Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Simon Songe Lusengekile (1 total)

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Mheshimiwa Waziri Mkuu tuna sera ya Cooperate Social Responsibility (CSR) kwa jamii yetu inayotoka kwenye makampuni, mashirika, wawekezaji na wakandarasi mbalimbali; lakini fedha hizi zimekuwa zikifika zinacheleweshwa sana kutumika. Leo tunaomba kauli ya Serikali juu ya ucheleweshwaji wa matumizi ya fedha hizi za CSR?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, kwanza kabla sijaanza kujibu swali la Mheshimiwa Songe Mbunge wa Busega, Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wenzangu na Watanzania wenzangu mnajua leo tarehe 01 timu yetu ya Dar Young Africans ambayo inapeperusha bendera ya Taifa itaondoka muda mfupi ujao uwanja wetu wa Dar es Salaam kuelekea nchini Jijini Algiers kwa ajili ya mchezo wa pili wa fainali. Naamini sote na tuendelee kila mmoja kwa dhehebu lake tuiombee timu yetu ya Dar Young African iweze kushinda mchezo huu wa pili kwa magoli mengi ya kutosha ili Watanzania tuweze kuwa mabingwa. Timu yetu ina uwezo mkubwa, muhimu zaidi tuwaombee wachezaji wetu, na mchezo wa tarehe 03 naamini watanzania tutakuwa kwenye sceen kuiombea na tunaamini tutashinda na watarudi na kombe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hili niungane na Watanzania kwa kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye ametoa usafiri wa ndege unaobeba wachezaji, viongozi na wapenzi kadhaa pamoja na viongozi wa Serikali kuisindikiza timu yetu ya Dar Young African kwenye mashindano hayo muhimu kwa Taifa letu. Tunatamani sana ushindi huu upatikane mkubwa ili tujenge historia ya kupata kombe hili kwa mara ya kwanza nchini Tanzania. Mwenyezi Mungu awajalie safari njema pia mchezo mwema, mafanikio makubwa kwenye michezo hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nijibu swali la Mheshimiwa Songe Mbunge wa Busega kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali tunayo sera ya CSR fedha ambayo inapatikana kutoka kwenye mashirika, makampuni na kwa wawekezaji waliowekeza na kufanya shughuli kwenye maeneo yetu kwa kutoa sehemu ya fedha. Iko sheria imetaja na asilimia, sina kumbukumbu ya haraka, lakini fedha ile inatolewa kwenda kwenye jamii iliyoko jirani na mradi huo au uwekezaji huo ulipo kwa ajili ya kufanya shughuli za maendeleo. Fedha hii inapotolewa inapoenda kwenye kijiji au halmashauri inapaswa kuingia kwenye mfuko wa mapato ya ndani ya kijiji au halmashauri ili iweze kuratibiwa na kupangiwa miradi ya kufanya kulingana na mahitaji ya jamii yenyewe; na fedha hii inapoingia kwenye mfuko kama mapato manake lazima inaingia kwenye bajeti, inapangiwa matumizi.

Mheshimiwa Sika, na kwa hiyo fedha ikiingia lazima itumike katika kipindi cha mwaka. Hata kama itakuwa imechelewa kuingia lakini wakati wanapofanya mabadiliko madogo ya bajeti ndogo na yenyewe lazima ziingizwe. Kwa hiyo fedha hii inapoingia inakuwa inaingia kama sehemu ya bajeti na ikiwa sehemu ya bajeti ni lazima itumike. Kwa hiyo Serikali inasimamia hili kupitia halmashauri zetu kwa sababu miradi inakuwa kwenye wilaya, vijiji; na pindi fedha hii inapoingia mamlaka husika zinazopanga matumizi lazima zipangie matumizi.

Mheshimiwa Spika, tunajua baadhi ya halmashauri zinazopata bahati kuwa mashirika haya, makampuni haya ya uwekezaji wanapopata fedha hii wanaiona kama ni fedha nje ya bajeti na kwa hiyo upangaji wa matumizi yake unachukua muda mrefu na mwisho wanaingia kwenye migogoro. Sasa nitoe maelekezo, Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI yuko hapa, na wanufaika wakubwa wanakuwa ni halmashauri ya wilaya au vijiji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, pindi tunapopata makampuni au wawekezaji na wanatoa gawio hili la maendeleo ya jamii na linaingia kwenye halmashauri basi fedha hii isimamiwe na maelekezo yatoke, wale maafisa masuhuli kwa maana ya mkurugenzi lazima azitambulishe kwenye Baraza la Madiwani. Baraza la Madiwani lipange utaratibu na utaratibu ule uende kwenye miradi moja kwa moja ili wananchi waweze kunufaika kwa mradi waliotamani wao kuujenga, na itaingia pia kwenye kaguzi mbalimbali. Kwa hiyo mkaguzi wa ndani wa halmashauri anawajibika moja kwa moja kufuatilia matumizi ya fedha hizo. Tukifanya hili litaanza kuleta manufaa.

Mheshimiwa Spika, na sisi Serikali tunajua fedha ikiingia huko inatumika kama ilivyokusudiwa, ahsante sana. (Makofi)