Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Antipas Zeno Mgungusi (12 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwanza naunga mkono hoja, lakini pili napenda nijikite kwenye hii hotuba ukurasa wa 46 ambao unazungumzia masuala ya utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa pongezi kwa Serikali, hasa Wizara ya Maliasili, Waziri na wasaidizi wake kwa kuongeza idadi ya wageni kutoka 2015 mpaka sasa hivi 2021 idadi ambayo imetajwa pale sambamba na mapato yameongezeka kama ambavyo imetajwa kwenye hotuba kwa wale waliopitia, lakini pamoja na hayo niseme tu kwamba, hii dira ya Rais, maono yake ya kutaka kuongeza idadi ya wageni kutoka milioni moja na kitu mpaka milioni tano mwaka 2025 itafikiwa tu kama Wizara na wataalam wake wakitoa ushirikiano wa kutosha, lakini hasa kubadilisha mind set kwa maana ya kwamba, lazima tukubaliane utalii ni biashara. Kwa uzoefu tu wa kawaida kumekuwa na hali ya kwamba, uhifadhi umekuwa unashindana na utalii ndani ya Wizara na taasisi zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yangu ni kwamba, kunapokuwa na changamoto ya bajeti kwenye Wizara pamoja mashirika, lakini bajeti ya kwanza kuonewa ni ya utalii, lakini hasa ya masoko, kwa maana ya tourism promotion. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake na wengine kwenye mashirika waanze kubadilika kwa maana ya kuona utalii ni biashara, lakini pia utalii ndio unamlea uhifadhi. Shughuli zote za doria za magari, za mafuta, uniform za wapiganaji, posho na vitu vingine vinanunuliwa au vinalipwa kutokana na makusanyo yanayotokana na utalii. Kwa hiyo, niwaombe sana ndugu zangu waweze kutoa kipaumbele kwenye bajeti za utalii kuliko vinginevyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hata Bodi yetu ya Utalii ambayo sasa ndio inayofanya masoko imekutana na changamoto ya bajeti kwa miaka mingi. Tumekuwa tunajitahidi inawekwa fedha nyingi, lakini fedha ambayo inatoka kwa utekelezaji inakuwa ni ndogo sana, hali ambayo inafanya tusiweze kushindana kama ambavyo inapaswa. Ukiangalia wenzetu nchi jirani ya Kenya, wengine wa Afrika Kusini na Wamoroko wanafanya vizuri zaidi kitakwimu, wanaingiza wageni wengi, lakini hawana vivutio vingi kama ambavyo sisi tunavyo Watanzania. Kwa hiyo, utalii ni biashara, lazima tukubali kwamba, utalii ndio unalea uhifadhi, ili uhifadhi ufanyike kwa kiwango tunachokipenda, basi tupate fedha kwanza kutoka kwenye utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, niwashukuru wafanyabiashara kwa maana ya wakala wa utalii. Wao ndio wamekuwa wakileta wageni kwa zaidi ya asilimia 80 hapa nchini. Kwa hiyo, niombe tu Wizara iendelee kushirikiananao kwa ukaribu kujifunza kuona wenzetu wanachokifanya, ili wageni waweze kuja kwa wingi kufikia hili lengo la Rais la kufikisha wageni milioni tano mwaka 2025.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, kumekuwa na changamoto ya migogoro ya mipaka ya ardhi. Sisi kwetu Bonde la Kilombero tuna changamoto nzuri kidogo niseme kwa sababu, kuna hili suala la mradi wetu wa umeme wa Nyerere, Stiegler’s George. Ni mradi mkubwa wa kitaifa ambao sote tunaupenda na tunautakia heri, hatuko tayari kumuona mtu yeyote ambaye anaharibu, lakini sisi watu wa Bonde la Kilombero imeonekana tunatoa sehemu kubwa ya maji ya mradi ule, kwa hiyo, kwa maana yake ni kwamba, baadhi ya maeneo ambao tulikuwa tunalima muda mrefu na kufuga kwa sasa yanakwenda kuathirika. Suala la uhifadhi limekuwa serious sana na Serikali kwa hiyo, baadhi ya vitongoji vyetu vya Jimbo la Malinyi, Ulanga na Mlimba vitaenda kupotea kwa maana ya vinafutika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kijiji kimoja cha Ngombo ambacho kipo Malinyi nacho kwa msimamo wa Serikali lazima kifutwe kwa sababu, inasemekana ndio chanzo cha maji mengi ambayo yanakwenda Stiegler’s. Pengine sisi hatuna pingamizi sana, niiombe Serikali, Waziri Mkuu yupo hapa na ndugu yangu Dkt. Ndumbaro, Waziri, yuko hapa tutatoa ushirikiano kadiri inavyotakiwa, lakini naomba tu tusaidike kwa maana ya Kijiji cha Ngombo kibaki, lakini kwa masharti ili tusiharibu uhifadhi. Kwa hiyo, tuko radhi kupunguza idadi ya mifugo. Serikali tutashirikiana nayo kupunguza hata matrekta na masuala mengine ambayo tunaona yanachangia kuharibu uhifadhi, ili mradi wetu huu mkubwa usikwame, lakini naomba Serikali itufikirie wananchi waweze kubaki kwa masharti ambayo watayatoa au ambayo tutaafikiana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, maeneo ya ziada ya kulima kwa Jimbo zima la Malinyi imekuwa ikitusumbua. Kuna mpaka wa mwaka 2012 uliwekwa, badaye kuna mpaka mwingine mpya 2017, yote hayo inasemekana hayapo kwenye GN, lakini niombe Serikali, hatubishani nao, lakini naomba tufikiriwe angalau mita 700 tu kutoka kwenye mpaka ule wa 2017 tuweze kupatiwa ili tuweze kuendeleza shughuli zetu za uchumi. Sasa hivi Malinyi imesimama, watu hawalimi, tunasubiri hatma ya mwisho ya Serikali kutuambia mustakabali wetu ukoje.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliambiwa kuna Mawaziri wanane wale watakuja kutoa hatima, lakini muda unazidi kwenda watu hawana cha kufanya, majibu yanatakiwa na mimi kama Mbunge majibu sina. Kwa hiyo, niwaombe Serikali basi itoe official statement tuweze kujua nini ni nini na nini kinachofuata, maana sasa hatujui hatima yetu. Kwa hiyo, nashukuru sana, naamini Wizara na Waziri Mkuu watashirikiana kuweza kutufikiria sisi watu wa Malinyi, Ulanga na Kilombero.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, ni suala la changamoto ya miundombinu ya barabara. Kwetu Malinyi kuna barabara kubwa ambayo tunaisubiria, maarufu kama Barabara ya Songea, lakini Kiserikali inaitwa Lupilo – Malinyi – Londo – Namtumbo, kilometa 296 ambayo itaunganisha Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Ruvuma kupitia Wilaya ya Malinyi na Namtumbo.

Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Miundombinu na Serikali kiujumla kutufikiria hili jambo liweze kuanza kwa uharaka ili tuweze kutokea Songea na mikoa mingine. Jambo hili likifanyika itakuwa imetusaidia kukuza uchumi wa Malinyi na Ulanga Kilombero kama mbadala wa kilimo ambacho sasa inaelekea tunaenda kuacha kutokana na changamoto ya mpaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, nitoe shukrani kwa Mheshimiwa Spika, Wizara ya Afya, hasa kunisaidia wakati nimeumwa Novemba, Disemba. Nilipata huduma nzuri Ofisi ya Bunge ilinisaidia, lakini Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Hospitali ya Sokoine Morogoro, walinisaidia nilipata huduma nzuri kwa hiyo, nimesema nichukue wasaa huu kuwashukuru. Mwisho wazazi wangu Mzee Zeno Mgungusi na mke wake Theopista Nghwale na mke wangu Mariam Ali Mangara aka mama Moringe nawashukuru wote kwa kunipa ushirkiano.. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi. Nina masuala kama matatu; la kwanza ni sakata la KADCO na Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro; la pili, suala la TIC kwa maana kwenye Muswada wa Uwekezaji; na la mwisho, suala nguvu za Kamati zako za Bunge ambazo sisi tunazitumikia dhidi ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, mimi ni mtumishi mstaafu, nilibahatika kufanya kazi Wizara na Maliasili na Utalii. Kipindi changu nikiwa Wizarani nilishiriki katika shughuli za kufanya utafiti wa hali ya utalii nchini na bahati nzuri nilikuwa napangwa Kiwanja wa Ndege cha Kilimanjaro kwa miaka takribani mitano mfulululizo. Utafiti huo tulikuwa tunafanya watu wa Idara ya Utalii ya Wizara ya Maliasili, Commission ya Utalii ya Zanzibar, Idara ya Uhamiaji Tanzania pamoja na Benki Kuu.

Mheshimiwa Spika, kipindi chote sehemu yangu nilipangiwa Kilimanjaro ndipo nilipata kuufahamu ule uwanja na kuifahamu KADCO. Kwa bahati mbaya sikubahatika kipindi kile kuifahamu KADCO vizuri mpaka juzi baada ya kuisoma taarifa ya CAG na baada ya kualikwa kwenye Kamati ya PIC kuweza kusikiliza haya masuala yanakwendaje.

Mheshimiwa Spika, kimsingi KADCO kwa sasa ni kama kigenge au kibubu cha watu kufanyia maisha nje ya mfumo wa Serikali. Kinachonisikitisha sikuona kama Katibu Mkuu wa Wizara ile au watu wa Wizara kama wanaumwa na hali hii. Sinema zinazoendelea KADCO wao wako comfortable kabisa, wanapumua vizuri na wanaendelea kula vizuri kana kwamba hakuna kinachoendelea mpaka CAG, Wabunge na wadau ndio wanakuja kuona matatizo ya mle ndani, jambo ambalo linasikitisha sana.

Mheshimiwa Spika, katika ushirki wangu wa kikao, tunamhoji Katibu Mkuu na watu wake ambao walikuja jopo zima pale, Waraka wa Baraza la Mawaziri Na.5 wa mwaka 2009, ulitoa maelekezo kuwa tutanunua hisa zote za KADCO kutoka kwa wale wabia ambao walikuwa wajanja wajanja. Tutanunua kwa 100% baada ya kumaliza zile hisa, umiliki uende kwa TAA. Aidha, iendelee ku-operate kama kampuni tanzu ya TAA au KADCO ifariki kabisa uwanja uendeshwe direct na TAA kama wanavyofanya Kiwanja cha Dar es Salaam na viwanja vingine, lakini jambo hilo halikufanyika.

Mheshimiwa Spika, tunawauliza watu wa Wizara kwa nini hamjatekeleza maagizo haya? Wanajibu, Waheshimiwa mnajua tulikuwa na mchakato wa kutafuta mbia mpya wa kuendesha. Tukawaambia KADCO nani anawapa mamlaka ya kutafuta mbia, nadhani lilipaswa liwe ni jambo la Wizara na Mkuu wa masurufu (Accounting Officer) wa Wizara ni Katibu Mkuu pengine wangefanya wao. Hata hivyo wanasema kwamba huu mchakato tulikuwa tunafikiria kutafuta mtu. Hali ambayo inaonesha kabisa mashaka na kuna nia ovu ya wazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuliwahoji, kama kuna mchakato wa kutafuta mtu mpya, sasa hivi ni miaka 12, maana ni mwaka 2010 ndio tulinunua hisa zote, hivyo kampuni imekuwa ya Serikali kwa 100%. Hadi leo tunazungumza mwaka 2022 ni miaka 12, mnachakata kwa miaka mingapi kumtafuta mtu wa kuendesha? Hawana majibu yaliyonyooka, wanaongea vitu ambavyo havieleweki. Nilitamani kumshawishi Mwenyekiti tuwafukuze kwenye kikao. Kwa hekima ya Mheshimiwa Hasunga, alisema tuwasikilize mpaka mwisho, tuone inakuwaje?

Mheshimiwa Spika, tukasema kama kweli huo mchakato ulikuwepo, mmetangaza wapi kwamba jamani tunatoa tangazo, tunatafuta mbia, tunatafuta mtu wa kuendesha Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro, mna tangazo ambalo mmelitoa juu ya hili? Halipo. Katika mazingira yoyote inaonekana kabisa kuna nia ovu, hawa watu hawana nia nzuri na ni mchongo tu, wanataka watupige na waendelee kutupiga zaidi.

