Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Bhagwanji Maganlal Meisuria (6 total)

MHE. BHAGWANJI MAGANLAL MEISURIA: Mheshimiwa Spika, nashukuru Mheshimiwa Naibu Waziri amenijibu vizuri lakini nina maswali ya nyongeza. Ni kweli kabisa aliyosema, nakubali wazazi wote wapate haki kamili ya kumlea mtoto.
Ikiwa mtoto yupo kwa mama aruhusiwe kwenda na kwa baba. Hata hivyo, katika Tanzania yetu wananchi wengi hawampi baba haki ya kumlea mtoto au hata kumwona, je, Serikali inasemaje kuhusiana na suala hili? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Huyu mtoto
kuanzia miaka mitatu hadi saba yupo kwa mama, ikiwa mtoto huyo amefikisha miaka saba, je, baba anayo haki ya moja kwa moja kumlea, kumsomesha na kumuangalia kiafya? Kwa sababu watoto wengi wa Tanzania hawapati
nafasi ya kulelewa na baba. Kwa hiyo, baba apate nafasi ya kulea, baada ya miaka saba apewe mtoto.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Yaani kumtia mwanamke mimba haitoshi kukufanya uitwe baba. Ili kuwa baba kamili, pindi unapompa mimba mwanamke unapaswa kwanza kuitunza
mimba yenyewe, lakini baada ya hapo kumtunza mtoto baada ya kuzaliwa, muwe mnaishi pamoja ama hamuishi pamoja na huyo mwanamke. Hilo ni jukumu la kwanza unapokuwa mwanaume na imetokea umempa mimba mwanamke. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama kuna mgogoro wowote ule unaoweza kutokea katika mchakato huu kuna taratibu za kufuatwa. Moja ya taratibu ni za kimila ambapo yanaweza yakatokea mashauriano ya kimila kwenye jamii kati ya upande wa baba na upande wa mama na
wakaelewana kimila na kuna gharama za kutoa. Kwa mfano, kwa Wasukuma kuna ngwegwe na nafahamu kwenye makabila mengine pia kuna taratibu za kufuata. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kama ikishindikana kimila ndiyo unafuata huo mchakato wa kisheria niliousema ambapo utapaswa kwanza kumpa haki mama kumlea mtoto mpaka miaka saba ifike na katika kipindi hiki cha miaka saba unapaswa kuwa umemtunza yule mama. Pale mwanzoni
kama hukumuoa huyo mwanamke unapaswa
ukajitambulishe rasmi kwamba wewe unahusika na ile mimba, siyo umeikataa mimba halafu mtoto akizaliwa anafanana na wewe unasema mtoto ni wa kwako, hapana! (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwanza kwa mujibu wa sheria unapaswa ama ufuate taratibu za kimila ujitambulishe kwamba wewe ndiye uliyetia mimba, uilee mimba na mwisho wa siku umlee mtoto au kwa taratibu za kisheria ujitambulishe mahakamani kwamba wewe ndiye umetia mimba na utailea. Sasa ikifika ile miaka saba una haki ya kudai mtoto. Nadhani Mheshimiwa Meisuria amenielewa.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, nataka kuongezea hiyo sehemu ya pili.
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto Na.21 ya mwaka 2009, presumption ni kwamba mtoto anatakiwa akae na mama in the best interest of the child lakini akifika miaka saba sheria inasema in the opinion of the court anaweza akakaa na mzazi yeyote pale mahakama
itakapojiridhisha kwamba mtoto huyu atapata matunzo na malezi mazuri.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe wasiwasi
Mheshimiwa Bhagwanji kwamba kama mtoto amefikisha miaka saba siyo lazima akae na mama, mahakama itapima na kuona in the best interest of the child mtoto huyu atapata malezi mazuri wapi, kwa baba au kwa mama.
MHE. MAGANLAL MEISURIA BHAGWANJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana umenipa nafasi, Mungu akuweke.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme jambo moja katika Jimbo langu la Chwaka, hakuna gari katika Jimbo la Chwaka pamoja na Jozani kwa sababu pana bahari na hoteli zipo nyingi sana. Kwa hiyo, wanaweza kuja majambazi, inaweza kuwa ni mambo ya siasa, hivyo ni muhimu sana gari ipatikane haraka kwa watu wangu wa Jimbo la Chwaka pamoja na Jozani, kwa hisani yako. (Makofi/Kicheko
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, tumelipokea ombi la Mheshimiwa Mbunge na tutalifanyia kazi. (Makofi)
MHE. BHAGWANJI MAGANLAL MEISURIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kinipa nasafi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nazipongeza Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Muungano kwa sababu katika Jimbo langu wamejenga kituo cha polisi Chwaka na Jozani. Lakini mimi naomba Serikali, wameniomba nizungumze Serikali ya Muungano pamoja na Zanzibar wapatiwe gari za doria, Chwaka na Jozani.
La kwanza kwa kuboresha wananchi wangu wapate hitaji lao, lakini lingine mimi mwenyewe binafsi nimetoa gari mbili hospitali za Chwaka na Kongoroni. Lakini hii gari ya polisi lazima tuhudumie tupate na mimi nimesaidia Jozani polisi walikuwa wanahitaji computer na nimewasaidia, lakini hii gari mnipatie zote mbili. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI):
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bhagwanji hakuuliza swali, ilikuwa ni ombi la gari la doria na mimi tu kwa niaba ya Serikali tumepokea ombi lake na tutalifanyia kazi pindi pale nafasi itakaporuhusu basi tutaona namna ya kuweza kufanya.
MHE. BHAGWANJI MAGANLAL MEISURIA: Mheshimiwa Spika, nampongeza Naibu Waziri amesema maneno mazuri naunga mkono. Hata hivyo, nataka nimwambie wananchi wa Jimbo langu la Chwaka wana matatizo vilevile. Wabakaji wengi na watu mbalimbali wanakuja kufanya uhaini katika Jimbo langu huko Chwaka na Jozani. Mimi mwenyewe nimeshachangia computer moja Jozani lakini nimeomba gari mbili angalau hata moja ipatikane kwa sababu hali ni ngumu na ni lazima tupate gari moja kwa heshima na taadhima.
Mheshimiwa Spika, ni hayo tu, naomba Serikali na Waziri wanipatie gari gari moja ya Polisi ili liweze kusaidia wananchi wa Jimbo langu. Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bhagwanji, Mbunge wa Chwaka, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimejibu swali la msingi kwamba mchakato utakapokamilika wa upatikanaji wa magari kwa kuzingatia vigezo ambavyo nilivyovieleza tutaangalia kuona kama Chwaka inakidhi vigezo hivyo na idadi ya magari yaliyopo ili tupeleke. Nimuombe Mheshimiwa Mbunge avute subira mpaka magari hayo yatakapokuwa yamepatikana.
MHE. BHAGWANJI MAGANLAL MEISURIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru Waziri amejibu vizuri. Katika Mkoa nimepata gari lakini mimi nagombania Jimboni kwangu Chwaka na Jozani nipate gari kwa sababu pana vibaka, ubakaji na wananchi wameongezeka. Kama sijapata hilo gari itakuwa matatizo katika Jimbo langu.

