Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nyingine tena. Na mimi kutoka mwanzo niseme kwamba naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi niungane na wenzangu kukubali kwamba viongozi wa Wizara hii, Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na wengine wote wamejitahidi sana hasa katika eneo la kuondoa migogoro. Tunawapongeza na tunaomba muongeze bidii. Mimi namfahamu Waziri, Mheshimiwa Lukuvi tulikuwa naye Ofisi ya Waziri Mkuu na najua jinsi anavyochapa kazi, endelea kuchapa kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ardhi ndiyo rasilimali kuu ya Tanzania na pengine nchi hii ya Tanzania imejaliwa kuwa na ardhi yenye rutuba lakini ardhi inakuwa na thamani pale tu ambapo imepangwa, imepimwa na kumilikishwa. Bila ya kuwa na vipimo, bila kuwa na hati miliki, ardhi kwa kawaida pamoja na kwamba ni rasilimali muhimu lakini inakuwa haina thamani. Mpaka sasa hivi ni asilimia 15 tu ya ardhi ya Tanzania imepimwa na imemilikishwa. Kwa hiyo, asilimia ile yote 85 maana yake haina thamani. Kama Tanzania tunataka kuondokana na umaskini inabidi kwa kweli tuipe rasilimali hii muhimu thamani inayotakiwa kwa kupangwa, kupimwa na kumilikishwa. Wananchi wanapokuwa na hati miliki au haki miliki wanaweza wakaitumia ile ardhi kwa shughuli za uchumi lakini ikatumika vilevile kama dhamana kukopa kuweza kutumia ile ardhi vizuri zaidi. Kwa hiyo, ndugu zangu nawaombeni kipaumbele kipelekwe kwenye kupima ardhi hii ya Tanzania na kumilikishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wananchi zaidi ya dhamana wanaweza wakatumia ardhi hii ikiwa na hati miliki kama hisa na kuungana na wenye mtaji wa fedha ili ardhi hii itumike katika uwekezaji. Watanzania wanashindwa kuwekeza kwa sababu ardhi waliyonayo haina thamani na kwa hivyo hawawezi kuwa na hisa kwenye uwekezaji. Kwa kiingereza inaitwa land for equity ambapo alipokuwa Waziri Mheshimiwa Anna Tibaijuka na mimi tuliibuni ili Watanzania wawe na uwezo wa kushiriki kwenye uwekezaji bila ya kutafuta fedha, wanaweza wakatumia hiyo ardhi kwa kukopa au wanaweza kuwa na hisa kwenye uwekezaji kupitia ardhi hiyo hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niende kwa wawekezaji na nataka nijielekeze Hanang. Hanang ni eneo la kilimo na mifugo na ardhi ipatayo heka 70,000 iko mikononi mwa wawekezaji. Wawekezaji wenyewe wale hawaitumii ardhi ile kama inavyopaswa. Kwanza wametumia sehemu tu ya ardhi ile waliyopewa wakati watu hawana ardhi ya kutosha wanaingalia ile ardhi na kuitamani, napenda tuwasimamie wale ili waitumie hiyo ardhi vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hivyo tu, sioni sababu ya mwekezaji kutoka nje achukue ardhi ya Tanzania, kwa mfano pale Hanang watu wa Hanang wanazalisha ngano nyingi zaidi kwa heka moja kuliko wawekezaji waliokuja na ina-defeat the whole purpose inakuwa haina maana. Kwa hiyo, naomba tuangalie na tija katika uwekezaji ili tupate faida ya kutosha kwenye uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini zaidi ya hivyo kutokana na uwekezaji kwenye ile ardhi, wawekezaji walituahidi kufanya mambo mbalimbali. Siwezi kuorodhesha, lakini moja ambalo nalijua ni kujenga mabwawa makubwa kwa ajili ya umwagiliaji na wananchi kuweza kunufaika lakini mpaka sasa limechimbwa bwawa moja na halijakamilka. Nataka na ahadi zile zote nazo ziweze kutekelezwa ili watu wa Hanang wanufaike na uwekezaji ule na kama hawalimi vya kutosha, kuna wengine wana mashamba zaidi ya moja, mashamba yale ambayo hawawezi kuyalima yarudi mikononi mwa