Mheshimiwa Spika, kituko kingine, wanajibu sasa hivi tuko kwenye mchakato wa ku-renew mkataba wa uendeshaji, ile concession agreement. Awali ile concession agreement ilikuwa baina ya wale wawekezaji na Serikali. Sasa hivi wawekezaji hawapo uwanja ni wetu tangu awali na KADCO imekuja kwetu kwa 100%, Mkataba Serikali inataka isaini na nani? Maana yake wanajadili Serikali kuingia makubaliano ya kuendesha uwanja na jini au hewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna muda huwa nawaambia wenzangu tukiwa tunazungumza, muda mwingine Mungu akikusaidia ukiwa huna akili unaishi kwa amani sana, lakini ukiwa na akili utapata stress. Maana upeo wako ukiwa mfupi unaona kila kitu sawa tu, nyeupe na nyekundu ni sare, ndefu na fupi unaona ni sawa tu. Kwa hiyo wenzetu ambao hawana akili wanaishi sawa kuliko sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine ambacho nakishangaa, kwa maana baada ya sisik kuinunua ile kwa 100% nilitarajia Katibu Mkuu wa Wizara ndiye Mkuu wa Masurufu na watu wake waiagize moja kwa moja KADCO iende TAA, maana, KADCO pamoja na kwamba tumeinunua haiwezi kujipeleka yenyewe na watendaji ambao wako pale wananufaika na KADCO, hawawezi kujipeleka na kusema tumekuja TAA. Ni Katibu Mkuu wa Wizara (KM) anatakiwa aiagize iende, lakini hafanyi hivyo, hakufanya hivyo na anapumua na ana amani tele kabisa, ni kituko. Kwa hiyo, mambo haya yanakera na ni mambo ya wazi kabisa, inaonesha kuna nia ovu, kitu ambacho sisi sote hatukukubaliana.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, kwa hekima za Mheshimiwa Hasunga ambaye alikuwa anakaimu Uenyekiti katika kile kikao alisema, Waheshimiwa hebu tuwape muda kidogo, maana wenyewe waliomba walisema, tunahitaji muda tukajadiliane tutaleta majibu. Tukasema kwa nini mlete majibu mkishajadiliana, mnajadiliana na nani? Katibu Mkuu wa Wizara tuko naye hapo mbele, Mwenyekiti wa Bodi na Bodi yake ya KADCO yuko pale, Mkurugenzi wa KADCO yuko pale, Mwanasheria wa KADCO yuko pale, timu nzima ambayo wanayojua hili sakata wako pale. Pembeni mnaenda kujadiliana na nani ili mtuletee majibu baada ya wiki moja? Ni vitu ambavyo havieleweki. Bahati nzuri kwa hekima za Mwenyekiti, Mheshimiwa Hasunga alisema tuwavumilie kwa wiki moja, Ijumaa inayofuata watuletee majibu. Akasema pia Mheshimiwa Mgungusi tutakualika tena, uje ushiriki na hicho usione kwamba leo tunakwepesha. Hata hivyo, mpaka kesho, mpaka mwakani, hawakuleta majibu.

Mheshimiwa Spika, hapa kuna picha mbili, nia ovu ya moja kwa moja, kwamba wanapiga mchongo, lakini pia ni dharau kwa Kamati yako ya Bunge. Kwa hiyo, pamoja na mambo hayo yote, nashauri kwenye sakata hili tuagize ukaguzi maalum ukafanyike kuhusu KADCO kuanzia mwaka 2010 tangu tumenunua hisa kwa 100%.

Mheshimiwa Spika, kwa kipindi kirefu KADCO hawakuwa na Mwanasheria. Kituko kingine wana-hire huduma mtaani kwa maana wana Mwanasheria wao private mtaani na wanalipa. Ukiangalia zile legal services za kila mwezi unaweza ukazimia, bora usijue. Kwa hiyo, siwezi nikasema mengi, naomba tukubaliane ukaguzi maalum ukafanyike kule KADCO, wanaweza wakaona vituko vya hatari.

Mheshimiwa Spika, kingine niseme tu, kama ikiwapendeza, naomba Katibu Mkuu wa Wizara ajitafakari kwa maana ya sehemu ya Uchukuzi, Mwenyekiti wa Bodi ya KADCO ajitafakari, maana ni nje ya mamlaka yangu, lakini nashauri tu wajitafakari, Mkurugenzi wa KADCO na safu yake, Menejimenti nzima ijitafakari. Kwa suala la KADCO naomba niishie hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni kwenye Muswada wa Uwekezaji. Suala la TIC- Kituo cha Uwekezaji Tanzania. Kwenye ule Muswada ambao tulipitia Wizara ya Viwanda na Biashara katika kipengele cha Board Members, Wajumbe wa Bodi ya TIC tulipendekeza kuwepo na Wizara ya Mambo ya Nje kama moja ya member wa ile Bodi ya TIC. Kwa sasa kuna Wizara zimetajwa, Wizara ya Fedha ipo, Wizara ya Ardhi, TAMISEMI ipo lakini Wizara ya Mambo ya Nje haipo kwenye Bodi ya Wakurugenzi ya TIC. Kwa hiyo, sisi tulipendekeza, lakini sasa Serikali nadhani hawakuichukua hii, wakaacha kama ilivyokuwa awali.

Mheshimiwa Spika, naona haja ya Wizara ya Mambo ya Nje kuwepo TIC kwa sababu gani? Tunapozunguzma Uwekezaji mkubwa leo Foreign direct investment zinatoka nje, makampuni makubwa yanatoka nje na leo hii mnajua sera yetu sisi ya kimataifa ni diplomasia ya uchumi. Tunawataka Mabalozi wapambane kuacha siasa bali watafute wawekezaji kuja Tanzania. Wawekezaji wanakuja na mitaji yao au pengine wanakopa lakini wanaingia hapa nchini, wangependa kuona mwenyeji wao yupo kwenye huduma zao. Mwenyeji wao ni Wizara ya Mambo ya Nje kupitia Mabalozi. Inawezekanaje katika Bodi ya Wakurugenzi ya TIC hakuna mtu wa Wizara ya Mambo ya Nje, lakini kuna TAMISEMi? Nawaza sijui kwa nini kuna TAMISEMI au kwa sababu ya ardhi, wanamiliki maeneo, lakini Wizara ya Ardhi ipo!

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tulipendekeza aidha, iongezeke Wizara ya Mambo ya Nje kwenye Bodi au apunguzwe mmoja, apunguzwe hata TAMISEMI, Wizara ya Ardhi anamwakilisha, lakini hakuna sababu ya msingi ya kufanya Foreign Affairs asiwepo kwenye Bodi ya Wakurugenzi ya TIC, maana hata wawekezaji wanapoona wanalalamika au hawahudumiwi vizuri mwenyeji wao yupo wanabanana naye pale inapendeza, kuliko mtu wa Mambo ya Nje akienda kulalamikiwa na wawekezaji wake ambao amewaleta na yeye aanze kuuliza pembeni hai-make sense kwa hali ya kawaida. Hivyo, napenda kushawishi Bunge kama litakubaliana Wizara ya Mambo ya Nje iongezwe kwenye Bodi ya Wakurugenzi pamoja na ile Kamati ya Kitaifa ya Uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, suala la mwisho ni suala la nguvu za Kamati zako za Bunge ambazo tunazihudumia dhidi ya watendaji wa Serikali. Nimekuwa na uzoefu mdogo tangu nimekuwa nikifanya kazi za Kamati miaka hii miwili ya Ubunge, watendaji wa Serikali mara nyingi hawako serious. Wanakuja kwenye Kamati tunakaa nao, unaona kabisa hawako serious. Kuna watu ni Maprofesa na elimu kubwa lakini wengi unakuta hawa-own taarifa ambazo zinazokuja. Tunauliza maswali ya kawaida kabisa very obvious, hawawezi kusema mpaka unabaki unashangaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunatoa maelekezo kwa mfano Bunge la Bajeti, tunawaambia Bunge lijalo mje na taarifa fulani, fulani wanaitikia ndio Waheshimiwa. Session inayokuja mnakutana hawaleti, yaani kama wametuzoea au wanatuweza hivi. Muda mwingine watendaji wanaambiana kwamba wewe peleka tu taarifa hata zikiwa kubwa, Waheshimiwa Wabunge huwa hawasomi. Waambie tu Mheshimiwa, Mheshimiwa huwa hawasomi. Sasa bahati mbaya wanakosea njia, siku hizi watu wanasoma sana na hata kukesha inapolazimu watu tunakesha, we read between lines, hata wakileta vitabu vikubwa tunasoma na tunafuatilia.

Mheshimiwa Spika, nitoe rai kwa Wabunge wenzangu ambao ni Mawaziri na Naibu Mawaziri, sisi ni wenzenu. Tupo kuwasaidieni kuhakikisha kwamba tunasaidia hii nchi na inakwenda mbele, there is nothing personal. Mara nyingi utakuta Mawaziri au Naibu Waziri, hawatumii muda mwingi kubanana na watendaji wao. Sijui wanazoeana? Baadaye unakuta Kaibu Mkuu anamwingiza chaka, Waziri anakuja kukaangwa kwa ajili ya mambo ya watendaji wake. Naibu Waziri anakaangwa kwa ajili ya Mkurugenzi fulani aliye chini ya Taasisi zao, kwa nini? Wasiwachekee, sisi tukija kwenye Kamati tunakaza, wakitulaumu sawa, mahusiano yetu ya urafiki yakivunjika sawa, lakini you need to be serious kuwasimamia watendaji.

