Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Jafari Chege Wambura (1 total)

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nimuulize Mheshimiwa Waziri Mkuu na mimi swali. Mheshimiwa Waziri Mkuu kumekuwa na mwingiliano wakati wa utekelezaji wa majukumu kati ya Wizara tatu, kwa maana Wizara ya TAMISEMI, Wizara ya Maliasili pamoja na Wizara ya Ardhi hasa kwenye eneo la utoaji wa GN. Kwa mfano, Wizara ya TAMISEMI wanatoa GN wakati wa uanzishaji wa vijiji, Wizara ya Maliasili wanatoa GN kwenye maeneo yao ya hifadhi lakini Wizara mama ambayo ni Wizara ya Ardhi pia inawajibika kwa mujibu wa sheria kutoa GN kwenye maeneo yote haya ya mipaka.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuwa utoaji wa GN wakati mwingine hupelekea mogogoro ya ardhi kwenye maeneo haya. Nilitaka nijue tu Serikali ina mpango gani madhubuti wa kuboresha Sera ya Taifa ya Ardhi ya ya mwaka 1995, ambayo pia itapelekea maboresho ya Sheria ya Ardhi ya Mwaka 1999 ili kuondokana na kutengeneza formality ya utoaji wa GN kwa sekta moja ya Ardhi badala ya mgongano ulioko kwa sasa, nashukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu.

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, maneno yake ya awali sikuyasikia vizuri naomba arudie tena ili niweze kumjibu kwa usahihi zaidi.

SPIKA: Mheshimiwa Jafari Chege.

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu kumekua na mwingiliano wa kiutendaji wakati wa utoaji wa GN kati ya Wizara tatu kwa maana Wizara ya TAMISEMI, Wizara ya Maliasili na Wizara ya Ardhi. Nikatoa mfano Wizara ya TAMISEMI wanatoa GN wakati wa uanzishaji wa vijiji kwa maeneo fulani ambayo yanaweza yakawa ndani ya hifadhi, Wizara ya Maliasili nao wanatoa GN kwenye maeneo yao ya hifadhi wakati huo huo Wizara ambayo ni Wizara mama ambayo ni Wizara ya Ardhi nayo inawajibika kutoa GN kwenye maeneo hayo hayo. Kwa hiyo kunakuwa na mgongano wa Wizara tatu zote kutoa GN kwenye eneo moja la umiliki wa ardhi.

Mheshimiwa Spika, wakati mwingine utoaji huu wa GN husababisha uzalisha mgogoro wa ardhi, hasa kijiji kinapopandikizwa ndani ya eneo moja la hifadhi na wote wakinwa na GN zinazotoka Serikalini. Nilikuwa nataka nijue sasa Serikali ina mpango gani wa maboresho wa Sera ya Taifa ya Ardhi ambayo ni ya Mwaka 1995 ambayo itapelekea maboresho pia ya Sheria ya Ardhi ya Mwaka 1999 ili kutengeneza formality ya utoaji wa GN kwa Wizara moja ili kuondoa muingiliano wa Wizara zote tatu kutoa GN kwenye eneo moja la umiliki wa ardhi?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Chege, Mbunge wa Rorya kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hizi Wizara zote zilizotajwa na Mheshimiwa Chege, Wizara ya Ardhi, TAMISEMI pamoja na Maliasili. Tunajua zinazo sheria zinazosimamia ardhi; lakini hakuna muingiliano wa moja kwa moja kwa sababu tumejitahidi kila Wizara kuwa na majukumu yake hasa katika utoaji wa GN. GN inatolewa na Wizara moja tu. Ardhi wanalo jukumu la kusimamia sera ya ardhi nchini na inayo kujumu la kupeleka watendaji wa sekta ya ardhi wenye taaluma ya ardhi kwenye mamlaka hizi hasa mamlaka ya serikali za mitaa.

Mheshimiwa Spika, mamlaka ya serikali za mitaa kwa maana ya halmashauri za wilaya wajibu wake ni kusimamia matumizi, upimaji wa ardhi kwenye maeneo yao ya halmashauri, na wao ndio wanaanzisha mchakato wa upatikanaji wa hati kwa wale wanaotakiwa kumiliki. Lakini pia halmashauri hizi ndizo ambazo zinasimamia mipaka ya kiutawala. Kijiji na kijiji mipaka yake, kata na kata mipaka yake, wilaya na wilaya mipaka yake hata mkoa na mkoa. Kwa hiyo jukumu lao liko tofauti kidogo ingawa kuna mahusiano ya kiutendaji kwa kupeana taarifa baad aya mmoja kukamilisha jukumu lake.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Maliasili na Utalii wale wanahusika na maeneo ya uhifadhi maliasili zetu na uratibu wa maliasili zote nchini. Wanapokuwa na mipaka wanalazimika kwenda sasa mamlaka ya Serikali za mtaa wanalazimika pia kutoa taarifa ardhi; na mipaka hiyo inapothibitishwa na ardhi wao sasa ndio wanatoa hiyo GN. Tumefanya kazi kubwa kwenye migogoro mbalimbali ya mipaka kati ya maeneo mawili ya utawala, kati ya maeneo mawili ya utendaji kama wakulima na wahifadhi lakini ni vijiji na hifadhi. Na tunapokuwa na mgogoro hii ndiyo kwa sababu tunaita Wizara zote tatu; Wizara ya Ardhi, Maliasili, TAMISEMI kwa sababu kila mmoja ana jukumu lake, na huo ndio utaratibu ambao sasa hivi unaendelea Serikalini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo utoaji GN kama vile kule Mbarali ambako baada ya muda mfupi tutatoa GN ile mpya baada ya GN 28 ambayo tumeifanyia kazi sana, hiyo ndio Wizara itahusika siyo kila Wizara tu inatoa GN, Maliasili inatoa GN, Hapana, ni Wizara moja imeshapewa jukumu la kutoa GN Wizara nyingine ina facilitate, nyingine inasimamia. Kwa hiyo Wizara zetu tatu hizi wakati wote wamekuwa wakiangalia maeneo yenye mwingiliano na wanafanya marekebisho halafu tunawawekea sheria, ili kubainisha ile mipaka ya utendaji.

Mheshimiwa Spika, tutaendela kusimamia maeneo yote yenye changamoto, yenye mwingiliano ili kubainisha majukumu ya kila Wizara ili kusiwe na muingiliano ambao unaweza kuleta migogoro ndani ya Serikali. Kwa hiyo huo ndio mkakati ambao tunao ndani ya Serikali, ahsante sana.