Swali la pili, kama sijapata hilo gari hii Baniani peke yake Bungeni sitaweza kurudi kwa mara ya pili. Kwa hiyo, naomba nipatiwe hiyo gari ili niweze kurudi na wananchi wangu wapate huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache Mheshimiwa Waziri, naomba nipate gari katika Jimbo la Chwaka. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nimpongeze Mheshimiwa Bhagwanji kwa jinsi ambavyo amekuwa mstari wa mbele kabisa kupigania maslahi ya askari wetu kwenye Jimbo lake. Mimi ni shahidi mara kadhaa hapa nimekuwa nikijibu maswali yake na nikiona jitihada zake na hata wananchi wake, nina hakika wanaona jitihada hizo. Kwa hiyo, kwa jitihada hizo sioni kama wananchi wake watakuwa na mashaka naye na kuacha kumrudisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na ombi lake, kama ambavyo nimejibu swali la msingi kwamba kwa sasa hivi tumepata magari machache ambayo tumeyagawa katika level ya Mikoa na gari mbili za Mkoa Kusini Unguja zimeenda kwenye Ofisi za Wilaya zote mbili. Hata hivyo, kwa kuwa gari nyingine zinakuja na kuzingatia vipaumbele ambavyo nimevieleza basi tunalichukua ombi lake na kulifanyia kazi kwa uzito unaostahili.
MHE. BHAGWANJI MAGANLAL MEISURIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nataka nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri, hao watu wa bodaboda wana tabia moja mbaya sana, na mimi wameshafanyiwa wageni wangu, wanapora simu, halafu wanakimbia na hapa juzi katika eneo la Area D ninapokaa mimi, mama mmoja alikuwa na simu wamekuja watu wa bodaboda wamepora, sasa hatua gani Mheshimiwa Rais anawapenda wanyonge watu wa bodaboda lakini tabia hii ni mbaya sana kwa kupora.

Mheshimiwa Spika, kesho watakuwa na bastora watakwenda majumbani au madukani, kwa hiyo, mimi naomba Mheshimiwa Naibu Waziri atuambie ni sheria gani hawa watu wa bodaboda wanafanya tabia hiyo mbaya kwa kupora simu pamoja na begi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, si sahihi nadhani kuwajumuisha waendesha bodaboda na matukio ya wizi, waendesha bodaboda ni raia ambao wanafanya kazi zao, wanapaswa kufanya kazi zao kwa mujibu wa sheria ya kujipatia riziki ambazo zimeruhusiwa kisheria ni shughuli za kihalali.

Mheshimiwa Spika, sasa kama kuna watu ambao wanatumia pikipiki ama hiyo pikipiki ya kawaida ama iwe bodaboda kwa ajili ya uporaji hao ni wahalifu kama wahalifu wengine na kwa hiyo basi kama ambavyo ilivyo kawaida na desturi ya Jeshi letu la Polisi kuweza kukabiliana na wahalifu imekuwa ikifanya hivyo kushughulika na watu ambao wakitumia pikipiki ama bodaboda kwa ajili ya kupora wananchi na tutaendelea kufanya hivyo kuwashughulikia bila huruma wale wote ambao wanatumia pikipiki ama bodaboda kwa ajili ya kufanya uporaji.