Mheshimiwa Spika, naomba uwatie moyo Wabunge wako kwenye Kamati kwamba waendelee kufanya kazi seriously. Mtu anashindwa kujibu halafu baadaye wanaongea pembeni kwamba hili suala ni zito sana, msilijadili sana maana huwezi kujua kwa nini halitatuliwi kwa miezi yote halitatuliwi, kutakuwa kuna kit utu. Wanataka kama kuanza kutishatisha watu, lionekane jambo sijui ni la nani? Halipo. kinachokuja kwenye Kamati tunajadili na tunakaza na watalifanyia kazi tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa leo nashukuru sana, lakini nasisitiza Katibu Mkuu wa Uchukuzi na timu yake wajitafakari. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Awali ya yote, naomba uniruhusu niweze kutoa shukrani kwa Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya TAMISEMI ingawa siyo Wizara hii, lakini waliweza ku-attend dharura ya Malinyi ya mafuriko ya maji yaliyoathiri barabara zetu. Fedha zimetolewa, sasa wakandarasi wapo site wanatatua tatizo Wanamalinyi watakuwa na amani hawataathirika tena na masuala ya mvua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wizara hii nina mambo mawili au matat. La kwanza, Jimbo langu la Malinyi lina changamoto ya mawasiliano, sehemu kubwa ya jimbo huwezi kupatikana, karibia asilimia thelathini au arobaini ya Jimbo ndiyo wanapatikana hewani, lakini zaidi ya asilimia sitini, sabini hakuna mtandao voice na data ndiyo kabisa ni changamoto kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka hivi ninavyozungumza Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na Ofisi ya Mkurugenzi hazipatikani kwa maana huwezi kumpata mtu hewani akiwa kwenye Ofisi hizo mpaka jioni wakirudi mtaani ndiyo unaweza wakapatikana. Kwa hiyo, naona Wizara inanisikiliza naomba walichukulie hili jambo kwa udharura watu Malinyi waweze kusaidika tuweze kupata mawasiliano kama maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia changamoto ya cyber-crimes kwa maana ya wizi wa mtandao umeendelea kuwepo. Mnakumbuka tulifanya usajili wa line kwa njia ya vidole ili kuweza kudhibiti changamoto hii, lakini mpaka leo hii bado watu wanafanya utapeli na namba ambazo zinatumika kufanya utapeli bado zinapatikana hewani mpaka hivi ambavyo ninazungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi binafsi ni muhanga wa jambo hili, watu wame-forge akaunti kwenye mitandao ya facebook wanawatapeli watu kuna masuala ya ajira mtume nauli na kadhalika ili ufanyiwe mipango, namba ambazo zinatolewa watu wanapiga bado zipo hewani na watu wanaendelea kutapeliwa fedha. Nimefanya majaribio kadhaa rasmi kwa maana ya kuripoti Polisi miaka miwili iliyopita, tumeandika barua, nimepewa RB naambiwa watu wa cyber wanafuatilia lakini mpaka leo wanaendelea kutapeliwa na tunachafuliwa heshima zetu. Sasa mimi ni
kiongozi nina access ya kusema, sijui watu wangapi kwenye nchi hii wanakumbana na adha ya namna hii na hawezi kusema. Kwa hiyo, naomba Wizara ilichukulie jambo hili serious.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, ni suala la mawasiliano ya simu katika vivutio vya utalii kwenye National Parks, Game Reserve na maeneo mengine. Kwa mfano, Hifadhi kama ya Mlima Kilimanjaro tuna watalii wengi wanapanda lakini asilimia 90 ya mlima ule mawasiliano hakuna. Watangazaji wazuri wa utalii ni watalii wenyewe, watalii wa ndani na watalii wa nje, watu wanapanda milima wanapenda ku-share experience yao moja kwa moja, watume picha kwenye mitandao, wafanye live video calls kuwahamasisha wengine lakini jambo hili haliwezekani kwa maana ya kwamba network hakuna kabisa mlimani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe tu Mheshimiwa Waziri alichukue hili washirikiane na Wizara ambayo ni mlaji ya Maliasili wahakikishe Mlima Kilimanjaro ambacho ni kivutio chetu kikubwa mawasiliano yawepo muda wote hasa ya data. Jambo hili linaendelea hata kwenye hifadhi zingine Ruaha, Ngorongoro maeneo mengine ya misitu yote yana changamoto kubwa za network. Kwa hiyo, naomba suala hili lichukuliwe kwa uzito kusaidia watalii kui-enjoy na kuwashawishi wenzao kwa kuona kwenye mitandao uzuri wa vivutio vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo changamoto pia ya doria, askari wetu ambao wapo porini wanafanya doria kulinda maliasili za nchi yetu, wanakutana na changamoto kubwa ya mawasiliano. Siyo mara zote radio call zinafanya kazi vizuri lakini mawasiliano ya simu yanaweza kuwa rahisi kuhakikisha watu waliopo kule porini wanafanya kazi vizuri, wanatoa taarifa kwa wakati, muda mwingine ni rahisi hata ku-track majangili, mambo ya kuviziana ni ya kizamani sana lakini technology ndiyo inafanya kila kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini Wizara inanisikia walichukue jambo hili, hata majangili ambao wapo porini wanapanga mipango unaweza ukawa-track kupitia technology. Maeneo makubwa ambayo yanaathari ya ujangili hayapatikani kwa simu tunatumia tu radio call. Kwa hiyo, naomba Serikali ilichukue suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa leo mchango wangu ni huu, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi. Awali ya yote nakupongeza wewe kwa kuteuliwa kuwa Mwenyekiti, lakini pia umetosha kwenye kiti kana kwamba ni mzoefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nitoe shukrani kwa Wizara ya Maliasili. Pamoja na changamoto nyingi za Bonde la Kilombero, nimekuwa tukipishana nao mara nyingi tunagombana, lakini walau kwa kidogo tunashukuru kwamba wametoa idhini wananchi wetu waliolima kule waweze kuvuna kipindi hiki ambapo mpunga upo tayari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hilo, niseme tu, natoa pongezi kwa Watendaji wa Jeshi USU la Uhifadhi, Kamishna wa Uhifadhi wa Ngorongoro Daktari Manongi; Kamishna wa TFS, Profesa Silayo Dos Santos, Kamishna Kijazi wa TANAPA, ambaye kwa sasa amepanda kuwa Katibu Mkuu wa Wizara. Nawapongeza kwa utendaji mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yote kwa yote, niseme utalii nchi hii unakumbana na changamoto kubwa mbili; ya kwanza, ni utegemezi wa aina moja ya utalii kwa maana ya utalii wa wanyamapori ndiyo sehemu ambayo tumelalia sana. Changamoto ya pili ni utangazaji wa utalii usiotosheleza. Kipande hicho hicho cha utangazaji wa utalii na chenyewe kina changamoto mbili; ya kwanza ni ufinyu wa bajeti; na ya pili ni ubunifu usiotosheleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika suala la kutegemea utalii wa aina moja, zaidi ya asilimia 80 au 90 ya watalii wanaokuja Tanzania wanaenda kwenye Hifadhi ya Taifa, kwenye Mapori ya Akiba na maeneo mengine mbalimbali ambayo tumejaliwa kuwa nayo. Ila ukiangalia takwimu za nchi ambazo zinafanya vizuri duniani na Afrika kiutalii kwenye kumi bora zote za Afrika, zimetajwa hapa asubuhi; Morocco, South Africa na maeneo mengine hawana vivutio vingi kwa maana ya wanyamapori, hawana hifadhi nyingi nzuri kama za kwetu, lakini wanafanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa jambo hili linatakiwa liifikirishe Wizara, Serikali na nchi kwa maana tunakoelekea utalii wa wanyamapori unaweza ukapotea na utalii mwingine mbadala ndiyo ambao unashika hatamu. Kwa hiyo, naomba Wizara ichukue hili kama changamoto. Tuna vivutio vya asili; ukiangalia beach ya Lake Tanganyika, kule Kirando na Kipili Nkasi, ukiangalia tuna kimondo pale Mbozi, Olduvai Gorge kule Ngorongoro na maeneo mengine mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utalii wa kitamaduni ni vitu ambavyo vinapendwa sana na watalii wengi. Kwa hiyo, naishauri Serikali tujikite kwenye maeneo hayo. pamoja na kwamba tunafanya utalii wa wanyamapori, lakini utalii mbadala hasa wa kitamaduni uweze kuzingatiwa na kuangaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya utangazaji wa utalii, nilizungumza suala la kibajeti, ni kweli bajeti yetu ni finyu, Bodi ya Utalii ambayo ina dhamana ya kufanya matangazo, imekuwa ikitoa fedha ambazo siyo toshelezi kulinganisha na nchi shindani, lakini hata hicho hicho kidogo hatufanyi ubunifu kuweza kukitumia vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninafahamu hata tufanye vyovyote vile hatuwezi kuwa na fedha nyingi kama nchi nyingine ambazo zimetajwa saa zile, lakini ubunifu ndiyo kila kitu. Nitolee mfano, kufanya matangazo ya utalii kwenye Media kubwa kama CNN kwa dakika moja haipungui milioni 200, 300 na kuendelea. Ukweli ni kwamba tunaweza tusimudu sana, lakini ubunifu ni kwamba television zote kubwa; CNN na Aljazeera na wengine wana vipindi vya Makala kwa maana ya documentaries, wanaonyesha uhaba wa maji Afrika, Sudan, Tanzania na kwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaweza kufanya lobbying tukatumia documentaries, tukawaalika wakafanya kama documentary kuonesha vivutio vyetu, sisi tunakuwa tumepitia humo humo, tukaonwa na dunia nzima kwa bei rahisi ambayo pengine inaweza ikawa bure kabisa kuliko kutegemea kujaza bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia bajeti ndogo ambayo imekuwa ikitolewa kwa ajili ya Bodi ya Utalii, maisha yangu yote ambayo nimekuwa Wizarani haikuwahi kutolewa hata kwa asilimia 90. Bajeti inatengwa, lakini fedha ambazo zinatolewa kwa ajili ya utekelezaji kazi ni ndogo mno. Kwa hiyo, katika hali hii hatuwezi kushindana na mataifa mengine ambayo yametutangulia Afrika na dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kuongezea kwenye ubunifu, nilikuwa naishauri Serikali, jambo hili Wizara ya Maliasili isaidiwe na Serikali kiujumla, kwa maana kwenye balozi zetu; watalii wengi tunawategemea wanatoka kwenye mataifa ya nje, tunawaagiza mara kadhaa mabalozi wafanye kazi kuleta watalii Tanzania, lakini unaweza ukakuta wenyewe hawana uelewa mkubwa juu ya suala la utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nishauri Wizara ya Maliasili na Mambo ya Nje wakashirikiana, tuwapeleke waambata wa utalii kwenye balozi zetu. Kuna waambata wa jeshi, kuna waambata wa idara, wapo kwenye balozi. Kwa hiyo, naomba Wizara ya Mambo ya Nje na Maliasili zishirikiane tuwaweke Maafisa Utalii kwenye balozi zetu waweze kuwasaidia mabalozi kuweza kutangaza nchi yetu. Kinyume na hapo, tutaishia kuwalaumu mabalozi tu, lakini kazi haitaonekana kwenye sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikihama kwenye eneo hilo, kuna suala la vita dhidi ya ujangili. Mara nyingi kumekuwa na malalamiko na Jeshi USU la Hifadhi kutokana na kutotosheleza kwa manpower, kwa maana wapiganaji ni wachache. Mara kadhaa TANAPA, Ngorongoro, TFS na TAWA wamekuwa wakilalamika pengine na kuhitaji nguvu kazi kwa ajili ya ziada. Niseme, jambo hili tuli-support lakini ushirikiano uwe mkubwa kwa Serikali kiujumla wake. Tukimwachia Maliasili peke yake hataweza kulingana na manpower aliyonayo. Kwa hiyo, naomba tu, Wizara ya Ulinzi, Wizara ya Maliasili kuunganishwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, wafanye ushirikiano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna vijana wanamaliza JKT, wanakaa kwenye makambi yetu, wanajitolewa miaka miwili kumwagilia maua, kupanda bustani; wamekuwa trained, wale ni askari, wachukuliwe, wapate short course kidogo ya uhifadhi, waripoti kwenye Jeshi USU la Uhifadhi, wakisimamiwa na Maafisa wa kule waweze kufanya operation ambazo zinapaswa hizo za kisheria. Kinyume chake tutalia suala la kuongeza askari, inaweza ikachukua miaka mingi tusiweze kumudu kupata idadi toshelezi, wakati tayari tuna nguvu kazi ya JKT au Jeshi la Wananchi Wapiganaji ambao wapo tu sasa hivi ambao ni ziada. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba hili jambo lisiachiwe Wizara ya Maliasili peke yake, askari wengine watumike, wapate course ya muda mfupi. Kule watalipwa tu posho kwenye paramilitary ile ya conservation, mishahara yao itaendelea kwenye majeshi yao ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano kwenye suala la TFS kwa maana Wakala wa Huduma ya Misitu, wamekutana na changamoto kubwa za kihifadhi. Doria zimekuwa ngumu, changamoto ni kubwa, askari wanalemewa hasa kwenye misitu yetu ambayo ipo karibu na mipaka. Kule Kigoma Misitu ya Makere Kusini na Kaskazini, majangili wamekuwa wakiingia kufanya uvunaji haramu wa misitu, TFS wanalemewa. Mara kadhaa kumekuwa na incidents wapiganaji wanazidiwa, wengine wanauliwa, mambo kama haya huwa hatutangazi, huwa hayasemwi, lakini yapo. Kwa hiyo, kuna haja ya Jeshi la wananchi au JKT kuongeza nguvu kwa TFS na Jeshi la Uhifadhi kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kuna suala la muundo mzima wa conservation paramilitary, Jeshi USU la Uhifadhi. Sasa kwa sababu masuala mengi ni ya kijeshi, siwezi kuyasema hapa, lakini nimeandika kitabu changu cha Maisha Yangu ya Uaskari kama Afisa wa Jeshi USU, humu kuna madini mengi. Naomba Wizara wakichukue, watapata vitu vingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kwa upendeleo, Jeshi la Uhifadhi kwa sasa lina-operate differently kwa maana ya kila…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, ahsante. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi na mimi pia ni Mjumbe wa Kamati ya Viwanda, Uwekezaji na Biashara. Nina masuala kadhaa ya kuzungumza, lakini kubwa zaidi ni suala la ugonjwa wa malaria hapa Tanzania. Ni jambo la Wizara ya Afya, lakini suluhisho la malaria lipo katika Wizara hii ya Viwanda kwa maana tuna kiwanda cha kuzalisha viuwadudu kipo Kibaha (Tanzania Biotech Limited) ambacho kinapaswa kuzalisha dawa zinazoweza kuuwa viuwadudu na kumaliza malaria hapa Tanzania. Hii ni ajenda ya Serikali tangu Serikali ya Awamu ya Nne, Serikali ya Awamu ya Tano na sasa Serikali ya Awamu ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni mshabiki au nina interest kubwa kuona kwamba malaria inakuwa zero Tanzania. Tunajadili sana kwenye Kamati masuala haya, lakini ninachokiona kinachotakiwa ni nia ya dhati ya Serikali kuhakikisha malaria inakuwa sifuri, lakini kwa sasa bado sijaona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni dhahiri nafahamu kwamba Waziri ameingia mpya Mheshimiwa Dkt. Kijaji, yeye ni mgeni. Nina imaninaye kubwa ninaamini anaweza kufanya kitu, lakini pia Wizara ya Afya ina Waziri Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa yuko pale Mheshimiwa Bashungwa, ninaimani nao kubwa sana wao pamoja na wasaidizi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi kiwanda kilijengwa na kimeanza uzalishaji mwaka 2016 kwa ajili ya kuzalisha hiyo dawa iweze kumaliza malaria. Kiwanda uwezo wake wa kuzalisha ni lita milioni sita kwa mwaka, lakini uhitaji wetu ili kumaliza malaria tunahitaji lita milioni tano na laki saba kwa mwaka. Mpango ulikuwa ndani ya miaka mitano Tanzania iwe na malaria free. Kwa hiyo, ukiangalia hapa uzalishaji na uhitaji wa lita milioni tano na laki saba kwa mwaka, maana yake ndani ya miaka mitano tunahitaji lita milioni kama 28 na gharama yake ya jumla ni kama bilioni 330. Kwa hiyo, kimsingi Tanzania haihitaji story nyingi, inahitaji bilioni 330 kufanya malaria sifuri, lakini jitihada ambayo sidhani kama imefanywa kwa ukubwa ambao unastahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kampuni hii kwa maana ya hiki kiwanda ambacho tunacho kilikuwa na mikataba miwili, kwa maana ya na taasisi mbili; ya kwanza na Kampuni ya Labio Farm ambao ndio wenye teknolojia ya uzalishaji wa hii dawa ya kule nchini Cuba. Tulikuwa na mikataba nao kama mitatu, wa kwanza watusaidie kujenga kiwanda, tuliweka fedha karibu shilingi bilioni 46 kiwanda kijengwe na kilijengwa pale Kibaha, lakini mkataba wa pili tulikubaliana nao watusaidie ku-transfer technology kwa maana ya kufanya management ya muda mfupi wa kile kiwanda kuwa-train Watanzania waweze kuzalisha dawa na baadaye tuwe free tuendelee kujitegemea. Mkataba wa tatu ulikuwa wa kutumia jina la brand yao, ile dawa ambayo inazalishwa kampuni yetu tutumie brand yao, tumesaini nao mkataba tumekubaliana nao ili tuweze kutumia zile dawa kwa maana kuweza kutumia lile jina kuweza kuuza nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa changamoto zipo kadhaa; kwenye mkataba wa kwanza kwa maana ya ujenzi ulishakamilika, lakini kwenye management, mkataba wa pili ulikuwa kidogo una shida kwa maana wale mabwana wakawa wanafanya management yote ya kwao, wanazalisha dawa kwa ukubwa na udogo ambao walifanya, lakini uuzaji wa dawa kwa asilimia nyingi ile kampuni kwa maana ya Labio Farm walikuwa wanauza wao. Wanauza dawa nje ya nchi na fedha nyingine mpaka leo Serikali tunawadai, kwa maana ya Tanzania inawadai hela wale mabwana wa Cuba, hizo fedha hawajatulipa mpaka leo ambazo wameuza dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia suala lingine ni suala la mkataba wa kutumia jina lao kwa zile dawa. Sioni kama hili jambo lina mantiki kwa sababu lengo letu la kwanza kufanya malaria iwe sifuri Tanzania. Tunashindwa kufanya hili jambo kuna sababu zilikuwa zikisemwa hapa kuna suala la ithibati, Umoja wa Mataifa kwa maana ya WHO hawajatoa ithibati kwa dawa ambazo tunazalisha pale Kibaha na hili jambo mchakato wake umechukua muda mrefu kidogo. Sasa nikawa nawaza unahitaji ithibati ya Umoja wa Mataifa kuuwa viuwadudu kule Nachingwea? Unahitaji WHO ije itupe ithibati ili Malinyi kule malaria iishe? Katika hali ya kawaida haiingii akilini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa hiyo, mimi jambo hili tumekuwa tumekuwa tukibishana nao muda mrefu na mpaka sasa suing mkono suala la mikataba hiyo ambayo ilikuwa imetokea. (Makofi)

