Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Livingstone Joseph Lusinde (1 total)

MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na mimi kunipa nafasi hii ya kuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa Majaliwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya kazi kubwa sana ya ujenzi wa vituo vya afya nchini. Sambamba na kazi hiyo vilevile Serikali imepeleka vifaa tiba takriban kwenye vituo vyote vya afya nchini Tanzania. Swali langu, kumekuwa na upungufu mkubwa sana wa wataalam katika hivyo vituo wa kutumia hizo mashine na vifaa tiba vilivyopelekwa na Serikali.

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka wataalam kwenye vifaa vyote ili kuweza kunusuru maisha ya Watanzania?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Livingstone Lusinde Mbunge wa Mvumi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naungana naye, kwamba Serikali yetu kutoka awamu ya tano na sasa awamu ya sita imefanya kazi nzuri sana kwa ujenzi wa maeneo ya kutolea huduma nchini; zahanati, vituo vya afya, hospitali za halmashauri za wilaya pia mikoa na kanda, na sasa tunaimarisha pia na huduma kwenye hospitali za kitaifa. Kazi kubwa imefanywa nataka nitumie nafasi hii kumpongeza sana Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maelekezo yake na kwa usimamizi wake, na sisi tunaendelea kuimarisha maeneo hayo ya utoaji huduma. Awamu ya kwanza ilikuwa ni kujenga miundombinu ya majengo. Kazi hiyo imefanywa vizuri, na tunataka tuwahakikishie Watanzania, kwamba tutaendelea kujenga vituo vya afya na zahanati kulingana na mahitaji kwenye halmashauri zetu na vijiji.

Mheshimiwa Spika, awamu ya pili ni ya kupeleka vifaa tiba na dawa, kazi ambayo sasa inaendelea kwa kasi. Baada ya majengo sasa tunaweka vifaa vya maabara, pia dawa na vifaa vingine kama vile vitanda kwenye wodi. Kazi hii pia inaendelea vizuri.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kujua mpango wa Serikali wa kupeleka sasa watumishi. Kwa eneo hili la watumishi kazi sasa inaendelea vizuri. Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshatoa vibali kwa Wizara ya Afya pamoja na mamlaka Serikali za Mitaa kuwaajili ya watumishi wa sekta ya afya ili kuwapeleka kwenye maeneo haya yote, zahanati, vituo vya afya na hospitali zote ili waweze kutoa huduma. Tunajua tuna maeneo mengi ya kutolea huduma, mahitaji ni makubwa kulingana na Ikama; kwa hiyo Serikali itaendelea kuajiri kulingana na uwezo wa kifedha kwa lengo la kutoa huduma kwa Watanzania kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, wakati huo tukiwa tunapewa kibali pia huku ndani tunafanya mapitiom, kwa sababu tunajua kuna maeneo mengine kuna watumishi wengi zaidi kuliko maeneo mengine, kwa hiyo tunahamisha walikojaa na kuwapeleka maeneo na hasa kutoka maeneo ya mijini ambako kuna mrundikano wa watumishi na kwenda kwenye maeneo ya vijiji ili maeneo yote yaweze kupata huduma. Pia wale waliopo tunawaongezea uwezo kwa kuwapeleka kwenye mafunzo, semina na warsha ambazo pia zitawasaidia kuwafanya waweze kutoa huduma hii kwa urahisi zaidi. Kwa hiyo nitoe pia maelekezo kwa wakurugenzi kufanya mapitio ya kina ya idadi ya watumishi tulionao na maeneo yenye mrundikano mkubwa kuwahamisha kuwapeleka kwenye maeneo ambayo yana watumishi wachache. Malengo yetu ya Serikali huduma hizi zitolewe kwa usawa kwenye maeneo yote.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimwakikishie Mheshimiwa Lusinde kwamba Serikali inaendelea na ajira, na ajira hizi malengo yetu ni kutosheleza watumishi kulingana na ikama inayotakiwa, na Watanzania sasa waweze kupata huduma za afya kama ambavyo Serikali inataka ione Watanzania wakinufaika, ahsante sana. (Makofi)