa na umuhimu wa kipekee kwa wakinamama wajawazito.

Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuweka huduma hiyo ya ultrasound katika vituo vya kliniki ya mama na mtoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni adhma ya Serikali hii ya awamu ya sita kuhakikisha kwamba inakuwa ina vifaatiba vya kisasa katika vituo vyetu vyote vya afya hapa nchini. Tutahakikisha kwamba kadri miaka inavyokwenda na bajeti inatakavyoruhusu tunatenga fedha kwa ajili ya kununua vifaa vya ultrasound kwenye maeneo yenye wodi za mama na mtoto kama ambavyo Mheshimiwa Kisangi amezungumza.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kata ya Swaya ni Kata ambayo iko pembezoni sana. Je, ni lini Serikali itaamua kujenga kituo cha afya maeneo yale katika Wilaya ya Rungwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakagenda kuhusu kata ya Swaya, ninatoa agizo kwa Mganga Mkuu wa Mkoa kuhakikisha anafika katika Kata hii na kufanya tathmini, kuona ni namna gani kama kuna zahanati pale basi iweze kuombewa kupandishwa hadhi na maombi hayo yaletwe Ofisi ya Rais - TAMISEMI ili tuweze kuyachakata na baada yakipandishwa hadhi tutafutie fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha afya.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Ni lini Serikali itapeleka majokofu kwenye vyumba vya kuhifadhia maiti kwenye vituo vya afya vya Muriti na Bwisya Jimboni Ukerewe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya majokofu haya katika vituo vya afya kule Ukerewe alivyovitaja Mheshimiwa Mbunge kadri ya upatikanaji wa fedha na tutaangalia katika bajeti hii tunayoenda kuitekeleza ya 2023/2024, kama imetengwa fedha tutahakikisha inafika mara moja kwa ajili ya kupunguza changamoto hii iliyopo katika Wilaya ya Ukerewe.

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nimshukuru Mheshimiwa Rais ametupa fedha za x–ray mashine 150,000,000 katika Kata ya Sirari ambayo inahudumia Bumera, Mwema, Susuni Sirari, Kanyange, Itiryo, Mbuguni, Pemba na Ganyange.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kujua x–ray mashine ipo pale hakuna ukaguzi wa mataalam wa mionzi na hakuna mtaalam, hawa wananchi wanapata shida. Nini kauli ya Serikali katika jambo hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hii x–ray iliyopo Kata ya Sirari pale, tuna timu ambayo ni ya Ofisi ya Rais - TAMISEMI inayozunguka nchini kote kutoa mafunzo kwa wataalam wetu wa afya namna ya kutumia vifaa hivi vya kisasa. Sasa nitumie nafasi hii mbele ya Bunge lako tukufu kuelekeza timu ile iweze kufika Mkoani Mara na kufika Sirari kwa ajili ya kutoa mafunzo ili x–ray hii mashine iweze kuanza kutumika mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara ya mwisho timu hii ilikuwa Mkoa wa Simiyu, kwa hiyo siyo mbali kutoka Mkoa wa Simiyu na kuweza kufika Sirari kwa ajili ya kutoa mafunzo haya ili wananchi waweze kupata huduma.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Hospitali ya Wilaya ya Hai x–ray mashine ni ya muda mrefu sana na ni chakavu na imekuwa ikiharibika mara kwa mara.

Je, ni lini Serikali itatununulia x–ray mashine mpya kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya ya Hai?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge amekuwa hili pia akilifuatilia sana la x–ray mashine Wilaya ya Hai, tutaangalia katika mwaka wa fedha huu 2023/2024 kama fedha imetengwa na kama haijatengwa basi tutaangalia katika mwaka wa fedha 2024/2025 kuhakikisha kwamba wananchi wa Hai wanapata x–ray mashine basi Serikali iweze kutenga fedha hizo katika 2024/2025.(Makofi)
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Pamoja na majibu ya Serikali, Kondoa Girls hii ilikuwa ni Shule ya Kidato cha Kwanza mpaka cha Nne, lakini Serikali ilifanya maamuzi ya kuibadilisha kuwa Kidato cha tano na sita na ikawaondoa wale wa O’level. Sasa Kondoa bado tuna uhitaji wa Sekondari ya Bweni ya Wasichana: Je, ni lini Serikali itairudishia sekondari ambayo waliichukua kujengea sekondari ya wasichana ya bweni ya O’Level?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Wananchi wa Kata ya Bolisa wana hamu ya kuona sekondari yao ya kata inaazwa kujengwa, na tayari kama Halmashauri ya Mji tulipokea barua ya mapokezi ya fedha: Sasa ni lini Serikali italeta fedha ili wananchi wa Bolisa waanze kujenga sekondari yao ya kata?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Makoa, kwanza kutokuwa na shule ya bweni ya wasichana katika Halmashauri ya Mji wa Kondoa, Serikali kwa sasa inaweka nguvu katika kuhakikisha kila mkoa unapata shule moja ya wasichana ya bweni ambayo ni kubwa itakayoweza kuchukua watoto katika mkoa husika na tayari shilingi bilioni 30 ilikuwa imeshatengwa, ambapo shule 10 katika mikoa 10 zimeshajengwa na tunaenda kwenye Phase II ambapo tutajenga tena shule tano. Vilevile tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuona Kondoa nao wanapata shule ya bweni ya wasichana ya Kidato cha Kwanza mpaka cha Nne kadiri ya bajeti itakavyoruhusu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la Kata ya Bolisa kupata shule yao ya sekondari, nilijulishe Bunge lako Tukufu kwamba tayari Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI, imeshakamilisha michakato yote ya kuweza kupeleka fedha katika Halmashauri zote 184 nchini kwa ajili ya ujenzi wa shule za sekondari. Muda siyo mrefu Halmashauri hizi 184 zitapata fedha hii kwa ajili ya ujenzi wa sekondari ikiwemo Kata ya Bolisa kule Halmashauri ya Kondoa Mjini.
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa haya majengo yanayoelezwa yamejengwa kwa nguvu za wananchi na fedha za mapato ya ndani ya Halmashauri: Ni lini Serikali kwa maana ya Wizara ya TAMISEMI itapeleka fedha kukamilisha majengo haya yaliyobaki; jengo la maabara, jengo la mochwari na jengo la mganga? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Godwin Emmanuel Kunambi, kwanza nipongeze jitihada za wananchi wa Mlimba kwa kuweza kujenga kituo hiki cha afya kwa shilingi milioni 500. Serikali kwa sasa itatafuta fedha kadiri ya bajeti itakavyoruhusu ili tuweze kwenda kujenga maabara, mochwari na nyumba ya mganga. Tayari Mheshimiwa Mbunge hili alikuwa amekuja kulifuatilia na tunaona uwezekano wa upatikanaji wa hizi fedha katika bajeti ya mwaka huu tunaoenda kuanza 2023/2024. Kama ikikosekana hapo, basi tutenge katika mwaka 2024/2025.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kituo cha Afya cha Ngongowele kilipata fedha za Matokeo Makubwa Sasa, tulipata shilingi milioni 250, mradi ambao umeshaisha; je, Serikali haioni imefika wakati kutupatia shilingi milioni 250 nyingine kumalizia kituo kile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kituo hiki cha afya cha Ngongowele kule katika Halmashauri ya Wilaya ya Liwale, Serikali itatenga fedha ya kumalizia kadiri ya upatikanaji wa fedha hizi na bajeti itakavyoruhusu.

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Tangu mwaka 2010 tuliahidiwa shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Kata ya Nyarubanda, lakini zaidi ya miaka 12 mpaka leo ujenzi haujaanza: Nataka kujua, ni lini hasa ujenzi huo utaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi huu katika Kata ya Nyapanda utaanza kadiri ya upatikanaji wa fedha. Tutaangalia katika bajeti hii ambayo inakuja ya 2023/2024 kama haijatengewa, basi tutaangalia kutenga fedha katika mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei. Je, lini Serikali itakarabati kituo cha Mwika Kaskanzini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika maeneo ambayo kuna zahanati, lakini maeneo ni madogo: Je, Serikali ipo tayari kupandisha zahanati za Rombo kuwa vituo vya afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza; la kwanza kuhusu lini Serikali itafanya ukarabati wa katika Kituo cha Afya cha Mwika, Serikali itafanya ukarabati katika kituo hiki cha afya kadiri ya upatikanaji wa fedha. Tutaangalia katika mwaka wa fedha 2023/2024 kama kimetengewa fedha ya ukarabati, basi tutahakikisha fedha inaenda mara moja. Kama hakijatengewa fedha kwenye mwaka huu wa fedha, tutahakikisha katika mwaka wa fedha 2024/2025 Kituo cha Afya cha Mwika kinatengewa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali la pili la kupandisha hadhi zahanati kuwa kituo cha afya katika eneo la Rombo, tunalipokea hili kama Serikali. Nichukue nafasi hii kumwelekeza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro kufika katika zahanati hizi ambazo zimetajwa na kuangalia kama zinakidhi vigezo vya kupandishwa kuwa vituo vya afya na kuwasilisha taarifa hii katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kuona ni namna gani tunawasaidia wananchi wa maeneo haya kupata vituo vya afya.
MHE. ANTON A. MWANATONA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini maana yangu hasa ilikuwa mgawanyo wa fedha za TARURA kwa kuzingatia mtandao wa barabara katika Halmashauri zetu. Kwa mfano, ukichukua Mbeya peke yake, Rungwe ni ya pili. Mbeya Vijiji ya kwanza, mtandao mkubwa kama kilometa 1,000 na Rungwe inafuata, lakini bajeti tunayopata ni ndogo kuliko Halmashauri nyingine. Kwa hiyo, naomba Serikali ituambie ni vigezo gani vinatumika kugawanya hizi pesa za barabara katika Halmashauri zetu, kwa mfano, utakuta Halmashauri ina kilometa nyingi zaidi, lakini inapata fedha chache?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, mwaka jana 2022 Mheshimiwa Rais alitembelea Rungwe akaahidi kutoa kilometa mbili za lami pale Mji wa Tukuyu: Je, ni lini fedha hizo zitakuja ili mradi huo wa barabara ya kilometa mbili za lami uweze kutekelezwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwantona, la kwanza hili la vigezo vya mgawanyo. TARURA ilipokea vigezo vilevile vilivyokuwepo awali kabla ya taasisi hii kuanzishwa ambapo vilikuwa vimetengenezwa na Road Fund nchini kuweza kuwapelekea fedha Halmashauri mbalimbali. Baada ya TARURA kuanzishwa, changamoto hii Serikali imeiona na tayari Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI Mheshimiwa Angellah Kairuki alielekeza TARURA kufanya tathmini na kuona ni namna gani fedha inaweza ikapelekwa kulingana na barabara ambazo zipo na ukubwa wa maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba tayari kazi hiyo ilikuwa imeshafanyika na baada ya kazi hiyo kufanyika, sasa kuna independent team ambayo imepewa ku-verify tu, kuona. Vigezo ambavyo vitatumika sasa, ni kuona urefu wa barabara, kuangalia ukubwa wa eneo husika, vilevile kuangalia milima, wingi wa mvua, agri-connect katika maeneo hayo shughuli za kilimo zinafanyika kiasi gani, na kadhalika kuweza kutoa fedha ya kwenda kwenye barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la pili la nyongeza la kilomita mbili ambazo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan hii tutaendana kadiri ya upatikanaji wa fedha kuweza kukamilisha ahadi hii. Nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi za Dkt. Samia Suluhu Hassan huwa zinatekelezeka kwa wakati, na tayari tutaangalia katika bajeti ya mwaka huu kupitia Taasisi ya TARURA kuona ni nini kinaweza kikatengwa ili ahadi hii ianze kutekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu aliyoyatoa, naomba kuuliza swali kwamba, Jimbo la Njombe Mjini ambalo ndiyo Halmashauri kubwa kuliko Halmashauri zote katika nchi hii; je, litaangaliwa kwa namna ya kipekee katika hiyo tathmini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Njombe Mjini na maeneo mengine yote ya nchi yetu ya Tanzania ambayo Waheshimiwa Wabunge mnatokea, yataangaliwa kwa vigezo vile vile ambavyo nimevitaja hapa. Ukubwa au urefu wa barabara katika wilaya husika, kuangalia ukubwa wa eneo husika, kuangalia milima, kuangalia wingi wa mvua, kuangalia shughuli za kiuchumi kama kilimo…

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa ameshakuelewa.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Napenda kuuliza, hivi ni lini Serikali itaamua kutengeneza mikataba ya Kiswahili katika utengenezaji wa barabara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, hili la Mheshimiwa Getere, niseme tunalichukua na tutaangalia ni namna gani tunaweza tukaboresha na kuwa na mikataba ya Kiswahili.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii nami niulize swali la nyongeza. Pamoja na kwamba Mji wa Tabora unaitwa Toronto kwa sababu ya ubora wake, lakini kuna kata nyingi ambazo zina shida pale mjini kwenye barabara, hasa Kata ya Ng’ambo, Kata ya Isevya, Kata ya Kitete, na kata nyingine; je, Serikali lini ita…
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Barabara kadri upatikanaji wa fedha hizo katika Kata za N’gambo, Isevya na Kitete katika Manispaa ya Tabora Mjini.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mbunge wangu wa Jimbo la Rungwe ameuliza swali la msingi tukizingatia Wilaya ya Rungwe ina mvua nyingi na ina mtandao mkubwa sana. Ninaomba kuhakikishiwa kwa sababu yeye ndiye swali lake Mbunge wangu ameuliza ni lini mtatutengenezea hizo Barabara za TARURA na kutupatia fedha za kutosha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyokuwa nimeishasema kwenye majibu yangu ya msingi ukiangalia mwaka wa fedha 2020/2021 TARURA katika Halmashauri ya Wilaya Rungwe ilikuwa imetengewa milioni 962 tu lakini mwaka huu wa fedha tunaoenda kuutekeleza TARURA inatengewa fedha kiasi cha shilingi bilioni 2.31 katika Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunakwenda kutekeleza barabara nyingi zaidi kuliko hapo awali na hiyo ndiyo azma ya Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwanza nipongeze sana majibu ya Serikali na nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais na Mawaziri wa Fedha, TAMISEMI na Ujenzi kwa kuendelea kuchakata jambo hili liende vizuri katika mchakato huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina swali moja tu la nyongeza; kwa sababu Serikali ipo katika hatua za upembuzi yakinifu na usanifu wa kina maana yake tayari imeshafanya utambuzi wa barabara zote zitakazoingia kwenye mradi wa DMDP Awamu ya Pili.

Je, ni barabara zipi ndani ya Jimbo la Kibamba ambazo na zenyewe zitakuwa sehemu ya mradi huu DMDP Awamu ya Pili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtemvu, Mbunge wa Kibamba kwa niaba ya Mheshimiwa Dkt. Ndugulile, namna mradi huu ulivyokuwa design kwamba kila Halmashauri katika Mkoa wa Dar es Salaam imewasilisha mapendekezo ya barabara ambazo zitatakiwa kufanyiwa ukarabati kupitia mradi huu wa DMDP II.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumjulisha Mheshimiwa Mtemvu na Wabunge wote wa Dar es Salaam kwamba kwa maelekezo ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI Mheshimiwa Anjela Kairuki wiki ijayo mtaitwa wote Waheshimiwa Wabunge wa Jiji la Dar es Salaam ili kushuhudia utiaji saini wa mradi huu wa consultancy ambazo anaenda ku-design barabara zetu hizi. Kwa hiyo, nimtoe hofu ni barabara zote kama walivyoziwalisha wao katika halmashauri zao ambazo zitawekwa katika mradi huu.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naishukuru Serikali kwa majibu angalau yenye matumaini.

Swali langu la kwanza; barabara ya Rulama -Kanyantama - Ruita mpaka Mabira barabara hii inaunganisha kata nne; Kata ya Kibale, Businde, Kamuli mpaka Mabira na inaunganisha Tarafa mbili na ni muhimu sana kuna wakulima wengi. Ni lini barabara hii itatengewa fedha iweze kutengenezwa ili iweze kupitika kipindi chote?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; ni lini barabara ya Nkwenda mpaka Mabira itapandishwa hadhi iwe chini ya TANROADS kwa sababu inahitaji fedha nyingi na ni muhimu sana kwa wananchi wa Kyerwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Bilakwate, kwanza nitumie nafasi hii mbele ya Bunge lako tukufu kumwarifu Mheshimiwa Bilakwate kwamba ombi lake kama mwakilishi wa Wanakyerwa la fedha kwa ajili ya barabara ya Kasoni - Mkuyu tayari pesa hiyo imepatikana na muda si mrefu Mheshimiwa Mbunge mkandarasi atapatikana ili kuingia site na kuanza ujenzi wa barabara hii kama alivyokuwa ameiomba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye maswali yake; hii barabara ya Ruhama – Kanywaa – Ntama - Ruhita ambayo inaunga kata nyingine na Kata ya Mabira tayari andiko lilikuwa limewasilishwa na Meneja wa TARURA katika Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa na Meneja wa TARURA Mkoa wa Kagera lilishawasilishwa Makao Makuu ya TARURA na walikuwa wameomba shilingi milioni 700 kwa ajili ya ukarabati wa barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kadri ya upatikanaji wa fedha TARURA itapeleka fedha katika Mkoa wa Kagera kwa ajili ya utengenezaji wa barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili barabara ya Nkwenda inayokwenda Mabira kupandishwa hadhi na kuwa barabara ya TANROADS.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taratibu za kisheria ziko wazi, ni lazima wao wenyewe katika Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa waanze na vikao vyao ikiwemo DCC ikitoka DCC waipeleke katika RCC halafu kikao cha Bodi ya Barabara ya Mkoa na baada ya Kikao cha Bodi ya Barabara ya Mkoa wanawasilisha ombi lile kwenda kwa Waziri mwenye dhamana ya barabara yaani Waziri wa Ujenzi ndipo barabara hiyo iweze kupandishwa hadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi naomba niwaase waanze mchakato huo kwa ajili ya kuwasilisha kwenda kwa Waziri wa Ujenzi.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsanste na nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; katika Wilaya ya Meatu kuna vituo vya afya ambavyo vimefunguliwa viwili Iramba Ndogo pamoja na Mwasengela. Iramba ndogo ina wafanyakazi watatu; mmoja ni mganga na wawili ni wauguzi, kwa hiyo hawatoshi kabisa, lakini katika Kituo cha Afya cha Mwasengela chenyewe hakina kabisa watumishi wa afya na kinategemewa kufunguliwa tarehe 1 Julai; naomba majibu ya Serikali kuhusu wafanyakazi katika vituo hivi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili liko katika Hospitali ya Wilaya ya Maswa; Hospitali ya Maswa ni kubwa sana lakini watumishi hawatoshi, naomba nipate jibu la uhakika kwamba ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha katika Hospitali ya Wilaya ya Maswa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Minza, la kwanza la Iramba Ndogo kupata watumishi wa ziada na Mwasengela; niseme tu kama nilivyokwishakutoa maelezo kwenye majibu yangu ya msingi kwamba Serikali inaajiri watumishi wa afya 8,070 na katika hawa tutapanga kwanza kwenye maeneo yale yenye upungufu mkubwa ikiwemo Iramba Ndogo, lakini vilevile kwa sababu kituo hiki cha Mwasengela ni kituo kipya ambacho kinaenda kufunguliwa tarehe 1 Julai na kama sikosei kipo Kisesa, tutahakikisha hizi ajira mpya kwa sababu wataingia kazini mwaka huu wa fedha ambao tunautekeleza sasa na tarehe 1 Julai ni mwaka ule mwingine wa fedha, tayari kituo hichi kinapofunguliwa watumishi hawa wa afya watakuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda tu kwenye hili alilogusia la Hospitali ya Wilaya ya Maswa vilevile kwenye hizi ajira tutapeleka maeneo ambayo yana upungufu mkubwa ikiwemo Hospitali ya Wilaya ya Maswa. (Makofi)
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulingana na ukubwa wa jiografia wa Wilaya ya Hanang; je, ni lini Serikali itaongeza watumishi wa afya katika Hospitali ya Wilaya pamoja na vituo vya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Halamga kuhusu Hanang na vituo vya afya, zahanati, hospitali ya wilaya na vituo vya afya ambavyo vina upungufu wa watumishi, kama nilivyokwishakusema kwenye majibu yangu ya msingi katika ajira hizi zilizotangazwa na Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu ajira 8,070 nitahakikisha pia Hanang wanapata watumishi wa afya.
MHE: DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la watumishi linaendana na vifaa tiba. Njombe tuna vituo vya afya viwili vimejegwa kwa nguvu za wananchi na mapato ya ndani. Watumishi wameshapelekwa tunashukuru Serikali, lakini watumishi hao sasa ni kama hawana kazi kwa sababu vifaa tiba havijapelekwa.

Sasa swali langu, Serikali haioni ni busara kuhakikisha kwamba pale ambapo watumishi wamepelekwa, lakini vifaa tiba havijaenda basi wakafanya haraka kupeleka vifaa tiba ili watumishi hao sasa wafanye kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwanyika la vifaa tiba, kwanza nichukue nafasi hii kuwapongeza sana wananchi wa Jimbo la Njombe kwa kujenga kwa nguvu zao wenyewe vituo hivi vya afya na vilevile Halmashauri ya Mji kwa kujenga pia kwa kupitia mapato yao ya ndani na hili ndio tunatamani kuliona kila Halmashauri ikitenga fedha kwa ajili ya kujenga miundombinu ya kusaidia wananchi katika sekta ya afya na sekta ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa suala la vifaa tiba ni kipaumbele cha Serikali hii ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha vifaa tiba vya kisasa vinakwenda katika maeneo yote nchini ikiwemo kule Wilayani Njombe na tutakaa na Mheshimiwa Mbunge na kuangalia kwenye bajeti iliyotengwa ni kiasi gani kimetengwa kwa jaili ya vifaa tiba na hiyo fedha iliyokuwepo basi vifaa tiba hivyo viweze kupataikana mara moja.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Kata ya Soya, Wilaya ya Chemba tulijengewa na wafadhili, kuna baadhi ya vifaa tiba vipo na baadhi havipo ikiwemo x–ray machine, lakini na watumishi mpaka leo kituo kimekamilika tangu mwaka jana. Hivyo vifaa tiba havijakamilika na watumishi hatuna kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini Serikali itatupelekea vifaa tiba pamoja na watumishi ili hospitali kwa maana ya kituo cha afya hicho kiweze kufanyaa kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Kituo cha Afya cha Kata ya Soya, Wilayani Chemba Serikali itapeleka watumishi, katika hawa watumishi wanaoajiriwa kama nilivyokwisha sema katika majibu yangu ya msingi na kwenye vifaa tiba tutaangalia kwenye bajeti iliyotengwa ni kiasi gani inatakiwa kwa ajili ya kwenda kununua hivi vifaa kama x–ray na vinginevyo basi Serikali iweze kupeleka fedha hizo na vifaa hivi viweze kununuliwa na wananchi wa Soya waweze kupata huduma hii.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na wimbi kubwa la kuhama watumishi kwenye Idara ya Afya kwenye Halmashauri hasa zile za pembezoni. Mfano Liwale tulipata watumishi 80 lakini watumishi wale leo ukienda kuwahesabu hata 15 hawafiki, wanahama 36 wanahamia wawili; je, Serikali ina mpango gani kudhibiti huo uhamaji wa watumishi holela?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, suala ambalo ananiuliza Mheshimiwa Kuchauka Serikali imelitambua na tayari tunaweka mikakati hasa kwenye ajira hizi ambazo wanaingia kazini muda siyo mrefu, kuona tutaweka mikakati ambayo itadhibiti hili la watu kuhama. Lakini pia nichukue nafasi hii kuwaeleza Wakurugenzi wa Halmashauri ambao ndio waajiri katika maeneo haya wahakikishe hawapitishi barua za watumishi ambao hawajathibitishwa kazini. Mtumishi anatakiwa walau akae miaka mitatu katika kituo chake kipya cha ajira, kwa hiyo, wafuate taratibu hizi, wasipitishe barua hizi ili watumishi hawa maana yake wameajiriwa kwenda kujaza upungufu ule ambao upo katika maeneo hayo. Sasa wanapopitisha barua hizi ili hawa wahame tayari wanazidisha upungufu katika maeneo haya.

Kwa hiyo, niliona nichukue muda kulizungumzia hili hapa ndani ili Wakurugenzi wetu wa Halmashauri ambao ni waajiri waweze kuelewa kufuata taratibu hizi za kiutumishi.
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, je, Serikali haioni haja ya kuweka kipaumbele kuongeza watumishi wa afya kwenye Halmashauri mpya ikiwepo Halmashauri ya Mji wa Nanyamba pamoja na Newala Vijijijni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la Mheshimiwa Hokororo, ni kweli tunaona haja ya kuongeza watumishi hasa katika Halmashauri hizi mpya kama ya Nanyamba na ndiyo maana Serikali ilitenga bajeti katika mwaka huu wa fedha kuajiri watumishi 21,390 nchi nzima katika sekta ya elimu na afya, kwa ajili ya kupeleka katika maeneo yenye uhitaji mkubwa kama Halmashauri ya Nanyamba.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana Naibu Waziri wa Afya alitembelea Zahanati ya Kata ya Lemooti, Kijiji cha Lemooti, Wilayani Monduli, Mkoa wa Arusha na kuwaahidi kuwa Serikali itapeleka pesa kwa ajili ya kumalizia miundombinu.

Je, ni lini sasa pesa hizo zitaenda ili kina mama wapate huduma ya uhakika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kupeleka fedha katika Zahanati hii ya Lemooti kule Wilayani Monduli, tutaangalia katika bajeti ambayo imepitishwa na Bunge lako tukufu ya mwaka 2023/2024 kuona ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya ujenzi au ukarabati wa zahanati katika Wilaya ya Monduli ili iweze kuelekezwa katika Zahanati hii ya Lemooti na kama haikutengewa fedha, basi tutaangalia katika mwaka wa fedha 2024/2025 zahanati hii iweze kutengewa fedha.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, pamoja na majibu yake mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri juu ya watumishi na mikakati ambayo ataiweka. Sasa swali langu ni kwamba je, mkakati gani wa ziada utakaouweka hasa kwa Mkoa wa Lindi kwa sababu suala la uhamaji wa watumishi ni kubwa sana? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Salma Kikwete, Mbunge wa Mchinga ni kama ambavyo nimetoa maelezo wakati namjibu Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale ambao wote wanatoka Mkoa wa Lindi na kweli Waheshimiwa Wabunge hawa wamekuwa wakilifuatilia sana suala hili Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuhakikisha Mkoa wao unapata watumishi wa kutosha na watabaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati ambao tumeuweka ni wa kuhakikisha wale wote walioomba ajira hizi, watambue kwanza tutawafahamisha wanapochukua barua zao za ajira kwamba ajira hizi ni zimekwenda kujaza nafasi katika maeneo yenye upungufu mkubwa hapa nchini wa watumishi ili wahudumie Watanzania ikiwemo Mkoa wa Lindi. Hivyo basi itakuwa ni lazima atumikie nafasi hiyo katika eneo hilo ule muda ambao anatakiwa awe katika mtazamio (probation period) wa mwaka mmoja na baada ya hapo bado hatohama walau kwa miaka mingine miwili ina maana jumla inakuwa ni miaka mitatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nirudie tena hapa kusema na kuongea na Wakurugenzi kupitia Bunge lako tukufu hili, wasipitishe barua ya mtumishi yeyote ambaye ni ajira mpya kwa sababu wakati anaomba ajira hiyo alitambua Serikali inafanya kazi kila pembe ya nchi yetu, na kwamba unapoomba kazi hiyo utapangiwa kwenda kuwatumikia Watanzania mahali popote nchini hapa. Kwa hiyo, wanapopewa barua za ajira waende wakatumikie Watanzania katika maeneo hayo.
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafsi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza, imekuwa ikiripotiwa mara kwa mara majanga ya moto katika mabweni ya shule zetu. Je, Serikali imefanya uchunguzi gani kujua chanzo ni nini na ni upi mkakati wa Serikali kupambana na janga hili?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika shule ambazo tayari mabweni yamekamilika kumekuwa hakuna walezi wa watoto au walezi wa wanafunzi katika shule zetu yaani patrons na matrons je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kuwaajiri walezi wa watoto katika shule zetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Regina Qwaray, la kwanza hili juu ya majanga ya moto ambayo hujitokeza katika shule za bweni. Serikali kupitia Jeshi letu la Zima Moto na Uokoaji imekuwa ikitoa mafunzo mbalimbali hasa katika shule hizi za bweni juu ya namna bora ya kujikinga na majanga ya moto.

Mheshimiwa Naibu Spika, na tutaendelea kushirikiana na wenzetu wa Wizara ya Mambo ya Ndani na Jeshi la Zima Moto na Uokoaji kuhakikisha kwamba mafunzo haya yanazidi kutolewa kwenye halmashauri mbalimbali na nitumie nafasi hii mbele ya Bunge lako hili kutoa wito kwa halmashauri za Wilaya zote hapa nchini ambazo zina shule za bweni ziweze kuhakikisha zinashirikiana na Jeshi la Zima Moto na Uokoaji katika kutoa elimu ya kujikinga na moto katika shule zote za bweni.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la pili la Mheshimiwa Regina Qwaray la mabweni kutokuwa na ma-patron na ma-matron, kwa sasa Serikali imeweka kipaumbele katika kuhakikisha inaajiri walimu wa kutosha kadiri ambavyo bajeti inaruhusu tunaajiri. Pale ikama itakapotimia tutaanza kuangalia ni namna gani tutaweza kuajiri ma-patron na ma-matron lakini kwa sasa walimu waliopo ndio wanateuliwa kwa ajili ya kuangalia watoto katika shule zile mabweni ambao ndiyo wanaokuwa ma-patron ndiyo wanaokuwa ma-matron.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutakaa na wenzetu wa Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora kuona ni namna gani bora tunaweza tukapata vibali kwa ajili ya kuajiri ma-matron na ma-patron kwa ajili ya kutimiza ikama na upungufu ambao upo.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Je, ni lini Serikali itajenga Sekondari mpya Kata ya Ketare eneo la Nyaburundu na Kata ya Mihingo eneo la Machimero kwa sababu ni muda mrefu Serikali imeahidi kujenga sekondari hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, lini Serikali itajenga sekondari mpya katika maeneo ambayo ameyataja Mheshimiwa Mbunge, kwa sasa Serikali inajenga shule mpya katika kila halmashauri hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwa Mheshimiwa Getere pia amepata zaidi ya shilingi milioni 580 kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya na tutazidi kutafuta fedha kwa sababu Serikali hii ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka kipaumbele cha kuhakikisha kata zote ambazo hazina sekondari zinajengewa sekondari mpya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge avute subira tutakapomaliza ujenzi wa hii shule ya shilingi milioni 580 ambayo iko jimboni kwake tutaendendelea kutafuta fedha nyingine kwa ajili ya ujenzi wa shule za sekondari katika kata ambazo amezitaja.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Kwa kuwa kuna smoke detecters ambao ndio utaaalamu wa kisasa wa kujua kama moto unakuja. Kwa nini Serikali haioni ni muhimu chombo hicho kuwekwa katika kila jengo la shule au taasisi inayojengwa ili waweze kupata alert?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shally Raymond hili la smoke detectors. Kama nilivyokuwa nimeshazungumza hapo awali tutashikiana kwa karibu na wenzetu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Jeshi la Zima Moto na Uokoaji kuona sasa ni namna gani tunaweza kuhakikisha majengo yote ya shule zetu yanakuwa ya smoke detectors hasa zile shule za bweni ambazo zina wanafunzi wanaolala pale muda wote.
MHE. DKT. CHARLES. S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba Serikali imetoa majibu mazuri na nimeyafurahia sana, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Bodi ya Barabara ya Mkoa wetu wa Kilimanjaro imeshatuma maombi kwenye Wizara ya kuipandisha hadhi Barabara hii ya Chekereni – Kahe – Mabogini – TPC.

Je, tutapata uthibitisho gani kwamba maombi haya yameshughulikiwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, nashukuru sana Serikali imeweza kutengeneza Daraja la Marangu Mtoni; lakini tunaomba kauli ya Serikali kuhusiana na kukamilisha kipande kilichobaki cha barabara hiyo kuanzia Kawawa – Nduoni kuja Marangu Mtoni ambayo ipo pia kwenye Ilani ya CCM, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Vunjo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ni juu ya Bodi ya Barabara kuipandisha hadhi Barabara ya Kahe – Chekereni. Suala hili ni la kisheria na taratibu za namna ambavyo barabara inatakiwa kupandishwa hadhi na kwenda kwa wenzetu wa Wizara ya Ujenzi zipo wazi. Hivyo basi, tutakaa na Mheshimiwa Kimei kuona ni hatua zipi ambazo maombi haya yamefikia ili kuona kama tayari yamefika kwa Waziri wa Ujenzi mwenye dhamana ya kupandisha hadhi barabara hii. Kama maombi haya hayajafika basi tutaona ni namna gani yanaweza kufika ili timu iweze kwenda kufanya assessment na barabara hii iweze kupandishwa hadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naenda kwenye swali lake la pili linalohuau Saraja la Marangu Mtoni, ambalo linaunganisha barabara ya Kawawa – Kahe – chekereni. Nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Vunjo, kwamba Serikali ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mwaka wa fedha 2023/2024 imetenga zaidi ya shilingi milioni 989 kuhakikisha kwamba barabara katika jimbo la Mheshimiwa Kimei zinafanyiwa ukarabati ikiwemo Barabara hii ambayo inaitwa Fungate – Mabogini – Kahe – Chekereni ambapo kwa sasa kuna shilingi milioni 39. Inasubiri tu daraja lile likamailike ili barabara nayo iweze kuendelea kutengenezwa na iweze kupitika.
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Mji mdogo wa Mbalizi una kilomita 33 za vumbi. Je, ni lini Serikali itajenga barabara hizo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Suma Fyandomo juu ya barabara hizi za Mbalizi zenye urefu wa kilomita 33. Tutatuma timu ya kuweza kufanya tathmini kutoka Wakala wa barabara za Vijijini na Mijini (TATURA) ili kuona ni kiasi gani kinahitajika ili kujenga barabara hizi kwa kiwango cha lami. Baada ya kufanya tathmini hiyo tutaona ni kwa namna gani Serikali inaweza ikatafuta fedha kadri ya upatikanaji wake kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hizi.
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Nishukuru Serikali kwa majibu mazuri lakini napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, ni lini Serikali itapeleka fedha kukamilisha ujenzi wa mabweni katika Shule ya Sekondari ya Mogabiri? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, katika Shule ya Sekondari Tarime mabweni yana uwezo wa ku-accommodate watoto 750 lakini wanafunzi waliopo katika shule ile ni zaidi ya 1,500. Je, ni lini Serikali itajenga mabweni zaidi ili kutoa huduma ya mabweni mazuri katika Shule ya Sekondari Tarime?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kembaki. La kwanza kuhusu mabweni katika Shule ya Sekondari Mogabiri kwamba ni lini Serikali itapeleka fedha kumalizia ujenzi wa mabweni.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anafahamu kwamba Serikali Kuu ilipeleka shilingi milioni 200 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni na madarasa mawili katika shule hii. Walibadilisha eneo ambalo lilikuwa limewekwa mwanzo kwa ajili ya ujenzi wa mabweni haya hivyo kupelekea gharama za ujenzi kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, tathmini imeshafanyika na Halmashauri ya Tarime Mji na imefahamika kwamba inahitajika shilingi milioni 120 kwa ajili ya ukamilishaji wa mabweni haya. Serikali iko katika mchakato wa kutafuta fedha hizi kupitia mapato ya ndani ya halmashauri yenyewe na Serikali Kuu ili kuweza kumalizia ujenzi wa mabweni haya. Mkurugenzi wa Halmashauri hii tayari ameshaleta maombi hayo Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili la Shule ya Sekondari ya Tarime kuwa na wanafunzi wengi, ni kweli kwamba shule hii ina wanafunzi wengi. Kwa kulitambua hilo, Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI katika kupanga wanafunzi wa kidato cha tano mwaka huu shule hii ilipelekewa wanafunzi wachache kulingana na miundombinu ambayo ipo. Tunaendelea kutafuta fedha ili kuona ni namna gani ambavyo tunaweza tukapeleka kwa ajili ya kuongeza mabweni katika shule hii ya Tarime Sekondari.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Kwa kuwa wanafunzi wanaosoma katika Shule ya Sekondari ya Masinda, Kata ya Ihanja, Jimbo la Ikungi Magharibi hutembea umbali mrefu kufuata huduma za masomo. Napenda kujua je, ni lini Serikali itajenga bweni katika shule hiyo ili kuwawezesha wanafunzi kusoma kwa utulivu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itajenga mabweni katika Kata hizi za Msinda na Ihanja ambazo wanafunzi wanatembea umbali mrefu kufuata elimu kadri ya upatikanaji wa fedha. Natoa wito kwa halmashauri hii waanze kujenga kwa mapato yao ya ndani wakati Serikali Kuu inatafuta fedha kwa ajili ya kwenda kumalizia majengo haya.

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia, Serikali hii ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imepeleka shilingi bilioni tatu katika Mkoa wa Singida kwa ajili ya ujenzi wa shule ya wasichana pale Solya. Ambayo watoto wote wa kike katika Mkoa wa Singida wataenda pale Solya kwa ajili ya kupata elimu ambapo tayari kuna mabweni. Hivi karibuni kuna shilingi bilioni moja nyingine imeongezwa na Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za walimu katika shule ile ya Mkoa wa Solya.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, ya kwanza umesema imepeleka kiasi gani?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali ilipeleka shilingi bilioni tatu na sasa imepeleka shilingi bilioni moja.

SPIKA: Sawa, maana ulisema shilingi milioni tatu sasa nataka Taarifa zetu Rasmi za Bunge zikae sawa.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni shilingi bilioni tatu.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Spika ahsante kwa kunipa nafasi.

Je, ni lini Serikali itajenga bweni katika shule ya sekondari ya Busagara ili tuweze kutoa huduma ya Kidato cha Tano na cha Sita kama tulivyoomba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itajenga mabweni katika shule hii ya Busagara kadri ya upatikanaji wa fedha. Mkurugenzi wa Halmashauri aanze kutenga fedha kwenye mapato ya ndani kwa ajili ya ujenzi wa mabweni haya na kisha kuleta maombi Serikali Kuu kwa ajili ya kumalizia mabweni haya ambayo yataanza kwa jitihada za halmashauri yenyewe.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Serikali imepeleka shilingi milioni 470 kwa shule za Kata 231. Je, ni lini sasa Serikali itapeleka fedha za mabweni kwa ajili ya shule hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, shilingi milioni 470 zilizopelekwa kwenye shule hizi 231 nchini ilikuwa ni kwa ajili ya kata ambazo hazina sekondari bado katika Taifa letu hili la Tanzania. Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliona kuna umuhimu wa kuhakikisha kata ambazo bado hazikuwa na sekondari zinapata sekondari na ndiyo maana ametoa shilingi milioni 470 na mwaka huu kuna shilingi milioni 560 na kuna wengine wamepata hadi shilingi milioni 603 kwa ajili ya ujenzi wa shule hizi za Kata.

Mheshimiwa Spika, tutakapomaliza ujenzi wa shule hizi za kata Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya mabweni kwenye shule hizi.
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona. Serikali itapeleka lini fedha za kumalizia ujenzi wa bwalo la chakula katika shule ya sekondari ya mfano ya wasichana ambayo ipo katika Jimbo la Shinyanga Mjini?

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali kwanza inamalizia miundombinu mingine, hii ni shule kama niliyosema mwanzo ya Singida ya shilingi bilioni tatu ambayo imejengwa pale Shinyanga Mjini.

Mheshimiwa Spika, Shinyanga Mjini walipata bilioni tatu kwa ajili ya ujenzi wa shule hii ya wasichana ya Mkoa wa Shinyanga, na tayari kuna shilingi bilioni moja nyingine Serikali hii ya Awamu ya Sita imepeleka kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu iliyokuwa imesalia na baada ya hapo itafanyika tathmini nchi nzima kwa ajili ya mabwalo ambayo yanakuwa bado hayajakamilika ili Serikali iweze kutafuta fedha na kuipeleka kwenye ukamilishaji huo.
MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Spika ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa hizi shilingi milioni 470 kuna baadhi ya maeneo sekondari hizi hazikukamilika bado maabara nyingine hazikukamilika, je, Serikali ina mpango gani wa kufanya tathmini ya kina na kuweza kuongeza ili miundombinu ya shule hizi mpya ikamilike? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Subira Mgalu. Hizi shilingi milioni 470 ambazo zilikwenda kwenye ujenzi wa shule za Kata kwenye kata ambazo hazikuwa na shule zilienda na maelekezo maalum na zilitakiwa kutosha. Kuna Halmashauri kwa mfano pale Kongwa Mkoani Dodoma na Bahi Mkoani Dodoma walimaliza kwa shilingi milioni 470. Ni wao kule chini ambao hawakutekeleza maelekezo yaliyopelekwa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI na wakategemea kuna fedha nyingine ya kuja kumalizia.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilishafanya tahmini na baada ya tathmini hiyo ikaongeza fedha kwenye awamu hii ya pili kutoka shilingi milioni 470 mpaka kwenye minimum ya shilingi milioni 560 katika halmashauri zote hapa nchini. Tutaendelea na tathmini kuona ni namna gani tunaweza tukatafuta fedha kwa ajili ya kumalizia kule ambapo hawakumalizia lakini wengine ilikuwa ni uzembe wao wenyewe.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa fedha hizi shilingi milioni 470 ziligawanywa kwa kiwango sawa nchi nzima wakati gharama za ujenzi hazifanani kati ya Dar es Salaam na mikoa mingine, ni upi mkakati wa Serikali katika kuhakikisha kwamba wanapogawa fedha zisifananishwe katika mikoa yote? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama nilivyokuwa nimemjibu Mheshimiwa Subira Mgalu namjibu Mheshimiwa Kanyasu. Baada ya shilingi milioni 470 hii kwenda na kuonekana kuna changamoto baadhi ya maeneo kwa mfano Makete kwa Mheshimiwa Festo Tuntemeke Sanga, wao mchanga wanauchukua Makambako kuweza kwenda kujenga kule Makete kwa hiyo, gharama inakuwa tofauti.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana kwenye awamu hii ya pili fedha ikaongezwa kwa kulingana na maeneo. Fedha waliyopata Dar es Salaam siyo aliyopata Mheshimiwa Sanga kule Makete na siyo aliyoipata Mheshimiwa kule Mbinga Vijijini.
MHE. GEORGE N. MALIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Shule ya Sekondari ya Berege yenye Kidato cha Tano na cha Sita ina idadi kubwa ya wanafunzi lakini ina upungufu mkubwa wa mabweni. Je, ni lini Serikali itajenga mabweni katika shule hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itajenga mabweni katika Shule ya Sekondari Berege kule Wilayani Mpwapwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Nitoe wito kwa Mkurugenzi wa Halmashauri kuanza kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa mabweni haya katika Shule ya Sekondari Berege na kisha kuleta maombi vilevile Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa ajili ya kuweza kutafutiwa fedha ya kuweza kuendelea na ujenzi wa mabweni hayo.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Ujenzi wa hostel unahitaji miundombinu ya maji na shule nyingi hazina maji, kwa mfano Shule ya Ndugu iliyopo Mbozi. Ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha maji yanakuwepo kwenye shule zote za hostel? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni mkakati wa Serikali kuhakikisha shule zote zinazojengwa ambazo ni za bweni zinakuwa na maji. Ndiyo maana tunasisitiza coordination kati ya taasisi zote za Serikali katika maeneo husika. Pale ambapo shule inajengwa, Mkurugenzi wa Halmashauri afanye kazi kwa karibu na wenzetu wa RUWASA kwa ajili ya kuhakikisha miundombinu ya maji inafika karibu.