Kwa hiyo, ninachoishauri Serikali management ya sasa ya Watanzania ina uwezo mkubwa, wameshajifunza kutoka Labio Farm wanaweza kuzalisha dawa vijana wetu, wanaweza kufanya hivyo, hilo jambo lifanyike mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kabla ya kuzalisha dawa kwa maana ya kabla ya operation pale kuanza Wizara ya Viwanda na Biashara kwa maana ya NDC ilisaini mkataba na Wizara ya Afya, ilisaini mkataba na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa tarehe 11 Machi, 2015 ili waweze kununua dawa yote ambayo itazalishwa pale. Kwa hiyo, maana yake kiwanda kile hakina haja ya kuhangaika kutafuta wateja, lakini kilisimama muda mrefu kwa kukosa wateja wa kuuza ile dawa ya kumaliza malaria. Wizara ya Afya ndio jukumu lake walisaini kukubaliana na NDC, lakini hawakununua dawa hata kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa unajaribu kuwaza, sitaki kutumia lile neno gumu ambalo huwa anatumia Mheshimiwa Halima, lakini nichukue tu la Mheshimiwa Kirumbe Ng’enda, kweli hii ni busara? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanda cha Serikali, fedha zilizojenga za Serikali, mteja anatakiwa awe Serikali Wizara ya Afya na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, halafu bado hainunui dawa zake yenyewe? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hali ya kawaida inafikirisha na muda mwingine inatia hasira, lakini sijaona seriousness ya Serikali kwenye kumaliza malaria Tanzania. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kushiria kwisha muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi kuwa mtu wa nne kuchangia jioni ya leo kwenye Wizara hii ambayo nina interest nayo kubwa sana kama mtu wa Malinyi na bonde la Kilombero hasa kutokana na changamoto ya Barabara. Nina masuala kadhaa hapa ya kuchangia yale ya jimboni kwa maana ya barabara yetu ya kwenda Songea kuunganisha Mkoa wa Morogoro na Ruvuma na pia kuna kipande cha kuunganisha Wilaya ya Malinyi na Kilombero kwa maana ya Mlimba kupitia kivuko. Vile vile kwa masuala ya kitaifa, kuna hili sakata la bandari ambalo linasemwa semwa, nami nitasema kidogo. Pia kuna suala la uchumi wa masaa 24, kwa maana ya kutamani kuona usafiri wa mabasi yanakesha hapa nchini na mwisho, kuhusu mabasi madogo (Costa Mini Buses) kutoa huduma kubwa kabisa kama mabasi makubwa.

Mheshimiwa Spika, nitoe shukrani zangu kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maana ametuheshimisha watu wa Malinyi na watu wa bonde la Kilombero wote. Imekuwa historia tangu dunia imeumbwa, sisi hatukuwahi kuwa na lami. Leo hii ukijadili Wilaya ya Malinyi, ni mara tano, yaani uchukue Mkoa wa Dar es Salaam wote uuzidishe mara tano au mara sita ndiyo unakutana na Malinyi moja na hatuna lami hata kilometa mbili. Kwa hiyo, hata watoto wanaozaliwa kule, lami ni mpaka uende Morogoro Mjini.

Mheshimiwa Spika, kwenye Kampeni tumesema sana tutakwenda kufanya jambo la lami kuunganisha Morogoro na Ruvuma kwa maana ya kupita Ifakara, Malinyi na kutokea Namtumbo kule, watu wanasema hii siasa ni uongo uongo, miaka yote mbona inasemwa? Litawezekanaje jambo hili? Hata mimi nilikuwa nazungumza, kwenye kampeni tumeahidi na nimeendelea kuwaambia Wana-Malinyi tutafanya, huku kimoyomoyo kidogo moyo unadunda, unaogopa, unasema hawa jamaa (Serikali) watasaidia kweli? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Rais amekwenda kunitoa hofu, amekwenda akuwafurahisha Wana-Malinyi, tunakwenda kusaini mkataba mwezi ujao kwa huu mtindo wa EPC+ F kwa maana ya kuunganisha Mkoa wa Morogoro na Ruvuma, Malinyi inakwenda kuwa na lami. Pia kipande cha kutoka Ifakara kwenda Ulanga - Mahenge inakwenda kuwa na lami, ni sehemu ya mradi huu mmoja. Kwa hiyo, namshukuru sana Mheshimiwa Rais na zaidi wasaidizi wake.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

TAARIFA

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nampa taarifa mzungumzaji, katika Mkoa wa Morogoro, kwa muda mrefu ilikuwa kilio cha Mkoa mzima wa Morogoro. Mkoa huu tangu tupate uhuru haukuunganishwa na Mkoa wa Ruvuma kama anavyosema mzungumzaji, siyo tu Mkoa tu wa Ruvuma, bali sasa historia inakwenda kuandikwa. Mlimba inakwenda pia kuunganishwa na Njombe. Kwa hiyo, Mkoa huu kwa mwaka huu wa fedha unakwenda kuunganishwa na Mikoa yote miwili, Ruvuma na Njombe kwa upande wa Mlimba na Malinyi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Kicheko/Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa niwakumbushe tu kwamba muda wa taarifa ni muda wa anayekuwa anazungumza. Mheshimiwa Antipas Zeno Mgungusi, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa, lakini naomba unisaidie hata dakika moja ya nyongeza muda wangu ukiisha. (Kicheko)

SPIKA: Hapana. Muda huu ninaotumia sasa hivi ni wa kwangu, kwa hiyo huu unalindwa. Kwa sababu nikiwakumbusha kila wakati, mnaona kama kiti kinawabana. Kwa hiyo, taarifa muwe mnaambiana wenyewe huko. Mkishakubaliana ninyi, mimi sina hiana hapa mbele. Kanuni zinawaruhusu kabisa. Mheshimiwa Mgungusi.

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwenye jambo hilo hilo, tunafahamu, nadhani mmekuwa mkiona hata kwenye taarifa ya Habari kila masika watu wa Malinyi tumekuwa tukilia mabasi yanakwama, Malinyi hapaingiliki wala hapatokeki. Hata juzi imetokea hivyo, lakini kwa mara ya kwanza kabisa hili jambo naamini linakwenda kuisha.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, kipindi hiki wakati tunasubiri hili jambo litokee barabara ianze kujengwa mwaka huu, basi ukarabati ambao unaenda kufanyika na watu wa TANROAD ufanyike kwa ubora ambao unapaswa. Sehemu kubwa ya maeneo ya barabara ambapo tunakwama ni matope ambayo wakandarasi huwa wanaleta wakati wa kiangazi, wanakarabati barabara inaonekana safi, ikija mvua tunapata shida kubwa. Kwa hiyo, niseme tu Mheshimiwa Waziri wasiliana na watu wako wa TANROAD, ingawaje wananipa ushirikiano mkubwa sana, wakandarasi awamu hii wasilete tope, wakati wa kiangazi kukarabati vije vifusi vya changarawe au mawe.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, ilikuwa ahadi yetu ya Chama cha Mapinduzi, naimi kama Mgombea wao wa Ubunge kuunganisha Wilaya ya Ulanga na Wilaya ya Malinyi kupitia kivuko pale Kikove kwa maana ya Kijiji cha Lupunga na Ngalimila kule Mlimba. Kwa mara ya kwanza mwaka huu inapaswa twende kuunganika, tutakuwa na kivuko. Ile pantoni itakuwa pale inaunganisha watu wa Malinyi, maana yake hata watu wa Njombe watakuwa wanapita pale kwa mwaka huu. Jambo hili linaonekana kama ni ndoto, lakini linaenda kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ila changamoto ni kwamba Mkandarasi ambaye yuko site hebu saidia kumkimbiza kimbiza. Mimi sitaki kugombana na wewe, ni mtu mzuri, umenipa ushirikiano mkubwa, nachoka kufuatilia mkandarasi mmoja mmoja. Kwa hiyo, naomba hili jambo ulichukue waweze kuharakisha kuhakikisha kwamba lile gati linakamilika kwa wakati tuweze kupitisha watu wa Malinyi na Mlimba kuungana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye masuala ya Kitaifa, kuna suala hili la bandari ambalo linazungumzwa; maboresho au kubinafsisha ile shughuli ya operation, menejimenti. Mimi binafsi kama mpenda maendeleo, naunga mkono jambo lifanyike kwa sababu kadhaa kubwa. Naamini ni vema mtumishi wa Umma ukawa mbunifu, ukabuni vitu vya kufanya kuhakikisha kwamba huduma zinakwenda vizuri na mapato yanaongezeka kuliko kutofanya lolote kabisa. Kwa hiyo, kubaki kama tulivyo kama bandari siyo jambo ninalotamani kuliona au kurudi nyuma tulikotoka, siyo jambo ninalotamani kuliona. Natamani tusogee, lakini ninaamini kwenye majaribio ya nia njema inaweza kutokea tukakosea mbeleni, bora likazungumzika tukifanya makosa mbeleni kuliko kutofanya mabadiliko kabisa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kimsingi nawatia moyo wale wanaofanya, watu wa Wizara endeleeni kusaidia. Matamanio yangu ni kwamba, hata TANESCO na taasisi nyingine za maji, sijui RUWASA na kadhalika ikibidi kupata private sector siku za mbeleni ikitufikirisha tufanye. Tunafahamu utendaji wa Serikali kidogo sehemu kubwa watumishi hawako serious sana, lakini private sector naamini inaweza ikafanya vizuri. Kwa hiyo, jambo hili naliunga mkono ila tu zile hofu za watu zijibiwe. Wengine wanasema kuna masuala ya usalama, wengine mapato yatakuwaje? Ajira za ndugu zetu zitakuwaje? Wale wanaohusika na Wizara wazijibu kuwatoa watu hofu, lakini ni jambo jema, mimi naunga mkono liendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu uchumi wa masaa 24, mnafahamu dunia nzima tunazunguka, watu wanakesha, mabasi yanakesha, sisi kwa nini tulale? Mnaona yale magari madogo ya IT yanaenda nje ya nchi, mnaona magari ya magazeti yanagombaniwa Dar es Salaam kila mahali kusafirisha watu usiku, kwa nini? Uhitaji ni mkubwa sana kusafiri usiku. Kwa nini sisi tulale? Wenzetu wa LATRA tunagombana nao, lakini najua wao wanasimamia sheria au maelekezo ya wakubwa kwa maana ya Wizara. Wizara ikiwaambia vinginevyo, watatekeleza kama wanavyoambiwa, hawawezi kujiamulia wenyewe. Naomba niishawaishi Wizara turidhie.

