Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kunipa nafasi ya kuchangia katika hoja ya bajeti kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza na mimi nichukue fursa hii ya dhati kabisa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema aliyetupa nafasi ya kufika siku hii ya leo ya Ijumaa ndani ya Mwezi wa Ramadhani. Pia nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa hatua kubwa alizozichukua na kwa kutanguliza uzalendo kwa nchi yake, ameweka uzalendo mbele kuliko maslahi yake binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu nzima ya utendaji wa Wizara ya Fedha kwa kuleta bajeti nzuri inayoonyesha mwelekeo halisi wa Taifa letu kwa mwaka huu. Pia kama walivyozungumza wenzangu ni bajeti ambayo imetoka kwenye mawazo ya Watanzania na Wabunge wenyewe. Nakumbuka tulijadili kwa kina Mpango ulipoletwa hapa Bungeni kama Wabunge tukapendekeza mapendekezo mengi na Serikali imeyapokea. Kwa hiyo, hilo tunapaswa kushukuru kwa sababu kama alivyosema Mbunge mmoja mwaka jana Serikali haikutusikiliza lakini mwaka huu hii bajeti ni ya kwetu, michango mingi ilitokana na michango tuliyopendekeza wakati wa Mpango. Kwa hiyo, tunajisikia kwamba tunai-own bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa wanasema kwamba unapomsifia mwizi msifie na yule anayemfukuza. Nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete aliyetuletea chuma kama alivyosema yeye. Alituambia mimi naondoka nawaletea chuma hiki ili kitekeleze pale nilipochoka mimi yeye aende kwa kasi zaidi. Leo ndiyo tunamuelewa Mheshimiwa Dkt. Kikwete kwamba chuma kinatema cheche. Tofauti yake na Marais waliotangulia huyu wa sasa ni mpole sana, kwa hiyo, ni vizuri akaongeza kidogo ukali na usimamizi wa karibu katika mali za Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nayasema haya kwa sababu tumechezewa vya kutosha. Nimuombe Mheshimiwa Rais, kwa sababu Serikali iko hapa, aende nje ya boksi, kama alivyosema mwenye ng’ombe amekwenda kumkagua Mchungaji kama ripoti anayomwambia ni sahihi, basi ni vizuri akaenda pia kukagua kwenye vitalu vya uwindaji. Huko nako mambo si mazuri kama tulivyokuwa tunasikia Mabunge ya zamani. Kwa kasi hiyohiyo aliyoifanya kwenye madini aende na upande wa huko ili tujiridhishe kama taarifa wanazotupa wachungaji ni sahihi ili mwenye ng’ombe wake ajiridhishe kwa sababu kama alivyosema tulimchagua Watanzania kwenda kusimamia rasilimali hizi ili ziweze kutunufaisha wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna matatizo makubwa sana huko vijijini, leo barabara za Kinole, Mkuyuni na Mkulazi hazipitiki. Tatizo kubwa hatuna rasilimali fedha ya kuweza kuzitengeneza, tunaambiwa maskini na tunadanganywa kwa misaada midogomidogo kumbe kama Taifa, kama anavyosema Mheshimiwa Rais, tuna uchumi mzuri na mapato mazuri. Kwa mwendo huu aliouanza naamini barabara zote hizo zitaweza kutengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo, niende kwenye mchango wangu wa leo. Mchango wangu wa leo kitu cha kwanza naomba kuishauri Serikali, pamoja na bajeti nzuri na mipango mizuri na nia nzuri ya kuwatumikia Watanzania lakini nataka kupendekeza kwenye mfumo wetu wa bajeti. Sina tatizo na mfumo wetu wa cash budget kwa maana kwamba utekelezaji wake unategemeana na mfumo wa upatikanaji wa fedha, shida yangu kidogo iko kwenye huo utekelezaji.

Leo hapa kama Bunge tumekaa tumekubaliana au tulishakubaliana haya yaliyoletwa na Waziri kwenye bajeti kuu au bajeti za kisekta tunaamini ndiyo vipaumbele na ndiyo mipango ambayo wananchi wametutuma ili kwenda kuitekeleza. Kwa mfano inatokea wakati mwingine ile mipango tuliyokubaliana humu haikutekelezwa na mwaka wa fedha umekwisha, mwakani tukija ingawa tunaanza zero na ile mipango yote tuliyoipanga msimu uliopita tunaisahau kama vile tulishaikamilisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili nataka nitoe mfano kabisa, nianze na mfano wa Kitaifa kabla sijaenda kwenye Jimbo. Kama Taifa katika kwenda kwenye uchumi wa viwanda au wa kipato cha kati tulikubaliana mwanzoni lazima tuongeze uzalishaji kwenye kilimo, kuboresha
miundombinu kwa miaka mitano iliyopita. Kwa bahati mbaya sana kilimo chetu hakikuboreka miaka mitano kuanzia 2010 mpaka 2015 lakini bado leo tulivyoanza 2015 Mpango wa Miaka Mitano tumeacha mambo ya kilimo, kuimarisha uzalishaji na kuongeza tija katika kilimo kama vile tulishakamilisha kila kitu na kilimo kinakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushahidi upo katika kitabu chako mwenye Mheshimiwa Waziri umesema kabisa hali ya kilimo haiendi vizuri, kilimo kinashuka kutoka asilimia 2.3 kwenda asilimia 2.1. Nilitarajia kwamba sasa uje na mikakati mizuri ya kwenda kuimarisha kilimo lakini sasa tumekiacha kama vile tulishamaliza. Niseme kabisa Taifa hili tunategemea sana kilimo, zaidi ya asilimia 70 tunategemea kilimo, tukiacha sekta hii nyuma maana yake tumewaacha Watanzania wengi nyuma.