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya alikotaja Mheshimiwa Neema Mwandabila kuhakikisha kwamba anawasiliana na wenzetu wa RUWASA kuvuta maji katika shule hii ambayo maji bado hayajafika.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali langu la kwanza; kwa kuwa fedha za ujenzi zilitengwa tangu 2023/2024 na kwa kuwa eneo hakuna;

Je, ni kwa nini hizo fedha zisitumike sasa kufidia eneo la kujenga stendi hii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; kutokana na umuhimu wa stendi hiyo juu ya Serikali pamoja na wananchi wa Temeke;

Je, haioni sasa kuna umuhimu wa kuwa na sababu ya kuipa fedha za miradi ya mikakati Halmashauri yetu ya Temeke ili kuendeleza ujenzi huu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Chaurembo; la kwanza, hili la mwaka wa fedha 2024/2025 hii ni fedha ambayo wameitenga. Kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, fedha hii bilioni mbili imetengwa katika mwaka wa fedha tunaoenda kuanza, yaani July mwaka 2023/2024 sasa ni maamuzi yao wenyewe kupitia kikao chao cha finance na maamuzi ya halmashauri, kama wataweza kufanya fidia kutokana na fedha hii wanaweza wakalipa ili wa-secure ili lile eneo liwe ni la kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali la pili, umuhimu wa Serikali kuipa fedha, Halmashauri ya Manispaa ya Temeke. Tunatambua kwamba ni jambo la muhimu sana kuwa na maeneo ya miradi ya kimkakati hapa nchini ili kuziwezesha halmashauri zetu kuongeza uwezo wa kipato. Tutawapatia fedha wakiandika andiko na kulileta Ofisi ya Rais TAMISEMI na kisha sisi kulichakata na kulipeleka katika Wizara ya Fedha ambapo ndio wanaotoa fedha hizi. Kwa hiyo niwaatoe hofu wana Temeke na wana Mbagala kwamba pale tutakapo pokea andiko lao basi tutatenga fedha hizo kwa ajili ya ujenzi wa stendi hii.
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, wakazi wa Mkoa wa Kagera wamekuwa wakipata adha kwa kukosa stendi ambayo iko ndani ya Manispaa ya Bukoba, ambayo Mbunge wa Jimbo ndugu yangu Steven Byabato amekuwa akifatilia.

Je, ni lini sasa Stendi hiyo itajengwa ili kuweza kusaidia wananchi wa Mkoa wa Kagera?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kyombo kuhusu stendi ya Manispaa ya Bukoba. Serikali itapeleka fedha hizo pale maandiko haya yatakuwa yamepitiwa na kuona sustainability.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni miradi ya kimkakati, na kwa kuwa ni ya kimkakati lazima ioneshe sustainability, kwamba watakapopatiwa fedha na kujenga miradi hii basi halmashauri itaweza kuingiza mapato ya kujiendesha. Kwa hiyo pale ambapo tutamaliza mchakato wa ku-review andiko hili lililoletwa na Manispaa ya Bukoba tutawasilisha Wizara ya Fedha ili nao waweze kutenga fedha kwa ajili ya stendi hii.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia nafasi niweze kuulizwa swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, halmashauri ya Wilaya ya Karatu pia ina mpango wa kujenga stendi ya kisasa, na kwenye bajeti ijayo, halmashauri umetenga fedha kidogo, tunajua haitaweza kutosheleza.

Je, Serikali kuu iko tayari sasa ku top-up hicho kidogo kilichotengwa na halmashauri ili malengo yaweze kufikiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Paresso la Stendi ya Karatu. Kwanza ni pongeze jitihada za halmashauri ya Karatu kwa kutenga fedha zao kwenye mapato ya ndani kwa ajili ya ujenzi wa stendi hii. Ni dhamira ya Serikali hasa hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha inawezesha halmashauri zetu zote nchini kuwa na uwezo wa kupata mapato, kama nilivyosema awali, ambayo ni sustainable kwa ajili ya uendeshaji wa halmashauri hizi. Hivyo tutakapo pokea andiko kutoka Halmashuri ya Karatu juu ya ujenzi wa stendi hii basi tutaangalia tutachakata andiko hilo na kuliwasilisha Wizara ya Fedha.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hali iliyoko Kalenga ni sawa sawa na hali iliyoko Busanda tunavyo vituo viwili vya Chikobe na Bukori. Nini mkakati wa Serikali wa kuviboresha vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu swali lake la nyongeza la lini Serikali itatenga fedha za katika Vituo vya Afya vya Chikobe na Bukoli. Ni lengo la Serikali kuhakikisha inajenga vituo vya afya vya kimkakati kote nchini; na ndiyo maana katika mwaka wa fedha huu ambao unamalizika tarehe 30 Juni mwaka huu Serikali ilitenga bilioni 117 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya vya kimkakati kote nchini. Hivyo basi tutaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi huo. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pale ambapo fedha zitapatikana tutavitenga vituo hivi vya afya vya Chikobe na Bukoli.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Kituo cha Afya cha Kiloreli kilipandishwa hadhi, kutoka zahanati na baadaye kikawa kituo cha afya, lakini bado hakina majengo yoyote yenye kukidhi kuwa kituo cha afya;

Je, Serikali ina mpango wowote kuleta fedha kwa ajili ya kuongeza majengo pale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba inajenga majengo yote ambayo yanahitajika kwenye vituo vya afya hapa nchini, kikiwemo ambacho amekitaja Mheshimiwa Songe cha kule Wilayani Busega. Hivyo basi kadri ya upatikanaji wa fedha tutahakikisha tunapeleka fedha katika kituo hiki cha afya ili kiweze kuapata majengo yanayohitajika.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wananchi wa Bunda Mjini katika Kata ya Manyamanyama walianza ujenzi wa nyumba mbili za watumishi kwa nguvu zao;

Je, ni lini Serikali sasa mtakamilisha maboma hayo ya nyumba za watumishi ambayo yamekaa kwa muda mrefu kwenye Hospitali ya Manyamanyama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitumie nafasi hii kuwapongeza sana wananchi wa Bunda Mjini na wa Kata hii ya Manyamanyama kwa kuweza kujitoa na kuanza ujenzi wa majengo ya nyumba za watumishi. Serikali itafanya tathmini ya majengo hayo kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Bunda Mjini, na pale tathmini itakapokamilika tutaona ni namna gani tunatenga fedha katika mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba nipongeze majibu mazuri ya Serikali. Lakini pamoja na pongezi hiyo naomba niulize maswali madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uhitaji wa vituo vya afya kwa ajili ya kutoa huduma za afya unahitajika sana katika Wilaya ya Kalambo na Halmashauri ya Kalambo na wananchi kwa kulijua hilo wameweza kujenga zahanati nane na ziko usawa wa lintel. Zahanati hizo ni pamoja na Uyumi, Sengakalonje, Limba, just to mention. Je, Serikli haioni kwamba iko sababu ya kuhakikisha kwamba inapeleka fedha ili kumalizia juhudi kubwa zilizofanywa na wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, uhitaji wa kujenga kituo cha afya katika Kata ya Katete ni wa muhimu sana kwa kuzingatia jiografia yake; Je, Serikali haioni kwamba iko sababu ya kuhakikisha kwamba katika bajeti inayokuja maeneo haya yanapelekewa fedha ili vituo vya afya vijengwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kandege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza juu ya hizi zahanati ambazo zimejengwa kwa jitihada za wananchi wa kule Kalambo. Kwanza nitoe pongezi tena kwa wananchi wa kule Kalambo kwa jitihada zao za kujenga maboma haya ya zahanati, lakini vile vile niseme mbele ya Bunge lako tukufu kwamba ni azma ya Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha ina boresha afya za Watanzania kwa kujenga zahanati na vituo vya afya, hospitali za wilaya na hospitali za mikoa na rufaa kadri ya upatikanaji wa fedha. Hivyo basi sisi kama Serikali tutaangalia zahanati hizi na kuona ni namna gani tunaweza tuka-support katika mwaka wa fedha wa 2024/2025 katika umaliziaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda katika swali lake la pili la kujenga Kituo cha Afya cha Katete. Tutatuma timu kule Kalambo kwenda kufanya tathmini ya Kituo hiki cha Afya cha Katete, na tutaona ni namna gani tunaweza tuka-support jitihada hizi ambazo Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa kule Kalambo wote wamezifanya, za kupata kituo cha afya hapa. Mara tu tathmini itakapokamilika basi tutaona ni namna gani tunatenga fedha katika mwaka wa fedha wa 2024/2025.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Kwa kuwa nilishaomba Kata ya Mgombasi tunashida ya kuwa na kituo cha afya ilhali ni kata ambayo ina watu wengi sana.

Je, Serikali iko tayari kutuambia ni lini au iko katika mpango wa bajeti hii kujenga kituo cha afya kata ya Mgombasi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyotoka kujibu swali la Mheshimiwa Kandege la kutuma timu kufanya tathmini ya kuona wingi wa watu na uhitaji wa kituo cha afya, basi pia nichukue nafasi hii kusema kwamba timu hii tutahakikisha pia inafika kwa Mheshimiwa Kawawa kule katika kata ya Mgombasi na kufanya tathmini na kuona idadi ya watu waliokuwa pale na uhitaji uliopo ili Serikali iweze kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha afya.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kata za Kia, Muungano, Uroki, Mnadani na Weruweru ni kata ambazo hazina vituo vya afya na wananchi wanatembea umbali mrefu sana kwenda kufata huduma kule Bomang’ombe.

Je, ni lini Serikali itajenga vituo vya afya kwenye kata hizi muhimu sana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itajenga vituo vya afya hivi muhimu katika Kata za Kia, Muungano, Uroki katika halmashauri ya Wilaya ya Hai kadri ya upatikanaji wa fedha. Lakini vile vile nichukue nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kumwelekeza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro kuweza kufanya tathmini ya zahanati hizi zilizoko katika kata alizozitaja Mheshimiwa Saashisha ili kuona ni namna gani zinakidhi vigezo vya kupandishwa hadhi na kuwa vituo vya afya ndipo tuweze kuona ni namna gani tunatenga fedha katika mwaka wa fedha wa 2024/2025.

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa juhudi kubwa za Serikali zimefanyika kujenga hospitali vituo vya afya vya kileo;

Je, Serikali ina mpango gani kuhimarisha huduma ya kinywa na meno katika vituo vya afya na zahanati zote nchini, kwa sababu sehemu hiyo inaonekana kusahaulika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha inaboresha afya za Watanzania ikiwemo afya ya kinywa na meno. Na ndio maana Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imetenga fedha nyingi sana katika ununuzi wa vifaa tiba vikiwemo hivi vya kinywa na meno. Tayari tuna timu ya Ofisi ya Rais TAMISEMI ambayo inazunguka kwenye maeneo yote yaliyopatiwa vifaa tiba kutoa mafunzo kwa wataalam wetu kuona ni namna gani wanaweza kuanza kutumia vifaa hivi kutoa huduma ya kinywa na meno kwenye hospitali zetu za wilaya na kwenye vituo vyetu vya afya vya kimkakati.
MHE AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kituo cha Afya Kabwe kikikamilika kinategemea kuhudumia zaidi ya kata tatu. Je, ni lini sasa Serikali itapeleka fedha ili kumalizia kituo hiki kifanye kazi katika hizo kata tatu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itapeleka fedha katika Jimbo la Nkasi kwa Mheshimiwa Aida kule kwa ajili ya kujenga kituo cha afya ambacho amekitaja kadri ya upatikanaji wa fedha. Vilevile nitumie nafasi hii kusema tutatuma timu ambayo nimeisema pia itaelekea kule Kalambo kwa sababu ni mkoa mmoja timu hii pia iweze kufika katika kituo hiki cha afya na kufanya tathmini na kuona ni namna gani tunaweza tukatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hiki cha afya.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mheshimiwa Waziri Mkuu alipofanya ziara kwenye Wilaya ya Chemba kwenye Kijiji cha Itwalo aliahidi Serikali kujenga kituo cha afya, lakini hivyo hivyo kwenye Kata ya Tarangi. Naomba kujua ni lini utekelezaji wa ujenzi huu utafanyika? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Monni kwanza nilitaarifu Bunge lako kwamba, Serikali inatoa kipaumbele cha kukamilisha ahadi zote za Viongozi wetu wa Kitaifa kuanzia Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi tutaangalia katika kata hizi mbili ambazo Mheshimiwa Monni amezitaja ni namna gani tunaweza tukatenga fedha ama kama imetengewa fedha kwenye mwaka huu wa fedha unaoenda kuanza wa 2023/2024, tuweze kuanza ujenzi huu mara moja na kama fedha haijatengwa, basi tutenge fedha kwenye mwaka wa fedha wa 2024/2025.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Suala la andiko tayari Wilaya ya Chemba mwaka 2020/2021 tulishaandika hilo andiko na likaenda TAMISEMI na TAMISEMI wakatushauri tuanze kwa mapato yetu ya ndani. Mpaka sasa tumeshatumia zaidi ya milioni 36 kwa ajili ya ulipaji wa fidia pamoja na kufanya usafi katika eneo hilo. Sasa tunataka kujua, je, ni lini Serikali inakwenda kutekeleza maagizo yake kwenye suala zima la ujenzi wa stendi hii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, stendi hii pia mwaka 2020 Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati John Pombe Magufuli alipopita Wilaya ya Chemba wananchi wa Wilaya ya Chemba walimwomba ujenzi wa stendi hii na akaahidi itajengwa haraka iwezekanavyo. Sasa na Mheshimiwa Waziri umesema hapa kwamba mko kwenye mchakato wa kukamilisha ahadi zote za viongozi. Je, ni lini Serikali inakwenda kutekeleza ahadi hii ya Hayati John Pombe Magufuli ili tuweze kumuenzi wananchi wa Wilaya ya Chemba? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kunti Majala, hili la kwanza la andiko. Mpaka sasa Ofisi ya Rais, TAMISEMI haijapokea andiko lolote kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Chemba juu ya ujenzi wa stendi hii, si kusema kwamba Serikali haijapokea, andiko hili huenda liliandikwa likapelekwa moja kwa moja Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutafuatilia juu ya andiko hili la Chemba na nitakaa na Mheshimiwa Mbunge kuweza kuona andiko hili limefikia wapi na kama kuna marekebisho yoyote, basi yaweze kufanyika na kurejeshwa tena kufanyiwa tathmini ili fedha iweze kutafutwa kadri ya upatikanaji wake kwenda kujenga stendi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la ahadi ya Mheshimiwa Rais, nirejee tena kusema ni kipaumbele cha Serikali kuhakikisha inatekeleza ahadi zote za Viongozi wetu Wakuu wa Nchi kuanzia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu wa Rais na Waziri Mkuu kadri ya upatikanaji wa fedha na tutaangalia ili tuone tunatenga fedha kwenye mwaka upi wa fedha kadri bajeti itakavyoruhusu.
MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Serikali ina mpango wa kujenga miradi ya kimkakati katika halmashauri mbalimbali, Halmashauri ya Mji wa Mbinga ni moja ya halmashauri ambayo inatakiwa ipate miradi hiyo ya kimkakati, nataka nijue kupitia mradi wa TACTIC ni lini serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kujenga mradi huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii ya kimkakati upatikanaji wake unaendana sambamba na tutakavyopokea maandiko kutoka kwa wataalam wetu kwenye halmashauri mbalimbali nchini ikiwemo Halmashauri ya Mbinga na Mradi wa TACTIC alioutaja upo unaratibiwa na Taasisi ya TARURA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakaa na Mheshimiwa Mbunge kuona kama TACTIC phase one mradi wa mkakati wote upo katika halmashauri ile, kama haupo tuone ni phase two, kama haupo tuone kama ni phase three, lakini nitumie jukwaa hili la Bunge lako Tukufu kusema tu kwamba kuwaasa wataalam wetu Maafisa Mipango na Wakurugenzi wa Halmashauri kuwa wabunifu wanapofanya maandiko haya ya miradi ya kimkakati. Lengo la Serikali kutoa miradi hii ya kimkakati ni ili halmashauri ziweze kupata uwezo wa kimapato, wasibuni tu mradi ili mradi halmashauri fulani imefanya na wao wakataka, waangalie jiografia yao, eneo lao, ni mambo gani ambayo wakiyafanya basi miradi hii itawaingizia kipato.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Halmashauri ya Wilaya ya Momba ni miongoni mwa halmashauri 56 ambazo zimewekwa kwenye kundi ambalo tutapangiwa hela za maendeleo asilimia 20. Je ni upi mkakati wa TAMISEMI kutujengea stendi kwenye Kata ya Kamsamba ukanda wa chini, Kata ya Ikana ukanda wa juu kwa sababu sehemu zote hizi zinaunganisha Mkoa wa Songwe na Mkoa wa Rukwa na kuna uhitaji kubwa sana wa stendi ili zitumike kaka chanzo cha mapato kwenye halmashauri.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Sichalwe amekuwa akilifuatilia sana hili na amekuja mara kadhaa Ofisi ya rais TAMISEMI kulifuatilia hili jambo na tutaendelea kutenga fedha kadri ya upatikanaji wake ili tuweze kuwajengea wananchi wa Momba stendi hizi na kuiwezesha Halmashauri ya Momba kuwa na uwezo wa kupata fedha ya mapato kutokana na miradi hii.

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naishukuru Serikali kwa majibu mazuri ya kuona mahitaji ya barabara za lami kwenye Jimbo la Ukonga. Naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mvua zinazoendelea kunyesha Jijini Dar-es-Salaam zimeharibu sana miundombinu ya barabara ikiwemo Jimbo la Ukonga, barabara nyingi zimekatika ikiwemo barabara ya Banana – Kitunda – Kivule – Msongola. Nini mpango wa Serikali wa kuzikarabati kwa dharura, hasa kipindi hiki ambacho wananchi wanapata taabu na barabara hizi?

Swali la pili. Barabara ya Mwembe Supu – Kwakupepeteka – Bangulo CCM mpaka Mwembe Kiboko kwenye Kata ya Pugu Station haijawahi kutengenezwa kwa kiwango chochote. Je, Naibu Waziri yuko tayari kuambatana na mimi kwenda kuona barabara hii na kuweza kutoa kauli ya Serikali mbele ya wananchi wa Kata ya Pugu Station? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Jerry Silaa kwamba, Mheshimiwa Mbunge amekuwa akilifuatilia sana hili suala, hasa la kupata fedha kwa ajili ya emergency kwenye barabara zake Jimboni kule.

Ninalitaarifu Bunge lako tukufu kwamba Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mheshimiwa Angellah Kairuki amekuwa akifanya vikao mbalimbali na wenzetu wa TARURA na Wizara ya Fedha kuhakikisha TARURA inaongezewa bajeti ya kutoka bilioni 11 ya emergency mpaka bilioni 46, niwatoe mashaka vikao hivyo vinaenda vyema na Wizara ya Fedha imeahidi kutafuta fedha hizo kwa ajitihada za Mheshimiwa Angellah Kairuki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, nipo tayari kuongozana na Mheshimiwa Jerry William Silaa kuelekea katika Jimbo lake la Ukonga na kuzikagua barabara zake. Ninamuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaangalia ratiba hata weekend tutoke hapa tuelekee Jimbo la Ukonga tuweze kukagua barabara hizo na kuona ni kipi Serikali inaweza ikafanya. (Makofi)
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika Halmashauri ya Kasulu Vijijini ipo barabara ya kutoka Mgombe kwenda Kagerankanda, barabara hiyo hutumika kwa wakulima kupitisha mazao kupeleka majumbani kwao.

Je, ni lini Serikali itatoa pesa kwa TARURA ili barabara hiyo iweze kutengenezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Genzabuke kuhusu hii barabara ya Mgombe iliyopo kule Kigoma:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tayari inafanya jitihada kubwa sana za kuhakikisha TARURA inakuwa na fedha ya kutosha ya kufanya matengenezo ya barabara mbalimbali hapa nchini. Tukirudi katika Mwaka wa Fedha 2020/2021 TARURA ilikuwa ina bajeti isiyozidi bilioni 226, lakini kwa jitihada za Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, TARURA imeongezewa fedha zaidi ya mara tatu na kwenda kuwa na bilioni mia saba na sabini na kitu. Hivyo nimtoe mashaka Mheshimiwa Genzabuke kwamba, TARURA itafikia barabara hizi na kuhakikisha zinatengenezwa kwa wakati kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza:-

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga Barabara ya kuanzia pale SUA mpaka Mzinga Jeshini - Magadu, katika Manispaa ya Morogoro Mjini? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaangalia katika bajeti hii iliyopitishwa na Bunge lako tukufu ya 2023/2024 kwa TARURA, kuona kama barabara ya SUA kwenda Mzinga imetengewa fedha. Kama haikutengewa fedha katika mwaka huu wa fedha basi tutaiangalia ni namna gani inaweza ikatengewa fedha katika mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. JANETH M. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ambayo sijaridhika kidogo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na bajeti kuwa ndogo ambayo haikidhi mahitaji halisi ya barabara za Mkoa wa Dar es Salaam, ukizingatia Dar es Salaam ina wakazi wengi ambao unaweza kulinganisha na Mikoa minne, mitano ama sita katika nchi hii.

Je, Serikali haioni haja ya kuunda mamlaka itakayoshughulika na barabara za Mkoa wa Dar es Salaam? (Makofi)

Swali la pili, kwa kuwa, Mkoa wa Dar es Salaam hatuna ruzuku ya pembejeo, mbolea, shida yetu ni barabara, mifereji, madaraja, labda na panya road.

Je, Serikali haioni huruma kwa adha wanayoipata wananchi kwa kuhangaika na ukizingatia sasa hivi barabara nyingi zimejengwa kutokana na ujenzi wa reli na barabara zile za BRT? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Massaburi:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la bajeti ndogo kwa Barabara, nimuarifu Mheshimiwa Masaburi kwamba ni jitihada za Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha barabara za Jiji la Dar es Salaam zinapitika wakati wote na kutengenezwa kwa kiwango cha lami, kwanza kwa kuweka shilingi bilioni 800 na zaidi ya hapo katika Mradi wa DMDP I.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa siku hizi mbili hapa Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mheshimiwa Angellah Kairuki, amewakaribisha Wabunge wote wa Dar es Salaam kwenda kushuhudia utiaji saini wa mikataba ya consultants katika mradi wa DMDP II ambapo nao ni commitment kubwa ya Serikali katika Jiji la Dar-es-Salaam, kuhakikisha barabara zote zinapitika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninakuomba Mheshimiwa Massaburi uwe na subira na wananchi wa Dar es Salaam Serikali inaweka fedha zaidi tena ya bilioni 800 katika kutengeneza miundombinu mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili la kwa nini Serikali isiongeze miundombinu kama reli na kadhalika. Hili tunalipokea kama Serikali na tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi kuona ni nanma gani tutaboresha zaidi miundombinu, lakini tayari kama nilivyosema hapo awali katika mradi huu wa DMDP II, Dar es Salaam inakwenda kupendezeshwa chini ya Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha barabara zinapitika, mito inajengwa vizuri na mifereji ya kupitisha maji ili wananchi wa Dar es Salaam waweze kufanya shughuli zao za kiuchumi bila kupata bughudha yoyote ya kiusafiri.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia fursa ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Mkoa wa Dar es Salaam ni Mkoa mkubwa na ni Jiji la kibiashara, kwa kuzingatia vigezo vyote, kwa maana ya idadi ya watu, kiuchumi na idadi ya magari ni kubwa sana. Je, nini mtazamo wa Serikali wa kuanzisha Mamlaka ya Usimamizi na Kuendeleza Jiji la Dar es Salaam kwa maana ya Dar es Salaam Metropolitan Authority?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Ndugulile la kwa nini Serikali isianzishe Mamlaka ya Usimamizi wa Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tunalipokea kama ushauri na tayari Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kwa maelekezo yake Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Mheshimiwa Angellah Kairuki, kuna timu ambayo inaliangalia hili na kuona ni namna gani linaweza kufanya kazi, pale timu hii itakapowasilisha ripoti hii kwa Mheshimiwa Waziri, basi tutaona hatua zinazifuata za kuchukuliwa.
MHE. TUMAINI B. MAGESA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara, mitaro na madaraja katika Mji Mdogo wa Katoro ni mibovu, katika Kata tatu za Ludete, Nyamigota na Katoro yenyewe. Nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba miundombinu hiyo inatengenezwa ili wananchi waweze kuhudumiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa Serikali ni kuhakikisha kwamba, taasisi yetu ya TARURA ambayo inasimamia barabara za Mijini na Vijijini inakuwa na fedha ya kutosha kwa ajili ya kutengeneza barabara hizi, zikiwemo za Mji Mdogo wa Katoro, ndiyo maana Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeiongezea fedha TARURA mara tatu ya bajeti iliyokuwepo 2021. Hivyo, tutakaa na Mheshimiwa Mbunge kuona katika barabara hizi za Mji Mdogo wa Katoro kama zimetengewa fedha kwenye mwaka huu wa fedha tunaoenda kuuanza Julai na kama hazijatengewa fedha basi tutahakikisha zinatengewa fedha katika mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Jimbo la Ukerewe limekuwa likipata wakati mgumu sana wa kupata Wakandarasi na Wakandarasi kushindwa kuja Ukerewe kwa sababu ya gharama kubwa ya kusafirisha vifaa vyao. Nini mkakati wa Serikali wa kuichukulia Ukerewe kama eneo maalum la kibajeti kwa ajili ya barabara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nilitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba, tayari kuna timu ambayo inafanya tathmini kwa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuangalia jiografia ya nchi yetu, kuona bajeti inayopelekwa kwa ajili ya barabara na kama kuna uwiano ambao ni sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, timu ile tayari ilikuwa imemaliza kazi yake na sasa imepelekwa kwa independent consultants kuweza kuiangalia vilevile taarifa ile na kisha mapendekezo yale yakirudi basi formula ya kutoa fedha iweze kubadilika kadri ya mapendekezo ambavyo yatakuja kwa ajili ya utengenezaji wa barabara. Hivyo, basi nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge kwamba, naamini katika maeneo yenye jiografia ngumu ya ufikaji kama ya Ukerewe na yenyewe timu hii itakuwa imeangalia hayo matatizo ambayo yapo. (Makofi)
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina swali moja la nyongeza. Napenda kufahamu: Je, mradi huu utazingatia ujenzi wa soko la vitunguu na Soko Kuu la Ipembe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sima ambalo limeulizwa kwa niaba yake, mradi huu unazingatia miradi ile ambayo ilipendekezwa na Halmashauri za Manispaa, Halmashauri za Majiji na Town Councils wenyewe. Kwa hiyo, huwa mapenekezo yanaletwa kwa wenzetu wa TARURA kupitia waratibu wa mradi huu wa TACTIC. Yanapoletwa, basi wanachambua na 30 percent ya miradi ile iliyoletwa, ndiyo ambayo inapitishwa na kutengewa fedha. Kwa hiyo, kama wao wenyewe Manispaa walileta soko hili la vitunguu na soko kuu, basi naamini itakuwemo katika mradi huu wanapopatikana hao Consultants kufanya usanifu.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kumwuliza Mheshimiwa Waziri; je, Manispaa ya Moshi katika Mradi huu wa TACTIC itaanza lini? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyotoa maelezo kwenye majibu yangu ya msingi, hivi sasa wapo katika kuwapata consultants wa ku-design miradi hii na pale watakapopatikana, basi designs zitafanyika na ndipo mradi huu utaanza mwisho wa mwaka wa fedha 2023/24.

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mradi huu pamoja na mambo mengine utahusisha ujenzi wa miradi ambayo itakuwa chanzo cha mapato katika hiyo miji 45; na kwa kuwa huu ni mkopo: Je, Serikali haioni umuhimu wa kukaa na Benki ya Dunia ili awamu ya pili na awamu ya tatu zote zikaenda pamoja ili utekelezaji wa mradi huu uanze mapema? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tunalipokea. Tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Fedha ambao ndio wanzungumza na World Bank kuona kama hili linaweza likafanyika, lakini kwa sababu ya ukubwa wa miradi hii ni lazima iende kwa awamu ili kuhakikisha monitoring ya miradi hii inakuwa ni nzuri ili fedha zinazoletwa, kama alivyosema yeye mwenyewe, Mheshimiwa Chumi, kwamba ni mkopo, hivyo basi Watanzania watalipa, zisitumike vibaya. Kwa hiyo, ni vyema tuka-monitor miradi hii kwa awamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Chumi kwamba miradi hii itafika katika maeneo yote ya majiji haya 45 kwa wakati ambao umepangwa.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ni lini sasa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni nayo itaingizwa kwenye Mradi wa TACTIC? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, tukimaliza tathmini ya hizi tier tatu za miji hii 45, ndipo tutaangalia kama Serikali kuona uwezekano wa kuongeza Miji, Halmashauri za Manispaa na Halmashauri nyingine DC ambazo zipo nchini, ikiwemo ya Manyoni. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge avute subira, na pale ambapo tutakamilisha mchakato huu, kama nilivyokuwa nimemjibu Mheshimiwa Chumi, basi tutaangalia na maeneo mengine ya nchi yetu.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la barabara hii ambayo inapita Lukhumeda – Setet kwa upande wa Babati, ambayo kwa Hanang inapita Bassodesh – Dang’aida – Hilbadaw, lakini ukienda upande wa Singida inaenda Singa – Ilongero – Singida, imejadiliwa kwenye kikao cha Bodi ya Barabara mwaka 2021. Hapa Bungeni nimeshaisema hii barabara zaidi ya mara tano; je, Serikali ina kauli gani juu ya nini kifanyike ili barabara hii iweze kufanyiwa kazi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwenye bajeti ya mwaka 2021/2022, tuliongeza bajeti ya TARURA kwa uwiano kwa majimbo yote, lakini kwa majimbo yale makubwa ambayo mtandao wa barabara ni mkubwa, fedha hizi ni kidogo; kwa mfano kwa Hanang tuna kata 33 na vitongoji 414; je, Serikali ina kauli gani kuziongezea bajeti zile Halmashauri kubwa au majimbo makubwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Hhayuma, hili la kwanza la kauli ya Serikali juu ya barabara hii ya Hilbadaw – Bashnet iliyopo kule Hanang kupandishwa hadhi; kama nilivyoeleza kwenye majibu yangu ya msingi, hili ni takwa la kisheria la kupitisha barabara hii kwenye vikao hivi. Mheshimiwa Mbunge ameshasema barabara hii ilipitishwa mwaka 2021, hivyo basi, kwa sasa litakuwa chini ya Waziri mwenye dhamana na barabara ambaye ni Waziri wa Ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilitakiwa timu ije kufanya tathmini ya barabara hiyo kabla ya kuipandisha hadhi na kumshauri Waziri wa Ujenzi. Kwa hiyo, tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi na kuona hili limekwamia wapi? Pale lilipokwamia basi hatua ziweze kuchukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili kuhusu uwiano wa bajeti ya barabara za TARURA katika majimbo mbalimbali hapa nchini, ikiwemo na Jimboni kwake Hanang; hapa wakati najibu swali mojawapo la nyongeza, nilisema tayari kuna timu ambayo inafanya tathmini ya maeneo yetu hapa nchini juu ya bajeti ya barabara ambayo inatolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa TARURA ilirithi mfumo ule ule uliotoka kwenye Bodi ya Barabara wakati taasisi hii inaanzishwa. Tathmini ile itakapokamilika kuangalia maeneo ya kijiografia, kiuchumi na masuala ya kilimo yanayotokana na maeneo mbalimbali hapa nchini, basi formula mpya itatolewa. Kama nilivyosema, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, analifanyia kazi na timu yake muda siyo mrefu itamshauri.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Manispaa ya Moshi, barabara inayotoka YMCA kwenda KCMC ni barabara ambayo ina msongamano mkubwa sana. Kuna Chuo cha Ushirika, kuna Chuo cha CCP Moshi na kuna Chuo Kikuu cha Katoliki, lakini kwenda pale hospitali kwenyewe watu wanaoenda kuona wagonjwa wanachelewa na wakati mwingine pia wanapata matatizo; bajaji zimo humo humo, bodaboda zimo humo humo, vi-hiace na hata magari binafsi; kutokana na majibu ya msingi, kwamba vikao vifanyike na ni matakwa ya sheria, vyote vimeshafanyika: ni lini Serikali itaona umuhimu na udharura wa kubadilisha barabara hiyo kutoka TARURA kwenda TANROADS? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa barabara ya YMCA kwenda KCMC katika Halmashauri ya Manispaa ya Moshi. Tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi kuona hatua zipi ambazo wamezifikia katika kwenda kupandisha hadhi barabara hii kuwa barabara ya mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema hapo awali kwenye majibu yangu ya msingi, kwamba haya ni matakwa ya kisheria, na yakishapita kutoka kwenye vikao hivi vyote na vikipitishwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Barabara ya Mkoa ambaye ni Mkuu wa Mkoa, sasa yanakwenda kwenye mamlaka ya Waziri wa Ujenzi ambaye ndiye mwenye dhamana ya barabara. Kwa hiyo, Serikali inalichukua na tutakaa na wenzetu wa barabara kuona imefikia wapi?
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Katika Jimbo la Arumeru Magharibi hivi karibuni mvua kubwa zimenyesha na kuharibu miundombinu kweli kweli yakiwemo madaraja, barabara na sasa wananchi hawana mahali ambapo wanapita katika maeneo haya ambapo yalitakiwa kujengwa maradaja mapya.

Ni lini sasa Serikali itapeleka hizo fedha za dharura ambazo tumeziomba kwa ajili ya kuokoa wananchi ambao hawana jinsi ya kwenda shambani, hospitali au popote wanapohitaji kupata huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu Mollel, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa sasa kupitia Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini (TARURA) inaangalia namna ya kupata fedha za ziada za dharura. Bajeti ya TARURA kwa ajili ya dharura kwa mwaka ni shilingi bilioni 11. Kama nilivyosema hapo awali, tayari Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Kairuki, ameshakaa na Waziri wa Fedha kuona ni namna gani TARURA inaweza ikaongezewa fedha za dharura kwenda shilingi bilioni 46 ili barabara hizi zilizoharibika katika kipindi hiki cha mvua ziweze kutengenezwa, zikiwemo hizi za kule Arumeru Magharibi kwa Mheshimiwa Lemburis. Pale ambapo Wizara ya Fedha itaridhia TARURA kuongezewa fedha hii, basi barabara hizi zitaanza kutengenezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wabunge, nimalizie tu kwa kusema kwamba tunakwenda kuanza kutekeleza mwaka mpya wa fedha mwezi mmoja na siku kadhaa zijazo (mwezi Julai), hivyo basi, wataona barabara hizi zitengenezwe katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Katika kikao cha Barabara cha Mkoa wa Kilimanjaro na Kikao cha RCC cha Mkoa wa Kilimanjaro, tulipitisha barabara kadhaa tangu mwaka juzi kupandisha hadhi kutoka TARURA kwenda TANROADS; na tayari kikoa cha mwisho cha RCC Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa alituambia ameshawasilisha Wizarani ili barabara hizi ziweze kupandhishwa hadhi.

Je, ni lini sasa barabara hizi za majimbo yote ya Mkoa wa Kilimanjaro na Hai zitapandishwa hadhi kutoka TARURA kwenda TANROADS?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni takwa la kisheria kwamba barabara hizi na vikao vyote vinavyokaa kule vya kisheria katika ngazi ya wilaya na mkoa zinafikishwa kwa Waziri mwenye dhamana na barabara ambaye ni Waziri wa Ujenzi. Hivyo, tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi kuona ni hatua zipi ambazo zimefikiwa na kupandisha hadhi barabara hizi za Mkoa wa Kilimanjaro, na Jimbo la Hai kule kwa Mheshimiwa Saashisha.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, pamoja na jitihada kubwa za Serikali kuboresha miundombinu na kutoa vifaa, nini mpango wa Serikali sasa kutoa posho ya kufundishia (teaching allowance) kwa Walimu wote nchini ili kuongeza morali ya kazi?

Swali la pili, nini mkakati wa Serikali sasa kutoa posho ya mazingira magumu kwa watumishi hasa Walimu wanaofanya kazi kwenye mazingira magumu kijiografia kama ilivyo Ukerewe na Mafia? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Joseph Michael Mkundi, Mbunge wa Jimbo la Ukerewe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza kuhusu hii posho (teaching allowance) Serikali itaendelea kuangalia suala hili na kadri ya uwezo wake wa kibajeti tutaendelea kuliona ni namna gani tunaweza tukalitekeleza. Vilevile kuna Halmashauri ambazo Wakurugenzi wao wenyewe kupitia mapato yao ya ndani wamekuwa wakitoa motisha kwa Walimu hasa wale ambao wanaenda kuripoti kwa kuwapa magodoro na vifaa vingine vya kwenda kuanzia maisha.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la posho ya mazingira magumu. Hili tunalipokea kama Serikali na tutaendelea kulifanyia analysis na kuona ni namna gani tunaweza tukapata fedha ya kuweza kulitekeleza hili lakini kwa sasa bado tutaendelea katika mazingira yote kuwa-treat watumishi wetu sawa na haki sawa katika maeneo yote.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Spika, uhamisho pia ni sehemu ya maslahi ya walimu, je upi utaratibu ambao Serikali inautumia kwa ajili ya kuhamisha walimu kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine ili waache kutufuata Wabunge tuwasaidie uhamisho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, suala hili la uhamisho kuwa ni sehemu ya maslahi ya walimu, utaratibu uko wazi na Mwalimu anapokuwa ameajiriwa kwanza atakaa mwaka mmoja wa probation katika eneo lake ambalo amepelekwa kufanya kazi. Baada ya hapo pia atatumikia nafasi hiyo kwa miaka mingine miwili kabla ya kuomba uhamisho.

Mheshimiwa Spika, kwenye hili kumekuwa kuna influx kubwa sana ya watumishi kutaka kuhamia Mijini na kuhama maeneo ya pembezoni. Wakumbuke wakati wanaajiriwa waliajiriwa kwa sababu ya upungufu uliopo maeneo ya pembezoni ikiwemo maeneo mengine ya Halmashauri ya Wilaya ya Momba kule. Hivyo ni wajibu wao kubaki katika maeneo yale na kuhudumia Watanzania waliokuwepo kwenye maeneo yale.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, suala la mazingira magumu ni suala kubwa sana na kuna walimu wanaofundisha sehemu ambazo ni ngumu sana kama milimani, kuna wengine wanaishi mijini na tambarare. Serikali hamuoni kwamba ni muhimu kulichukua hili suala mara moja na kuliangalia kuliko kila wakati muwe mna repostponed na sehemu hizo ngumu zinakosa walimu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kwamba kuna maeneo magumu ya mazingira magumu kama milimani kama Jimboni kule kwa Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, tutaendelea kuliangalia kadri ya uwezo wa kibajeti wa Serikali tutaona ni namna gani tunaweza tukaanza kufanya hivyo.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwanza ninaishukuru sana Wizara pamoja na Madaktari wote wa Wilaya ya Nyasa kwa huduma ambayo inatolewa.

Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza kwa kuwa hali ya kituo hiki mbali ya kukosa wodi kabisa hasa ya akina mama pia hawana ultrasound kiasi kwamba hata inapofikia kupasua mama labda kwa ajili ya mtoto mimi naona ni suala la kubahatisha, hiyo inapelekea pia kuleta changamoto.

Je, ni lini Serikali itafikiria sasa kupeleka mashine hiyo ya ultrasound ili hawa wakina mama wafanyiwe huduma iliyo kamilifu?

Swali la pili, Mheshimiwa Rais akiwa Makamu wa Rais wakati wa kampeni alipita katika Kata ya Lituhi na baada ya wananchi kumuomba akaahidi wajengewe kituo cha afya. Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hii ya Mheshimiwa Rais ikizingatiwa kwamba ni Kiongozi Mkuu wa nchi na wananchi wanayo matumaini makubwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Manyanya kuhusu hali ya kituo cha afya hiki ambacho ameulizia kwenye swali lake la msingi, tutaangalia katika bajeti ambayo tunaanza kuitekeleza mwaka wa fedha 2023/2024 kuona ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba katika Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa ili waweze kununua ultrasound mara moja ambayo itaenda kuhudumia akina mama wajawazito katika eneo hili la Kihangara.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la ahadi iliyotolewa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Kata ya Lituhi kuhusu kujengewa kituo cha afya. Naomba nitumie nafasi hii kumwelekeza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma kuweza kufika katika Kata ya Lituhi na kufanya tathmini, kuona uhitaji ambao upo, idadi ya watu waliopo katika eneo hili na kisha kuwasilisha taarifa hizi katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ili katika mipango yetu tunayoweka ya ujenzi wa vituo vya afya, tuweze kuweka ujenzi wa Kituo cha Afya Lituhi ili kutimiza ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kituo cha Afya cha Nzihi na Kituo cha Afya cha Mgama kwa kweli havina kabisa wodi za akina baba na wamekuwa wakilalamika muda mrefu na nimeshaomba mara kadhaa. Je, ni lini sasa Serikali itatujengea hizo wodi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kuhusu ujenzi wa wodi katika Kituo cha Afya Nzihi na Kituo cha Afya Mgama kama nilivyokwishakusema kwenye majibu ya msingi, Serikali baada ya ujenzi wa vituo vya 807 sasa tunaenda kuona ni namna gani tunapata fedha kwa ajili ya ujenzi wa wodi kwenye vituo vya afya vilivyofanyiwa ukarabati na kupewa majengo yale ya awali yaliyoenda kujengwa katika vituo vya afya na tutaangalia pia kuhusu Kituo hichi cha Nzihi na Mgama.
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na jinsi walivyojibu katika swali la msingi. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa katika Daraja la Mto Garamoha ni daraja linalounganisha Kata tatu, Kata ya Mwaswale, Nkuyu na Ndolelezi na daraja lile hupelekea kipindi cha mvua wananchi kushindwa kupita katika eneo hilo kwenda kupata huduma katika Kata ya Sagata. Sasa kwa kuwa fedha ni kiasi kidogo cha bajeti ya TARURA kwa nini Serikali isiweke kwenye fedha za maendeleo ili kusudi wananchi waweze kujengewa daraja hilo?

