Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Martha Nehemia Gwau (3 total)

MHE. MARTHA N. GWAU aliuliza:-

Je, ni kiasi gani cha Zebaki kinaingizwa nchini kila Mwaka?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Nehemia Gwau, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2019 kiasi cha Zebaki kilichoingizwa nchini kilikuwa ni tani 24.42, ambapo mwaka 2020 kilikuwa ni tani 22.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kwamba zebaki ni kemikali inayotakiwa kudhibitiwa kwasababu ina madhara ya afya ya binadamu kama vile kusababisha upofu, kutetemeka viungo, kupoteza kumbukumbu, kuharibika ngozi, tatizo la ini na figo.

Mheshimiwa Spika, hivyo basi Serikali, kupitia Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali imeendelea kuchukua hatua za kudhibiti uingizaji wa Zebaki kwa kuwasajili wale wanaoingiza Zebaki nchini na kuchukua hatua kwa wale wanaokiuka sheria.
MHE. MARTHA N. GWAU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga nyumba za kuwahifadhi waliofanyiwa ukatili ikizingatiwa kuwa ukatili kwa watoto na wanawake umeongezeka?
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Nehemia Gwau, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mpango wa kuwahifadhi waliofanyiwa ukatili (kujenga nyumba za kuwahifadhi waliofanyiwa ukatili), Serikali imeandaa Mwongozo wa Uanzishaji na Uendeshaji wa Nyumba Salama wa Mwaka 2019, kwa ajili ya manusura wa vitendo vya ukatili pamoja na wahanga wa biashara haramu wa usafirishaji wa binadamu. Lengo ni kuweka mazingira wezeshi kwa uanzishaji huduma ya nyumba salama kwa manusura wa ukatili wa kijinsia na kwa watoto hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hadi kufikia June 2023 jumla ya nyumba salama 12 zimeanzishwa na kusajiliwa katika Mikoa ya Arusha, Kigoma, Kilimanjaro, Dar es Salaam na Mwanza. Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa sekta binafsi kuhakikisha upatikanaji endelevu wa huduma hii kwa mujibu wa Mwongozo wa mwaka 2019.
MHE. YAHAYA O. MASSARE K.n.y. MHE. MARTHA N. GWAU aliuliza: -

Je, Serikali haioni kuna haja ya watoto wachanga kutumia Bima za Afya za Mama zao?

NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martha Nehemia Gwau, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kumekuwa kukitokea changamoto kwa wazazi wenye bima wanaojifungua watoto wao kushindwa kupata huduma hasa kwenye vituo vya huduma za afya vya sekta binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri wa Afya alishatoa maelekezo kwa Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kuhakikisha watoto wachanga wenye uhitaji wa huduma wanapata huduma za afya bila kikwazo chochote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutumia fursa hii kuelekeza Watendaji wa Mfuko wa Bima ya Afya na vituo vyote vya huduma za afya nchini kuhakikisha watoto wanapata huduma kwani Mama yupo na kadi yake inayoonesha ushahidi wote kuhusu mtoto husika na ni mtoto wa ngapi kwenye familia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaasa wazazi na viongozi wa hospitali husika kukomesha kabisa matukio ya kughushi nyaraka ambayo pia ndiyo yanapelekea kuwepo na usumbufu wakati mwingine. Naomba kuwasilisha.