Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Salome Wycliffe Makamba (1 total)

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa nafasi kuuliza maswali kwa Waziri Mkuu Mheshimiwa Waziri Mkuu naiona nia ya dhati ya Serikali kuboresha mazingira ya wachimbaji wadogo wadogo kwa hasa kwa kuwatafutia mitaji kwenye taasisi za kifedha hasa benki. Lakini benki hizi zinapokuwa zinawapa mikopo machimbaji wadogo wadogo zinawapa kwa masharti ambayo hayaendani na uhalisia wa biashara hii ya wachimbaji wadogo hasa ukizingatia musa wa uzalishaji na upatikanaji wa madini hayo.

Je, ni nini mkakati wa Serikali kutengeneza mazingira rafiki ya taasisi za kifedha ili waweze kuwapa mikopo wachimbaji wadogo ambayo itazingatia mazingira yao ya upatikanaji wa madini na mazingira yao ya uzalishaji wa madini?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salome Makamba, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kujua nafasi ya Serikali katika kusimamia fursa ya wachimbaji wadogo wa madini na upatikanaji wa mitaji bila ya kuathiri utendaji wao. Serikali yetu inayo sera inayoimarisha wajasiriamali, wachimbaji wadogo wa madini, kwa kutumia fursa walizonazo kwa maeneo yao panapopatikana madini kuchimba kwa uhuru na Mheshimiwa Waziri wa Madini mara kadhaa ameeleza mpango wa Serikali wa kupima viwanja kwa ajili yao na kuwasisitiza wajitokeze kushiriki kikamilifu kwenye fursa hii ya uwepo wa madini.

Mheshimiwa Spika, tunatambua changamoto ya wachimbaji hawa ya kukosa vifaa muhimu pamoja na mitaji ya kuanzishia kazi ya uchimbaji. Serikali tuchofanya ni kuelekeza kwenye taasisi za fedha, benki kwa maana ya sekta binafsi na wale wote ambao wanakopesha mikopo na wanaotambulika rasmi upande wa Serikali, tunazo halmashauri za mikopo midogo kwa wanawake na walemavu na tuna mifuko pia ya uwezeshaji ambayo yote hii, maeneo yote haya ni fursa kwa vijana wetu kukopa. Tunatambua ipo changamoto ya masharti mbalimbali ya hizi taasisi za kifedha.

Mheshimiwa Spika, ni nini tumefanya; ni kutoa maelekezo kwa taasisi hizi. Kwanza lazima wajue huyu anayekuja kukopa anataka kufanya shughuli gani, na shughuli hii kuanzia uwekezaji wake mpaka uzalishaji wake inatumia muda gani, na kwa hiyo masharti yale lazima yalenge utendaji wa sekta hiy,o kwa sababu kila eneo lina muda wake wa uwekezaji na uzalishaji wake na kuingia kwenye masoko. Itakuwa haipendezi kama anajua kwamba mchimbaji mdogo tangu anachimba mpaka kuuza anajua ni ndani ya miezi sita halafu unampa mkopo wa miezi mitatu, utakuwa humtendei haki. Kwa hiyo basi Serikali tunachofanya tumetoa maelekezo sahihi na thabiti kwa taasisi za fedha kuzingatia nature ya shughuli au mradi ambao mjasiriamali anaufanya ikiwemo na wachimbaji wadogo. Sisi tunajua uchimbaji mdogo unapaa paa bila ya kuwa na uhakika kwamba je, utapata madini yenyewe? Na ukipata madini yenyewe, na ukipata ile process mpaka kwenye masoko.

Mheshimiwa Spika, mara kadhaa tumeenda kuwasisitiza wajasiriamali lakini mara kadhaa tumehamasisha taasisi za fedha kufanya study ya uchimbaji mdogo na kuwafikia wachimbaji wadogo na kuwakopesha tena kwenye riba ndogo, ikiwezekana bila riba kabisa, ili kuwawezesha vijana wetu wajasiriamali kupata mikopo na kuitumia na hatimaye wapate faida. Mara kadhaa pia tumemuagiza Mheshimiwa Waziri wa Madini kusimamia sekta hii; na tumemuona akipita maeneo mbalimbali akizungumza na wajasiriamali wadogo pamoja pia na sekta za fedha ili kuhakikisha kwamba zinatenga fedha kwenye dirisha hili la wachimbaji wadogo ili waweze kupata mikopo yenye mazingira mazuri ya ukopaji na urejeshaji kwa lengo la kuwaondolea adha ya au kufungwa au kunyang’anywa mali zao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Serikali inaendelea kukaa na taasisi za fedha na kuzihamasisha kutenga mitaji kwenye dirisha hilo kwa masharti lakini waangalie utendaji wa sekta hiyo ili wajasiriamali waweze kupata mikopo yao vizuri. Tumeendelea pia kuwataka pia hata wajasiriamali hawa kuunda vikundi vikundi. Wakiwa kwenye vikundi ni rahisi zaidi kwa sababu taasisi nyingi zinaogopa kupoteza fedha, kwa hiyo ushirika ni mkombozi sana kwao. Na sisi tunaendelea kusimamia hasa sheria zilizosajili taasisi hizi za fedha kwa masharti ambayo hawaendi kwa kuweka riba kubwa inayomfanya yule mkopaji kushindwa kurejesha na hatimaye kuuzwa nyumba, labda kunyang’anywa au kufungwa. Kwa hiyo haya yote Serikali tunazingatia. Nataka nitoe wito kwa wajasiriamali washiriki kikamilifu na kwa uhuru mkubwa na wajenge matumaini na Serikali yao kwamba tunasimamia sekta hii ili waweze kupata maslahi kwenye sekta ya madini.

Mheshimiwa Spika, nimuagize Mheshimiwa Waziri wa Madini kufatilia taasisi za fedha zinazokopesha wajasiriamali hawa, kuwa wanapokwenda kukopesha hawaweki riba kubwa inayomuathiri mchimbaji; tunataka kila mmoja afanye kazi hii vizuri na apate faida, ahsante sana.