Swali la pili, kwa kuwa katika Kata ya Mwaswale kuna barabara ambayo TARURA wamejenga kutoka Makutano hadi Mwakubija lakini bado kilomita 51 za kutoka Mwakubija kwenda Sopalodge. Serikali sasa haioni umuhimu wa kufungua barabara ya kutoka Mwakubija kwenda Sopalodge kwa ajili ya kwenda kufanya shughuli za kiutalii katika Wilaya hii ya Itilima? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Silanga swali lake la kwanza kuhusu fedha iliyotengwa kwa ajili ya daraja hili la Mto Garamoha, tutaangalia katika utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024 tuone fedha hii iliyotengwa kwa ajili ya ujenzi wa daraja hii inakwenda mara moja ili kuweza kujenga daraja hili kuweza kutoa huduma kwa wananchi wa maeneo aliyoyataja Mheshimiwa Silanga.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la kujenga barabara hii ya kilometa 51 kutoka Maswale kuelekea Sopalodge. Barabara hii tayari ujenzi wake ulikuwa umeshaanza hapo awali na kwa sasa hii barabara inapita katika Pori Tengefu la Maswa katika maeneo ya Nyasosi kuelea Sopalodge ambapo barabara kufika Nyasosi pale wameishia pale na bado hizo kilometa 51. Kwa sababu barabara hii ni muhimu sana ambayo inafupisha wananchi wa maeneo haya badala ya kuzunguka kilometa 250 wanakuwa wanaenda chini ya kilometa 100 kufika katika maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, tutaendelea kuipa kipaumbele kadri ya upatikanaji wa fedha ili tuweze kujenga barabara kuanzia Gwalali kuelekea Makutano hadi kufika Mwakibija na kuelekea kule Sopalodge.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga madaraja ya kuunganisha Jimbo la Mbagala na Jimbo la Mkuranga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango wa kujenga madaraja ya kuunganisha Wilaya hizi mbili au Mikoa hii miwili, Mkoa wa Pwani na Mkoa wa Dar es Salaam. Kwa sasa, tumeweka daraja la Mto Kitonga kuhakikisha katika mradi wa DMDP II ambapo fedha hizi zitakapopatikana kuanzia mwaka wa fedha huu Novemba, 2023 tutaanza utekelezaji wa kujenga daraja hili. Barabara hii ni ya muhimu sana kwa sababu kuna huduma nyingi za mchanga unaotoka katika Wilaya ya Mkuranga kuelekea Mkoa wa Dar es Salaam inapita katika barabara hii.

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Kwa kuwa, wananchi wa Kata ya Mwamanga Kijiji cha Mwamanga, Inolelo na Kisasa B, wanapata shida sana wakati wa mvua kwenda kwenye huduma hasa wanafunzi wa sekondari. Je, Serikali ina mpango gani wa kutupa fedha kwa ajili ya kujenga barabara na daraja hili kuunganisha hasa bottleneck ili wananchi wapate huduma hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nitakaa na Mheshimiwa Kiswaga tuone katika bajeti ya 2023/2024 ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya kuanza ujenzi huu wa daraja katika Kata ya Mwamanga kule Wilayani Magu na kama haijatengewa fedha katika mwaka wa fedha 2023/2024 basi tutaangalia kutenga fedha kwenye mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. CHATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Je, ni lini Serikali kupitia TARURA itajenga Daraja la Mto Juwe kuunganisha Kijiji cha Eyasi, Mdito, Oldonyosambu na Jema Wilayani Ngarongoro Mkoa wa Arusha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali tayari imeanza usanifu wa Daraja la Mto Juhe katika Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro kupitia Wakala wa Barabara Vijijini (TARURA) na ilikuwa imetengwa shilingi milioni 200 kama na nane hivi, kwa ajili ya usanifu na ujenzi wa madaraja na makaravati katika barabara hii ambayo inapita katika eneo hili la Mto Juhe.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa daraja la Mto Nyahende kule Nyansulula?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la Mheshimiwa Amsabi Mrimi la Mto Nyahende kule Wilayani Serengeti tutaangalia katika mwaka wa fedha huu ambao tumeidhinishiwa na Bunge lako tukufu wa 2023/2024 kuona kama fedha ilitengwa ya kuanza ujenzi wa daraja hili. Kama fedha hiyo haikutengwa tutaangalia katika kuitenga kwenye mwaka wa fedha wa 2024/2025.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru hadi hapo ilipofikia ni kazi kubwa imefanywa na Serikali, Mheshimiwa Rais Samia alipita njia hiyo akaiona hiyo adha kwenye hilo daraja. Je, Serikali iko tayari kutoa kipaumbele kwenye mwaka ujao wa fedha kwa sababu Wilaya tumetenga hizo fedha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mvua inaponyesha Kata ya Mwabuzo, Mwamanongu, Imaraseko, Mwamalole hukata mawasiliano na Wilaya. Je, Mheshimiwa Waziri upo tayari kuja kuiona hiyo adha wanayopata Wananchi wa Jimbo la Meatu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali ipo tayari kutoa kipaumbele kwa ajili ya ujenzi wa daraja hili ambalo Mheshimiwa Mbunge aliliuliza kwenye swali lake la msingi na tutaangalia kadri ya upatikanaji wa fedha kwenye mwaka wa fedha 2023/2024, kuona ni namna gani tunaweza kuanza na kama fedha basi zitakuwa hazitoshi katika mwaka huo wa fedha tutaenda kuona tunatenga fedha kwa ajili ya kutekeleza pia ahadi hii ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika mwaka wa fedha 2024/2025.

Mheshimiwa Spika, nikijibu swali lake la pili la kama nipo tayari kuongozana naye kwenda kuona namna miundombinu ilivyoharibika katika maeneo haya ya Jimbo lake kule Meatu. Nipo tayari kuongozana nae na baada tu tukihitimisha Bunge hili la bajeti tarehe 30 Juni mwaka huu, mimi nipo tayari kupanga na Mheshimiwa Komanya ili tuweze kuelekea wote kule Meatu.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante, Kata ya Mwamishali ina changamoto ya daraja la kutoka Mwambiti, Tongoleangamba hadi Buliashi ambayo ni Makao Makuu.

Je, ni lini Serikali itajenga daraja hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itajenga daraja hili la Mwamishali kuelekea Makao Makuu ya Kata kadri ya upatikanaji wa fedha. Tutaangalia katika mwaka huu wa fedha 2023/2024 kuona kama fedha imetengwa kwa ajili ya usanifu na ujenzi wa daraja hili na kama haijatengwa tutatenga katika mwaka wa fedha wa 2024/2025 kadri ya upatikanaji wa fedha hizo.
MHE. ERIC J SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kuishukuru sana Serikali kwa kutekeleza jambo hili ambalo kwa muda mrefu nimekuwa nikilipigia kelele, kwamba fedha milioni 500 wakati vifaa havikuwa vimenunuliwa. Sasa ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa ina mahitaji ya watumishi 166 lakini waliopo ni watumishi 39 pekee na hili linafanya vifaa hivi vishindwe kutumika ipasavyo;

Je, Serikali iko tayari kufanya commitment ya lini watumishi hawa watapelekwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kumbukumbu za wananchi wa Buchosa hasa katika Kisiwa cha Kome kwenye Kituo cha Afya cha Nyamisri waliwahi kuahidiwa kupelekewa X–Ray mpya, wakati ule Waziri wa TAMISEMI akiwa dada yangu, Mheshimiwa Ummy Mwalimu;

Je, Serikali inaikumbuka ahadi hii au imekwishakuisahau; na kama inaikumbuka, iko tayari kuitimiza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la kwanza la nyongeza la Mheshimiwa Shigongo la kuhusu ni lini Serikali itapeleka watumishi katika Hospitali ya Wilaya ya Buchosa: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imetangaza ajira za sekta ya afya 8,070 nchini, na hii ni kwenda kujazia maeneo yenye upungufu wa watumushi, ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa. Hivyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika hawa watakaoajiriwa hivi karibuni nao watapata watumishi hawa katika hospitali ya wilaya.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la X-Ray iliyoahidiwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, katika Kituo cha Afya Nyamisi; tutatekeleza ahadi hii kadiri ya upatikanaji wa fedha. na tutaangalia katika bajeti ya mwaka 2023/2024 kama kituo hiki kimetengewa fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba basi x-ray iwe kipaumbele kupelekwa kwa ajili ya kuhudumia wananchi.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, Wilaya ya Nyamagana ina tarafa moja tu, na idadi ya wananchi ni kubwa. Ukigawa kulingana na tarafa mbalimbali maana yake unawanyima fursa wananchi wa Nyamagana kupata huduma stahiki hasa walio pembezoni kule Ngwanyima na Kishiri;

Je, Serikali ina mpango gani wa kuangalia, hasa idadi ya wananchi na umbali wa kupata huduma kwenye maeneo hayo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa hali ileile ya Nyamagana inalingana kabisa na hali ya Jimbo la Magu, hasa Kata ya Mwamanga na Kata ya Lutale;

Je, Serikali ina mpango gani wa kuziona kata hizi ambazo ziko mbali na huduma katika vituo vya afya kwenye wilaya zao? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mabula; la kwanza kuhusu Jimbo la Nyamagana kuwa na tarafa moja tu.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, Serikali iliangalia maeneo ambayo ni pembezoni na yako mbali na huduma za afya kabisa na kuyapa kipaumbe na kuwa ni kata za kimkakati. Hili la Nyamagana tunalipokea kama Serikali na kuweza kuangalia ni namna gani tutapeleka timu ya kufanya tathmini na kuona vituo vya afya vya Serikali vilivyopo katika jimbo hili na kuona uwezekano wa kutenga bajeti ya kuwaongezea vituo vya afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Nyamagana.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la kata hizi alizozitaja ikiwemo Kata ya Mwamanga katika Halmashauri ya Wilaya ya Magu, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa kata hizi za kimkakati kote nchini, ikiwemo katika Halmashauri ya Wilaya ya Magu. Tutaangalia katika bajeti ya mwaka 2023/2024 ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Magu, ili tuweze kuanza na ujenzi wa kata hizi za Mwamanga na nyingine ambayo aliitaja Mheshimiwa Kiswaga.

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona: -

Mheshimiwa Spika, Tarafa ya Makambako inahudumia Halmashauri mbili, yaani Jimbo la Lupembe…

SPIKA: Swali lako Mheshimiwa? Nenda moja kwa moja kwenye swali, unataka Serikali ikujibu nini?

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nimekuelewa. Nataka Serikali, katika Jimbo la Makambako tarafa moja ina majimbo mawili, kila tarafa iwe na jimbo lake ili Serikali inapopanga mipango ya kuhudumia tarafa tuweze kuhudumiwa vizuri kwenye Tarafa yetu ya Makambako. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tunalipokea hilo na tutaangalia katika bajeti zilizotengwa tuone tupeleke kituo cha afya.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, Jimbo la Singida Mashariki, Kata ya Misupaa pamoja na Isuna hazina vituo vya afya;

Je, ni lini Serikali itajenga vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutajenga vituo vya afya hivi katika Kata ya Isuna na nyinginezo kule Singida kadiri ya upatikanaji wa fedha, na tutaangalia kwenye bajeti inayofuata kuona ni kiasi gani kimetengwa ili Serikali ianze ujenzi huo.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Katika Tarafa ya Kipatimu Kata ya Chumo tumekamilisha ujenzi wa kituo cha afya mwezi uliopita.

SPIKA: Unataka Serikali ifanye nini?

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, je, ni lini Serikali italeta vifaa tiba, dawa pamoja na watumishi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali imetenga shilingi bilioni 7.1 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba kwenye vituo vya afya mbalimbali hapa nchini, na tutaangalia katika bajeti hii ambayo imetengwa kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba hivi; kama Tarafa ya Kipatimu kwenye kituo cha afya alichokitaja Mheshimiwa Ndulane imetengwa na tutapeleka vifaa tiba huko.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, kile Kituo cha Afya cha Bweri ni kituo cha muda mrefu, lakini kimeshindwa kwisha na kwa hiyo, wananchi wa eneo lile wanashindwa kupata huduma;

Je, ni lini Serikali itamalizia hicho kituo ili wananchi wapate huduma nzuri za kituo cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutaangalia katika mwaka wa fedha unaofuata kama kuna fedha imetengwa kwa ajili ya umaliziaji wa Kituo hiki cha Afya cha Bweri ili tuweze kumalizia, na kama haijatengwa tutaangalia katika mwaka wa fedha wa 2024/2025.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; je, ni lini Serikali itafungua kituo cha afya cha Kata ya Lyamugungwe na kupeleka vifaa tiba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutaangalia katika mwaka wa fedha unaofuata kama kuna fedha imetengwa, na kama bado haikutengwa basi tutatenga kwenye mwaka wa fedha wa 2024/2025.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Je, ni lini Serikali itajenga kituo cha afya katika Tarafa ya kimkakati ya Mbuji yenye kata tano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni kipaumbele cha Serikali kuhakikisha inajenga vituo hivi vya afya katika kata za kimkakati. Na tutaangalia katika mwaka wa fedha unaofuata tuweze kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya hiki.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante, je, ni lini Serikali itajenga kituo cha afya katika Tarafa ya Nangaru na Milola?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni kipaumbele cha Serikali kuhakikisha inajenga vituo vya afya kwenye kata na tarafa za kimkakati kote nchini. Na tutatafuta fedha katika mwaka wa fedha 2023/2024 na kama hakuna fedha hizo basi tutatengea bajeti kwenye mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi, je, ni lini Serikali itajenga wodi za wanaume na wanawake katika Kituo cha Afya cha Ifingo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutaangalia katika mwaka wa fedha unaofuata ili ifingo waweze kupata fedha hii. Lakini vilevile nichukue nafasi hii kuomba Wakurugenzi wa halmashuri kuwa wanatenga fedha kwa ajili ya ujenzi na umaliziaji wa zahanati na vituo vya afya kwenye halmashauri zao. Serikali Kuu imeshapeleka fedha nyingi sana kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya hivi na zahanati hizi na fedha nyingi ya vifaa tiba na wao wasaidie sasa.
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, lini Serikali itajenga vituo vya afya katika Kata ya Igundu na Namura katika Jimbo la Mwibara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itajenga vituo hivi vya afya kadiri ya upatikanaji wa fedha na tutaangalia tena katika mwaka wa fedha unaofuata ili tuweze kuweka kipaumbele fedha hiyo iweze Kwenda. Na kama haipo tutatengea kwenye mwaka wa fedha 2024/2025.

MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ninashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

a) Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Afya Udekwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili linatoka katika Mkoa wa Simiyu, Wilaya ya Maswa, Wilaya ya Binza;

b) Je, ni lini Serikali itajenga kituo cha afya katika Kata ya Binza? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili haya ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kata hii ya Budekwa ipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo. Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wake kadiri ya upatikanaji wa fedha; na tutaangalia katika mwaka wa fedha unaofuata kama kuna fedha imetengwa, ili iweze kwenda mara moja kujenga.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la kituo cha afya hiki alichokiulizia kilichoko Mkoani Simiyu, tutaangalia vilevile kuona ni namna gani kama fedha imetengwa basi iweze kwenda mara moja kwa ajili ya ujenzi wa kituo hiki cha afya.

MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, napenda kuuliza swali la nyongeza, kama ifuatavyo: -

Je, ni lini Serikali itajenga vituo vya afya katika Kata ya Vudee na Siji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya Mundee na Suji kadiri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, je, ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba kwenye vituo vya afya viwili vilivyokamilika; Kituo cha Afya cha Magazini na Ligela?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutaangalia katika mwaka wa fedha unaofuata kama kuna fedha imetengwa basi tutahakikisha iweze kwenda mara moja na kama haipo basi tutatenga katika mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kumalizia Kituo cha Afya Samunge, Kata ya Samunge?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutaangalia katika mwaka wa fedha unaofuata ili tuweze kutenga fedha hii ya kumalizia Kituo cha Afya cha Samunge.
MHE. JEREMIAH A. MRIMI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya ukarabati wa Kituo cha Afya Iramba kilichochakaa sana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutaangalia katika mwaka wa fedha unaofuata na kuipa kipaumbele kata hii na kuweza kupeleka fedha kadiri ya ilivyotengwa.

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, ningependa kuuliza kuna vituo vya afya vingi nchini ambavyo havijamaliziwa OPD. Ni lini OPD zitamaliziwa katika vitu vya afya ambavyo havina OPD?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikipeleka fedha kwa awamu katika halmashauri mbalimbali hapa nchini kwa ajili ya umaliziaji wa majengo haya. Tunaendelea kutafuta fedha kuona ni namna gani tunapeleka kwa ajili ya umaliziaji wa majengo ambayo bado hayajakamilika. Na kwa yale yaliyokamilika Serikali inaendelea pia kupeleka vifaa tiba ili huduma kwa wananchi iweze kuanza kutolewa kwa wakati.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Afya Lupila kwa sababu, majengo yake yamechakaa sana na ni ya muda mrefu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024 Kituo cha Afya Lupila kimetengewa fedha za World Bank na kitaenda kujengwa katika mwaka huo wa fedha. Vilevile kuna maombi maalum ya Mheshimiwa Mbunge ya Kituo cha Afya Mfumbi ambayo nayo yanafanyiwa kazi, ili kituo cha afya hicho kiweze kujengwa.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali. Serikali imetoa wito kwamba Wabunge tutoe elimu. Mimi kama Mbunge wa kundi hili, nimetoa elimu sana na kundi hili limekuwa likiitikia, lakini Halmashauri na Manispaa huwa hazitekelezi mwongozo huu na kanuni ambayo imeelezwa kwenye jibu la msingi: Nini kauli ya Serikali kwa Halmashauri na Manispaa zetu nchini? Kwa sababu kama mwongozo upo na kanuni zipo, kwa nini halitekelezeki? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, natambua kwamba huenda kukawa kuna mabadiliko ya jinsi ya utolewaji wa mikopo hii. Niendelee kuiomba Serikali kwamba kwa kundi hili la watu wenye ulemavu, iendelee kufikiria kukopesheka mtu mmoja mmoja, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Ikupa kwa maana amekuwa champion hasa katika mabadiliko ya kanuni hizi za kuwezesha walemavu kuweza kupata mkopo kwa mtu mmoja mmoja.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake kuhusu kwa nini kanuni hizi hazitekelezeki, nichukue nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kuwaelekeza Wakurugenzi wote wa Halmashauri nchini, kutekeleza mabadiliko haya ya sheria na kuhakikisha watu wenye ulemavu wanapata mkopo kwa mtu mmoja mmoja. Pia kama Mheshimiwa Ikupa alivyosema kwenye ushauri wake, katika mapitio mapya ambayo yanafanyika kwa maelekezo ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tutaweka kipaumbele kwenye kundi hili la walemavu vilevile kuweza kuendelea kupata mkopo mtu mmoja mmoja.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kuwa Serikali imeweka utaratibu wa kutangaza ajira ambazo zinatoka TAMISEMI na hivyo kukadiria watumishi kupelekwa TARURA: Kwa nini sasa Serikali isiruhusu TARURA wenyewe waweze kuajiri wakandarasi au wahandisi?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Kwa kuwa, Jimbo la Msalala liko katika mazingira magumu sana kwenye maeneo hayo kwa maana ardhi yake ni mbuga: Sasa Serikali haioni haja ya kuongeza bajeti ili iendane na uhalisia wa maeneo hayo kwenye Jimbo la Msalala? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Iddi Kassim, la kwanza hili la kwa nini TARURA wasipewe vibali vya kuajiri wenyewe, ni kwamba ajira katika utumishi wa umma hutolewa kulingana na ukomo wa bajeti ambayo imepitishwa na Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. TARURA wenyewe wanaomba vibali kwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais, Utumishi na tutaendelea kutoa kipaumbele ajira za ma-engineer kwenye taasisi hii ya TARURA kadiri ya fedha ambavyo inapatikana na bajeti ya Serikali inaruhusu.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la mgawanyo wa fedha, hasa kule Msalala kwa sababu ya mazingira magumu, kwa sasa tayari kuna review inayofanyika chini ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa maelekezo ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Angellah Kairuki, kuangalia ni namna gani mgawanyo wa fedha unakwenda katika maeneo mbalimbali hapa nchini ikiwemo kule Msalala. Naomba Mheshimiwa Mbunge awe na Subira na muda siyo mrefu timu hii itawasilisha taarifa yake mbele ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na baada ya timu hiyo kuwasilisha taarifa hiyo, tutaangalia upya formula inayotumika kwa ajili ya kupeleka fedha maeneo mbalimbali nchini.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa, kwenye nchi yetu majira yanatofautiana: Je, Serikali haioni umuhimu wa kuiruhusu na kuielekeza TARURA juu ya muda wa kutangaza na kutekeleza miradi kwa kuzingatia majira ya maeneo husika? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, TARURA inatangaza kazi zake hizi kote nchini mara baada tu ya bajeti yao kuidhinishwa. Ni kama hivi sasa bajeti ya Shilingi bilioni 776 imeidhinishwa na Bunge lako Tukufu, hivyo katika mwaka mpya wa fedha unaoanza mwezi Julai mwaka huu 2023, ndipo kazi zote zitaanza kutangazwa.
MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kuishukuru Serikali kwa hatua iliyofikia kuhusu hawa walimu wangu, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na Serikali kutuambia kwamba hawa walimu 13 ambao walikuwa ni raia wa Burundi, wakimbizi, wamepatiwa ajira, lakini mpaka tunavyoongea hivi, hakuna barua waliyopewa inayoonesha kwamba wamepewa ajira za kudumu: Je, Serikali iko tayari kuiambia Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua na mamlaka zinazoshughulikia masuala ya walimu kuhakikisha hawa walimu wanapata barua zao za ajira na stahiki nyingine? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Kuna walimu hawa 29 ambao umri wao umevuka miaka 45 walikuwa wanajazishwa mikataba ya muda, lakini pamoja na kujazishwa mikataba ya muda walikuwa hawapewi gratuity yao.

Je, pamoja na kwamba wamejazishwa hii mikataba, lini watapewa stahiki zao kulingana na mikataba waliyokuwa wamejaza? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la kwanza la Mheshimiwa Migilla la hawa 13 kwamba bado hawajapata barua za ajira zao, tutakaa na Mheshimiwa Mbunge na kuwasiliana na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kaliua na kuona changamoto iko wapi kwa ajili ya hao walimu kupata barua zao kama ambavyo kibali kilitolewa na Ofisi ya Rais, Utumishi kwa ajili ya kuweza kuwaingiza katika ajira ya kudumu.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, hili ni suala la kisheria. Ni sheria iliyopitishwa na Bunge hili Tukufu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba, mtumishi yeyote wa umma ni lazima anapoingia katika utumishi wa umma asiwe amevuka umri wa miaka 45 ili aweze kuwa amechangia katika Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa miaka isiyopungua 15. Ndiyo maana hawa baada ya kupata uraia wao na vibali kutoka Ofisi ya Rais, Utumishi walikuwa wameshavuka ule umri wa miaka 45.

Mheshimiwa Spika, hivyo basi, Katibu Mkuu Utumishi alitoa kibali kwa hawa 29 kuendelea kuwa na ajira ya mkataba, ambapo ni mikataba ya miaka mitano mitano, tofauti na mikataba mingine ya mwaka mmoja mmoja. Watapata kiinua mgongo chao pale watakapofikia umri wa kustaafu kwa mujibu wa sheria ilivyo ya kustaafu.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naishukuru Serikali Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi alisharidhia kupandisha hadhi hiyo barabara kuwa ya Mkoa. Kwa vile hii barabara iko kwenye hali mbaya sana.

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa hii barabara ili ianze kupitika?

Swali la pili, katika hali hiyo hiyo kuna barabara ya Ilembo - Isonso ambayo inaunganisha Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Songwe. Je, ni lini hii barabara nayo itapandishwa hadhi kuwa ya Mkoa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Njeza kwanza lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara hii ambayo tayari imeshapandishwa hadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, barabara ikiwa imeshakidhi vigezo vya kupandishwa hadhi na ikapandishwa hadhi na kuwa inahudumiwa na TANROADS basi ni wajibu wa TANROADS kutenga bajeti hiyo kuweza kutengeneza barabara. Tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi na kuona wao wamejipanga vipi kwa ajili ya kutengeneza barabara hii ambayo ni muhimu sana kule Jimboni kwa Mheshimiwa Njeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la barabara ya Ilembo-Isonso ambayo inaunganisha Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Songwe lakini hasa katika Wilaya ya Ileje. Barabara hii itapandishwa hadhi pale ambapo watafuata vile vigezo vya kisheria kama ambavyo barabara nyingine zinafanya. Waanze vikao vyao katika DCC waende kwenye RCC na baadaye Bodi ya Barabara ya Mkoa na kisha kumwandikia Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi mwenye dhamana ya barabara hizi za Mkoa, ili timu iweze kutumwa kwenda kwenye barabara hii ya Ilembo - Isonso, kufanya tathmini na kisha kumshauri Waziri wa Ujenzi kuhusu barabara hii kupandishwa hadhi.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri yenye matumaini kutoka Serikalini na nina hakika wananchi wangu wa Mabogini na Kahe watakuwa wamepata faraja kubwa sana. Pamoja na hayo nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza tunaishukuru Serikali ilitenga shilingi milioni 475 kutengeneza barabara ya TPC, Samanga hadi Chemchem lakini tamanio la wananchi hawa ilikuwa ni kutengeneza daraja kwenye mto Ronga unaounganisha vijiji vya Samanga na Chemchem.

Je, Serikali ina mpango gani kutengeneza daraja hili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili barabara ya International School Kibosho KNCU hadi kwa Raphael haijakamilika kwa kiwango cha lami.

Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha ujenzi wa barabara hii? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Profesa Ndakidemi, kwanza ni hii barabara ya Samanga – Chemchem kuhitaji daraja katika mto unakopita.

Kwanza kama alivyosema yeye mwenyewe Mheshimiwa Mbunge Serikali ilitenga shilingi milioni 475 kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii na tutaangalia katika bajeti tunayoenda kuanza hii ya TARURA ya mwaka 2023/2024, kuona imetengewa kiasi gani kwa ajili ya ujenzi wa daraja hili na tutamwelekeza Meneja wa TARURA Mkoa wa Kilimanjaro kuweza kuelekeza fedha mara moja kwa ajili ya ujenzi wa daraja hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili hili la International School hadi Kibosho barabara hii. Serikali itaendeleza ujenzi wa barabara hii kadri ya upatikanaji wake wa fedha na tutaangalia Mheshimiwa Mbunge katika bajeti hii inayokuja kuona ni namna gani ambavyo tunaweza tukatenga fedha kwa ajili ya kwenda kuanza ukarabati wa kiwango cha lami kwenye barabara hii.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, ni lini Serikali itakarabati na kujenga upya majengo ya shule chakavu Wilaya ya Njombe, Ludewa, Wanging’ombe na Makete ndani ya Mkoa wa Njombe?

Swali la pili, ni lini Serikali itatua tatizo la upungufu wa Walimu wa Sayansi ndani ya Mkoa wa Njombe? ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mgaya, swali lake la kwanza kuhusu ni lini Serikali itakarabati shule hizi kongwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kwamba Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Daktari Samia Suluhu Hassan ilikwisha karabati shule 89 hapa nchini, ambapo kule Mkoani Njombe kuna shule mbili ambazo zilipata fedha ya kukarabati ambayo ni shule ya Kivavi Sekondari iliyokuwepo Wilayani Makambako vilevile Njombe sekondari. Tunaendelea kuangalia ni namna gani tunaweza tukaendelea ukarabati wa shule kongwe ikiwemo zile zilizokuwepo Mkoani Njombe. Nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI Mheshimiwa Kairuki analishughulikia hili suala kuona ni namna gani atapata fedha ya ukarabati wa shule hizi kongwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la Walimu wa Sayansi. Hivi sasa Serikali ipo katika ukamilishaji wa mchakato wa kuajiri Walimu wa Sayansi na walimu kwa ujumla ambao ni 13,390 ambao wataanza kazi muda Serikali mrefu. Kwa hiyo, nikutoe shaka Mheshimiwa Neema Mgaya kwamba kule Mkoani Njombe nanyi mtapata mgao wa Walimu hawa ambao wanakuja. Mheshimiwa Neema amekuwa akilifatilia sana hili suala na nimwakikishie kwamba Serikali imekusikia na italifanyia kazi suala la upungufu wa walimu katika Mkoa wa Njombe. (Makofi)
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa, kuna Halmashauri zenye uwezo wa kuanza mchakato huu kwa kutumia mapato ya ndani kuweza kuweka hii miundombinu. Ni nini commitment ya Serikali kuzisaidia Halmashauri hizi kukamilisha utaratibu huo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili je, kama kuna shule zenye miundombinu na ziko tayari kubadilisha baadhi ya madarasa kuwa ya kidato cha tano na sita. Je, Serikali iko tayari kuruhusu watumie hostel za binafsi wakati wanasubiri kujenga mabweni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tarimo, kwanza kuhusu Halmashauri ambazo zina uwezo wa kujenga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu uko wazi kama, Halmashauri ina uwezo wa kujenga miundombinu inayohitajika kwa ajili ya shule yenye mkondo wa Kidato cha Tano na Sita hawakatazwi kujenga miundombinu hiyo lakini ni lazima wafuate taratibu za kukaguliwa na Mkaguzi wa Elimu kwa kuomba usajili wa Kidato cha Tano na Sita kutoka Wizara ya Elimu na kisha shule hii iweze kupandishwa hadhi. Lakini kama wana uwezo wa kujenga hawakatazwi kuweza kujenga lakini wafuate taratibu za usajili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili kuhusu shule ambazo tayari zina miundombinu. Kama kuna shule ambazo tayari zina miundombinu hii hawakatazwi nao kuandika Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili na tuweze kukagua kuona miundombinu iliyopo na kisha kuwasiliana na Wizara ya Elimu kuweza kuomba sasa usajili wa mkondo wa Kidato cha Tano na Sita. Hivyo, niwaombe wenzetu wa Manispaa ya Moshi Mjini kama wanazo shule ambazo tayari wanaziona zinakidhi vigezo basi waombe kwa maandishi kwa Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI na tuweze kutuma timu kwa ajili ukaguzi na kisha kuwasiliana na wenzetu wa Wizara ya Elimu kuweza kuona ni namna gani tunapandisha hadhi shule hizi.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali kwanza nitumie fursa hii kuipongeza Serikali na kuishukuru wametupatia bilioni moja kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa shule ya sekondari ya wasichana ya Mkoa. Ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya cha Kintiku kinahudumia takribani Halmashauri tatu, Halmashauri ya Bahi, Halmashauri ya Chemba na baadhi ya vijiji vya Halmashauri ya Manyoni. Kituo hiki kipo kwenye high way ya kutoka Dodoma kwenda Mwanza. Je, lini Serikali itapeleka gari la wagonjwa (ambulance) ili iweze kusaidia kwenye kituo hicho?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili katika Kata ya Nkonko kuna kituo cha afya ambacho kilijengwa, vilevile walijenga jengo la x-ray ambalo bado halijakamilika. Je, lini Serikali itakamilisha jengo hilo la x-ray katika Kituo cha Afya cha Nkonko ili kiweze kuanza kutoa huduma? ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Pius Stephen Chaya, kwanza kuhusu hichi Kituo cha Afya cha Kintiku. Ni kweli ninakiri kwamba kituo hiki cha afya ni muhimu sana kwa sababu kipo barabarani na kama alivyosema Mheshimiwa Chaya ni kituo kinachohudumia Wilaya ya Chemba, kinachohudumia wakazi wa Wilaya ya Bahi na Wilaya ya Manyoni yenyewe na kipo kilometa takribani kama 26 ama 27 kutoka mpakani mwa Dodoma na Mkoa wa Singida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hivi sasa imetenge bilioni 93 kwa ajili ya ununuzi wa magari 316 ya wagonjwa nchi nzima na kwa kuanzia kila Halmashauri itapata walau magari mawili ya wagonjwa. Tayari magari 117 yameshanunuliwa mpaka kufika mwezi Mei mwaka huu na tutahakikisha tunaweka kipaumbele kwenye vituo vya afya vya maeneo ya kimkakati kama Kituo cha Afya cha Kintiku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la Kituo cha Afya Kata ya Nkonko ambacho kinahitaji jengo la x-ray. Tutaangalia katika mwaka wa fedha 2023/2024 kuona ni namna gani Serikali Kuu itaongeza nguvu kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni kuweza kukamilisha ujenzi wa jengo hili la x-ray katika Kituo cha Afya cha Nkonko ili wananchi wa maeneo haya waweze kuanza kupata huduma za x-ray.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Kituo cha Afya Kiloleni Wilaya ya Busega hakina wodi za kulaza wagonjwa kabisa. Je, lini Serikali itajenga wodi hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa ujenzi wa wodi ni katika vipaumbele vya Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Daktari Samia Suluhu Hassan, ujenzi wa wodi za kulaza wagonjwa, ujenzi wa vyumba vya upasuaji, ujenzi wa mochwari na kadhalika katika vituo vya afya na tutaangalia ni namna gani katika kituo cha afya alichokijata Mheshimiwa Midimu kinaweza kipata fedha kwa ajili ya ujenzi wa wodi hizi kule Wilayani Busega.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kata ya Lahoda, Kata ya Jangalo na Kata ya Kinyamshindo zote zipo mpakani mwa Singida pia na Manyara. Je, ni lini mkakati wa Serikali wa kujenga vituo vya afya katika Kata hizo? ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata hii ya Lahoda, Jangalo na nyinginezo zilizokuwepo pembezoni katika Halmashauri ya Wilaya ya Chemba, Serikali itaweka kipaumbele kuhakikisha kwamba tunaanza ujenzi wa majengo ambayo yanahitajika kwenye vituo hivi vya afya na tutaangalia katika bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024 ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya Halmashauri ya Wilaya ya Chemba ili tuweze kupeleka fedha hizi kuanza ujenzi wa vituo hivi vya afya.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi niulize swali dogo la nyongeza.

Wananchi walihamasika sana katika ujenzi wa vituo vya afya pamoja na zahanati. Je, Serikali hamuoni kwamba kuna haja ya kumaliza yale maboma yote nchi nzima kabla hamjaanza ujenzi mpya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nimfahamishe Mheshimiwa Bulaya kwamba Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mama Samia Suluhu Hassan ilianza ujenzi wa vituo vya afya 234 nchi nzima ambavyo vimekamilika na ilitumika gharama ya bilioni 117. Sasa tunaangalia kutafuta fedha kwa ajili ya ku-support jitihada za wananchi katika maeneo mbalimbali nchini, kwa ajili ya umaliziaji wa vituo vya afya na zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu kwa kusema kuna shilingi milioni 50 ambazo zilipelekwa katika kila Halmashauri kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa zahanati za maeneo ambayo wananchi walianza ujenzi wenyewe. Hii inaonesha ni namna gani Serikali hii ya Daktari Samia Suluhu Hassan ipo committed katika ku-support jitihada za wananchi ambazo wameanza kujipelekea maendeleo.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muda mrefu sasa Kituo cha Afya Mlola hakina gari la wagonjwa na hii imepelekea hasa kwa wagonjwa mahtuti kupelekwa na bodaboda katika Hospitali ya Wilaya ya Lushoto. Je, Serikali lini itapeleka gari la wagonjwa katika Kituo cha Afya Mlola ili kuokoa maisha ya wananchi wetu?

Swali la pili, nimeongea kwa muda mrefu sana kuhusu kupeleka fedha katika Kituo cha Afya Gare lakini mpaka sasa hivi hakuna mafanikio yoyote, kama waswahili wanavyosema kuona ni kuamini. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri upo tayari kuongozana na mimi kwenda kuona nguvu za wananchi wale wa Gare kwa ajili ya ku-support Kituo kile cha Afya Gare?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Shekilindi kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amekua akifuatilia sana suala hili la magari katika Kituo cha Afya Mlola.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye kumjibu maswali yake mawili ya nyongeza hili la magari Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Daktari Samia Suluhu Hassan imetenga fedha shilingi bilioni 93 kwa ajili ya ununuzi wa magari 316 ambayo kila Halmashauri ya Wilaya itapata walau magari mawili ya kubebea wagonjwa. Vilevile kuna bilioni 61 ambayo Serikali hii ya Daktari Samia Suluhu Hassan imetenga kwa ajili ya ununuzi wa magari mengine ambayo kila Halmashauri itapata gari moja walau la supervision katika Halmashauri za Wilaya ili wataalam wetu wa afya waweze kutembelea zahanati zetu na vituo vyetu vya afya. Hivyo nimhakikishie Mheshimiwa Shekilindi kwamba tutahakikisha vilevile katika magari haya mgao huo basi Mlola nayo inapewa kipaumbele kupata gari hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la Kituo cha Afya cha Gare kule Wilayani Lushoto nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge niko tayari kuongozana naye Mheshimiwa Shekilindi, kuelekea Wilayani Lushoto kwa ajili ya kuweza kukagua jitihada hizi za wananchi na kuona ni namna gani Serikali kuu inaweza ika-support juhudi hizi za wananchi wa eneo la Gare.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Je, lini Serikali itatekeleza ahadi ya Rais wa Awamu ya Tano ya kujenga Kituo cha Afya katika Kata ya Mulungu Jimboni Muhambwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Daktari Samizi la lini Serikali itatekeleza ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kujenga kituo cha afya. Tutaangalia ahadi hii na nitakaa na Mheshimiwa Samizi kuona ni namna gani tunaweza tukakaa na wataalam wetu kuona tunapataje fedha za kutekeleza ahadi hii katika mwaka wa fedha wa 2023/2024. (Makofi)
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru pamoja na majibu mazuri ya Serikali lakini nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Kwa Mkoa wa Mbeya kuna shule nyingi kongwe ambazo zimechakaa sana zinahitaji ukarabati mkubwa. Je, lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya ukarabati wa shule hizi ndani ya Mkoa wa Mbeya lakini na kwa Tanzania kwa ujumla?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ndani ya Wilaya ya Chunya tuna shule kongwe ambazo zipo toka enzi za mkoloni lakini Serikali ilisema itatoa fedha na mpaka sasa hivi haijatoa fedha kwa ajili ukarabati.

Je, lini Serikali itatoa fedha hizo ili ukarabati uweze kufanyika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kasaka, kwanza kuhusu shule kongwe lini Serikali itakarabati shule hizi Mkoani Mbeya. Niseme tu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alitafuta fedha kwa ajili ya kuanza ukarabati wa shule kongwe na tayari shule kongwe 84 hapa nchini zimekwisha karabatiwa ikiwemo nyingine zilizo katika Mkoa wa Mbeya. Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuendelea na ukarabati wa shule hizi kongwe hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya maelezo yanaenda pia kwenye swali lake la pili la shule kongwe kule Wilayani Chunya, tutaangalia katika awamu inayofuata ya ukarabati wa shule kongwe tuweze kuweka kipaumbele vilevile katika shule kongwe ambazo zilijengwa na mkoloni kule Wilayani Chunya.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kulitokea changamoto katika shule yetu ya sekondari ya Utemini ambapo ilipelekea sasa kuwahamisha wanafunzi wale wote kuwapeleka kwenye shule zingine Utemini sekondari Mheshimiwa Waziri. Miundombinu haikuwa rafiki katika ufundishaji na Serikali ikawa imeahidi kuleta fedha za kujenga shule ya Utemini sekondari, nataka kujua tu ni lini fedha hiyo itakuja kuhakikisha shule hiyo inajengwa? ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sima, Serikali kwa sasa imetenga shilingi bilioni 63 kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya za sekondari katika kila Halmashauri hapa nchini. Muda si mrefu Waheshimiwa Wabunge wataona katika Halmashauri zao shilingi milioni 570 ndiyo minimum ambayo itapelekwa kwa sababu tumeangalia na uwiano wa maeneo na gharama za ujenzi, lakini minimum inakwenda shilingi milioni 570 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa shule za sekondari mpya ikiwemo hizi za katika Manispaa ya Singida.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Tarafa ya Hagati ina shule ya Sekondari ya Hagati ni shule kongwe.

Je ni lini Serikali itatenga fedha na kuikarabati shule hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyokuwa nimeshasema kwenye maelezo yangu ya awali. Serikali hii ya Awamu ya Sita ilikuwa imeshatenga fedha ya kukarabati shule kongwe 89 kote nchini na hiyo ilikuwa ni katika awamu ya kwanza na bado Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya ukarabati wa shule zingine kongwe ikiwemo hii Shule ya Hagati iliyopo kule Jimboni kwa Mheshimiwa Kapinga.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nilitaka tu kusema kwamba, pamoja na kuchimba miamba hiyo, barabara hiyo bado magari hayawezi kupanda. Kwa hiyo, pamoja na kufanya jitihada zote hizo wanapaswa kufanya kazi ya ziada kuhakikisha magari yanapanda katika ule mlima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maswali yangu mawili ya nyongeza ambayo nilitaka Mheshimiwa Waziri aweze kunijibu. Kuna Barabara ya Kanga – Ifwekenya haijalimwa muda mrefu. Nilitaka kufahamu ni lini Serikali itailima barabara hii na kuiweka kuwa kwenye kiwango cha kokoto?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Barabara ya Mlowo – NAFCO – Magamba ambayo inaunganisha Wilaya ya Songwe na Makao Makuu ya Mkoa. Ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha barabara hii inaweza kupitika muda wote na kutengenezwa kiwango cha lami ili iweze kuunganisha Mkoa wa Songwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwandabila, la kwanza juu ya hii Barabara ya Kanga hadi Ifwekenya. Barabara hii ina urefu wa kilometa 20.4 na tayari Serikali kutoka mwaka wa fedha 2021/2022 ilianza kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa maeneo korofi ya barabara hii. Mwaka wa fedha huo nilioutaja, Serikali ilitenga Shilingi milioni 250 kwa ajili ya ukarabati na hivi sasa kuna fedha nyingine katika mwaka wa fedha tunaomaliza, ilitengwa kwa ajili ya ukarabati wa kilometa saba kwa barabara hii ya Kanga kwenda Ifwekenya. Mwaka wa fedha tunaoenda kuanza Julai mosi 2023/2025 kuna Shilingi milioni 60 ambayo imetengwa kwa ajili ya ukarabati wa barabara hii. Serikali itaendelea kukarabati barabara hii kwa kadiri ya upatikanaji wa fedha kuhakikisha kwamba huduma kwa wananchi zinapatikana muda wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili kuhusu barabara hii ya Mlowo – NAFCO, nikiri kwamba ni barabara muhimu sana ambayo inaunganisha Wilaya ya Songwe na Makao Makuu ya Mkoa wa Songwe pale Mlowo. Barabara hii imetengewa fedha katika mwaka wa fedha 2023/2024 kwa ajili ya matengenezo ya kawaida. Kwa sababu barabara hii pia na yenyewe haipo katika kiwango cha changarawe, kwa hiyo, katika mwaka wa fedha unaoanza wataanza ukarabati katika maeneo korofi kuweka changarawe badala tu ya kuwa wameilima na greda, wataanza kuweka kifusi katika maeneo korofi na tutaendelea kuitengea fedha kadiri ya miaka ya fedha inavyokwenda na upatikanaji wake.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi. Ni kweli tulitengewa fedha, Shilingi bilioni moja kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amejibu kwenye maswali yangu ya msingi. Barabara hii ya Ikana – Chitete ni barabara ambayo inaunganisha Tarafa ya Ndalambo pamoja na Tarafa ya Msangano ambapo Tarafa ya Ndalambo ndiyo kuna soko la kimataifa. Shilingi milioni 400 ambazo tumetenga kwa sasa haziwezi kushusha ule mlima; je, Serikali haioni kupitia Wizara ya TAMISEMI angalau mtuongezee shilingi milioni 600 nyingine ili tuweze kushusha ule mlima kikamilifu kama ambavyo Mlima wa Jimbo la Kwela unapitika? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge, jiografia ya kule na kuna mito mingi kwa ajili ya kueleka katika Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya hii ya Momba kule Chitete na inaunganisha pia tarafa hizi mbili ya Ndalambo na Msangano. Kama nilivyokuwa nimeshasema kwenye majibu yangu ya msingi, tayari Serikali ilikuwa imeanza ukarabati wa njia hii katika yale maeneo ambayo yalikuwa ni korofi sana. Tutakaa na Mheshimiwa Mbunge kuona ni namna gani tunaweza tukaongeza nguvu kwa ajili ya kuongeza ukarabati wa maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari kuna maeneo ambayo mto unapita ukitoka juu kwa sababu tunapozungumzia ni chini na unatakiwa upite kwenda kupanda mlima mrefu sana na kukutana na barabara ya Zambia. Tayari Serikali ilikuwa imeshaanza ukarabati wa vivuko vile katika maeneo ambayo maji pia yanapita. Kwa hiyo, tutakaa na Mheshimiwa Condester kuweza kuona ni namna gani tunaendelea na ukarabati huu. (Makofi)
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali kwanza tunaishukuru lakini nataka kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ili barabara hii ilete ile tija ambayo imekusudiwa ni vyema ikakamilika kwa haraka ili kunusuru maisha ya wananchi pamoja na mali zao. Ni upi sasa mkakati wa Serikali wa kuhakikisha barabara hii inatengewa fedha za dharura ili iweze kukamilisha ujenzi kwa haraka iwezekanavyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, jiografia ya Wilaya ya Newala kila upande ambao utaingilia unakutana na vilima vikali. Kwa mfano Nadimba Chiwata, Mikumbi, Mpanyani, Mkoma II Chimemena, Lihanga Chikalole. Ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kwamba barabara hizi ambazo nimezitaja zinajengwa angalau kwa kiwango cha changarawe? nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mtanda la kwanza la mpango wa dharura.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimekwishakusema katika majibu yangu ya msingi kwamba Serikali katika mwaka wa fedha huu ambao tupo sasa tumeutekeleza ilitenga shilingi milioni 825 kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii. Mwaka wa fedha tunaoenda kuuanza mwezi Julai 2023/2024 TARURA imetenga shilingi bilioni moja na tayari bado matengenezo haya yanaendelea na yapo asilimia 52.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendelea kuhakikisha kwamba hii bilioni moja inaenda haraka katika Jimbo la Newala Vijijini kwa ajili ya kutekeleza kipande cha barabara ambacho kimetengwa kwa utekelezaji wake ili wananchi waweze kupita kwa sababu barabara hii inaunganisha Jimbo la Ndanda na Jimbo la Newala Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Mwambe na Mheshimiwa Mtanda wamekuwa wakifatilia sana barabara hii. Nikienda kwenye swali lake la pili la barabara hii ambayo inapita Nandimba, Chiwata ambayo inatoka Newala Vijijini kuelekea Masasi tutaendelea kutafuta fedha na kutenga fedha kwa ajili ya kutengeneza barabara hii na kipaumbele kikiwa katika maeneo ya vilima vikali.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kwenye swali langu la msingi. swali la kwanza ni lini sasa Ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tanga kwa kushirikiana na hao wataalam wa TAMISEMI uliowasema watafanya tathmini hiyo ya kujenga kituo cha afya pale Kwamagome?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ahadi hii ya ujenzi wa kituo cha afya ilifanywa kwenye mkutano wa hadhara na Waziri wa TAMISEMI.