Mheshimiwa Spika, umekuwa ukilisemea sana hili. Hili jambo ni la kwako, umelisema muda mrefu, na sasa mabasi nafikiri yanaanza kuanzia saa tisa usiku. Kama unakubali saa tisa mabasi yaanze, kwa nini yasianze saa saba? Kwa nini yasianze saa mbili usiku? Kuna shida gani? Madereva ni wale wale. Kwa hiyo, naomba sana hili jambo Waziri wakati ana-wind up alisemee, atoe maelekezo, kwa sababu hata zuio la kusafiri usiku halikuwa kisheria. Tumefanya tu mazoea. Sisi tangu tukiwa wadogo kuna mabasi yalishatekwa, wakasema tusisafiri usiku. Sasa kama tunaogopa kusafiri usiku kuogopa majambazi, maana yake tunawapa umaarufu majambazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna Polisi, majeshi na kila kitu, tunaogopa majambazi kusafiri usiku, kwa nini? Kwa hiyo, hatutakiwi kuwapa wahalifu umaarufu mwepesi. Serikali inaweza kufanya, tutoe tamko, watu wasafiri masaa 24. Hamna suala la kusikilizia kusema tuanze kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, kuhusu mabasi madogo, kwa maana ya minibuses na Costa haziruhusiwi kupewa route rasmi kupeleka watu mikoani, lakini mabasi makubwa yanafanya. Mabasi makubwa hayana uwezo wa kumaliza watu wote. Nadhani mnafahamu barabarani, wote tunapenda kudandia magari ya kuunga. Kwa nini Costa hazipewi vibali au kufunguliwa zipate route kama mabasi makubwa? Wanafanya kama special hire; ukiwa na msiba unakodisha; ukiwa na shughuli za Kwaya, watu wanaenda wanakodisha. Kwa nini wasipewe route rasmi?

Mheshimiwa Spika, watu wakifariki, familiwa wanaruhusiwa kusafirisha msiba na kutumia Costa usiku, lakini mfanyabiashara akitumia Costa kupeleka hizo dawa ili watu wasife anaambiwa sheria hairuhusu, lakini wakifariki watu wake, anaruhusiwa kusafirisha. Haileti maana katika hali ya kawaida. Kwa hiyo, naomba kushawishi, naomba Bunge lako liridhie, kama Waziri akihitimisha lazima tusafiri masaa 24 na Costa ziweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, watu wa LATRA wanasema, sheria inataka basi angalau liwe na watu 40 ndiyo linaweza kusajiliwa kupewa route. Sasa mbona taxi ina watu wanne, lakini inasafirisha mtu Dar es Salaam mpaka Mwanza? Idadi ya watu inahusianaje? Hai-make sense. Kwa hiyo, naomba kuwafikirisha ndugu zangu, tusiwe na mawazo mgando, tubadilike. Basi linabeba watu 65 linapeleka Mwanza, taxi watu wanne inapeleka Mwanza, kwa nini coster yenye watu 29 au 39 haitakiwi kubeba mtu mpaka itimie 40? Mantiki ni nini kuhusu idadi ya watu? Suala security nafahamu tuna vyombo vyetu, vifanye kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la barabara kama siyo salama, TANROADS na mamlaka nyingine zifanye kazi zao. Sasa muda mwingine watu wa Serikali huwa wanaamua tu kuwaza kidogo halafu jambo tunalimeza wote, Mawaziri nao wanalichukua linakuwa jambo la kitaifa, lakini hai-make sense. Kwa hiyo, naomba nishawishi Bunge lako liridhie kama watu wa Serikali wataleta kama ni sheria, tuko ladhi kuunga mkono ibadilishwe lakini watu wakeshe barabarani. Tunalala ili itokee nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa leo, lakini nasisitiza kwamba namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa barabara yetu ya Malinyi kutokea Songea.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi kwanza nimesimama ku-withdraw mchango wangu wa leo kwa maana ya kwamba nimeshapata majibu jana kwa Waziri nimepata minara ya kutosha Malinyi na sasa wakandarasi wako site kwa hiyo sina cha kuchangia nashukuru UCSAF na Wizara ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii ya kuwa mchangiaji wa pili jioni ya leo katika Wizara hii ambayo nina maslahi nayo moja kwa moja. Kwanza, na-declare interest, hii ni Wizara yangu kwa maana nimefanya kazi kwa zaidi ya miaka 11. Nimefundishwa kazi na kulelewa na Wizara hii ambayo ninaipenda sana. Sasa nina machache ya kumshauri Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ni mgeni, sasa nichukue fursa hii kumshauri. Sina mengi ya kusema, labda mengine tutazungumza wakati mwingine, lakini leo nimshauri tu. Aidha, Bunge la Septemba, Novemba na yanayofuata kama tutaona tunayoshauri hayajafanyiwa kazi, basi tutaona namna ya kuzungumza, lakini kwa sasa nimshauri, sina cha kumlaumu na nimhakikishie leo sitashika Shilingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpitishe kwa mambo machache ambayo yako pending kwenye Wizara yake ambayo yanahusiana na maeneo yetu ya kijimbo na wananchi wetu. Kwanza, kwangu Malinyi na Bonde la Kilombero wanafahamu kuhusu Kijiji chetu cha Ngombo, ilizungungumzwa na Tume ya Mawaziri wanane kwamba Kijiji kile kifutwe kwa sababu ya sensitivity ya uhifadhi na kadhalika, jambo ambalo tulimalizana nao kwenye mkutano wa wananchi, lakini kilichofuata ni kwamba wananchi wanatakiwa wapewe fidia ili waweze kuhama pale Ngombo na kutafuta maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa jambo hili ni la muda mrefu tangu mwaka 2022, lakini hadi sasa hakuna kinachoendelea au hakuna ambacho Mbunge ana taarifa nacho. Sasa hofu ni kwamba mwezi wa Kumi na Kumi na Moja watu wanaandaa mashamba kulima, watu wa Ngomnbo sijui watalima wapi? Nasema hivi kwa sababu wanapaswa walime wapate chakula, ila wakilima watagombana na watu wa maliasili kwamba wamelima hifadhini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa nini wasitoke mapema wapewe hela yao kama ambavyo tumekubaliana? Sasa muda ukifika tutaanza tena kugombana. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri alichukue hili alifanyie kazi haraka. Ilikuwa ni jambo gumu kufikia hatua hii, lakini muda umefika, naomba liishe mapema ili watu wasije wakaonekana ni wakorofi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kulikuwa na biashara ya viumbe pori hai, wale wanyama na wadudu wadogo wanaosafirishwa kwenda nje ya nchi wanafanya watu wa TWEA, ilisimamishwa karibia mwaka 2016 leo miaka mitano au sita. Nilizungumza hapa Bungeni kipindi fulani, Serikali waliahidi watafanyia kazi, lakini juzi nimesikia hapa Mheshimiwa Waziri anatoa maelekezo kwamba huenda jambo hili likaruhusiwa na biashara ika-resume. Ni jambo la heri kabisa na ninawatakia heri na ninatamani kuona hilo linafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna suala la upandishaji hadhi pori la akiba la Kilombero (Kilombero Game Controlled Area) kuwa game reserve. Nimeona imefanyika na GN inatembea mitandaoni kwenye ma-group ya WhatsApp kwamba eneo hili limeshapandishwa hadhi sasa linakuwa ni game reserve na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina tatizo kidogo na hilo kwa maana sina shida na upandishaji hadhi wa maeneo, ndiyo umuhimu wa uhifadhi kulingana na sensitivity yake, lakini procedure yake sina amani nayo sana. Sasa nimesema nisizungumze sana ili tusigombane, Mheshimiwa Waziri ni mgeni. Nadhani wanafahamu kuna utaratibu wanapaswa kushirikisha wananchi tuweze kujadili mambo haya yaweze kwenda vizuri na mwisho wa siku tujue tunafanya nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya maeneo ya Kijiji yanaingia kwenye eneo hilo amablo linatajwa, kuna baadhi ya maeneo ya wananchi wa kawaida yanaingia mle. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri hili alifanyie kazi au tutazungumza na nitapata mrejesho kutoka ofisini kwenu. Tusijadili sana hapa kwa sababu nina vitu vingine vya kuvisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kuna suala la wanyama vamizi, (wanyamapori wasumbufu). Kule kwangu Malinyi tuna National Park ya Nyerere, bado kuna Selous na kadhalika. Tembo wamekuwa wakisumbua sana kama ambavyo wanafanya sehemu kubwa ya nchi, lakini bado usaidizi haupo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nimetoa hizi highlights uzichukue. Hata hivyo, bajeti ya mwaka 2022 niliahidiwa hapa kwamba Malinyi itakuwa moja kati ya wilaya kadhaa ambazo zitapata vituo vya kudumu vya Askari wa Wanayamapori. Nadhani TANAPA na TAWA wali-share, sasa natarajia kuona pengine wakati wa kuhitimisha utasema hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba nianze kuchangia. Nilikuwa nampitisha tu Waziri nina mambo makubwa mawili ya wizara hii. Kwanza, napenda nimshauri Waziri, natamani abadilishe thinking au approach ya conservation ya nchi hii. Pili, kwenye Jeshi letu la uhifadhi kwa maana ya Conservation Paramilitary, namna muundo wake ulivyokaa kidogo haujashiba na kidogo haujatosheleza. Kwa hiyo, haya ndiyo mambo makubwa mawili ambayo nilisema nataka nianze kuchangia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye approach ya uhifadhi ninaozungumzia, mara zote nimekuwa nawaambia wenzangu jambo la ushirikishwaji ndiyo kila kitu kwenye uhifadhi, na ninadhani dunia nzima ndivyo inavyotakiwa kuwa. Wizara yangu ambayo ninaipenda, we have been too militarily, kila jambo ni vurugu, kugombana, hata migogoro mingi ambayo inaendelea kila Mbunge akisimama hapa anazungumzia migogoro ni kwa sababu ya kutoshirikisha wananchi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kushirikisha kwa namna gani? Wananchi, wenzao ni wawakilishi watu wa kuchaguliwa kwa maana ya Mbunge na Waheshimiwa Madiwani kwenye maeneo yetu. Watu wa Serikali na hata ile Tume ya Mawaziri wanane, ukiwauliza wanasema, tumefanya ushirikishaji nchi nzima. Ushirikishaji wenyewe, wanaenda mikoani kuzungumza na Mkuu wa Mkoa, wanaenda Wilayani kuzungumza na DC, Wakurugenzi na vyombo vya ulinzi na usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi kiutaratibu unajua jeshini kiongozi huwezi ukawa unashauriana na watu wa ulinzi, kwa maana ya Polisi, wanajeshi wa kawaida hawa, watu wa uhifadhi ni maelekezo, “ndiyo Afande, jambo limekwisha.” Sasa unakuta Serikali inajadiliana yenyewe. Kwa hiyo, Serikali inatoka Wizarani wanakwenda kujadiliana mkoani ambayo ni Serikali tena. Wanashuka chini wanakwenda wilayani, wanazungumza na DC ambayo Serikali tena na watu wa kuchaguliwa kwa maana ya Wabunge na Madiwani ushirishwaji siyo mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nawashauri wenzangu, ili isionekane sisi ni wakorofi, hakuna mtu ambaye anataka mambo yaharibike au uhifadhi uharibike. Sisi Malinyi na Bonde la Kilombero Samaki ilikuwa unaokota bure kama takataka, tunakula hivyo, lakini leo samaki ni gharama kubwa Malinyi, Ulanga na Kilombero kuliko hata Dar es Salaam. Maeneo ni kweli yameharibika na kadhalika ni changamoto kubwa. Hakuna anayependa kuona uhifadhi unakufa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara kadhaa nimesimama hapa kueleza, mimi ni mhifadhi na nilishaapa na ni msimamo wangu, siko radhi kushiriki kuharibu uhifadhi kwa sababu ya umashuhuri wa kisiasa, lakini wenzangu hatuelewani kwa sababu hatusikilizani, approach yao siyo sahihi na mimi siwezi kunyamaza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa ninawauliza mara kadhaa, miaka ya nyuma Jeshi la Uhifadhi au niseme zamani maliasili nzima hatukuwa na silaha za kutosha, hatukuwa na magari ya doria ya kutosha, hatukuwa na Askari wa kutosha, lakini sasa hivi kila kitu kimeongezeka. Tuna Askari wengi, silaha za kutosha, tuna magari ya kutosha, lakini je, uhifadhi uko salama? Uhifadhi hauko salama. Sasa jambo hili linapaswa liwafikirishe kwamba they have to change approach ya conservation.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tushirikishe sisi tutazungumza vizuri na watu tuwaelekeze na tutakubaliana, mambo yatakwenda, lakini muda mwingi hawashirikishi Madiwani wala Wabunge. Wanasema hawa wanasiasa wakorofi. Wanafanya vikao kama siri. Jambo jema la conservation ni la wote, lakini linafanywa siri kama la magendo, Wabunge na Madiwani wanatengwa hawawashirikishi. Unaona mtandaoni vitu fulani vimeshafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ni mgeni kwenye Wizara hii, ni kijana lakini sina mashaka na uzalendo wako, nakupa nafasi, fanyia kazi. Naomba kwa sababu bahati nzuri wewe sio mhifadhi, nadhani ni mwanasheria, hebu tusaidie kubadilisha thinking approach towards conservation. Hatupingi, lakini wenzangu hawaelewi hawashirikishi wanataka waseme bwana hawa wenzetu wanasiasa wakorofi; sisi ni wanasiasa lakini pia wataalamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ni mhifadhi, lakini humu kuna wanasheria na pia kuna Ma-engineer. Kila taaluma iliyoko Serikalini iko Bungeni. Tushirikisheni tutafanya mambo yaende kuwa marahisi, hakuna kiasi chochote cha silaha au Jeshi, uhifadhi na kadhalika ambao kinaweza kusaidia uhifadhi upone bila ushirikishaji. Tusikilizeni, hata nikisema Waheshimiwa Wabunge tufanye vikao tutumie mafuta yetu tutafanya. Lakini wanakuwepo wanaangalia sijui DC, kule kwa Mkurugenzi wanaongea vikao vya ndani, mimi nakaa nawaaangalia, lakini mwisho wa siku utaonekana. Kwa hiyo mimi sisemi kwa sababu Waziri ni mgeni, tutaongea wakati mwingine in case nikiona mambo hayaendi kama ambavyo inapaswa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusu muundo wa Jeshi la Uhifadhi ambao upo sasa hivi. Kuna changamoto kadhaa, Mheshimiwa Waziri naomba uzisikilize. Ya kwanza Jeshi la Uhifadhi halina Mkuu wa Jeshi la Uhifadhi, kwa maana Kamishna Jenerali, kama Jeshi hili ni moja. Lakini ya pili kuna changamoto ya majina kijeshi kwenye vyeo ambavyo maafisa wadogo na wapiganaji wanavyo. Lakini la mwisho ni kuhusu mrundikano wa Makamishna wa Kanda wa Jeshi moja la Uhifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi hili nadhani mnafahamu, kama Jeshi lingine ambalo tunayo hususani Polisi, Magereza na kadhalika wana Makamishna Jenerali. Kwa hiyo nilitaka nijue kama Jeshi la Uhifadhi tumekubaliana ni moja basi lazima liwe na Kiongozi Mkuu pale juu lakini leo hakuna. Kamishna wa TFS anafanya mwenyewe, wa TAWA the same Kamishna wa Ngorongoro, Kamishna wa TANAPA kila mtu anafanya mwenyewe ndiyo final. Lakini nikawa nimeuliza hata swali siku moja hapa Bungeni, kwamba in case Rais anataka kuongea na Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama, Wakuu Jeshi la Uhifadhi mnampeleka nani? Hapa Wizara ikanijibu ikasema Katibu Mkuu ndiye anakaimu. Katibu Mkuu ni mtu mkubwa sana kukaa na hawa Makamishna Jenerali kwenye level. Hata hawa Wizara ya Mambo ya Ndani kuna Wakuu wale Makamishna Jenerali lakini pia kuna Katibu Mkuu wao, hata Jeshi la Wananchi kule kuna CDF Mkuu wa Chombo lakini kuna Katibu Mkuu, Maliasili kuna shida gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Mheshimiwa Waziri alifanyie kazi jambo hili na pia nishauri, washauriane jambo hili na ndugu zangu, pengine Makamishna wa Jeshi la Uhifadhi pengine najua wazee wangu labda wana hofa na wanasema mimi nitakuwa nani kukiwa na Bosi juu. Niwatoe hofu tunatengeneza mfumo wa kudumu kwa ajili ya nchi siyo kwa ajili ya kwao. Kesho wao hawatakuwa pale walipo kama ni Makamishna, kesho mimi sitakuwa hapa kama Mbunge. Kwa hiyo tutengeneze kitu ambacho kimekamilika. Mpaka leo hakielezeki kwa nini hakuna, haielezeki. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri naomba nikupe kama changamoto ili ulifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni kuhusu suala la vyeo vile vya kijeshi kwa maafisa wadogo pamoja wale wapiganaji. Mtu mwenye nyota mbili, wanafahamu majeshi yote hususani Magereza, Polisi, anaitwa inspekta, huku Jeshi la Uhifadhi hawatumii majina hayo wanasema huyu ni Conservation Officer One au Two na kadhalika. Yule Koplo au Sargent anaitwa Conservation ranger two and whatever, vitu vya namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikasema hayo ni majina mazuri lakini majina ya kiutumishi ya kiraia, kwa sababu hata Polisi mwenyewe anaitwa Police Officer, Magereza anaitwa Prison Officer, lakini military naming anaitwa Inspector au Assistant Inspector au Mratibu, wherever wherever. Kwa nini Jeshi la Uhifadhi hakuna? Haielezeki. Sasa shida naona ilianzia muda mrefu iliyoundwa kikosi cha raia huko katika Jeshi la Uhifadhi kutengeneza mfumo wa Jeshi labda ni shida ndio ilianzia hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba Mheshimiwa Waziri ulichukue hili ulifanyie kazi, ni vitu ambavyo havieleweki. Hawa maafisa wanapokutana na wenzao wa Jeshi la Polisi, Jeshi la Wananchi, wamevaa kiraia anataja cheo gani? Anasema mimi ni Conservation Officer Nyota mbili hizi sawasawa na Luteni unaanza kujieleza kwa nini. Jeshi halina maelezo ukishakiona kimesomeka straight forward; na kwa majeshi hili si jambo jipya. Sasa hawa TANAPA, TAWA, TFS Ngorongoro wanaonekana kama umekuja na kitu cha peke yako kutoka peponi ni suala la kukopi vyeo vya polisi ku-paste huku biashara imeisha, wakijichekecha nani anatosha wapi, lakini hawafanyi. Kwa hiyo nikushauri Mheshimiwa Waziri lifanyie kazi hili kwa sababu ni kituko. Jeshi jipya bado halija-commend…

