Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

Hon. Joseph Zacharius Kamonga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia Bajeti hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri ambazo zinaendelea na kule Jimboni kwangu Ludewa wananchi wanazishuhudia zinaonekana kwa macho. Ila leo naomba nijikite zaidi kwenye maeneo ya miundombinu ya barabara Jimboni kwangu Ludewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya yote, nianze kwa kutoa pole nyingi sana kwa wananchi wa Kijiji cha Liugayi kilichopo Kata ya Luilo, Kijiji cha Lifuma na Kitongoji cha Liumba kwa mafuriko makubwa ambayo wazee wenye umri mkubwa wanasema mara ya mwisho yalionekana mwaka 1963/1964. Mto Ketewaka kutokana na mvua nyingi ambazo zilinyesha upande wa Ruvuma kwa maana ya Mbinga na upande wa Ludewa na Njombe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mto Ketewaka ambao unaenda kuungana na Mto Ruhuhu ulifurika sana na kuweza kuathiri wananchi wa Kijiji cha Liugayi kama nilivyoeleza ambapo nyumba zao zimebomoka, mazao yao yamesombwa na maji, kwa hiyo, hawana chakula, hali kadhalika, mifugo yao imesombwa na maji. Kwa hiyo, kuna wananchi kama wa kaya 20 wanaishi kwenye Kanisa hivi sasa. Hali kadhalika, Kijiji cha Kiyogo, Kijiji cha Kipingu, Ngerenge na baadhi ya mashamba ya wananchi wa kandokando ya Mto Mchuchuma, Kijiji cha Igalu na Kijiji cha Mbongo. Kwa hiyo, nitoe pole nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa huko, nilikwenda kuwafariji wananchi, kimsingi naomba Serikali iweze kutoa msaada wa haraka. Hatuwezi kumkufuru Mwenyezi Mungu kwa kuleta mvua nyingi kwa sababu mvua tunaihitaji, tunaiombea wakati wote tuweze kuipata na kule Ludewa imetusaidia, mwaka huu tuna mahindi mengi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Waziri wa Kilimo aanze kututafutia masoko, ni mvua hiyo hiyo ndio imewezesha kutokana na Mheshimiwa Rais kuleta ruzuku ya mbolea, wananchi wamelima zaidi na mazao wamepata zaidi, lakini mvua kutokana na kuzidi imesababisha maafa kama ambavyo nimesema. Kwa hiyo nitoe pole nyingi kwa wananchi na niwasihi waendelee kuwa na subira kwa sababu Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya na wasaidizi wake wanaendelea kuliratibu vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa miundombinu ya barabara, natambua kwamba Wizara hii inashughulika na mambo mengi ya wananchi na jana nimetoka Ludewa, wananchi wanatarajia kusikia nikisemea changamoto mbalimbali ambazo zinazikabili barabara mbalimbali za Ludewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na barabara ambazo ziko chini ya TANROADS, niishukuru Serikali awamu ya kwanza ilitoa shilingi bilioni 179 kwa ajili ya kutujengea barabara kwa kiwango cha zege, kilometa 50 kutoka Lusitu hadi Mawengi. Barabara imekamilika na inatumika vizuri na ni barabara bora sana kutokana na kiwango kile cha zege. Changamoto ni kuwa, jiografia yetu ina milima mikali sana kwa hiyo kifusi kimekuwa kikiporomoka, milima inaporomoka inafunga barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi mimi mwenyewe nimepata vikwazo sehemu mbili, kwenye hii Barabara ya Itoni – Ludewa – Manda, pale Mlima Kimelembe kuna kazi inaendelea ya kukata mlima mita 20 ambao ulikuwa unagharimu maisha ya watu na mali zao, Serikali ilitoa fedha bilioni tano kwa ajili ya kuukata mlima. Sasa bahati mbaya mvua ziliwahi kufika kabla mkandarasi hajafika mwisho wa kazi, lakini nadhani hata ule upana wa barabara nao ulikuwa mdogo, kwa sababu ule udongo ni udongo ambao uko kwa asilimia mia moja. Kwa hiyo mvua inaponyesha unayeyuka kama biskuti unaporomoka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiwa Manda kuwafariji wale wananchi wa Bonde la Ruhuhu nilikuwa siwezi kupita Ruvuma kwa sababu Mto Ruhuhu ulifurika. Kuna Mto Kipingu nao ulijaa maji, gari haiwezi kupita na kwa upande wa Nyasa maji yalikuwa yamejaa, hakuna gari linapita, lakini Mlima Kimelembe ulikuwa umeporomoka umefunga barabara. Kwa hiyo ningeugua kule, nisingeweza kufikishwa hata hospitali ya wilaya labda ningepewa milungulungu na wale wananchi ambazo ni tiba mbadala ambazo wao wamekuwa wakitumia muda wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwamba tukio hili lilinikuta mimi, sasa wananchi wanakuwa katika hali gani pale ambao barabara zinafunga, wanakuwa hawawezi kupelekwa sehemu yoyote. Kwa hiyo naomba juhudi za haraka sana na za makusudi ziweze kufanywa na Serikali kuongeza wataalam ili kwenda kutathmini na kuweza kuona ni namna gani tunaweza tukapata suluhisho la kudumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Mlima Kimelembe kwa bahati mbaya sana uligharimu maisha ya kijana mmoja wa bodaboda ambaye hata miaka 30 hajafikisha. Kifusi kilishuka na kwa bahati mbaya alikuwa