Je, uko tayari baada ya Bunge hili la bajeti tuambatane mpaka Kata ya Kwamagome ili ukawaeleze wananchi kwa nini ahadi hii haijatekelezwa kwa miaka miwili tangu imetolewa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kwagilwa hili la kwanza la Ofisi ya Mganga Mkuu lini itaenda na hii timu ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Naomba nitumie Bunge lako hili Tukufu kumwelekeza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tanga pamoja na timu yetu ya tathmini iliyopo Ofisi ya Rais TAMISEMI kuhakikisha wanafika katika Halmashauri ya Mji Handeni na Kata ya Kwamagome kwa ajili ya kufanya tathmini na kuona kama idadi ya watu inayohitajika na ukubwa wa kata ile vinakidhi vigezo vya kupata kituo cha afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili naomba nisisitize wafanye hivyo mara moja huku wakiwasiliana vilevile na Mheshimiwa Kwagilwa ili aweze kuwepo kwa niaba ya wananchi wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pii nipo tayari kuongozana na Mheshimiwa Kwagilwa kuweza kufika Kata ya Kwamagome.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya Kemgesi pamoja na Ligicha Wilayani Serengeti?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ni majuzi tu ambapo tulikaa na Mheshimiwa Mrimi aliwasilisha maombi haya katika Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa ajili ya kituo cha afya Kemgesi na kadiri ya upatikanaji wa fedha tutahakikisha Mheshimiwa Mrimi kule wanaserengeti wanapata kituo hichi cha afya.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, je, lini Serikali itajenga vituo vya afya kwenye Kata za Bwawani, Bangata, Kidina, Otoroto na Kimnya kwenye Jimbo la Arumeru Magharibi?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, tutakaa na Mheshimiwa Mbunge Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu kuweza kuona kwenye bajeti ya mwaka 2023/2024 ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya hivi ndani ya jimbo lake na pale ambapo fedha imetengwa tutahakikisha inaenda mara moja kwa ajili ya kuanza ujenzi wa vituo hivi vya kata.

MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Je, lini Serikali itaanza ujenzi wa Kituo cha Afya Sangamwalugesha Wilaya ya Maswa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaanza ujenzi wa vituo hivi vya afya ambavyo amevitaja Mheshimiwa Mbunge Wilayani Maswa kadiri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwanza namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Kwa kuwa club nyingi ambazo zinaanzishwa hapa nchini zimekuwa zikitumia maeneo ya taasisi ambayo sasa hivi ni machache na sehemu zingine hakuna kabisa. Ni upi mkakati wa Serikali wa Kitaifa wa kuhakikisha kwamba tunakuwa na maeneo ya public ambayo ni theme ya michezo mbalimbali nchini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili hivi karibuni Serikali ilitangaza ajira za walimu takribani 15,000. Nataka kufahamu katika idadi hiyo ya walimu ni walimu wangapi wenye taaluma ya michezo ambao wamechukuliwa kwa taaluma yao na kupelekwa kwenye halmashauri kama ajira ya Serikali? Nakushuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Kanyasu la kwanza nini mkakati wa Serikali kuwa na maeneo yake ya michezo na kuacha kutegemea taasisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni tumeona mbele ya Bunge lako hili Wizara ya Michezo ikipitisha bajeti yake na tayari kwa mfano hapa Dodoma wana mkakati wa kujenga uwanja pale katika eneo la nane nane ambalo litakuwa linamilikiwa na Serikali. Katika mikoa mingine vivyo hivyo wameendelea kuweka mpango kwa ajili ya kuwa na maeneo ya wazi na tutashirkiana na wenzetu wa Wizara ya Michezo kuona ni namna gani tunaweka kipaumbele hicho katika kujenga maeneo haya ili wanafunzi waweze kufanyia mazoezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili kwenye idadi ya walimu walioajiriwa hawa hivi karibuni ni wangapi ni walimu wa michezo. Nitakaa na Mheshimiwa Kanyasu ili kuona katika orodha hii ya majina ambayo hivi karibuni Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI ametangaza ni walimu wangapi ambao wameingia wa kada ya michezo.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza niishukuru Serikali kwa kufanya jitihada za kupeleka mradi hasa wa ujenzi wa Daraja la Mto Mnyamansi. Kwa kuwa eneo la Ifinsi kwenda Kijiji cha Bugwe hakuna mawasiliano ya aina yoyote. Serikali ina mpango gani wa kujenga barabara hiyo ili iweze kuwasaidia wananchi kwenye eneo hilo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili tunatambua jitihada za Serikali zilizofanywa, mmefungua barabara ya Kamibanga hadi Ifinsi, Majalila hadi Ifinsi lakini barabara zote hizo zilizofunguliwa hazijawekewa molamu na madaraja. Ni lini Serikali itaanza kujenga na kuboresha barabara hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kakoso. La kwanza juu ya mpango wa ujenzi wa barabara hii ya Ifinsi – Bugwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba barabara hii haikuwepo na ilikuwa wananchi hawa wanakaa kwenye kisiwa kipindi ambapo mvua zinanyesha. Tayari baada ya utengaji huu wa bajeti ya 1.5 billioni, Serikali pia katika Mwaka wa Fedha 2023/2024 imetenga kiasi cha shilingi milioni 475 kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha changarawe kwenye vipande korofi na kuweka mifereji katika maeneo mbalimbali ya barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili lla Barabara za Kambanga – Ifinsi na maeneo mengine aliyoyataja Mheshimiwa Kakoso tutakaa naye Mheshimiwa Mbunge na kuona ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya ukarabati na kuweka kifusi katika barabara hizi.

MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya kutoka Mwamkulu – Kakese hadi Misunkumilo yenye kilometa 30 kwa kiwango cha lami kupitia TACTIC Awamu ya Pili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ya Mwakulu – Kakese ipo katika mpango wa ujenzi wa mradi ule wa TACTIC na hivi karibuni watatangaza kazi ya kuweza kuwapata wale watakaofanya usanifu wa barabara hii na itaanza ujenzi wake kwa vipande. Kwa hiyo, wakipata wale watu wa kwenda kufanya usanifu tutamjulisha Mheshimiwa Kapufi ili naye aweze kushiriki katika zoezi la utiaji saini kama ambavyo tulifanya kwenye miradi mingine ambayo ipo chini ya TAMISEMI.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa. Je, ni lini Serikali itajenga daraja la kutoka Mlambalasi ambayo ni Kata ya Kiwere kwenda Kalenga ambako ndiko kwenye Makumbusho ya Chifu na wananchi wamekuwa wakipata shida sana? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, tutakaa na Mheshimiwa Mbunge kuweza kupitia bajeti ya TARURA ya mwaka 2023/2024 na kuona ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa daraja hili la Mlambalasi kuelekea Kalenga; na kama bajeti imetengwa tutahakikisha mara moja fedha hiyo inakwenda ili ujenzi huu uweze kuanza.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa niaba ya Mheshimiwa Tarimba Abbas, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa Serikali iko kwenye maboresho ya utoaji wa hizi asilimia 10; Serikali haioni ni wakati sahihii wa kufanya marekebisho ya sheria pia ili kuongeza kundi la wanaume kwenye utoaji wa mikopo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili; kwa kuzingatia mila, desturi na utamatudini wetu, jamii nyingi ya Tanzania mwanaume ni kiongozi wa familia; hauoni kwa kumuondoa mwanaume kwenye utoaji wa mkopo ni kufanya kumdumisha mwanaume lakini ni ubaguzi unaoondoa umoja wetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Tarimba, ambayo yameulizwa kwa niaba yake na Mheshimiwa Mafuwe la kwanza juu ya maboresho haya, kwa sasa kama ambovyo amesema mwenyewe Mheshimiwa Mbunge, Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI ipo katika mapitio ya sera hii na sheria hii kwa ajili ya kuona ni namna gani inaweza kuboreshwa kuendana na wakati wa sasa na tayari kuna timu ambayo wajumbe wake wameshateuliwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Mheshimiwa Kairuki na imeishaanza kazi yake na pale itapomaliza kazi yake basi tutaleta kwenye Bunge hili kupitia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya TAMISEMI na baada ya hapo kuileta ndani ya Bunge hili kwa ajili ya kuweza kufanya marekebisho ya sheria hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la kuwa na wanaume ni namna gani wanaingizwa kwenye unufaikaji wa mikopo hii? Tayari timu hii itaangalia pia uwezokano wa hili lakini katika makundi haya wanaume wapo kwenye makundi ya vijana, wanaume wapo katika makundi ya walemavu lakini tutachukua ushauri wa Mheshimiwa Mafuwe na kuona ni namna gani nao tunaweza tukaangalia wanaingizwaje katika kupata au kunufaika na mikopo hii.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Serikali inaendelea na maboresho na VICOBA ni vikundia ambavyo wananchi ususani wanawake wa Kilimanjaro wameshamiri sana; ni kwa nini VICOBA visiusishwe sasa katika mikopo hii ya asilimia 10?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyokuwa nikisema awali maboresho haya yanafanyika kwanza ni kutokana na maagizo aliyoyatoa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania juu ya kuangalia upya utoaji wa mikopo hii kwa vikundi. Kwa hiyo, naamini katika timu ambayo inafanya kazi watapitia pia hili la VICOBA kuona uwezekano au upi ni urahisi kuweza kuwafikia wananchi wengi zaidi.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa Mji wa Kharumwa unazidi kupanuka na matengenezo yanafanywa ya mara kwa mara kwenye barabara zetu za mitaa pale Kharumwa, lakini zinaponyesha mvua barabara zile huwa zinaharibika kwa ajili ya ukosefu wa mitaro. Je, Wizara iko tayari kutenga fedha kwa ajili ya kujenga hiyo mitaro ili kunusuru uharibifu wa barabara hizo wakati wa mvua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia TARURA imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya maboresho ya Mji wa Kharumwa kule Wilayani Nyang’wale anakotoka Mheshimiwa Amar na tutaendelea kuangalia ni namna gani tunapeleka fedha ya kutosha kadri ya upatikanaji wake, kwa ajili ya kuboresha mazingira ya mji huu hasa ujenzi wa mitaro ambayo upo kule Wilayani Nyang’wale. Nimtoe shaka Mheshimiwa Mbunge, yeye ni shahidi vile vile kwamba TARURA imeongezewa fedha zaidi ya mara tatu ya ile iliyokuwepo mwaka wa fedha 2020/2021 na hii ni commitment kubwa ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Watanzania kwa kutenga fedha ya kutosha kwa TARURA kuhakikisha barabara nyingi zaidi zinatengenezwa.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, Serikali kupitia TARURA, Mkoa wa Simiyu iliahidi kujenga Daraja la Mto Sanjo linalounganisha Itilima na Meatu na Daraja la Mto Sanga linalounganisha Maswa na Meatu kwa muda mrefu. Je, ni lini Serikali itatimiza azma yake hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itatimiza azma ya kujenga madaraja haya katika mito hii miwili aliyoitaja Mheshimiwa Mpina, inayounganisha kati ya Wilaya ya Itilima na Wilaya ya Maswa, lakini kuna mingine ambayo ametaja pia ya Wilaya ya Meatu anakotoka yeye Mheshimiwa Mpina. Tutaangalia katika bajeti hii ambayo tunaenda kuitekeleza 2023/2024 na kuona ni kiasi gani kimetengwa na nitakaa na Mheshimiwa Mpina kuweza kuona tunaanza vipi kwa haraka kadri ya fedha iliyotengwa ya ujenzi wa madaraja haya mawili.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, majibu ya Serikali ni mazuri sana na Mkoa wa Simiyu umepewa fedha kwa ujumla kama walivyopewa Mikoa mingine. Namuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa umuhimu wa Mkoa wa Simiyu kwa sababu ya zao la pamba, kwa sababu kuna njia mbovu sana kwa mfano sasa hivi tunakwenda kusafirisha mazao ya pamba njia ni mbaya sana kutoka vijijini.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri uko tayari sisi kwa kushirikiana na TARURA tulete hesabu ya kipekee kwa ajili ya kupambana na tatizo hili ili muweze kutujengea barabara mbovu katika Mkoa wa Simiyu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nyongo la kuleta maombi ya kipekee; hivi sasa Serikali kupitia Ofisi ya Rais TAMISEMI imeteua timu ya kufanya mapitio ya namna ya kutoa mgao wa fedha za barabara kwenye Halmashauri zetu kote nchini kwa kuangalia umuhimu wa maeneo, kuangalia masuala ya kilimo yaliyokuwepo hapo, upitwaji wa magari kwa wingi na kadhalika.

Kwa sasa TARURA ilirithi mfumo ambao ulikuwa katika Road Fund ya namna ya mgawanyo wa fedha hizi zinazopelekwa, lakini baada ya timu hii kumaliza itawasilisha taarifa yake kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na baada ya kuwasilisha taarifa hiyo, watakaa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, pamoja na TARURA kuona ni namna gani sasa mgawanyo wa fedha utaendana kutokana na mazingira yaliyoko katika maeneo mbalimbali hapa nchini ikiwemo kule Jimbo la Maswa anakotoka Mheshimiwa Nyongo.

MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa barabara nyingi za ndani ya Mji wa Mugumu kule Wilayani Serengeti zina hali mbaya sana na haziwezi kupitika; je, ni lini sasa Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa barabara hizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Amsabi Mrimi la lini Serikali itaongeza ukarabati wa barabara zake katika Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti?

Mheshimiwa Naibu Spika, nilijulishe Bunge lako tukufu kwamba hivi tunavyoongea hivi sasa kuna barabara ambayo inazunguka Soko Kuu la Mji wa Mugumu ambayo inatengenezwa kwa kiwango cha lami kupitia Wakala wetu wa TARURA na tutaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuboresha mazingira ya Mji wa Mugumu kwa sababu ndiyo Makao Makuu ya Wilaya ya Serengeti. Lakini vilevile kupitia Wilaya nzima ya Serengeti barabara za changarawe vilevile tutaendelea kuhakikisha fedha inatengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara zake na nyingine Mheshimiwa Mbunge Mrimi amekuwa akija kwa ajili ya kuzielezea na kusema barabara zipi ziweze kutengewa fedha kwa ajili ya kuzifungua.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana pamoja na majibu mazuri ya Serikali ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Moja; kwa kuwa changamoto za barabara na za Mkoa wa Simiyu zimekuwa zikiongezeka siku hadi siku, barabara ni mbovu, wananchi wanashindwa kupita na kusafirisha mazao yao; je, Serikali ina mpango gani sasa wa muda mfupi kuhakikisha wanarekebisha barabara za Mkoa wa Simiyu zile ambazo zinachangamoto kubwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa changamoto ya barabara za Mkoa wa Simiyu inafanana na zile za Mkoa wa Dar es Salaam. Mkoa wa Dar es Salaam umekuwa na changamoto kubwa ya barabara chakavu lakini na kukosa mitaro hali ambayo inasababisha wakati wa mvua shuhuli zote za kiuchumi kusimama katika Mkoa wa Dar es Salaam; je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuhakikisha wanajenga mitaro na kurekebisha ili sasa wakati wa nyakati za mvua magari yaweze kupita? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza la kwanza hili la mpango wa barabara za Mkoa wa Simiyu kama ambavyo nimeisha kwenye majibu yangu ya msingi, ukiangalia mwaka 2021 Serikali ilikuwa imetenga shilingi bilioni tano kwa Mkoa wa mzima wa Simiyu kwa ajili ya ukarabati wa barabara lakini kuonyesha ni namna gani Serikali inajali wananchi wa Mkoa wa Simiyu, inajali wananchi wake wa Tanzania iliiongezea fedha TARURA kutoka shilingi bilioni 226 na kwenda shilingi bilioni 776 zaidi ya mara tatu ya ile bajeti ya mwanzo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ukiangalia Mkoa wa Simiyu peke yake kutoka shilingi bilioni tano kwenda shilingi bilioni 17 ambayo imetengwa kwa ajili ya mwaka wa fedha 2023/2024. Hivyo Serikali itaendelea kuweka kipaumbele cha kuhakikisha kwamba barabara zinatengenezwa kwa wakati ili ziweze kupitika na kuendelea kupunguza asilimia ya barabara mbovu kwa kuhakikisha TARURA inaendelea kuwekewa fedha kwa ajili ya matengenezo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la pili kuhusu Mkoa wa Dar es Salaam; wewe pia ni shahidi kwa sababu ni Mbunge wa Mkoa wa Dar es Salaam tayari hivi karibuni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Angellah Kairuki alikaa na Wabunge wote wa Mkoa wa Dar es Salaam na vilevile aliita Kamati ya Bunge ya TAMISEMI na kusaini mikataba kwa ajili ya kuanza Mradi wa DMDP II ambayo itakwenda barabara zote ambazo zinachangamoto, zilizosalia ambazo hazikuwepo kwenye DMDP I katika Mkoa wa Dar es Salaam ni zaidi ya shilingi bilioni 800 ambayo Serikali hii ya Mama Samia Suluhu Hassan imetenga kwa ajili ya kuhakikisha Mkoa wa Dar es Salaam unaboreka. (Makofi)
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii. Sehemu kubwa ya Jimbo la Arumeru Mashariki liko kwenye miteremko ya Mlima Meru, kwa hiyo barabara zake kwa mwaka mzima zinakuwa ni mavumbi au mifereji wakati wa mvua. Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga fedha kwa ajili ya kuzijenga kwa kiwango cha lami au tabaka gumu la namna nyingine kwa teknolojia nyingine yoyote? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo la barabara zake hizi za Arumeru Mashariki kwamba, Serikali imeweka commitment kubwa kwa kuiongezea fedha TARURA kuhakikisha barabara nyingi zaidi zinatengenezwa kwa kuwapa bajeti mara tatu ya ile ambayo Dkt. Samia Suluhu Hassan aliikuta mwaka 2021. Sasa tutakaa na Mheshimiwa Dkt. Pallangyo tutazidi kuangalia ni namna gani TARURA inaweza ika-fast track utengenezaji wa barabara hizi ambazio wananchi wa Arumeru Mashariki wanazihitaji.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa mahitaji ya Walimu wa shule za msingi katika Jimbo la Babati Vijijini ni 1,956 na waliopo ni 1,226 na hivyo kuwa na upungufu wa Walimu 730. Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha Walimu wanaopatikana katika shule za msingi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyokwishasema kwenye majibu yangu ya msingi, Serikali inaendelea kuweka kipaumbele cha kuajiri Walimu na hasa katika shule za msingi kuhakikisha inapeleka Walimu wa kutosha kwenye maeneo yenye upungufu ikiwemo kule Jimboni kwa Mheshimiwa Sillo. Katika hao 13,130 tutaangalia ni mgao kiasi gani ambao Mheshimiwa Sillo amepata kule katika Halmashauri yake na nitakaa naye kumpa hiyo orodha.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Mkoa wa Tabora ni moja kati ya mikoa ambayo shule nyingi sana ziko katika maeneo ya vijijini na hazina Walimu wa kutosha. Je, Serikali haioni sasa umefika wakati wa kupeleka Walimu maeneo hayo ili kunusuru elimu ya Mkoa wetu wa Tabora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikitoa kipaumbele katika maeneo mbayo yana upungufu wa walimu ikiwemo Mkoa wa Tabora na ndio maana katika miaka ya fedha iliyopita ikiwemo wa 2021/2022, ukijumlisha wote Mkoa wa Tabora ulipokea Walimu 1,111 na kwa kutambua bado kuna upungufu huo, Serikali ndio maana ilitoa ajira 13,130 kwa kupitia kibali alichokitoa Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan. Kwa sababu Mheshimiwa Rais anapeleka fedha nyingi za ujenzi wa miundombinu ya madarasa naku – invest hela nyingi katika elimu hapa nchini, Serikali itaendelea kuweka kipaumbele cha kuajiri Walimu na ikiwemo katika Mkoa ule wa Tabora.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, ni lini Serikali itapeleka Walimu wa kike katika shule ya msingi iliyoko Nkasi inaitwa Shule ya Itete na Shule ya Kala?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, katika ajira hizi mpya 13,130 ambazo Serikali imetoa katika mwaka huu wa fedha tutaangalia na kuweka kipaumbele katika shule hizi alizozitaja za Itete na Kala kule Wilayani Nkasi.

MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Katika Jimbo la Same Magharibi maeneo ya milimani hasa Kata za Msindo, Mshewa, Vudee, Tae, Suji, Chomi, Muhezi na Ruvu kuna shida kubwa sana ya Walimu na kwa sababu pengine mazingira magumu ya milima. Je, ni lini Serikali itapeleka Walimu wa kutosha katika kata hizo za milimani na kuwapatia motisha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itapeleka Walimu katika mgao huu wa hawa 13,130, Wilaya ya Same nayo itapata Walimu hawa kwenda kufanya kazi kule na tutaendelea kuajiri kadri ya bajeti itakavyoruhusu kwa ajili ya kuweza kupeleka Walimu kwenye maeneo yote yenye upungufu hapa nchini, ikiwemo kule kwa Dkt. Mathayo, Wilayani Same.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika Serikali imeboresha, imejenga shule nyingi za msingi na sekondari na kuna uhaba wa Walimu. Je, Serikali ina mpango gani wa kukidhi mahitaji ya Walimu ambao ni takribani Walimu 1,000 ni pungufu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali mipango yake ya kuhakikisha hakuna upungufu wa Walimu katika Wilaya ya Tanganyika na wilaya zingine hapa nchini, ndio maana imeendelea kuajiri na hivi karibuni ajira 13,130 zimetolewa za Walimu kwa ajili ya kwenda kuziba mapengo na uhitaji uliopo katika maeneo mbalimbali hapa nchini ikiwemo kule Tanganyika.

MHE. JACQUELINE K. ANDREA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa majibu mazuri ya Wizara, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza; Serikali haioni kwamba kuna haja ya kuweka motisha kwa Walimu walioko vijijini, ili tuweze kupata Walimu wengi waweze kwenda kuajiriwa vijijini ili tuweze kuondokana na upungufu maeneo ya vijijini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; Serikali haioni kuna haja ya ajira hizi zinazotoka nyingi zielekezwe vijijini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza aliyouliza Mheshimiwa Kainja. La kwanza hili la motisha kwa Walimu vijijini, tayari Serikali inalifanya hili kwa kupitia Wakurugenzi wa Halmashauri husika, kuna Halmashauri ambazo Walimu wanaporipoti kazini wamekuwa wakipatiwa magodoro na vifaa vingine vya kuweza kuwapa motisha kubaki katika maeneo yao ya kazi. Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe kule imekuwa ikifanya hivyo na maeneo mengine nchini na tutaendelea kuona ni namna gani tunatoa motisha kwa Walimu hawa wanaoenda vijijini kadri ya upatikanaji wa fedha na uwezo wa Serikali na bajeti kuruhusu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, la haja ya ajira hizi hawa Walimu kwenda vijijini. Walimu hawa wanaajiriwa kutokana na upungufu uliopo kwenye maeneo husika hasa maeneo haya ya vijijini. Sasa naomba nitoe rai hapa kwa Wakurugenzi wa Halmashauri ambao ndio waajiri wa Walimu hawa na wale wa Mkoani Tabora kule anakotoka Mheshimiwa Kainja vile vile, kuhakikisha kwamba hawa wanaopangiwa maeneo haya kwenda kufundisha wanabaki kule kwenye maeneo yale kwa mujibu wa sheria, taratibu na kanuni za utumishi wa umma. Kwa sababu Serikali ilifanya review ya maeneo yote yenye upungufu wa Walimu na ndiyo maana hawa wanaajiriwa kwenda kuziba mapengo yale yaliyokuwepo kwenye maeneo yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kila mmoja akiomba kuhama, ina maana mapengo yale yanazidi kuwepo. Vile vile nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote Serikali itaendelea kuajiri Walimu hawa kwa ajili ya kuziba mapengo haya na upungufu uliopo kadri ya bajeti itakavyoruhusu.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kunipa fursa hii, kwa kuwa Wilaya ya Namtumbo ni wilaya ambayo iko pembezoni kabisa mwa nchi hii Kusini mwa Tanzania mpakani na Msumbiji na ina upungufu mkubwa wa Walimu katika shule zake za msingi. Je, Serikali inaweza ikatupa umuhimu kutugawia Walimu wa kutosha katika shule zetu zenye upungufu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua upungufu uliokuwepo katika Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo kule Jimboni kwa Mheshimiwa Kawawa na katika ajira hizi mpya 13,130, Wilaya ya Namtumbo nayo itapata mgao wa Walimu wapya kwa ajili ya kwenda kupunguza upungufu uliopo kule wilayani.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipa nafasi hii. Kwa kuwa Halmashauri zote za Mkoa wa Shinyanga hasa vijijini zina upungufu mkubwa wa wafanyakazi. Je, ni nini kauli ya Serikali kutatua tatizo hili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Dkt. Mnzava kwamba, Serikali itaendelea kutatua upungufu wa watumishi wa umma ikiwemo Walimu katika Mkoa wa Shinyanga na mikoa mingine hapa nchini kadri ya bajeti yake itakavyoruhusu na ndio maana katika bajeti ya 2022/2023 Serikali ilitenga ajira 21,000 kwa ajili ya Walimu na kada ya afya, kwa ajili ya kupunguza upungufu uliopo kote nchini ikiwemo kule Shinyanga.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na mgao huu wa Walimu 13,100 Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ziko shule zilionekana zina upungufu sana wa Walimu, lakini katika mgao huo hazikupata Mwalimu hata mmoja, ikiwemo Shule ya Msingi Litoho. Je, ni lini, sasa Serikali itapeleka Walimu kwenye Shule hii ya Msingi Litoho na shule nyingine za Halmashauri ya Mbinga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu upungufu ambao ameuzungumzia Mheshimiwa Kapinga uliokuwepo kule Wilayani Mbinga, Serikali ndio maana imekasimu mamlaka kwa Makatibu Tawala wa Mikoa kufanya msawazo wa Walimu kuhakikisha shule mbalimbali zinapata Walimu kwa kutoa maeneo yenye Walimu wengi zaidi na kuwapeleka kwenye maeneo yenye uhitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi nichukue nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu, kumwelekeza Katibu Tawala wa Mkoa wa Ruvuma kuhakikisha kwamba anapeleka Walimu kwa kufanya msawazo ndani ya Mkoa wake katika shule alizozitaja Mheshimiwa Kapinga.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mheshimiwa Waziri amesema kwamba mwajiri wa Walimu hawa ni Mkurugenzi wa Halmashauri, lakini Mkurugenzi huyo wa Halmshauri amemnyima nafasi ya kukataa uhamisho wa mtumishi, jambo linalofanya watumishi wengi kuchukua namba tu kwenye hizi wilaya ambazo zipo pembezoni na kuondoka. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha Wakurugenzi wanakuwa na Mamlaka ya kuhamisha kulingana na wanavyoona nafasi inayopatikana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kuchauka. Hili la kukataa uhamisho liko wazi, Waraka wa Katibu Mkuu Utumishi unaeleza wazi kwamba mtumishi wa umma anapoajiriwa atatumikia mwaka mmoja wa probation na baada ya mwaka ule anatakiwa kukaa katika kituo chake kipya cha kazi kwa muda usiopungua miaka miwili kabla ya kuomba uhamisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, namna utaratibu ulivyo ni lazima mtumishi anapoomba uhamisho katika barua yake ile awaweke pale KK, Mkuu wake wa Shule, amuweke Afisa Elimu wa Wilaya, amuweke muajiri wake ambaye ni Mkurugenzi wa Halmashauri na wale wote wanatakiwa kuweka comment pale, kama wanaona kuna uhaba wa watumishi katika maeneo yao, katika barua ile wanavyoandika imepitishwa, aandike kwamba kuna uhaba na huyu nashauri asihame. Barua ile inapofika Ofisi ya Rais, TAMISEMI, wataangalia na zile comment za mwajiri na kuzifanyia kazi na kuhakikisha kwamba Mwalimu yule au mtumishi yule hatoki katika maeneo yale ikiwemo kule Liwale. Kwa hiyo naomba Mkurugenzi wa Liwale afuate utaratibu.
MHE. MARYAM AZAN MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa vile tayari Serikali imeshatenga bajeti ya kutoa kifungua kinywa katika shule. Je, ni vipi Serikali itaangalia kwa uangalifu zaidi vifungua vinywa hivyo ambavyo vitatolewa katika shule hizo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza. Kwanza Serikali siyo kwamba imetenga bajeti kwa ajili ya vifungua kinywa, nilichokisema kwenye majibu yangu ya msingi ni kwamba Serikali kupitia Wizara ya Elimu, imetoa mwongozo wa namna gani ya kupata lishe ikiwemo wazazi wa maeneo husika kuchangia katika kupata lishe watoto hawa wakiwa shuleni.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, lakini je, haioni iko haja ya kufanya nguvu zaidi kwa ajili ya shule hizi za sekondari ambazo ni kongwe hasa katika Jimbo langu la Temeke, Shule ya Kibasila?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; je, Serikali haioni iko haja ya kuongeza pia nguvu katika shule ambazo zilianza kujenga ofisi hizi lakini mpaka sasa hazijaendelezwa mfano kwangu, shule inaitwa Ally Hassan Mwinyi ambayo ni jina kubwa sana. Je, ni lini sasa Serikali itaweza kumalizia ofisi hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Dororth Kilave, Mbunge wa Temeke, kwanza kuhusu kuongeza jitihada ya Serikali kwa ajili ya kukarabati na kujenga shule hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimfahamishe Mheshimiwa Mbunge na wana-Temeke kwa ujumla kwamba, Serikali hivi karibuni imepeleka shilingi milioni 700 katika Shule ya Sekondari Kibasila kwa ajili ya ujenzi wa mabweni na madarasa, likiwemo jengo la utawala katika shule ile. Kwa hiyo, ni jitihada kubwa za Serikali hii ya Awamu ya Sita katika kuhakikisha inaboresha miundombinu ya shule za sekondari na shule za msingi katika Halmashauri ya Wilaya ya Temeke na nchini kote.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali la pili kuhusu shule zilizoanza ujenzi wa majengo haya ya utawala zenyewe, ikiwemo shule ya Ali Hassan Mwinyi, nitakaa na Mheshimiwa Mbunge na kuona ni namna gani Serikali inaweka jitihada kupitia Halmashauri ya Manispaa ya Temeke kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa jengo hili la utawala katika shule hii yenye jina la Rais wetu wa Awamu ya Pili, Mheshimiwa Dkt. Ali Hassan Mwinyi.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu hayo ya Serikali ambayo yamenipa mashaka katika mawanda ya ushirikishwaji wa wadau, niseme tu kwamba, katika sehemu ambayo Serikali inatakiwa kuwa makini ni katika kutunga sera hii kwa sababu, ndiyo inakwenda kujibu Ibara ya 146 ya Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Swali la kwanza; Ni kwa kiwango gani wadau katika Mikoa, Wilaya na Halmashauri na kwa upekee wake Waheshimiwa Madiwani wameshirikishwa katika utungaji wa sera hii?

Swali la pili; Je, Serikali iko tayari kutoa commitment hapa Bungeni kwamba, katika mchakato huu kabla ya maamuzi sera hii ipitiwe na Wabunge, kama tulivyopitia Sera ya Elimu, kwa lengo la kutoa input zaidi na kuboresha utungaji wa sera hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Ally Kassinge, swali lake la kwanza anasema ana mashaka, nimtoe mashaka haya kwamba Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ina imani kubwa na Sera nzima ya D by D na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, chini ya uongozi wake Mheshimiwa Angellah Kairuki itaendelea kusimamia sera hii ya D by D ambayo ni ugatuaji wa madaraka kwenye Halmashauri. Halmashauri hizi ziweze kuwa na uwezo wa kufanya maamuzi yao wenyewe kwa kushirikiana na wataalam ambao wanapelekwa na Serikali katika maeneo yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye Sali lake la pili ambalo anataka commitment, commitment kama nilivyosema hapo nikimjibu swali lake la nyongeza la kwamba, Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan, inaamini katika D-by-D. Baada ya mwongozo huu kufanyiwa mapitio tutaileta kwenye Kamati ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, ili nao waweze kupitishwa kwenye mwongozo ule ambao upo, lakini tutabaki katika D by D Mheshimiwa Mbunge na hatutatoka katika hilo kwa ajili ya kuwapa nguvu Waheshimiwa Madiwani kufanya maamuzi yao katika Halmashauri zao.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kumekuwa na migogoro mingi sana katika maeneo mbalimbali ya Kata kwa Kata, Kijiji kwa Kijiji, Mkoa kwa Mkoa, Wilaya kwa Wilaya. Sasa na wataalam wetu wamekuwa wakisoma hizi ramani kwa muda mrefu sana.

Je, kupitia Wizara yako hauoni kutoa maagizo mahsusi kwa wahusika wakamalize migogoro hii kwa haraka?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili. Kwa kuwa, mgogoro huu mahsusi wa Kata ya Tura na Wilaya ya Singida (Ikungi). Je, hauoni haja ya mimi na wewe Naibu Waziri tukaenda tukaumaliza ili sasa wananchi wabaki na amani na wajue nini wanachotakiwa kuenda na wapi ni mpaka wao? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Venant Protas, Mbunge wa Igalula:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna mgogoro wa muda mrefu katika eneo hili ambalo Mheshimiwa Mbunge amelizungumzia na hasa kuna vijiji viwili vya Makene ambayo ipo katika Kata ya Iyumbu, Wilayani Ikungi na Kijiji cha Nkongwa kilichopo Kata ya Tura, Wilayani Uyui. Tayari jitihada za Serikali kupitia Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya hizi mbili ya Uyui na Ikungi, vilevile Mikoa hii miwili zimekuwa zikifanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nitumie Bunge lako Tukufu hili kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuwaelekeza, Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya wa Wilaya hizi mbili kukutana mara moja wiki hii, kwa ajili ya kupata suluhu ya mgogoro huu na kufanya majadiliano haya yafike mwisho ili mipaka ya Mikoa hii miwili iweze kujulikana na wananchi wajue wanapata huduma kutoka upande gani wa maeneo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, mimi nipo tayari kuongozana na Mheshimiwa Mbunge kadri tutakapopata tu taarifa ya Kamati za Ulinzi na Usalama hizi mbili za Wilaya ya Ikungi na Uyui, nitaongozana na Mheshimiwa Mbunge ambae amekuwa mstari wa mbele katika kuwapigania wananchi wake wa Uyui. Nitaongozana nae kwenda kuhakikisha tunafanya mkutano na wananchi hawa na kuwaeleza mipaka iliyopo kwa mujibu wa GN.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Serikali, lakini nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; kwa kuwa bado kuna idadi kubwa sana ya Walimu wa Masomo ya Sayansi ambao bado hawajapata ajira na Serikali ilikuwa inaendelea kuajiri kidogo kidogo.

Je, ni upi mkakati wa Serikali sasa kuhakikisha kwamba angalau inaongeza wigo wa ajira angalau kuchukua Walimu wote walioko katika soko ambao kwa sasa wako tu hawana shughuli za kufanya?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa suala zima la sayansi pia linaendana na uwepo maabara na wananchi nchi nzima maeneo yote wamejenga sana maboma mengi ya maabara, lakini kulikuwa na kasi ndogo ya ukamilishaji wa miradi hiyo ya Maabara. Je, Serikali ina mpango gani mahususi kuhakikisha kwamba ndani ya kipindi kifupi maboma yote yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi yanakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza yaliyoulizwa na Mheshimiwa Shangazi kwa niaba ya Mheshimiwa Kapinga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, hii idadi ya Walimu ambao bado hawajapata ajira hawa wa sayansi, nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali hii ya Awamu ya Sita itaendelea kutoa kipaumbele katika kuziba mapengo na kuajiri Walimu wengi zaidi kwa sababu kama walivyoona, Wabunge wote ni mashahidi, Serikali hii imejenga miundombinu mingi sana kwenye suala zima la elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa Walimu 13,130 ni kwenye mwaka wa fedha huu ambao tunaumaliza, kwa maana ilikuwa 2022/2023 na vilevile Serikali imetenga bajeti kwa ajili ya 2023/2024 na pale ambapo fedha zitaruhusu, basi Serikali itaendelea kuajiri Walimu wengi zaidi na kuwapeleka katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la uwepo wa maabara. Ni kweli Serikali iliweka kipaumbele katika ujenzi wa maabara katika maeneo mbalimbali hapa nchini kwa kupeleka shilingi milioni 30, 30 katika shule nyingi sana hapa nchini kwa ajili ya ujenzi wa maabara hizi. Baada ya ujenzi huu kukamilika sasa Serikali iko katika harakati za kutafuta fedha kwa ajili ya kupeleka vifaa vya maabara hizi. Mara baada ya vifaa hivyo kufika kwenye maabara hizi, vilevile tutaangalia tena namna gani ya kupata fedha kuendeleza ujenzi wa maabara zingine kote nchini.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Swali la kwanza; Hospitali ya Wilaya ya Chemba tayari imefungwa mashine za x-ray na ultra-sound lakini hakuna mtaalam hata mmoja. Naomba kujua ni lini Serikali itapeleka wataalam hao ili mashine hizo zifanye kazi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Kituo hicho hicho cha Afya cha Mrijo kinahudumia Kata nne zikiwemo Kata za Wilaya ya Kiteto. Naomba kujua ni lini sasa watapeleka gari la wagonjwa ili liweze kuhudumia kituo hicho?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mohamed Lujio Monni, Mbunge wa Chemba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza hili la wataalam wa mionzi katika Hospitali ya Wilaya. Nimtoe mashaka Mheshimiwa Monni, Serikali inaendelea kutafuta wataalam hawa hata katika ajira ambazo zilikuwa zimetangazwa na Serikali katika upungufu ambao tulipata kwa kutokuwa na watu walioomba nafasi, ni nafasi kama hizi za wataalam wa mionzi, lakini Serikali itaendelea kuweka jitihada kubwa kwa ajili ya kuajiri wataalam hawa ili Hospitali ya Wilaya ya Chemba nayo iweze kupata watumishi watakaosaidia katika kutumia mashine hizi za x-ray na nyinginezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la Kituo cha Afya Kata ya Mrijo ambacho kinahudumia kata nne kama alivyosema Mheshimiwa Monni. Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imewekeza fedha nyingi katika sekta hii ya afya vilevile na tayari fedha imeshatolewa kwa ajili ya ununuzi wa magari ya kubebea wagonjwa ambapo kila halmashauri hapa nchini ikiwepo Halmashauri ya Wilaya ya Chemba itapata magari mawili kwa ajili ya kubebea wagonjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali haikuishia hapo, Mheshimiwa Rais bado aliona kuna umuhimu wa kupata magari kwa ajili ya supervision, kwa ajili ya watalaam wetu kutembelea zahanati zetu na vituo vya afya ambavyo vipo katika Halmashauri hizi, kwa hiyo pia halmashauri hizi zitapata angalau gari moja kwa ajili ya supervision.
MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Naomba nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali kwa jinsi inavyoweka mikakati mizuri ya kufanya ukarabati wa miundombinu katika shule zetu za msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Mbinga Mjini lina Kata 19 na Kata nane ziko mjini, Kata 11 ziko vijijini lakini bado kuna changamoto kubwa sana ya Walimu katika eneo hili la Jimbo la Mbinga Mjini. Katika mgao wa Walimu ambao wameajiriwa hivi karibuni Jimbo la Mbinga Mjini halijapata Mwalimu hata mmoja. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inamaliza changamoto hii katika Jimbo la Mbinga Mjini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kumwelekeza Katibu Tawala, Mkoa wa Ruvuma kuhakikisha anafanya msawazo ndani ya Mkoa wake kwa maeneo ambayo yana upungufu wa watumishi. Kuna maeneo ambayo yatakuwa na watumishi au Walimu wengi zaidi na yale ambayo bado hayajapata watumishi, basi Katibu Tawala wa Mkoa aweze kuhakikisha anapeleka watumishi ikiwemo katika Jimbo la Mheshimiwa Mbunda la Mbinga Mjini.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza. Katika Jimbo la Manyoni Mashariki, Shule ya Msingi ya Iseke, Makanda na Sasagila ni kongwe sana. Je, nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba wanapeleka madarasa kwenye hizi shule kongwe? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pius Chaya, Mbunge wa Manyoni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hili lini Serikali itapeleka fedha katika shule hizi kongwe. Tayari Serikali kupitia mradi wa BOOST imetenga zaidi ya bilioni 230 kote nchini kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa shule kongwe hapa nchini na shule mpya katika halmashauri mbalimbali ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni. Hizi shule za Iseke, Makanda na Sasajira nazo tutazifanyia tathmini kuona uhitaji uliopo na baada ya hapo tutaziweka katika mipango yetu kwa ajili ya ofisi kutoa fedha.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Moja ya sababu za kushuka kwa ufaulu katika maeneo ya vijijini hasa Mbulu Vijijini ni kukosekana kwa nyumba za walimu na sisi tumejenga maboma yamefikia hatua mbalimbali.

