Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Benaya Liuka Kapinga (1 total)

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi.

Mheshimiwa Waziri Mkuu mwaka jana nchi yetu ilikumbwa na tatizo kubwa la soko la mahindi, hali iliyopelekea kwa Mikoa ya Kusini ikiwemo Ruvuma, Rukwa, Mbeya na Iringa kuuza zao hilo kwa shilingi 15,000 kwa gunia; na hii ilitokana na baadhi ya wakulima na wafanyabiashara kudhani kwamba zao hili kuna zuio la kuuza nje ya nchi.

Swali langu, nini kauli ya Serikali kuhusu zao hili kwa msimu huu? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kapinga, Mbunge wa Mbinga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba nchi yetu kupitia Mikoa ya Kusini na Nyanda za Juu Kusini wanazalisha sana mahindi na mimi nitumie nafasi hii kuwapongeza na kuwashukuru wakulima wa maeneo haya. Kwa sababu leo hii nchi yetu tunaposema tuna uhakika wa usalama wa chakula kwa maana ya kuwa na kiwango kikubwa cha chakula kinatokana na jitihada zinazofanywa na wakulima nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zao la mahindi ni kweli mwaka jana tulipata tatizo kidogo kwa sababu bei ilishuka na kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema wakulima wengi walidhani kwamba tumeweka zuio la kupeleka mahindi nje katika kutafuta soko. Tumekuwa na mikutano mingi na Waheshimiwa Wabunge wa mikoa hiyo kuwahakikishia kwamba Serikali haina zuio hilo. Pia tuliwahi kutoa tangazo hapa mbele ya Bunge lako tukufu ili kuwahakikishia wakulima.

Mheshimiwa Spika, nini tunachokifanya kwenye eneo hili, kwanza lazima tujiridhishe na usalama wa chakula au kiwango cha chakula ndani ya nchi kwamba tuna chakula cha kutosha pia tunakuwa na ziada. Ile ziada ndio ambayo tunaruhusu kuuzwa nje ili ndani ya nchi tusiwe na shida ya chakula. Kwa hiyo, pia hata msimu huu uzalishaji wa chakula msimu huu pindi Wizara ya Kilimo ambayo imekamilisha bajeti yake jana ikishafanya tathmini zake na kujua kiwango cha chakula tulichonacho na kuitambua ile ziada; ile ziada tunatoa kibali cha kuuza nje ili wakulima waweze kupata masoko ya uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa utaratibu tunaoutumia hapa hatupeleki tu nje holela, bali yule mkulima ambaye anataka kupeleka nje kwa mfano Mikoa ya Rukwa, kupeleka Zambia, Congo na maeneo mengine omba kibali tu kwa Mkuu wa Wilaya ili Mkuu wa Wilaya ajue leo tunatoa tani ngapi nje na sisi itatusaidia pia kujua tumeingiza shilingi ngapi fedha za kigeni kupitia zao la mahindi. Kwa hiyo, utaratibu ni huo mkulima yeyote anayetaka kuuza nje atakwenda kwa Mkuu wa Wilaya kuomba kibali cha kupeleka nje na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ina Afisa wetu wa Kilimo ambaye pia anaangalia kiwango cha chakula na uzalishaji wake ziada. Kwa hiyo, na yeye pia anajua leo imeombwa kibali cha tani 10, kesho tani 20 akijumlisha anajua kwamba tunafikia kile kiwango cha ziada ambacho tunacho.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kufatilia eneo hili Serikali inaendelea kufatilia mwendeno wa masoko ya nje ili kuwaruhusu wakulima waliozalisha hapa ndani waweze kupata masoko pia nje huo ndio utaratibu ambao tunautumia wa Serikali. (Makofi)