pale, akafunikwa akafariki. Tunaiombea roho yake ipumzike kwa amani huko aliko. Kwa hiyo naomba sasa Serikali iweze kutuma wataalam waungane na wale wa TANROADS waliopo Njombe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Meneja wa TANROADS pale Njombe, ni msikivu na mwepesi sana, ukimpigia simu yuko tayari kuacha shughuli zake kwenda kusaidia. Siku ile nimefungiwa nilimpigia simu, alitoka mwenyewe na wataalam wakaenda kufungua barabara. Sasa kwa bahati mbaya sana ilifunga maeneo mawili na huku kwenye hii ya Lusitu - Mawengi na yenyewe ilikuwa imefunga hata kupeleka mitambo ilikuwa haiwezekani. Kwa hiyo zinahitajika juhudi za makusudi na za haraka sana ziweze kuchukuliwa ili kuondoa vikwazo hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hali kadhalika kuna barabara nyingine ambayo ni ya TANROADS ambayo inaitwa Mkiu - Liganga kwenda Madaba, barabara hii ndio inayoenda kwenye Mgodi wa Liganga, ambako kuna utajiri mkubwa, tani milioni 126 za chuma ambazo ndani yake ina titanium na vanadium. Madini ambayo yana thamani zaidi ya mara 20 ya chuma chenyewe. Kwa hiyo ni barabara muhimu na ni barabara ya kiuchumi na inaunganisha na Mkoa wa Ruvuma kwa jirani yangu Mheshimiwa Joseph Kizito Mhagama. Sasa pale kuna lile eneo la Ndolela na kwenyewe kuna daraja pale limeondolewa na maji. Kwa hiyo, naomba sana, tunashirikiana vizuri na Mheshimiwa Mhagama kufuatilia kwa sababu wananchi wangu nayo ni alternative route na hilo eneo la Ndolela lina mashamba makubwa ya kiuchumi ambayo nayo ni barabara ya kimkakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali ule mpango wa kuijenga Barabara hii ya Mkiu – Liganga - Madaba ungeanza haraka, kwa sababu Mheshimiwa Rais anavyozungumzia uwekezaji wa Mchuchuma na Liganga amechoka kusikia ngonjera hizi za muda mrefu. Hii inatakiwa iwe reflected kwenye barabara. Namwona Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi anaandika, namshukuru sana Mheshimiwa kwa usikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Rais anavyozungumzia barabara ya kiuchumi, ya kimkakati, ya uwekezaji, haya yawe reflected kule kwenye barabara hata wananchi wakiona ujenzi umeanza kwa kiwango cha lami watajua ni yale ambayo Mheshimiwa Rais anayazungumza. Kwa hiyo niombe sana Serikali iweze kuchukua hatua za haraka kwa sababu hata kutoka Mkiu kwenda Lugarao mwaka huu wananchi wamehangaika sana. Kuna daraja pale, unapotoka Lugarao kwenda Shaurimoyo kwenye Chuo cha VETA napo pana hali ngumu kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, licha ya yote hayo, nimpongeze sana yule Meneja wa TANROADS Mkoa wa Njombe yule mama, kwa kweli anafanya kazi nzuri, anajituma sana. Namwomba Waziri wa Ujenzi wasituhamishie labda kama watampandisha cheo, hilo sitakuwa na uwezo wa kuzuia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara vilevile inaanzia Mlangali – Lupanga kwenda Ikonda, Ikonda ni hospitali kubwa sana ambapo wananchi wengi wanategemea kwa ajili ya matibabu. Namshukuru Mheshimiwa Bashungwa, mwezi uliopita alikuja Ludewa, alifanya mkutano mkubwa pale Mlangali na alitoa ahadi nzuri sana kuhusu hii barabara. Kwa hiyo naomba nisiizungumzie sana ila tu ule mpango wa kuendeleza lot three kutoka pale Mawengi mpaka Nkomang’ombe. Naomba sana Serikali iendelee na iweze kujengwa kwa kiwango cha zege kwa sababu sasa hivi malori ya makaa ya mawe zaidi ya 40 yanakwama mle barabarani. Ukiwauliza kwa nini msisubiri mvua ziiishe ndio mje? Wanasema haiwezekani Wakurugenzi wa Makampuni wamekuja wana order kubwa nzuri zenye faida, kwa hiyo malori lazima yaendelee kwenda. Kwa hiyo ni ishara kwamba tusipojenga kipande hiki kilometa 68 kutoka Mawengi mpaka Nkomang’ombe, tunafunga uchumi wa nchi na tunazuia pato la Taifa kuongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzetu Ruvuma walipoanza kuchimba makaa ya mawe waka-shoot kwenye makusanyo ya TRA kutoka kusikojulikana mpaka kuwa namba tatu, kwa hiyo kuna uchumi, kuna kodi nyingi pale. Barabara kama hizi ambazo zinakuza pato la Taifa, zinaleta uchumi, zingepewa kipaumbele kwa sababu zinaweza kuongeza fedha ambazo zitakwenda kujenga barabara maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna barabara ambazo ziko chini za TARURA, Kata ya Ibumi nayo iko kisiwani, mwananchi akiugua pale hawezi kupelekwa hospitali ya wilaya, hawezi kupelekwa popote kwa sababu vifusi vimedondoka na vimefunga barabara. Daraja la Mto Ketewaka na lenyewe limekuwa changamoto. Halikadhalika kuna barabara hii inayoanzia Kigasi inakwenda Milo - Ludende mpaka Amani inaunganisha kata nne na barabara nyingine inayokwenda Madilu eneo la…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kamonga pole na msiba, muda wako umekwisha.

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)