Je, ni lini uko tayari kupeleka fedha katika majengo hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei la nyumba hizi za walimu zilizojengwa kwa nguvu za wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Ofisi ya Rais, TAMISEMI, inafanya tathmini ya maboma yote ya nyumba za walimu ambayo yamejengwa kwa nguvu za wananchi na pale tathmini hii itakapokamilika basi itawasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI na tutaiwekea katika mipango yetu kwa ajili ya utafutaji wa fedha ya ukamilishaji wa nyumba hizi.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa majibu lakini pia na swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Jimbo la Busega wamejenga maboma ya madarasa 69 na nyumba za walimu 11. Je, Serikali sasa iko tayari kupelekea fedha kwa ajili ya kumalizia maboma ya wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala hili la maboma kama nilivyotoka kusema hapa awali, tayari kuna timu kutoka Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa maelekezo yake Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Angellah Kairuki ambayo inafanya tathmini kujua maboma ya nyumba za walimu lakini vilevile maboma ya madarasa, pale tutakapopata idadi kamili kutoka kwenye Halmashauri hizi ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Busega tukaa na kutafuta fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma haya. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shule ya Msingi Mshizii, Mategho na Mavului zina hali mbaya sana. Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kupeleka pesa kwa ajili ya ukarabati wa shule hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kumuelekeza Afisa Elimu wa Mkoa wa Tanga kufika katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto na kufanya tathmini katika shule ambayo ameitaja Mheshimiwa Shekilindi na tathmini hiyo ikikamilika basi wawasilishe Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kuona namna gani tunatafuta fedha katika mwaka wa fedha unaofuata kwa ajili ya ujenzi wa maboma hayo katika shule hiyo.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shule ya Sekondari Mpandapanda katika Wilaya ya Rungwe, Kata ya Kiwila ina wanafunzi wengi sana lakini ina idadi ndogo sana ya matundu ya vyoo. Ni lini Serikali itaongeza nguvu kuweza kujenga vyoo kwa ajili ya kuweza kuwasaidia wanafunzi hao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la matundu ya vyoo katika shule hii ya Mpandapanda Wilayani Rungwe, ni Mkurugenzi wa Halmashauri sasa nae aweze kuangalia katika mapato yake ya ndani, atenge fedha kwa ajili ya kujenga matundu ya vyoo katika shule hii ambayo ina upungufu wa matundu hayo ya vyoo. Vilevile tutakaa na Mheshimiwa Mbunge tuweze kupata taarifa zaidi ya shule hii nakuona namna gani Serikali Kuu inaweza ikachangia.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaishukuru sana Serikali kwa kuendelea kujenga vituo vya afya na vingine vile zamani kukarabatiwa lakini ningependa kujua ni lini Serikali sasa itapeleka vifaatiba vya kutosha katika Vituo vya Afya vya Hedaru, Kisiwani, Makanya, Ruvu na Shengena?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; zahanati nyingi katika Jimbo la Same Magharibi hususan katika Tarafa ya Mwembembaga, Chemesuji na Same, zahanati zimekamilika lakini hazina watumishi. Je, ni lini Serikali sasa itapeleka watumishi wa kutosha na waganga katika zahanati hizo ili wananchi waweze kupata huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Dkt. David Mathayo David.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhusu upatikanaji wa vifaatiba katika Jimbo la Same Magharibi. Niseme tu kwamba Serikali tayari imetenga shilingi milioni 300 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba katika vituo vya afya vilivyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Same. Vilevile, shilingi milioni 100 kwa ajili ya zahanati zilizokuwepo katika Halmashauri ya Wilaya ya Same katika Mwaka wa Fedha wa 2023/2024. Hivyo nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge kwamba pale ambapo tutaanza utekelezaji wa bajeti mpya kwenye mwaka wa fedha unaokuja, tutaweka kipaumbele hizi fedha ziweze kwenda haraka kwa ajili ya ununuzi wa vifaa hivi tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili la zahanati hizi kukosa watumishi kule Halmashauri ya Wilaya ya Same. Serikali imeajiri watumishi wa afya zaidi ya 8,070 katika mwaka huu wa fedha ambao tupo na tunaenda kuumalizia. Tutaangalia ni wangapi ambao wamepangiwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Same ili zahanati hizi nazo Mkurugenzi nae aweze kufanya allocation ya hawa watumishi wapya watakaokwenda kwenye zahanati alizozitaja Mheshimiwa Mathayo.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Tunaishukuru Serikali kwa kujenga vituo vya afya katika Mkoa wa Manyara. Je, ni lini sasa Serikali itapeleka wataalam wa kutosha pamoja na vifaatiba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ni commitment ya Serikali hii ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha kwamba ina wataalam wa kutosha wa afya, ndiyo maana hivi karibuni Serikali ilitoa ajira 8,070 kwa wataalamu wa afya kote nchini na Mkoa wa Manyara nao wamepata mgao wao wa wataalam hawa wa afya.
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri lakini wananchi wa Longido wana hamu sana na shule hii, hadi sasa wako tayari kujitolea kwa nguvu kazi zao wenyewe ili basi kuendeleza shule hii. Je, Serikali haioni haja kuwapa kipaumbele wananchi hawa ambao wako site tayari? (Makofi)

Swali la pili, kwa kuwa Serikali ya CCM ina malengo mema ya kuzalisha wahitimu mahiri wa masomo ya sayansi na wananchi wa Kata ya Kikatiti katika Wilaya ya Meru wamejitolea ujenzi wa maabara katika Shule ya Ngyeku Sekondari. Je, Serikali itawasaidiia wananchi hawa kumaliza maabara hii lini? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zaytun Swai.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze yeye mwenyewe Mheshimiwa Mbunge kwa maana amekuwa mstari wa mbele katika ufuatiliaji wa fedha hizi kuweza kupelekwa katika Mkoa wa Arusha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza, Serikali kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi ilianza na phase one ya shule 10 za mwanzo ambapo bilioni 30 zilitumika, kwa sasa katika mwaka huu wa fedha ambao tupo 2022/2023 tunaenda kwenye phase two ambapo disbursement ya shule tisa, fedha za shule tisa, itafanyika muda si mrefu ikiwemo ya Shule ya Arusha ambayo wao wenyewe wamepanga kuijenga kule Longido.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili, kama nilivyosema hapo awali kwenye majibu mengine, Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI, inafanya tathmini kwa ajili ya maboma haya yakiwemo haya ambayo yapo kule kwenye Kata ya Kikatiti katika Shule hii ya Ngyeku kwa ajili ya kuona ni uhitaji wa fedha kiasi gani ambao tunao ili baadaye tuweze kukaa na wenzetu wa Wizara ya Fedha na kuomba fedha hizi kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma haya.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Kwa kuwa, barabara ile ni ya changarawe na magari yenye uzito mkubwa ndiyo yanapita kuelekea kule kwenye matanki ya mafuta yanapojengwa na gharama ya kurudishia changarawe imekuwa ni kila baada ya miezi miwili ambayo inapelekea maintenance cost kuwa kubwa. Je, hamuoni haja kuishauri EACOP barabara ile ijengwe kwa kiwango cha lami kupunguza maintenance cost na kuweza kutumika baada ya mradi kukamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Engineer Ulenge, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi kwamba barabara hii tayari baada ya utiwaji saini wa mkataba wa bomba la mafuta la Hoima tayari imehama kutoka TARURA na sasa inawahudumiwa na wao wenyewe EACOP. Tayari wameshaingia mkataba na mkandarasi wa kwao ambaye ataihudumia mpaka pale mradi huu utakapokamilika. Tunapokea ushauri wa Mheshimiwa Mbunge na tutaufanyia kazi kupitia wenzetu wa TARURA, kuweza kukaa na wenzetu wale wa EACOP kuona ni namna gani wanaweza kuanza walau taratibu kui - upgrade barabara hii lakini haya yote yanategemeana na uwepo wa fedha.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza naishukuru sana Serikali kwa fedha ambazo zimewekwa kwa ajili ya barabara ya Mogitu – Dawar – Ziwa Chumvi, lakini pia kwa shilingi milioni 53 ambayo imetengwa kwa ajili ya Dawar – Endasak. Pamoja na pongezi hizo, nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza maeneo ya Mara – Getaqul ambayo iko Kata ya Measkron, na Merekwa – Gauror ambayo iko Kata ya Dirima na Sosomega ambayo iko Kata ya Hirbadaw kipindi cha mvua huwa yanakuwa kama yako kisiwani.

Je, Serikali ina mkakati gani wa haraka kufikisha mkono wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan maeneo hayo ili nao waweze kufurahia maisha kwenye eneo hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; tuna changamoto kubwa ya daraja kule Sirop. Serikali imeshatenga fedha shilingi milioni 568; je, ni lini ujenzi wa daraja hilo utaanza ili wananchi waachane na adha ya daraja hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hhayuma. Swali lake la kwanza hili la Kata ya Dirima aliyotaja na vijiji ambapo barabara hizi zipo katika kata ambayo mvua ikinyesha wanakuwa wako kisiwani, naomba nichukue nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kumwelekeza Meneja wa TARURA wa Wilaya ya Hanang’ kwenda kufanya tathmini ya barabara hii na kisha kuiwasilisha Makao Makuu ya TARURA ili kuona ni namna gani tunaweza tukai-accommodate katika bajeti zifuatazo kuitengeneza barabara hii ili wananchi hawa wasiwe kisiwani kipindi cha mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Hhayuma kwa sababu amekuwa akifuatilia sana upatikanaji wa fedha wa daraja hili ambalo linaenda kujengwa kwa Shilingi milioni 568 ambalo amelitaja yeye mwenyewe, nimhakikishie kwamba mara tu tutapoanza mwaka wa fedha wa 2023/2024 ujenzi huu utaanza kwa kutangaza kazi hii ili apatikane kandarasi kwa ajili ya kujenga daraja hili.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi. Mheshimiwa Naibu Waziri, barabara ya kutoka Korongo kwenda Utinta imekuwa na changamoto kubwa sana na kuleta hatari kwa wanafunzi: Ni lini mtawaongezea fedha TARURA ili waweze kujenga kipande hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, Serikali imeongezea fedha TARURA ukilinganisha mwaka wa fedha 2020/2021 na 2021/2022, 2022/2023 na hata 2023/2024 tunayoenda kutekeleza, TARURA wameongezewa zaidi ya mara tatu ya bajeti ambayo ilikuwepo hapo awali. Kwa hiyo, ni kukaa na Meneja wa TARURA wa Mkoa kuangalia ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya kukarabati vile vile eneo la Wilaya ya Nkasi anakotoka Mheshimiwa Khenani ambapo wanafunzi wanavuka kama ambavyo amesema Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba vile vile Meneja wa Wilaya ya Nkasi awasilane na Mheshimiwa Khenani ili kuona ni namna gani wanaweza wakaanza ukarabati wa barabara hii.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu DC Barabara ya Mgombe – Kagerankanda mpaka Mvinza ni barabara ya kiuchumi na hupitisha malori makubwa kwenda kuchukua chokaa kupeleka nchi jirani ya Burundi; je, ni lini Serikali itajenga barabara hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ambayo ameiulizia Mheshimiwa Genzabuke kwenye swali lake la nyongeza, ni barabara ambayo inaambaa ambaa pembezoni mwa Mto Malagarasi. Kule wanaenda kufuata clinker ambayo inatengenezea madini ya ujenzi (cement). Kwa hiyo, tunaiona changamoto hii iliyopo kwa sababu mwanzo wakati barabara hii inahudumiwa na TARURA kulikuwa bado hakuna malori mengi yanayopita yenye uzito mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa kwa sababu malori tayari ni mengi sana, tutakaa na wenzetu wa TANROADS kuona ni namna gani ambapo wao wenyewe wataanza kwanza kule Kasulu kuona ni namna gani wanapandisha hadhi barabara hii kuwa barabara ya TANROADS ili iweze kuhudumiwa kwa ubora zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwongezee tu Mheshimiwa Mbunge kwamba hata Mamlaka ya Bandari Tanzania nayo ilikuwa inaangalia uwezekano wa kupanua mto ule ili zile barge kubwa ziweze kuwa zinapita kuchukua ile clinker badala ya kupitisha kwenye barabara zile.
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniruhusu niulize swali la nyongeza. Kwa sababu ya wingi wa mvua zinazonyesha katika Jiji la Dar es Salaam, barabara nyingi zilizo chini ya TARURA katika Jimbo la Kawe zimekatika vipande vipande.

Ni nini mpango wa Serikali ku-repair barabara hizi ili wananchi waweze kupita na kuondoa usumbufu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gwajima la barabara za Dar es Salaam kukatikakatika kwa sababu ya mvua, tunaenda kuanza kutekeleza Bajeti ya mwaka 2023/2024 kwa Wakala wa barabara ikiwemo Dar es Salaam. Mheshimiwa Mbunge naye ni shahidi kwamba hivi karibuni wamesaini mkataba kwa ajili ya uanzishwaji wa mradi wa DMDP II ambao utakwenda kuwa mwarobaini wa barabara hizi mbovu za Jiji la Dar es Salaam kwa kujenga mifereji na kuhakikisha barabara pia zinapitika wakati wote.
MHE. VINCENT P. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Vijiji vya Lusembwa, Ng’undwe, Mlambo, Minza na Ifinga vinashindwa kupata huduma ya maji, miradi ya maji, mawasiliano pamoja na minara ya simu.

Je, ni lini Serikali itajenga barabara katika hivi vijiji ambavyo viko Kata ya Wampembe? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kata ya Wampembe na Kata ya Kala kuna vilima ambavyo ni korofi, vinasababisha magari ya abiria kutopita; je, ni lini Serikali itajenga kwa zege katika vilima hivi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbogo, la kwanza, hii barabara ya Ng’undwe – Mlambo – Lusembwa – Mvinza na Ifinga vilivyokuwepo kwenye Kata hii ya Wampembe, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, barabara hizi zilikuwa bado hazijafunguliwa na kuingizwa kwenye mtandao wa TARURA. Hivyo basi, muda siyo mrefu Meneja wa TARURA Wilaya ya Nkasi atapita kufanya tathmini ya barabara hizi na kuona ni kiasi gani kinatakiwa kutengwa ili barabara hizi ziweze kuchongwa na greda, na kadiri miaka inavyoenda na fedha kuruhusu basi nazo ziweze kuanza kuwekewa changarawe ili wananchi waweze kupita wakati wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili kuhusu barabara inayounganisha Kala na Wampembe, kwamba ina vilima vingi, nichukue nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kumwelekeza Meneja wa TARURA Nkasi, kuweza kufika katika barabara hii ya Kala na Wampembe na kuanza tathmini, na kuona ni kiasi gani kinahitajika kwa ajili ya kuweka zege katika vilima hivi ili barabara hizi ziweze kuwa zinapitika wakati wote wa mvua na hata kipindi ambacho hakuna mvua.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Barabara ya kutoka pale Nyasho kupitia Mwanangi – Badugu kwenda Busami imekuwa ikiharibika mara kwa mara na ni ya muhimu sana katika uchumi wa Jimbo la Busega: Je, lini Serikali iko tayari kujenga barabara hii kwa kiwango cha changarawe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la Mheshimiwa Songe la barabara zake kule Jimboni Busega, wote ni mashahidi kwamba TARURA sasa imeongezewa fedha mara tatu na Mheshimiwa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan tangu aingie madarakani, na bajeti ile imebaki pale pale katika kiwango cha juu cha zaidi ya Shilingi bilioni 776 ambayo Bunge hili lilipitisha. Hivyo basi, niwatoe hofu Wabunge wengi kwamba sasa tunakwenda kufungua barabara nyingi zaidi za mijini na vijijini na vile vile kukarabati barabara nyingi zaidi zikiwemo za kule kwa Mheshimiwa Songe Wilayani Busega.

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Barabara ya kutoka Liweta mpaka Mpopoma ni barabara ambayo ni muhimu sana kiasi kwamba inatenga hicho kijiji kuwa katika mawasiliano na Wilaya ya Nyasa ambayo ndiyo wilaya yake.

Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kipekee kuisaidia barabara hii ambayo pia ina milima kama ilivyo barabara ya Wampembe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la Mheshimiwa Eng. Stella Martin Manyanya la barabara hii ambayo inapita Liweta – Mpopoma kule Wilayani Nyasa, nayo vilevile nichukue nafasi hii kumwelekeza Meneja wa TARURA wa Wilaya ya Nyasa kwenda kwenye barabara hii aliyoitaja Mheshimiwa Engineer Manyanya na kuifanyia tathmini na kuona ni kiasi gani kitahitajika kwa ajili ya kuweza kujenga ili tuweze kutengea fedha katika miaka ya fedha ambayo inafuata.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, ujenzi wa barabara za lami kilometa tatu kwenye Mji wa Mombo ni ahadi ya Serikali iliyotolewa na Mgombea wa Urais wa Chama cha Mapinduzi mwaka 2015 na ikarejewa mwaka 2022. Kazi inayoendelea haiathiri ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami, nataka kujua, ni lini ahadi hii ya Serikali kwenye Mji wa Mombo itatekelezwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Wilaya ya Korogwe ni eneo muhimu sana kwenye uzalishaji wa mazao ya kilimo, kilimo cha mkonge lakini Tarafa ya Bundi kilimo cha chai: Ni lini Serikali itaiingiza Wilaya ya Korogwe kwenye mradi ule mahususi wa miundombinu kwenye maeneo ya uzalishaji na maeneo ya kilimo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Timotheo Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini, la kwanza hili kwamba barabara hii ya lami ni ahadi ya Serikali, nikiri kwamba ni ahadi ya Serikali na kwamba tutaendelea kuipa kipaumbele kwa sababu iliahidiwa na Kiongozi Mkuu wa Nchi alipopita katika eneo la Mombo. Tutaendelea kutafuta fedha na tutaona ni namna gani katika mwaka wa fedha huu tunaoenda kuuanza ni nini kinaweza kikafanyika na Serikali kuweza kuendelea kutekeleza ahadi hii ya viongozi wakuu wa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili kwamba kule kuna uzalishaji mkubwa kuingiza katika miradi mbalimbali mingine, nimtoe mashaka, Korogwe vijijini ipo katika mradi ule wa bottleneck removal ambao unakwenda kujenga madaraja na vivuko mbalimbali katika maeneo tofauti hapa nchini, ikiwemo kule kwake Mheshimiwa Mnzava, Korogwe Vijijini. Najua alichokuwa anataka ni kwamba Mkoa wa Tanga wawekwe katika Mradi wa Agri-connect, lakini mradi huu wa Agri-connect upo katika Southern Highlands, mikoa yetu ya nyanda za juu kusini tu, na wao Korogwe wapo katika hii bottleneck removal kwa vijijini; kwa Korogwe Mjini, kwa Dkt. Kimea kule, wamo katika TACTIC na Tanga Mjini vile vile wapo katika TACTIC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kufanya ukarabati na matengenezo ya barabara mbalimbali kule Korogwe Vijijini.
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nami ninalo swali linalofanana na Korogwe. Pale Mji wa Nguruka Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano aliwaahidi kilometa tano za lami, lakini mpaka sasa zimejengwa mita 250 tu. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kujenga barabara za lami pale Nguruka? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nashon kwenye hii barabara ya Nguruka ambayo ni ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tutakaa kupitia ahadi zote za Viongozi Wakuu, kupitia wakala wetu wa TARURA na kuona ni namna gani tunaweza tukakaa na wenzetu wa Wizara ya Fedha kwa ajili ya kuona tunapataje fedha ya kuanza kutengeneza taratibu kutenga ili kila mwaka angalau kwenye ahadi hizi tuweze kuwa tunapunguza kilometa hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge, kwamba tunalifanyia kazi chini ya Waziri wetu Mheshimiwa Angellah Kairuki, kuhakikisha kwamba tunajua ahadi zote na kuziratibu na kuhakikisha barabara hizi zinajengwa kwa wakati.
MHE. JAPEHT N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Barabara ya Vwawa – London – Iganduka hadi Msiya hivi sasa haipitiki kabisa; Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba barabara hiyo inawekwa lami ili iweze kupitika wakati wote?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la Mheshimiwa Hasunga la Barabara zake hizi za Vwawa kuwekewa lami. Nitakaa naye Mheshimiwa Hasunga kuona ni kiasi gani kimetengwa katika mwaka wa fedha 2023/2024 katika jimbo lake kule ili tuweze kuhakikisha kwamba upatikanaji wa fedha huu unakuwa wa haraka na hizi ziweze kuanza kujengwa mara moja na kama hazijatengewa fedha basi tutahakikisha na Mheshimiwa Hasunga tutakaa naye kuona zinatengewa fedha katika mwaka wa fedha wa 2024/2025.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, je lini Serikali itajenga Barabara ya Mikumi, Kisanga, Maroro kwa kiwango wa changarawe? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itajenga Barabara hii ya Mikumi, Kisanga kama ambavyo ameuliza Dkt. Ishengoma kadiri ya upatikanaji wa fedha na tutaangalia katika mwaka wa fedha huu unaoanza, ambapo TARURA vile Bunge hili lilipitishia bajeti kubwa ya kuweza kutekeleza barabara hizi kuona kama imetengewa fedha na kama haijatengewa fedha tutaangalia katika mwaka wa fedha unaofuata ili barabara hii iweze kutengewa fedha.
MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante je, lini Serikali itatekeleza ahadi ya kilometa 10 katika Mji wa Karatu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakaa naye Mheshimiwa Mbunge kwa sababu bado sijaelewa ahadi hii ilikuwa iko vipi. Nitakaa naye Mheshimiwa Mbunge ili aweze kunielewesha vizuri ahadi hii ya kilometa 10 ilikuwa ni ahadi ipi na tuweze kujua kama ni ya TANROADS au ni ya kwetu halafu tuone ni namna gani tunaweza tukapata fedha ya kuanza kutekeleza walau kwa kilometa moja moja ili iweze kukamilika kule Karatu.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa niaba ya Mheshimiwa Masache nashukuru sana Serikali kwa majibu mazuri na tunaamini wananchi wa Lupa kwenye mgawanyo wa magari watapata. Naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza lini Serikali itapeleka fedha za kumalizia ujenzi wa kituo cha afya Masamakati na Mkwansira?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili wananchi wa Kata ya Rom pamoja na ufinyu wa maeneo wamehangaika sana wamepata eneo la kujenga kituo cha afya pale Rowsinde. Je, lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kujenga kituo cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kasaka yaliyoulizwa kwa niaba yake na Mheshimiwa Mbunge wa Hai rafiki yangu Saashisha Elinikyo Mafuwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza la lini Masamakati itapelekewa fedha? Naomba nijibu haya maswali mawili kwa pamoja hili la kwanza na la pili. La kwanza ni kuwataka wao Halmashauri ya Wilaya ya Hai kuanza kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo hivi vya afya vya Rowsinde na hichi ambacho cha Masamakati. Pale watakapokuwa wanakwenda na kukitengea fedha katika bajeti zao ndipo napo Serikali wakati tunatafuta fedha ya kuendelea kujenga vituo vya afya, tunaona ni namna gani tutakuja kuongeza nguvu za halmashauri walikofikia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii ya awamu ya sita ya mama Samia Suluhu Hassan imejenga vituo vya afya 234 kote nchini kwa kutenga bilioni 116 na tayari vituo hivyo vingi vimeshakamilika na kuanza kazi. Sasa ni wajibu wa halmashauri hizi nazo ku-support jitihada hizi za Dkt. Samia Suluhu Hassan za kuweka fedha kwa ajili ya ujenzi huu kwa wao kuanza ujenzi wa vituo hivi vya afya. Naamini kule wenzetu wa Hai nao watakaa halmashauri na kuweka fedha kwa ajili ya kuanza kupeleka huduma ya wananchi huku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii vilevile kumwelekeza Mganda Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro kwenda kufanya tathmini katika maeneo haya aliyoyataja Mheshimiwa Saashisha na kuona idadi ya wananchi waliokuwepo pale, uhitaji uliopo kwa ajili ya kupata vituo hivi vya afya na kuwasilisha taarifa ile Ofisi ya Rais TAMISEMI.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipa mimi ruhusa ya kuuliza swali la mwisho la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Chitage na Kata ya Usagari Mbunge kwa kushirikiana na wananchi tunajenga vituo vya afya.

Je, Serikali ina mpango gani wa kutusaidia kumalizia vituo hivyo vya Chitage na Usagari Mikungumalo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Almas Maige yeye pamoja na wananchi wake kuweza kujitoa kuanza ujenzi wa vituo hivi vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba vilevile nimtake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tabora kufika katika vituo hivi vya afya ambavyo vimeanza kujengwa kwa nguvu ya wananchi na kufanya tathmini na kuona vile vigezo ambavyo vinahitajika kwa ajili ya kusajili kituo cha afya kama wanakidhi hawa wananchi wa Mheshimiwa Maige na wawasilishe taarifa hiyo Ofisi ya Rais TAMISEMI ili tuviweke katika mipango yetu ya utafutaji wa fedha katika Ofisi ya Rais-TAMISEMI.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona, wananchi wa Mji wa Mafinga walishaanza kujenga Kituo cha Afya cha Upendo na kwa nguvu zao wenyewe.

Ni lini Serikali itapeleka nguvu za ujenzi katika kituo hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itapeleka fedha katika Kituo hicho cha Afya Upendo ku-support nguvu za wananchi kadiri ya upatikanaji wa fedha. Vilevile nao wana uwezo wa kuanza kutenga bajeti kwa ajili ya ku-support jitihada hizi za wananchi hawa.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi. Je, lini Serikali itapeleka fedha za kutosha kumalizia Kituo cha Afya cha Makuro Jimbo la Singida Kaskazini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itapeleka fedha za kumalizia Kituo cha Afya Makuro kadiri ya upatikanaji wa fedha na tutakaa na Mheshimiwa Mbunge kuona kama kimetengewa fedha katika mwaka wa fedha ujao.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Je, lini Serikali itajenga vituo vya afya kwenye Kata za Rwamgasa, Nyakagomba na Magenge tulizoziomba mwaka 2021?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itajenga vituo vya afya hivi alivyovitaja Mheshimiwa Magessa kadiri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu wa barabara na kwa kuwa nyumba zilizo mbele ya Barabara hii, viwanja vyake vilipimwa na mamlaka ya upangaji.

Je, Serikali ina mpango gani wa kufidia walau mita sita ili wananchi wa eneo hili wapate Barabara ya uhakika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili nini hatma ya barabara ya Mabwawa ya Samaki na Mlima habarizenu iliyopo katika Kata ya Mianzini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abdallah Chaurembo. La kwanza hili la kipande cha mita 400 kilichosalia katika barabara hii ya Zakhiem.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara hii kwa kumbukumbu zangu ni barabara ambayo inaunganika na maandazi road ambayo barabara hii ya Maandazi Road imewekwa katika mpango wa DMDP II. Sasa kwa sababu ni mita chache kutoka pale tutakaa na wenzetu wa Manispaa ya Temeke na vilevile tutakaa na wenzetu wa TARURA Mkoa wa Dar es Salaam kuona ni namna gani tunaweza tukachepusha barabara hizi mita 200 kwa kuona kama tunaweza kuingiza katika mpango wa kulipa fidia. Halmashauri wenyewe baada ya kufanya tathmini walipe fidia kwa ajili ya kuchepusha barabara hii ili iweze nayo kuingizwa katika mipango ya kuwekewa lami au zege ili wananchi hawa waweze kupata huduma sahihi wanayostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili, barabara hii aliyoitaja ya Bwawa la Samaki hadi Kilima cha Habaribzenu. Naomba nitumie nafasi hii kumwelekeza Meneja wa TARURA wa Halmashauri ya Wilaya ya Temeke kufika katika barabara hii na kuweza kufanya tathmini na kuona ni namna gani inaweza ikatengewa fedha ya kuweza kutengeneza ili iweze kupitika wakati wote.
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali moja la nyongeza. Mvua za masika zimekuwa ni ndefu sana kwenye Mkoa wa Dar es Salaam na miundombinu mingi ya barabara imeharibika. Tarehe 30 Mei Mheshimiwa Naibu Waziri aliniahidi kwamba Barabara ya Banana-Kitunda-Kivule - Msongola itapitika na hali bado ni mbaya ikiwemo Barabara ya kwa Diwani – Bomba mbili. Nini kauli ya Serikali kuhusiana na miundombinu hii ya Jimbo la Ukonga ambayo ina hali mbaya kwa sasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jerry William Silaa naomba nitumie nafasi hii kumwelekeza Meneja wa TARURA Mkoa wa Dar es Salaam aweze kutembelea barabara hizi ambazo amezitaja Mheshimiwa Jerry William Silaa na kufanya tathmini ya haraka na pale tunapoanza utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024 kuzipa kipaumbele barabara hizi kwa ajili ya kuzitengeneza.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana swali langu ni dogo tu kusiana kama lililokuwa Mbagala. Iko barabara inayopita ndani ya Jimbo la Temeke, sawa sawa na sambamba na Reli ya TAZARA ambayo nayo katika mvua hizi imeharibika sana.

Je, Serikali mtatusaidiaje changamoto ya TAZARA pamoja na Manispaa yetu ili waturuhusu hata kuitengeneza tu kwa changarawe au hata kuweka lami kidogo kwa sababu ni Barabara ambayo inatumika sana kwa wananchi wa Temeke.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii alimradi inapita kandokando mwa reli kuna sheria ambazo zinalinda ile mipaka ya reli inakopita. Hivyo tutakaa na wenzetu wa TAZARA kuona ni namna gani wataruhusu ipitike kwa muda kwa sababu haitoweza kutengenezewa miundombinu kama ya zege na lami kwa muda ili kuweza kutoa huduma kwa wananchi na TAZARA wakiridhia basi tutaona ni namna gani Meneja wa TARURA Mkoa wa Dar es Salaam anaweza akatengea fedha kwa ajili ya kuweza kuweka changarawe.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafsi niulize swali la nyongeza. Je, lini Serikali italeta fedha kwa ajili ya ujenzi wa Barabara ya Ilula, Ibumu ili ijengwe japo kwa kiwango cha changarawe tu na madaraja manne ili wananchi waweze kupita, manake sasa hivi wanapata mateso makubwa sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakaa na Mheshimiwa Kabati kuona kama barabara hii ya Ilula - Igumu imewekwa katika mradi wa Agri-connect ambao wao Iringa ni wanufaika wa mradi huu. Kama haijawekwa basi kuona ni namna gani bajeti ya TARURA ya Wilaya ya Kilolo inaweza ika-accommodate barabara hii katika mwaka wa fedha unaofuata na kama sio mwaka wa fedha unaofuata basi ule wa 2024/2025.

MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana swali langu ni dogo tu kusiana kama lililokuwa Mbagala. Iko barabara inayopita ndani ya Jimbo la Temeke, sawa sawa na sambamba na Reli ya TAZARA ambayo nayo katika mvua hizi imeharibika sana.

Je, Serikali mtatusaidiaje changamoto ya TAZARA pamoja na Manispaa yetu ili waturuhusu hata kuitengeneza tu kwa changarawe au hata kuweka lami kidogo kwa sababu ni Barabara ambayo inatumika sana kwa wananchi wa Temeke.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii alimradi inapita kandokando mwa reli kuna sheria ambazo zinalinda ile mipaka ya reli inakopita. Hivyo tutakaa na wenzetu wa TAZARA kuona ni namna gani wataruhusu ipitike kwa muda kwa sababu haitoweza kutengenezewa miundombinu kama ya zege na lami kwa muda ili kuweza kutoa huduma kwa wananchi na TAZARA wakiridhia basi tutaona ni namna gani Meneja wa TARURA Mkoa wa Dar es Salaam anaweza akatengea fedha kwa ajili ya kuweza kuweka changarawe.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafsi niulize swali la nyongeza. Je, lini Serikali italeta fedha kwa ajili ya ujenzi wa Barabara ya Ilula, Ibumu ili ijengwe japo kwa kiwango cha changarawe tu na madaraja manne ili wananchi waweze kupita, manake sasa hivi wanapata mateso makubwa sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakaa na Mheshimiwa Kabati kuona kama barabara hii ya Ilula - Igumu imewekwa katika mradi wa Agri-connect ambao wao Iringa ni wanufaika wa mradi huu. Kama haijawekwa basi kuona ni namna gani bajeti ya TARURA ya Wilaya ya Kilolo inaweza ika-accommodate barabara hii katika mwaka wa fedha unaofuata na kama sio mwaka wa fedha unaofuata basi ule wa 2024/2025.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwanza niishukuru Serikali kwa kutoa watumishi hao 68. Lakini sasa kutokana na ongezeko hili kubwa la ujenzi wa vituo vya afya, ambapo tuna vituo viwili tayari vimekamilika, Kituo Cha Afya cha Mkumbi na Kituo cha Afya Matili, pamoja na ongezeko hili havijapata watumishi;

Je, ni nini kauli ya Serikali?

Mheshimiwa Spika, kutokana na upungufu uliopo Serikali iko tayari kuipa kipaumbele halmashauri ya Wilaya ya Mbinga kutokana na upungufu Mkubwa uliopo wa watumishi?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nijibu maswali mawili ya myongeza ya Mheshimiwa Benaya Kapinga. Kwanza hili la vituo viwili vya afya ambavyo vimejengwa na havijapata watumishi, naomba nitumie Bunge lako Tukufu kumwelekeza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma kuweza kufika katika vituo hivi viwili vya afya ambavyo amevitaja Mheshimiwa Kapinga na kufanya tathimini yake na kuona ni namna gani ambavyo tunaweza tukafanya msawazo wa watumishi ndani ya Mkoa wa Ruvuma walau kuanza kupeleka watumishi wachache ili waanze kutoa huduma kwa wananchi wa maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la pili, Serikali itaweka kipaumbele cha kupeleka watumishi kwenye maeneo yenye upungufu mkubwa ikiwemo kule Mbinga Vijijini kwa Mheshimiwa Kapinga. Na Kadri tutakavyoendelea kluajiri basi tutaweka kipanumbele kwenye maeneo hayo.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante. Jimbo la Mbulu vijijini tumepata vituo vya Afya vitatu na tuna upungufu wa watumishi. Je, ni lini mnatuletea watumishi hao?

NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) Mheshimiwa Spika, nijibu swali la Mheshimiwa Massay, hivi sasa Serikali imetoka kuajiri watumishi 8070 wa kada ya afya nchini kote katika mwaka huu wa fedha 2022/2023. Pia tumeweka kipaumbele katika maeneo yenye upungufu ikiwemo kule Jimboni Mbulu Vijijini. Hivyo, basi ni wajibu wao na Mkurugenzi kuhakikisha kwamba hawa watumishi watakaopelekwa katika halmashauri yao wapangiwe kwenye maeneo ambayo yana upungufu zaidi.

MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa sisi Namtumbo tuna vituo viwili vya afya ambavyo vimejengwa na viko mwishoni kabisa kukamilika;

Je, Serikali haioni iko haja sasa ya kuanza kutuletea vifaa tiba na watunishi ili iweze kuanza na majengo yale yasikae muda mrefu?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) Mheshimiwa Spika, kama nilivyomjibu Mheshimiwa Kapinga kwa kumwelekeza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, anapotembelea kule Mbinga vijijini basi afike kule Namtumbo kwa Mheshimiwa Vita Kawawa ili kufanya tathimini kwenye vituo hivi vya afya ambavyo amevitaja Mheshimiwa Kawawa na kuona ni namna gani Serikali inaweza ikapaleka watumishi pale. Vile vile katika mwaka huu wa fedha tunaouanza wa 2023/2024 kuna fedha iliyotengwa kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kote nchini. Hivyo basi, tutaona ni namna gani vituo hivyo vya Namtumbo vinapata.

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Hospitali ya Mji wa Mafinga kutokana na sababu za kijiografia inahudumia zaidi ya halmashauri tano. Je, Serikali iko tayari kutufanyia upendeleo wa kipekee?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema awali kwamba Serikali imeajiri watumishi 8,070 wa kada ya afya kote nchini na muda sio mrefu wametoka kuchukua barua zao katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI na kuweza kuripoti katika maeneo ya kazi waliyopangiwa ikiwemo Halmashauri ya Mji wa Mafinga. Hivyo basi, ni imani yangu kuwa halmashauri hii imepata watumishi hawa wa kada ya afya. Ni wajibu wa Mkurugenzi kuwapangia kule kwenye upungufu ikiwemo katika hospitali ya wilaya.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Vituo vya Afya vya Mwang’aranga, Mwigumbi na Ukenyenge ni vituo ambavyo vina upungufu mkubwa sana wa watumishi;

Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba inapeleka watumishi kwenye vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, katika Vituo hivi vya Afya vya Mwang’aranga, Mwigumbi na hicho kingine alichokitaja Mheshimiwa Butondo, muda sio mrefu Serikali imetoka kuajiri watumishi wa kad ya afya, hivyo tutakwenda kuangalia na kuona ni wangapi wamepangiwa kwenda katika Halmashauri ya Shinyanga DC na kuweza kuona ni namna gani wanaweza wakapelekwa katika vituo vya afya alivyovitaja Mheshimiwa Butondo.

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Kwa kuwa posho ya Waheshimiwa Madiwani inayotumika hivi sasa ni shilingi 350,000 imekaa takribani miaka kumi sasa.

Je, Serikali haioni kuwa ni wakati muafaka wa kuongeza posho ya waheshimiwa Maadiwani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa halmashauri nyingi nchini zinapata mapato madogo, ikiwemo halmashauri ya Mbulu, na kushindwa kulipa posho ya wenyeviti wa vijiji na mitaa;

Je, Serikali haioni kuwa ndio wakati muafaka wa kutazama jambo hili ili kila halmashauri nchini zitekeleze takwa hili la kikanuni kwa mujibu wa huduma wanazotoa?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Issaay, kwanza kuhusu hili la posho kuwa zimekuwa ni za muda mrefu. Mwaka wa fedha 2021/2022 ambapo Serikali kuu ilichukua jukumu la kulipa posho hizi Madiwani moja kwa moja kutoka hazina, hivyo, kuwapunguzia mzigo mamlaka hizi za Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, baada ya kupunguza hilo, na kwa sababu ni jambo la kisheria na Mheshimiwa Issaay ni Mheshimiwa Diwani kwenye halmashauri yake ilitakiwa wakae ili zile fedha am,bazo wanafanya saving baada ya Serikali Kuu kuchukua la kulipa posho za Madiwani waone ni namna gani wanatenga kwa ajili ya wenyeviti wao wa vijiji na wenyeviti wao wa mitaa n.k.

Mheshimiwa Spika, pia, fedha nyingi zimekuwa zikipelekwa kutoka Serikali kuu. Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ameweka fedha nyingi kwenye miundombinu, afya na elimu. Hivyo, halmashauri nyingi zimepunguziwa ule mzigo mkubwa. Ni wajibu wao kutenga na kuhakikisha wanalipa kama inavyosema Sheria ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, nikimalizia kujibu swali lake la kwanza la nyongeza, mwaka huu wa fedha tunaokwenda kuuanza wa 2023/2024 Serikali Kuu vile vile, imewapunguzia mzigo halmashauri zote nchini kwa kuanza kulipa zile stahiki za wakuu wa idara, na zitaanza kulipwa moja kwa moja na Serikali kuu. Hivyo, kuwaacha halmasahuri kuwa na uwezo wa mapato zaidi na kuweza kutenga fedha za kulipa wenyeviti hawa na madiwani vile vile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, linalohusu mapato kuwa madogo. Halmashauri huanzishwa kwa mujibu wa sheria; na moja ya kigezo kikubwa cha uanzishwaji wa halmashauri au mamlaka za Serikali za mitaa ni uwezo wake wa kukusanya mapato. Vile vile, huwa wanaainisha vyanzo zaidi ya 30. Na kwa mujibu wa Sheria ile Na. 287 ya Mamlaka za Wilaya, 288 Mamlaka za Miji inaelezea wazi. Vile vile, Sheria ile ya Fedha ya Mamlaka za Serikali za Mitaa Kifungu cha (6) (7) (8) na (9) inaelezea wazi namna ambavyo wanatakiwa kubanana kuweka mapato yao sawa.

Mheshimiwa Spika, ukisema kila kitu kichukulliwe na Serikali Kuu ina maana dhana nzima ya D by D inakuwa imeondoka.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, Ahsante. Nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Pamoja na majibu yake nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza. Katika Wilaya ya Buhigwe Kata ya Mkatanga, wananchi wa Kijiji cha Kitambuka waliomba kujengewa kituo cha afya na ombi hilo walilitoa mbele ya Makamau wa Rais Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, na tayari wanayo matofali.

Je, Serikali iko tayari kutoa pesa ili wananchi waweze kujengewa kituo hicho? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika Halmashauri ya Wilaya ya Kasulu DC, Kata ya Kagera Nkanda iko umbali mrefu sana kutoka yaliko Makao Mkauu ya Halmasahuri ya Kasulu DC, ambapo ni kilometa 77 kutoka Makao Makuu.

Je, Serikali iko tayari kujenga kituo cha afya katika Kata ya Kagera Nkanda?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nijibu maswali yote mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Genzabuke. Kuhusu Kata hizi za Mkatanga pamoja na Kagera Nkanda nichukue nafasi hii kumwelekeza Mgamga Mkuu wa Mkoa wa Kigoma kuweza kutembelea katika Kata hizi na Kufanya tathimini ili kuona kama vigezo vile vya kuwa na vituo vya afya vinatimia. Kama vigezo vile vinatimia basi Mganga Mkuu awasilishe taarifa il;e katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo hivi.

Mheshimiwa Spika, lakini Mheshimiwa Genzabuke amekuwa akifuatilia sana Kituo hiki cha Afya cha Kagera Nkanda muda mrefu na tutakaa nae kuona ni namna gani katika mwaka wa fedha ujao tunaweza tukatenga fedha.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa Mahongole wana kituo cha afya;

Je, ni lini Serikali itamalizia ujenzi wa kituo cha Afya Kata ya Mahongole?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itamalizia Kituo cha Afya cha Mahongore kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kituo cha Afya cha Ipogolo ni kati ya vituo vikongwe vya afya na vinahudumia zaidi ya wanawake 600 kwa mwezi lakini hakina combined ward.

