Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Maryam Azan Mwinyi (1 total)

MHE. MARYAM AZAN MWINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, kwa vile nchi yetu ni ya pili katika Afrika kwa uzalishaji wa mifugo na kwa vile ina wafanyabiashara wengi wa mifugo wanaokwenda katika nchi mbalimbali kama vile Kenya, Madagascar na Comoro. Je, Serikali ina mkakati kuimarisha usafirishaji wa mifugo hiyo na bidhaa zake ili kudumisha biashara hiyo?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwinyi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge amezungumzia sekta ya mifugo na pia ametaka kujua Serikali ina mkakati gani wa kuimarisha usafirishaji, na vile vile amezungumzia masoko. Ni kweli kwamba nchi yetu ina mifugo mingi sana; ina ng’ombe wengi wa kutosha, mbuzi, kondoo na wameingia kwenye soko la kuuza ndani na nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kufanya maboresho makubwa kwenye biashara hii ambapo baadhi ya Watanzania wamejihusisha nayo kwa kusafirisha mifugo hii. Inaweza ikawa wanasafirisha mifugo hai au baada ya kuwa wamepitisha viwandani. Sasa mkakati wa kuboresha usafirishaji, wote tunajua, kuna kazi kubwa tunaifanya ya kuboresha usafirishaji kwa njia ya ndege na sasa tunajenga pia reli ambayo inakwenda mpaka nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, tunachokifanya sasa ni kuhakikisha kwamba tunatafuta masoko nje ili kuwezesha kufanya biashara hii na kila mmoja atatumia usafiri ambao anauona ni rahisi kufika kwenye nchi anakohitaji kupeleka mifugo hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali inachokifanya sasa, kwanza ni kuhakikisha ufugaji wa ndani unakuwa bora, unaweza kutoa mifugo yenye afya, uwezo na yenye thamani kubwa. Vile vile kazi kubwa tunayoifanya ni kuimarsiha mifugo hii iwe thamani kubwa kuhamasisha wafugaji kufuga kisasa zaidi ili mifugo hii iweze kuwa na thamani. Kwa hiyo, kazi zote ambazo tunazifanya kwa pamoja za kuimarisha ufugaji, ufugaji wa kisasa, kuhakikisha pia tunapeleka viwandani kwa wale wanaotaka kupata nyama au kusafirisha mifugo iliyo hai kupitia njia zetu za usafiri, sisi tumetoa kibali kwa Mtanzania yeyote anayetaka kuingia kwenye uwekezaji huo, afanye hilo ili iweze kumletea tija kwenye shughuli yake ya kila siku ya kibiashara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee kutoa wito kwa wafugaji. Jana jioni nilikuwa na wafugaji kama 60 hivi tukizungumza namna bora ya uboreshaji wa mifugo hii. Kwa hiyo, naamini ufugaji kupitia Wizara ambayo imemaliza bajeti yake hapa jana, wataendelea kusikiliza maboresho yaliyotamkwa hapa ili wafugaji sasa waweze kuzalisha mifugo yenye thamani kubwa na usafirishaji upo kama ambavyo Serikali tunafanya ili waweze kutumia huduma hiyo waweze kupata tija zaidi. Huo ndiyo mkakati wa Serikali wa kuimarisha usafirishaji, pia kwenye masoko na ufugaji wa ndani wenye viwango, wenye kuleta faida kwa wafugaji, ahsante sana. (Makofi)