Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Eng. Mwanaisha Ng'anzi Ulenge (1 total)

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu na nitauliza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara 52A, Waziri Mkuu ametajwa kuwa ndio mdhibiti, msimamiaji wa shughuli za Serikali za kila siku. Idara za Serikali Kuu na Serikali za Mitaa zimekuwa zikitekeleza mpango, wakati huo huo zinajifanyia tathmini zenyewe. Mfano, hai ni Wizara ya Fedha na Mipango imekuwa na kitengo cha tathmini ndani ya Idara ya Mipango.

Mheshimiwa Spika, sasa ili tuweze kuisimamia na kuidhibiti Serikali ipasavyo: Je, hatuoni haja ya kuwa na taasisi inayojitegemea ya kuisimamia Serikali na kufanya tathmini, kutunga mifumo ya ufuatiliaji na tathmini nchini?

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Mbunge wa Mkoa wa Tanga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo umepata shida kulielewa vizuri lakini niseme suala la tathmini na kuona mwelekeo wa kazi hiyo baada ya tathmini, mbali ya kwamba tumeipa Wizara ya Fedha na tukaiita Wizara ya Fedha na Mipango, lakini bado kila Wizara na kila sekta yenyewe tunaitengea bajeti hapa Bungeni kwa ajili ya kujiwekea mpango wake na kwenda kufanya tathmini yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanapokuja awamu ya pili, wanaweza kuweka mipango yao kutokana na tathmini waliyoifanya msimu uliopita. Kwa hiyo, hatujaishia Wizara ya Fedha na Mipango pekee, kila Wizara na kila sekta tumeipa mamlaka hiyo na utakuta pia hata kwenye maombi ya fedha ya bajeti ya miradi kuna element ya usimamizi.

Mheshimiwa Spika, tunaposema usimamizi, maana yake wanakwenda kuikagua mipango waliyoiweka katika kipindi cha mwaka na kuitekeleza ili kupata mwelekeo wa kama: Je, wamefanikiwa au hawajafanikiwa? Kama hawajafanikiwa inawawezesha kuweka mpango ule kuwa endelevu kwa msimu ujao. Kwa hiyo, hiyo tumeishusha mpaka Wizarani na kwenye sekta zetu, hatujaishia kwenye Wizara ya Fedha pekee.

Mheshimiwa Spika, nalichukua hilo, tutafanya mapitio huku kuona swali lako limetokana na nini? Je, kazi hiyo inafanywa na Wizara ya Fedha pekee? Hapo baadaye naweza kukupa majibu kwa namna nyingine ili uweze kupata uelewa mpana juu ya wajibu huo na kama huko kuna udhaifu, basi tutaangalia na kuweza kuboresha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla wake, suala la mipango na tathmini lipo katika kila sekta.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)