wananchi. Mimi najua wananchi wa Hanang wanaweza kulima ardhi ile na kuweza kuleta manufaa ambayo wawekezaji hawaleti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ndugu zangu migogoro ya ardhi iko mingi Wilayani Hanang. Kuna migogoro ya mipaka kati ya kata na kata, vijiji na vijiji na hata wilaya na wilaya zingine zinazopakana na Hanang hata Mkoa wa Manyara na Mkoa wa Singida, Mkoa wa Dodoma na mikoa mingine tunakuwa na migogoro. Namuomba Waziri Mheshimiwa Lukuvi aje Hanang na Mkoa wa Manyara ili migogoro ile itatuliwe maana kila wakati kumekuwa na vifo kupitia migogoro hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana wale wawekezaji watimize ahadi yao moja ambayo wameahidi ya kujenga branch ya university ya Sokoine kwenye yale mashamba, mpaka sasa imebakia ahadi tupu hakuna utekelezaji wowote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ambalo nataka kuongelea kuhusu ardhi ni kwamba jamani bila ya kupima hii ardhi na kuiweka kwenye shughuli mbalimbali, mifugo, kilimo, biashara, huduma za jamii, migogoro itaendelea kuwepo. Migogoro itaendelea kuwepo kati ya wafugaji na wakulima, migogoro itaendelea kuwepo kati ya wakulima, wafugaji na hifadhi mbalimbali, migogoro itaendelea kuwepo kati ya wawekezaji na wananchi wa Tanzania. Kwa sababu bila ya kujua wafugaji wawe wapi, wakulima wawe wapi, wawekezaji wawe wapi, jamani hatuwezi kuondokana na mambo haya hata tukiwa na operation ngapi haitasaidia. Ukiwatoa wananchi kutoka kwenye hifadhi na haijulikani wapi wanakwenda kwa ajili ya kuhakikisha ng‟ombe wao zinabakia kuwa hai watavizia kurudi kule. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nathamini hifadhi za Tanzania na ni mmoja wa watu ambao nitakuwa wa mwisho kabisa kuondoa hifadhi lakini lazima tuone kwamba wakulima na wafugaji wana maeneo ya uhakika la kufanya shughuli zao. Wakijua eneo lao ni hekta ngapi watahakikisha ng‟ombe wanaoweza kubaki kule watabaki na wengine watauzwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namna nyingine ya kuwasaidia ni kuwa na masoko mbalimbali tushirikiane pamoja kushughulikia suala hili. Mheshimiwa Waziri Mkuu aliagiza Wizara zile zikae mara moja ili kuona kwamba wananchi wavyotolewa kutoka kwenye hifadhi, wananchi wanavyogombania ardhi kunakuwa na mahali mahsusi pa wale wananchi kwenda kama ni wafugaji au wakulima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Shirika la Nyumba, mambo ya msingi kwa binadamu ni chakula, mavazi na makazi. Shirika la Nyumba linafanya kazi nzuri lakini kama lilivyoundwa zamani baada ya uhuru ilikuwa ni kuwapatia maakazi watu wanyonge zaidi kuliko wale wanaojiweza.
Kwa hiyo, naombeni sana Shirika la Nyumba lifanye kazi hiyo ya kuona watu wa Manzese, Keko wamepata nyumba, watu wa maeneo ya chini wamepata nyumba. Maeneo yale ya matajiri wajenge wenyewe kwa sababu wana mali ya kuweza kuweka dhamana kwenye benki na kujenga nyumba zao, sisi tujielekeze kwa Watanzania wanyonge, wana haki ya kukaa kwenye nyumba na hakuna mtu ambaye ana fedha yake mwenyewe asijenge, lakini ni kwa sababu ya kukosa mali ya kuweka dhamana hawawezi kujenga nyumba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirudie pongezi zangu na shukrani zangu za dhati kwa Wizara na viongozi wa Wizara, watendaji na taasisi ambazo zipo kwenye Wizara hii. Na mimi nashukuru sana migogoro inapungua, tuendelee kupunguza migogoro hii hadi inapokwisha. Sisi wengine tumekaa kwenye migogoro tukiona watu wanakufa na hatutaki kuendelea kuona watu wetu wanakufa. Ahsanteni sana.