Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Noah Lemburis Saputi Mollel (2 total)

MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimuwa Waziri Mkuu kwa kuwa changamoto hii ya Walimu kuchapa watoto bila utaratibu na tena kikatili, nini sasa Serikali haioni kama kuna haja ya kuwaelimisha Walimu hawa somo la maadili la namna ya malezi ya watoto na makuzi katika shule zetu za Msingi na hata Sekondari?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lemburis, Mbunge wa Arumeru kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, taasisi zote za elimu zina taratibu zake, na uendeshaji wa elimu nchini una sheria na kanuni zake ambazo zimewekwa, na ndizo zinazosaidia kuongoza wakuu wa taasisi na wale watumishi wa taasisi husika katika kuzingatia sheria na kanuni zilizowekwa; na ndiyo sababu unaona mambo yanaenda vizuri. Hiyo ni kuanzia elimu ya awali, ya msingi, sekondari mpaka elimu ya juu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo uainishaji wa sheria hizi na kanuni ndio unaoongoza watumishi walio kwenye sekta hiyo au taasisi hiyo kufuata. Ndiyo maana tunaona sasa utulivu upo na kazi zinaenda kwa sababu kila mmoja anazingatia sheria na kanuni zilizopo. Kwa hiyo hatuwezi kusema tutachukua hatua kali kwa sababu miongozo ipo pale ambapo mtumishi anakiuka taratibu na sheria, sheria ile imeelekeza na adhabu ambazo zinatolewa kwa mhusika. Kwa hiyo utaratibu huo unatumika kama ni adhabu ndogo kwa aliyekiuka utaratibu umeainishwa, kama ni adhabu kubwa imeainishwa lakini pia hata akitakiwa kwenda mahakamani imeainishwa.

Mheshimiwa Spika, lakini tuzingatie tu kwamba taaluma ya ualimu ina misingi yake na imewekea utaratibu pia chini ya Wizara ya Elimu na kwa hiyo zipo kamati za maadili mioongoni mwa walimu. Wakati mwingine vyama vya wafanyakazi kama vile CWT yenyewe inachukua nafasi pia kukaa na walimu kuwafanyia counselling pia kuwaelimisha ili kufanya mambo yanavyokwenda kama utulivu ambao sasa upo na utaratibu huo ndio ambao tunautumia kwa sasa.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu tumekuwa tukiona jitihada zako za kuzunguka nchi nzima kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo. Lakini katika ukaguzi huo umekuwa ukikuta miradi hiyo haitekelezwi vizuri kwa maana kunakuwepo na ubadhirifu, wizi na uzembe wa aina mbalimbali na hata ripoti ya CAG imekuwa ikitoa ubadhilifu huo na wizi mara kwa mara katika ripoti hiyo.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, je, nini kauli ya Serikali kuhusu hali hii ambayo imekuwa ikijitokeza mara kwa mara. Ni mkakati upi wa makusudi na wa maalum ambao Serikali inachukua ili kuhakikisha kwamba wizi na ubadhirifu katika miradi ya umma haitokei kabla haijafanyika ili basi wananchi waweze ku…

SPIKA: Mheshimiwa Waziri Mkuu, majibu.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lemburis, Mbunge wa Arumeru kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu inao mfumo wa kufanya tathmini kwenye sekta mbalimbali ikiwemo na kufanya mapitio ya mwenendo wa matumizi ya fedha na mali za umma kwenye sekta hizo. CAG ni taasisi mojawapo ambayo inakwenda kuona mwenendo wa matumizi ya mali na fedha za umma kwenye sekta zote za Serikali na ikibidi pia hata sekta binafsi ambayo ina maslahi ya moja kwa moja kwa Serikali.

Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba wanapofanya kazi hiyo wanabaini mapungufu na wakati mwingine mapungufu hayo wachache wanafanya kwa makusudi na CAG anachokifanya ni kuishauri Serikali namna bora ya kudhibiti hali hiyo kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli na mimi nilipata nafasi ya kufanya ziara kwenye Halmashauri zetu, taasisi mbalimbali za Serikali na ninapokwenda wakati mwingine nakwenda na taarifa ya CAG ambayo pia inashauri Serikali namna bora ya kusimamia maeneo hayo na kuchukua hatua. Sasa namna gani nzuri ya kuendelea kusimamia.

Mheshimiwa Spika, kwanza tunatambua mchango mzuri wa taasisi hii ambao pia unatuainishia na kubainisha mapungufu hayo kwenye sekta zetu za Serikali na kazi yake ya kuishauri Serikali tunachukua ushauri huo na kuufanyia kazi, pale ambako tunauona ubadhirifu wa moja kwa moja tunachukua hatua na pale ambako anashauri namna ya kuboresha tunafanya hilo na sasa Serikali yetu imeandaa mfumo mzuri sana wa kufatilia sekta zetu kabla CAG hajafika.

Mheshimiwa Spika, ofisi yangu, Ofisi ya Waziri Mkuu, imeanzisha sasa Kitengo cha Ufatiliaji na Tathmini kwenye Sekta za Serikali ambazo zinabaini mapungufu hayo kabla CAG hajafika na kitengo hiki tumekiimarisha zaidi na kimeshaanza kazi. Sasa hivi kinapita kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa, taasisi mbalimbali za Serikali ili kuona hali hiyo, kufanya tathmini, lakini pia kushauri pale ambapo kuna mapungufu kwenye sekta hiyo kabla CAG hajafika, lakini tunapokuta mapungufu tunaendelea kuchukua hatua.

Kwa hiyo, niendelee kumuhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali iko makini kwenye hili, inafatilia na itaendelea kufatilia ili kuweza kudhibiti mali na fedha za Serikali, iwe ni kwa ajili ya mradi au kwa matumizi ya kwawaida kwenye ofisi yote haya ni majukumu ambayo Serikali inayafanya, ahsante sana. (Makofi)