Kwa hiyo, kwa sababu hizi sekta nyingine ni consumption, ukizungumza afya na elimu zinahitaji fedha, lakini hii tukiiimarisha ni sekta ya kiuzalishaji, ni ya haraka sana kutubadilishia uchumi wa wananchi wetu mmoja mmoja lakini pia uchumi wa Taifa, itatuongezea mapato ya kigeni ili kuweza kuimarisha uchumi wetu kama Taifa. Pamoja na kwamba labda ilisahaulika, niishauri Serikali kuweka mikakati thabiti ya kuimarisha kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mapendekezo katika hili, miongoni mwa changamoto tunazozipata kwenye kilimo moja ni upatikanaji wa mbegu. Kwa hiyo, ni vizuri Serikali kwa sababu resource ni ndogo tukawezesha vyombo vyote vya usalama, hususan Magereza tukatafuta mashamba yao kwa sababu wanayo ya kutosha tukawekeza bwawa kubwa la umwagiliaji kwa ajili ya kilimo cha kisasa ili tuzalishe mbegu. Tuanzie hapo tu, tuzalishe mbegu ili tuondokane kabisa na tatizo la upatikanaji wa mbegu nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ili kuimarisha uzalishaji ni vizuri kuingia mikataba na makampuni wazoefu wenye teknolojia, wenye ujuzi, wenye ufahamu katika mazao kwa ajili ya kuzalisha miche kwa ajili ya mazao ya biashara. Kwa mfano, kama wanavyofanya Naliendele kwa ajili ya korosho, tutafute sasa watu wenye uzoefu ili wazalishe miche kwa ajili ya kahawa, kokoa, mazao yote ya muda mrefu na kuigawa bure kwa Watanzania yaani ruzuku ipelekwe kwenye kuzalisha tu hiyo miche halafu tuigawe bure kwa Watanzania ili tuweze kuongeza uzalishaji mkubwa sana katika mazao ya kilimo ili tuondoke hapa tulipo kwenda mbele zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema tatizo kubwa la mfumuko wa bei ni suala la ukame na upatikanaji wa maji. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri, ni vizuri mngeweka sasa mikakati ya kuondokana na kukabiliana na ukame na ukosefu wa mvua kwa kujenga mabwawa na majosho kwa ajili ya wafugaji na mambo yote ambayo yanahusiana na maji, hatuwezi kujenga nchi nzima lakini tunaweza tukaanza na sehemu fulani. Mheshimiwa Waziri anafahamu tuna Bwawa la Kidunda ni la muda mrefu sana. Kwa nini tusingeanza na hili ili liweze kutumika kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji ili tuweze kulisha Taifa hili na tuwe na uhakika wa chakula, malighafi na ajira kwa watu wetu, hususan wanaoweza kuishi vijijini na sehemu nyingine zipo fursa nyingi za kutengeneza mabwawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho lakini siyo kwa umuhimu katika suala la leo, nikupe mfano mwingine kuhusu mfumo ule wa bajeti. Kwa mfano, mwaka jana mlitutengea shilingi bilioni 17 kwa ajili ya kulipa fidia kwa watu waliopisha ujenzi wa Bwawa la Kidunda pamoja na kutengeneza ile barabara ya kwenda Kidunda. Hata hivyo, mpaka leo hata senti tano haijafika na tumebakiza wiki mbili tunamaliza mwaka. Kwenye bajeti mmetutengea shilingi bilioni 1.5 kwa Bwawa hilo la Kidunda wakati fidia tupu inadaiwa shilingi bilioni nne. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wiki mbili hizo zikiisha tutawaambia nini wananchi maana mnatusababishia ugomvi mkubwa sana na wananchi Mheshimiwa Waziri kwa kushindwa kutekeleza bajeti kama ilivyopangwa. Kwa sababu sisi kama wawakilishi wa wananchi tukitumwa hapa

tumetumwa na wananchi kuja kuleta shida zao baadaye tukirudi tuwaeleze Serikali imewapangia kuwafanyia nini. Kama mwaka jana nimewaeleza wametengewa shilingi bilioni 17 kwa ajili ya kutengeneza barabara hiyo pamoja na kulipwa fidia yao. Mwaka jana nimewaambia watu wa Kinole wametengewa shilingi milioni 105 kwa ajili ya kutengenezea barabara yao, barabara ile haijatengenezwa mpaka leo na leo kuna ugomvi mkubwa sana inaonekana kama vile Mbunge hawasemei wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu utakwisha na mwakani hata nikimdai Meneja wa TANROADS atasema haipo kwenye bajeti, nikimdai Meneja wa Maji anasema kwamba haipo kwenye bajeti mwaka huu Mheshimiwa tumetengewa shilingi bilioni 1.5, kwa hiyo haiwezekani kutekeleza tusubiri mwakani. Nikuombe sana, ni vizuri muuangalie mfumo huu wa bajeti ili uendane na hali halisi kwa sababu yale mnayotuambia hapa tunakwenda kwa wananchi kuwaeleza, sasa isije kuonekana kama sisi viongozi tunasema uongo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nichukue nafasi hii tena kuunga mkono bajeti hii kwa asilimia mia moja. Ahsante sana, Mwenyezi Mungu ampe uhai mrefu na uzima Rais wetu ili aweze kuonesha maajabu ndani ya nchi yetu, ndani ya Afrika na ndani ya dunia. Rais Trump alisema Waafrika wengi tatizo tuna Marais wezi, lakini Mheshimiwa Dkt. Magufuli amemhakikishia hakuna Marais wezi, tuna Marais wazalendo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii, naunga mkono hoja.