Je, Serikali inaweza kutusaidia kutujengea combined ward katika kituo hiki ili kupunguza msongamano?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutatuma timu kwenda Halmasahuri ya Manispaa ya Iringa kwa ajili ya kufanya tathimini ya kituo hiki cha afya cha Ipogolo na kuona kama eneo linaruhusu kuweza kujenga maeneo haya ambayo Mheshimiwa Mbunge ameomba na kama inaruhusu tutaweka katika mipango yetu ya kutafuta fedha ili kuweza kujenga kituo hiki cha afya ambacho ni kongwe.
MHE TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza. Kwenye kata ya Salale Kijiji cha Nyamisati tuna shida kubwa sana ya kituo cha afya ukizingatia zahanati ya pale inahudumia wilaya mbili…

SPIKA: Mheshimiwa Twaha, uliza swali.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, je, lini Serikali mtatujengea kituo cha afya pale?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali ina vigezo vyake vya kuanza kujenga vituo vya afya. Hivyo, basi tutauma timu kwa ajili ya kwenda kule katika Kijiji cha Nyamiisati, kata ya Salale, Jimboni Kibiti kuweza kufanya tathimini na kuona kama vigezo vile vimefikiwa vya kuweza kujenga kituo hiki vya afya.

MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza;

Je, ni lini Serikali itajenga kituo cha Afya Kata ya Sawida wilaya ya Itilima?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itajenga kituo hicho cha afya baada ya kufanya tathimini ya kuona uhitaji ulioko pale lakini vile vile kadri ya upatikanaji wa fedha; na tutatenga katika bajeti za miaka ya fedha inayofuata.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante nami kwa nunipa swali la nyongeza. Kituo cha afya cha Misha katika kata 29 za Tabora kimekamilika lakini bado hakina vifaa vya Afya vya kutosha;

Je, ni lini serikali itapeleka vifaa hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakasaka kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya hiki Misha kipo pembezoni mwa Manispaa ya Tabora na tayari katika mwaka wa fedha 2022/2023 ambao tunaenda kuumaliza Serikali ilikuwa imetenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba katika kituo hiki cha afya, nitakaa na Mheshimiwa Mwakasaka ili tuweze kupitia hivi na kuona tunapeleka hivi vifaa tiba kwa haraka sana.
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya ya Mheshimiwa Rais ya kujenga Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Bunda katika Jimbo la Mwibara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Fedha na kuona, maana yake Ofisi ya Rais, TAMISEMI imefanya compilation ya ahadi zote za viongozi wetu Wakuu wa Nchi na kuziwasilisha Wizara ya Fedha na kuona namna gani tutapata fedha kwa ajili ya utekelezaji wa ahadi hizi. Hivyo basi, nimtoe mashaka Mheshimiwa Kajege kwamba baada ya kukaa na wenzetu wa Wizara ya Fedha na kuona ni namna gani Serikali itapata fedha hizi, tutaanza ujenzi huu wa Hospitali hii.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kituo cha Afya Mtina kilitengewa milioni 250 katika bajeti tunayoendelea nayo ili kujenga jengo la akinamama na watoto. Je, ni lini pesa hiyo itaenda?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nitakaa na Mheshimiwa Mpakate ili kuona katika mwaka wa fedha huu 2023/2024 tunaoenda kuanza kutekeleza kama Kituo hiki cha Afya cha Mtina kimetengewa fedha na kama hakijatengewa fedha, basi tutaangalia ni namna gani tunaweza tukakiweka katika mipango ya mwaka wa fedha 2024/2025.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi ya swali la nyongeza. Je, ni nini mpango wa Serikali wa kujenga kituo cha afya katika Kata ya Likawage, Jimbo la Kilwa Kusini, kata ambayo iko mbali kutoka sehemu ambayo huduma ya afya inapatikana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutatuma timu kwenda katika Kata ya Likawage kufanya tathmini na kuona kama vile vigezo vya idadi ya watu na kadhalika vimefikiwa eneo walilolitenga wao katika maeneo hayo na kama vigezo vile vimefikiwa, basi tutaweka katika mipango yetu ya kutafuta fedha.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nataka kujua tu, ni lini Serikali italeta vifaa tiba katika vituo vyetu vya afya na hospitali ya wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nitakaa na Mheshimiwa Sima kuweza kupitia katika fedha iliyokuwa imetengwa ya ununuzi wa vifaatiba kwa mwaka wa fedha 2022/2023, kuona Halmashauri ya Manispaa ya Singida imetengewa kiasi gani na kama ilikuwa haijatengewa tutaangalia katika mwaka wa fedha huu tunaoenda kuanza kuutekeleza wa 2023/2024 ili tuweze kuona namna gani fedha hiyo inaenda kwa haraka kupata vifaa tiba hivyo.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kuuliza swali moja dogo la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali toka robo ya tatu imesitisha kutoa mikopo hii ya asilimia 10 mpaka sasa na kwa kuwa akina mama wanahangaika na mikopo ya kausha damu huko mitaani; je, ni lini sasa Serikali inakwenda kuanza kutoa mikopo hii ya asilimia 10?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali ilisitisha utoaji wa mikopo hii ili kufanya tathmini na mapitio ya namna ambavyo mikopo hii inatolewa na hili lilikuwa ni agizo la Kamati ya Kudumu ya Bunge lako tukufu ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Hivi sasa timu ile imeshaundwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tayari wameanza kufanya kazi ya kufanya mapitio na vilevile ilikuwa ni malekezo yake Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha mapitio haya yanafanyika haraka ili fedha zile nyingi zisipotee pale mikopo inapotolewa. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, tayari tumeshatoa maelekezo kwa Wakuu wa Mikoa wote, Makatibu Tawala wa Mikoa na Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri. Kwa mujibu wa kifungu au Kanuni ya 24(2) ya kanuni za utoaji wa mikopo hii, tayari kila Halmashauri ina akaunti mahususi kabisa ya mikopo hii na tumewaelekeza hakuna kusimama katika kupeleka asilimia 10. Kwa hiyo hela zitapelekwa na pili utaratibu mpya utakapotangazwa, basi tutakuwa tuna hela tayari kwa ajili ya kupeleka kwenye huo utoaji wa mikopo.

Kwa hiyo, hawatakiwi kusimama, wanatakiwa kuendelea kuzitenga katika akaunti za mikopo. Kilichosimama tu ni ule utoaji kwenda katika vikundi vya wanufaika, nakushukuru.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Je, ni lini Serikali sasa itapeleka vifaranga bora vya mbuzi, kuku na ng’ombe ili kuboresha mikopo hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kuweza kuona ni namna gani tunapata mbegu bora kwa ajili ya kupeleka kwenye vikundi hivi ili waweze kufanya ufugaji ambao una tija na ambao utawaongezea kipato vilevile.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, Serikali itazingatia kuongeza umri wa vijana kutoka ile miaka ya awali 30 mpaka kufikia 45 kama tulivyopendekeza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, umri ule wa vijana uliowekwa pale ni kwa mujibu wa miongozo ya kimataifa ambayo inataja umri wa vijana ni upi. Kwa hiyo sisi tunaendana na convention zile za kimataifa na mikataba ya kimataifa. Kwa hiyo umri wa vijana utabaki vilevile.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, tumeona changamoto kubwa kwenye suala zima la mikopo; je, Serikali iko tayari sasa kubadili mfumo wa mikopo badala ya kutoa fedha kwenda kuwapa huduma kama ni ufugaji wa kuku, Serikali ikaamua kuwanunulia kuku ikawapatia wana kikundi badala ya kuwapa fedha ambazo haziendi kutimiza malengo ya ule mkopo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, baada ya maelekezo yale ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kufanya mapitio ya utoaji wa mikopo hii ya asilimia kumi na maelekezo ya Kamati yako ya Bunge ya TAMISEMI, hivi ni vitu ambavyo vinaenda kuangaliwa na timu ile ambayo ameiteua Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI.
MHE. MARTHA F. MARIKI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali lakini katika Mkoa wetu wa Katavi katika Jimbo la Nsimbo tuna x-ray ambayo Serikali imetupatia lakini x-ray hiyo imeshindwa kufanyakazi kutokana na kwamba hatuna mtaalam wa mionzi.

Je, ni lini Serikali itatupatia mtaalam wa mionzo ili x-ray iweze kufanyakazi kwa kuwahudumia wananchi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini swali langu la pili; katika Wilaya ya Tanganyika Kata ya Ilangu wananchi ususani kinamama wajawazito wamekuwa wakifata huduma mbali sana kutokana na kwamba hawana kituo cha afya; je, ni lini Serikali itatujengea kituo cha afya katika Kata hiyo ya Ilangu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Martha Mariki, la kwanza hili la wataalamu wa mionzi, hivi karibuni katika mwaka huu wa fedha Serikali imeajiri watumishi wa kada ya afya 8,000 na tayari katika matangazo yale wakati yanatolewa ilikuwa tunatafuta watalamu wa mionzi ya x-ray 69. Lakini nilitaarifu Bunge lako tukufu kwamba katika ajira hizi walipatikana watumishi 61 tu na hizi nafasi nyingine zilizosalia tutazitangaza upya ili kuweza kuwapata watalam hawa wa mionzi na tuweze kuwapeleka maeneo mbalimbali nchini ambapo Serikali imewekeza fedha nyingi katika ununuzi wa vifaa tiba ikiwemo mitambo ya mionzi na kule Nsimbo napo tutapaangalia kwa ajili ya kuwapeleka watalamu hawa wa mionzi.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la Kituo cha Afya katika Kata ya Ilangu iliyopo kule katika Wilaya ya Tanganyika, tutatuma timu ya watalaam kwa ajili ya kwenda kufanya tathimini katika Kata ya Ilangu, kuona idadi ya watu waliokuwepo pale na vile vigezo vinavyotakiwa vya umbali kwenda kufata huduma ya afya na kadhalika na baada ya tathimini hiyo kufanyika tutapata taarifa katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI na kuweka katika mipango yetu kuhakikisha kwamba wananchi wa Kata ya Ilangu wanapata huduma ya afya iliyobora kwa kupata kituo cha afya.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona.

Kwa kuwa kituo cha afya cha Kata ya Nyang’hwale kinatoa huduma zaidi ya miaka 30 kuhudumia kata zifuatazo; Kata za Shabaka, Kaboha, Busolwa, Nyabulanda, Nyijundu, Mwingiro hakina huduma ya x-ray je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka huduma hiyo ya x-ray kwenye Kituo cha Afya cha Nyang’hwale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Dkt. Samia imeweka kipaumbele katika kuhakikisha wananchi wake wanapata afya iliyobora kwa kuwekeza kwenye miundombinu ya afya vilevile kwenye vifaa tiba na katika bajeti ya mwaka 2023/2024 Serikali imetenga zaidi ya shilingi bilioni 112 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba ikiwemo vifaa vya mionzi kama vile x-ray na pale tutapoanza ununuzi wa vifaa hivi tiba tutaweka kipaumbele kwa ajili Kituo cha Afya cha Kata ya Nyang’hwale anapotoka Mheshimiwa Amar kule. (Makofi)

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupeleka vifaa tiba vya kisasa katika Hospitali ya Wilaya ya Hanang kama ventilator, anesthesia machine na diathermy ili koboresha huduma za afya ya mama na mtoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba hospitali zote za Wilaya zinakuwa zina vifaa tiba vya kisasa na tayari tumeshapeleka fedha kwa wenzetu wa MSD kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. MSD imeanza kupeleka vifaa hivi katika Hospitali za Wilaya mbalimbali hapa nchini. Nitakaa na Mheshimiwa Hhayuma kuweza kuona Hospitali ya Wilaya ya Hanang ipo katika awamu ipi ya kupokea vifaa tiba hivi vya kisasa katika Hospitali ya Wilaya ya Hanang.

MHE ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.

Kituo cha Afya cha Ngw’angw’ali na Ngulyati Wilaya ya Bariadi kina upungufu wa vifaa tiba; je, ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba vya kutosha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kuhusu upelekaji wa vifaa tiba Bariadi kama nilivyotoka kusema hapa awali, Serikali katika mwaka wa fedha 2023/2024 imetenga kiasi cha shilingi bilioni 112 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kote nchini na katika hivyo tutahakikisha yale maeneo yenye uhitaji mkubwa yanapata vifaa tiba hivi ikiwemo kule Bariadi alikokutaja Mheshimiwa Midimu.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Hospitali ya Mji wa Mafinga inahudumia watu wengi sana pale, nini mkakati wa Serikali kuongeza vifaa tiba vya kisasa? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali hii ya Awamu ya Sita ni kuhakikisha kwamba vifaa tiba vya kisasa vinakuwepo katika hospitali zote za Wilaya na vilevile katika vituo vyetu vya afya vya kimkakati. Katika kuhakikisha hilo linafanyika Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 112 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba hivyo vya kisasa na tutahakikisha pia Hospitali ya Mji wa Mafinga nayo inaongezewa vifaa tiba kama ilivyofanyiwa katika mwaka wa fedha huu tunaomaliza sasa.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na Serikali naomba kuuliza swali moja tu la nyongeza.

Shule husika ililetewa fedha shilingi milioni 80 kwa ajili ya kujenga bweni la watoto wenye mahitaji maalum, je, ni lini Serikali italeta fedha za kukamilisha bweni hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Leah Komanya, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge. Mheshimiwa Komanya amekuwa akifuatilia sana shule hii ya Mwanhuzi na alinieleza nilipokutana naye ofisini kwamba ndipo alipotokea yeye kwenye kata hiyo na atahakikisha kwamba fedha hii shilingi milioni 348 inapatikana, kwa hiyo, nimpongeze sana Mheshimiwa Leah kwa hili.

Mheshimiwa Spika, nikijibu swali lake la nyongeza la bweni ambalo lilianzwa kujengwa katika shule hii hii ya Msingi ya Mwanhuzi. Serikali ilipeleka shilingi milioni 80 kwa ajili ya ujenzi wa bweni kwa watoto wenye mahitaji maalum katika shule hii na sio shule hii pekee yake bali ilipeleka nchi nzima kwa ajili ya ujenzi wa mabweni haya, lakini baada ya kupeleka fedha hizi ujenzi ule haukukamilika na changamoto hii tunaifahamu na timu ya wataalam ilitumwa kwa ajili ya kufanya tathmini kwenye mabweni yote na mabwalo yote ambayo yalipelekewa fedha na hayakukamilika. Baada ya tathmini hiyo kufanyika sasa tupo katika mchakato wa kutafuta fedha kwa ajili ya kupeleka kukamilisha ujenzi wa mabweni haya na mabwalo haya. (Makofi)
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze kwa majibu mazuri ya Serikali, na ni kweli majengo saba yamejengwa. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, katika majengo hayo hatuna wodi ya watoto, akina baba, akina mama pamoja na theatre;

Je, ni lini sasa wodi hizo zitajengwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, ili hospitali hiyo iendane na kutoa huduma ya haraka kama ambavyo speed ya ujenzi imeenda inahitaji kuunganishwa na barabara ya lami ambayo iliahidiwa na kiongozi wa kitaifa.

Je, na barabara hiyo ambayo iko chini ya TARURA ni lini itajengwa kwa kiwango cha lami kuelekea katika hospitali iweze kutumika itakapo funguliwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Kyombo, la kwanza hili la kutokuwa na wodi ya watoto, akina baba na theatre vile vile katika Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nilikuwa nimeshasema kwenye majibu yangu ya msingi kwamba Serikali imetenga shilingi milioni 800 katika mwaka wa fedha wa 2023/2024 ambayo itakwenda kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa Hospitali hii ya Wilaya ya Misenyi na watapata wodi ya watoto, baba na vilevile theatre. Ni lengo la Serikali hii ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha kwamba miundombinu katika sekta ya afya ipo ya kutosha kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi wa nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la barabara inayounganisha hospitali. Barabara hii ina urefu kama wa kilomita nne kutoka kwenye barabara kuu inayokwenda Mtukula ambayo ni barabara ya TANROADS. Hivyo naomba nichukue nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kumwelekeza Meneja wa TANROADS Mkoa wa Kagera kwenda kufanya tathmini ya barabara hii na kuiweka katika mipango yetu kwa ajili ya kutafuta fedha na kuweza kuijenga ili wananchi waweze kufika hospitali kupata huduma za afya kwa wakati.
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza niipongeze Serikali ya Chama Cha Mapinduzi kwa kutujengea Vituo vya Afya kwenye tarafa tatu. Tuna tarafa nne Wilaya ya Kilindi lakini tuna Tarafa moja ya Kimbe haina kituo cha afya na umbali kutoka tarafa hiyo hadi Makao Makuu ya Wilaya ni takribani kilomita 120;

Je, nini mpango wa Serikali wa kujenga kituo cha afya kwenye tarafa hiyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu swali la Kigua Mbunge wa Kilindi, kwamba Tarafa ya Kimbe haina na kituo cha afya. Serikali imetenga mwaka wa fedha uliopita zaidi ya bilioni 117 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya vya kimkakati kote nchini ambapo vingine vilikwenda kwa Mheshimiwa Kigua kule Kilindi. Tutakaa na Mheshimiwa Kigua kuona hii Tarafa ya Kimbe nayo tunafanyaje ili iweze kutengewa fedha kupata ujenzi wa kituo cha afya kama vile kata ya kimkakati ili hizi kata zote zinazozunguka tarafa hii ziweze kupata huduma nazo za afya.

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa. Tunaishukuru sana Serikali kwa kutujengea Kituo cha Afya cha Uru Kusini na kinakaribia kinakamilika;

Je, Serikali ina mpango gani kupeleka vifaa na wahudumu ili wananchi waanze kupata huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka huu wa fedha 2022/2023 imeajiri watumishi wa afya wapatao 8,000 ambapo wengine watapangiwa katika Halmashauri ya Moshi Vijijini anapotoka Prof. Ndakidemi kule. Lakini vile vile katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali imeweka kwenye bajeti shilingi bilioni 112 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. Vitakapo nunuliwa tutahakikisha na Moshi Vijijini napo kwa Mheshimiwa Profesa Ndakidemi nao wanapata vifaa tiba hivi.
MHE. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Wilaya ya Muleba ni Wilaya kongwe hapa nchini lakini haina hospitali ya Wilaya na mwaka jana Mheshimiwa Rais alitupatia fedha kuanza ujenzi wa hospitali hiyo.

Je ni lini sasa ujenzi utakamilika wa Hosoitali ya Wilaya ya Muleba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa Hospitali hizi za Wilaya huwa unaenda kwa awamu na fedha hutolewa kwa awamu.

Awamu ya kwanza hutolewa milioni mia tano ama wakati mwingine bilioni moja kwa ajili ya kuanza ujenzi huo; na katika kila mwaka wa fedha Serikali hutenga fedha kwa ajili ya kuendelea na kumalizia ujenzi wa Hospitali hizi za Wilaya. Nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge, tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Fedha kuona katika mipango yao wameweka kiasi gani katika mwaka wa fedha unao fata ili ziweze kwenda Muleba kule kwa ajili ya ukamilishaiji wa Hospitali hii ya Wilaya.
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Tarafa ya Balangaralu Makao Makuu yake yako Kata ya Balanga na pale hakuna Kituo cha Afya.

Je, Serikali ni lini itapeleka fedha ili kituo cha afya kijingwe pale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itapeleka fedha katika Tarafa aliyoitaja Mheshimiwa Hhayuma kule Hanang kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Tutaangalia katika mipango iliyopo katika mwaka wa fedha unaofata 2023/2024 kuona kama fedha yoyote imetengwa kwa ajili ya kwenda Halmashauri ya Wilaya ya Hanang ili tuweze kuhakikisha inaenda haraka kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya.

MHE. SYLIVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niipongeze Serikali na niishukuru kwa majibu mazuri. Tunashukuru kwa hizo milioni mia tano kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, Wilaya ya Kibondo kata ya Nyaruyoba hakuna Kituo cha Afya na wananchi wanahangaika. Tumeahidiwa milioni 200 kwa ajili ya ujenzi wa wodi.

Je, ni lini Serikali itatuletea milioni 200 hizo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali la pili Wilaya ya Buhigwe kata ya Mbanga na Kata ya Mhinda hakuna Vituo vya Afya, wananchi wanatembea umbali mrefu kupata huduma.

Je, ni lini Serikali itajenga Vituo vya Afya katika kata hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu maswali mawili ya nyongeza yaliyoulizwa na Mheshimiwa Sigula; la kwanza hili la Nyaruyoba kule Wilayani Kibondo milioni mia mbili, tutakaa na Mheshimiwa Mbunge ili tuweze kuwasiliana na idara ya afya katika Ofisi ya Rais TAMISEMI kuona fedha hizi zilizo ahidiwa zinaweza kwenda mara moja kwa ajili ya kuanza ujenzi wa kituo cha afya kule Wilayani Kibondo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili, tutafanya tathmini kule Wilayani Buhigwe na kuona vituo hivi vya afya alivyoviomba Mheshimiwa Sigula kama vina kidhi vigezo vya kuweza kupandishwa hadhi na kuwa vituo vya afya ili tuweze kutenga fedha katika mwaka wa fedha unaofata kwa ajili ya kuanza ujenzi wake mara moja.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kata ya Kiwila katika Jimbo la Rungwe ni kata yenye wakazi wengi sana na kituo cha afya bado hakija malizika.

Je, ni lini Serikali mtatuongezea nguvu ili tuweze kumaliza kituo kile na kusaidia wananchi wa kata ile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakagenda kuhusu kata ya Kiwila kumaliziwa kituo chao cha afya. Nitakaa naye kuweza kujua ni majengo yapi ambayo bado hayajakamilika na kuhakikisha kwamba tunaona ni mipango ipi iliyotengwa na Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe. Lakini vile vile sisi katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI tutaona kwenye bajeti ya mwaka 2023/2024 ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya Kituo hiki cha Afya Kiwila ili fedha hizo ziweze kwenda mara moja kwa ajili ya kumalizia majengo hayo.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi. Mbulu Vijijini wananchi wamechanga na wamejenga kwenye Kata ya Geterei OPD kama Kituo cha Afya, na Kata ya Maseda vilevile; je, lini mtapeleka fedha kuunga juhudi za wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwapongeze Mheshimiwa Mbunge Flatei Massay vile vile na Mheshimiwa DC wake pale Ndugu Heri James kwa jitihada kubwa ambazo wanazifanya kwa ajili ya kusukuma gurudumu la maendeleo kwa kuhamasisha wananchi kujenga miundombinu ya afya. Nitakaa na Mheshimiwa Flatei kuona ni mipango gani ambayo imewekwa kwetu katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa ajili ya kumalizia vituo vya afya ambavyo amevitaja.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Mwaka mmoja nyuma Waheshimiwa Wabunge wote tulitakiwa kutoa vipaumbele vya ujenzi wa Vituo vya Afya kwenye majimbo yetu. Mimi Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini ni miongoni na nilipewa Kituo cha Afya cha Kata ya Ruvu, lakini hadi leo hakuna kinachoendelea; je, nini kauli ya Serikali kwenye kuanzisha ujenzi wa kituo hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha wa 2021/2022 Serikali ilijenga vituo vya afya 234 kote nchini, na hii ni commitment kubwa ya Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha tunapata vituo vya afya kwenye maeneo yote ya kimkakati hapa nchini ikiwemo kule Kibaha Vijijini alipotaja Mheshimiwa Mwakamo. Tutakaa tuone katika mipango iliyowekwa mwaka 2023/2024 wa fedha, ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya Kibaha Vijini ili kqenda kujenga kituo cha afya hicho cha kimkakati ambacho amekitaja Mheshimiwa Mwakamo.
MHE.BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Jimbo la Bunda limekuwa na kituo cha muda mrefu cha zamani kinaitwa Ikizu, na kimechaka sana, na Serikali imetoa ahadi ya kukarabati vituo vya zamani vya afya;

Je, ni lini Kituo cha Ikizu kitakarabatiwa kwa ahadi ya Serikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakaa na Mheshimiwa Getere ili kuweza kuona ahadi hiyo ya Serikali ilitolewa lini ili tuweze kuifatilia vizuri kwenye idara husika ambayo ilitoa ahadi hiyo na tuweze kuhakikisha tunapata fedha kwa ajili ya kukarabati kituo cha afya hicho alichokitaja Mheshimiwa Getere.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana majibu ya Serikali yamekuwa mazuri. Lakini kwa hali ya Jimbo la Sikonge ilivyo, kilometa za mraba 27,873, kuna wananchi wanatembea kilomita 70 mpaka kilometa 100 kufikia kituo cha afya cha karibu; je, Serikali haioni kwamba Wilaya au Jimbo kama la kwangu wanatakiwa waweke kipaumbele maalum ili watu wasiwe wanatembea kilomita 100 kufata kiyuo cha afya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili hizo fedha ambazo nimeuliza mimi bilioni 1.5 ni ela kidogo sana kwa Serikali; je, lini watatupatia hizo ela ili tuanze na hivyo vituo vitatu tulivyopendekeza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Kakunda Mbunge wa Sikonge, la kwanza la Serikali kuona umuhimu. Serikali inaona umuhimu wa kujenga vituo vya afya kote nchini na ndio maana Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ilijenga vituo vya afya 234 kwa kutumia zaidi ya bilioni 117 kwa ajili ya kupeleka huduma karibu na wananchi. Tutakaa kuona ni mipango ipi iliyowekwa katika mwaka wa fedha 2023/2024 kwa ajili ya kujenga vituo vya afya katika Wilaya ya Sikonge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali la pili, tutaangalia kadri ya upatikanaji wa fedha. Tutawasiliana na wenzetu wa Wizara ya Fedha kuona tunapataje fedha hii kwa ajili ya kusogeza huduma karibu kule Jimboni Sikonge.
MHE. SELEMANI J. ZEDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mwaka huu wa fedha unaoisha 2022/2023 Serikali ilitenga milioni 500 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Kituo cha Afya kwenye Kata ya Igusule, Jimbo la Bukene Halmashauri ya Wilaya ya Nzega. Sasa, ukizingatia kwamba bado siku chache mwaka huu uishe;

Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusu kupeleka fedha hizi sasa milioni 500 ambazo ilizitenga kwenye Kata ya Igusule ili ujenzi wa Kituo cha Afya uanze?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakaa na Mheshimiwa Zedi kuona hizi milioni 500 zilizotengwa ni hatua gani imefikiwa kwa ajili ya kuzipeleka kwa ajili ya kuanza ujenzi wa kituo cha afya kule Igusule, Jimboni Bukene.
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Niipongeze Serikali kwa kujenga vituo 234 vya afya nchini kikiwemo kituo cha kisasa kabisa pale katika Kata ya Kinondoni ambacho tayari kimeanza kufanya kazi. Tatizo ni uhaba wa madaktari na wauguzi;

Je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kuhakikisha vituo hivi vipya ambavyo vimejengwa vinapata na kuondolewa tatizo la kuwa na madaktari na wauguzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tarimba la kupata madaktari na wauguzi katika kituo cha afya Kinondoni. Jitihada za Serikali ya Awamu hii ya Sita katika kuhakikisha vituo vya Afya vyote vilivyojengwa na vilivyopo vinapata watumishi wa kutosha imefanyika kubwa katika mwaka wa fedha huu 2022/2023 kwa kuajiri watumishi wa afya 8070. Tayari watumishi hao wameanza kupangiwa maeneo yao ya kazi ikiwemo Halmashauri ya Kinondoni. Hivyo basi nimtake Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni kuhakikisha kati ya wale ajira mpya atakao wapokea aweze kuwapangia katika vituo hivi vya afya ambavyo vimejengwa kwa fedha nyingi iliyotolewa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kituo cha Afya cha Matwiga, Isangawana na Mafyeko vilipata milioni mia tatu kila kituo na ujenzi wake ulishaanza;

Je, ni lini Serikali itatoa fedha ili vituo hivyo viweze kumalizika na baadaye wananchi waweze kupata huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Masache Kasaka Mbunge wa Lupa; changamoto iliyojitokeza kule Wilayani Chunya ilikuwa kwamba fedha ilipelekwa na Serikali kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya kimoja. Wao wenyewe walikaa kwenye Baraza la Madiwani wakaamua kugawanya fedha ile na kuanzisha ujenzi wa vituo vya afya viwili. Ni mategemeo yangu kwamba walipopitisha maamuzi yale walijua wana mapato ya kutosha kwa ajili ya kumalizia vituo vya Afya hivi vya Isangawana na Mpepo kule. Lakini nitakaa na Mheshimiwa Kasaka kuona ni namna gani tunaweza tukakaa, tukazungumza na Mkurugenzi wa Halmashauri ili waweze kumalizia maeneo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro ule ulianzishwa na wao wenyewe Madiwani kwa kugawanya fedha iliyotolewa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya kimoja.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Kituo cha Afya cha Mafiga ni kituo kikubwa ambacho hasa kinatoa huduma kwa akinamama wajawazito. Je, ni lini Serikali itatoa hela ya kumalizia jengo la upasuaji?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itatoa fedha kwa ajili ya umaliziaji wa Kituo hiki cha Afya Mafiga kadri ya upatikanaji wake, lakini tutaangalia katika mwaka wa fedha 2023/2024 kama kuna fedha imetengwa ili iweze kupelekwa mara moja kwa ajili ya kumalizia kituo hicho.

MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa ukosefu wa nyumba unasababisha walimu na hao wafanyakazi wa Serikali kuchelewa, lakini katika vijiji vingine kuna nyumba za wananchi ambazo hawaishi huwa wanakuja tu wakati wa sikukuu ikiwemo Christmas. Je, Serikali ina mpango gani sasa kuziagiza Halmashauri ziingie mkataba na hawa watu wenye ma–bungalow huko vijijini ili waweze kupatia wafanyakazi nyumba za kuishi?

Swali la pili, upungufu ulioandikwa ni mkubwa sana, hata tungejenga kwa miaka 10 bado hatutatosheleza. Serikali inasema nini sasa kuongeza hela zaidi katika mfuko huo wa ujenzi ili hii kazi iende kwa uhakika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEORGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shally Raymond.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza kuhusu Serikali ina mpango gani kuingia mkataba. Hili ni jukumu ambalo linaachiwa Halmashauri wenyewe kuweza kuingia mikataba na wenye nyumba ambazo hazitumiki na naamini hili Mheshimiwa Mbunge amelileta kwa sababu kule Mkoa wa Kilimanjaro wengi wanakuwa wapo katika Mikoa mingine na wanarudi kipindi cha mwisho wa mwaka. Kwa hiyo, tutakaa na kuona ni namna gani tunaweza tukazungumza na Halmashauri ambazo zina mazingira kama ya Mkoa wa Kilimanjaro, kuona ni namna gani wanaweza kuingia mikataba hii kwa ajili ya kuweza kuwaweka watumishi wa umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la hela ya ujenzi. Ni wajibu wa Halmashauri kuanza kuweka fedha, kutenga fedha katika mapato yao ya ndani kwa ajili aya ujenzi wa nyumba za watumishi wa kada ya elimu na afya. Serikali Kuu tayari imeshachukua jukumu kubwa sana, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, amepeleka fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa maboma, madarasa katika Halmashauri hizo na ukamilishaji wa maboma lakini vilevile katika afya ameshapeleka fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa zahanati na vituo vya afya.

Kwa hiyo, ni wajibu wao sasa kuanza kuunga mkono jitihada zile za Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutenga fedha kwa ajili ya kujenga na kukamilisha maboma yaliyojengwa na wananchi kwa ajili ya nyumba za watumishi wa umma. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za pembezoni katika Halmashauri wa Mji wa Tarime ni pamoja ya Kata ya Nyandoto na Kata ya Kenyamanyori. Wananchi wa Kata ya Kenyamanyori walishaanza kujenga kituo cha afya kwa nguvu zao wenyewe na baadhi ya maboma yamekamilika kuanzia mwaka 2019, Serikali iliahidi kwamba itapeleka fedha kuhakikisha kwamba kituo kile kinakamilika maana wako nje ya mji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka kujua commitment ya Serikali sasa ni lini watapeleka fedha ili waweze kukamilisha Kituo cha Afya cha Kenyamanyori kupunguza adha ambayo wanaipata kuja kupata huduma kwenye hospitali ya Mji wa Tarime?

Swali langu la pili, katika Kata za Susuni na Mwema katika Halmashauri ya Wilaya ya Tarime ni Kata ambazo zipo pembezoni na wanapata huduma sana sana wakienda kituo cha Sirari kule au hospitali ya Nyamwaga lakini wengi wanakuja Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tarime. Ninataka kujua ni lini Serikali itahakikisha kwamba Kata hii ya Susuni na Kata ya Mwema na zenyewe zinapata vituo vya afya ili kuweza kupunguza adha ya wananchi wale kusafiri mwendo mrefu kutafuta huduma ya afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEORGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Esther Matiko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la kwanza la lini fedha itakwenda kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Afya Kenyamanyori.

Kwanza nichukue nafasi hii kuwapongeza wananchi wa Kata ya Kenyamanyori kwa kuweza kuanza kwa jitihada zao wenyewe ujenzi wa kituo chao cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la fedha tutatuma timu pale ya Mganga Mkuu wa Mkoa kwa ajiili ya kufanya tathmini ya ujenzi ule ambao umefanyika na kuona kama vinakidhi mahitaji yanayotakiwa ili kusajili kituo cha afya kipya katika Kata ile na baada ya tathmini ile wataiwasilisha Ofisi ya Rais – TAMISEMI, kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunatafuta fedha ya kupeleka kuunga mkono juhudi hizi za wananchi wa Kenyamanyori kumalizia kituo kile cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la Kata ya Susuni na Mwema zilizoko kule Halmashauri ya Wilaya ya Tarime. Tutafanya vivyo hivyo kama ambavyo nimemjibu swali lake la kwanza la kuhakikisha timu ile inapoenda Tarime Mji, wafike vilevile kwenye Halmashauri ya Wilaya Tarime na kufanya tathmini katika Kata hizi mbili ambazo amezitaja Mheshimiwa Matiko na kisha walete taarifa Ofisi ya Rais - TAMISEMI ili tuweke katika mipango yetu ya kutafuta fedha na kuhakikisha kwamba tunapeleka kwa ajili ya kujenga vituo hivi vya afya.
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Wananchi wa Tarafa ya Msitu wa Tembo wamekuwa na changamoto kubwa ya kufuata huduma za afya kwa umbali mrefu. Je, ni lini sasa Serikali itawajengea wananchi hao kituo cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEORGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itajenga vituo hivi vya afya ambavyo ametaja Mheshimiwa Regina Ndege, katika mwaka wa fedha unaofuata tutaangalia kama kuna fedha iliyotengwa kujenga kama hakuna tutatenga katika mwaka wa fedha wa 2024/2025.

MHE. JEREMIAH A. MRIMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni lini, sasa Serikali itatusaidia fedha ya nyongeza kwa ajili ya ukamilishaji ujenzi kituo cha afya Machochwe kama tulivyoomba? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEORGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, hili Mheshimiwa Mrimi amekuwa akilifuatilia sana kuhusu fedha hizi za Kituo cha Afya Machochwe na tutaendelea kama ambavyo nimeonana naye ofisini mara kadhaa kumueleza kwamba, tunaangalia namna gani bora tutapata fedha ya kumalizia kituo hiki cha afya na pale ambapo Serikali itapata fedha basi tutapeleka katika kituo hiki cha afya cha Machochwe ili kiweze kukamilika. (Makofi)

MHE. SYLVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza ninashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini kutokana na majibu ya Serikali utaona kabisa bado tuko kwenye asilimia 31.5 ya utekelezaji, hii inaonesha bado kazi inatakiwa kufanyika. Nataka kujua ni nini mkakati maalum wa Serikali, kuhakikisha wanawake wengi na vijana wengi wanapata uelewa na umuhimu wa masuala haya ya SACCOS ili waweze kujiunga wajikwamue kiuchumi?

Swali la pili, kulikuwa na VICOBA vingi vya wakinamama na vijana. Je, Serikali iko tayari kuviwezesha vitambulike rasmi ili viingie kunufaika kwenye mikopo ya asilimia 10 katika mfumo huu mpya unaokuja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEORGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sylvia Sigula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza la mkakati maalum wa Serikali kwa ajili ya kutoa elimu kwa wingi zaidi ili kufahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Halmashauri za Wilaya na Majiji na Halmashauri za Miji, zina utaratibu na watumishi waliokuwa kule Maafisa Biashara, Maafisa Maendelo ya Jamiii pamoja na Maafisa Ushirika. Ni wajibu wao kuhakikisha kwamba wanasajili vikundi vingi zaidi au SACCOS nyingi zaidi kwenye maeneo yao na kuendelea kutoa elimu juu ya umuhimu wa SACCOS hizi. Hivyo basi, nitumie Bunge lako Tukufu kuwaelekeza tena Wakurugenzi wote wa Halmashauri za Wilaya hapa nchini kuhakikisha hawa niliowataja Maafisa Biashara, Maafisa Maendeleo ya Jamii pamoja na Maafisa Ushirika wanafanya kazi kwa pamoja kwa ajili ya kuweza kutoa elimu juu ya umuhimu kuwa na SACCOS na kusajili SACCOS nyingi ambazo zinakidhi vigezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili la VICOBA kutambuliwa zaidi na kupewa mikopo. Hili linategemeana vilevile na wao VICOBA kukidhi vigezo vile vya masharti ya mikopo ile ya asilimia 10. Hata katika mapitio yanayofanyika kwa maelekezo yake Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, juu ya utoaji wa mikopo hii bado mikopo hii itakuwa ni ya vijana, wanawake na walemavu. Kinachofanyika ni review ya namna ya utoaji wa mikopo ile, siyo ubadilishwaji wa namna mikopo ile inavyotolewa kwa watu. Kwa hiyo, kama vikundi hivi vitakuwa vinakidhi vigezo, VICOBA hivi kwamba vina vijana, vina wanawake na walemavu, vinatakiwa pia kunufaika na mikopo ile inayotolewa. Kwa hiyo, tutazingatia hili pia katika timu ile inayofanyia mapitio haya ili waweze kuongeza SACCOS nyingi zaidi. (Makofi)
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa katika Halmashauri hakuna sheria inayoruhusu vikundi vya SACCOS kukopeshwa. Je, ni lini Serikali italeta sheria Bungeni ili kufanya marekebisho SACCOS ziweze kukopeshwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEORGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Sheria ile ya Fedha za Serikali za Mitaa ambayo inaelezea namna ya utoaji wa mikopo ya vikundi, tayari kama nilivyokuwa nikimjibu Mheshimiwa Sigula kwamba kama SACCOS hizi zinakidhi vile vigezo vilivyotajwa kwenye Sheria ile ya Fedha ya Serikali za Mitaa, ya kuwa ni kuna vijana kwenye SACCOS hizo, ama SACCOS hizo zinaongozwa na walemavu au wanawake watastahili kupata fedha hizi za vikundi za asilimia 10, haina haja ya SACCOS hizi tena kusajiliwa kama vikundi kwa sababu tayari ni SACCOS zilizosajiliwa na kama viongozi wao wale mwenyekiti, katibu na muweka hazina wanakidhi vigezo vya umri kwa vijana na ni wanawake au walemavu basi wanastahili kupata mikopo hii ya asilimia 10. (Makofi)
MHE. JACQUELINE K. ANDREA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza; kwa nini Serikali inapotenga pesa za majengo ya zahanati na vituo vya afya isitenge sambamba na pesa za vifaa? Kwa sababu mara nyingi majengo yanafunguliwa wakati vifaa hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; nini tamko la Serikali kwa majibu mazuri yaliyojibiwa hapa kwamba kuna pesa zimetengwa kwa ajili ya vifaa, tamko la Serikali katika Mkoa wetu wa Tabora kwa zahanati ambazo hazina vifaa na tayari wananchi wanachangishwa pesa za mabenchi kama Zahanati ya Goweko, Kalangale, Wilaya ya Uyui lakini vilevile Wilaya ya Igunga, Kagongo, Kata ya Itunduru na Ibuta - Kata ya Mbutu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacqueline Kainja Andrea, la kwanza, kwa nini Serikali isitenge fedha ya vifaa tiba kwanza; kimekuwa ni kipaumbele cha Serikali kujenga miundombinu kwanza ili huduma zile za msingi ziweze kuanza kutolewa na baada ya kuwa majengo yale yamekamilika na huduma za msingi kuanza kutolewa, ndipo Serikali inatenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba na kuvipeleka kwenye zahanati hizo.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nilisema kwenye majibu yangu ya msingi, katika mwaka huu wa fedha ambao tunaumaliza, Serikali ilitenga shilingi bilioni 15 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba ambapo tayari bilioni 12.90 imeshanunua vifaa tiba hivyo na vimeanza kusambazwa katika zahanati zote nchini.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili; tamko la Serikali kwa zahanati kupata vifaa tiba katika Mkoa wa Tabora anaotoka Mheshimiwa Mbunge, Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka kipaumbele katika kuhakikisha vifaa tiba vinakuwa katika zahanati zote, vituo vyote vya afya vilevile katika hospitali za wilaya kote nchini katika kuhakikisha afya za Watanzania zinaboreka.

Mheshimiwa Spika, na kwa ajili ya kutekeleza hilo, Serikali imetenga shilingi bilioni 112 kwenye mwaka wa fedha 2023/2024 na vifaa tiba hivyo vitaanza kununulia mara moja mwaka wa fedha unapoanza, na tutaanza kuvisambaza katika maeneo yote nchini ya zahanati, vituo vya afya na hospitali za wilaya, yakiwemo maeneo yale ambayo ameyataja Mheshimiwa Jaqueline Kainja.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; je, ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba katika zahanati za Wilaya ya Lushoto zilizokamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itapeleka vifaa tiba kwenye zahanati za Wilaya ya Lushoto pale ambapo tutaanza utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha wa 2023/2024 ambapo Serikali imetenga shilingi bilioni 112 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kote nchini.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mamlaka ya Mji mdogo wa Katesh ni ya muda mrefu na Mji wa Katesh umepanuka sana. Je, Serikali lini itachukua hatua ya kuanzisha Mamlaka kamili ya Mji wa Katesh?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hhayuma, Serikali kwa sasa bado inaweka kipaumbele katika kumalizia ujenzi wa miundombinu kwenye maeneo ambayo ni mapya na maeneo yale ambapo Halmashauri zilihamia kwenye maeneo yale ya kiutawala na pale Serikali itakapomaliza ujenzi wa miundombinu hii muhimu, tutaanza kuangalia tena namna ya kuweza kuanza kupandisha hadhi maeneo mengine ya Mamlaka za Miji.
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Naibu Waziri Mji mdogo wa Kibaya na Matui imekuwa ipo kwa muda mrefu sana, sasa imewaacha wale siyo wenyeviti siyo Wenyeviti wa Mitaa wame-hang tu kwa muda mrefu.