MHE. AHMED M. SHABIBY: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

TAARIFA

MHE. AHMED M. SHABIBY: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ni kweli nataka kumsaidia mchangiaji, kama ni kweli hawa hawaeleweki, wana vyeo lakini havieleweki vyeo vyao ni vipi basi tuseme tu hawa ni Mgambo. (Kicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Antipas, unapokea taarifa?

MHE. ANTIPAS. Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napata ukakasi kwa jina alilolitumia lakini kimsingi ni kweli, ni Jeshi ambalo halijanyooka, sasa jina zuri sijalifahamu ni lipi. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri Mgeni nikushauri kwa nia njema kabisa hata mimi nilikuwa Officer nilikuwa Assistant Inspector nimestaafu nikiwa na nyota yangu pale nikikutana na wenzangu nimevaa kiraia nashindwa kujieleza, story ni nyingi. kwamba unajua hii iko vile, why? Nyota moja ni Assistant Inspector, inyooke hivyo. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri naomba hili ushauriane na makamishna usishauriane na watumishi wenzangu wa Jeshi hili, tafuta vyomba, kaa navyo, wapeni mfumo maelekezo watekeleze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwenye angle hii, nilizungumza, hata kitabu changu niliandika kuhusu maisha yangu ya jeshi, na nimeshauri vitu vingi sana. Tungekuwa Jeshi linalofanya kazi kwa umoja hizi division, TAWA na TANAPA, wangekuwa pamoja kusingekuwa na utitiri wa hivi vyeo na kadhalika. Leo hii kuna Kamishna wa TANAPA wa Kanda ya, lakini wakati huo TAWA nao wana Kamishna wa Kanda ya Kusini, TFS wanafanya vivyohivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huku Iringa, Mbeya kuna Kimondo sijui kuna vitu kama viwili vya Ngorongoro. Kwa hiyo Ngorongoro nao waweke Kamishna wao kwa ajili ya vitu, havieleweki. Alipaswa awepo mtu mmoja ndiye awe Kamishna wa Jeshi la Uhifadhi wa Kanda fulani, wengine wote wadogo wenye station watalipoti kwake na yeye atapeleka juu. Lakini kinachofanyika sasa hivi kwa kweli sina imani nacho. Naamini wenzangu Wizarani mnakiona, naongea kwa nia njema kabisa. Tunatengeneza mfumo wa jeshi ambao umenyooka na si kwa ajili ya mtu mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi. Mheshimiwa Waziri natamani Bunge la mwezi wa tisa tusiongee mambo haya na wala tusigombane. Nashukuru sana, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi. Nina masuala kadhaa hapa ya kuchangia, kwanza ni migogoro ya ardhi baina yetu wananchi wa Bonde la Kilombero na Wizara, lakini suala la biashara ya viumbepori hai ambayo imesitishwa, suala la kutaka Jeshi la Uhifadhi li-retain mapato yake, pia ukamilifu wa Jeshi la Uhifadhi na mwisho masuala ya wastaafu kama muda utaniruhusu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitoe shukrani kwa Serikali, hasa kwa Mheshimiwa Rais kwa kuunganisha barabara yetu ya Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Ruvuma kwa lami ambapo kwa sasa haipitiki. Tumetajwa kwenye mpango kupitia Mpango wa EPC + F. Natoa shukrani sana kwa hilo kwa niaba ya wenzangu wa Ruvuma na wa Malinyi, pia kuna suala la vifo vya wananchi na usumbufu kwenye mazao kutokana na tembo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipiga kelele na mwezi huu nadhani mlisikia wananchi watatu wa Malinyi walipoteza maisha kutokana na ajali ya tembo, lakini bahati nzuri Wizara imeridhia wametuweka kwenye mpango tutapata kituo cha kudumu cha Askari Wanyamapori kule Kilosa kwa Mpepo. Kwa hiyo, kwa hayo natoa shukrani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni Mhifadhi Mstaafu. Nimehudumu Wizara ya Maliasili na Utalii miaka kadhaa, nikahudumu katika Jeshi la Uhifadhi kama Afisa Askari miaka kadhaa, katika maisha yangu yote niliapa kwamba, sitakubali kushiriki kuharibu uhifadhi kwa sababu ya umashuhuri wa kisiasa, huu ndiyo msimamo wangu mpaka sasa hivi. Tofauti napishana na wenzangu jambo dogo tu, kwa maana ya wahifadhi wenzangu wa maliasili na wale mabwana Waheshimiwa Mawaziri Nane ambao walikuwa assigned ku-solve migogoro ya nchi hii. Shida yao kubwa ninayopishana nao ni approach, namna gani wana-enenda katika suala la ku-solve migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwangu katika Bonde la Kilombero kwa maana ya Wilaya ya Malinyi na majirani Mlimba, Ulanga na Kilombero tuna migogoro na Wizara kwa namna mbili. Kwanza kuna Kijiji kinaitwa Ngombo kule kwangu Malinyi, wananchi wanaishi pale tangu mwaka 1935, thelathini na kitu mpaka leo, lakini pia lile bonde limekuwa hifadhi mwaka 1952, iliwekwa GN. 107 na wakoloni tangu kipindi kile mpaka leo Wizara ime-maintain.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi hatuna tatizo. Nafahamu kulingana na uhifadhi eneo lolote likionekana ni nyeti kuna haja ya kuhifadhiwa, Serikali inaamua inafuata utaratibu na inakuwa hifadhi. Kama kuna wananchi, wanapisha, ndiyo utaratibu. Kwa hiyo, nilitarajia watu wa maliasili na Mawaziri Nane walipaswa kusema tunatambua Kijiji cha Ngombo ambacho kimesajiliwa na Serikali, wananchi wanaishi miaka hiyo kabla hata uhifadhi pale kuanza. Tunafikiria kuna haja ya watu kutolewa kwa sababu ya mradi wetu wa Stigler’s Gorge na vitu vya namna hiyo kama kuna haja. Wangetusikiliza, tusikilizane nao, pengine tusingeweza kubisha. Watu wa maliasili mara zote wamekuwa wakiimba hata wakijibu maswali yangu hapa walikuwa wanasema wananchi wamevamia kule Ngombo, wamefanya maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuwa nawauliza walivamia mwaka gani? Ukisema umevamia lazima uwe specific utaje mwaka gani wamevamia? Hawakuweza kutaja na mpaka kesho hawataweza kwa sababu wananchi wameanza kuishi kabla ya uhifadhi. Kwa hiyo, sisi hatuna shida sana na hilo, nilikuwa nasema suala la approach.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekubaliana Mawaziri Nane wamekuwa assigned, wakati tunawasubiri wao wafanye maamuzi ya mwisho kuhusu Kijiji chetu cha Ngombo, wananchi waendelee na Maisha, watakapoamua tutachukua kile ambacho Serikali itasema, lakini mpaka sasa maamuzi hayajatoka, wananchi kule tunalima kwa kubahatisha, Askari Wanyamapori wa TAWA kila mara wamekuwa wakiingia kufanya doria. Watu wanaishi kuna nyumba, kuna shule, kuna kila kitu, tunaendelea kuishi mpaka leo, wananchi zaidi ya Elfu Nne.

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa, Mheshimiwa Naibu Waziri.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa Mheshimiwa ambaye amemaliza kuzungumza sasa kwamba, ni kweli kuna Kamati ya Mawazi Nane ambao wamezunguka, lakini Kijiji cha Ngombo hakiko kwenye hifadhi ambayo watumishi wa TAWA wanasimamia mapori. Pori ambalo linasimamiwa na watumishi wa TAWA ni Pori la Kilombero. Kijiji cha Ngombo kiko mbali kidogo na Pori la Kilombero. Kwa hiyo, haya maamuzi siyo kwamba ni ya uhifadhi wa maliasili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa tu mzungumzaji kwamba, maamuzi ya Baraza la Mawaziri hayakuangalia pori hili kwamba linasimamiwa na watu wa Maliasili, isipokuwa vyanzo vya maji viliangaliwa kwenye eneo ambalo ni kijiko au bakuli ambalo eneo hilo Kijiji cha Ngombo kiko ndani yake. Tuliangalia hilo kwamba, eneo hili ni mahsusi kwa ajili ya mchango mkubwa wa maji ambayo yanatiririka kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere, ahsante.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Antipas.

