Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers from Prime Minister to Hon Omary Juma Kipanga (2 total)

MHE. PRISCUS J. TARIMO Aliuliza:-

Kumekuwa na wimbi la kukosa mikopo ya elimu ya juu kwa wanafunzi wenye ufaulu mzuri waliomaliza kidato cha sita kwenye shule binafsi kwa madai kuwa wanafunzi wanaosoma shule binafsi wazazi au walezi wao wana uwezo wa kuwalipia ada ya chuo.

Je, Serikali katika kuleta usawa kwenye fursa hii ya mikopo ya elimu ya juu haioni haja ya kutoa mikopo hiyo kwa kuzingatia ufaulu wa wanafunzi wote?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa vile na mimi ni mara yangu ya kwanza kusimama mbele kwenye Bunge lako tukufu, nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuniona na kuniamini kwamba na mimi naweza nikawa miongoni wa watu wa kuweza kumsaidia.

Mheshimiwa Spika,baada ya hayo sasa, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge Moshi Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mikopo inayotolewa na Serikali kupitia Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu inawalenga vijana wenye sifa za kitaaluma za kujiunga na taasisi za elimu ya juu lakini hawana uwezo wa kumudu gharama za elimu. Upangaji na utoaji mikopo unaongozwa na Sheria ya Bodi ya Mikopo (Sura 178) ambayo inabainisha sifa za msingi za mnufaika ambazo zinajumuisha.Awe Mtanzania; awe amedahiliwa kwenye chuo kinachotambulika; awe ameomba mkopo, asiwe na vyanzo vingine vinavyogharamia masomo yake. Aidha, kusoma shule binafsi za sekondari siyo kigezo cha mwanafunzi mwombaji kunyimwa mkopo wa kugharamia elimu ya juu. Wapo wanafunzi waliosoma shule binafsi na wanapata mkopo baada ya kuthibitisha uhitaji wao kwa mujibu wa vigezo vya utoaji mikopo.

Mheshimiwa Spika, vilevile kwa mujibu wa sheria tajwa, Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu, ina mamlaka ya kuweka utaratibu wa kubaini wahitaji. Kwa sababu hiyo, Bodi huandaa mwongozo unaopaswa kuzingatiwa na waombaji na kuweka masharti ya utoaji mikopo kwa mwaka husika. Sifa za ziada zinazoainishwa kwa waombaji ni pamoja na; uyatima, ulemavu au wazazi wenye ulemavu na wale ambao masomo yao ya sekondari au stashahada yalifadhiliwa ambapo katika kundi hili wapo waombaji wengi waliosoma katika shule za sekondari za kulipia.

Mheshimiwa Spika, nashauri Waheshimiwa watusaidie kutoa elimu ili kuwezesha jamii kubadili mtazamo huu. Aidha, wawashauri waombaji wajaze kikamilifu fomu za maombi na kuzingatia maelekezo yanayotolewa na Bodi wakati wa uombaji wa mikopo ikiwa ni pamoja na kuambatanisha nyaraka zote muhimu ili kuepuka uwezekano wa mwanafunzi mwenye sifa stahiki kukosa mkopo kutokana na kutojaza kwa usahihi fomu ya maombi ya mkopo.
MHE. EDWARD K. OLELEKAITA Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Chuo cha VETA katika Jimbo la Kiteto?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Edward Kisau Olelekaita, Mbunge wa Kiteto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na mpango wa kujenga vyuo vya ufundi stadi ikiwa na lengo la kuwa na Chuo cha Ufundi Stadi katika kila mkoa na kila wilaya. Kwa mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, ilitenga jumla ya shilingi bilioni 48.6 kwa ajili ya kujenga vyuo 29 vya VETA katika ngazi za wilaya ambavyo kwa sasa viko katika hatua mbalimbali za ujenzi.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutafuta vyanzo mbalimbali vya fedha ili kuendelea kutekeleza azma yake ya kuwa na chuo cha ufundi stadi katika kila mkoa na wilaya nchini ikiwemo Wilaya ya Kiteto. Aidha, endapo Halmashauri ya Kiteto inayo majengo ambayo yanakidhi vigezo vya kutumika kwa VETA, Wizara yangu itakuwa tayari kununua vifaa kwa ajili ya kuwezesha majengo hayo kuanza kutumika mara moja. Ahsante.