Je, ni lini Serikali italeta mpango ili suala hili likae vizuri? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema hapo awali Serikali kwa sasa imeweka kipaumbele katika umaliziaji wa miundombinu na ujenzi wa miundombinu mingine katika maeneo mapya ya kiutawala ambayo yalianzishwa hivi karibuni na yale maeneo ambapo Halmashauri zilihamia kwenye maeneo hayo ya utawala. Pale ambapo zoezi hili litakamilika la ujenzi wa miundombinu hii tutaanza kuangalia namna gani ya kuanza kupandisha hadhi Miji hii, ikiwemo Kibaya na Matui kule Kiteto.
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, mchakato wa kupandisha hadhi Mji wa Kibaha kuwa Manispaa ya Kibaha umefikia hatua gani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma la kupandisha hadhi Mji wa Kibaha kuwa Manispaa. Ombi hili la Manispaa ya Kibaha la kukidhi vigezo, kwanza walipewa vigezo vya kuweza kufikia ili waweze kupandishwa hadhi ikiwemo idadi ya watu. Waliwasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI Aprili mwaka huu lile ombi lao la kuweza kupandishwa hadhi na tayari lipo kwenye timu ambayo wanaiangalia kuona kama vigezo vile vimekidhi kwa ajili ya kupandishwa hadhi na kuwa Manispaa ya Kibaha.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali ninaomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza, shule hii ya Mjimwema Makambako ni shule ambayo Mheshimiwa Mbunge aliiweka moja kati ya vipaumbele vya shule zake ambazo tulivileta TAMISEMI ili ziweza kujengwa kutokana na eneo hili kuwa na uhitaji mkubwa wa sekondari.

Je, ni lini Serikali itafanyia kazi mapendekezo ya Mheshimiwa Mbunge ili shule iweze kujengwa pale?

Swali la pili, hata Wilaya ya Makete nilileta kipaumbele kwenye Kata ya Kigala ambayo kwa muda mrefu haina Shule ya Sekondari ya Kata. Ni lini Serikali itajenga Sekondari ya Kata kwenye Kata ya Kigala ili wananchi waweze kupata elimu kwa mazingira ya karibu? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza. Kuhusu swali hili la kwanza la Kata ya Mjimwema kupata shule, kama nilivyokwisha sema kwenye majibu yangu ya msingi, Serikali kwa sasa ipo mbioni kupeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya katika Kata ambazo hazina shule kwenye Halmashauri mbalimbali nchini na kila Halmashauri kwenye Halmashauri 184 itapata shule moja. Tumetenga kiasi cha shilingi milioni 570 kwa ajili ya ujenzi wa shule hizo. Awamu ya kwanza ya hizo shule 231 ilienda milioni 470, Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeangalia hali ya mabadiliko ya vifaa, bei na kadhalika na kuweka minimum kuwa ni milioni 570. Sasa ni wajibu wa Halmashauri ya Mji wa Makambako wenyewe kuhakikisha kwamba fedha hii inapofika waweke kipaumbele Shule ya Mjimwema ili iweze kujengwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili la Kata ya Kigala kule Makete vilevile Halmashauri ya Wilaya ya Makete itapokea shilingi minimum milioni 570 kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya katika Halmashauri yao, hivyo basi ni wajibu wao kuhakikisha kwamba wanapeleka fedha katika Kata hii ya Kigala kwa ajili ya ujenzi wa sekondari mpya.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je ni lini Serikali itapeleka fedha kwenye ukarabati wa shule ya Sekondari ya SUA?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu swali la Dkt. Ishengoma la Serikali kupeleka fedha kwa ajili ya ukarabati wa shule ya Sekondari ya SUA. Tutatuma timu pale ya Afisa Elimu wetu wa Sekondari katika Halmashauri ile kuweza kufanya tathmini ya nini kinachohitajika kufanyika katika ukarabai ule na watawasilisha taarifa ile Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kutafuta fedha kwa ajili ya kufanya ukarabati wa Shule ya Sekondari SUA.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Halmashauri nyingi zinakosa fedha za kujiendesha zenyewe kutokana na Serikali Kuu kuchelewesha zile asilimia ambazo zinawekwa na zinatengwa kwamba, kwa kisheria asilimia 20 ndiyo inabaki asilimia 80 inakwenda Serikali Kuu.

Je, Serikali iko tayari kutengeneza mfumo ambao utafanya Halmashauri zinapokusanya fedha zile asilimia 20 zibaki moja kwa moja katika Halmashauri zake, badala ya kusubiri zirejeshwe kama ambavyo Serikali inakuwa hairejeshi wakati mwingine?

Swali langu la pili, kwa kuwa Halmashauri ndiyo watekelezaji wakuu wa sera na mipango ya Serikali Kuu kwa ngazi ya chini. Je, Serikali haioni umuhimu wa kurejesha vyanzo vyote vya mapato ambavyo vinakusanywa katika Halmashauri ili viweze kuwasaidia kuendesha Halmashauri hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Grace Tendega kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza la Serikali kuwa tayari kutengeneza mfumo kwa ajili ya kubakiza asilimia hizi kulekule kwenye Halmashauri ni wazo zuri na tunalipokea, tutakaa na timu ya wataalam kuona wamefikia wapi kwa sababu tayari pia wao walikuwa wanalifanyia kazi kwa ajili ya kutengeneza mfumo huo. Tutakaa kuona wamefika wapi na wenzetu vilevile wa Hazina kuona wamefikia wapi kwa ajili ya kuweza kutengeneza mfumo huu lakini ni wazo zuri.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, tayari Serikali Kuu imeanza kuzirudishia Halmashuri vyanzo vile ambavyo wanakusanya. Mfano, katika mwaka wa fedha huu tunaoenda kuuanza wa 2023/2024 vyanzo vya makusanyo vile vya mabango ya matangazo vimerudishwa kule kwenye Halmashauri zenyewe ili ziweze kukusanya na tunaendelea kuangalia kama Serikali kwa ujumla wake ni vyanzo vipi viweze kuendelea kurudishwa kwenye Halmashauri zile ili kuziongezea uwezo.

Mheshimiwa Spika, vilevile Serikali kuu imekuwa ikipeleka fedha nyingi kwenye miradi ya maendeleo kwenye Halmashauri hizi hata zile ambazo hazina uwezo kutoka Serikali Kuu kwa ajili ya kuwasaidia katika ujenzi wa madarasa, katika ujenzi wa zahanati, katika ujenzi wa vituo vya afya na kadhalika ili kuwapunguzia mzigo Halmashauri hizi.
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na ninaishukuru Serikali kwa majibu mazuri tu. Nina maswali mawili madogo tu ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa sababu barabara hii inaunganisha Kata tatu. Kata ya Msanja, Kata ya Kilindi Asilia na Kata ya Kimbe, ni Kata ambazo zina uzalishaji mkubwa sana wa mahindi na kipindi cha mvua inakuwa ni shughuli kubwa magari kupita. Sasa kwa sababu suala hili liko Serikalini; Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kuelekeza Mkoa sasa kufanya tathmini hiyo na iweze kupandishwa hadhi barabara hiyo?

Swali la pili ni kwamba barabara hii ina madaraja mengi na ina vivuko vingi sana na kipindi cha mvua haipitiki. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri uko tayari kutoa maelekezo kwa TARURA ili maeneo haya yaweze kurekebishwa na Wananchi wa Wilaya ya Kilindi waweze kupata huduma ya Serikali? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ninaomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kigua, swali la kwanza kuhusu kuelekeza mkoa; kama nilivyokuwa nimesema kwenye majibu yangu ya msingi kwamba, taratibu za kupandisha au kuteremsha barabara kuwa ya Mkoa ni taratibu za kisheria. Hivyo basi, ningeshauri Mkoa wa Tanga waanze kuchukua hatua stahiki za kupandisha barabara hii kwa kukaa Mheshimiwa Kigua kule Kilindi kupitisha kwenye DCC yao na ikitoka DCC iweze kwend RCC na baadaye kwenda kwenye Bodi ya Barabara ya Mkoa, kisha waweze kuandika kwa Waziri mwenye dhamana ya barabara ambaye ni Waziri wa Ujenzi ili na yeye aweze kutuma timu ya kufanya tathmini ili barabara hii iweze kupandishwa kuwa ya Mkoa. Nitakaa na Mheshimiwa Kigua tuone tunafanya vipi na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi ili barabara hii iweze kuanza huu mchakato wa kupandishwa.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la madaraja na vivuko ambavyo vinahitajika sana. Ni kweli nikiri kwamba barabara hii ni muhimu sana kwa uzalishaji na wananchi wa kule Kilindi kwa ajili ya kutoa bidhaa zao mashambani Mheshimiwa Mbunge amekuwa akilifuatilia sana, tutakaa naye vilevile kuona ni namna gani tutapata fedha kwenye bajeti ya TARURA hii inayokuja 2023/2024 ili kuweza kutengeneza vivuko zaidi kwa sababu tayari katika mwaka huu pekee wa fedha tunaoumaliza tulitengeneza boksi Kalavati 15, drift ndefu yenye mita 15 lakini imechongwa vilevile kilometa 21 kwenye barabara hii, lakini kwa sababu ina urefu wa kilometa 47 tutakaa tuone ni namna gani tunaendelea kutengeneza maeneo hayo yaliyosalia. (Makofi)
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, tangu Serikali ya Awamu ya Sita iingie madarakani Jimbo la Mufindi Kusini haikujengewa kituo cha afya hata kimoja, wakati maeneo mengine yamepata fursa hiyo. Wananchi wa Mufindi Kusini wana uhitaji mkubwa.

Je, ni lini Serikali itajenga kituo cha afya cha Mtwango?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya kwenda kujenga kituo cha afya Mtwango. Kwa hatua za mwanzo naomba nimuelekeze Mganga Mkuu wa Mkoa wa Iringa kutuma timu kwenye eneo la Mtwango na kufanya tathmini na kuona mahitaji ambayo yako katika Kata ile, baada ya kufanya tathmini hiyo aiwasilishe Ofisi ya Rais – TAMISEMI Ili tuweze kuona ni namna gani tunapeleka fedha.

Mheshimiwa Spika, nimtoe mashaka Mheshimiwa Kihenzile Serikali hii ya Awamu ya Sita imeweka kipaumbele cha kujenga vituo vya afya kwenye maeneo yote ya kimkakati nchini ikiwemo kule Kata ya Mtwango Jimboni kwake.

MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Je, ni lini sasa Serikali itapeleka pesa kwa ajili ya upanuzi wa Kituo cha Afya cha Nyambiti ambapo imekuwa ikiahidi kila mara tunapouliza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itapeleka fedha katika kituo hiki cha afya alichokitaja Mheshimiwa Kasalali Mageni kule Jimboni Sumve kadri ya uapatikanaji wa fedha, lakini tutatuma timu iweze kuangalia pia ukubwa wa eneo lililopo pia na majengo ambayo yanahitaji kufanyiwa upanuzi halafu tuweze kupata taarifa kamili na kutafuta fedha hizo.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, Kata ya Mapinga katika Jimbo la Bagamoyo katika sensa ya mwaka huu ina watu 42,000 na haina kituo cha afya.

Je, Serikali ina mpango gani kujenga kituo cha afya katika kata hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutatuma timu katika Kata ya Mapinga kule Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo kuweza kufanya tathmini na kuona kama vigezo vimefikiwa kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya, halafu tutatafuta fedha kwa ajili ya kujenga kituo hicho cha afya.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kuwa Kata ya Didia ni Kata ya kimkakati na ina idadi kubwa sana ya watu ukizingatia kwamba ni maarufu kwa zao la mpunga.

Je, ni lini Serikali itajenga kituo cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni dhamira ya Serikali hii ya Awamu ya Sita kuhakikisha inajenga vituo vya afya kwenye maeneo yote ya kimkakati nchini, ikiwemo Kata hii aliyoitaja Dkt. Christina Mnzava, tutafanya tathmini na kuona mahitaji yanayohitajika pale na kisha kuiweka kwenye mipango yetu ya kutafuta fedha. (Makofi)
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Serikali ambayo ni ya jumla sana, naomba kuuliza swali dogo moja tu la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, maeneo ambayo yanataka kumegwa kutoka kwenye vijiji ambavyo nimevitaja ni maeneo makubwa na tayari pande zote za vijiji zina miundombinu muhimu kama vile shule na zahanati na kuna ahadi ya viongozi wakiwemo Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ni lini, Serikali itavigawa vijiji hivi ili kurahisisha shughuli za maendeleo na kuwasogezea wananchi huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama ambavyo ametoka kusema Mheshimiwa Mnzava hapa, kwamba kama maeneo haya tayari yana miundombinu muhimu kwa ajili ya kukidhi vigezo vile vinavyotakiwa kuwepo kwa ajili ya kugawa vijiji vipya, basi tutatuma timu katika maeneo hayo ili kuweza kufanya tathmini hiyo na kisha baada ya thathmini hiyo tutakaa na wataalam pale kwetu Ofisi ya Rais - TAMISEMI na kisha kuona ni namna gani tunaweza kuwapatia vijiji hivyo kwa sababu tayari maeneo hayo yameshakidhi vigezo vile vinavyotajwa kwa mujibu wa sheria na kanuni zilizopo.
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Ni lini Serikali itaigawa Kata ya Mwangeza ambayo ina idadi ya watu 32,000 na hivyo huduma ni ngumu sana kwa wananchi?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mtinga ni kwamba, kwa sasa Serikali imeweka kipaumbele katika kuboresha maeneo yale ambayo tayari yameshagawanywa, kwa sababu tutapogawanya Kata mpya maana yake itabidi kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa sekondari nyingine, ambapo nyinyi ni mashahidi Waheshimiwa Wabunge humu ndani, kwa sasa Serikali inapeleka fedha katika kila Halmashauri kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya za sekondari na hivyo tunaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya vya kimkakati kote nchini.

Mheshimiwa Spika, hivyo basi tukimaliza kupeleka vitu vya msingi katika Kata zilizopo ambazo ni mpya zilianzishwa mwaka 2010 na nyingine zilianzishwa mwaka 2015 Serikali ikikamilisha katika kuweka mazingira bora katika maeneo hayo tutaangalia vilevile katika Kata ambayo ameitaja Mheshimiwa Mbunge.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nataka nijue Serikali ina mpango gani wa kupandisha hadhi Barabara ya Bukama - Nyamagaro mpaka Kiangasaga kuwa hadhi ya barabara ya Mkoa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chege kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Barabara Na. 13 ya mwaka 2007, Kifungu cha 11 na Kanuni za Usimamizi wa Barabara ya mwaka 2009 imeelezea wazi namna ya kuomba kupandisha hadhi barabara. Inatakiwa waanze kukaa vikao vyao kule na kupendekeza kwa Kikao cha Bodi ya Barabara ya Mkoa, Mkoa wao wa Mara. Wakishapendekeza pale, baada ya hapo wanawasilisha maombi yale kwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi mwenye dhamana ya ujenzi.

MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Barabara ya Kibaoni – Endabash itapandisha kuwa hadhi ya Mkoa?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama nilivyotoka kusema hapo awali, kwa mujibu wa Sheria ile ya Barabara Na. 13 ya mwaka 2007, kifungu cha 11 na Kanuni za Usimamizi wa Barabara ya Mwaka 2009, zinaelezea ule utaratibu, inatakiwa mchakato uanze kwao wenyewe kwa kupendekeza barabara hiyo kupandishwa hadhi kwenye Bodi ya Barabara ya Mkoa, kisha aandikiwe Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi mwenye dhamana ya barabara na atume timu kwa ajili ya kufanya ukaguzi wa barabara hiyo, ndipo barabara hiyo iweze kupendekezwa na kufikiriwa kupandishwa hadhi.

MHE. ALLY Y. MHATA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu haya ya Serikali, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kituo hiki ninachokieleza ni cha muda mrefu sana. Cha kushangaza kituo hiki kililetewa vifaa, vifaa tiba, vyote vya kituo cha afya ambapo kituo cha afya hakijajengwa. Sasa nauliza vile vifaa walivyovileta walikuwa na malengo gani, yaani vitumike wapi wakati kituo hakijafanyiwa ukarabati? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; vifaa vile sasa hivi vimepelekwa katika sehemu nyingine je, Waziri anawahakikishia vipi wananchi wa ile Tarafa kwamba endapo watafanya ukarabati vifaa vile vitarejeshwa pale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mhata kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza kuhusu hiki kituo cha muda mrefu ambacho kimepelekewa vifaatiba, ni wao wenyewe kama halmashauri ambao wanapanga vifaatiba viende kwenye kituo gani cha afya. Kwa hiyo ina maana wao walifanya maamuzi ya kupeleka vifaatiba hivi vipya katika kituo ambacho ni chakavu.

Mheshimiwa Spika, nimtake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Nanyumbu kutenga fedha kwa ajili ya kuanza kukarabati Kituo hiki cha Afya kongwe cha Nanyumbu wakati bado tunatafuta fedha. Nitakaa na Mheshimiwa Mhata kuona ni namna gani tunaweza tukapata fedha ya kupeleka kukarabati kituo hiki cha afya.

Mheshuimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la vifaa hivi tiba ambavyo vimehamishwa kwenda kwenye Kituo cha Afya cha Tarafa nyingine na kuhama hapa Nanyumbu. Katika mwaka wa fedha wa 2023/2024, Serikali imetenga bajeti ya bilioni 112 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. Ni jitihada kubwa ya mama yetu Samia Suluhu Hassani, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhakikisha kwamba tunapata vifaatiba kuanzia ngazi ya zahanati mpaka vituo vya afya. Nimhakikishie Mheshimiwa Mhata kwamba tutapeleka tena vifaatiba vingine katika Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Je, Serikali ina mpango gani wa kupanua Kituo cha Afya Tandale katika Wilaya ya Kinondoni ili kipate Jengo la Mama na Mtoto na hasa ukiangalia idadi ya watu wanaoishi katika Kata ya Tandale ni wengi sana? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MIKOA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutatuma timu katika kituo hiki cha afya ambacho amekitaja Mheshimiwa Kisangi kufanya tathmini na kuona ukubwa wa eneo uliopo na kama linaweza likahimili kupata majengo mengine. Baada ya tathmini hiyo kufanyika itawasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kutafuta fedha kwa ajili ya kukipanua kituo hiki cha afya.
MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza, lakini pia niishukuru Serikali kwa kuendelea kufanya ukarabati wa barabara hiyo mara kwa mara.

Mheshimiwa Spika, kama alivyoeleza Naibu Waziri kwamba ni kilometa 14 tu za barabara hizo zimewekwa changarawe na maeneo ya Mbinga ni maeneo ya mteremko na milima, naomba kujua sasa Serikali ina mpango gani wa kuendelea kuweka changarawe katika kilometa zilizobaki pamoja na kuhakikisha kwamba mitaro imetengenezwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Barabara ya kutoka Mbinga – Kitanda – Miembeni – Lupilo – Mpepai na Mtua iliharibika sana hasa katika kipindi cha mvua, je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba barabara hiyo inatengenezwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza, hii barabara ambayo ni Kitanda Road yenye urefu jumla ya kilometa 32. Serikali katika mwaka wa fedha 2023/2024 imetenga fedha kwa ajili ya kutengeneza kilometa sita kwa kiwango cha kifusi. Kama nilivyosema awali tayari ilikuwa imeshatengenezwa kilometa 14 na katika mwaka wa fedha unaofuata Serikali itatengeneza kilometa sita na kuweka mifereji katika maeneo ambayo huwa maji yanajaa.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la barabara hii ambayo ameitaja Mheshimiwa Mbunge, nimhakikishie kwamba katika mwaka wa fedha huu unaoanza 2023/2024, Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuweka concrete (zege) katika yale maeneo korofi ya milimani kwa sababu jiografia ya kwa Mheshimiwa Mbunda kule ni ya vilima vingi. Kwa hiyo tutaweka concrete katika maeneo korofi na vilevile nimpe taarifa tu Mheshimiwa Mbunda kwamba ana Barabara hii ya Utili – Mahande ambayo ina kilometa 14 inaenda kuwekewa lami kama ambavyo aliomba yeye kwenye Mradi ule wa Agri–connect.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pia nishukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Serikali ni lini itapeleka fedha kujenga Vituo vya Afya katika Kata ya Kwayi pamoja na Kata ya Makanya? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa Kituo cha Afya Gare kimezungukwa na kata mbili ambazo hazina vituo vya afya. Je, Serikali haioni sasa ipo haja ya kupeleka gari la wagonjwa ili kurahisha huduma kwa wananchi wetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shekilindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza hili kuhusu ujenzi wa Vituo vya Afya vya Kwayi na Makanya, tutakaa na Mheshimiwa Shekilindi kuona katika mwaka wa fedha wa 2023/2024 ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya Ujenzi wa Vituo vya Afya katika Halmashauri yao na tuhakikishe fedha hizi zinakwenda katika walau kituo cha afya kimojawapo, kwa sababu ni mpango wa Serikali wa kujenga vituo vya afya kwenye maeneo ya kimkakati nchini kote ikiwemo Kwayi na Makanya.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la gari ya wagonjwa katika Kituo cha Afya cha Gare. Mheshimiwa Mbunge ni shahidi kwamba muda siyo mrefu kituo hiki cha afya kimetoka kukamilika kwa maana kilipelekewa fedha na tayari kimeshakamilika. Sasa kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi kwamba Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imenunua magari 316 kwa ajili ya kila Halmashauri kupata walau magari mawili ya wagonjwa. Sasa magari haya mawili yatayoelekea kule Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto waelekeze moja katika Kituo hiki cha Afya cha Gare. (Makofi)
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa magari ya wagonjwa yaliyoagizwa na Serikali yanakuja kwa awamu, je, Serikali haioni umuhimu kwa awamu ya kwanza kuanza na Hospitali ya Mji Handeni kwa sababu haina gari la wagonjwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, magari haya yanakuja kwa awamu kama ambovyo nimesema awali na kila Halmashauri ilikuwa tumepanga kupeleka magari mawili na gari lingine la tatu kwa ajili ya monitoring and evaluation katika Halmashauri hizi.

Mheshimiwa Spika, tunapokea ushauri ambao umeutoa wa kuangalia Halmashauri zile ambazo zitakuwa zina eneo dogo lakini lile gari la monitoring and evaluation, bado litakwenda kwa ajili ya kuhakikisha kwamba huduma za afya zinasimamiwa vizuri.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali la Mheshimiwa Kwagilwa, tutakaa naye na kuona katika awamu hii ya kwanza, Hospitali ya Mji pale Handeni inaweza kupata gari pia. (Makofi)
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Swali kwanza, tarehe 29 Septemba, 2022, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI alitutembelea na kati ya miradi aliyokagua, alikagua ujenzi wa barabara za lami Mji wa Katesh aliahidi kwa mwaka ule wa fedha 2022/2023 ameshaongea na Mheshimiwa Rais angeongeza fedha kwa ajili ya kilometa moja na hizo fedha hazikuja kwa mwaka huo wa fedha.

Je, Serikali sasa iko tayari kwa mwaka huu wa fedha 2023/2024 kutupa fedha za kilometa moja?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; mradi huu kidogo hauendi kwa kasi ili kufikia kilometa 10; je, Serikali ina mkakati gani mahususi ili kujenga barabara za lami katika Mji wa Katesh? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Samwel Hhayuma. Swali la kwanza na la pili yote nitayajibu kwa pamoja. Ahadi hizi za viongozi ni lengo la Serikali kuzikamilisha zote kwa wakati na kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge anafahamu tayari asilimia 30 ya ahadi hii ya barabara ya kilometa 10 imeshafikiwa mpaka hivi tunavyozungumza.

Mheshimiwa Spika, tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha ahadi hiyo ya kilometa 10 iliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ahadi pia iliyotolewa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutahakikisha fedha inapopatikana ahadi hizi zinaenda kutekelezwa kwa ujenzi wa barabara hizi za lami.
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa Serikali iliahidi ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami, kilometa tano katika Halmashauri ya Mji wa Tarime. Je, ni lini Serikali itapeleka pesa ili mradi huo uanze?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ili barabara hiyo ya kilometa tano ambayo imeahidiwa na Serikali Tarime iweze kuanza kujengwa, tutakaa na Mheshimiwa Mbunge kuweza kuona ni nini kinaweza kikafanyika na fedha ikipatikana basi ahadi hii iweze kutekelezwa mara moja.

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itakamilisha ahadi ya Mheshimiwa Rais ya ujenzi wa kilometa tano za lami Babati Mjini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, ni lengo la Serikali kuhakikisha ahadi zote za Viongozi wetu Wakuu, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Naibu Waziri Mkuu zinatekelezwa kwa wakati na tutaendelea kuratibu kupitia Ofisi ya TARURA, Mkoa wa Manyara, Ofisi ya TARURA, Wilaya ya Babati, kuona ni kiasi gani kinahitajika ili tuweze kutafuta fedha kuweza kutekeleza ahadi hiyo.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi. Pamoja na kwamba Mheshimiwa Rais alipokuja Liwale ametuahidi kutujengea barabara ya Nangurukuru - Liwale, vilevile alituahidi kutujengea barabara kilometa mbili kwa ajili ya Liwale Mjini. Je, ahadi hiyo itatekelezwa lini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ziara ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mkoani Lindi, ilifanyika muda si mrefu sana kutoka sasa. Tunaendelea kuratibu ahadi zote ambazo zimetolewa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kutafuta fedha kwa ajili ya kupeleka mara moja katika maeneo mbalimbali ambapo ahadi hizi zimetoka ikiwemo kule Liwale kwa Mheshimiwa Kuchauka.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Pamoja na jitihada za Serikali kujenga barabara za lami kwenye miji yetu, kumekuwa na shida kubwa ya ubora wa wakandarasi wanaotekeleza miradi hii hasa maeneo ya pembezoni kama ilivyo Ukerewe. Je, ni nini mkakati wa Serikali kushughulikia changamoto hii? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mkundi. Ni mkakati wa Serikali sasa kupitia Taasisi yetu ya TARURA kuhakikisha tunanunua mitambo na kupeleka maeneo ya pembezoni ikiwemo kule Ukerewe kwa ajili ya kuweza kutengeneza barabara hizi mara kwa mara. Changamoto ambayo inapatikana kwenye maeneo kama Ukerewe, maeneo kama Mafia ni wakandarasi kuweza kupeleka mitambo katika maeneo yale na tayari Serikali imeliona hili na itanunua mitambo yake yenyewe kwa ajili ya kupeleka kwenye maeneo hayo.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kuboresha barabara kwa kiwango cha lami katika Kata za Mikumi na Ruaha ambazo ni Kata za kimkakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itatekeleza ahadi hii ya kuboresha Barabara za Mikumi na Ruaha kwa kiwango cha lami kadri ya upatikanaji wa fedha. Nitakaa na Mheshimiwa Londo kuona ni namna gani ambavyo tunaweza tutaratibu hili kupitia Ofisi ya Meneja wa TARURA Wilaya ya Kilosa na Meneja wa TARURA Mkoa wa Morogoro ili tuweze kutekeleza ahadi hiyo.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, je, ni lini Serikali itaanza kujenga kwa kiwango cha lami Barabara ya kutoka Vwawa – London - Msiya hadi Isarawe, ambayo ni ahadi ya Serikali kwa muda mrefu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tutaanza kutekeleza ahadi hii kadri ya upatikanaji wa fedha, lakini tutakaa tena na Mheshimiwa Mbunge, kuweza kuona ni namna gani tutaratibu hili kupitia Mameneja wetu wa mikoa na hasa Meneja wa Mkoa wa Songwe kuona tunaanzaje kutekeleza ahadi hii ya Serikali.
MHE. DKT. ANGELINE S. L. MABULA: Mheshimiwa Spika, ningependa kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, wamejenga barabara ya kilometa 2.5 ya breweries kwa kiwango cha lami kwa kilometa 1.7 na kimebaki kipande kidogo cha mita 750. Je, ni lini watakamilisha ujenzi huo kwa maana sasa ujenzi umesimama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nitakaa na Mheshimiwa Mabula kuona ni namna gani ambavyo Serikali inaweza ikaliratibu hili na kukamilisha kipande hiki cha barabara ambacho kimesalia kwa kuwasiliana na Meneja wa TARURA, Mkoa wa Mwanza na Meneja wa TARURA, Wilaya ya Ilemela kuona ni kiasi gani kinahitajika ili kuweza kukamilisha ahadi hiyo.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, je, Serikali kwa sababu miradi hii pamoja na mambo mengine itajenga pia vitega uchumi ambavyo vitakuwa vinazisaidia Halmashauri zetu kupata mapato ya ndani. Je, Serikali iko tayari kuharakisha mchakato ule hasa mara baada ya kutangazwa zabuni?

Swali la pili, kwa kuwa Mafinga ni mnufaika wa mradi huu lakini katika tier ya tatu; je, Serikali iko tayari ku-fast track ili ile tier ya tatu na yenyewe iende sambamba na hii tier ya pili kusudi kuwawezesha Wananchi wa Mji wa Mafinga kupata barabara na kujengewa stendi na kujengewa pia mradi mmoja ambao utakuwa ni chanzo cha mapato ya ndani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato Chumi, kwanza hili la Serikali kuharakisha zabuni hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyokwishasema kwenye majibu yangu ya msingi, mara pale ambapo hawa Wakandarasi Washauri watamaliza kufanya usanifu ule mwezi Agosti mwaka huu, mwezi Septemba zabuni zile zitatangazwa ili waweze kupatikana wakandarasi wa kujenga miradi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii si tu kwa barabara tayari usanifu unafanyika pia katika ujenzi wa masoko na ujenzi wa stendi katika maeneo mbalimbali hapa nchini ambayo yamo katika tier 2.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili ni kwamba Mji wa Mafinga kweli upo kwenye tier 3 na mara baada ya usanifu kukamilika kwenye tier 2 mwezi Agosti, sasa usanifu utaanza kwenye tier 3 ambayo ni Miji 18 ikiwemo Halmashauri ya Mji wa Mafinga. (Makofi)
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, Barabara ya kutoka Chemba – Soya – Mwailanje – Zajilwa – Dodoma na Zajilwa ni Jimboni kwake, kwa sasa imeharibika sana, naomba sasa commitment ya Naibu Waziri mwenyewe, ni lini barabara ile itajengwa ili ipitike wakati wowote? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Monni, nikiri kwamba alipotaja Zajilwa na Itiso zimo katika Jimbo langu la Chamwino na barabara hii ya Chemba – Soya – Mwailanje itaanza ukarabati wake mara moja. Ipo katika bajeti ya mwaka huu wa 2023/2024 na tayari Meneja Maganga pamoja na Lamela - Meneja wetu wa Mkoa na Meneja wa TARURA wa Wilaya ya Chemba, wameshakaa na kuona ni namna gani wanaanza utekelezaji wa ujenzi wa barabara hii, hasa katika maeneo ambayo ni korofi.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.

Hali ya barabara za Halmashauri ya Mji wa Ifakara katika Kata 19 ni mbaya sana kutokana na mvua hizi. Naishukuru Serikali kwa kutuletea fedha za kujenga kwa lami barabara za Ifakara Mjini, lakini barabara zimejengwa chini ya kiwango na ni mbovu. Naomba kujua Serikali itachukua hatua gani kwa wakandarasi ambao wamejenga Barabara ya Kibaoni na Ifakara Mjini sokoni ambazo mpaka sasa hivi zimeshaharibika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asenga, naomba nitumie Bunge lako Tukufu hili kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kumwelekeza Meneja wa TARURA Mkoa wa Morogoro kuhakikisha Mkandarasi ambaye alijenga barabara hizi alizozitaja Mheshimiwa Asenga, kama mkataba wake ulikuwa bado haujaisha, aweze kurudi na kurekebisha yale maeneo ambayo tayari yameharibika bado barabara ni mpya kabisa. (Makofi)
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nitumie nafasi hii kuishukuru sana Serikali kwa kutukumbuka watu wa Lupembe kupata barabara ya Agri-Connect. Sasa, hii Barabara ya Lupembe – Kanikelele – Ukalawa ambayo ni Kilometa 18.5 inaishia nyuma kidogo ya Makao Makuu ya Kata ya Ukalawa, umbali kama wa Kilometa moja tu kwenye Makao Makuu ya Kata ya Ukalawa yenyewe.

Je, Serikali haioni haja ya kuongeza hii Kilometa moja ili wafikishe pale Makao Makuu ya Kata ya Ukalawa yenyewe? (Makofi)

Swali langu la pili, ziko barabara kwa mfano ya pale Lupembe Jimboni, kupita kwa Mzee Msambwa kwenda Idamba, kwenda mpaka Mfiriga. Ni lini barabara hii na yenyewe itafanyiwa usanifu na kuanza ujenzi wa lami? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Swalle, swali lake la kwanza hili la kilometa moja hii ya nyongeza katika zile kilometa 18.5 ili kuweza kufika katika Makao Makuu ya Kata ya Ukalawa, nimtoe mashaka Mheshimiwa Swalle kwamba, mradi huu wa Agri-Connect upo katika Mikoa ya Iringa, Njombe, Mbeya pamoja na Songwe. Hivyo basi, katika usanifu wa awamu inayofuata nitahakikisha kwamba na hicho kipande pia kinaweza kumalizika kuweza kufika katika Makao Makuu ya Kata ya Ukalawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la usanifu kwa barabara nyingine ambazo amezitaja. Kama ambavyo nimemjibu swali lake la nyongeza la kwanza, katika hatua inayofuata Serikali itaangalia kwa sababu mradi huu bado upo, ni kweli wanazalisha sana chai katika Jimbo lake kule la Lupembe, Serikali itaangalia pia barabara hizi ambazo zimesalia ili ziweze kuweka katika mipango inayofuata. (Makofi)
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwa ajili ya kuimarisha shughuli za kiuchumi na kijamii, je Serikali ina mpango gani wa kufanya marekebisho katika barabara za Kata ya Nyamoko, Kisangura, Tarafa ya Ngoreme na Tarafa ya Ikorongo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Dkt. Mrimi, kwanza kuhusu hili la marekebisho, kama ambavyo tulizungumza hapa awali katika Bunge hili ambalo linaendelea kwamba, Serikali ilikuwa katika mchakato wa kuhakikisha TARURA inaletewa fedha ya dharura haraka.

Mheshumiwa Mwenyekiti, tathmini imefanyika kote nchini, tathmini ile ilikamilika mwisho wa mwezi Januari mwaka huu wa 2024, ikiwemo kutoka kule kwa Mheshimiwa Mrimi, hivyo basi fedha ile ambayo itapatikana itaenda katika maeneo yale kuweza kuanza kurekebisha barabara zote korofi, ikiwemo kule Jimboni kwa Mheshimiwa Mrimi.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kupitia Mradi wa Agri-Connect tulikuwa tumeomba Kilometa 15 ambazo zimo tayari kwenye bajeti ya Agri-Connect zijengwe kutoka Kilolo hadi Kidabaga ambapo ndiko shamba la chai lilipo. MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kupitia Mradi wa Agri-Connect tulikuwa tumeomba Kilometa 15 ambazo zimo tayari kwenye bajeti ya Agri-Connect zijengwe kutoka Kilolo hadi Kidabaga ambapo ndiko shamba la chai lilipo.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama anavyosema Mheshimiwa Nyamoga kwamba, mradi huu ulipoanza (Agri-Connect) Mkoa wa Iringa ulikuwa ni Mkoa wa kwanza kabisa kuanza utekelezaji. Vilevile, niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, Mheshimiwa Nyamoga alikuwa beneficiary wa kwanza kabisa wa ujenzi wa barabara hizi za Agri-Connect katika Jimbo lake. Hivyo basi, Serikali pia italiangalia hili la barabara ya Kilolo kwenda Kidabaga ambapo kuna uzalishaji mkubwa wa chai katika awamu ambayo inafuata kama nilivyomjibu Mheshimiwa Swalle ili kuziweka katika mpango na barabara hizi ziweze kujengwa. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, Barabara ya Orbesh ambayo inatoka kwenye Kata yako kuja Bashneti na kwenda mpaka Haiderere iliahidiwa na Katibu Mkuu kujengwa na sasa hivi hali ni mbaya.

Je, ni lini TARURA itakwenda kujenga barabara ile ili wakulima wapate nafuu ya kuleta mazao yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikia Mheshimiwa Flatei akiuliza kwamba barabara hii inaanzia kwenye, Jimboni kwako Kata yako ya Orbesh na kuelekea Bashneti ambako anatoka yeye Mheshimiwa Flatei. Nitakaa na Mheshimiwa Flatei ili kuona ni namna gani TARURA, Eng. Bwaya, Meneja TARURA Mkoa wa Manyara pamoja na timu yake walivyojipanga katika kuanza utekelezaji wa matengenezo ya barabara hii mara moja. (Kicheko/Makofi)
MHE. SANTIEL E. KIRUMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali, licha ya hivyo nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; mradi huu umekuwa ukikabiliwa na changamoto ndogo ndogo ambazo ni ukosefu wa miundombinu, maji safi na salama, ongezeko la shule mpya nyingi ambazo haziko kwenye mradi, zimepelekea watoto wetu wanapokuwa shuleni kukosa chakula.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Wadau hawa wa Sekta ya Elimu wameelekeza watoto wanapokuwa shuleni wafundishwe namna bora ya kupanda mbogamboga na kupanda matunda ili yaweze kuwasaidia kupata mlo bora ambao utawatoa wasiweze kushindwa kupata udumavu, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Santiel Kirumba; la kwanza, hili la ukosefu wa miundombinu mbalimbali hasa katika shule mpya ambazo zimejengwa hivi karibuni miundombinu kama maji na kadhalika. Tunashirikiana na Wizara ya Maji, Wizara ya Nishati na kadhalika katika kuhakikisha miundombinu muhimu inafika katika Taasisi zetu za Serikali kwenye maeneo mbalimbali hapa nchini ikiwemo shule na tutaendelea kufanya hivyo ili kuhakikisha huduma bora inatolewa katika shule zetu zote hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili; Kuna club mbalimbali katika shule zetu katika kuhakikisha kwamba upandaji wa mbogamboga unafanyika na kuendelea kufundishwa kwa wanafunzi wetu katika shule zile na Serikali itaendelea kutilia mkazo uwepo wa club hizi. Hivyo basi, nitumie nafasi hii kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuwaelekeza ma-REO wote na ma-DEO wote nchini (Maafisa Elimu Mkoa na Maafisa Elimu Wilaya) kuhakikisha kwamba club hizi za upandaji wa mbogamboga zinaendelezwa katika shule zetu za sekondari na shule zetu za msingi nchini kote.
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Katika korongo lile zipo nyumba ambazo ziko jirani sana, wananchi na wakazi wa Mtaa ule wangependa kujua wale wananchi waliopo karibu na korongo zile kaya, je, Serikali ina mpango gani, watawafidia au itakuwa namna gani?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; korongo hili ni hatarishi sana; je, ni lini hasa Serikali itaanza ujenzi wa korongo hili? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kembaki; la kwanza hili la nyumba zilizopo jirani na korongo hili. Kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi kwamba Serikali itatenga fedha katika mwaka wa fedha 2024/2025 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa daraja hili kwenye korongo.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nichukue nafasi hii mbele ya Bunge lako Tukufu kumwelekeza Meneja wa TARURA, Mkoa wa Mara kwa kushirikiana na Meneja wa TARURA, Wilaya ya Tarime kwenda kufanya tathmini katika eneo hili na kuona hizi nyumba ambazo Mheshimiwa Kembaki amezitaja zipo umbali gani kutoka kwenye road reserve ambayo imewekwa na kisha kuwasilisha taarifa hii TARURA Makao Makuu.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, nirejee tena majibu yangu ya msingi kwamba Serikali itatenga fedha mwaka wa fedha 2024/2025 na fedha hii itakapotengwa ndipo kazi hii itatangazwa na kuanza kujengwa daraja hili katika Bonde hili la Mto Starehe.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa wananchi wamejitolea kwa kiwango kikubwa sana katika ujenzi wa maboma haya na waliahidiwa kwamba Serikali itakamilisha na maboma hayo ni mengi sana, je, Serikali haioni umuhimu wa kutenga bajeti maalum ili kukamilisha majengo hayo kuwaunga mkono wananchi hawa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa katika maeneo mengi sasa hivi Serikali imekuwa ikipeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa madarasa mapya, ni kwa nini Serikali isipeleke fedha kukamilisha haya madarasa ambayo yameshaanzishwa na wananchi badala ya kuanza madarasa mapya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hasunga, la kwanza kwa nini isitengwe bajeti maalum kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma haya?

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, Serikali imekuwa ikishirikiana na wadau mbalimbali na wananchi wenyewe katika kuhakikisha kwamba maboma yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi nchini kote yanakamilishwa. Hivi sasa Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan ipo katika mchakato wa kutafuta fedha kwa ajili ya kwenda kuunga mkono jitihada za wananchi nchini kote waliojenga maboma yao ikiwemo kule jimboni kwa Mheshimiwa Hasunga ambapo kuna maboma zaidi ya elfu moja na mia tano kwa ajili ya kwenda kuyakamilisha.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili; kwa nini hizi fedha zinazokwenda sasa kwenye kujenga madarasa, kwenye kujenga shule mpya zisiende kwa ajili ya kumalizia yale maboma?

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikijenga shule na madarasa kupitia miradi mbalimbali, ambayo ni vigezo vya miradi ile kuhakikisha kwamba inajenga madarasa mapya inajenga shule mpya na kupimwa kulingana na matokeo yale yanayotokana na ujenzi ili tuweze kupata fedha nyingine nyingi zaidi kwa ajili ya kujenga shule nyingine nyingi na madarasa mengine mengi.

Mheshimiwa Spika, nirejee katika majibu yangu ya swali lake la nyongeza la kwanza, Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan ipo katika mchakato wa kutafuta fedha kwa ajili ya kuunga mkono jitihada za wananchi nchini kote waliojenga maboma ya madarasa. Vilevile kuna fedha ile ya maendeleo ambayo Halmashauri inatakiwa kutenga na ndiyo kazi yake hii, Wakurugenzi kuhakikisha kwamba wanaunga mkono jitihada za wananchi kwa kutumia fedha ile ya maendeleo kwenye halmashauri zao.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Shule za msingi Kwai, Kweboma zimechoka mno; je, ni lini Serikali itapeleka fedha za ukarabati katika shule hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali hii ya Awamu ya Sita ilitenga zaidi ya bilioni 230 kote nchini kwa ajili ya ukarabati wa shule za msingi zilizochoka na ujenzi wa shule mpya za msingi, zikiwemo nyingine kule Jimboni kwa Mheshimiwa Shekilindi. Hizi shule alizozitaja za Kwai na kwingineko Serikali itaendelea kutafuta fedha na kadri ya upatikanaji wa fedha itapeleka fedha kwa ajili ya ukarabati wa shule hizi.
MHE. MARTHA F. MARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kuishukuru Serikali kwa kutenga bilioni tano kwa ajili ya ununuzi wa vifaa hivi, lakini, pamoja na jitihada za Serikali kuhakikisha kwamba inaboresha elimu nchini hususan elimu ya sekondari kwa upande wa sayansi. Nidhahiri kabisa katika Mkoa wetu wa Katavi bado kuna upungufu mkubwa sana wa walimu hususan walimu wa kike na walimu wa sayansi. (Makofi)

Je, Serikali inatoa tamko gani kuhusiana na Mkoa wa Katavi ambao una upungufu mkubwa, ikiwepo shule ya Mwangaza ina mwalimu mmoja tu wa sayansi na Shule ya Rungwa ambayo ina zaidi ya wanafunzi 1500 lakini haina kabisa walimu wa sayansi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Je, Serikali inaongeza jitihada gani kuhakikisha kwamba ina boresha elimu ya sayansi hususan kuhakikisha watoto wa kike wanakwenda kuongezeka na kupata elimu ya sayansi nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Martha Mariki na hili la kwanza la upungufu wa walimu Mkoani Katavi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan imeweka kipaumbele katika kuhakikisha inaondoa upungufu wa walimu katika maeneo yote nchini ikiwemo Mkoa wa Katavi; na katika Mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali iliajiri jumla ya walimu wa sayansi 6,949.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka huu ambayo inatekelezwa ya 2023/2024 Serikali imetenga ajira kwa ajili ya kupunguza upungufu wa walimu wa sayansi. Tunaendelea kuratibu na wenzetu wa Ofisi ya Rais, Utumishii li kuweza kupata vibali vya kuweza kuajiri walimu hao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nijibu swali la pili la Mheshimiwa Martha Mariki linalohusu jitihada za Serikali; Serikali hii, hasa utashi wa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, alihakikisha kwamba tunakwenda kujenga shule za wasichana za sayansi katika kila mkoa. Awamu ya kwanza, Mheshimiwa Rais alitoa fedha kwa ajili ya kujenga shule kumi kwenye mikoa kumi na awamu ya pili kuna fedha bilioni 48 imekwenda kwenye mikoa 16. Hii yote ni kuhakikisha kwamba watoto wa kike wanapata elimu iliyobora na elimu ya sayansi katika mikoa yote. Hivyo, awamu ya kwanza jumla ilienda bilioni 40 na awamu ya pili bilioni 48.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Naipongeza Serikali kwa majibu mazuri. Pamoja na hayo, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuweza kujenga shule mpya katika Jimbo la Kibiti?