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri Mary Masanja ninaheshimiana nae, ninajisikia vibaya kumsema vibaya kwa hiyo, ninamsitiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi Kijiji cha Ngombo hata ukichukua ramani mpaka leo wanakijadili kwenye Pori Tengefu la Kilombero kipo katikati ndiyo ukweli wake, kipo katikati. Kama hafahamu, nadhani anafahamu, wanaruka na ndege mara nyingi kipo katikati, aidha hakumbuki au pengine hafahamu au anajisahaulisha, sitaki kumsema vibaya. Namsitiri, naomba nisizungumze juu ya hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuliomba na mimi niliomba Kijiji chetu cha Ngombo kulingana na unyeti wake kama kinataka kitolewe it is ok, pengine tunaweza tukaridhia, niliomba tupunguze hata ukubwa wa Kijiji tuko radhi tubki eneo letu la asili dogo, watu waendelee kuishi, watu wanaishi pale miaka mingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mnamfahamu Waziri Juma Ngasongwa kazaliwa mwaka 1941 katika Kijiji cha Ngombo, kasoma shule ya msingi pale Ngombo, Shule ya Msingi ipo kabla ya mwaka 1950, wao wanasema wananchi tumevamia! Mzee wangu Mzee Zeno Mgungusi Mhifadhi, kazaliwa Ngombo, kasoma shule ya msingi pale kabla ya uhifadhi. Hawa wanaendelea kusema tumevamia, siyo sahihi! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi niliomba, sibishani na Serikali, nimeomba tuko radhi kupunguza ukubwa wa Kijiji sehemu nyingine iwe hifadhi, sehemu ndogo ibaki tuendelee kuishi. Kama mnafahamu kabila linaitwa Wandamba akina sisi, akina Joti, akina Ngasongwa, akina Beno Ndulu wote asili yatu ni Ngombo. Tuko radhi tupunguze ukubwa wa Kijiji libaki eneo dogo tuweze kuishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukisema tusifanye kilimo kikubwa cha matrekta na kadhalika tuko radhi, nilisema …

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Antipasi lakini bila maji vilevile hamtaweza kuishi.

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, naam.

NAIBU SPIKA: Bila maji hamtaweza kuishi. Maji alikuwa anazungumzia Mheshimiwa Waziri hifadhi, bila maji hamtaweza kuishi. Wewe endelea na mchango.

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa, ninalifahamu hilo ndiyo maana nimetoa mapendekezo. Tulikuwa tunaomba tuko radhi kupunguza idadi ya mifugo hata kwa asilimia 90, tupunguze ukubwa wa Kijiji hata kwa asilimia ngapi, nilitoa maombi nilikuwa natarajia Serikali ikubali, lakini hata kama ikikataa sina tatizo, basi wafanye maamuzi kwa wakati. Kama wanasema hatusikilizi mawazo ya Mbunge tunataka watu watoe it is ok, waseme hata kesho, mimi kama Mbunge nitatoa ushirikiano.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wanashindwa kuamua kila siku tunaviziana, tunaviziana. Mpaka sasa hivi ninavyokuambia watu wamekamatwa kule wananyang’anywa mchele, wananyang’anywa mpunga, watu wanaishi mpaka leo. Toeni tamko kwamba watu waondoke, tunaondoka, sasa hamsemi. Kila siku mnasema Mawaziri Nane wanakuja kesho, Bunge lijalo, kesho, Mimi Mbunge nifanye nini? Tukisema mtaanza kusema Mbunge mkorofi anaonea Serikali, sasa mimi nitakuwa Mbunge wa namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatakiwa iwe serious, wafanye maamuzi, kama mnataka mtutoe basi isemwe hata kesho, mimi kama Mbunge sitabisha, nitawaambia watu wangu, tutatoa ushirikiano wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili mgogoro huo ni mpaka. Kuna mpaka wa mwaka 2012 wa hilo Bonde la Kilombero lote, Majimbo Manne ya uchaguzi. Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori (TAWIRI) ilisema ili bonde liwe salama mpaka ukae hapa na tukaweka mpaka 2012. Wananchi tumeshirikishwa, tumeridhia, hatuna shida, lakini 2017 ukaja mpaka mwingine kuja kuchomekwa, wamekuja watu wa maliasili wameweka beacon mpaka ambao mpaka leo hauna GN, lakini mpaka leo kuna watu wamewakamata wamepewa kesi za uhujumu uchumi, wapo ndani ya hifadhi, lakini kwenye mpaka ambao hauna GN.

Mheshimiwa Naibu Spika, hilo nalo mimi silibishii, wakisema na huko tuache kulima tutaacha, nitawaambia watu wangu, lakini Serikali watamke wanapochelewa kufanya maamuzi maana yake wanatuweka sisi kwenye wakati mgumu. Mnataka sisi tunyamaze, sasa mimi nitakuwa Mbunge wa namna gani? Tukisema mnasema tunaionea Serikali, mnataka tufanyeje? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siasa zetu zinakuwa ngumu, wenzetu Mawaziri Nane watusaidie. Ninajua muda mwingine tunagombana na watu wa maliasili, watu wa TAWA, TANAPA, wanaonewa, lakini nadhani asilimia kubwa ni wale Mawaziri Nane ndiyo tatizo. Huu ni mwaka wa Sita tangu Tume imeundwa! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kituko kingine hawa Mawaziri Nane hawajawahi kukanyaga Malinyi, hawajawahi kufika hata pale Mlimba, wanaruka na ndege tu juu Kilombero wanaondoka, hawajawahi kufika, lakini pamoja na hayo mimi sijali sana, fanyeni maamuzi sitabisha. Msitutafutie lawama tuonekane wajeuri naomba mfanye maamuzi tutazingatia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hilo, suala la pili ni suala la Mheshimiwa Waziri wa Fedha anahangaika kutafuta vyanzo vipya vya mapato fedha zipo Maliasili. Kuna biashara ya viumbehai pori kwa maana ya wadudu, kusafirisha wadudu nje ya nchi, hawa panzi mnawajua, kumbikumbi, sijui vinyongana kadhalika. Biashara hii ilikuwa inafanyika tangu uhuru Mwalimu Nyerere anaifahamu, walikuwa wanafanya Wazungu, badaye Shirika la TAWICO likapewa kazi ya kusafirisha wadudu nje ya nchi. Mwalimu Nyerere akazuia akasema wazawa wafanye hii kazi mwaka 1967 mpaka leo Watanzania walikuwa wanafanya biashara ya kukamata wadudu wanapeleka nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maliasili na Utalii ilizuia mwaka 2016, Machi 2017, Waziri Maghembe alitoa sitisho hawa wadudu wasipelekwe nje ya nchi tena, nadhani ilikuwa kwa miaka mitatu, lakini mpaka leo mwaka wa sita, wale wafanyabiashara walishalipia kila kitu, wamelipa leseni, wamelipa kodi, wametumia gharama zote, tangazo limetolewa ghafla la kusitisha na tangazo lenyewe nadhani halikuwa kisheria, wale wafanyabiashara wamepata hasara zaidi ya Bilioni 1.6 Serikali haijawarejeshea.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo wakisema waende hata Mahakamani ni kesi nyepesi, mnaitia hasara Serikali, kwa nini? Wanasheria huko maliasili wapo, mnashindwaje kuishauri Serikali ama wawalipe fidia, lakini wenyewe wanazungumza hawana haja sana ya fidia wanachotaka wafungue biashara iendelee?

Mheshimiwa Naibu Spika, pengine najua kuna hofu, wengine wanasema wadudu wetu wanasafirishwa nje ya nchi, kule Wazungu watawazalisha watakuwa wengi, wakiwa wengi wadudu Wazungu hawatakuja kutalii Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa wale wadudu hawakamatwi hifadhini wanakamatwa mitaani, pili mnafahamu Wizara ya Kilimo inatenga bajeti, dawa ya kuuwa wadudu…

NAIBU SPIKA: Ahsante, kengele ya pili hiyo. Malizia sekunde kumi, ahsante.

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, aah, umeniongezea.

NAIBU SPIKA: Eeh, sekunde kumi.

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, hawa wadudu bajeti wanatenga Wizara ya Kilimo kuua ndege kweleakwelea, kuuwa viwavidudu, wale sijui viwavi jeshi na kadhalika, ambao wanaathiri mashamba ya watu. Wale wadudu ni deal watu wanawahitaji, wanakamatwa mtaani wanapelekwa nje tunapata fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hatupati fedha, tunatumia fedha kuwauwa wadudu ambao wanatakiwa kule Ulaya, kama kulikuwa na kutokuwa na uadilifu kwa wafanyabiashara au watendaji haipaswi kuwa kisingizio. Kwa hiyo, ninaomba Serikali ifungulie biashara ya viumbepori hai tuweze kupata fedha za kigeni tupate mapato. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Awali ya yote naunga mkono hoja iliyowasilishwa.

Mheshimiwa Spika, pili nataka tu kukumbusha Wizara kwa maana Waziri tulishafanya mawasiliano kadhaa kadhaa kuhusu Wilaya yetu ya Malinyi kuna shida ya usafiri kwa maana ya Polisi wanahangaika namna ya kufanya kazi. Kwa hiyo, nilishafanya mawasiliano rasmi na Ofisi ya Waziri ninaamini wanalifanyia kazi ninawakumbushia tu. Mtu yoyote akisikia Malinyi afahamu maana yake ni Wilaya ambayo ina ukubwa zaidi ya mara nne ya ukubwa wa Dar es Salaam yote. Kule kuna migogoro mikubwa sana ya wakulima na wafugaji hali ambayo inaleta ugumu Polisi kufanya mobility kufika kila angle. Malinyi inakaribia square meter 10,000 kwa hiyo unaweza ukaona zaidi ya mara tano mara sita ya Dar es Salaam na maeneo mengine. Kwa hiyo, uhitaji ni mkubwa sana kwa ajili ya sisi kusaidika, kwa hiyo niombe tu Mheshimiwa Waziri atoe kipaumbele mgao wa magari ambao utakuja lakini hata kama yapo mahali ya akiba yaliyotumika sisi tutayapokea uhitaji ni mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili suala la Jeshi la Magereza. Tumeangalia hapa katika taarifa yao kuna masuala mengi tu kuna sehemu bajeti zimewekwa za ujenzi wa Magereza, lakini naamini bado haitoshelezi. Mimi ni mjumbe wa Kamati ya Bunge ya masuala ya UKIMWI, tumefanya ziara Magereza mengi msongomano ni mkubwa sana, sana. Mahabusu ni wengi kuliko wafungwa wenyewe, sasa hili jambo limekuwa maarufu tangu mimi nikiwa mdogo tunasikia msongamano, msongamano lakini sijaona jitihada kubwa ile ya moja kwa moja ya kumaliza changamoto hii. Nimeona kwenye taarifa wameandika kuna masuala mengine vifungo vya nje na kadhalika, lakini bado uhitaji wa Magereza ni mkubwa. Hata tuweke kwa bajeti kwa namna gani Jeshi la Magereza halitokaa kamwe liweze kujenge Magereza ya kutosha. Wizara ya Mambo ya Ndani peke yake hata tuiache yenyewe haitoweza kumaliza changamoto hii. Kwa hiyo nilikuwa natoa ushauri kwa Serikali suala la ujenzi wa Magereza iwe kampeni ya Kitaifa kuisadia Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, mtakumbuka tulisadia kwa pamoja kampeni ya ununuzi au ujenzi wa madarasa. Mheshimishiwa Rais ametoa fedha tumejenga madarasa kila mahala lakini hata kampeni ya madawati mtakumbuka miaka miwili, mitatu iliyopita ilikuwa ni ajenda ya Kitaifa siyo suala la TAMISEMI, wala siyo suala la Wizara ya Elimu kila mdau, kila Taasisi iilipambana kuhakikisha tunafakisha jambo hili na tulifanya sehemu kubwa, ninaomba nguvu ileile iletwe Wizara ya Mambo ya Ndani tuisaidie Jeshi la Magereza kuweza kupata Magereza mengi.