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, naomba kuuliza: Serikali ina mpango gani wa dharura wa kuweza kukarabati Shule ya Msingi ya Mchukwi pamoja na Shule ya Msingi ya Nyanjati iliyopo katika Kata ya Mahenge?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Twaha Mpembenwe, hili la kwanza la mpango wa Serikali kujenga shule mpya katika Wilaya ya Kibiti, nimtaarifu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kupitia Mradi wa Boost, imejenga shule mbili mpya katika Jimbo lake la Kibiti. Jumla ya shilingi milioni 821 zilipelekwa katika Halmashauri ya Kibiti kujenga shule hizo ambazo ipo ya Itonga Kata ya Bungu na vilevile kuna shule inaitwa Mpembenwe ambayo imejengwa, ilipelekewa shilingi milioni 306 kwa ajili ya ujenzi wa shule hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakwenda kwenye swali la pili sasa. Mheshimiwa Twaha Mpembenwe amekuwa akiifuatilia sana juu ya ujenzi wa shule hizi za Mchukwa na nyingineyo ambayo imetajwa. Namtoa mashaka, Serikali hii itatafuta fedha na kuweza kupeleka kwa ajili ya ukarabati wa maeneo haya ambayo ameyataja.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, kule Kibiti kuna shule mpya ya Sekondari ambayo sasa fedha imepelekwa kwa jitihada zake Mheshimiwa Mbunge na Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, alitoa fedha kwa ajili ya kujenga shule katika Kata ya Kibiti.
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Kwenye Jimbo la Igunga, kuna changamoto kubwa sana kwenye Shule ya Msingi Butamisuzi Kata ya Mbutu na Mwajinjama. Tunaishukuru Serikali, Shule ya Msingi ya Buta wametupatia fedha kuboresha madarasa chakavu. Imebaki changamoto kwenye Shule ya Msingi Mwajinjama iliyopo Kata ya Mtungulu: Je, ni lini Serikali mtapeleka fedha kwa ajili ya kutusaidia kuboresha madarasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ngassa, kwa sasa kuna tathmini ambayo ilikuwa inafanyika na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kupitia kwa Maafisa Elimu wetu wa Msingi katika Halmashauri zote hapa nchini ili kuweza kupata taarifa sahihi ya idadi ya madarasa yanayohitajika ili fedha iweze kutafutwa na kupelekwa. Vilevile kule kwa Mheshimiwa Ngassa, itafanyika hivyo.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kutokana na uchakavu wa majengo kwenye shule za msingi kule Makete, Waratibu Kata Elimu leo wamekuja kutoka Makete wako hapa wanataka kujua ni lini Serikali itapeleka fedha za kukarabati Shule ya Msingi Lupalilo, Shule ya Msingi Ikungula, Shule ya Msingi Iwawa na Shule ya Msingi Kijombo? Waratibu wangu wa Elimu Kata wako hapa leo, wanataka waondoke na majibu ya Serikali. Ni lini fedha zitatoka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, fedha itapelekwa na Serikali katika Shule za Msingi Lupalilo, Ikungula na maeneo mengine ambayo ameyataja Mheshimiwa Sanga hapa kadri ya upatikanaji wa fedha hizo. Kama nilivyomjibu Mheshimiwa Ngassa, kwa hiyo na tathmini inayofanyika hivi sasa na baada ya tathmini hiyo kukamilika, Serikali itatafuta fedha hizo na kuweza kupeleka huko.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, kuna shule za msingi ambazo ni kongwe zimejengwa miaka ya 1960 na 1970 ambazo hazifai kabisa kukarabatiwa bali inabidi Serikali iende na mkakati wa kuzijenga upya. Mathalan Shule ya Msingi Nyabilongo, Kikomori na Kiongera zilizopo Kata ya Susuni, Jimbo la Tarime Vijijini. Ni shule ambazo ni hatarishi hata kwa wanafunzi wanaposoma katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba inapeleka fedha kwa uharaka ili hizi shule kongwe ziweze kujengwa na kuweza kunusuru maisha ya wanafunzi wale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Matiko, kwanza niliarifu Bunge lako Tukufu kwamba katika kipindi hiki cha uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ndiyo kipindi ambacho Serikali hii ya Awamu ya Sita imewekeza zaidi ya shilingi bilioni 230 katika ujenzi wa shule mpya na ukarabati wa madarasa kwenye Elimu Msingi kuliko wakati mwingine wowote ule. Hivyo basi, nimtoe mashaka Mheshimiwa Matiko, shule hizi alizozitaja tutaziweka katika mpango na kuona ni namna gani fedha inazifikia kwa ajili ya ukarabati wa madarasa na ujenzi wa majengo mapya katika shule hizi. (Makofi)
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Tunaipongeza Serikali kwa jitihada kubwa ya ukarabati na ujenzi wa shule mpya hapa nchini. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kujenga nyumba za walimu ambazo hazifai kabisa katika hizo shule kongwe nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikimjibu Mheshimiwa Issaay, kutoka mwaka 2021 hadi 2023, Serikali hii imejenga zaidi ya nyumba 562 za walimu kote nchini ambapo imetumika zaidi ya shilingi bilioni 56,325,000,000/= kwa ajili ya ujenzi wa nyumba hizi za walimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimtoe mashaka Mheshimiwa Mbunge, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa nyumba zaidi za walimu kama ambavyo umeona jitihada hizi zinafanyika kwa sasa.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru kwa majibu, lakini lengo la swali langu lilikuwa ni Serikali kuingia ubia na TBA, kwanza halmashauri watenge maeneo ya makazi, waingie mkataba na TBA, wajenge nyumba za gharama nafuu, ambazo walimu watagawiwa kwa mkataba ambao wataingia nayo. Kwa maana ya kwamba zile nyumba ambazo watamiliki wao hata kama ukistaafu itakuwa nyumba za kuanzia maisha sio nyumba za shule ambazo zinamilikiwa na halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu je, Serikali haioni namna bora ya kuwasaidia walimu hasa wale wastaafu wanapotangatanga baada ya kukosa makazi na umri wao wa kuishi nao unapungua kwa sababu ya stress za kukosa makazi. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwajengea nyumba walimu hawa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kuchauka, kwanza nikiri tunapokea mawazo na maoni ya Mheshimiwa Kuchauka aliyoyatoa na kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi ya kwamba itabidi tukae na walimu wenyewe kwa sababu jambo lenyewe ni la hiari la wao kuweza kuchangia au kukatwa katika mishahara yao kulipia nyumba zile ambazo zitakuwa zimejengwa kwa ajili yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kukubaliana nao ndipo basi Serikali itakaa ubia na TBA, National Housing, Watumishi Housing, taasisi nyingi nyingine na Serikali kwa ajili ya kuona ni namna gani nyumba hizi zinaweza zikajengwa kwa ajili ya kuweza kuwauzia walimu.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Swali la kwanza; kwa kuwa mchakato huu wa utoaji wa mikopo ya asilimia 10 umesitishwa ni mrefu sasa, na kwa kuwa akina mama bado wanahangaika na mikopo ya kausha damu huko mitaani. Je, ni lini sasa Serikali itaanza tena zoezi hili la utoaji mikopo ili kuondoa adha kwa akina mama wa Mkoa wa Tanga na Watanzania kwa ujumla? (Makofi)

Swali la pili; kwa kuwa Halmashauri huwa zinatenga mikopo ya asilimia 10 kutoka kwenye mapato ya ndani kila robo ya mwaka, na kwa kuwa mchakato huu pia umesimama kwa muda mrefu. Je, Serikali inahakikisha Halmashauri zinaendelea kutenga fedha za asilimia 10 ili wakianza mchakato huu akina mama waweze kupatiwa mikopo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zodo. Swali lake la kwanza juu ya mchakato kusitishwa, ni kweli mchakato huu ulisitishwa baada ya Mheshimiwa Rais kupokea ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na kuonesha kwamba kuna fedha nyingi ambazo zilikuwa hazijarejeshwa za mikopo hii, hivyo maelekezo ya Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Dkt. Samia Suluhu Hassah yalikuwa, yafanyike mapitio sasa ya namna ya mikopo hii inavyotolewa.

Mheshimiwa Spika, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa aliunda timu, ambayo ilifanya mapitio ya namna ya mikopo inavyotolewa, timu ile ikawasilisha taarifa kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na sasa mapendekezo yale yamewasilishwa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hivi tunavyozungumza Waziri wa nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, amekumbushia kwa Mheshimiwa Rais ili jambo hili liweze kurudi sasa na kuanza utekelezaji wake. Kama kuna Sheria ya kubadilika iletwe mbele ya Bunge hapa ili sheria hizo ziweze kubadilika.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la fedha hizi je bado hutengwa. Ndiyo, fedha hizi bado zinatengwa kwa sababu, kwa mujibu wa Sheria ile ya Fedha ya Serikali za Mitaa, fedha hii iko ring fenced na inaendelea kutengwa. Pale mikopo hii itakapoanza kutolewa tena basi fedha hii ipo, nawatoa mashaka hayo. Ahsante sana.
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naishukuru na kuipongeza Serikali yetu ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutupatia fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya elimu. Wiki iliyopita walitupatia shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu, Shule ya Sekondari ya Igurubi ilianzishwa mwaka 2000 na sasa ina miaka zaidi ya 20. Ina madarasa 19 lakini yanayotumika ni tisa tu, madarasa kumi yamebaki, ambayo inaongeza idadi ya miundombinu ya majengo ambayo tunaweza tukaibadilisha ikawa mabweni na mabwalo. Je, nini kauli ya Serikali katika kuhakikisha tunapata kidato cha tano na sita kwenye Shule ya Sekondari ya Igurubi? Aahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, najibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ngassa, kwanza naanza kwa kumpongeza yeye Mheshimiwa Ngassa kwa kuweza kufuatilia sana suala hili ya Shule ya Igurubi. Amekuja ofisini mara kadhaa kwa ajili ya kufuatilia iweze kupandishwa hadhi na kuwa shule ya A level.

Mheshimiwa Naibu Spika, shule hii kama nilivyokwishasema kwenye majibu yangu ya msingi, tayari Serikali imeshapeleka fedha nyingi kwa ajili ya miundombinu mingine ya madarasa. Tutaendelea kutafuta fedha kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Igunga kwa ajili ya kujenga miundombinu inayohitajika kwa ajili ya kusajiliwa. Baada ya miundombinu hiyo kuweza kujengwa tutawasiliana na wenzetu wa Wizara ya Elimu kwa ajili ya kuweza kuipandisha hadhi shule hii na kuwa ya kidato cha tano na sita. (Makofi)
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Kwa kuwa, shughuli nyingi za maendeleo zinazofanyika vijijini zinafanywa na wananchi wenyewe na vijiji vingi ni vikubwa kiasi kwamba kumekuwa na mivutano. Serikali haioni kwamba ni wakati sahihi sasa angalau wa kufanya mgawanyo wa vijiji ili shughuli za maendeleo vijijini ziendelee kufanyika vizuri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mnzava, mchakato wa kuanzisha maeneo ya utawala ya Mikoa, Wilaya, Tarafa, Kata na Vijiji ni mchakato unaofanywa kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na taratibu zilizopo. Wao wanatakiwa waanzishe wenyewe mchakato ule kupitia vikao vyao na kama ni katika ngazi ya Wilaya wanalipitisha kwenye DCC kisha inakwenda Mkoani kwenye RCC na ndipo mapendekezo yanaletwa.

Mheshimiwa Spika, lakini kama nilivyojibu kwenye majibu yangu ya msingi, kwa sasa Serikali imeweka kipaumbele katika kuyaendeleza yale maeneo ambayo ni mapya ya kiutawala.
MHE. MWITA. M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mwaka jana Serikali ilitoa maelekezo kwenye Majimbo yetu na Mikoa yetu na wakapeleka masharti wapendekeze maeneo ambayo wanataka kuongeza vitongoji, vijiji na Kata. Kwa hiyo, Kata mbalimbali zilikaa na kutumaini kwamba watapewa maeneo hayo waliyoomba.

Kwa sasa, nini kauli ya Serikali juu ya maelekezo ambayo waliyatoa katika maeneo yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Waitara. Ni kama kwenye majibu yangu ya msingi kwamba kwa sasa, Serikali imeweka kipaumbele katika kuhakikisha yale maeneo mapya ya kiutawala yaliyopo yanapata miundombinu ambayo ni stahiki kwa maeneo yale.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni tumeona Halmashauri nyingi zimekwenda katika maeneo yao ya kiutawala na Serikali imepeleka fedha nyingi katika ujenzi wa miundombinu ikiwemo ofisi za Halmashauri, ofisi za Wakuu wa Wilaya kwenye Wilaya mpya na kadhalika. Kwa hiyo, mpaka pale ambapo Serikali itakapokuwa imekamilisha ujenzi wa miundombinu ya msingi katika maeneo yaliyopo sasa ndipo itaendelea na mchakato wa kuongeza maeneo mengine.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo tulifuata taratibu zote, vikao vya Kata vilifanyika, Halmashauri (DCC na RCC) kuomba kugawanyika kwa vijiji na Kata: Je, Serikali wakati ukifika mtatupatia kipaumbele?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Namtumbo ni mojawapo ya maeneo ambayo yameshakamilisha mchakato mzima wa kuomba maeneo mapya ya kiutawala kama ilivyo katika Halmashauri na Wilaya nyingine na Mikoa mingine hapa nchini; na pale Serikali itakapoanza mgawanyo, basi kipaumbele pia kitawekwa kwa wenzetu wa kule Namtumbo.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Jimbo la Chemba lina Kata tano…

SPIKA: Simamisha kisemeo vizuri.

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, Jimbo la Chemba lina Kata tano ambazo zina vijiji zaidi ya vinane, hivyo imekuwa ni kazi kubwa sana kwa Watendaji wa Kata kufanya kazi. Nini sasa msimamo wa Serikali kugawa Kata hizo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Monni, nirejee katika majibu yangu ya msingi, pale ambapo miundombinu itajengwa katika maeneo ya kiutawala yaliyopo sasa ya kukidhi mahitaji yote ya wananchi katika maeneo hayo, ndipo Serikali itaenda katika mchakato wa kugawa maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, ni kwa sababu unapogawa kata, maana yake inabidi shule, zahanati na vituo vya afya na huduma nyinginezo ziweze kujengwa.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa sote ni mashuhuda, Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan ameweka fedha nyingi katika kuhakikisha vituo vya afya vinajengwa, shule mpya zinajengwa katika kata ambazo zilikuwa hazina shule za sekondari. Kwa hiyo, mpaka pale mchakato huu utakapokamilika ndipo Serikali itaanzisha maeneo mapya ya kiutawala.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naishukuru Serikali kwa kazi ambayo imefanyika kwenye barabara hii.

Nina maswali mawili ya nyongeza; swali la kwanza; barabara hii ni muhimu sana, barabara hii pamoja na barabara za Kwetonge – Donge - Kizara, barabara ya Mombo - Mzeri, barabara ya Makuni - Zege Mpakani zimeunganisha Wilaya ya Korogwe na Wilaya ya jirani.

Ni lini Serikali itatimiza ile ahadi yake ya kuzipandisha hadhi barabara hizi kuwa kwenye hadhi ya barabara za mkoa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, barabara nyingi zinazosimamiwa na TARURA ni za changarawe na udongo na zinahitaji matengenezo ya mara kwa mara. Serikali haioni sasa ni wakati sahihi kununua vifaa kwa TARURA kila mkoa ili matengenezo madogo madogo ya barabara yafanywe na TARURA wenyewe kwa kutumia wataalam wao wa ndani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, najibu maswali mawili ya Mheshimiwa Timotheo Mnzava; la kwanza hili la barabara hii kupandishwa hadhi, barabara ambazo ametaja Mheshimiwa Mnzava taratibu ziko wazi kwa mujibu wa sheria. Vikao vile vya kisheria lazima vikae, wanaanza kwanza wao kwenye DCC vinatoka vinakwenda kwenye Bodi ya Barabara ya Mkoa na kisha wanamuandikia Waziri mwenye dhamana ya barabara hizi za mikoa yaani TANROADS kuomba kupandisha hadhi. Tutafuatilia kuona maombi hayo yamefikia wapi kwa ajili ya kuweza kupandisha hadhi barabara hii kwa wenzetu wa Wizara ya Ujenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la mitambo, TARURA kuweza kununua mitambo. Tayari mkakati wa Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ni kutoa fedha kwa wenzetu wa taasisi ya TARURA kuweza kununua mitambo hasa katika maeneo ambapo upatikanaji wa mitambo ni mgumu. Tayari mpango huu umeanza kufanya kazi kule visiwani Mafia. Maeneo mengine ni pembezoni mwa nchi yetu ambapo tayari wameanza na kadri ya upatikanaji wa fedha tutazidi kufanya hivyo ili mitambo ile iweze kutumika wakati wa dharura.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara ya Holili - Tarakea kwa kuwa kumekuwa na msongamano mkubwa sana katika barabara ya Rombo ambayo inabeba malori mengi, inachukua malori yanayopeleka mchanga katika nchi ya Kenya? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zuena Bushiri, Barabara hii ya Holili – Tarakea, tutakaa na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi kuona ni namna gani ambavyo bajeti imetengwa kwa ajili ya kupanua barabara hii ili iweze kupitika wakati wote.
BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Barabara ya Bukama – Salamakati – Mkomalilo, taarifa zote za kuipandisha kutoka kwenye Halmashauri, kutoka TARURA kwenda TANROADS zimeshafanyika. Je, ni lini sasa itakwenda TANROADS?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere la Barabara hii ya Nkama – Nkomalilo kupandishwa hadhi. Taratibu za kisheria zipo wazi, wao wamekamilisha taratibu zile kwenye ngazi yao ya Halmashauri na sasa lipo katika Wizara ya Ujenzi kwa Waziri mwenye dhamana wa kuweza kupandisha hadhi hii. Tutalifuatilia kwa wenzetu wa Wizara ya Ujenzi na kuona limefikia wapi na ikiwezekana timu iweze kwenda kuweza kukamilisha taratibu hizo.
MHE. JOSEPHINE T. CHAGULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, shule za sekondari za kata zimeonesha mafanikio makubwa sana katika ufaulu, lakini tatizo lililopo ni kufeli kwa somo la hesabu na mwanafunzi anapopata F ya hesabu inakuwa imemuharibia kabisa kombi yake.

Je, Serikali ina mpango gani sasa wa haraka wa kupeleka walimu wa somo la hesabu katika shule zetu hizi za kata, ili tuweze kupunguza au kutoa F hizo zinazojitokeza kwa watoto wetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali la pili, kumekuwa na changamoto kubwa kwa walimu wetu wa shule za msingi na sekondari kupata uhamisho kuwafuata wenza wao na hasa hawa ajira mpya. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuwapangia moja kwa moja walimu hawa kuwafuata wenza wao kwa vile wana vyeti vya ndoa, ili tuweze kutoa usumbufu huo wanaoupata walimu wetu hawa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Chagula; la kwanza hili juu ya kuajiri walimu wa hesabu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, Serikali hivi karibuni itatangaza ajira za walimu. Na katika ajira hizo kipaumbele kitakuwa kwa walimu wa sayansi na hisabati ambao wataajiriwa. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wengine humu ndani, kuwa na subira pale ajira hizi zitakapotangazwa basi walimu hawa wa hesabu na sayansi wataajriwa na kwenda katika halmashauri mbalimbali hapa nchini, ili kuongeza nguvu katika shule zetu za kata ambazo Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amewekeza fedha nyingi zaidi ya bilioni 219 katika kuhakikisha kuna shule mpya za sekondari kwenye kata ambazo zilikuwa bado hazina shule hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la uhamisho wa kuweza kuwafuata wenza; Serikali hutoa ajira kulingana na upungufu uliopo. Tathmini hufanyika nchi nzima kuangalia maeneo mbalimbali ambayo yana upungufu wa walimu kisha ndipo kibali hutolewa kwa ajili ya kuajiri wale walimu kwenda kuziba yale mapengo. Kwa hiyo, mtu anapoomba ajira anaenda kwenye eneo kuziba pengo ni lazima atumikie kwanza mwaka mmoja kwa ajili ya kuweza kuthibitishwa kazini akiwa katika eneo lile ambalo amepangiwa. Baada ya kuthibitishwa kazini baada ya ule mwaka mmoja anatakiwa aendelee kuwepo kwenye kile kituo cha kazi kwa miaka mingine isiyopungua miwili ambayo jumla inakuwa ni miaka mitatu ndipo aweze kuona ni namna gani anahama katika kituo kile na kwenda kituo kingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ajira hizi si kwamba, ni njia tu ya kuingilia kwenye ajira ya Serikali halafu aweze kuhama na kuhamia maeneo mengine na mara nyingi wanaotaka kuhama huwa wanahamia kwenye majiji na Manispaa, wale waliokuwa pembezoni huwa mara nyingi wanataka kuhama. Sasa tukisema mtu tu akishapata check number aweze kuomba uhamisho na kumfuata mwenza wake ina maana maeneo ya pembezoni mwa nchi yetu kutaendelea kuwa na upungufu wa idadi ya walimu ambao wanahitajika. (Makofi)
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa, mahitaji ya walimu wa shule za msingi katika Jimbo la Babati Vijijini ni 2,349 na waliopo ni 1,379 hivyo kuwa na upungufu wa walimu 970. Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza walimu katika shule za msingi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sillo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka wa fedha 2021/2022 na 2022/2023 Serikali iliajiri walimu na katika ajira hizo Jimboni kwa Mheshimiwa Sillo nako walipata walimu wapya, walienda katika shule za msingi na shule za sekondari. Kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, Serikali inaendelea kutoa ajira mpya na hivi karibuni zitatangazwa na baada ya kupatikana hawa waajiriwa wapya tutaweka kipaumbele vilevile kule kwa Mheshimiwa Sillo.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naishukuru sana Serikali yangu kwa kutujengea shule nyingi za sekondari na msingi katika Mkoa wa Simiyu, lakini kuna upungufu mkubwa wa walimu. Je, ni lini Serikali italeta walimu wa kutosha katika Mkoa wetu wa Simiyu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itapeleka walimu zaidi katika Mkoa wa Simiyu pale ambapo ajira hizi ambazo nimesema zitatangazwa hivi karibuni zitakamilika mchakato wake na wao wenyewe katika Mkoa wa Simiyu watapata mgawo wa walimu hao wapya.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Kwanza niipongeze Serikali kwa kuendelea kupunguza upungufu wa walimu katika Wilaya ya Nyang’hwale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, uko tayari kumuelekeza Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya ya Nyang’hwale azipitie shule zote zikiwemo za sekondari na msingi kuangalia uwiano wa walimu ‘ke’ na ‘me’ kwa sababu, kuna baadhi ya shule za msingi zina wanawake peke yake na baadhi ya shule za msingi zina wanaume peke yake, ikiwemo Shule ya Msingi ya Mama Samia.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Amar:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipo tayari kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale kuweza kufanya tathmini hiyo na ninaomba kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuchukua nafasi hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Nyang’hwale kuanza kufanya tathmini hii, kama alivyoshauri Mheshimiwa Amar na kuona ni namna gani anafanya msawazo wa ikama ndani ya halmashauri yake katika walimu. (Makofi)
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, katika Wilaya ya Hai tunaishukuru Serikali imetujengea shule tatu mpya kwa hivyo, kuongeza mahitaji ya watumishi pamoja na kujengewa vituo vitano vya afya. Je, ni lini sasa Serikali itatuletea watumishi kwenye maeneo haya ya elimu na afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirejea majibu yangu ya msingi, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali italeta watumishi hawa, hasa walimu katika hii ajira mpya ambayo itatangazwa hivi karibuni, basi Wilayani Hai nako mtapata mgawo katika walimu hao.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante; je, Serikali ina mpango gani mahususi wa kupeleka walimu katika maeneo ya pembezoni, ikiwa ni pamoja na Mkoa wa Kigoma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kufanya tathmini ya upungufu wa walimu waliopo kote nchini, yakiwemo maeneo ya pembezoni, kama vile Mkoa wa Kigoma na kwenye ajira hizi mpya ambazo zitatolewa Serikali itaendelea kuweka kipaumbele hasa katika maeneo ya pembezoni ambayo yana uhitaji mkubwa wa walimu, ikiwemo Mkoani Kigoma.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uhamisho kwa walimu wanawake au wanaume kufuata wenza wao ni suala muhimu sana kwa ajili ya maadili, lakini pia, kulinda ndoa za walimu hawa. Mnaonaje Serikali kuhakikisha wale ambao wamefunga ndoa kweli, waende wakafuate wenza wao kuepukana na matatizo na maambukizi na mambo mengine kama hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilipokuwa nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chagula, utumishi wa umma unaongozwa kwa sheria, taratibu na kanuni na miongozo mbalimbali iliyomo katika utumishi wa umma. Na mtu anapokuwa ameajiriwa katika utumishi wa umma anafuata zile sheria, taratibu na kanuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria inasema ajira mpya atafanya kazi kwa mwaka mmoja kisha atafanyiwa assessment na kuthibitishwa kazini. Baada ya kuthibitishwa kazini ni lazima atumikie nafasi kwa muda usiopungua miaka miwili katika lile eneo ambalo yupo, baada ya hapo anaruhusiwa kuomba uhamisho kwenda katika eneo lolote la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini hilo linategemea pia na uwepo wa nafasi kule anakotaka kwenda kwamba, ule mshahara wake ile bajeti je, imetengwa kwa muajiri yule anayetaka kuhamia.

Kwa hiyo, Serikali haikatishi mtu tamaa kuweza kuhama, lakini pia, inatakiwa kufuata sheria, taratibu na kanuni na miongozo iliyopo ya utumishi wa umma.
MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa majibu. Swali langu la kwanza; kwa nini, Serikali isitoe fedha kwa haraka kukamilisha hayo mabima?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa, bado kuna upungufu mwingi wa madarasa, je, Serikali inachukua mkakati gani wa kudumu kuhakikisha hali hii haijitokezi tena? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Thea Ntara. La kwanza, kwa nini Serikali isitoe fedha hizi kwa haraka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe ya kwamba, katika Sera ya Ugatuaji wa Madaraka (D-by-D) jukumu la kujenga miundombinu yoyote ya maendeleo katika halmashauri zetu nchini ni jukumu la Halmashauri yenyewe. Serikali Kuu inafanya usimamizi na ku-complement jitihada za wao wenyewe katika zile halmashauri kule. Hivyo basi, ni jukumu la Mkurugenzi kuweza kufanya tathmnini katika eneo lake na kutenga fedha katika fedha za maendeleo kuweza kumalizia nguvu za wananchi zilipokwenda kama kwenye zahanati, vituo vya afya na madarasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha inayotafutwa Serikali Kuu ni kwenda kuongeza tu nguvu na kasi katika eneo husika. Hivyo, basi, Serikali Kuu inaendelea kutafuta fedha hizo kama ilivyotafuta fedha za kuweza kumalizia maboma na kuongeza madarasa katika miaka mingine kama ambavyo kila Mbunge humu ndani na halmashauri yake walipata shule mpya kupitia Mradi wa SEQUIP na Mradi wa BOOST.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikkienda kwenye swali lake la pili; hali hii itaendelea kuwa hivi kwa sababu, elimu ya awali ni bure, kwa Sera ya Serikali yetu hii. Elimu ya msingi ni bure, elimu ya sekondari ni bure kwa hiyo, idadi huongezeka kadiri mwaka unavyokwenda na huwa mahitaji nayo yanaendana na wale wanaotoka huku nyuma, wanaotoka awali kwenda darasa la kwanza, wanaotoka darasa la saba kwenda Form One. Kwa hiyo, kila mwaka Serikali inaendelea kufanya tathmini na maoteo ya wale ambao wanamaliza na kuona ni namna gani ambavyo fedha inaweza ikapatikana kwa ajili ya kuondoa upungufu huu wa madarasa.
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Suala la nyumba za walimu ni la kila watumishi, hasa kada yetu ya watendaji wa kata ambao wako vijijini kabisa na wakati mwingine maisha yao huwa hayana usalama wa kutosha. Je, Serikali ina mkakati gani kuwajengea nyumba za kuishi hawa watendaji wa kata?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itafanya tathmini juu ya mahitaji ya nyumba za watendaji wa kata kote nchini, kama ambavyo amesema Mheshimiwa Janejelly na kisha kuona ni bajeti ya kiasi gani inahitajika kwa ajili ya kuweza kujenga nyumba hizi.
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa upungufu wa walimu Mkalama bado ni mkubwa sana, Serikali inasema nini kuhusu upendeleo maalum kwa Mkalama kwa mgawo unaofuata wa walimu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa, watumishi wote wa umma tayari wapo wale wanaofariki na wale wanaostaafu, tayari wapo kwenye ikama ya kibajeti ya Serikali. Serikali ina mpango gani wa haraka wa kuziba mapengo yote yanayoachwa na watumishi hawa badala ya kusubiri zile ajira ambazo Rais anatupatia kila mwaka? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Isack; la kwanza, la upungufu mkubwa wa walimu Mkalama:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyokwishasema kwenye majibu yangu ya msingi, Serikali iko mbioni kuajiri, ajira mpya za walimu hivi karibuni zitatangazwa na baada ya mchakato huo kukamilika, Serikali itaweka kipaumbele katika maeneo ya pembezoni, ikiwemo jimboni au Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama kule anakotokea Mheshimiwa Francis Isack. Kwa hiyo, nikutoe mashaka katika hizi ajira mpya bado utaendelea kupata mgawao wa walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili, hili la vifo, uhamisho na ile mishahara inayobaki; kwa mujibu wa Kanuni B.4(1) – (2) ya Standing Order ya mwaka 2009 ya Utumishi wa Umma, mshahara ule upo katika bajeti ya mwaka husika kwa sababu mshahara ni cash budget. Sasa, mwajiri akichelewa kuomba kibali cha ajira mbadala, ule mshahara unakuwa haupo carried forward kwenye mwaka mwingine wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwatake sasa waajiri, pale wanapopata kifo katika maeneo yao ya halmashauri zao, kwa maana kuna mwajiriwa wake mmoja amefariki au amehama, waombe vibali vya ajira mbadala mara moja ili sisi tuweze ku-compile maombi yote yale na kuyapeleka kwa wenzetu wa Ofisi ya Rais, Utumishi, kuweza kupata vibali vya ajira mbadala, ndani ya mwaka wa fedha husika kama Standing Order ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2009 inavyotaka.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Je, ni lini sasa Serikali itapeleka walimu katika Jimbo la Singida Mashariki, Wilaya ya Ikungi pamoja na shule za sekondari Lighwa, Mang’onyi, Shule ya Msingi Mbughantigha, Choda, kote? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itapeleka walimu kule Singida Mashariki mara baada ya mchakato huu wa ajira mpya kukamilika na Singida Mashariki na maeneo aliyoyataja Mheshimiwa Nusrat kama Ikungi na mengineyo watapata nao mgao wa walimu hao wapya.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naishukuru sana Serikali kwa majibu haya mazuri ambayo yanaleta shangwe kubwa katika Tarafa hii ya Hagati. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shule hii ya Hagati Secondary, Halmashauri ya Mbinga ina shule ya wasichana inaitwa Mbinga Girls na yenyewe iko katika hali nzuri. Kupitia barua yenye Kumb. Na. MDC/E.80/136/135, tumeomba kibali cha shule hii nayo ichukue kidato cha tano na cha sita. Je, Serikali iko tayari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, halmashauri hii kwa kushirikiana na wananchi tumejenga shule za Benaya Secondary na Nguzo Secondary. Shule hizi zina upungufu wa miondombinu na sasa hivi zipo kidato cha pili. Je, Serikali iko tayari kutoa fedha kwa ajili ya miundombinu ikiwemo maabara? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Benaya Kapinga; hili la kwanza kuhusu Mbinga Girls nayo kuweza upandishwa hadhi na kuwa A – Level, Serikali ipo tayari kuweza kupandisha hadhi shule hii lakini kuna taratibu zile zilizowekwa kwa ajili ya upandishaji hadhi wa shule kuweza kuwa ya A – Level. Hivyo basi, nimtake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mbinga Vijijini kuweza kuanza taratibu za kupandisha hadhi shule hii, kwa mujibu wa sheria inavyotaka. Kwa maana lazima kwanza ifanyike assessment, pili waweze kumpeleka yule Mkaguzi wa Elimu pale na kisha waandike Wizara ya Elimu kwa ajili ya kuweza kuomba kupandisha hadhi shule hii.

Mheshmiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili la fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu katika shule alizozitaja ikiwemo Shule hii ya Benaya: Tutaendelea kutafuata fedha kama Serikali kwa ajili ya kuweza kuboresha miundombinu ya shule mbalimbali hapa nchini ikiwemo Mbinga DC. Hivyo basi, nimtake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mbinga DC kuweza kuorodhesha mahitaji yale ambayo yanahitajika katika shule hizi ili aweze kumwandikia Katibu Mkuu Ofisi ya Rais, TAMISEMI na kuweza kuona namna gani Serikali itapeleka fedha kadri ya upatikanaji wake. (Makofi)
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itapandisha hadhi Shule ya Sekondari Kwambegu iliyoko Kata ya Mahore ambalo ni hitaji la wananchi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itapandisha hadhi shule hii iliyopo Kata ya Mahore. Kama nilivyokuwa nikimjibu Mheshimiwa Kapinga kwamba, ni kwa mujibu wa sheria na taratibu zile zilizopo; ni lazima kwanza iwe imekidhi vigezo ambavyo vimewekwa. Hivyo basi, nimatake Mkurugenzi wa halmashauri husika kuweza kuanza kufanya tathmini hii na kisha Mkaguzi kwenda kuona kama vile vigezo vimetimia na kuweza kuomba kwa wenzetu wa Wizara ya Elimu kuweza kupandisha hadhi shule hii. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, Halmashauri ya Mji wa Tarime ina shule moja tu ya kidato cha tano na cha sita ambayo ni Tarime Secondary, kufuatia uhitaji mkubwa wa shule za kidato cha tano na cha sita, Halmashauri ya Mji wa Tarime imeanzisha mchakato wa kuipandisha hadhi Shule ya Sekondari Mogabiri kwa kujenga mabweni mawili, madarasa mawili ya advance pamoja na maabara zote za sayansi.

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuipandiisha hadhi shule hii ili iweze kusajili wanafunzi wa kidato cha tano Julai mwaka huu, ukizingatia tumeshakamilisha taratibu zote kama ambavyo umeainisha hapa na vigezo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwneyekiti, nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko juu ya Shule hii ya Mogabiri iliyoko kule Tarime Mjini; tutakaa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Tarime Mjini kuona kama vigezo hivi vilishapitishwa na ni lini aliweza kuwaandikia wenzetu wa Wizara ya Elimu ili tuweze kufuatailia ndani ya Serikali na kuona tuweze kupandisha hadhi shule hii kama vigezo vyote vimefikiwa.
nakushukuru. Kutokana na umbali mrefu wa kwenda sekondari, wakulima na wafugaji wa Kata ya Nyaburundu na Kata ya Manchimweru wameamua kujenga sekondari wenyewe kwa mikono yao na sasa hivi wameshafikisha madarasa mawili.

Je, ni nini kauli ya Serikali ya kuunga mkono? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere juu ya Serikali kupeleka fedha kuunga mkono juhudi za wananchi katika Kata ya Matowelo na Nyatwindu. Nimtake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bunda kuweza kupeleka timu kuweza kufanya tathmini juu ya mahitaji katika maeneo haya. Vilevile, nimtake Mkurugenzi wa Halmashauri hii ya Bunda kuhakikisha kwamba anatenga fedha kati ya mapato yake ya ndani, kuweza kuunga mkono juhudi za wananchi hawa wa kata hizi ambazo Mheshimiwa Getere amewataja. (Makofi)
MHE. JACQUELINE K. ANDREA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa Mkoa wetu wa Tabora ni wa tatu kwa ukubwa kwa population na vilevile, ni wa kwanza, kijiografia, Serikali haioni kuna haja ya kutuwekea walimu wengi wa kutosha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, idadi ya walimu wa shule za msingi tunayohitaji kwa mkoa wetu ni 19,666 na waliopo ni 8,950; upungufu ni 10,716. Je, Serikali ajira zinazofuata imepanga Mkoa wetu wa Tabora kutuletea walimu wangapi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacqueline Kainja Andrea, la kwanza hili haioni haja ya kuweka walimu wengi zaidi Tabora? Naomba kwa ridhaa yako nijibu yote mawili kwa pamoja kwa sababu yanakaribiana.

MWENYEKITI: Ndiyo.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la kwanza la kwamba haioni haja ya kuweka walimu wengi Mkoa wa Tabora; na la pili, je, ajira za walimu zinazofuata kama Mkoa wa Tabora nao utapata mgao wa walimu hao; nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali hii inatambua upungufu wa walimu uliopo na ndiyo maana inaendelea kuajiri walimu kadri ya upatikanaji wa fedha. Pale ambapo ajira hizi zitatangazwa hivi karibuni kama alivyotoa tangazo Mheshimiwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, basi ajira zile zikishakamilika na hao walimu kupatikana, Mkoa wa Tabora ni kati ya mikoa ambayo itapewa kipaumbele kwa ajili ya kuweza kupata walimu hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ajira zilizopita katika mwaka wa fedha uliopita, Mkoa wa Tabora ulipata walimu jumla 262 wa sekondari na walimu 476 wa shule za msingi. Kwa hiyo, Serikali imekuwa ikipeleka walimu katika Mkoa wa Tabora kwa kutambua ni Mkoa mkubwa na una watu wengi.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua changamoto ya upungufu wa walimu nchini. Wilaya ya Nkasi ni miongoni mwa Wilaya ambazo zina changamoto kubwa hasa walimu wa kike. Serikali mna mpango gani wa haraka ili kuokoa mimba za utotoni ambazo zinaendelea Wilaya ya Nkasi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani juu ya upungufu wa walimu waliopo Nkasi; katika ajira ambazo zitatangazwa mwishoni mwa mwezi huu wa Februari kwa ajili ya kupata walimu wapya, basi tutaweka kipaumbele vile vile kwa Mkoa wa Rukwa na hasa Wilaya ya Nkasi.
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru; Wilaya ya Chunya ina changamoto ya upungufu mkubwa sana wa watumishi hasa kwenye sekta ya elimu pamoja na sekta ya afya; je, ni lini Serikali itatupatia watumishi wa kutosha kwenye sekta hizi hasa kwenye ajira ambazo zinafuata?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Masache Kasaka. Tutaweka kipaumbele vilevile katika hizo ajira mpya zinazokuja katika maeneo kama vile Chunya anakotokea Mheshimiwa Kasaka.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa kuwa katika Mkoa wa Shinyanga kuna baadhi ya shule za sekondari na shule za msingi, hazina kabisa walimu wanawake, nini kauli ya Serikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ajira hizi ambazo zitatangazwa hivi karibuni, Serikali itaangalia namna bora ya kuweza kupata walimu wanawake ili kwenda kujaza mapengo yale yaliyopo katika maeneo mbalimbali hapa nchini ikiwepo Mkoa wa Shinyanga ambao Mheshimiwa Dkt. Mnzava amezungumzia. (Makofi)
MHE. MARTHA F. MARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi niweze kuuliza maswali ya nyongeza. Kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali kwa kuona umuhimu na kutoa hizo shilingi bilioni tatu kwa ajili ya ujenzi wa shule ya wasichana nchi nzima. Mkoa wetu wa Katavi unaongoza sana kwa mimba za utotoni, vile vile katika shule zetu za sekondari kuna upungufu mkubwa sana wa mabweni kwa ajili ya watoto wa kike; je, upi mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba unajenga mabweni kwa ajili ya kuwanusuru watoto wa kike na mimba za shuleni na utotoni? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, katika elimu ya msingi, kuna shule zilizojengwa miaka ya 1970 ambazo zimekuwa chakavu sana; pamoja na jitihada za Serikali kutuletea pesa za BOOST, lakini shule nyingi sana bado ni chakavu na zinavuja maji hususan wakati wa masika. Je, upi mkakati wa Serikali kukarabati shule kongwe nchini kuweza kuwa katika level nzuri?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mariki. Swali la kwanza juu ya uhitaji wa mabweni katika Shule za Sekondari Mkoa wa Katavi, katika mwaka huu wa fedha ambao tupo sasa unatekelezwa, Serikali imetoa zaidi ya shilingi bilioni 7.04 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni na tayari kuna mabweni 60 ambayo yamejengwa maeneo mbalimbali hapa nchini ikiwemo katika Mkoa wa Katavi. Serikali itaendelea kutafuta fedha ya kuweza kujenga mabweni haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa rai kwa Wakurugenzi wa Halmashauri zote nchini kuhakikisha katika fedha zao za miradi ya maendeleo wanajenga mabweni katika Shule za Sekondari ambazo Serikali Kuu, Serikali hii ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan imepeleka fedha nyingi katika ujenzi wa shule hizi za sekondari kote nchini, ukiwemo Mkoa ule wa Katavi anakotoka Mheshimiwa Mariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye swali lake la pili, kwanza nikiri kwamba Mheshimiwa Martha amekuwa akilifuatilia sana jambo hili na amekuja mara kadhaa Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuulizia juu ya shule hizi kongwe za msingi katika Mkoa wa Katavi. Tayari Serikali kupitia Mradi wa BOOST ilijenga shule 302 kote nchini. Hii ni kwa mara ya kwanza kwa kipindi kirefu sana ambapo Serikali inawekeza fedha nyingi zaidi ya shilingi bilioni 230, katika shule za msingi. Hii inaonesha ni namna gani Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameweka kipaumbele katika shule zetu za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika shule kongwe hizi kuna madarasa zaidi ya 3,350 ambayo yamejengwa nchi nzima kupitia mradi huu wa BOOST ikiwemo katika maeneo mengine shule kongwe na Mkoa wa Katavi nao walipata madarasa katika mgao huu wa madarasa 3,350. Serikali itaendelea kutafuta fedha zaidi kwa ajili ya kuweza kujenga shule au kukarabati shule kongwe zilizopo hasa zile za msingi. (Makofi)