Mheshimiwa Spika, Malinyi tuna maeneo makubwa kama kuna uhitaji tuko radhi kutoa maeneo kule Magereza kule ijengwe. Lakini naomba tu wale ambao hawajawahi kutembelea Magereza wajue kule hali ni mbaya sana. Kwa sababu Magereza wateja hawapelekwi kwa hiyari kama shuleni, au hawaendi kwa hiyari kama hospitali ndiyo maana Taifa linaweza lisione ukubwa wa changamoto ya msongamano. Lakini suala la shule kila mtu anaguswa kwa sababu anapeleka watoto, Hospitali, Zahanati kila mtu anapeleka kule wagonjwa ndiyo maana tunaona kila siku, lakini Magereza ni tofauti. Kwa hiyo niombe tu Serikali suala la ujenzi wa Magereza iwe kampeni ya Kitaifa. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi. Mimi pamoja na mambo mengine ni mwanataaluma wa Michezo, Wizara hii nasema inanihusu sana. Mimi ni Mwalimu wa Mpira wa Miguu kwa taaluma, nina Diploma C ya CAF. Kwa hiyo nachangia kama mdau wa michezo sio tu wa siasa peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kuendelea napenda nitoe pongezi kwa rafiki yangu Paul Nonga ambaye ni kocha mwenzangu, mchezaji wa Mbeya City. Leo ni siku yake ya mwisho kuwa kama mchezaji wa mpira. Ametumikia nchi hii zaidi ya miaka kumi kucheza mpira Yanga na timu zingine pamoja na Timu ya Taifa ya Tanzania. Kwa hiyo namtakia Kheri katika maisha yake mapya ya ualimu na menejimenti ya mpira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze ndugu yangu Waziri, Mheshimiwa Pindi Chana na Mheshimiwa Hamis Mohamed Mwinjuma kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kuchukua nafasi ya kuendesha Wizara hii. Mimi nina matarajio makubwa kwao na nawapongeza, naamini kabisa watafanya kitu kutusogeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nina machache tu nataka niwapitishe Waheshimiwa Mawaziri, ni highlights, lakini kubwa zaidi wanafahamu kuna changamoto hii ya jana au juzi kulikuwa na tuzo hizi za wasanii, Mheshimiwa Khadija hapa amezungumzia. Wasanii kutokuwepo ukumbini, kwangu mimi hilo sio kubwa sana, lakini la kwangu nimesikia uvunguni watu wanalialia kwamba tuzo zilikuwa mikono mitupu hazikuwa na chochote. Mwaka jana watu walipata fedha kidogo angalau motisha, lakini mwaka huu kulikuwa hamna kitu, imesikia, wanalalamika uvunguni. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri naomba alifanyie kazi, kama sio sasa hivi basi wakati ujao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, linguine, naomba Mheshimiwa Waziri anisaidie kuzungumza na Baraza la Michezo la Taifa. Najua kuna masharti ya usajili wa vyama vya michezo. Mimi ni mdau wa mchezo wa kuvuta kamba, nimekuwa Mwalimu wa kamba Timu ya Bunge na nimewezesha timu hii kuweza kushinda Ubingwa wa Afrika Mashariki kwa upande wa Mabunge kule Arusha, nadhani wengi watakuwa wanakumbuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa sasa ni matamanio yangu kusajili Chama cha Mchezo wa Kamba. Masharti yanataka kila wilaya kuwe na vyama na nini iendelee mpaka juu, nafikiri ndio sheria, wako sahihi, lakini naomba tuombe kama special case, michezo isiyo maarufu iweze kuanza na tuweze kwenda mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nina mambo mawili makubwa ya kuchangia leo. La kwanza, ni namna ya kupata Timu ya Taifa kwa baadaye kwa maana ya kutengeneza watoto wetu, lakini la pili, manung’uniko yangu au discomfort kwa namna ambavyo Chama cha Mpira Tanzania wanafanya. Kabla ya kwenda popote niwapongeze tu hao watu wa TFF, menejimenti ya sasa wakati wao tunaona achievement kubwa kwa mpira wetu wa Tanzania. Timu ya Walemavu, Timu ya Wanawake, Timu za Simba na Yanga zimekwenda mbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Yanga juzi ametoka fainali bahati mbaya hakuchukua, tunawapa pole, lakini tunawapongeza kwa hatua. Kwa hiyo yote haya mazuri ambayo yanasemwa ni wakati wa Menejimenti hii ya TFF. Kwa hiyo nawapongeza sana wale seating leaders.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Baraza la Michezo la Taifa, kiongozi yupo pale mtendaji Neema Msita binti mdogo na timu yake, wengine wote kiujumla nawapongeza kwa sababu haya yote mazuri ya nchi hii yametokea wakati wao wako madarakani. Kwa hiyo niseme tu wanastahili pongezi nawashukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kuhusu Timu za Taifa; nadhani tuafahamu wachezaji wengi tunawaona wakiwa wameshakuwa maarufu kwenye Vilabu vya Ligi Kuu, tunawaita National Team, lakini sidhani kama kuna mtu anawajua wachezaji wa Timu ya Taifa ambao wapo leo, lakini miaka kumi iliyopita au kumi na moja tulikuwa tunawafahamu wakiwa wadogo, ukweli hatukuwafahamu. Kwa hiyo kulingana na uchache wa muda naomba tu nishauri machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, niombe jambo hili la kutengeneza future ya Timu yetu ya Taifa liwe la Serikali kiujumla kwa maana ya TAMISEMI na Wizara ya Michezo na Wizara ya Fedha tulichukue liwe jambo la kwetu. Napendekeza Halmashauri zote nchini zielekezwe na Serikali kuwa na academies, kuwe na timu za watoto under twelve, under seventeen zisimamiwe na halmashauri wenyewe. Watu wa TFF au watu wa Serikali kwa maana ya Wizarani watatoa tu utalaam kule chini. Watakuwa na timu ya wataalam kwenda kuangalia facilities ziweje.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

TAARIFA

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mgungusi, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Sanga.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, anachokizungumza Coach wangu pale ni kitu right kabisa. Kwa Afrika the best development modal ya soka iko Zanzibar ambayo wameitumia Ghana, wameitumia Nigeria, wameitumia Cameroon. Kwa hiyo mfumo mzuri wa kuzalisha wachezaji, upo kwa majirani zetu Zanzibar ambao tunaweza tukautumia na tukazalisha wachezaji wazuri kwa kuwa na academy kwenye kila eneo. Ahsante.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mgungusi, taarifa unaipokea?

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa na nashukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni hilo nilikuwa nakazia tu. Kuna kila sababu ya zile halmashauri zetu ziweze kuwa na timu. Tunatenga fedha mapato ya ndani kufanya vitu kama zahanati na vingine vingi vya msingi, lakini jambo la michezo kuwa na timu za watoto kwenye halmashauri ni jambo la msingi. Tunajua unaweza kuwa mzigo mkubwa sana kwa halmashauri, lakini Wizara ya Michezo, Wizara ya Fedha iweze ku-subsidize.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapelekewa kule chini fedha za maendeleo hata fedha ya kulea hizi academy kule halmashauri ziwepo. Tuna Walimu wengi wanazalishwa na TFF, hawa watu wanasoma intermediate level wengine wanasoma preliminary ualimu, wengine diploma C, wapo mtaani wanazurura wangeweza kupata ajira kwenye halmashauri zote kuwatengeneza watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mtoto anatengenezwa, professionally tangu akiwa mdogo ana miaka 12, ana miaka 10, akifika huko juu anakuwa na uelewa mkubwa kuliko leo, mtu anatokea mtaani amejilea mwenyewe, anakuja kukutana na Coach Professional akiwa tayari mkubwa amezeeka, hafundishiki. Ni changamoto kubwa, wengine watalaumiwa wahuni, hawazingatii, hawafundishiki kwa sababu ya mazingira kama hayo. Kwa hiyo naomba hilo tu nishawishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, linguine, tumwombe Mheshimiwa Rais kama tunakwama. Ametoa fedha tumejenga madarasa nchi nzima. Miundombinu mingine mingi ya Barabara, kila Jimbo limepata fedha, amesaidia, sidhani kama atashindwa kutusaidie kujenga viwanja vile vya standard nzuri kwenye kila halmashauri, halafu mambo ya malezi tutafanya wenyewe kama halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, ni suala la manung’uniko yangu. Kutokuwa na furaha na amani namna ambavyo ndugu zangu TFF ya leo wanaendesha hii hali ya mpira wetu. La kwanza kabisa, tunafahamu na wenyewe wanafahamu na Wizara pengine inafahamu kumekuwa na malalamiko mengi dhidi yao. Pengine najua wako kwenye nafasi nzuri kama hizo za maendeleo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Muda wako umekwisha, malizia sentensi.

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naam.

MWENYEKITI: Kengele ya pili imelia, kwa hiyo muda wako umekwisha.

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sekunde chache nimalizie.

MWENYEKITI: Sekunde thelathini, malizia.

MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Waziri, naomba asimamie, kuna wataalam ambao ni Walimu wetu wa mpira wanadai TFF fedha waweze kulipwa, lakini kuna watu wengine nafikiri wanafungiwa fungiwa, TFF wanashindwa kuwavumilia, naomba awasaidie.

la mwisho, kuna suala la uchaguzi wa Chama cha Mpira wa Wanawake amezungumzia Mheshimiwa Chumi, naomba TFF walifanyie kazi. Wizara naikabidhi tutaonana Bunge la Septemba, tutazungumnza vizuri. (Makofi)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwa sababu ya muda, nilikuwa na mambo mengi, lakini na-summaries. Nina suala la uduni wa mawasiliano Malinyi, kuna suala la cybercrime kwa maana ya uhalifu wa mitandao, lakini kuna suala la uhifadhi kwa maana ya suala la mawasiliano katika maeneo ya utalii na uhifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu Malinyi, nazungumza hili kwa kurudia kwani mwaka 2021 nililisema, tuna shida kubwa. Mpaka hivi ninavyozungumza mawasiliano hakuna kwenye Ofisi ya Halmashauri. Utendaji kazi kwa watumishi ni changamoto na wananchi wa eneo lile pia wanapata ugumu sana katika kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Kata kama ya Sofi, Kata ya Kilosa kwa Mpepo ambayo iko mpakani inashikana na Namtumbo - Ruvuma, hakuna mawasiliano. Kwa kifupi hakuna hata kata moja ya Jimbo la Malinyi ambapo kuna uhakika unaweza kuwasiliana kwa asilimia 100 au hata 90. Kwa hiyo, naomba Wizara ilichukue hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2021 tulipata mnara kutoka UCSAF, namshukuru Mkurugenzi Mashiba, na tuliambiwa tu mchakato unaanza kwa ajili ya ujenzi, walipewa kazi TTCL, lakini mpaka leo bado. Namshukuru Mheshimiwa Waziri Nape ameniahidi, sasa ameingia analivalia njuga, kwa hiyo, ninaamini atafanya kitu kwa ajili ya watu wa Malinyi. Kwa hiyo, tunawaamini, naomba mtusaidie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, suala la TCRA. Nadhani uwezo wetu wa mitambo ya kisasa kuweza kudhibiti suala la uhalifu mitandaoni bado ni mdogo. Kwa hiyo, kama shida ni bajeti, basi naomba Mheshimiwa Waziri bajeti ijayo ulete tuwe na mitambo ya kisasa kama ya wenzetu huko nje, tuweze kutatua tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mimi mpaka sasa hivi nilipoteza simu, tablets na vitu vingine, lakini wanaendelea kufuatilia, wanasema tunashughulikia. Mpaka simu iwe hewani ndiyo wanaweza wakaipata, lakini nilidhani ingefaa kabisa tuweze kupata hizi gadgets hata kama simu imezimwa, basi ionekane iko sehemu fulani, ila inaonekena kama bado tunabahatisha. Kwa hiyo, naomba tu tujitahidi mwakani kwenye bajeti mlete tuwe na uwezo mkubwa kama wenzetu wa nchi nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine hata kwenye mitandao ya face book. Watu wame-forge account fake, wametengeneza kama ya kwangu tangu 2018, nimelalamika, nimepewa RB iko Iringa, nimeandika barua Serikalini, mpaka leo watu wanaendelea kutapeli watu kwenye mitandao, accounts za face book zinafanya kazi ambazo ni fake. Namba za simu ambazo matapeli wanapokea fedha bado zipo hewani. Sasa unashangaa, inatakiwa tufanye nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama shida ni teknolojia, basi mwakani kwenye bajeti muilete, lakini kwa sasa Mheshimiwa Waziri mtusaidie hili jambo liweze kukoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, ni suala la mawasiliano kwenye maeneo ya utalii na uhifadhi. Maeneo mengi ya misitu (TFS), maeneo yetu ya game reserves, maeneo ya National Parks, kule kwenye vivutio mawasiliano hakuna. Wageni wanatalii; kwa mfano, Mlima Kilimanjaro pale ni maeneo mazuri ya watu kuona. Mtu anapiga picha na video anataka ku-share wakati huo huo dunia ione, iweze kutamani na yenyewe kupanga safari za kuja, lakini hawawezi, mawasiliano hakuna kabisa. Kwa hiyo, mtu akienda kutalii anakuwa kama ameenda sijui maeneo gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kifupi kuna haja kubwa sana ya mawasiliano yapatikane kwenye vivutio vyote. Kwa hiyo, Mheshimiwa Nape ushirikiane na watu wa Maliasili, kwenye vivutio vyetu vyote mawasiliano ya simu yapatikane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kabisa ni suala la vita dhidi ya ujangili pamoja na mawasiliano. Leo tunafanya doria kama za kienyeji niseme kwa Jeshi la Uhifadhi lote, tunabahatisha kutegemea tu nguvu za miguu na wapiganaji wa kawaida, lakini teknolojia ingeweza kurahisisha ujangili kwa maana ya kupiga vita ujangili. Kupitia mawasiliano ya simu ambayo unayafanya ingekuwa rahisi sana kuwa-track majangili, lakini leo kwenye vivutio vya utalii hakuna mawasiliano. Kwa hiyo, zoezi la doria linakuwa gumu, tunafanya kienyeji. Teknolojia ingeweza kutatua tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naomba niishie hapa kwa leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)